Skip navigation.
Home kabah

Dini Ya Kweli Ya Mwenyezi Mungu

 

Mwandishi: Dkt. Abu Amiynah Bilaal Philips

Mfasiri: Muhammad Al-Maawy

 

NI IPI DINI YA KWELI YA MWENYEZI MUNGU?

 

Kila mtu anazaliwa katika hali isiyokuwa ya uchaguzi wake. Dini ya familia yake au ideolojia ya dola inalazimishwa kwake.

 

Kuanzia mwanzo wa kuwepo kwake katika dunia hii. Wakati anapofika miaka ya ujana, anakuwa tayari ametiwa kasumba kuamini kuwa itikadi za jamii yake ndizo sahihi ambazo kila mtu anafaa kuzifuata. Hata hivyo, pindi baadhi ya watu wanapo baleghe na kuwa na akili timamu na kufunuliwa kwao mifumo ya Imani, wanaanza kuuliza usahihi wa Itikadi zao wenyewe. Mtafutaji ukweli mara nyingi anafikia mahali ambapo anatatizika pale anapotambua kuwa kila dini, dhehebu, ideolojia na falsafa yoyote inadai kuwa ndiyo njia ya pekee iliyo sahihi kwa mwanadamu. Kwa hakika, zote zinawahimiza watu kufanya mambo mema na mazuri. Hivyo, ipi ndiyo iliyo sahihi? Haiwezekani zote kuwa sahihi kwa vile kila moja inadai kwamba zile nyengine hazipo sawa. Kwa hivyo, vipi mtafutaji haki na ukweli ataweza kuchagua njia ya sawa.

 

Mwenyezi Mungu Ametupatia sote akili na bongo kutuwezesha kufanya uamuzi huu muhimu. Ni uamuzi muhimu sana katika maisha ya mwanadamu. Kwayo kunategemea mustakbali wake. Kwa hiyo, kila mmoja wetu ni lazima achunguze dalili zilizotolewa bila ya jazba wala upendelea na achague ile inayoonekana kuwa sawa mpaka dalili nyengine zitakapopatikana au kujitokeza.

 

Kama Dini au falsafa nyengine yoyote, Uislamu pia unadai kuwa ndio njia moja na ya pekee katika kumfikia Mwenyezi Mungu. Kwa muono huu haina tofauti na mifumo mingine. Kijitabu hiki kina lengo ya kutoa baadhi ya dalili kwa usahihi wa dai hilo. Hata hivyo, ni lazima kwa wakati wote ifahamike kuwa mtu anaweza tu kuamua njia ya kweli kwa kueka kando mhemuko, jazba na upendeleo ambao mara nyingi zinatupofua katika kuona uhakika wa mambo. Baadaye tu, ndio tutaweza kutumia akili tuliyopewa na Mwenyezi Mungu katika kufanya uamuzi wa kimantiki na wa sawa.

 

Zipo hoja nyingi ambazo zinaweza kutolewa kuunga mkono dai la Uislamu kuwa ni Dini ya kweli ya Mwenyezi Mungu. Zifuatazo ni hoja tatu tu za wazi. Hoja ya kwanza inahusiana na asli yake ya kuwa inatoka kwa Mwenyezi Mungu kwa majina ya Dini na ukamilifu wake katika maana yake. Ya pili inahusu mafunzo ya kipekee na yasiyokuwa na utata wala mafumbo kwa yale mahusiano baina ya Mwenyezi Mungu, mwanadamu na uumbaji. Hoja ya tatu inatokana na hakika kuwa Uislamu unaweza kufikiwa kilimwengu na watu wote kwa wakati wote. Hizi ni sehemu tatu za msingi ambazo mantiki na akili zinaamuru ulazima kwa Dini kutambuliwa kuwa ni Dini ya kweli ya Mwenyezi Mungu. Kurasa zifuatazo zitajaribu kukuuza na kufafanua kwa kina fikra hizi.