Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt

 

Mapenzi Ya Ahlus Sunnah Juu Ya Ahlul Bayt

(Watu Wa Nyumba Ya Mtume Wa Allaah (Swalla Allaahu ‘Alayhi Wa Sallam)

 

Imekusanywa na Muhammad Faraj Salim As-Sa’ay

Imepitiwa na Abu 'Abdillaah

 

Share

00-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Yaliyomo

 

Yaliyomo

 

Utangulizi

Al-Mahdi na ‘Umar

Nani Ahlul-Bayt?

Hadithi ya shuka na dalili katika Hadithi

Mapenzi yetu kwa Ahlul-Bayt

1- Watu wa Ukoo

Elimu ya Ghaibu na Kukingwa

Fadhila za Ahlul-Bayt

Kwanza Fadhila za ujumla

Fadhila Makhsusi

'Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu)

Faatwimah (Radhiya Allaahu anha)

Al-Hasan na Al-Husayn

Al-‘Abbaas bin Abdil-Muttwalib (Radhiya Allaahu ‘anhu)

'Abdullaah bin ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhuma)

'Aliy Zaynul-‘Aabidiyn (Radhiya Allaahu ‘anhu)

Muhammad bin ‘Aliy bin Al-Husayn ‘Al-Baaqir’ (Radhiya Allaahu ‘anhu)

Ja’afar bin Muhammad (Radhiya Allaahu ‘anhu)

Muusa bin Ja’afar ‘Al-Kaadhwim’ (Radhiya Allaahu ‘anhu)

'Aliy bin Muusa ‘Ar-Ridhwaa’

Muhammad bin ‘Aliy bin Muusa ‘Al-Jawwaad’

2- Wake zake

Nani Swahaba – kilugha na kidini

Nani Mnafiki – kilugha na kidini

Tafsiri ya Al-Iyaashi

Kuoleana

Wajibu wetu

Hitimisho

 

 

Share

01-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Utangulizi

 

Utangulizi

 

 

Mmoja katika wana falsafa wa zamani alisema:

“Haki yote haiwezi kumilikiwa na upande mmoja, wala makosa yote hayawezi kuwepo upande mwingine, bali kila upande husibu sehemu yake. Mfano wa kundi la vipofu waliopelekwa mbele ya tembo wakatakiwa wamguse mwili wake, kisha kila mmoja aelezee umbile lake.

Katika muda mfupi waliopewa, hapana aliyewahi kukamilisha kuushika mwili wote. Kila mmoja alifanikiwa kugusa sehemu tu.

Aliyeushika mkonga akidhani kuwa amemshika tembo wote akasema: “Mwili wa tembo ni mrefu mfano wa gogo la mti”,

Aliyeshika mgongo akasema:

“Hapana, bali mwili wa tembo ni mfano wa jabali dogo”,

Aliyeshika sikio akasema:

“Nilivyouona mimi mwili wa tembo ni mpana, duara na laini”.

Kila mmoja anahadithia juu ya ile sehemu aliyodiriki kuishika katika muda mfupi ule akidhani anatoa maelezo kamili. Wote wamesema kweli, lakini kila mmoja amehadithia sehemu tu ya ukweli anaoujua yeye akidhani kuwa ndio ukweli wote.”

 

Hitilafu husababishwa na mambo mengi, yakiwemo upeo wa kufahamu, kupenda, matamanio ya nafsi, mielekeo ya elimu, ya kifikra, kuiga waliotangulia, kupenda umaarufu, kupenda ukubwa, hitilafu za ustaarabu. Wengine huiga waliyowakuta nayo wazee wao, na wengine wanafuata mafundisho ya walimu wao wanaowaamini n.k. Na wengine huiendeleza hitilafu kwa sababu ya ubishi au kiburi tu, hata kama wataiona haki mbele yao.

Si vibaya kuhitilafiana, kwa sababu Allaah Ametuumba kila mmoja na akili yake pamoja uwezo wake wa kufahamu.

Allaah Anasema:

 

وَلَوْ شَاء رَبُّكَ لَجَعَلَ النَّاسَ أُمَّةً وَاحِدَةً وَلاَ يَزَالُونَ مُخْتَلِفِينَ .إِلاَّ مَن رَّحِمَ رَبُّكَ وَلِذَلِكَ خَلَقَهُم

«Na Mola wako Angelipenda Angewafanya watu wote wakawa umma mmoja. Lakini hawaachi kukhitalifiana, Isipokuwa wale ambao Mola wako Amewarehemu; na kwa hiyo ndio Allaah Amewaumba.»

Huud-118-119

 

Anasema Al Hasan Al Basry: وَلِذَلِكَ خَلَقَهُمْ maana yake ni kuwa; Amewaumba ili wakhitalifiane.

 

Wenye kukhitilifiana wanaweza kusikilizana na kufahamiana ikiwa hapana chuki baina yao, lakini chuki inapoingia, hayapatikani tena masikilizano wala kufahamiana. Chuki inaondoa mapenzi na inavunja uhusiano mwema na inaendeleza bughudha na kuondoa uwezekano wowote wa masikilizano.

 

Imepokelewa kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) usiku mmoja aliamka uso wake ukiwa mwekundu huku akisema:

 

لا إِلهَ إِلاّ الله، وَيْلٌ للعَرَبِ، مِنْ شَرَ قَدِ اقْتَرَب

Laa ilaaha illa Allaah, Ole wao Waarabu kwa shari iliyo karibu

Alirudia maneno haya mara tatu.

 

Maulamaa wanasema kuwa;‘Hii ilikuwa ishara kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) juu ya hitilafu itakayotokea baada yake’.

 

Hitilafu iliyopo hivi sasa baina ya Shia na Sunni inakula kibichi na kikavu.

Mamia ya Waislamu wanauliwa kila siku huko Iraq, na wanaendelea kuuliwa, na mamilioni wengine wamejeruhiwa. Mamilioni wamekwishaihama nchi yao, na mamilioni hawana kazi wala bazi.

Lebanon, nchi iliyojaa neema, nchi ya elimu na ziraa. Nchi ya historia na sanaa, leo kila kitu kimesimama katika nchi hii kwa sababu ya fitna ya umadhehebu. Nchi haina serikali, ina majeshi mawili, kila moja linadai kuwa wao ndio wenye kuipenda nchi. Ina makundi mawili, kila moja linalituhumu jingine kuwa ni vibaraka. Watu hawaelewi wanapelekwa wapi, kila siku mapambano ya risasi na mabomu.

 

Huko Yemen, maelfu ya watu wamekwishapoteza maisha yao katika mapambano baina ya majeshi ya serikali na makundi ya watu wa kabila la Houthi wenye kufuata madhehebu ya Shia Ithnaashariyah.

Hii ni fitna iliyopenyezwa katika mwili wa Waislamu kwa ajili ya kuwagawa. Inatumiliwa na kuchochewa na wale wasiopenda kuuona umma wao umetulia huku ukipiga hatua katika kuziendeleza nchi zao na kuwaelimisha watu wao.

Na katika kila pembe ya ulimwengu chuki hizi zinaanza kupasua njia kidogo kidogo na ni Allaah peke Yake Anaelewa wapi yataishia.

 

Mambo yaliyotokea miaka elfu moja mia nne iliyopita yanaendelea kuwagawa na kuwafarikisha Waislamu hadi hivi sasa katika karne hii ya satellite na computer.

Umma huu ni Umma mmoja, Mungu wetu ni Mungu Mmoja, na Dini yetu ni moja na Mtume wetu ni mmoja, Lengo letu ni moja na adui yetu ni mmoja, kwa nini basi hatuungani tukawa kitu kimoja?

Ikiwa kuwapenda watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ni Ushia, basi sisi sote ni Mashia, na ikiwa kuwapenda Masahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) ni Usunni, basi sote tuwe Masunni. Waislamu hawatakuwa na kheri yoyote ikiwa watawachukia watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ambao Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ametuamrisha tuwaswalie kila tunapomswalia.

 

Na Waislamu hawatakuwa na kheri yoyote ikiwa watawachukia Sahibu zake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) (Radhiya Allaahu ‘anhum), ambao baada ya kufariki dunia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), wao ndio walioibeba bendera na kuueneza Uislamu kila pembe ya ulimwengu.

Waislamu wanatakiwa waone fahari kubwa kila wanapotajwa Masahaba hawa watukufu (Radhiya Allaahu ‘anhum), kwa sababu wao ndio waliotuletea Uislamu. Wao ndio waliotufikishia Qur-aan tukufu ambayo ni Nuru itokayo kwa Mola wetu.

 

Allaah Amewajaalia wao kuwa ndiyo sababu ya kutufikia dini hii kote huku tuliko. Kwa juhudi yao kubwa na kujitolea kwao mhanga kwa hali na mali waliuwezesha Uislamu kuingia na kuenea na kufuatwa na kupendwa Arabuni kote, Iran, Asia, Afrika hadi Ulaya na Marekani.

Wangelikuwa watu hawa ni makafiri basi wangelituletea ukafiri badala ya Uislamu. Wangelituletea misalaba na masanamu badala ya Qur-aan na Swalah na salamu amani.

 

Tunamshukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kuwa hitilafu baina ya madhehebu ya Kiislamu si katika kiini cha dini na asili ya mafundisho yake, kama vile kuabudiwa Allaah Mmoja na kwamba Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ni Mtume Wake. Hitilafu haikuwa juu ya Qur-aan tukufu, kwani AlhamduliAllaah Waislamu wote kwa pamoja wanaamini kuwa Qur-aan hii tuliyonayo hivi sasa ndiyo ile ile aliyoteremshiwa Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) miaka elfu moja mia nne iliyopita.

 

Tunaelewa kuwa walikuwepo baadhi ya Maulamaa wachache wa madhehebu ya Kishia mfano wa Nuwriy At-Tubrusiy aliyeandika kitabu ‘Faswlul Khitwaab fiy ithbaat tahriyf kitaab Rabbil Arbaab’, akidai ndani ya kitabu hicho kuwa Qur-aan hii tuliyonayo ilibadilishwa na kupunguzwa na kuzidishwa. AlhamduliAllaah katika wakati wetu huu hapana tena anayeziamini kauli hizo hata miongoni mwa wengi kati ya Mashia, kiwa si wote, na kama watakuwepo basi watakuwa wachache sana.

 

Tunamshukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) pia kuwa hitilafu hii haikuwa katika kuharamisha au kuhalalisha mambo yanayojulikana katika dini kuwa ni ya dharura kama vile uharamu wa Pombe, kula nyama ya nguruwe n.k. Juu ya kuwa hapana shaka yoyote kuwa ipo hitilafu juu ya baadhi ya mambo yanayohusiana na Itikadi ‘Aqiydah’.

Hapana shaka yoyote kuwa ipo hitilafu juu ya baadhi ya mambo yanayohusiana na Itikadi ‘Aqiydah’, kama vile kumuomba mwengine asiyekuwa Allaah na kuyatukuzu makaburi ya watu wema.

Naelewa pia kuwa wapo wanaojinasibisha na Ahlus Sunnah wenye kuwaomba wengine wasiokuwa Allaah na kuyatukuza makaburi ya watu wema, lakini tofauti iliyopo baina ya Sunnah na Shia ni kuwa Maulamaa wa Ahlus Sunnah wanayakemea na kuyakataza mambo haya, wakati maulamaa wa Shia wanayanyamazia na kuyapa kipaumbele.

 

Share

02-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Al-Mahdi Na 'Umar

 

Al-Mahdi na ‘Umar

 

 

Anasema Dr. Ahmad Al-Kaatib mwanachuoni wa Kishia kutoka Iraq ambaye ni mwalimu katika vyuo vikuu mbali mbali vya dini huko Iraq, Kuwait na Iran na ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuia ya Majadilianao ya Ustaarabu, 'Al Hiwaar al Hadhwaariy', ambayo makao yake makuu yapo London, alisema:

"Nimefanya utafiti ulionipa uhakika kuwa hitilafu iliyopo baina ya Sunnah na Shia hauna msingi wowote na imenithibitikia baada ya kuidurusu kadhia hii kuwa hitilafu zilizokuwepo ni za kisiasa tu na wala si za itikadi.

Baada ya kufanya utafiti wangu ulionichukua muda mrefu sana imenithibitikia kuwa hitilafu iliyokuwepo baina yetu (Shia na Sunnah) ni juu ya Imam Al Mahdi na pia yale madai kuwa ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhu) alimpiga Bibi Faatwimah  siku ile watu walipofungamana na Abu Bakr (Radhiya Allaahu ‘anhu).

Baada ya kumaliza utafiti wangu," anaendelea kusema Ahmad Al Kaatib ambaye hadi hivi sasa ni mwalimu mkubwa wa madhehebu ya Shia Ithnaashariyah; "imenidhihirikia kuwa madai hayo kuwa ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhu) alimpiga Bibi Faatwimah hayana msingi wowote na kwamba ni uzushi ulioenezwa na kuandikwa katika vitabu mbali mbali vya historia kwa ajili ya kuipa nguvu nadharia ya Uimamu, nadharia ambayo inafutika ikithibiti kuwa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alikubali kwa hiari yake kufungamana na Abu Bakr na ‘Umar na ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhum) walipochaguliwa kuwa Makhalifa, kwa sababu angelikuwa Imam ‘Aliy amechaguliwa na Allaah, basi asingekubali kufungamana nao kwa hiari yake.

Wazushi wa kisa hicho walidai kuwa ‘Aliy alikubali kufungamana na Abu Bakr baada ya ‘Umar kuingia kwa nguvu nyumbani kwake na kumpiga mkewe ambaye ni  Bibi Faatwimah binti wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) mpaka mimba ikamtoka."

 

Anasema Ahmad Al-Kaatib:

"Nilikifanyia uchunguzi kisa hiki lakini sijakikuta katika kitabu chochote chenye kutambulika na kuaminika miongoni mwa vitabu vya Kishia kama vile Al-Kafi na vyenginevyo.

Kinachokikanusha zaidi kisa hicho ni ule uhusiano mzuri uliokuwepo baina yao hadi kufikia kuwa ‘Aliy na Faatwimah walimuozesha binti yao Ummu Kulthum kwa ‘Umar.

Itawezekanaje basi, kwa mama akubali kumuozesha binti yake mtu aliyempiga mpaka mimba ikamtoka?"

"Ama kisa cha Uimamu," anaendelea kusema Ahmad Al-Kaatib: "Hata Ayatollah Sistani ametamka kuwa jambo hili si katika mambo ya msingi wa dini kwa Shia, na kwamba linaweza kujadiliwa.

Nilifuatilia vitabu vilivyoandikwa na waandishi wa Kishia katika karne ya tatu na ya nne na ya tano Hijri nikaona kuwa hapana ushahidi wowote unaothibitisha kuwa Imam huyu alizaliwa, na kwamba Sayed Murtadha na Al Umani na wengine wanasema: "Sisi tunaona kuwa haya ni mambo ya kukisia tu kwa dalili za kiakili na hatuna dalili za kielimu zisizopingika.

Kwa hivyo nadharia ya kuwepo kwa Imam wa kumi na mbili mwenye kusimamia, anayetokana na Imam Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhu) aliyepewa jina na Muhammad bin Hasan Al-Askary na nadharia ya kutoweka kwake, si katika itikadi za Ahlul Bayt, bali wamenasibishwa nazo na baadhi ya waandishi.

Na hivi sasa kwa vile serikali ya Iran imeamua kuipa nguvu nadharia ya Utawala wa mwanachuoni 'Wilayat Al-Faqiyh' na imeamua kufuata nidhamu ya kuchagua viongozi wa dini kwa njia ya kushauriana, 'Shuura' na kuchagua viongozi wa nchi kwa njia ya demokrasia (democracy), kwa hivyo haya yanafuta ile kauli ya kuwa kiongozi lazima awe aliyechaguliwa na Allaah, na badala yake mtu yeyote anaweza kuwa kiongozi ikiwa watu wataridhka naye na kumchagua, (pia siyo lazima awe katika ‘Ahlul-Bayt’)

 

Kwa ajili hiyo ile khitilafu iliyokuwepo baina ya Shia na Sunnah juu ya Uimamu sasa itakuwa ishaondoka pia kwa sababu Shia hawaamini tena juu ya ulazima wa kuwepo Imam aliyetoweka akaingia ndani ya pango na wala hawasubiri tena kutoka pangoni alipoingia miaka elfu moja iliyopita ili wapate kuisimamisha dola ya Kiislamu.

Na lile sharti ya kuwa Imam mwenye kuwaongoza Waislamu lazima awe Aliyechaguliwa na Allaah na awe aliyekingwa asiyefanya makosa anayetokana na ukoo maalum, nayo pia imeondoka kwa sababu kiongozi hivi sasa anachaguliwa kwa njia ya uchaguzi au kwa kushauriana ‘Shuura’."

Mwisho wa maneno ya Al Kaatib

(Website ya Al Arabiyah.net. Tarehe 27 May 2008)

 

Anasema mwanachuoni mwengine maarufu Dr. Muusa al Musawiy katika kitabu chake ‘Ash-Shi’ah wat-Tashyi’’:

«Baada ya utafiti mkubwa nilioufanya katika kulichambua tatizo hili la hitilafu kubwa iliyopo baina ya Shia Ithanaashariyah na Ahlus Sunnah, nimegundua kuwa yale yaliyotokea baada ya kufariki kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) siyo sababu ya hitilafu hii kubwa, wala si kwa sababu ya kuwa ‘Aliy ndiye anayestahiki ukhalifa baada ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), kwa sababu nawaona wenye kufuata madhehebu ya Shia Zaydiyah wapo kwa mamilioni katika ulimwengu na wanaishi kwa wema na mapenzi na masikilizano baina yao na  Masunni.

Kwa hivyo sababu ya hitilafu baina ya Shia Ithnaashariyah na Madhehebu mengine ya Kiislamu ni ule msimamo wao dhidi ya Makhalifa walioongoka na kuwatukana kwao na kuwalaani, jambo ambalo halipo upande wa Shia Zaydiyah na makundi mengine. Lau kama Shia Ithnaashariyah walingelifuata mwenendo wa Shia Zaydiyah basi hitilafu ingelipungua sana na tatizo lingekuwa dogo. Lakini Shia Ithnaashariyah wameingia katika shimo la kuwatukana Makhalifa walioongoka na kuwalani na kuwashambulia,  jambo linalosababisha hitilafu hii izidi na kuongezeka.»

Ash-Shi’ah wat-Tashyi’. Uk.4

 

Kutokana na maelezo haya ya Maulamaa wa Kishia, inatubainikia kuwa laiti kama wafuasi wa Shia wangeliacha mwenendo wa kuwatukana na kuwalaani Masahaba wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) pamoja na wake zake Mama wa Waislamu, na lau kama wataacha mwenendo wa kuwatukana na kuwalaani Waislamu wenzao katika siku za Muharram na kuwaapiza kwa kula kiapo kuwa lazima watalipa visasi vya kuuliwa kwa Al-Husayn, basi sehemu kubwa ya chuki baina ya makundi mawili haya yangeondoka.

 

Masunni wanawaheshimu sana na kuwatukuza watu wote wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na wanawaheshimu pia Masahaba wake (Radhiya Allaahu ‘anhum), na wanaamini kuwa wao ni watu bora ambao Allaah Ameridhika nao, kama ilivyoandikwa katika Qur-aan tukufu.

Masunni wanajitenga na kila aliyeshiriki katika vile vita vilivyosababisha kuuliwa kwa Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhu), na wanajitenga na wote waliomuua na waliosababisha kuuliwa kwa Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhu) na aila yake, na wanaamini kuwa wameuliwa kwa dhulma na kwa uadui, na kwamba wote wamekufa Shahiyd.

 

Masunni wanashangazwa wanaposikia vilio na maneno ya kulipwa visasi katika vikao vya Al-Husayniyah يا لتارات الحسين. Wanajiuliza; visasi hivyo watalipiwa nani wakati wote waliomuua Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhu) wamekwishafariki dunia.

 

Al Hurr bin Yazid At-Tamimiy keshakufa, Shumar bin Dhil Jawshan keshakufa, Zara'a bin Shariyk keshakufa, ‘Umar bin Sa’ad  keshakufa, UbayduAllaah bin Ziyad naye pia keshakufa, na wote walioshiriki katika vita vile wamekwisharudi kwa Mola wao tokea miaka elfu moja mia nne iliyopita.

Maneno haya ya kutaka kulipa visasi yanatafsiriwa na Ahlus Sunnah kuwa wao ndio wanaokusudiwa, na haya ni katika chuki zilizopandikizwa na wasiopenda kuwaona Waislamu wa kila  Madhehebu wanapendana na kushirikiana katika kuziendeleza mbele dola zao.

 

 

Share

03-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Nani Ahlul-Bayt

 

Nani Ahlul-Bayt?

 

 

Mojawapo ya hitilafu kubwa baina ya Sunnah na Shia ni juu ya tafsiri ya neno 'Ahlul Bayt'. (Watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

Wakati Shia wanasema kuwa Ahlul Bayt ni ‘Aliy bin Abi Twaalib na Faatwimah binti Muhammad na wanawe (Radhiya Allaahu anhum) peke yao, Ahlus Sunnah wanaitakidi kuwa Ahlul Bayt ni wote hao waliotangulia kutajwa pamoja na wake wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na binti zake waliobakia wasiotambuliwa na Shia, na pia wajukuu zake na baadhi ya waliohusiana naye katika ukoo wake.

Imeandikwa katika kamusi maarufu "Lisaanul Arab" kuwa; mke na jamaa za mtu ni Ahli Bayti yake.

Na katika Qur-aan tukufu, Allaah Anawataja wake wa mtu kuwa ni Ahli yake.

Allaah Anasema:

 

قَالُواْ أَتَعْجَبِينَ مِنْ أَمْرِ اللّهِ رَحْمَتُ اللّهِ وَبَرَكَاتُهُ عَلَيْكُمْ أَهْلَ الْبَيْتِ إِنَّهُ حَمِيدٌ مَّجِيدٌ

 

"Wakasema: Je, unastaajabia amri ya Allaah? Rehema ya Allaah na baraka Zake ziko juu yenu, enyi watu wa nyumba hii! Hakika Yeye ndiye Msifiwa wa kutukuzwa." Huud-73

 

Maulamaa wote wanasema kuwa neno (Watu wa nyumba), katika aya hii anakusudiwa Sarah mke wa Nabii Ibraahiym ( ‘Alayhis Salaam).

 

Na Akasema:

إِذْ رَأَى نَارًا فَقَالَ لِأَهْلِهِ امْكُثُوا إِنِّي آنَسْتُ نَارًا

 

"Alipouona moto, akawaambia watu wake (Ahli yake): Ngojeni! Mimi nimeuona moto." Twahaa-10

 

Inajulikana hapa pia kuwa neno (Ahli yake) anakusudiwa mke wa Nabi Musa (Alayhis Salaam) aliyekuwa amefuatana naye katika safari hiyo.

 

Na Allaah Akasema pia:

 

قَالَتْ مَا جَزَاء مَنْ أَرَادَ بِأَهْلِكَ سُوَءًا إِلاَّ أَن يُسْجَنَ أَوْ عَذَابٌ أَلِيمٌ

 

 "Hapana malipo ya mwenye kutaka kumfanyia maovu mkeo isipokuwa kufungwa au kupewa adhabu iumizayo." Yuusuf-25

Neno (Ahlika katika aya hii) na maana yake ni 'mkeo' aliyekusudiwa ni mke wa Al-Aziz.

 

Kwa hivyo dalili zote zinaonyesha kuwa neno Ahlul Bayt au Ahl linatumika zaidi kwa maana ya mke.

Na katika Surat Al-Ahzaab kuanzia aya ya 28 hadi ya 33 Allaah Anasema:

 

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ إِن كُنتُنَّ تُرِدْنَ الْحَيَاةَ الدُّنْيَا وَزِينَتَهَا فَتَعَالَيْنَ أُمَتِّعْكُنَّ وَأُسَرِّحْكُنَّ سَرَاحًا جَمِيلًا، وَإِن كُنتُنَّ تُرِدْنَ اللَّهَ وَرَسُولَهُ وَالدَّارَ الْآخِرَةَ فَإِنَّ اللَّهَ أَعَدَّ لِلْمُحْسِنَاتِ مِنكُنَّ أَجْرًا عَظِيمًا

 

"Ewe Nabii! Waambie wake zako: Ikiwa mnataka maisha ya dunia na pambo lake, basi njooni, nitakupeni kitoka nyumba, na kukuacheni mwachano mzuri.

 

Na ikiwa mnamtaka Allaah na Mtume Wake na nyumba ya Akhera, basi Allaah Amewaandalia wafanyao mema, miongoni mwenu, malipo makubwa."

 

يَا نِسَاء النَّبِيِّ مَن يَأْتِ مِنكُنَّ بِفَاحِشَةٍ مُّبَيِّنَةٍ يُضَاعَفْ لَهَا الْعَذَابُ ضِعْفَيْنِ وَكَانَ ذَلِكَ عَلَى اللَّهِ يَسِيرًا، وَمَن يَقْنُتْ مِنكُنَّ لِلَّهِ وَرَسُولِهِ وَتَعْمَلْ صَالِحًا نُّؤْتِهَا أَجْرَهَا مَرَّتَيْنِ وَأَعْتَدْنَا لَهَا رِزْقًا كَرِيمًا

 

"Enyi wake wa Nabii! Atakayefanya uchafu dhaahiri miongoni mwenu, atazidishiwa adhabu mara mbili. Na hayo kwa Allaah ni mepesi.

Na miongoni mwenu atakeyemtii Allaah na Mtume Wake, na akatenda mema, tutampa malipo yake mara mbili, na tutamwandalia riziki ya ukarimu."

 

يَا نِسَاء النَّبِيِّ لَسْتُنَّ كَأَحَدٍ مِّنَ النِّسَاء إِنِ اتَّقَيْتُنَّ فَلَا تَخْضَعْنَ بِالْقَوْلِ فَيَطْمَعَ الَّذِي فِي قَلْبِهِ مَرَضٌ وَقُلْنَ قَوْلًا مَّعْرُوفً

 

"Enyi wake wa Nabii! Nyinyi si kama yeyote katika wanawake wengine. Kama mnamcha Mungu basi msiregeze sauti zenu, akaingia tamaa mwenye maradhi katika moyo wake. Na semeni maneno mema."

 

وَقَرْنَ فِي بُيُوتِكُنَّ وَلَا تَبَرَّجْنَ تَبَرُّجَ الْجَاهِلِيَّةِ الْأُولَى وَأَقِمْنَ الصَّلَاةَ وَآتِينَ الزَّكَاةَ وَأَطِعْنَ اللَّهَ وَرَسُولَهُ إِنَّمَا يُرِيدُ اللَّهُ لِيُذْهِبَ عَنكُمُ الرِّجْسَ أَهْلَ الْبَيْتِ وَيُطَهِّرَكُم تَطْهِيراً ْ     

 

"Na kaeni majumbani kwenu, wala msijishauwe kwa majishauwo ya kijahilia ya kizamani. Na shikeni Swalah, na toeni Zakaah, na mtiini Allaah na Mtume Wake. Hakika Allaah anataka kukuondoleeni uchafu, enyi Watu wa Nyumba (ya Mtume), na kukusafisheni baarabara."

 

Ahlus Sunnah wanasema kuwa; kama vile katika aya zote zilizotangulia, kila anapotajwa Ahli ya mtu hukusudiwa mke, na katika aya hizi pia Allaah Anapotaja Ahli Anawakusudia wake zake Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

Ukizisoma kwa utulivu aya hizi utaona kuwa kuanzia aya ya 28 Allaah Anazungumza na wake wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam):

 

Allaah Anasema: "Ee Nabii! Waambie wake zako….”, Akaendelea: "Enyi wake wa Nabii! Nyinyi si kama yeyote katika wanawake wengine.”

Akaendelea kuwahutubia: «Kaeni majumbani mwenu» «Toeni Zakaah». «Mtiini Allaah».

Mpaka Aliposema: "Hakika Allaah Anataka kukuondoleeni uchafu, enyi Watu wa Nyumba (ya Mtume), na kukusafisheni baarabara."

Yote haya wanaambiwa wake zake Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kuanzia aya ya 28 hadi 33.

Hivi ndivyo ulivyo mfumo wote wa aya hizi zilizokamatana na haziwezi kutenganishwa isipokuwa kama mtu anataka kuvuka mipaka na kwenda kinyume na nassi.

 

Mtu anaweza kuuliza: ‘Kwa nini basi Allaah Ametumia ‘sigha’ (mfumo wa maneno) ya wingi wa wanaume na wanawake kwa pamoja Aliposema:

إِنَّمَا يُرِيدُ اللَّهُ لِيُذْهِبَ عَنكُمُ ‘Ankum’

Ikiwa Amewakusudia wake za Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kwa nini asitumie sigha ya wanawake peke yao Akasema:

 

إِنَّمَا يُرِيدُ اللَّهُ لِيُذْهِبَ عَنكُن  ‘Ankunnaُ

 

Kwa nini Asitumie sigha ya wanawake kama Alivyotumia katika aya nyingine zilizomo ndani ya mfumo huu?

 

Majibu ni kuwa; Aya za mwanzo Allaah Alipozungumza juu ya hukmu za kisheria na makatazo na maamrisho yanayowahusu wake za Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alitumia ‘Nuun’ ya wanawakeعنكن  ‘Ankunna’ lakini Alipozungumza juu ya wema anaotaka kuuingiza ndani ya nyumba ile pamoja na kuwasafisha watu wa nyumba ile barabara, Alimuingiza pia na mwenye nyumba ambaye ni mwanamume naye ni Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ili kheri hiyo iwaenee wote. Na kawaida katika Lugha ya Kiarabu wanapotajwa wanawake na wanaume kwa pamoja hutumiwa wingi wa wanaume عنكم ‘Ankum’

 

Nani wanaostahiki zaidi kusafishwa na kutakaswa kuliko wake zake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), watu wa nyumba yake, mama wa Waislamu, na wanaostahiki pia ni jamaa zake, watu wa aila yake. Kwa sababu Mtume wetu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) anastahiki kuwa pamoja na kila kheri na kila jema na kila kilicho bora, na anastahiki zaidi kuwa pamoja na watu wema, naye haridhiki isipokuwa awe pamoja na watu wema, kwani wema lazima siku zote uwe katika mtiririko mmoja.

 

Na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Alitaka kuwatakasa wake zake na jamaa zake, akamtunukia haya Mtume wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

 

Ikiwa tumemkubali mke wa Nabii Muusa (‘Alayhis Salaam) katika aya tuliyotangulia kuitaja kuwa ni Ahli yake na tukamkubali mke wa Al-‘Aziz kama ilivyokuja katika aya kuwa ni Ahli yake na tukamuingiza Sarah mke wa Nabii Ibraahiym (‘Alayhis Salaam) kuwa ni Ahli yake, juu ya kuwa katika aya ile Allaah Alitumia mfumo ule ule wa wingi wa wanaume na wanawake kwa pamoja Aliposema:

 

رحمة الله وبركاته عليكم أهل البيت

Alitumia neno (عليكمAlaykum)

 

Kama alivyotumia (عنكم Ankum) katika Suratul Ahzaab Aliposema:

 

إِنَّمَا يُرِيدُ اللَّهُ لِيُذْهِبَ عَنكُمُ الرِّجْسَ أَهْلَ الْبَيْتِ

 

Ikiwa tumewakubali wake wa Mitume wote hao kuwa ni watu wa nyumba, tunalazimika pia kuwakubali wake wa Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kuwa ni watu wa nyumba yake.

 

 

Share

04-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Hadithi Ya Shuka Na Dalili Katika Hadithi

 

Hadithi Ya Shuka Na Dalili Katika Hadithi

 

Kutokana na haya inafahamika zaidi tafsiri ya ile hadithi maarufu inayoitwa Hadiyth al-Kisaa na maana yake ni hadithi ya nguo au hadithi ya shuka, wakati Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alipowaingiza ndani ya shuka ile ‘Aliy na Bibi Faatwimah na Al-Hasan na Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhum), kwa ajili ya kuwaingiza na wao katika zile baraka zilizoteremshwa ndani ya aya ile ya Suratul Ahzaab.

Hadithi inasimulia kuwa baada ya kuwaingiza wote hao ndani ya shuka, akasema:

 

"أللهمَّ هؤلاء أهل بيتي فاذهب عنهم الرجس وطهرهم تطهيراً

 

"Mola wangu hawa ni watu wa nyumba yangu, waondolee uchafu na uwasafishe baarabara."

Na Ummu Salamah (Radhiya Allaahu ‘anha) mke wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alipoingiza kichwa chake ndani ya shuka hiyo akasema:

"Ewe Mtume wa Allaah na mimi ni katika watu wa nyumba yako.»

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamuambia:

 

تنحي فإنك على خير

 

"Wewe umo katika kheri wewe umo katika kheri."

 

Na maana yake ni kuwa Ummu Salamah na wake wenzake wote wamekwishatajwa na Allaah katika aya hiyo na kwamba wao wamo katika kheri hiyo ya kusafishwa na kutakaswa.

Ndiyo maana akaambiwa:

"Wewe umo katika kheri wewe umo katika kheri."

 

Dalili nyingine inayothibitisha kuwa wake wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ni katika watu wa nyumba yake imo katika Al-Bukhaariy na Muslim na At-Tirmidhiy na An-Nasaaiy na wengine kama ilivyopokelewa kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alipoulizwa na Masahaba:

"Vipi tukuswalie?

Akasema:

"Semeni:

 

اللهم صل على محمد وأزواجه وذريته، كما صليت على إبراهيم، وبارك على محمد وأزواجه وذريته، كما باركت على آل إبراهيم إنك حميد مجيد

 

"Mola wangu mswalie Muhammad na wake zake na vizazi vyake, kama ulivyomswalia Ibraahiym, na umbariki Muhammad na wake zake na vizazi vyake kama ulivyowabariki watu wa nyumba ya Ibraahiym hakika Wewe ni Mwenye kuhimidiwa uliye Mtukufu."

 

Ikajulisha kuwa mke wa mtu na vizazi vyake ni watu wa nyumba yake.

 

Ikiwa mtu hajatoshelezwa na dalili zote tulizozinukuu kutoka katika kitabu cha Allaah na mafundisho ya Mtume wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), basi ipo dalili nyingine katika Sahih Al-Bukhaariy itakayoondoa shaka yoyote iliyobaki kwa mwenye kuutafuta ukweli bila ya chuki moyoni mwake.

Inajulikana kuwa Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha) mke wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alisingiziwa uwongo katika kisa mashuhuri kinachojulikana kwa jina la Haadithatul Ifk, uwongo ambao Allaah aliteremsha aya katika Qur-aan tukufu kuukanusha, na wakati huo huo aya hizo ziliwaonya Waislamu kutorudia tena kueneza uvumi huo, na zikawatahadharisha juu ya adhabu kali itakayomfikia mwenye kurudia tena.

 

Wakati ule Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alipanda juu ya mimbari yake kuhutubia, akasema:

 

"يا معشر المسلمين من يعذرني من رجل قد بلغني أذاه في أهلي، فواللّه ما علمت على أهلي إلا خيراً، ولقد ذكروا رجلاً ما علمت عليه إلا خيراً، وما كان يدخل على أهلي إلا معي"

 

“Enyi Waislamu! Nani atakayenipumzisha na mtu aliyeniudhi katika Ahli yangu, kwani WAllaahi sijaona kwa Ahli yangu isipokuwa kheri tupu, na hakuwa akiingia kwa Ahli yangu isipokuwa akiwa pamoja nami.” Al-Bukhaariy

 

Atakayechunguza, ataona kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amelitaja neno أهلي Ahliy (watu wa nyumba yangu) katika hotuba hii fupi mara tatu, zote zikimaanisha mkewe Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu anha), ikituthibitishia kuwa neno أهلي Ahliy lina maana ya mke.

 

Sisi tunawakubali na tunawapenda na tunawapa heshima kubwa na tunawatambua watu wote wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), wale wanaokubaliwa na Shia na pia wasiokubaliwa na Shia kuwa ni katika Ahlul Bayt kama vile ‘ami zake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), watoto wa ami zake pamoja na watoto wao (Radhiya Allaahu anhum), hawa ambao Shia hawawatambui kuwa ni watu wa nyumba yake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), kama walivyotajwa katika hadithi iliyotangulia, nao ni kama ifuatavyo:

 

1.     Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam)

2.     Wake zake

3.     Binti zake wote

4.     Watu wa nyumba ya Al-‘Abbaas bin Abdilmuttalib

5.     Watu wa nyumba ya Aqiyl bin Abi Twaalib

6.     Watu wa nyumba ya ‘Aliy bin Abi Twaalib

 

7.     Watu wa nyumba ya Ja’afar bin Abi Twaalib

 

 

Hawa wote wametajwa katika hadithi iliyotolewa na Muslim wakati Zayd bin Al-Arqam (Radhiya Allaahu ‘anhu) alipoulizwa:

 

‘Wake zake si katika watu wa nyumba yake?’

Akasema:

‘Wake zake ni watu wa nyumba yake. Lakini watu wa nyumba yake (waliokusudiwa hapa) ni wale walioharimishwa kupokea sadaka.’

Akaulizwa:

‘Nani hao.

Akasema:

‘Hao ni watu wa nyumba ya ‘Aliy na watu wa nyumba ya ‘Aqiyl na watu wa nyumba ya Ja’afar na watu wa nyumba ya ‘Abbaas (Radhiya Allaahu anhum).’

 

Kwa hiyvo watu wa nyumba hizo juu ya kuwa wengine hawakuwemo ndani ya ile shuka lakini wametajwa kuwa ni watu wa nyumba yake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

Wake zake bila shaka wanaingia katika watu wa nyumba yake kwa sababu ya kutajwa katika Suratul Ahzaab kama ilivyotangulia, na ndiyo maana katika kuikamilisha aya hiyo Allaah Akasema:

 

{ وَاذْكُرْنَ مَا يُتْلَى فِي بُيُوتِكُنَّ مِنْ آيَاتِ اللَّهِ وَالْحِكْمَةِ إِنَّ اللَّهَ كَانَ لَطِيفاً خَبِير}

 

‘Na watajieni (watu) yasomwayo majumbani mwenu katika Aya za Allaah na hikima (ya Mtume), kwa hakika Allaah ni Mjuzi wa mambo ya siri na Mjuzi wa mambo ya dhahiri.’ Al-Ahzaab-34

 

Na maana yake ni kuwa zifanyieni kazi zile aya zilizoteremshwa ndani ya nyumba zenu, kwa sababu Allaah amezihusisha nyumba zenu kwa kuteremsha aya Zake, tofauti na nyumba nyingine. Na Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu anha) ndiye anayehusika zaidi kwa sababu hazikupata kuteremshwa aya juu ya kitanda cha yeyote miongoni mwa wake wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) isipokuwa kwake.

 

Na watoto na wajukuu wa Al-Hasan  bin ‘Aliy na Al-Husayn bin ‘Aliy na Abdullaah bin ‘Abbaas na Muhammad bin Al-Hanafiyah (mtoto wa ‘Aliy kwa mke mwengine), na Al-‘Abbaas bin ‘Aliy na wajukuu zao na wajukuu wa wajukuu zao, wote hao pia ni miongoni watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na hii ni kwa wale waliokuwa Waislamu.

 

Abu Lahab juu ya kuwa ni ami yake Mtume (Swalla Allaahu alayhi wa sallam), lakini yeye hayumo katika Ahli yake kwa sababu hakuwa Muislamu.

Nabii Nuuh (‘Alayhis Salaam) allipomuona mwanawe amekimbilia jabalini na maji yanaanza kumfikia alimuomba Allaah amuokowe.

Allaah Anasema :

 

وَنَادَى نُوحٌ رَّبَّهُ فَقَالَ رَبِّ إِنَّ ابُنِي مِنْ أَهْلِي وَإِنَّ وَعْدَكَ الْحَقُّ وَأَنتَ أَحْكَمُ الْحَاكِمِينَ {45}‏ قَالَ يَا نُوحُ إِنَّهُ لَيْسَ مِنْ أَهْلِكَ إِنَّهُ عَمَلٌ غَيْرُ صَالِحٍ فَلاَ تَسْأَلْنِ

مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ إِنِّي أَعِظُكَ أَن تَكُونَ مِنَ الْجَاهِلِينَ {46

 

“Na Nuuh alimuomba Mola wake akasema: ‘Ewe Mola wangu! Mwanangu ni katika watu wa nyumbani kwangu. Na hakika ahadi yako ni haki. Nawe ni Mwenye haki kuliko mahakimu (wote).

Akasema (Allaah), “Ewe Nuuh! Huyu si miongoni mwa watu wako. Yeye ni (mwenye) mwendo usiokuwa mzuri. Basi usiniombe ambayo huyajui mimi nakunasihi usiwe miongoni mwa wajinga.” Huud-45-46

 

Allaah Alimkatalia na kumuambia kuwa huyo si mwanawe, wala si katika watu wa nyumba yake kwa sababu ya kuukanusha ujumbe aliokuja nao Nabii Nuuh (‘Alayhis Salaam).

 

Shia hawakubali kuwaingiza wengine isipokuwa wale tu waliotajwa katika hadithi ya shuka pamoja na Maimamu kumi na mbili waliofuata wa madhehebu ya Ithnaashariyah kwa sababu wanaamini kuwa hao ndio viongozi wa Waislamu waliotakaswa wasiotenda makosa watakaowaongoza Waislamu baada ya kufa kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) mpaka Siku ya Qiyaamah.

 

Share

05-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Mapenzi Yetu Kwa Ahlul-Bayt

 

Mapenzi yetu kwa Ahlul Bayt

 

 1-   Watu wa Ukoo

 

Ahlus Sunnah wanawapenda na kuwaheshimu watu wa ukoo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na wamewaweka katika daraja ya juu wanayoistahiki.

Hawa ni binti zake wote, pamoja na Bibi Faatwimah na wanawe Al-Hasan na Al-Husayn na watu wa ukoo wake tuliotangulia kuwataja kuwa ni katika Ahlul Bayt wakiwemo ‘Aliy bin Abi Twaalib na watu wa nyumba yake, na Al-‘Abbaas bin Abdil-Muttwalib na watu wa nyumba yake, na ‘Aqiyl bin Abi Twaalib na watu wa nyumba yake na Ja’afar bin Abi Twaalib na watu wa nyumba yake (Radhiya Allaahu ‘anhum).

Allaah Amewaondolea uchafu na kuwasafisha barabara watu hawa na Akatuamrisha katika kitabu chake kitukufu kuwapenda, na pia Mtume wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ametuamrisha tuwapende.

Katika Sahih Muslim imeelezwa kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alipowahutubia watu mahali panapoitwa Ghadiyr aliwaambia:

 

{ وأهل بيتي، أذكركم الله في أهل بيتي، أذكركم الله في أهل بيتي }.

 

«Na watu wa nyumba yangu. Nakukumbusheni Allaah juu ya watu wa nyumba yangu, Nakukumbusheni Allaah juu ya watu wa nyumba yangu.» Muslim

 

Allaah Anasema:

 

((إِنَّ اللَّهَ وَمَلائِكَتَهُ يُصَلُّونَ عَلَى النَّبِيِّ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا صَلُّوا عَلَيْهِ وَسَلِّمُوا تَسْلِيمًا))

 

«Hakika Allaah na Malaika wake wanamswalia Nabii. Enyi mlioamini! Mswalieni na mumsalimu kwa salamu» Al-Ahzaab -56

 

Ilipoteremshwa aya hii Masahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) walimuuliza Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam):

 

«Vipi tukuswalie?»

Akawaambia:

«Semeni:

 

{اللهم صل على محمد وعلى آل محمد، كما صليت على إبراهيم وعلى آل إبراهيم إنك حميد مجيد، وبارك على محمد وعلى محمد، كما باركت على إبراهيم وعلى آل إبراهيم إنك حميد مجيد}.

 

Mola wangu Mswalie Muhammad na Aali ya Muhammad, kama ulivyomswalia Ibraahiym na aali ya Ibraahiym hakika Wewe ni Msifiwa na Mwenye kutukuzwa. Na umbariki Muhammad kama ulivyombariki Ibraahiym na aali ya Ibraahiym hakika Wewe ni Msifiwa na Mwenyeye kutukuzwa.”

 

Anasema Ibnul Qayyim katika kuisherehesha hadithi hii:

Kuwaswalia Aali zake ni katika kukamilisha kumswalia Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kwa sababu kufanya hivyo ni katika kumfurahisha Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na Allaah Anamuongezea daraja na heshima (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

 

Imepokelewa kuwa Abu Bakr Asw-Swiddiyq (Radhiya Allaahu anhu) alisema:

 

[[ارقبوا محمداً في آل بيته]].

 

“Mpeni heshima Muhammad kwa (kuwaheshimu) watu wa nyumba yake.”

 

Na alisema pia:

 

[[والله لأن أَصِلَ قرابة رسول الله صلى الله عليه وسلم أحب إلي من أصل قرابتي]]

 

“WaAllaahi, kuwasiliana na jamaa zake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ni bora kwangu kuliko kuwasiliana na jamaa zangu.” Al-Bukhaariy

 

Na ile hadithi isemayo: « Faatwimah ni Bibi wa wanawake wa Peponi.»

Imepokelewa kutoka kwa Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha).

 

Imepokelewa pia kuwa siku ile Abu Sufyaan alipokuja kusilimu mbele ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), ‘Umar bin Khattwaab (Radhiya Allaahu ‘anhu) alimuambia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam):

 

«Huyu hapa Abu Sufyaan amekuja mwenyewe kwa miguu yake, niruhusu nimkate kichwa chake».

Al-‘Abbaas (Radhiya Allaahu anhu) ami yake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akasema:

«Ewe Mtume wa Allaah mimi namuingiza Abu Sufyaan katika himaya yangu.»

Al-‘Abbaas akakaa karibu na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na alipomuona ‘Umar (Radhiya Allaahu anhu) anashikilia kutaka kumkata kichwa Abu Sufyaan, Al-‘Abbaas akamuambia:

«Taratibu ewe Umar angelikuwa huyu ni katika watu wa kabila lako la Bani ‘Uday bin Ka’ab usingelishikilia namna hii, lakini kwa vile huyu ni mtu (wa kabila langu) anayetokana na ukoo wa Abdu Manaf.»

Umar akasema kumuambia Al-‘Abbaas (Radhiya Allaahu anhum):

«Taratibu ewe ‘Abbaas, kwani WaAllaahi naapa kuwa siku uliyosilimu wewe ilikuwa bora kwangu kuliko angelisimu baba yangu Al-Khattaab, kwa sababu naelewa kuwa kusilimu kwako kulimfurahisha sana Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).» At-Twabaraaniy, Al-Bidaayah wan- Nihaayah- Ibni Kathiyr na Siyrat Ibn Hishaam

 

Hadithi hizi na nyingi nyingine zinatufundisha namna gani watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) walivyokuwa wakiwapenda Masahaba, na pia Masahaba walivyokuwa wakiwapenda watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na zinatufundisha pia namna gani Ahlus Sunnah walivyojishughulisha kuzitafuta na kuziandika hadithi zinazowahusu watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

 

Masahaba na pia ‘Tabi’iyna’ (waliokuja baada yao) walijishughulisha sana kutafuta na kuziandika fadhila za watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ili watakaokuja baada yao wazijuwe na kuzichunga na kuzifuata. Na hii ndiyo sababu utakaposoma kitabu chochote katika vitabu vya Ahlus Sunnah hukosi kuona ndani yake mlango maalum uliohusishwa kwa ajili ya sifa za Ahlul Bayt. Utayakuta haya katika vitabu vya Hadiyth na vitabu vya ‘Aqiydah na hata katika vitabu vya Tariykh ‘historia’.

Imam Al-Bukhaariy kwa mfano, amehusisha mlango maalum juu ya fadhila za Imam ‘Aliy (Radhiya Allaahu anhu), na amehusisha mlango wa fadhila za Bibi Faatwimah (Radhiya Allaahu ‘anha) n.k.

 

Imam Muslim katika mlango wa Fadhila za Masahaba ameandika juu ya fadhila za Maimaam Al-Hasan na Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhum).

Imam At-Tirmidhy na Ibni Maajah na Imam Ahmad bin Hanbal na Ibni Kathiyr na At-Twabariy na Ibni Taymiyah na Adh-Dhahabiy na wengine, wote hawa katika vitabu vyao wameandika kwa mapana na marefu juu ya fadhila za Maimam hawa wawili ambao Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amewaita ‘Mabwana wa vijana wa Peponi.’

Hizi zote ni dalili wazi juu ya heshima tunayowapa watu wa nyumba hii tukufu (Radhiya Allaahu ‘anhum).

 

Share

06-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Elimu Ya Ghaibu Na Kukingwa

Elimu Ya Ghaibu Na Kukingwa

 

Sisi tunawaheshimu na tunawaenzi watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), lakini hatuamini kama wanavyoamini Shia kuwa wao wanajua elimu ya Ghaibu na wamekingwa hawafanyi makosa n.k. Tunaamini kuwa mwenye kujua ghaibu ni Allaah Peke Yake.

 

Allaah Anasema:

 

قل لا يعلم من في السموات والأرض الغيب إلا الله" [النمل: 65]

 

Sema: “Hakuna aliyeko katika mbingu na ardhi ajuaye Ghayb (yasiyotokea) ila Allaah." An Naml-65

 

Na Akasema:

 

قل لا أملك لنفسي نفعا ولا ضرا إلا ما شاء الله ولو كنت أعلم الغيب لاستكثرت من الخير وما مسني السوء إن أنا إلا نذير وبشير لقوم يؤمنون

 

Sema: “Sina mamlaka ya kujipa nafuu wala ya kujindolea madhara ila Apendavyo Allaah; na lau kama ningelijua ghaibu ningejizidishia mema mengi; wala isingalinigusa dhara. Mimi si chochote ila ni muonyaji na mtoaji wa habari njema kwa watu wanaoamini.” Al-A’araaf-188

 

Na tunaamini kuwa aliyekingwa ni Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) peke yake.

 

Allaah Anasema:

 

وَاللّهُ يَعْصِمُكَ مِنَ النَّاسِ

 

Na Allaah Amekukinga Al-Maidah-67

 

Sisi tunaamini kuwa hapana yeyote aliyekingwa (Ma’aswuum معصوم), si katika watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) wala katika Masahaba wake, kwa sababu zifuatazo:

 

1.     Hapana nassw iliyo wazi isiyopingika inayoeleza juu ya kukingwa kwao. Lau kama ingekuwepo basi tungelifuata bila matatizo wala kipingamizi.

 

2.     Hapana hata mmoja katika watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) aliyedai kuwa yeye amekingwa, akawataka watu waamini hivyo, isipokuwa katika vitabu ambavyo Maulamaa wote kama vile Ibni Kathiyr na Ibni Hajar na Adh-Dhahabiy na wengineo wamesema kuwa hadithi hizo si dhaifu tu, bali maudhui. (zimepachikwa).

 

3.     Hapana hata mwanachuoni mmoja katika Maulamaa wetu aliyesema hivyo, juu ya kukhitalifiana kwao katika mambo mengi, lakini juu ya jambo hili hapana hitilafu baina yao.

 

4.     Lau kama wangelikuwa wamekingwa, basi wasingelikubali kukosolewa na mtu yeyote katika Ijtihadi zao. Kwa mfano kama ‘Aliy (Radhiya Allaahu anhu) angelikuwa amekingwa, basi asingelikubali kukosolewa na Abu Bakr au ‘Umar au ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhum), na anapokosolewa angelisema kwa mfano; ‘Vipi mnanikosoa wakati mimi nimekingwa?’

Lakini ‘Aliy alikuwa akiwakosoa na wao walikuwa wakimkosoa, akiwaheshimu na wao wakimuheshimu, akiwapenda na wao wakimpenda.

 

5.     Maulamaa wanasema kuwa التطهير  ‘kusafishwa’ kama ilivyokuja katika aya, maana yake si kukingwa, bali ni kusafishwa na kutakaswa. Na  si kila aliyetakaswa amekingwa akawa hafanyi makosa, ama sivyo basi kila aliyesifiwa kuwa ametakaswa au amesafishwa atakuwa amekingwa. Kama ilivyokuja katika hadithi:

 

واجعلني من التوابين واجعلني من المتطهرين

 

Na unijaalie niwe miongoni mwa waliotubu na unijaalie niwe miongoni mwa wenye kujitakasa.

 

Na  Allaah Anawapenda wenye kutubu na Anawapenda wenye kujitakasa, lakini haimaanishi kuwa hao wamekingwa hawafanyi makosa.

 

6.     Kama Muislamu atachukua elimu yake kutoka katika Qur-aan na Mafundisho ya Mtume wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) peke yake bila ya kuchukua kutoka kwa watu wa Ahlul Bayt, huyo Uislamu wake unakuwa sahihi na hauna dosari yoyote. Wangelikuwa Ahlul Bayt wamekingwa ‘Ma’aswuumiyn’, basi ingelimuwajibikia kila Muislamu kuchukua elimu kutoka kwao.

 

7.     Kwetu Ahlus Sunnah, Abu Bakr na ‘Umar ni viumbe bora kupita wote  baada ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam). Na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) mara zote alikuwa akiwatanguliza mbele ya ‘Aliy. Alikuwa akimuacha Abu Bakr aswalishe na ‘Aliy akiswali nyuma yake, na hapana hata mmoja katika Ahlus Sunnah aliyewahi kusema kuwa Abu Bakr amekingwa (Ma’aswuum معصوم). Itakuwaje basi awe mwengine asiyekuwa yeye?

 

8.     Imepokelewa kuwa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) aliwasifia waliojitenga katika vita vya wenyewe kwa wenyewe, na alijuta kwa yaliyotokea katika vita vya ngamia na vita vya Swiffiyn. Angelikuwa amekingwa asingetenda matendo kisha akajuta.

 

9.     Imepokelewa kuwa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alipanda juu ya mimbari katika mji wa Al-Kuufa akasema:

«Namshitakia Allaah dhiki zangu na matatizo yangu.»  Kisha akasema:

«Wana daraja zao kwa Allaah Muhammad bin Maslamah na Usaamah bin Zayd na Sa’ad bin Abi Waqaas. Kama ni shari basi ndogo, na kama ni kheri basi ni nyingi (kwa kujitenga kwao na fitna).»

Naye ni mkweli (Radhiya Allaahu ‘anhu), lakini angelikuwa Ma’aswuuwm basi asingetamka haya. Asingewasifia waliojitenga na  fitna ile wakati yeye mwenyewe alikuwemo ndani yake.

 

10.             Siku ya Saqiyfah, siku ile baada ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kufariki dunia, wakati Waislamu walipojumuika na kumchagua Abu Bakr kuwa Khalifa wao, hapana hata mmoja aliyejitokeza akasema : «Jamani tunaye aliyekingwa hapa, kwa hivyo yeye ndiye anayestahiki kuchaguliwa.» Hilo halijatokea, na siku ile walikuwepo waliopigana vita vya Badr na pia walikuwepo wale ambao Allaah Alitangaza kuridhika nao chini ya mti. Inaingia akilini kweli kuwa watu wote hao waliosifiwa na Allaah ndani ya Qur-aan Tukufu, na wakasifiwa na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) wafanye njama dhidi ya Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam)?

 

 

Share

07-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Fadhila Za Ahlul-Bayt

 

Fadhila Za Ahlul-Bayt

 

Tunaweza kugawa fadhila za Ahlul Bayt katika mafungu mawili:

1.     Fadhila za ujumla

2.     Fadhila makhsusi

 

 

Kwanza Fadhila za ujumla

Fadhila za ujumla mfano wa hadithi ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) aliposema:

 

{ وأهل بيتي، أذكركم الله في أهل بيتي، أذكركم الله في أهل بيتي }.

 

«Na watu wa nyumba yangu. Nakukumbusheni Allaah juu ya watu wa nyumba yangu, Nakukumbusheni Allaah juu ya watu wa nyumba yangu.» Muslim

 

Na fadhila zilizotajwa katika Suratul Ahzaab:

 

إِنَّمَا يُرِيدُ اللَّهُ لِيُذْهِبَ عَنكُمُ الرِّجْسَ أَهْلَ الْبَيْتِ وَيُطَهِّرَكُمْ تَطْهِيراً

 

"Hakika Allaah anataka kukuondoleeni uchafu, enyi Watu wa Nyumba (ya Mtume), na kukusafisheni barabara."

 

Ndani yake fadhila hizi wanaingia wake wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kwa sababu wao ndio waliokusudiwa, na pia wanaingia ‘Aliy na Bibi Faatwimah na Al-Hasan na Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhum) kupitia hadithi ya Al-Kisaa.

Fadhila za ujumla zinapatikana pia katika kutoa shahada ndani ya Swalah wakati wa kusoma Tahiyatu, tunaposema:

 

اللهم صل على محمد وعلى آل محمد

 

"Mola wangu mswalie Muhammad na Aali yake Muhammad”

 

Na yote haya yanatokana na fadhila zao na daraja yao mbele ya Allaah.

 

Fadhila Makhsusi

Wafuatao ni baadhi ya watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na hawa ni Maimamu kumi na mbili wa Shia:

 

1. ‘Aliy bin Abi Twaalib

2. Al-Hasan

3. Al-Husayn

4. ‘Aliy bin Al-Husayn (Zaynul ‘Abidiyn)

5. Muhammad bin ‘Aliy bin Al-Husayn (Al-Baaqir)

6. Ja’afar Asw-Swaadiq

7. Musa Al-Kaadhwim

8. ‘Aliy Ar-Ridhwaa

9. Muhammad Al-Jawwaad

10. ‘Aliy Al-Haadiy

11. Al-Hasan Al-Askariy

12. Muhammad (Imamu wa kumi na mbili wanayemsubiri)

 

Hawa tunaweza kuwagawa makundi manne.

1-    Kundi la mwanzo ni Masahaba (waliomuona Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam)), nao ni ‘Aliy na Al-Hasan na Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhum).

2-    Kundi la pili ni Maulamaa wachaji Allaah miongoni mwa Maulamaa wa Ahlus Sunnah wal Jama’ah nao ni:

 

1- ‘Aliy bin Al-Husayn

2- Muhammad Al-Baaqir

3- Ja’afar Asw-Swaadiq

4- Muusa Al-Kaadhim

5- ‘Aliy Ar-Ridhwa

6- Muhammad Al-Jawwaad

 

3-    Kundi la tatu; hawa ni wachaji Allaah lakini si katika Maulamaa na inawatosha fahari ya kuwa wanatoka katika nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na wanayo haki ya kwenda penye kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na kusema:

‘Assalaam ‘alayka ewe baba yangu.’

Na hawa ni: ‘Aliy Al-Haadiy na Al-Hasan Al-Askariy.

4-    Sehemu ya nne ni mtu asiyezaliwa wanayemsubiri, naye ni Muhammad bin Al-Hasan.

 

 

‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu)

 

Wa mwanzo wao ni ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu) ambaye ni mtoto wa ‘ami yake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na mume wa Bibi wa mabibi wa Peponi Faatwimah (Radhiya Allaahu ‘anha) binti wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam). Na ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) ni Khalifa wa nne muongofu, na ni katika wale kumi waliobashiriwa kuingia Peponi.

Ndani ya Al-Bukhaariy na Muslim ipo hadithi kutoka kwa Abul ‘Abbaas Sahl bin Sa’ad As-Sa’idiy (Radhiya Allaahu ‘anhu), aliyesema kuwa siku ya vita vya Khaybar, Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alisema:

 

(لأعطين هذه الراية غدا رجلا يفتح الله على يديه، يحب الله ورسوله ويحبه الله ورسوله)

 

"Nitampa bendera hii kesho, mtu ambaye atatupa ushindi Allaah kwa mikono yake. (Mtu huyo) Anampenda Allaah na Mtume Wake na anapendwa na Allaah na Mtume Wake".

 

Anaendelea kusema Sahl (Radhiya Allaahu ‘anhu):

 

"Usiku kucha watu walikuwa wakiwaza wakitaka kujua ni nani huyo mwenye kupendwa na Allaah na Mtume Wake atakayepewa bendera hiyo. Asubuhi yake watu wote wakaamkia kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), kila mmoja akitamani apewe yeye bendera siku hiyo".

Baada ya watu kujikusanya mbele yake, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akauliza:

"Yuwapi ‘Aliy bin Abi Twaalib?...."

Al-Bukhaariy na Muslim

 

Na akasema pia (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) juu ya ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu):

 

لا يحبك إلا مؤمن، ولا يبغضك إلا منافق

 

«Hakupendi isipokuwa Muumini na hakuchukii isipokuwa mnafiki »

 

Na sisi Wallahi tunampenda na kumuenzi na kumheshimu yeye na mkewe na watoto wake wote (Radhiya Allaahu ‘anhum). Hadithi zake zimejaa ndani ya vitabu vyetu. Hekima yake tunaitumia na tunawafunza watoto wetu. Mashairi yake yaliyojaa mafunzo ya kheri na busara tunayasoma na kuyarudia na tunamfunza kila mmoja wetu.

 

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amesema pia:

 

{أما ترضى أن تكون مني بمنزلة هارون من موسى} وزاد مسلم: { إلا أنه لا نبي بعدي}

Al-Bukhaariy

«Hutoridhika ukiwa wewe kwangu upo katika daraja ya Haaruun kwa Muusa» na Muslim akaongeza: «Isipokuwa hapana Mtume baada yangu».

 

Hadithi zote hizi na nyingi nyingine zimo ndani ya vitabu vya Ahlus Sunnah zikituhakikishia kuwa hatuna uzito wowote kwetu katika kuzitaja au kuziandika ndani ya vitabu vyetu na hata kuzisema hadharani, bali ni fahari kwetu kufanya hivyo, kwa sababu hawa ni watu wa nyumba ya Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

 

 

Faatwimah (Radhiya Llahu ‘anha)

 

Bibi Faatwimah (Radhiya Llahu ‘anha) binti yake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam). Kipenzi chake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam). Manukato yake mazuri aliyesema juu yake :

 

{إن فاطمة بضعة مني يؤذيني ما آذاها}

 

«Hakika Faatwimah ni sehemu inayotokana na mimi kinaniudhi kinachomuudhi» Muslim

 

Na akasema kumuambia Faatwimah:

 

{أما ترضي أن تكوني سيدة نساء المؤمنين، أو سيدة نساء هذه الأمة}

 

«Huridhiki ukiwa wewe ni Bibi wa wanawake waumini, au Bibi wa wanawake wa umma huu»

 

Na katika Al-Bukhaariy:

 

فاطمة سيدة نساء أهل الجنة

 

« Faatwimah ni Bibi wa wanawake wa Peponi»

 

 

Al-Hasan na Al-Husayn

 

Tunawaheshimu na kuwapenda pia Al-Hasan na Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhum), na ndani ya vitabu vya Ahlus Sunnah utakuta maelezo mengi juu ya wajukuu hawa wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) aliyokuwa akitamka mbele ya Masahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum). Alikuwa akisema:

 

اللهم إني أحبهما فأحبهما

 

‘Mola wangu kwa hakika mimi ninawapenda na Wewe wapende’

At-Tirmidhiy

 

Na akasema:

 

الحسن والحسين سيدا شباب أهل الجنة

 

‘Al-Hasan na Al-Husayn ni mabwana wa vijana wa Peponi’

At-Tirmidhiy na Ahmad na Al-Haakim na wengine

 

 

Al-‘Abbaas bin ‘Abdil-Muttwalib (Radhiya Allaahu ‘anhu)

 

Huyu ni ‘ami yake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) aliyesema juu yake:

 

عم الرجل صنو أبيه

 

‘Ami yake mtu ni sawa na baba yake

At-Tirmidhiy

 

 

 

Abdullaah bin ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhuma)

 

Huyu ni mtoto wa ‘ami yake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) aliyemuombea dua nzuri aliposema:

 

{اللهم علمه التأويل وفقهه في الدين}

 

“Mola wangu mpe elimu ya kujua uhakika wa mambo na mjaalie awe na fiq-hi katika dini."

Ahmad

 

 

‘Aliy Zaynul ‘Aabidiyn (Radhiya Allaahu ‘anhu)

 

Huyu ni ‘Aliy bin Al-Husayn bin ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhum) ambaye amesema Imam Az-Zuhry juu yake:

 

‘Sijapata kumuona mtu kutoka kabila la Quraysh aliye bora kupita yeye.’

 

Na alisema Sa’iyd bin Musayib:

 

‘Sijapata kumuona mcha Mungu kupita huyu.’

  

 

Muhammad bin ‘Aliy bin Al-Husayn ‘Al Baaqir’ (Radhiya Allaahu ‘anhu)

 

Amesema juu yake Abu Na’iym:

 

‘Alikuwa mtu wa kuaminika, mwingi wa elimu na hadithi.’

 

 

Ja’afar bin Muhammad (Radhiya Allaahu ‘anhu)

 

Huyu ndiye Ja’afar Asw-Swaadiq bin Muhammad Al-Baaqir ambaye Imam Abu Hanifa alisema juu yake:

 

‘Sijapata kuona mtu mwenye elimu ya fiq-hi kupita Ja’afar bin Muhammad.’

 

Amesema pia juu yake Ibni Hibbaan :

 

‘Mwenye kuaminika asiye na mfano.’

 

Amesema Imam Adh-Dhahabiy :

 

« Imam Asw-Swaadiq ni Sheikh katika Masheikh wa Kikureshi anayetokana na ukoo wa Bani Hashim na ni miongoni mwa Maulamaa wao.»

 

 

Muusa bin Ja’afar ‘Al-Kaadhwim’ (Radhiya Allaahu ‘anhu)

 

Huyu ni mtoto wa Ja’afar Asw-Swadiq (Radhiya Allaahu ‘anhu)

Amesema juu yake Ibni Taymiyyah:

 

« Mashuhuri kwa kufanya ibada na kuhiji.»

 

Akasema Abu Haatim Ar-Raazi:

 

« Ni mwenye kutegemewa msemakweli, Imam katika maimamu wa Kiislamu.»

 

Amesema juu yake Ibni Kathiyr:

 

« Alikuwa mwingi wa kufanya ibada na mwenye kuheshimika.»

 

Anasema Adh-Dhahabiy katika ‘Siyar’ kuwa siku moja Haaruun Ar-Rashiyd alipokuwa katika Hija alikwenda mbele ya kaburi la Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na alikuwa pamoja naye katika safari hiyo Muusa bin Ja’afar Al-Kaadhwim (Radhiya Allaahu ‘anhu). Haaruun Ar-Rashiyd alipofika penye kaburi la Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akasema kwa ufahari mbele ya watu: “Assalaam ‘alayka ewe mtoto wa ‘ami yangu.” Haaruun Ar-Rashiyd anatokana na ukoo wa Al-‘Abbaas bin ‘Abdil Muttalib (Radhiya Allaahu ‘anhu). Muusa bin Ja’afar naye akasogea mbele ya kaburi hilo kisha akasema: “Assalaam ‘alayka ewe baba yangu.”

Uso wa Haaruun Ar-Rashiyd ulibadilika. Akamtizama kisha akamuambia: “Hili Wallahi ni la kujionea fahari.”

 

 

‘Aliy bin Muusa ‘Ar-Ridhwaa’

 

Amesema juu yake Ibni Hibbaan:

 

« Huyu ni miongoni mwa mabwana wa Ahlul Bayt na katika wenye hekima.»

 

Na Adh-Dhahabiy amesema juu yake :

 

« Alikuwa mwenye shani kubwa mwenye kustahiki ukhalifa.»

 

 

Muhammad bin ‘Aliy bin Muusa ‘Al-Jawwaad’

 

Amesema juu yake Ibni Taymiyyah:

«Alikuwa miongoni mwa watu wema na mkarimu sana, na kwa ajili hii alipewa jina la Al-Jawwaad. Na alikuwa mwenye kuheshimika sana.»

 

Yote haya yanabatilisha zile kauli kuwa Masunni hawawapendi watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

Alipotuhumiwa ‘Abdullaah mwana wa Imam Muhammad bin ‘Abdil-Wahaab kwamba alisema kuwa watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) hawana haki yoyote” akajibu:

“Subhana Allaah huu ni uongo mkubwa. Waliotuzulia haya au kutunasibisha nayo wamesema uongo mtupu juu yetu.”

 

Na hivi ndivyo ilivyo kwa wote wanaotokana na ukoo wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na pia wajukuu wote wa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu), wote tunawapenda bila kuwafarikisha na wote wamepewa sifa wanazozistahiki ndani ya vitabu vya Sunni ikiwa ni dalili wazi kuwa watu hawa tunawaenzi na kuwaheshimu.

 

Shia juu ya kudai kwao kuwa wanawapenda na kufuata mwenenendo wa watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), lakini ukweli ni kuwa wao wanawafarikisha na kuwatenga wengine. Kwa sababu watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kwao ni ‘Aliy na Faatwimah na Al-Hasan na Al-Husayn na watoto wao na wajukuu zao peke yao, na wengine wasiokuwa hao wamewatoa katika sifa hii.

‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alioa wake wengine akazaa nao watoto wengi, lakini Mashia hawahesabu watoto hao kuwa  ni Ahlul Bayt.

 

Watoto wengine wa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) kama vile Muhammad bin AlHanafiyah, Abu Bakr bin ‘Aliy, ‘Umar bin ‘Aliy na ‘Uthmaan bin ‘Aliy na ‘Abbaas, wote hawa ni watoto wa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu).

 

Wamewatoa pia mabinti wengine wa ‘Aliy kama walivyowatoa mabinti wengine wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), nao ni Zaynab na Ruqayah na Ummu Kulthum, kama walivyowatoa wake wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) hapo mwanzo.

 

 

 

Share

08-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Wake Zake

 

1-   Wake Zake

 

Sisi tunaamini kuwa wake wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ni katika watu wa nyumba yake, na kwamba wao ni mama zetu.

Allaah Anasema:

 

(( النَّبِيُّ أَوْلَى بِالْمُؤْمِنِينَ مِنْ أَنْفُسِهِمْ وَأَزْوَاجُهُ أُمَّهَاتُهُمْ )) [الأحزاب:6]

 

«Nabii ana haki zaidi kwa Waislamu kuliko nafsi zao.na wakeze ni mama zao.» Al-Ahzaab -6

 

Na Akaharamisha kuwaoa baada ya kufariki Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

 

Allaah Anasema:

 

(( وَمَا كَانَ لَكُمْ أَنْ تُؤْذُوا رَسُولَ اللَّهِ وَلا أَنْ تَنْكِحُوا أَزْوَاجَهُ مِنْ بَعْدِهِ أَبَدًا))

 

«Wala haikupasieni kumuudhi Mtume wa Allaah. Wala kuwaoa wake zake baada yake kabisa. Hakika jambo hilo ni dhambi kubwa mbele ya Allaah.» Al-Ahzaab-53

 

Tunawapa heshima kubwa mama zetu hawa, na wa mwanzo wao ni Bibi Khadiyjah (Radhiya Allaahu ‘anha). Wa mwanzo kuamini, aliyemsaidia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kwa hali na mali huku akimpa moyo na kumliwaza kila anapopatwa na masaibu au shida. Bibi Khadiyjah  (Radhiya Allaahu ‘anha) ndiye aliyeambiwa na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam):

 

"إن اللّه أمرني أن أبشر خديجة ببيت في الجنة لا صخب فيه ولا نصب"

 

“Allaah Ameniamrisha nimpe bishara njema Khadiyjah juu ya nyumba yake Peponi ya Lulu, hamna zogo ndani yake wala tabu (yoyote).” Al-Bukhaariy na Muslim

 

Na kutoka kwa ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amesema:

 

خير نسائها مريم بنت عمران، وخير نسائها خديجة بنت خويلد

 

«Mwanamke bora (katika zama zake) ni Maryam binti ‘Imraan, na mwanamke bora (katika zama zake) ni Khadiyjah binti Khuwaylid» Al-Bukhaariy na Muslim

 

 

Kisha anafuatia Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha), binti wa Abu Bakr Asw-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ‘anhu), Bibi aliyetakaswa kutoka mbingu ya saba baada ya mnafiki yule aliyejitwika sehemu yake kubwa katika uzushi wake ambaye ni ‘Abdullaah bin Ubay bin Saluul kueneza uvumi mbaya juu ya mama huyu wa Waislamu kipenzi cha Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam). Maulamaa wote wamekubaliana kuwa kumsingizia uongo bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha) katika kile kisa cha uongo alichozuliwa (hadithi ya "Al-Ifki") wakati Allaah kishamtakasa, basi anakuwa si Muislamu tena.

Allaah Anasema:

إِنَّ الَّذِينَ جَاؤُوا بِالْإِفْكِ عُصْبَةٌ مِّنكُمْ لَا تَحْسَبُوهُ شَرّاً لَّكُم بَلْ هُوَ خَيْرٌ لَّكُمْ لِكُلِّ امْرِئٍ مِّنْهُم مَّا اكْتَسَبَ مِنَ الْإِثْمِ وَالَّذِي تَوَلَّى كِبْرَهُ مِنْهُمْ لَهُ عَذَابٌ عَظِيمٌ {11} لَوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ ظَنَّ الْمُؤْمِنُونَ وَالْمُؤْمِنَاتُ بِأَنفُسِهِمْ خَيْراً وَقَالُوا هَذَا إِفْكٌ مُّبِينٌ {12} لَوْلَا

جَاؤُوا عَلَيْهِ بِأَرْبَعَةِ شُهَدَاء فَإِذْ لَمْ يَأْتُوا بِالشُّهَدَاء فَأُوْلَئِكَ عِندَ اللَّهِ هُمُ الْكَاذِبُونَ {13} وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ لَمَسَّكُمْ فِي مَا أَفَضْتُمْ فِيهِ عَذَابٌ عَظِيمٌ {14} إِذْ تَلَقَّوْنَهُ بِأَلْسِنَتِكُمْ وَتَقُولُونَ بِأَفْوَاهِكُم مَّا لَيْسَ لَكُم بِهِ عِلْمٌ وَتَحْسَبُونَهُ هَيِّناً وَهُوَ عِندَ اللَّهِ عَظِيمٌ {15} وَلَوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ قُلْتُم مَّا يَكُونُ لَنَا أَن نَّتَكَلَّمَ بِهَذَا سُبْحَانَكَ هَذَا بُهْتَانٌ عَظِيمٌ {16} يَعِظُكُمُ اللَّهُ أَن تَعُودُوا لِمِثْلِهِ أَبَداً إِن كُنتُم مُّؤْمِنِينَ {17وَيُبَيِّنُ اللَّهُ لَكُمُ الْآيَاتِ وَاللَّهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ {18} إِنَّ الَّذِينَ يُحِبُّونَ أَن تَشِيعَ الْفَاحِشَةُ فِي الَّذِينَ آمَنُوا لَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ وَاللَّهُ يَعْلَمُ وَأَنتُمْ لَا تَعْلَمُونَ {19} وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ وَأَنَّ اللَّه رَؤُوفٌ رَحِيمٌ {20}‏

 

"Hakika wale walioleta uongo huo (wa kumsingizia bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha) mkewe Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) [kuwa amezini] Ni kundi miongoni mwenu (ni jamaa zenu) msifikiri ni shari kwenu bali hiyo ni kheri kwenu. Kila mtu katika wao atapata aloyachuma katika madhambi yao na yule aliyejitwika sehemu yake kubwa miongoni mwao atapata adhabu kubwa (zaidi).

Kwa nini mlipo sikia khabari hii, wanaume Waumini na wanawake Waumini hawakuwadhania wenzao mema, na kusema: Huu ni uzushi dhaahiri?

Kwa nini hawakuleta mashahidi wane? Na ilivyo kuwa hawakuleta mashahidi wane basi hao mbele ya Allaah ni waongo.

Na lau kuwa si fadhila ya Allaah juu yenu na rehema yake katika dunia na

Akhera, bila ya shaka ingeli kupateni adhabu kubwa kwa sababu ya yale mliyo jiingiza. Mlipoupokea (uongo huo mkawa mnautangaza) kwa ndimi zenu na mkasema kwa vinywa vyenu msiyoyajua, na mlifikiri ni jambo dogo, kumbe mbele ya Allaah ni kubwa.

Na kwa nini mlipo yasikia msiseme: Haitufalii kuzungumza haya. Subhaanaka (Mola wetu) Umetakasika! Huu ni uzushi mkubwa!?

Allaah anakuonyeni msirudi kabisa (msirejee tena) kufanya kama haya, ikiwa nyinyi ni Waumini! (Waislamu) kweli.”

An-Nuur – 11-17

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) katika aya hizi Ametumia neno; ‘Subhaanaka katika kumtakasa Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha) kutokana na uongo aliozuliwa, na neno hili ‘Subhaanaka’ Allaah Analitumia katika kukanusha uongo mkubwa tu, Anaponasibishwa na mwana au mshirika.

Allaah Amesema:

 

سُبْحَانَكَ هَذَا بُهْتَانٌ عَظِيمٌ

 

“(Mola wetu) Umetakasika! Huu ni uzushi mkubwa!?”

 

Wamasema baadhi ya Wafasiri:

 

“Alipokanusha kuwa hana mwana wala mshirka alisema:

 

وَقَالُواْ اتَّخَذَ اللّهُ وَلَداً سُبْحَانَهُ بَل لَّهُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَالأَرْضِ كُلٌّ لَّهُ قَانِتُونَ

 

“Na wanasema:”Allaah amejifanyia mtoto” ‘Subhaanahu’ Ameepukana na hilo bali ni vyake hivyo vilivyomo mbinguni na ardhini . Vyote vinamtii Yeye.” Al-Baqarah-116

 

Na Akasema:

 

مَا كَانَ لِلَّهِ أَن يَتَّخِذَ مِن وَلَدٍ سُبْحَانَهُ

 

“Haiwi kwa Allaah kufanya mtoto; ‘Subhaanahu’ Ametakasika.” Maryam-35

 

Amelitumia neno ‘SubhaAnahu’ kwa ajili ya kujitakasa na kukanusha kuwa Anaye mwana, na Amelitumia neno hilo hilo ‘SubhaAnahu’ katika kuukanusha uongo aliozuliwa Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha).

 

Miongoni mwa wake wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) pia ni Ummu Salamah (Radhiya Allaahu ‘anha), mama yetu mtulivu wa tabia, mwenye akili yenye uwezo wa kupima mambo, mwingi wa hekima ambaye Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) mara nyingi alikuwa akichukuwa ushauri wake katika baadhi ya mambo. Alimshauri siku ile ya Sulhu ya Hudaybiyah na akapata ushauri mwema kutoka kwake.

Hawa na wake zake wengine wote ni mama zetu. Ni watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kama ilivyokuja katika aya za Surat al Ahzaab, na kama tulivyoona katika dalili mbali mbali kutoka katika Qur-aan tukufu na katika Mafundisho ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

Inatuwajibikia kuwapenda na kuwaenzi na kuwaheshimu mama zetu hawa.

 

Baada ya kumalizika vita vya Ngamia (Waqi'at al Jamal), ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) aliamua kumuacha huru Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha). Wafuasi wake wakamuuliza:

 

«Inakuwaje halali kumwaga damu zao na haiwi halali kwetu mali zao na mateka wao?»

‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) akasema:

«Yupi kati yenu atakayefurahi Mama wa Waislamu awe mateka wake?»

Wote wakanyamaza.

 

Ikiwa ni haramu kumsema vibaya Muislamu yeyote, basi inakuwa vibaya zaidi kuwasema vibaya watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) wakiwemo wake zake na watu wa ukoo wake pamoja na wajukuu wake na wajukuu wa wajukuu wakiwemo Al-Hasan na Al-Husayn na ‘Abdullaah bin Al-Hasan na ‘Aliy bin Al-Hasan na Muhammad bin ‘Aliy na Ja’afar bin Muhammad na Muusa bin Ja’afar na ‘Aliy bin Muusa Ar-Ridhwaa na waliobaki, na pia Sahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) wote kwa pamoja wa Makkah na wa Madiynah, na wale ambao Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amewabashiria Pepo, na pia viongozi wetu wa dini.

 

Haiwezekani ukapatikana umoja wa Waislamu ikiwa kundi lolote litakuwa shughuli yao kubwa ni kuweka vikao vya kila mwaka kuwalaani na kuwatukana Watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) wakiwemo wake zake, au Sahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum), kwa sababu hawa ni viongozi wetu waliokuwa naye tokea siku ile ya mwanzo. Hawa ni mifano mema kwetu, walioisimamia dini hii na kuieneza ulimwenguni kote, na hawa ndio waliotufikishia dini hii baada ya kujitolea mhanga roho zao na mali zao.

 

Wakati huo huo sisi tunaamini kuwa watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) wanatoka katika nyumba bora kupita zote, lakini pia tunaamini kuwa hapana ajuaye Ghaybu isipokuwa Allaah peke Yake.

 

Allaah Anasema:

 

(( قُلْ لا يَعْلَمُ مَنْ فِي السَّمَوَاتِ وَالأَرْضِ الْغَيْبَ إِلَّا اللَّهُ  ))[النمل:65].

 

“Sema: ‘Hakuna aliyoko katika mbingu na ardhi ajuaye Ghayb ila Allaah.” An-Naml-65

 

Na Anasema:

 

(( وَعِنْدَهُ مَفَاتِحُ الْغَيْبِ لا يَعْلَمُهَا إِلَّا هُوَ ))[الأنعام:59]

“Na ziko Kwake (Allaah tu) funguo za siri (Ghayb) hakuna azijuaye ila Yeye tu.” Al-An’aam-59

 

 

 

Share

09-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Nani Swahaba Na Nani Mnafiki

 

Nani Swahaba – Kilugha Na Kidini

 

Katika kamusi la lugha ya Kiarabu, neno ‘Swahaba’, maana yake ni Rafiki, Mwenzi wake, Sahibu n.k.

Katika dini, neno ‘Swahaba’ maana yake ni Muislamu aliyemuona Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), akamfuata na kumuamini na akafariki katika imani hiyo.

Na hii ina maana kuwa, yeyote aliyewahi kumouna Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na asimuamini, basi hawezi kuingia katika maana ya neno ‘Swahaba’.

 

 

Nani Mnafiki – Kilugha Na Kidini

 

Katika kamusi la lugha ya kiarabu, neno ‘Mnafiki’ maana yake ni mtu mwenye kigeugeu au mwenye kuwa na sura mbali mbali: Leo hivi kesho vile.

Katika dini, neno ‘Mnafiki’ maana yake ni yule anayejidhihirisha kuwa ni Muislam na kumfuata Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), wakati undani wake ni kafiri na adui wa Allaah na adui wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

 

Baada ya tafsiri hii fupi ya nani Swahaba na nani Mnafiki, tutakubaliana kuwa maneno hayo mawili hayawezi kuwa na maana moja, (hayawezi kwenda sambamba) Kilugha wala Kidini.

Kwa sababu Swahaba ni yule aliyemuamini Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akafariki dunia akiwa Muislam, wakati Mnafiki ni mwenye kujidhihirisha kama ni Muislam wakati ndani ya nafsi yake ni kafiri.

Kwa hivyo haiwezekani Swahaba akawa Mnafiki na wala Mnafiki hawezi akawa Swahaba.

Sasa Mtu anaweza kuuliza:

'Vipi tutaweza kutofautisha baina ya Swahaba na Mnafiki?'

Majibu:

Mnafiki ana sifa na alama maalum tulizojulishwa katika Qur-aan na katika Mafundisho ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na kwa ajili hiyo tunaweza kutofautisha baina yake na Swahaba.

 

Wanafiki ni watu;

‘Wanaoeneza ufisadi ardhini, kuifanyia istihzai dini, kuwafanyia istihzai wacha Mungu, ni wavukaji mipaka katika kufanya maasi wenye kuununua upotofu (upotevu) kwa uongofu, wavivu katika kufanya ibada, hugeuka geuka, mara Waislamu mara makafiri, kama Alivyosema Allaah:

 

مُّذَبْذَبِينَ بَيْنَ ذَلِكَ لاَ إِلَى هَـؤُلاء وَلاَ إِلَى هَـؤُلاء

 

“Wanayumba yumba baina ya huku (kwa Waislam) na huko (kwa makafiri). Huku hawako wala huko hawako),” An-Nisaa-143

 

Na katika sifa za wanafiki pia ni;

‘Kuwa hawamwamini Allaah wala Siku ya Akhera na kwamba Waislam wanapopata kheri yoyote au mafanikio, wao wanahuzunika, na hufurahi pale Waislamu wanapopata tabu au wanapokumbwa na masaibu au mitihani.

Huchukizwa na kutoa mali zao katika njia ya Allaah na hufurahi wanaporudi nyuma na kumuacha Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) peke yake vitani.

Wameingia katika dini kwa ajili ya kujikinga wasiambiwe kuwa wao ni makafiri, na wanapenda kuwadhuru Waislam na kuwafarikisha. Na katika sifa za unafiki ni kuwa; wanaiahirisha Swalah mpaka nyakati zake za mwisho na hawahudhurii Swalah za jamaa na kwamba wanaionea uzito kabisa Swalah ya Alfajiri na ya ‘Ishaa’.

 

Hizi ni baadhi tu ya sifa za Wanafiki Alizozitaja Allaah katika Qur-aan tukufu, na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) katika mafundisho yake.

Bila shaka Maswahaba wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ni watu walio mbali kabisa na sifa hizi. Hawa ambao Allaah Amewaambia:

 

كُنتُمْ خَيْرَ أُمَّةٍ أُخْرِجَتْ لِلنَّاسِ تَأْمُرُونَ بِالْمَعْرُوفِ وَتَنْهَوْنَ عَنِ الْمُنكَرِ وَتُؤْمِنُونَ بِاللّهِ

 

“Nyinyi ndio umma bora kuliko umma zote zilizodhihirishiwa watu (ulimwenguni) mnaamrisha yaliyo mema na mnakataza yaliyo maovu, na mnamwamini Allaah.” Aali ‘Imraan- 110

 

Na Akasema juu yao:

 

يا أيها النبي حسبك الله ومن اتبعك من المؤمنين

 

“Ewe Mtume wa Allaah! Allaah anakutoshelezea wewe na wale walokufuata katika hao walioamini”. Al-Anfaal-64

 

Na Akasema juu yao:

 

مُّحَمَّدٌ رَّسُولُ اللَّهِ وَالَّذِينَ مَعَهُ أَشِدَّاء عَلَى الْكُفَّارِ رُحَمَاء بَيْنَهُمْ تَرَاهُمْ رُكَّعاً سُجَّداً يَبْتَغُونَ فَضْلاً مِّنَ اللَّهِ وَرِضْوَاناً

 

“Muhammad ni Mtume wa Allaah. Na walio pamoja naye ni wenye nyoyo thabiti mbele ya makafiri na wenye kuhurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama kwa kurukuu na kusujudu (pamoja), wakitafuta fadhila za Allaah na radhi (yake).” Al Fat-h- 29

 

Na Akasema:

 

وَالَّذِينَ آمَنُواْ وَهَاجَرُواْ وَجَاهَدُواْ فِي سَبِيلِ اللّهِ وَالَّذِينَ آوَواْ وَّنَصَرُواْ أُولَـئِكَ هُمُ الْمُؤْمِنُونَ حَقّاً لَّهُم مَّغْفِرَةٌ وَرِزْقٌ كَرِيمٌ

 

“Na wale walioamini wakahama (kuja Madiynah) na wakaipigania dini ya Allaah (Nao ni Muhajir); na wale waliowapa (Muhajir) mahala pa kukaa na wakainusuru dini (ya Allaah na Mtume wake).(nao ni Answaar) Hao ndio Waislam wa kweli. Watapata msamaha (wa Allaah) na kuruzukiwa kuzuri (kabisa huko Akhera).” Al-Anfaal – 74.

 

Maswahaba wa Makkah (Radhiya Allaahu ‘anhum) ndio walioamini, wakahama, na wakapigana jihadi. Na Maswahaba wa Madiynah (Radhiya Allaahu ‘anhum) ndio waliowapa mahala pa kukaa na wakainusuru dini.

Baada ya maelezo haya kutoka kwa Muumba wa mbingu na ardhi, asije mtu akatuambia kuwa Maswahaba na wanafiki ni kitu kimoja. Hakika haya ni matusi makubwa kabisa!

Hawawezi kuwa wanafiki watu ambao Allaah Amesema juu yao:

 

 “Nyinyi ndio umma bora kuliko umma zote zilizodhihirishiwa watu (ulimwenguni).”

 

Hawawezi kuwa wanafiki watu ambao Allaah Ameshuhudia kuwa ni:

 

“Wenye nyoyo thabiti mbele ya makafiri na wenye kuhurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama kwa kurukuu na kusujudu (pamoja), wakitafuta fadhila za Allaah na radhi (yake).”

 

Hawawezi kuwa wanafiki watu ambao Allaah Mwenyewe Anashuhudia  kuwa “Hao ndio Waislam wa kweli.”

                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                       

 Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alisema:

 

"لا تَسُبّوا أَصْحَابِي، فَوَالّذِي نَفْسِي بِيَدِهِ لَوْ أَنّ أَحَدَكُمْ أَنْفَقَ مِثْلَ أُحِدٍ ذَهَباً مَا أَدْرَكَ مُدّ أَحَدِهِمْ وَلاَ نَصِيفَهُ".

 

"Msiwatukane Swahaba wangu. Ninaapa kwa Yule ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake, hata mmoja wenu atajitolea katika njia ya Allaah kugawa dhahabu ukubwa wake mfano wa jabali Uhud, basi hatofikia gao lao wala hata nusu ya gao lao." Al-Bukhaariy na Muslim

 

Na akasema:

 

من سب أصحابي فعليه لعنة الله والملائكة والناس أجمعين

 

“Atakayewatukana Maswahaba wangu, basi itampata laana ya Allaah na (laana ya) Malaika na (laana ya) watu wote”.

((At-Twabariy, katika ‘Al-Kabiyr’, Abu Na’iym katika ‘Al Hiliyah’ na Abu ‘Aaswim, na hadithi hii pia inapatikana katika ‘Silsila za hadithi sahihi kilichoandikwa na Sheikh Al-Albaaniy)).

 

Na akasema (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam):

 

“Nihifadhieni Maswahaba wangu, kisha wale waliowafuatilia kisha wale waliofuatilia”. Imam Ahmad, Ibn Maajah, na Al-Haakim.

 

Ikiwa Maswahaba waliokuwa wengi wanatuhumiwa kuwa ni watu wenye kigeugeu na unafiki, hii italeta maana kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) hakuweza kuwalea na kuwafundishsa vizuri Maswahaba wake (Radhiya Allaahu ‘anhum) wakaijuwa haki, na kwamba yeye ni mlezi asiyefanikiwa, aliyeshindwa kuifanya kazi yake ya kuwalea Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum).

Haikubaliki akilini abadan kuwa baada ya kuishi nao muda mrefu wote huo alifanikiwa kuwalea na kuwafundisha Maswahaba watatu tu au wasiozidi saba?

 

Kila anayesoma na kuidurusu Siyrah (historia) ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), anaelewa kwamba wakati Waislam walipokuwa Makkah hapakuwa na unafiki, na hii ni kwa ajili ya adhabu kali walizokuwa wakipata waliosilimu wakati ule. Na inajulikana pia kwamba unafiki ulianza kujitokeza baada ya Waislam kuhamia Madiynah, na baada ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kupata nguvu, na dini ya Allaah kuanza kutambulika kila mahala.

Na inaeleweka pia kwa kila mwenye kuidurusu Siyrah ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kuwa Abu Bakr, ‘Umar na ‘Uthmaan na wengineo ni miongoni mwa Maswahaba walioingia katika dini ya Allaah tokea siku za mwanzo, wakapata tabu na shida kama walivyopata wenzao, na hii ni dalili wazi kuwa walikuwa mbali na sifa ya unafiki.

Allaah Amewafedhehesha wanafiki kwa kuwateremshia Suratul Munafiquun na At-Tawbah; Akaelezea ndani ya sura hizo juu ya hali zao na vitimbi vyao; na Akatuelezea yale yaliyofichika nyoyoni mwao katika kuwachukia Waislam, na ndiyo maana Suratut Tawbah ikaitwa 'Sura ya Kufedhehesha'. Katika sura hiyo Allaah Alitaja pia sifa za Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) na Akatujulisha kuridhika kwake nao. Na huu ni ushahidi utokao Kwake (Subhaanahu wa Ta’ala).

Ama Suratul Munafiquun, hii imeteremshwa kwa ajili ya kutujulisha juu ya mkubwa wa wanafiki na kiongozi wao aitwae Abdullah bin Ubay bin Saluul na wenzake.

 

Anasema Zayd bin Al-Arqam (Radhiya Allaahu ‘anhu):

 

"Nilikuwa vitani, nikamsikia Abdullah bin Ubay akisema:

“Msitoe mali kuwasaidia waliokuwa na Mtume wa Allaah mpaka watakapomwondokea pale alipo, na tutakaporudi Madiynah yule mtukufu (akimaanisha yeye Abdullah bin Ubay ‘mkuu wa wanafiki’ kuwa ni mtukufu) atamtoa (katika mji wa Madiynah) yule aliyedhalilika (akimaanisha Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam kuwa eti ndiye aliyedhalilika)”.

Nikamhadithia ‘ami yangu hayo niliyoyasikia (au ‘Umar) naye akamhadithia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam): Akaniita na mimi nikamhadithia. Kisha Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamtuma mtu amuite Abdullah bin Ubay pamoja na wenzake, wakaapa na kukanusha yale waliyosema, na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) hakunisadiki na akamsadiki yeye. Nikaona dhiki sijapata kuona mfano wake. Nikakaa nyumbani kwangu, lakini haujapita muda Allaah akateremsha Suratul Munafiquun, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamtuma mtu aniite, akanisomea (Sura hiyo) kisha akaniambia:

“Allaah Amesadikisha maneno yako ewe Zayd”. Al-Bukhaariy.

 

Tafsiri hii pia inapatikana katika kitabu cha tafsiri cha Mashia kiitwacho ‘Maj ma’ul bayaan fiy tafsiyril Qur-aan’, kilichoandikwa na At-Tubrusy ambaye ni miongoni mwa Maulamaa wakubwa wa Kishia. Na katika kitabu hicho, ameelezea sababu ya kuteremshwa Suratul Munafiqun kuwa ni juu ya Abdullah bin Ubay ‘mnafiki’ na wenzake …

(‘Maj ma’ul bayaan fiy tafsiyril Qur-aan’ ukurasa 85)

 

Kisha Mwanachuoni huyu wa Kishia akazitaja riwaya zile zile alizozielezea Imam Al-Bukhaariy zinazothibitisha hoja hiyo.

Inajulikana wazi kuwa Abdullah bin Ubay pamoja na wafuasi wake walikuwa wakijulikana na Maswahaba wote (Radhiya Allaahu ‘anhum) kuwa ni wanafiki, na mtu yeyote anaposoma Surat at Tawba ataona kuwa sura hiyo imeelezea juu ya vituko mbali mbali walivyokuwa wakivifanya wanafiki hao kiasi ambapo ilikuwa ikijulikana wazi mbele ya kila mtu kuwa wao ndio waliokusudiwa.

Kwa mfano kuanzia aya ya 44 hadi 49 ya sura hiyo Allaah Anasema:

 

لاَ يَسْتَأْذِنُكَ الَّذِينَ يُؤْمِنُونَ بِاللّهِ وَالْيَوْمِ الآخِرِ أَن يُجَاهِدُواْ بِأَمْوَالِهِمْ وَأَنفُسِهِمْ وَاللّهُ عَلِيمٌ بِالْمُتَّقِينَ {44} إِنَّمَا يَسْتَأْذِنُكَ الَّذِينَ لاَ يُؤْمِنُونَ بِاللّهِ وَالْيَوْمِ الآخِرِ وَارْتَابَتْ قُلُوبُهُمْ فَهُمْ فِي رَيْبِهِمْ يَتَرَدَّدُونَ {45} وَلَوْ أَرَادُواْ الْخُرُوجَ لأَعَدُّواْ لَهُ عُدَّةً وَلَـكِن كَرِهَ اللّهُ انبِعَاثَهُمْ فَثَبَّطَهُمْ وَقِيلَ اقْعُدُواْ مَعَ الْقَاعِدِينَ {46} لَوْ خَرَجُواْ فِيكُم مَّا زَادُوكُمْ إِلاَّ خَبَالاً ولأَوْضَعُواْ خِلاَلَكُمْ يَبْغُونَكُمُ الْفِتْنَةَ وَفِيكُمْ سَمَّاعُونَ لَهُمْ وَاللّهُ عَلِيمٌ بِالظَّالِمِينَ {47}‏ لَقَدِ ابْتَغَوُاْ الْفِتْنَةَ مِن قَبْلُ وَقَلَّبُواْ لَكَ الأُمُورَ حَتَّى جَاء الْحَقُّ وَظَهَرَ أَمْرُ اللّهِ وَهُمْ كَارِهُونَ {48} وَمِنْهُم مَّن يَقُولُ ائْذَن لِّي وَلاَ تَفْتِنِّي أَلاَ فِي الْفِتْنَةِ سَقَطُواْ وَإِنَّ جَهَنَّمَ لَمُحِيطَةٌ بِالْكَافِرِينَ {49}

 

“Hawatakuomba ruhusa wale wanao muamini Allaah na Siku ya Mwisho, wasende kupigana Jihadi kwa mali yao na nafsi zao. Na Allaah ni Mwenye kuwajua wachaji Allaah.

Wasiomuamini Allaah na Siku ya Mwisho na nyoyo zao zikatia shaka, hao tu ndio wanao kutaka ruhusa. Basi hao wanataradadi katika shaka zao.

Na ingelikuwa kweli walitaka kutoka bila ya shaka wangelijiandalia maandalio, lakini Allaah kachukia kutoka kwao, na kwa hivyo Akawazuia na ikasemwa: Kaeni pamoja na wanaokaa!

Lau wangelitoka nanyi wasingelikuzidishieni ila mchafuko, na wangetangatanga kati yenu kukutilieni fitna. Na miongoni mwenu wapo wanaowasikiliza. Na Allaah Anawajua madhaalimu.

Tangu zamani walitaka kukutilieni fitna, na wakakupindulia mambo juu chini, mpaka ikaja Haki na ikadhihirika amri ya Allaah, na wao wamechukia”.

Na miongoni mwao wapo wanaosema: ‘Niruhusu wala usinitie katika fitina’. Kwa yakini wao hivyo wamekwisha tumbukia katika fitina. Na hakika Jahannamu imewazunguka.” At-Tawbah – 44-49

 

Inaeleweka na kila mtu kuwa Maswahaba wote walitoka kwenda vitani siku hiyo ya vita vya Tabuuk (vita ambavyo aya hizo zinazungumzia juu yake), na waliobaki nyuma ni Abu Dharr na Abu Khaythamah (Radhiya Allaahu ‘anhum), kisha nao pia wakenda kujiunga na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) pamoja na wenzao, na walikutana nao njiani kabla ya kuwasili uwanja wa vita.

Na ineleweka pia kuwa miongoni mwa waliobaki nyuma ni Ka’ab bin Maalik, Hilaal bin Umayyah na Miraarah bin Rabi’ah (Radhiya Allaahu ‘anhum), nao ni katika watu wa Madiynah na inajulikana na kila mtu kuwa Allaah Aliwasamehe Maswahaba hao kama ilivyoelezwa katika kisa cha ‘Wale watatu waliongojeshwa’.

Ama wengine waliobaki Madiynah wasiende vitani walikuwa wakijulikana kuwa ni katika wale wanafiki waliomuendea Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kuomba udhuru wa uongo, au wale waliokuwa na udhuru wa kutopigana Jihaad kwa ajili ya ugonjwa au udhuru mwingine unaokubalika.

Na haya tulieleza hapo mwanzo katika kisa cha Ka’ab (Radhiya Allaahu ‘anhu)  kuwa katika waliobaki pale Madiynah wasende vitani hakuwa akimuona aliye kufu yake isipokuwa wenye udhuru au wale waliokuwa wakijulikana kuwa ni Wanafiki.

Na hii ni dalili kuwa wanafiki walikuwa wakijulikana na Maswahaba.

 

Na katika sura hiyo hiyo ya At-Tawbah, Allaah Anatujulisha kuridhika kwake na Maswahaba waliotangulia kuingia katika Uislamu miongoni mwa Wahajir (watu wa Makkah waliohamia Madiynah) na Answaar (Watu wa Madiynah waliowapokea Wahajir wa Makkah) na akawatayarishia Bustani zipitazo mito kati yake, wadumu humo milele.

Allaah Anasema:

 

وَالسَّابِقُونَ الأَوَّلُونَ مِنَ الْمُهَاجِرِينَ وَالأَنصَارِ وَالَّذِينَ اتَّبَعُوهُم بِإِحْسَانٍ رَّضِيَ اللّهُ عَنْهُمْ وَرَضُواْ عَنْهُ وَأَعَدَّ لَهُمْ جَنَّاتٍ تَجْرِي تَحْتَهَا الأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا أَبَداً ذَلِكَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ

 

“Na wale waliotangulia, wa kwanza, katika Wahajiri na Answaar, na walio wafuata kwa wema, Allaah Ameridhika nao, na wao wameridhika Naye; na Amewaandalia Bustani zipitazo mito kati yake, wadumu humo milele. Huko ndiko kufuzu kukubwa.” At-Tawbah - 100

 

Sasa tizameni ndugu zangu, vipi Allaah Anatuelezea juu ya kuridhika kwake na Maswahaba katika Muhaajir na Answaar kinyume na wanavyotuhumiwa unafiki, na kwamba walirudi nyuma na kukufuru, akiwemo mbora wa Maswahaba wote Abu Bakr Asw-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ‘anhu).

Sisi tunaridhika na wote alioridhika nao Allaah, na tunawafanyia uadui maadui wote wa Allaah, na tunafuata yale tuliyofundishwa na Allaah pamoja na mafundisho ya Mtume wa Allaah wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

 

Allaah Anasema:

 

لَقَد تَّابَ الله عَلَى النَّبِيِّ وَالْمُهَاجِرِينَ وَالأَنصَارِ الَّذِينَ اتَّبَعُوهُ فِي سَاعَةِ الْعُسْرَةِ مِن بَعْدِ مَا كَادَ يَزِيغُ قُلُوبُ فَرِيقٍ مِّنْهُمْ ثُمَّ تَابَ عَلَيْهِمْ إِنَّهُ بِهِمْ رَؤُوفٌ رَّحِيمٌ {117}‏

 

“Allaah Amekwisha pokea toba ya Nabii na Wahajiri na Answaar waliomfuata katika saa ya dhiki, pale baada ya kukaribia nyoyo za baadhi yao kugeuka. Basi akapokea toba yao, kwani hakika Yeye kwao wao ni Mpole na ni Mwenye kuwarehemu.” At-Tawbah - 117

 

Allaah ni Mpole kwao na Anawarehemu na Ameridhika nao na Anawasifia namna walivyosimama pamoja na Mtume wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) katika saa ile ya dhiki (vita vya Tabuuk), na huu ni ushahidi utokao kwa Allaah Asiye mshirika.

 

Utayakuta haya pia katika vitabu vya wanavyuoni wakubwa wa Kishia (Ithnaasheri) waliotamka ukweli ndani ya baadhi ya vitabu vyao vinavyotambulika.

 

Tafsiri ya Al-Iyaashi

Anasema Abu Naswr Muhammad bin Mas’uud, anayejulikana kwa jina la ‘Al-Iyaashi’ katika tafsiri yake juu ya kauli ya Allaah isemayo:

 

إِنَّ اللّهَ يُحِبُّ التَّوَّابِينَ وَيُحِبُّ الْمُتَطَهِّرِين

 

“Hakika Allaah huwapenda wanaotubu na huwapenda wanaojitakasa.’ Al-Baqarah – 222

 

Alisema:

"Kutoka kwa Salaam anasema: ‘Nilikuwa kwa Abu Ja’afar (Muhammad Al-Baaqir Imam wa tano kwa Shia) akaingia Hamran bin Ayun na kumuuliza baadhi ya mambo, na alipotaka kuondoka, Ayun akamuuliza Abu Ja’afar:

'Tuelezee Allaah Akupe umri mrefu, sisi tunapokuwa nawe nyoyo zetu hulainika na nafsi zetu zinakuwa mbali na dunia, tunadharau kila kilichomo mikononi mwa watu katika mali, lakini tunapotoka na kuchanganyika na watu na kufanya biashara, tunaanza kuipenda tena dunia.’

Abu Ja’afar akasema:

"Nyoyo zinashindwa na mambo baadhi ya wakati, na wakati mwengine mambo yanakuwa mepesi.’ Kisha Abu Ja’afar akaendelea kusema: ‘Kwa hakika Maswahaba wa Mtume wa Allaah walisema:

‘Ewe Mtume wa Allaah, tunajiogopea unafiki’ akasema: “Kwa nini mnaogopa?”

Wakasema:

“Sisi tunapokuwa nawe ukatukumbusha, huwa na uoga, na nyoyo zetu zinalainika tukaisahau dunia, hatuitamani, hata hufikia kuwa tunaiona Akhera Pepo na Moto mbele yetu. Lakini mara tunapotoka kwako na kuingia majumbani mwetu na kuanza kuwabusu watoto wetu na kuonana na wake zetu na mali zetu, tunaanza kubadilika hali zetu kinyume na pale tunapokuwa nawe, kama kwamba hatukuwa na kitu. Je! Hutuogopei unafiki?"

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akawaambia:

Kabisa sikuogopeeni hilo, kwani hizi ni katika hatua za Shaytwaan akijaribu kukupendezesheni dunia, Wallahi lau kama mungebaki katika hali ile mliyokuwa nayo pale mlipokuwa nami, basi Malaika wangekusalimieni majiani na mungekuwa mnatembea juu ya maji, na kama mungelikuwa hamtendi madhambi na kumuomba Maghfira Allaah, basi Allaah Angeliumba viumbe vingine ili wafanye madhambi kisha wamuombe maghfira ili apate kuwaghufiria, kwani Muislam siku zote yupo katika mtihani, hukuisikia kauli ya Allaah isemayo:

 

إِنَّ اللّهَ يُحِبُّ التَّوَّابِينَ

 

‘Hakika Allaah huwapenda wanaotubu?’

na isemayo:

 

وَأَنِ اسْتَغْفِرُواْ رَبَّكُمْ ثُمَّ تُوبُواْ إِلَيْهِ

 

“Na ili muombe msamaha kwa Mola wenu kisha mtubie (mrejee)?"

Huud – 3 (Tafsir Al-Iyaashi Juz. 1 uk. 128)

 

Katika riwaya hii, anatubainishia Al-Iyaashi katika tafsiri yake kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ameshuhudia kuwa hawaogopei Swahaba zake unafiki. Na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) hasemi kwa matamanio ya nafsi yake.

Kwa hivyo mwenye kumuita Swahaba yeyote kuwa ni mnafiki, mtu huyo atakuwa ana moja katika mawili:

1-    Ama anakwenda kinyume na mafundisho ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

2-    Au anajua zaidi kupita Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

Ikiwa tunautaka umoja wa Waislamu kikweli na kuiondoa chuki iliyopo, basi nawaomba ndugu zetu Mashia waache kuwakufurisha Maswahaba au kuwaita wanafiki na kuwaapiza, na badala yake tumfanye Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kuwa ni ruwaza njema kwetu, kuwa ni mfano mwema kwetu wa kuigwa, na tuwapende kama alivyokuwa akiwapenda (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

 

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alikuwa akiwapenda Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum). Na watu wa nyumba yake 'Ahlul Bayt' (Radhiya Allaahu ‘anhum) nao pia walikuwa wakiwapenda Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum), na Maswahaba nao walikuwa wakiwapenda Ahlul Bayt.

Huyu hapa Imam Al-Hasan Al-‘Askari, ambaye ni Imam wa kumi na moja wa Shia alipokuwa akiwafahamisha watu daraja ya Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum)  mbele ya Allaah alisema:

 

‘Miongoni wa masuala aliyouliza Muusa ('Alayhis Salaam) kumuuliza Allaah alisema:

‘Wapo Maswahaba wa Mtume yeyote wa Allaah walio bora kuliko Maswahaba wangu?'

Allaah Akamjibu:

“Ewe Muusa kwani hujui kuwa ubora wa Maswahaba wa Mtume wa Allaah Muhammad juu ya Maswahaba wa Mitume yote ni sawa na ubora wa watu wa nyumba ya Muhammad juu ya watu wa nyumba za Mitume yote, na mfano wa ubora wa Muhammad juu ya Mitume yote?”

Tafsiri ya Al-Hasan Al-‘Askariy uk. 11(Tafsiri ya Surat Al-Baqarah)

 

Ndani ya kitabu kitukufu kwa Shia kiitwacho ‘Nahjul Balaaghah’, Sharhi ya Muhammad ‘Abdu Uk. 225, imeandikwa kuwa Imam ‘Aliy alisema:

 

“Nimewaona Maswahaba wa Mtume wa Allaah (Swalla Laahu ‘alayhi wa sallam), na sioni yeyote kati yenu aliyeshabihiana nao. Walikuwa wakati wa asubuhi utawaona nywele zimetimka kwa sababu ya kusimama kwao usiku kucha wakisujudu na kusimama (kwa kuswali), wanaomba huku wakisujudu, na wanapolala, na wanapokumbuka Akhera yao utawaona wanasimama kama kwamba wamesimamia makaa ya moto. Na Anapotajwa Allaah basi macho yao yanatoa machozi mpaka nyuso zao zinaroa, na wanainamisha vichwa vyao chini mfano wa miti iliyopinda kwa upepo mkali wa kimbunga kwa kuhofia adhabu na kutarajia thawabu”.

 

Ama Ibraahiym At-Thaqafiy ambaye ni katika Maulamaa wakubwa wa Shia, katika kitabu chake kiitwacho ‘Al-Ghaaraat’ Juzuu ya 1 Uk. 177 akimnukuu ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu):

“Aliulizwa ‘Aliy: ‘Ewe Amiri wa Waislam, tuelezee juu ya Swahibu zako.’

Akauliza:

“Juu ya Swahibu zangu wepi?”

Wakamwambia:

“Juu ya Swahaba wa Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).”

Akasema:

“Maswahaba wa Muhammad wote ni Swahibu zangu”.

 

Tunamuomba msomaji arudie marejeo yote tuliyonukuu kutoka katika Qur-aan tukufu na kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na kutoka kwa Maulamaa wa pande zote mbili ili imbainikie heshima ya Maswahaba hawa wakiwemo Makhalifa watatu wa mwanzo wa Waislam mbele ya Allaah na mbele ya Mtume wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na mbele ya Maulamaa waliotangulia wa pande zote mble, kisha ajiulize; ni kwa maslahi ya nani mtu anaweza kuthubutu kuwatukana au kuwazulia uongo na kuwawekea vikao vya kila mwaka kuwalaani na kuapa juu ya kulipa visasi.

Bali hata Sayiduna Al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhu) alikuwa katika nchi ya Constantinople akipigana jihadi, na wakati huo Mu’awiyah (Radhiya Allaahu ‘anhu) ndiye aliyekuwa Khalifa wa Waislamu. Kwa hivyo Maswahaba na Watu wa Nyumba ya Mtume (Radhiya Allaahu ‘anhum) walikuwa wakishirikiana na kupendana na kunasibiana na walikuwa pamoja katika jihadi yao dhidi ya maadui wa Uislamu.

 

Siku moja kundi la watu lilikwenda kwa Imam ‘Aliy Zaynul-’Aabidiyn (Radhiya Allaahu ‘anhu) na walikuwa wakiwasema vibaya Maswahaba wa Mtume wa Allaah (Swalla Laahu alayhi wa sallam); Abu Bakr, ‘Umar na ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhum).

‘Aliy Zaynul-’Aabidiyn (Radhiya Allaahu ‘anhu) akawauliza:

 

“Kwanza nielezeni ni nani nyinyi? Nyinyi ni katika wale Wahajir (Watu wa Makkah) waliohama mwanzo waliotolewa majumbani mwao na katika mali zao wakitaka fadhila za Allaah na radhi zake na wakamnusuru Allaah na Mtume wake?”

 

الَّذِينَ أُخْرِجُوا مِن دِيارِهِمْ وَأَمْوَالِهِمْ  يَبْتَغُونَ فَضْلاً مِّنَ اللَّهِ وَرِضْوَاناً وَيَنصُرُونَ اللَّهَ وَرَسُولَهُ

Al-Hashr -8

 

Wote kwa pamoja wakasema: “La, sisi si katika hao”

Akawauliza tena:

“Basi nyinyi ni katika watu waliofanya maskani yao hapa (Madiynah) na wakautakasa Uislamu (wao barabara) kabla ya (kuja ) hao (Muhaajiriyn) na wakawapenda hao waliohamia kwao”

.

وَالَّذِينَ تَبَوَّؤُوا الدَّارَ وَالْإِيمَانَ مِن قَبْلِهِمْ يُحِبُّونَ مَنْ هَاجَرَ إِلَيْهِمْ

Al-Hashr -9

 

Wakajibu:

“La! Sisi si katika hao”

Kisha Imam ‘Aliy Zaynul-’Aabidiyn (Radhiya Allaahu ‘anhu)  akawaambia:

“Nyinyi wenyewe mumeshuhudia kuwa si katika hawa wala si katika wale. Basi na mimi ninashuhudia pia kuwa nyinyi si katika kundi lile la tatu ambalo Allaah Amesema juu yao:

 

وَالَّذِينَ جَاؤُوا مِن بَعْدِهِمْ يَقُولُونَ رَبَّنَا اغْفِرْ لَنَا وَلِإِخْوَانِنَا الَّذِينَ سَبَقُونَا بِالْإِيمَانِ وَلَا تَجْعَلْ فِي قُلُوبِنَا غِلّاً لِّلَّذِينَ آمَنُوا رَبَّنَا إِنَّكَ رَؤُوفٌ رَّحِيمٌ

 

“Na Waliokuja baada yao (wakawa wanapendana na Waislamu waliotangulia wanawaombea du’aa) wanasema; ‘”Mola wetu! Tusamehe sisi na ndugu zetu waliotutangulia (kufa) katika Uislamu. Wala usijaaliye katika nyoyo zetu undani kuwafanyia Waislamu (wenzetu). Mola wetu! Hakika Wewe ni Mpole sana, Mwenye Rehema mno.” Al-Hashr – 10

 

Katika aya hizi Allaah Anashuhudia kuwa watu wa Makkah waliacha majumba yao na mali zao na watu wao kwa ajili ya kutaka fadhila za Allaah na radhi Zake, na kwa ajili ya kumnusuru Allaah na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na akashuhudia kuwa ni wakweli.

Na Allaah Anashuhudia pia watu wa Madiynah waliutakasa Uislamu baraabara, juu ya kuwa walifikiwa na wageni wazito na hawakuwa na mali ya kutosha, waliwapokea wageni hao kwa moyo mkunjufu, wakahiari kujinyima wao kwa ajili ya kuwakirimu wageni.

Kisha Allaah Akatuamrisha tuliokuja baada yao kuwaombea maghfira na Akatutaka tusijaaliye ndani ya nyoyo zet undani wowote juu yao.

 

Imepokelewa kutoka kwa Yahya bin Kathiyr kutoka kwa Ja’afar bin Muhammad bin ‘Aliy bin Al-Husayn kutoka kwa baba yake ((Radhiya Allaahu ‘anhum) kuwa amesema:

 

« Alikuja mtu kwa baba yangu akamuambia : ‘Nihadithie juu ya Abu Bakr.’ Akasema: ‘Unauliza juu ya Asw-Swiddiyq.’ Akasema yule mtu : ‘Allaah akurehemu, na wewe pia unamuita Asw-Swiddiyq ?’ Akamuambia : ‘Akukose mama yako wewe. Ameitwa Asw-Swiddiyq na aliye bora kupita mimi na wewe, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na Watu wa Makkah na watu wa Madiynah. Asiyemuita kwa jina la Asw-Swiddiyq basi Allaah hatosadiki kauli yake duniani wala akhera. Nenda, tena umpende Abu Bakr na ‘Umar.»

 

Imeandikwa katika Nahjul Balaaghah pia kuwa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alimuandikia Mu’aawiyah bin Abi Sufyaan (Radhiya Allaahu ‘anhu) akimuambia:

 

Kwa Mu’aawiyah:

"BismiLlaahir Rahmaanir Rahiym,

Amma ba’ad, kwa vile watu wote wamefungamana nami katika mji wa Madiynah, basi nawe pia uliyeko huko Shaam (Syria) unalazimika kufungamana nami. Na hii ni kwa sababu watu waliofungamana nami ni wale wale waliofungamana na Abu Bakr na ‘Umar na ‘Uthmaan. Kwa hivyo aliyehudhuria hana haki ya kulikataa na asiyehudhuria hana haki ya kulipinga. Kwa hakika ushauri ni wa Muhaajiriyn na Answaar (Watu wa Makkah na wa Madiynah). Wanapokubaliana wote juu ya mtu na kumchagua kuwa Imam wao, na Allaah Anaridhika na uchaguzi wao.

Nimemtuma kwako Jariyr, naye ni katika watu wa Imani na watu waliohajir, kwa hivyo fungamana nami - Walaa quwwata illa biLlaah!!".

(Nahjul-Balaaghah- uk. 427 mlango wa 6)

 

SubhaanAllaah! Huyu hapa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) anakiri mwenyewe kuwa hapana mwenye haki ya kupinga uchaguzi wa watu wa Makkah na wa Madiynah na kwamba Allaah ameridhika na kuchaguliwa kwa Abu Bakr na ‘Umar na ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhum) kwa sababu wote wamechaguliwa kwa njia hiyo.

 

Share

10-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Kuoleana Na Majina Ya Watoto

 

Kuoleana

 

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ameoa mabinti wa Abu Bakr na ‘Umar. Na ‘Uthmaan alioa mabinti wawili wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), Mabibi Ruqayyah na Ummu Kulthuum, na alijulikana kwa jina la 'Dhiy Nnurayn', na maana yake ni Mwenye Nuru mbili kwa sababu ya mabinti hao wawili (Radhiya Allaahu ‘anhum).

Alihuzunika sana alipofariki mkewe wa pili Bibi Ummu Kulthuum (Radhiya Allaahu ‘anha) na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alipomuona katika hali ile akamuuliza:

 

"Kipi kinachokuliza ewe ‘Uthmaan?"

‘Uthmaan akajibu:

"Ninalia ewe Mtume wa Allaah kwa sababu kumekatika kunasibiana kwangu na wewe."

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia:

"Usilie ewe ‘Uthmaan, naapa kwa yule ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake, lau kama nina mabinti mia wanakufa mmoja baada ya mwengine, basi ningekuozesha mpaka wasibaki katika mia hao hata mmoja." At-Twabaraaniy na wengine.

 

Hii ni katika dalili za mapenzi makubwa yaliyokuwepo baina ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) pamoja na watu wa nyumba yake juu ya Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum).

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alimuoa Bibi ‘Aaishah binti wa Abu Bakr Asw-Swiddiyq na alimuoa Hafswah binti wa ‘Umar bin Al-Khattwaab na alimuoa pia Ummu Habiybah Ramlah binti Abi Sufyaan (Radhiya Allaahu ‘anhum).

 

‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alimuozesha binti yake Ummu Kulthuum kwa ‘Umar bin Al-Khattwaab.

(Al-Kafi/346/5)

Alipouliwa Ja’afar bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu), mkewe Asmaa binti Umays (Radhiya Allaahu ‘anha) aliolewa na Abu Bakr Asw-Swiddiyq na alipofariki Abu Bakr (Radhiya Allaahu ‘anhu), Bibi Asmaa aliolewa na ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu).

Ja’afar Asw-Swaadiq ni mjukuu wa Abu Bakr Asw-Swiddiyq, kwa sababu Muhammad Al-Baaqir mjukuu wa Al-Husayn alimuoa Ummu Farwah mjukuu wa Muhammad bin Abi Bakr, na kutokana na ndoa hiyo akapatikana Ja’afar Asw-Swaadiq. Kwa hivyo Ja’afar ni mjukuu wa Abu Bakr na mwanawe Muusa Al-Kaadhwim anakuwa pia mtoto wa mjukuu wa Abu Bakr na kwa njia hii Maimam wote waliofuata wa Shia ni wajukuu wa Abu Bakr Asw-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ‘anhum jamiy’an).

 

Imepokelewa kuwa Ja’afar Asw-Swaadiq alikuwa akisema:

“Amenizaa Abu Bakr mara mbili.”

Siyar A’alaam an-Nubalaa

 

Abaad bin ‘Uthmaan bin ‘Affaan alimuoa Ummu Kulthuum binti yake AbduAllaah bin Ja’afar bin Abi Twaalib.

Shia wa Ahlul Bayt/141

 

Sakina bint Al-Husayn bin ‘Aliy bin Abi Twaalib aliolewa na Mus’ab bin Az-Zubayr bin Al-A’waam.

Twabaqaat ibn Sa’ad183/5

 

(Allaah Awe radhi nao wote)

 

 

 

Majina ya watoto

 

‘Aliy bin Abi Twaalib aliwapa wanawe majina ya Abu Bakr na ‘Umar na ‘Uthmaan.

Kashf al-Ghummah 2/67.

 

Al-Hasan bin ‘Aliy alimpa mmoja wa watoto wake jina la Abu Bakr.

Kashf al-Ghummah 2/198.

 

Muusa bin Ja’afar alikuwa na watoto aliowapa majina ya ‘Aaishah na ‘Umar.

Kashf al-Ghummah 3/29.

 

Share

11-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Wajibu Wetu

 

Wajibu Wetu

 

Itakuwa siku ya furaha kubwa tutakapowaona wafuasi wa Sunni wakipeana mikono na wafuasi wa Shia kwa furaha bila kinyongo wala undani. Lakini hatuwezi kulifikia lengo hilo ikiwa Maswahaba wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) wataendelea kutukanwa na kukashifiwa na kulaaniwa.

Hatuwezi kulifikia ikiwa watu wataendelea kulizuru kaburi la Majusi Abu Luulua aliyemuua Khalifa wa Waislamu na Swahibu yake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ‘Umar bin Khattwaab (Radhiya Allaahu ‘anhu) na kuliita kaburi la Majusi huyo ‘Baba Shujaa ddiyn’ ‘Baba shujaa wa  dini.’

Dini gani wakati mtu huyu hakuwa Muislamu? Kwa nini wanakubali kuisherehekea siku ambayo Mmajusi aliyekuwa akiabudu moto alimuua Khalifa wa Wasilamu?

 

«Enyi viongozi wa Shia wenye akili na hekima, upigeni vita mnasaba huu kwa ajili ya umoja wa Waislamu. Inatosha jamani kueneza chuki kwa mambo yaliyotokea miaka 1500 iliyopita.»

 

Msisahau kuwa ‘Umar huyu ni ‘ami yake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), kwa sababu Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amemuoa bini yake Hafswah (Radhiya Llahu ‘anha), na ‘Umar huyu huyu ni mume wa Ummu Kulthuum binti ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu).

Nilifurahi sana nilipomskia Dr. Sabah Al-Khuza’iy katika channel Al-Mustaqillah, na huyu ni mtaalamu anayesomesha katika mojawapo ya Vyuo vikuu huko Uingereza, na ni mfuasi wa madhehebu ya Shia.

Anasema Dr. Khuza’iy:

 

«Sielewi kwa nini viongozi wetu wa Shia wanashadidia sana jambo hili la kufanya matanga kila mwaka wakidai kuwa hiyo ni siku aliyouliwa Bibi Faatwimah binti wa Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na ndani ya matanga hayo wanalaaniwa Maswahaba wakubwa wa  Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) hasa Makhalifa wawili wa mwanzo, Abu Bakr na ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhum).

Mimi siamini kuwa ‘Umar wala Abu Bakr walimshambulia Bibi Faatwimah! Haya yote ni uzushi mtupu uliotungwa na watu wasioitakia kheri dini yetu, na baadhi ya watu wakausadiki uongo huo na kuueneza.

Inaingia akilini jamani kwa watu hawa waliosifiwa ndani ya Qur-aan tukufu na katika hadithi mbali mbali za Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na huyu Abu Bakr aliyeruhusiwa na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kuswalisha wiki nzima ya mwisho kabla ya kufariki Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alikuwa akimtizama huku akitabasamu, na hii ni dalili ya kuridhika naye.

Na ‘Umar ambaye ‘Aliy alikubali kumuozesha binti yake Ummu Kulthuum. Kama kweli ‘Umar ndiyo sababu ya kufariki kwa Bibi Faatwimah wangelikubali kumuozesha binti yao mtu katili?

Hadithi sahihi kwa pande zote mbili Shia na Sunni inasema:

« Atakapokujieni mtakayeridhika na dini yake na khulka zake muozesheni. »

Bila shaka ‘Aliy na Faatwimah waliridhika na dini ya ‘Umar ndiyo maana wakakubali kumuozesha binti yao.

Hivyo ‘Aliy huyu aliyepigana vita vya Khaybar kwa ushujaa mkubwa akapambana na ‘Amr ibn ‘Abdi Wudd wakati Maswahaba wengine walihofia kupambana naye, leo ‘Aliy huyu avunjiwe heshima ya mke wake kisha anyamaze kimya? Isitoshe  ampe tunza muovu huyo ya kukubali kumuozesha binti yake?

Mimi, aliendelea kusema Dr. Al-Khuzaiy:

«Ni Shia wa ‘Aliy yule shujaa aliyeuvunja mlango wa Khaybar, nilikuwa pamoja naye siku ile, na nilikuwa pamoja na ‘Aliy siku ile alipokubali kuswali nyuma ya Abu Bakr wakati Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alipokuwa akiumwa maradhi yake ya mwisho. Nilikuwa na ‘Aliy siku ile alipochaguliwa Abu Bakr kuwa Khalifa wa Waislamu na ‘Aliy akamkubali na akaswali nyuma yake, na nilikuwa pamoja na ‘Aliy siku ile alipokubali kuswali nyuma ya ‘Umar bin Al-Khattwaab baada ya kuchaguliwa kuwa Khalifa wa Waislamu. Na nilikuwa pamoja na ‘Aliy siku ile ‘Abdur-Rahmaan bin ‘Awf alipowashauri Waislamu juu ya nani awaongoze, nusu yao walimchagua ‘Uthmaan na nusu nyingine walimchagua ‘Aliy. Mimi siku ile nilikuwa pamoja na ‘Aliy.

Na nilikuwa pamoja na ‘Aliy pia siku ile alipokubali kuswali nyuma ya ‘Uthmaan baada ya kuchaguliwa Khalifa wa Waislamu, na maisha yangu yote nitakuwa pamoja na ‘Aliy mpaka siku ya Qiyaama. Lakini siwakufurishi Maswahaba wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) wala wake zake wala sikubali mtu yeyote awaseme vibaya watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam).

Mimi naamini kuwa Bibi Faatwimah alikwenda kweli kwa Abu Bakr (Radhiya Allaahu ‘anhu) akidai ardhi ya Fadak na baada ya kufahamishwa hadithi ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kuwa Mitume hawarithiwi akaridhika, juu ya kukasirika kwake kidogo.

Na Abu Bakr (Radhiya Allaahu ‘anhu) alipomuendea nyumbani kumuomba radhi Faatwimah alikubali bila kinyongo. »

Mwisho wa maneno ya Al-Khuza’iy

 

Hadithi hii ya Mitume kutorithiwa ni sahihi na imo ndani ya vitabu vinavayotegemewa vya Shia na Sunni.

Imesimuliwa na Al-Kulayni katika kitabu chake maarufu ‘Al-Kaafi’ kuwa:

 

“Abu Abdillaah (Imam Ja’afar asw-Swaadiq) amesema:

“Na hakika Maulamaa ni warithi wa Mitume. Na hakika Mitume hawarithiwi Dinari wala Dirham, bali wao wanarithiwa elimu, kwa hivyo atakayeipata elimu hiyo amepata bahati kubwa” Al-Kaafi 1/42.

 

Imam Muhammad Al-Baaqir Al-Majlisi katika kitabu chake kiitwacho Mir'at al-‘Uquul 1/111 amesema kuwa hadithi hii ni sahihi.

 

Khomeini ameiandika hadithi hii katika kitabu chake kiitwacho ‘Al-Hukuumah al-Islaamiyah’ (Serikali ya Kiislamu), na akaitumia kama ni ushahidi wa Wilayat al-Faqiyh chini ya kichwa cha maneno; (Sahihat al-Qaddah) aliposema:

“Amesema ‘Aliy bin Ibraahim kutoka kwa baba yake, kutoka kwa Hammaad bin ‘Iysa kutoka kwa Abdullah bin Maymun al-Qaddah kuwa Abu Abdillah (Ja’afar asw-Swaadiq (‘Alayhis Salaam) amesema:

 

“Atakayefuata njia ya kutafuta elimu, basi Allaah Atamsahilishia njia ya Peponi. Na Maulamaa ni warithi wa Mitume. Na Mitume hawarithiwi Dinari wala Dirham, bali wao wanarithiwa elimu, kwa hivyo atakayeipata elimu hiyo amepata bahati kubwa.”

Al-Kaafi, kitab fadhl Al-‘Ilm, mlango wa Swiffat al-‘Ilm wa Fadhlihi, hadithi nambari 2

 

Na katika kitabu hicho hicho cha ‘Al-Hukuumah al-Islaamiyah’ ukurasa wa 133 Khomeini ameiandika hadithi nyingine iliyopokelewa kwa njia ya Muhammad Yahya kutoka kwa Ahmad bin Muhammad bin ‘Iysa kutoka kwa Muhammad bin Kahalid kutoka kwa Abu Abdillah (Imam Ja’afar asw-Swaadiq (‘Alayhis Salaam) kuwa amesema:

 

“Hakika Maulamaa ni warithi wa Mitume, na hii ni kwa sababu Mitume hawaachi Dirham wala Dinari kwa ajili ya kurithiwa, bali wao wanaacha maneno yao.” Al-Hukuumat al-Islaamiyah uk. 133

 

Kutokana na yaliyotangulia tunamaliza kwa kusema kuwa;

Si haki kutoikubali hadithi hii ya Kutorithiwa kwa Mitume katika kadhia ya Fadak, na kuikubali katika kadhia ya Wilayat al-Faqiyh, kama alivyoandika Khomeni na kabla yake Majlisi.

Kwa nini tuzikubali kauli za Mtume wa Allaah (Swalla Laahu alayhi wa sallam) pale tunapotaka na tuzikatae tusipotaka juu ya kujua kwetu kuwa kauli ya Mtume wa Allaah (Swalla Llahu alayhi wa sallam) haiwezi kubadilishwa na kiumbe chochote kile.

 

Na hadithi hii imo pia katika vitabu vifuatavyo :

Katika At-Tahdhiyb ameandika At-Tuwsi na katika Bihaar al-Anwaar ameandika Al-Majlisi:

 

“Nilimuuliza Abu Abdillah juu ya wanawake na haki zao katika urithi akasema:

“Wana haki zao katika thamani ya udongo na ujenzi na mbao na miti tu, ama ardhi na nyumba, wao hawana haki ya urithi (wowote ndani yake).”

 

Na kutoka kwa Muhammad bin Muslim kutoka kwa Abu Ja’afar (‘Alayhi Salaam) kuwa amesema:

 

“Wanawake hawana haki ya kurithi ardhi wala nyumba”.

 

Na kutoka kwa ‘Abdul-Malik bin Aayun kuwa mmoja wa ma-Imam alimwambia:

 

“Wanawake hawana haki ya urithi katika ardhi wala nyumba”.

 

 

Share

12-Mapenzi Ya Ahlus-Sunnah Juu Ya Ahlul-Bayt: Hitimisho

 

Hitimisho

 

Kwa kumaliza, hatusemi kuwa Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) wamekingwa na kufanya makosa 'Maaswuwmiyn' au 'hawakosei'. Bali wao ni viumbe wanaokosea kama viumbe wengine. Tunachotaka na kusisitiza ni kuwanasihi ndugu zetu; ikiwa kweli wanautaka umoja wa Kiislamu, na wanapenda Waislamu waungane wawe kitu kimoja bila kujali madhehebu, basi waache kuwatukana na kuwalaani na kuwadhalilisha na kuwafanyia chuki Maswahaba hawa waliotukuzwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Maswahaba walioibeba Qur-aan hii tukufu tuliyonayo majumbani mwetu na Misikitini na kila mahali wakaifikisha kwetu na kuieneza kila pembe ya ulimwengu. Bila ya juhudi zao kubwa na kujitolea kwao mhanga kwa hali na mali, wakapigana jihadi dhidi ya maadui wa Allaah, dini isingeweza kutufikia, na tungelibaki hadi leo tukisujudia moto na masanamu na mizimu.

 

Walipotawala, dola kubwa kubwa zilisalimu amri mbele ya majeshi yao, na ulimwengu wote ulikuwa chini ya amri yao.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema juu yao:

 

إِنَّ الَّذِينَ آمَنُواْ وَهَاجَرُواْ وَجَاهَدُواْ بِأَمْوَالِهِمْ وَأَنفُسِهِمْ فِي سَبِيلِ اللّهِ وَالَّذِينَ آوَواْ وَّنَصَرُواْ أُوْلَئِكَ بَعْضُهُمْ أَوْلِيَاء بَعْضٍ وَالَّذِينَ آمَنُواْ وَلَمْ يُهَاجِرُواْ مَا لَكُم مِّن وَلاَيَتِهِم مِّن شَيْءٍ حَتَّى يُهَاجِرُواْ وَإِنِ اسْتَنصَرُوكُمْ فِي الدِّينِ فَعَلَيْكُمُ النَّصْرُ إِلاَّ عَلَى قَوْمٍ بَيْنَكُمْ وَبَيْنَهُم مِّيثَاقٌ وَاللّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ ﴿72﴾ وَالَّذينَ كَفَرُواْ بَعْضُهُمْ أَوْلِيَاء بَعْضٍ إِلاَّ تَفْعَلُوهُ تَكُن فِتْنَةٌ فِي الأَرْضِ وَفَسَادٌ كَبِيرٌ ﴿73﴾ وَالَّذِينَ آمَنُواْ وَهَاجَرُواْ وَجَاهَدُواْ فِي سَبِيلِ اللّهِ وَالَّذِينَ آوَواْ وَّنَصَرُواْ أُولَئِكَ هُمُ الْمُؤْمِنُونَ حَقًّا لَّهُم مَّغْفِرَةٌ وَرِزْقٌ كَرِيمٌ

 

Hakika wale walioamini na wakahama na wakapigania Njia ya Allaah kwa mali yao na nafsi zao, na wale waliotoa mahala pa kukaa, na wakanusuru, hao ni marafiki na walinzi wao kwa wao. Na wale walioamini lakini hawakuhama, nyinyi hamna waajibu wa ulinzi kwao hata kidogo mpaka wahame. Lakini wakiomba msaada kwenu katika Dini, basi ni juu yenu kuwasaidia, isipo kuwa juu ya watu ambao yapo mapatano baina yenu na wao. Na Allaah Anayaona mnayoyatenda.

Na wale walio kufuru ni marafiki wenyewe kwa wenyewe. Msipofanya hivi itakuwako fitna katika nchi na fisadi kubwa.

Na walioamini wakahama na wakapigana Jihadi katika Njia ya Allaah, na waliotoa mahala pa kukaa na wakanusuru, hao ndio Waumini wa kweli. Watapata msamaha wa Allaah na kuruzukiwa kwema.

Al-Anfaal -72-74

 

Ndugu zangu Waislamu, aya hizi tukufu zinazungumza juu ya Maswahaba hawa (Radhiya Allaahu ‘anhum) walioamini wakahama (Watu wa Makkah) na walioamini wakatoa mahala pa kukaa (Watu wa Madiynah), kisha wakapigana Jihadi katika Njia ya Allaah wakiwemo Abu Bakr na ‘Umar na ‘Uthmaan na ‘Aliy na wenzao (Radhiya Allaahu ‘anhum jamiy’an).

 

Allaah Mwenye kujuwa yaliyodhihirika na yaliyojificha aliangalia ndani ya nyoyo zao akawapa sifa hizo wanazostahiki.

Allaah Anasema :

 

ألا يَعْلَمُ مَنْ خَلَقَ وَهُوَ اللَّطِيفُ الْخَبِيرُ {14)

 

Oh! Asijue Aliyeumba! Naye ndiye Avijuaye visivyojulikana na vinavyojulikana?

Al-Mulk - 14

 

Ndugu zangu Waislamu, zile kauli zisemazo kuwa ulikuwepo uadui baina ya Maswahaba na Watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) si sahihi. Hizi ni kauli zilizoingizwa ndani ya baadhi ya vitabu kwa ajili ya kujenga chuki baina yetu Waislamu na kututenganisha na kutudhoofisha. Msighururike nazo.

Na hapa tunakuleteeni mtiririko wa kauli mbali mbali kutoka kwa Maulamaa wa Kishia wenye kuonyesha mapenzi ya hali ya juu yaliyokuweo baina ya Maswahaba na baina ya Watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam):

 

Imam Hasan Al-Askariy ambaye ni Imamu wa kumi na moja katika madhehebu ya Shia Ithnaashariy akihadithia juu ya siku ya Hijrah allisema:

« Baada ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kumtaka ‘Aliy alale juu ya tandiko lake, alimuambia Abu Bakr  Asw-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ‘anhu): «Utakuwa radhi uwe pamoja nami ewe Abu Bakr ukitafutwa kama ninavyotafutwa na ukijulikana kuwa wewe ndiye mwenye kunisaidia katika haya ninayowalingania watu ndani yake, na utabebeshwa kwa ajili yangu kila aina ya adhabu?» Abu Bakr akasema: «Ewe Mtume wa Allaah, ama mimi hata kama nitaishi duniani nikaidhibishwa maisha yangu yote adhabu kali kali, bila ya kufa kifo cha uhakika na bila ya furaha, na yote haya yawe kwa ajili ya kukupenda wewe, basi hayo ni bora kwangu kuliko kuneemeka duniani nikiwamiliki wafalme wote dhidi yako. Kwani mimi na mali yangu na watoto wangu ni kitu gani isipokuwa ni kwa ajili yako.»

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akasema: «Bila shaka Allaah Ameangalia ndani ya moyo wako akaona kuwa unakubaliana na yanayotamka ulimi wako. Akujaalie uwe mfano wa masikio yangu na macho yangu katika mwili, na roho katika nafsi.»

Tafsiri ya Al-Hasan Al-Askariy na Bihaar Al-Anwaar

 

Imepokelewa pia kuwa ‘Aliy bin Abi Twaalib alimuambia ‘Uthmaan (Radhya Llahu ‘anhum:

 

«Na WAllaahi sijui nikuambie nini. Hapana ninachokijua mimi usichokijua wewe, na hapana ninachoweza kukufundisha usichokifahamu, hatukukutangulia katika jambo lolote hata tuweze kukupa habari zake, wala hapana kilichofichika kwao tukakujulisha nacho. Umeona tuliyoyaona, na umeyasikia tuliyosikia, na umekuwa pamoja na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kama tulivyokuwa pamoja naye, na wala si mwana wa Quhafa, (Abu Bakr Asw-Swiddiyq) wala si mwana wa Al-Khattwaab, (‘Umar bin Khattwaab) waliokutangulia katika haki. Na wewe umehusiana na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) zaidi kuliko wao, kwa sababu umeoa kwake zaidi kupita walivyofanya wao. Kwa hivyo Allaah Allaah katika nafsi yako…»

Nahjul-Balaghah

 

Anasema Al Majlisiy kutoka kwa At-Tuwsy kuwa Imam ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) aliwaambia sahibu zake :

 

«Nakuusieni juu ya sahibu zake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), msiwatukane kwani hawa ni Swahibu zake Mtume wenu, na ni Swahibu zake ambao hawajaongeza uzushi wowote katika dini, wala hawamuogopa mwenye kuleta uzushi. Ndiyo! Ameniusia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) juu yao hawa.»

Hayaat al-Quluub kilichoandikwa na Al-Majlisi- uk. 122

 

Na kutoka kwa Ja’afar Asw-Swaadiq kutoka kwa wazee wake kutoka kwa ‘Aliy amesema:

 

«Nakuusieni juu ya Swahibu zake Mtume wenu. Msiwatukane. Hawa hawajaongeza uzushi wowote, wala hawajampa ulinzi mwenye uzushi. Hakika Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ameusia juu yao kila la kheri. »

Bihaar al-Anwaar - 305 na Ash-Shi’ah al-Imaamiyah, kilichoandikwa na Dr. Al-Qifary - uk. 935

 

Na siku ile Ibni Muljam (mwenye kustahiki kutoka kwa Allaah kile anachostahiki) alipompiga upanga ‘Aliy bin Abi Twaalib na ‘Aliy alipohisi kuwa anafariki dunia, alimuusia mwanawe Al-Hasan akimuambia ; ‘Allaah Allaah (nakuusia) juu ya wake wa Mtume wenu, wasidhulumiwe wakati mpo hai. Na Allaah Allaah (nakuusieni) juu ya Sahibu zake Mtume wenu, kwa sababu Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ameusia (mema) juu yao.’

Kashf al- Ghummah - 2/59 na Muqaatil atw-Twaalibin kilichoandikwa na Al-Asfahaani uk.39

 

Kutoka kwa Urwa bin ‘Abdillaah alisema :

 

Nilimuuliza Abu Ja’afar Muhammad bin ‘Aliy juu ya kuzipamba panga, akasema ; ‘Hapana ubaya, hata Abu Bakr Asw-Swiddiyq alikuwa akiupamba upanga wake (Radhiya Allaahu ‘anhu)’ Nikamuambia : ‘Na unamuita ‘ Asw-Swiddiyq ?’ anasema : ‘Aliinuka kwa haraka sana akaelekea Qiblah, kisha akasema ; ‘Naam (namuita) Asw-Swiddiyq Naam (namuita) Asw-Swiddiyq Naam (namuita) Asw-Swiddiyq, na asiyemuita kwa sifa hii basi hana ukweli wowote duniani wala akhera.’

Kashf al-Ghummah - 2/360.

 

Anasema ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu):

«Nilipokwenda kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kumposa Faatwimah aliniambia: ‘Uza ngao yako kisha niletee thamani yake ili nipate kukutayarishia wewe na binti yangu Faatwimah kitakachoweza kukufaeni.» Anasema ‘Aliy : «Nikaichukua ngao yangu nikaenda nayo moja kwa moja mpaka sokoni nikamuuzia ‘Uthmaan kwa Dirham mia nne. Na baada ya kupokea pesa zangu na baada ya ‘Uthmaan kuipokea ngao yangu, akasema: Ewe Baba yake Hasan, ngao hii si imekuwa yangu na Dirham zimekuwa zako ?» Nikamuambia: «Ndiyo.» Akaniambia: «Basi ngao hii ni zawadi yako kutoka kwangu. »  Nikaichukua ngao na Dirham nikaenda kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) nikaiweka ngao pamoja na pesa mbele yake, nikamhadithia aliyonitendea ‘Uthmaan, akamuombea dua ya kheri. »

Al-Manaaqib/Al-Khawarizmi uk. 252 na Kashf al-Ghummah 1/359 na Bihaar al-Anwaar/Al-Majlisi uk. 39-40

 

Tunamuomba msomaji arudie marejeo yote upate kumbainikia ukweli na ili apate kufikiri na kutanabahi juu ya msimamo wa wenye kuwalaani Maswahaba wakiwemo Makhalifa watatu wa mwanzo wa Waislam.

 

Baada ya kuzisoma kauli hizi za Maimamu wa Ahlul Bayt zinazowapa Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) sifa zao wanazozistahi, kilichobaki hivi sasa ni kwa kila mwenye kudai kuwa anawapenda watu wa nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) nao pia wazitambue haki za Maswahaba hawa (Radhiya Allaahu ‘anhum) kama zilivyotambuliwa na Maimam wao.

Hili ni tumaini letu kwa kila mwenye kuitafuta haki na mwenye kujinasibisha na Ahlul Bayt.

Na baada ya kuujua  ukweli huu asije mtu akaanguka tena ndani ya shimo la kuwalaani na kuwatukana Maswahaba wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na kuwatuhumu kwa ukafiri na unafiki.

Tunamuomba Allaah Atuepushe na shari ya ukafir na unafik.

Wabillahi tawfiyq

 

 

 

Share