Talbiys Ibliys - Ufunikaji (Uhadaifu) Wa Ibilisi

 

 

 

 

TALBIYS IBLIYS

‘UFUNIKAJI WA IBILISI’

 

Shaykhul Islaam Ibn Taymiyyah

Imetafsiriwa Na:  Muhammad Faraj

Na Kupitiwa Na Abu 'Abdillaah

 

 

 

Share

001-Talbiys Ibliys - Ufunikaji (Uhadaifu) Wa Ibilisi: Upambaji Wa Ibilisi - Wasiwasi Katika Swalah: Wudhuu

 

Muhammad Faraj Saalim As-Sa’y

 

 

Talbiys Ibliys

 

Katika kitabu chake kiitwacho ‘Talbiys Ibliys’ (Upambaji wa Ibilisi), mwanachuoni maarufu Shaykhul Islaam Ibn Taymiyah anasema:

 

“Jua ya kwamba mlango mkubwa anaopitia Ibilisi katika kuwaharibia Waislam ibada zao ni mlango wa ‘ujinga katika dini’. Ibilisi huwaingilia watu kwa kupenya kupitia mlango huo kwa raha zake huku akiwapambia na kuziona kuwa ni njema. Kwani Ibilisi keshawaharibia wengi miongoni mwa wafanyao ibada kwa ajili ya kutokujuwa kwao namna ya kumuabudu Mola wao kama anavyotaka kuabudiwa. Ama wale wenye kufahamu, Ibilisi huwaingilia kwa kuibia ibia tu.”

 

Mmoja katika Maulamaa wakubwa aitwae Matraf bin ‘Abdillaah amesema:

“Fadhila ya elimu ni kubwa kupita fadhila ya ibada”.

 

Na hii ni kwa sababu elimu ni nuru inayomuongoza mja kuijua njia sahihi ya kumuabudu Mola wake bila kupunguza wala kuvuka mipaka. Na Allaah Amekwishatuelimisha kupitia kwa Mtume wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), namna gani anatutaka tumuabudu.

Allaah Anasema:

 

ثُمَّ جَعَلْنَاكَ عَلَى شَرِيعَةٍ مِّنَ الامْرِ فَاتَّبِعْهَا وَلا تَتَّبِعْ أَهْوَاء الَّذِينَ لا يَعْلَمُونَ

 

“Kisha tumekuweka juu ya Sharia ya amri yetu, basi ifuate, wala usifuate matamanio ya wale wasiojua (kitu).” Al-Jaathiyah: 18

 

 

Siku ile alipofukuzwa Peponi na kutolewa katika rehma ya Allaah, Ibilisi aliapa kuwa atazifisidi ibada za wanaadamu na kuwakalia juu ya kila  njia iliyonyoka.

Allaah Anasema:

 

قَالَ فَبِمَا أَغْوَيْتَنِي لأَقْعُدَنَّ لَهُمْ صِرَاطَكَ الْمُسْتَقِيمَ

 

“Akasema (Ibilisi); ‘Kwa kuwa umenihukumia upotofu (upotevu) basi nitawakalia (waja Wako) katika njia Yako iliyonyoka (ili niwapoteze).” Al-A’araaf: 16

 

Ibilisi hawaandami wale waliokwishapotoka, lakini moyo wake unaungulika kila anapowaona walio juu ya njia iliyonyoka wakiswali na kufanya ibada zao kama walivyoamrishwa.

 

Ili kuzifisidi ibada zao, Ibilisi hutumia hila nyingi zikiwemo:

1.     Kuwatia wasi wasi.

2.     Kuwafanya wahisi tabu au dhiki wanapoanza kufanya ibada.

3.     Kuwapambia ibada za uzushi na kuwafanya waongeze au wapunguze.

 

Ibilisi humfisidia mtu kwa kumtia wasi wasi akiwa ndani ya ibada na kumfanya ahisi kama kwamba hajaifanya vizuri, hakuikamilisha, ina kasoro, Wudhuu wake haukutimia nk. Na kutokana na hayo humfanya aongeze katika Swala au katika Wudhuu, akidhani kuwa hiyo ndiyo sahihi inayomridhisha Mola wake, bila kuelewa kuwa kufanya hivyo ni kwenda kinyume na mafundisho ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

 

Waliokula Hasara Katika Vitendo Vyao

 

Ibada yoyote isiyokuwa na amri ya Allaah au ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) haifai na haina uzito wowote juu ya mezani.

Allaah Anasema:

 

قُلْ هَلْ نُنَبِّئُكُمْ بِالأخْسَرِينَ أَعْمَالا. الَّذِينَ ضَلَّ سَعْيُهُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَهُمْ يَحْسَبُونَ أَنَّهُمْ يُحْسِنُونَ صُنْعًا.

 

“Sema; ‘Je! Tukujulisheni wenye hasara katika vitendo (vyao)?. Hao ambao bidii zao (hapa duniani) zimepotea bure katika maisha ya dunia, nao wanafikiri kwamba wanafanya ‘amali njema!” Al-Kahf: 103-104

 

Katika kuzifasiri aya hizi, anasema Ibn Kathiyr kuwa; ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema:

 

“Aya hii inamsibu kila mwenye kumuabudu Allaah kinyume na mafundisho ya Mtume wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), na huyo anakuwa mbali na njia inayomridhisha Allaah, akidhani kuwa ‘amali yake hiyo inakubaliwa, wakati ukweli ni kuwa anafanya makosa, na ‘amali zake hizo zinapotea bure.”

 

Allaah pia Anasema:

 

قُلْ إِن كُنتُمْ تُحِبُّونَ اللّهَ فَاتَّبِعُونِي يُحْبِبْكُمُ اللّهُ وَيَغْفِرْ لَكُمْ ذُنُوبَكُمْ وَاللّهُ غَفُورٌ رَّحِيمٌ

 

“Sema; ‘Ikiwa nyinyi mnampenda Allaah, basi nifuateni; (hapo) Allaah atakupendeni na atakughufirieni madhambi yenu. Na Allaah ni Mwenye maghufira (na) Mwenye rehema”.

Aali-‘Imraan: 31

 

 

Kuvuka Mipaka

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema:

 

يَا أَهْلَ الْكِتَابِ لاَ تَغْلُواْ فِي دِينِكُمْ وَلاَ تَقُولُواْ عَلَى اللّهِ إِلاَّ الْحَقِّ

 

“Enyi watu wa kitabu msipindukie mipaka katika dini yenu wala msiseme juu ya Allaah ila yaliyo kweli”. An-Nisaa: 171

 

Na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametukataza kuvuka mipaka katika ibada na kuifanya iwe nzito, kwani yeye (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ameletwa ili kutuwepesishia na si kuyafanyia mambo yakawa magumu.

 

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

“Mumeletwa ili muwepesishe na hamkuletwa kuyafanya mambo yakawa magumu” Al-Bukhaariy, At-Tirmidhiy, Al-Bayhaqiy, An-Nasaaiy na Imaam Ahmad

 

Na katika Hadiyth iliyopokelewa na Imaam Ahmad na An-Nasaaiy, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

“Msipindukie mipaka katika dini kwani kilichowaangamiza waliokuja kabla yenu ni kupindukia mipaka katika dini”.

 

Dalili juu ya ubaya wa kuzusha au kupindukia mipaka katika ibada, tunaipata katika Hadiyth iliyopokelewa na Al-Bukhaariy na Muslim na kusimuliwa na Anas (Radhiya Allaahu ‘anhu) inayosema:

 

“Watu watatu walikwenda katika kila nyumba ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na kuwauliza wakeze vipi Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akifanya ibada zake, na baada ya kujulishwa, mmoja wao akasema:

“Sisi wapi na Mtume wapi. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amekwishasamehewa madhambi yake yote yaliyotangulia na yanayokuja. Ama mimi nitakuwa nikiswali usiku kucha wala sitolala”.

Mwengine akasema:

“Ama mimi nitafunga siku zote na wala sitokula mchana tena”.

Wa tatu akasema:

“Ama mimi sitofunga ndoa kabisa (ili niweze kufanya ibada zangu vizuri).”

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliporudi na kuhadithiwa, alipanda juu ya minbari akasema:

“Nimesikia kuwa watu wanasema hivi na vile. Ama yule anayemjua Allaah zaidi na kumuogopa zaidi kuliko wote ni mimi. Lakini mimi ninafunga na ninakula. ninaamka usiku kuswali na (pia) ninalala, na ninaoa wanawake. Kwa hivyo yeyote atakayekwenda kinyume na mafundisho yangu basi huyo hayuko pamoja nami”.

 

Hadiyth hii inatufundisha umuhimu wa kufuata na ubaya wa kuzusha. Umuhimu wa kusahilisha na ubaya wa kuchupa mipaka katika ibada kwa kisingizio cha kujikurubisha zaidi kwa Allaah, hata kama Niyah ni njema. Niyah pekee haitoshi ikiwa ndani yake hapana muongozo wa mafundisho ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), kwa sababu Allaah Haridhiki na ibada yoyote isipokuwa ile tu aliyoitolea amri Yake.

 

 

Wasiwasi Katika Wudhuu

 

Baadhi ya watu hawaridhiki wanapotawadha kwa kuosha viungo vyao mara tatu kama tulivyofundishwa na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Ibilisi anawatia wasiwasi na utawaona wakizidisha idadi ya kuosha kwa kisingizio cha kuondoa wasiwasi, wakati ukweli ni kuwa huko kuongeza kwao ndio wasiwasi wenyewe.

 

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amekataza kuyafanyia israfu maji.

 

Siku moja alipomuona mmoja katika Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhu) akitawadha, alimuuliza:

“Kwa nini unafanya israfu katika maji?”

Swahaba (Radhiya Allaahu ‘anhu) akauliza:

“Kwani hata katika maji pana israfu?”

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamuambia:

“Ndiyo. Hata kama unatawadha penye mto wa maji yanayokwenda.”

Imaam Ahmad

 

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliwahi kutawadha kwa kuosha viungo vyake mara moja moja, aliwahi pia kutawadha kwa kuviosha mara mbili mbili na mara tatu tatu. Kwenda kinyume na hayo ni kupindukia mipaka katika mafundisho ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Mtu mmoja alimuuliza Imaam Ahmad bin Hanbal:

“Ninaweza kuongeza zaidi ya mara tatu katika Wudhuu?”

Imaam akamjibu:

“La, huwezi. Hafanyi hivyo isipokuwa mwenye maradhi (ya wasi wasi).”

 

Imepokelea kutoka kwa Abu Daawuud kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

“Kutakuwa na watu katika umati wangu wanaopindukia mipaka katika kujitwahirisha na katika kuomba du’aa”

 

Na akasema:

 

“Hakika katika kutia Wudhuu, pana Shaytwaan (mwenye kuwatia watu wasiwasi) anayeitwa Al-Walahan, kwa hivyo jiepusheni na wasiwasi wa Wudhuu”. At-Tirmidhiy

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema:

 

إِنَّهُ لاَ يُحِبُّ الْمُعْتَدِينَ

 

“Yeye (Allaah) hawapendi wapitao mipaka.” Al-A’araaf: 55

 

Kwa vile kuzidisha katika Wudhuu wa mwenye wasiwasi ni katika uchupaji wa mipaka, basi huo unaingia katika zile ibada asizozipenda Allaah.

 

Anasema Ibn Qudaamah, katika kitabu chake kiitwacho “Dhamm Al-lMuwaswasiyn”:

 

“Ukimuuliza mwenye wasi wasi kwa nini unatawadha zaidi ya mara tatu?

Atakujibu: 'Akiba ya maneno, pengine nimekosea au nimepunguza idadi ya kuosha viungo vyangu.'

“Mtu anaweza kuipa sababu anayoitaka,” anaendelea kusema mwanachuoni huyo. “Lakini suali linakuja; “Je, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) au Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) walikuwa wakifanya hivyo?"

Bila shaka jawabu itakuwa ;’La. Hawakuwa wakifanya hivyo’. Kwa sababu kusema kuwa walikuwa wakifanya hivyo, ni kuwazulia uongo."

 

Iwapo tutakiri kuwa hawakuwa wakifanya hivyo, basi itatulazimu na sisi kuacha mwenendo huo, kwani kuuendeleza ni kwenda kinyume na mafundisho ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)”.

 

 

Kuvunjika Kwa Wudhuu

 

Katika wasiwasi ni pale mtu anapokuwa ndani ya Swalah akasikia mingurumo tumboni mwake, akadhani kuwa upepo umekwishamtoka, akaamua kuvunja Swalah na kwenda kutawadha kwa dhana tu.

 

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametukataza kufanya hivyo aliposema:

 

“Mmoja wenu anaposikia sauti tumboni mwake akatia shaka, je, kimetoka kitu (upepo) au hakijatoka? Basi asivunje Swalah isipokuwa kama (ana hakika kuwa) amesikia sauti (ikitoka) au harufu”. Muslim

 

Imepokelewa pia kuwa mtu mmoja alimuuliza Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kuwa; huwa anahisi kila anaposwali kama kwamba upepo unamtoka. Akajibiwa kuwa asivunje Swalah mpaka asikie sauti au harufu. Al-Bukhaariy na Muslim

 

Katika Musnad ya Imaam Ahmad na Sunan za Abu Daawuud, Imeelezwa na Abu Sa’iyd Al-Khudriy (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

“Shaytwaan humjia mtu katika Swalah yake na kumfanya ahisi kama kwamba ametoa upepo, basi mtu asiivunje Swalah yake mpaka asikie sauti au harufu”.

 

Na katika Sunan ya Abu Daawuud, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

“Shaytwaan anapomjia mtu na kumwambia kuwa Wudhuu wako umevunjika”. Basi naye asema (moyoni pake); “Muongo wewe”, isipokuwa pale anaposikia harufu kwa pua yake au sauti kwa sikio lake”.

 

Katika kitabu chake kiitwacho; “Dhamm Al-Muwaswasiyn”, anasema Ibn Qudaamah:

 

“Kwa ajili ya kuyapiga vita maradhi ya wasi wasi, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anatuamrisha kumkadhibisha Shaytwaan, juu ya kuwa kitendo hicho (cha kutoka upepo) kinaweza kuwa kimetokea kweli. Vipi basi mtu anakubali kumfuata Shaytwaan pale uongo wake unapokuwa dhahiri, pale anapoambiwa na Shaytwaan kuwa; “Hukutawadha vizuri au hukutia Niyah sawa n.k., wakati anajua kuwa huo ni wasi wasi wa Shaytwaan tu, na kwamba anajaribu kumchezea”.

 

 

Share

002-Talbiys Ibliys - Ufunikaji (Uhadaifu) Wa Ibilisi: Wasiwasi Katika Kutia Niyah Na Utulivu (At-Twumaaniynah)

 

Wasiwasi Katika Kutia Niyah

 

Katika kutia Niyah ya Swalah, Shaytwaan hupata upenyo pia wa kuwachezea watu na kuwakosesha thawabu nyingi sana.

 

Utamuona mtu anafunga Swalah kisha anaivunja. Na mwengine huendelea hivyo mpaka Imaam anaporukuu, hapo ndipo huifunga Swalah kwa haraka na kurukuu pamoja naye.

 

Ameweza kuihudhurisha Niyah kwa haraka pale Imaam aliporukuu, wakati alishindwa kufanya hivyo tokea mwanzo wa Swalah.

 

Hii ni njia moja wapo ya Shaytwaan kumkosesha thawabu nyingi kama anglifunga Swalah pamoja na Imaam.

 

Wengine kabla ya kufunga Swalah utawasikia wakinyanyua sauti zao wakitamka maneno Fulani na kushadidia maneno hayo, kisha husema; “Allaahu Akbar”, kisha huivunja Swalah na kuanza kutamka tena maneno hayo akidhani kuwa amekosea kuyatamka, na akidhani pia kwamba maneno hayo yamepangwa na Mtume wa  Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), na kwamba akiyakosea Swalah yake inabatilika.

Utamuona akiendelea kukubali kuchezewa na Shaytwaan na kumkosesha thawabu nyingi za kujiunga na Imaam mapema.

 

Ukweli ni kuwa maneno hayo anayotamka, anayodhani kuwa ndiyo Niyah ya Swalah, hayajapata kutamkwa na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), wala na Swahaba zake watukufu (Radhiya Allaahu ‘anhum).

 

Anasema Ibnul Qayyim:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa anapotaka kuswali husema:

“Allaahu Akbar”, kisha hufunga Swalah. Hakuwa akisema kitu kabla yake kama vile; “Uswaliy fardha sSwalaatil Ishaa...” Au kauli zozote katika zile wanazozitamka watu hivi sasa. Hapana Hadiyth Sahihi wala hata dhaifu inayotujulisha kuwa kitendo hiki kimetendwa na Sahaba yeyote au Taabi'i au mmojawapo wa maImaam wanaojulikana kwa ucha Mungu wao. Hapana hata mmoja wao aliyewahi kutamka kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akifanya hivyo kabla ya kufunga Swalah….” (Kitabu ‘ Al-Qawlul Mubiyn Fiy Akhtwail Muswalliyn)

 

Anasema Mama wa Waumini ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha):

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa anapotaka kuswali huanza kwa kusema:

“Allaahu Akbar.” Muslim – 1/357 na 498

 

Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu), anasema kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipomuona mtu mmoja akikosea katika Swalah alimwambia:

“Unapotaka kuswali, tia udhu kisha elekea kibla kisha sema, “Allaahu Akbar”, kisha soma utakachoweza kusoma katika Qur-aan”. Al-Bukhaariy na Muslim

 

Ama ‘Abdullaah bin ‘Umar bin Al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ‘anhuma) alisema:

“Nilimuona Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akianza kuswali kwa kusema “Allaahu Akbar.” Al-Bukhaariy 2/221 na 738.

 

Hizi ni dalili chache katika nyingi zinazotujulisha kuwa kitendo cha kuitamka Niyah hakikuwepo katika mafundisho ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), na kwa ajili hiyo tusimpe fursa Shaytwaan kutuingilia na kutufisidia Swalah zetu au kutukosesha thawabu za kujiunga mapema na Imaam kwa kupitia mlango huo.

 

Imepokelewa kutoka kwa Ibn ‘Aqiyl, kuwa siku moja aliulizwa na mmoja katika watu wenye maradhi haya ya wasiwasi:

“Mimi kila ninapotawadha, huhisi kama kwamba sijatawadha vizuri, na kila ninapofunga Swalah huhisi kama sikuifunga vizuri, nifanye nini?”

Ibn ‘Aqiyl akamjibu:

“Wacha kuswali, kwa sababu wewe huna lazima ya kuswali”.

Alipoulizwa kwa nini alijibu hivyo, alisema:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

‘Haandikiwi dhambi wala thawabu mwendawazimu mpaka awe na akili …” na mtu aliyetawadha akahisi kuwa bado hajatawadha, kisha akafunga Swalah akahisi kuwa bado hajaifunga, huyo akili zake si sawa. Huyo ni mwendawazimu, na mwendawazimu halazimiki kuswali”. (Talbiys Ibliys – Ibn Taymiyyah Uk.169)

 

 

 

 

Utulivu (At-Twumaaniynah)

 

Utulivu (At-Twumaaniynah) ni nguzo muhimu sana katika nguzo za Swalah, na bila ya utulivu Swalah haiwi kamilifu.

Siku moja Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa amekaa Msikitini, akaingia mtu mmoja na kuswali. Baada ya kumaliza akainuka na kwenda kumsalimia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Mtume wa Allaah (Swallah Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamuambia:

“Rudi kaswali tena, wewe bado hujaswali.”

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimrudisha mtu huyo mara tatu, na kila anapomaliza kuswali alikuwa akimuambia:

“Rudi kaswali tena, wewe bado hujaswali.”

Yule mtu akamuambia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

“Sijui kuswali vizuri kuliko hivi, (bora) nifundishe.”

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamuambia:

“Unapotaka kuswali tia wudhuu, kisha elekea Qiblah, kisha soma utakachoweza kusoma katika Qur-aan, kisha rukuu mpaka utulie (tatwmaina - At-Twumaaniynah) na uwe na uhakika kuwa umerukuu (sawa), kisha inuka usimame sawa sawa (At-Twumaaniynah), kisha usujudu mpaka utulie (At-Twumaaniynah) na uwe na uhakika kuwa umesujudu sawa, kisha kaa vizuri mpaka utulie katika kikao chako (Tumaaniyna), kisha sujudu na utulie (At-Twumaaniynah) mpaka uwe na uhakika kuwa umesujudu sawa, kisha ufanye hivyo hivyo mpaka umalize kuswali.” Al-Bukhaariy, Muslim, Abu Daawuud, At-Tirmidhiy, An-Nasaaiy na Ibn Maajah.

 

Hadiyth hii na nyingi kama hizi zinatujulisha kuwa Swalah haiwi kamili bila ya utulivu (At-Twumaaniynah). Nako ni kutulia katika kila kitendo cha Swalah. Mtu anatakiwa atulie mpaka awe na uhakika kuwa ametulia.

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amempa jina la ‘Mwizi’ mtu anayeswali bila utulivu.

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

“Katika wezi wabaya kabisa ni wale wanaoiba katika Swalah zao, hawarukuu kwa ukamilifu wala hawasujudu kwa ukamilifu na hawawi na khushuu.”

 

Na katika riwaya nyingine amesema juu ya ‘Mwizi wa Swalah’:

“Na wala haunyoshi mgongo wake sawa pale anaporukuu na anaposujudu.”

Imaam Ahmad, Al-Haakim na imesahihishwa na Imaam Adh-Dhahabiy.

 

 

Share