07-Imaam Ibn 'Uthaymiyn: Akitoharika Nifaas Au Hedhi Kabla Ya Alfajiri Lakini Akajitoharisha (Ghuslu) Baada Ya Alfajiri Swawm Yake Itasihi?

 

07-Akitoharika Nifaas Au Hedhi Kabla Ya Alfajiri Lakini Akajitoharisha (Ghuslu)

Baada Ya Alfajiri Je, Swawm Yake Itasihi?

 

Fataawaa Mas-ala 60 Kuhusu Hedhi Na Nifaas

 

Imaam Ibn 'Uthaymiyn (Rahimahu-Allaah)

 

Alhidaaya.com

 

 

 

 

SWALI:

 

Mwenye hedhi au mwenye Nifaas akitoharika kabla ya Alfajiri na hakukoga ila baada ya Alfajiri, je, Swawm yake itasihi au hapana?

 

 

JIBU:

 

Naam. Swawm ya mwanamke mwenye hedhi inasihi akitoharika kabla ya Alfajiri lakini hakujitoharisha (ghuslu) ila baada ya Alfajiri. Kadhalika mwenye Nifaas kwani wakati huo atakuwa ni miongoni mwa wenye Swawm na anafanana na mwenye janaba itakapopambazuka akiwa ana janaba basi Swawm yake  inasihi kwa dalili ya kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

فَالْآنَ بَاشِرُوهُنَّ وَابْتَغُوا مَا كَتَبَ اللَّـهُ لَكُمْ ۚ وَكُلُوا وَاشْرَبُوا حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَكُمُ الْخَيْطُ الْأَبْيَضُ مِنَ الْخَيْطِ الْأَسْوَدِ مِنَ الْفَجْرِ ۖ  

Basi sasa waingilieni na tafuteni Aliyokuandikieni Allaah kwenu. Na kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu uzi mweupe (mapambazuko) wa Alfajiri kutokana na uzi mweusi (wa kiza cha usiku).  [Al-Baqarah: 187]

 

Hivyo basi ikiwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ameidhinisha kujamiiana mpaka ibainike Alfajiri,  imelazimika kufanya ghuslu inapoingia tu Alfajiri.

 

Na Hadiyth ya ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) amesema kuwa: “Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akiamka asubuhi akiwa na janaba ya kujamiiana na ahli wake naye akiwa katika Swawm. Yaani: Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  alikuwa hajitoharishi (ghuslu) kutokana na janaba isipokuwa baada ya kuingia Alfajiri.

 

 

Share