32-Du’aa Toka Kwenye Qur-aan Tukufu Na Sharh Yake: Kuokolewa Na Watu Madhalimu

Du’aa Toka Kwenye Qur-aan Tukufu

 

Na Sharh Yake

 

Alhidaaya.com

 

 

32- Kuokolewa Na Watu Madhalimu

 

 

"رَبِّ نَجِّنِي مِنَ الْقَوْمِ الظَّالِمِينَ"

 

“Rabb wangu!  Niokoe na watu madhalimu”.  [Al-Qaswas: (28)].

 

Ni katika du’aa za Nabiy Muwsaa (‘Alayhis Salaam) zilizokariri kwenye Kitabu cha Allaah ‘Azza wa Jalla.  Ndani yake kuna maelekezo toka kwa Allaah Ta’aalaa kwetu ya kushikamana na njia ya kheri na kujiepusha na njia za baatwil ili tuwe katika Hifadhi ya Allaah katika dini yetu na dunia yetu.

 

Ameanza du’aa yake kwa kutawassali kwa Allaah kwa Jina Lake la Rabb. Akamwomba Amwokoe kutokana na dhulma za Fir-‘awn na kundi lake.  Fir-‘awn huyu na wasaidizi wake hawa walijidhulumu wenyewe kwa kukataa wito wa iymaan wa Nabiy Muwsaa (‘Alayhis Salaam) pamoja na miujiza dhahiri waliyoishuhudia wenyewe yenye kuthibitisha ukweli wa wito wake.  Na hii ni mbali na jeuri yao na dhulma zao nyingi walizokuwa wakiwafanyia Bani Israel. Allaah Alimjibu du’aa yake kama ilivyo Ada Yake kwa Manabii na Vipenzi Vyake ambao wanakimbilia Kwake kwenye mambo yao yote na katika hali zao zote.

 

Kumwomba Allaah uokozi kutokana na madhalimu, kama ilivyo ada na mwenendo wa Manabii na Mitume, ilikuwa pia ni sehemu ya du’aa za Waumini wema.  Bibi Aasiyah mke wa Fir-‘awn alimwomba Allaah pia vile vile Amwokoe kutokana na mumewe Fir-‘awn na vitimbi vyake na watu madhalimu.  Qur-aan inatuambia:

 

"وَضَرَبَ اللَّـهُ مَثَلًا لِّلَّذِينَ آمَنُوا امْرَأَتَ فِرْعَوْنَ إِذْ قَالَتْ رَبِّ ابْنِ لِي عِندَكَ بَيْتًا فِي الْجَنَّةِ وَنَجِّنِي مِن فِرْعَوْنَ وَعَمَلِهِ وَنَجِّنِي مِنَ الْقَوْمِ الظَّالِمِينَ"

 

“Na Allaah Amewapigia mfano wale walioamini, mke wa Fir’awn, aliposema: Rabb wangu!  Nijengee nyumba Kwako kwenye Jannah, na Niokoe na Fir’awn na vitendo vyake, na Niokoe na watu madhalimu”.  [At-Tahriym: (11)].

 

 

Bi huyu ameomba aokolewe kutokana na Fir-‘awn dhalimu, kisha akaeneza ombi la kuokolewa kutokana na kila mwenye sifa hii mbaya ya udhalimu.

 

 

Tunapata faida zifuatazo kutokana na du’aa hii:

 

 

1-  Muislamu anatakiwa awe na pupa ya kuomba himaya toka kwa Allaah dhidi ya madhalimu.  Hii ni kutokana na hatari yao kwa dini na nafsi.

 

 

2-  Hakuna kinachovuta neema na kuondosha mabalaa kama du’aa.  Ndio maana ikawa ni kimbilio la Manabii na Vipenzi vya Allaah nyakati zote na mahala popote.

 

 

3-  Umuhimu wa kutawassal kwa Sifa za Allaah wakati wa kuomba du’aa.  Ni kama alivyotawasali Muwsaa (‘Alayhis Salaam) kwa kusema:  “Niokoe”, na hii ni Sifa Tukufu ya kivitendo ya Allaah inayoonyesha ukamilifu wa nguvu, matakwa na utoaji misaada.

 

 

 

Share