Skip navigation.
Home kabah

Majibu Kwa Dr. Zaki Badawi Kwa Fatwa Yake Ya Kupinga Hijaab

a


Imeandikwa na : Alhidaaya.com




بِسْم اللَّه والصَّلاَتُ والسَلامُ عَلَى رَسُولِ اللَّه صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وآلِه وَ صَحْبِهِ وَسَلَّم

Allaah سبحانه وتعالى Amesema:

}}وَأَطِيعُواْ اللّهَ وَأَطِيعُواْ الرَّسُولَ وَاحْذَرُواْ فَإِن تَوَلَّيْتُمْ فَاعْلَمُواْ أَنَّمَا عَلَى رَسُولِنَا الْبَلاَغُ الْمُبِين{{

{{Na mtiini Mwenyezi Mungu, na mtiini Mtume, na tahadharini. Na ikiwa mtageuka basi jueni ya kuwa juu ya Mtume wetu ni ufikisha ujumbe tu  ulio wazi}} Al Maida  5:92

}}وَأَطِيعُواْ اللّهَ وَرَسُولَهُ وَلاَ تَنَازَعُواْ فَتَفْشَلُواْ وَتَذْهَبَ رِيحُكُمْ وَاصْبِرُواْ إِنَّ اللّهَ مَعَ الصَّابِرِينَ{{

Na mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala msizozane  mkaingiwa woga, na zikapotea nguvu zenu. Na subirini. Hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja na wanao subiri}} Al-Anfaal 8:46

Baada ya kutanguliza aya mbili hizo za kumtii Allaah سبحانه وتعالىtungelipenda kutanguliza Swali hili: Kwa nini tumtii Allaah سبحانه وتعالى ?

Jibu ni kwamba tumtii Allaah سبحانه وتعالى kwa sababu Yeye ndiye Muumba wetu, na Yeye ndiye Aliyetuamrisha tumtii kwa kufuata amri Zake na kuacha makatazo Yake Aliyotukataza katika Kitabu Chake Qur'aan pamoja na yale aliyotuamrisha au kutukataza Mtume Wake wa mwisho Muhammad   صلى الله عليه وآله وسلم kama Alivyosema Allaah سبحانه وتعالى:

}}وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا{{

{{Na anacho kupeni Mtume chukueni, na anacho kukatazeni jiepusheni nacho}} Al-Hashr 59:7

Kwa hiyo tunamtii Allaah سبحانه وتعالى kwa sababu katuamrisha, tunaamini kuwa Yupo, tunaaamini Mitume yake wote, na vitabu vyake, na tunaamini siku ya Kiyaama ambayo tutasimamishwa mbele yake tuulizwe na tuhesabiwe kwa vitendo vyetu na tuhesabiwe kama tumemtii au tumemuasi. 

Muhimu tujue kwamba hatumtii Yeye kwa sababu tu yale tunayomtii yana manufaa kwetu na inapokuwa manufaa hayo hayapo tena, basi na kumtii kwe kumekwisha! Hapana.

Sisi Waislamu tujue kuwa tuko katika mipaka ambayo tumewekewa na mafundisho ya dini yetu, hatuwezi kujua wenyewe yapi ni mazuri kwetu na kuamua kuyafuata kwa kutumia akili zetu au kufuata matamanio ya nafsi zetu, bali tunatambua ambayo ni mazuri kwa kipimo cha Kitabu cha Allaah سبحانه وتعالى na Sunnah za Mtume wake kwani katuambia katika Qur'aan:

}}وَعَسَى أَن تَكْرَهُواْ شَيْئًا وَهُوَ خَيْرٌ لَّكُمْ وَعَسَى أَن تُحِبُّواْ شَيْئًا وَهُوَ شَرٌّ لَّكُمْ وَاللّهُ يَعْلَمُ وَأَنتُمْ لاَ تَعْلَمُون{{

{{Mmeandikiwa kupigana vita, navyo vinachusha kwenu. Lakini huenda mkachukia kitu nacho ni kheri kwenu. Na huenda mkapenda kitu nacho ni shari kwenu. Na Mwenyezi Mungu anajua na nyinyi hamjui}} Al-Baqarah 2:216

Na hii ndio imani iliyo thabiti kwa Mu'min mwenye kuamini kuwa kila jambo Alilomkidhia Mola wake ni kheri tu kama alivyosema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم katika hadithi sahihi.  

  ((  عجباً لأمر المؤمن إن أمره كله له خير، وليس ذلك إلا للمؤمن، إن إصابته سَّراء شكر، فكان خيراً له وإن أصابته ضراء صبر فكان خيراً له ((    صحيح مسلم

((Ajabu ya mambo ya Mu'min kwamba mambo yake yote ni kheri, na haiwi hivyo ila kwa Mu'min hasa.  Akifikwa na mema ya kumfurahisha hushukuru na huwa kheri kwake, na akifikwa na madhara husubiri na huwa kheri kwake))Muslim

Maisha ya Muislamu siku hizi popote alipo yamekuwa magumu na yenye mashaka kutokana na matatizo ya kidunia yanayohusu uchumi, siasa na usalama. Matatizo hayo ndiyo yaliyofanya wengi wahamie katika nchi za nje kutafuta maisha bora zaidi. Ingawa Muislamu amepata  baadhi ya faida kuishi nchi za nje na  kuwa na  maisha   bora zaidi kuliko maisha ya nyumbani, haswa zaidi kwa upande wa kiuchumi na labda kielimu, lakini matatizo na madhara ni makubwa na mengi kuliko faida hiyo ndogo anayoipata ya kiuchumi au kielimu. Bila shaka katika moja ya neema ya mwanaadam ni kuwa na uhuru, na kupata raha na  utulivu wa nafsi na mtu kuweza kulea watoto wake katika mwendo wa Kiislamu bila ya kubughudhiwa, kuwekewa vikwazo, au kuathiriwa na mazingira ya nchi hizo.   

Na mada yetu hii ya leo, ndio tunaona mojawapo ya masaibu anayokutana nayo Muislam anayeishi Ulaya hivi sasa. Masaibu au fitna ya kupata khofu ya kuwa alivyo, au kujiweka anavyopaswa kujiweka kwa mujibu wa mafunzo ya dini yake, ndio mtihani mkubwa alionao Muislam Ulaya na haswa Mwanamke. Mtihani wa kupoteza kitambulisho chake cha Uislam; ima kwa kulazimishwa na mazingira yanayomzunguka, au kulazimishwa na Fatwa za ‘Maulamaa’ wa Ulaya!!

Na msiba zaidi ni kwamba ‘viongozi’ wa Kiislamu wengi wao sio wa kuwategemea kuongoza waislam kwa mujibu wa  Amri ya Mola wetu, bali hutumia nafasi na nyadhifa walizonazo kuwapoteza watu kwa kutoa Fatwa bila ya khofu wala wasiwasi kuwa wanamkhalifu Allaah سبحانه وتعالى waziwazi na kupinga Maamrisho Yake katika Qur’an.

Baada ya kutokea mlipuko wa London Dr. Zaki Badawi, kiongozi wa Chuo cha Kiislam London, na Mwenyekiti wa Baraza la Misikiti na Maimam, ametoa Fatwa kuwa wanawake wanaoishi  Uingereza ambako kumekuwa kunatokea matusi na kubughudhiwa wanawake wanaovaa hijaab kuwa wavue hijaab zao ili wasiudhiwe au kudhuriwa, akisema kuwa, "Hijaab asili yake ni kumhifadhi mwanamke asiudhiwe na kudhuriwa" na kuitaja aya hii kama ndio kigezo chake cha kuwataka wanawake wavue Hijaab:

}}يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ وَبَنَاتِكَ وَنِسَاء الْمُؤْمِنِينَ يُدْنِينَ عَلَيْهِنَّ مِن جَلَابِيبِهِنَّ ذَلِكَ أَدْنَى أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ وَكَانَ اللَّهُ غَفُورًا رَّحِيمًا {{

{{Ewe Nabii! Waambie wake zako, na binti zako, na wake za Waumini wajiteremshie nguo zao. Hivyo ni karibu zaidi kuweza kutambulikana wasiudhiwe. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu}} Al Ahzaab:59

Na akasema, "Kama hijaab ndio sababu ya kuudhiwa na kudhuriwa mwanamke Uingereza  basi nasema wavue hijaab ili wasitambulikane na kuvamiwa"  (mwisho wa kumnukuu)

Tunataka hapa kumuuliza Dr. Zaki Badawi au mwengine yeyote anayekubaliana na fatwa hii kuwa, je? Aya hiyo inaunga mkono maoni yake na fikra zake nyembamba zilizopwaya? Je, ayah hiyo ndio makusudio ya fatwa yake au inapingana nayo?

Kwanza: Tukiitazama aya hiyo kwa makini, tunaona kuwa wanawake wameambiwa wajiteremshie nguo zao (wajistiri kikamilifu) na sio wavue au wazitoe hizo nguo zao kama anavyodai.

Dr. Badawi amegusia kwamba 'illah  yaani kusudio la amri katika aya hiyo au kwa maana nyingine sababu hasa ya amri iliyokusudiwa katika aya hii ni kwamba kujifunika (hijaab) ni kwa sababu ya kuwahifadhi wanawake wasiudhiwe. Je, hii ni dalili iliyothibiti katika sheria ambayo imemfanya yeye kutoa Fatwa yake hiyo?  Hebu tutumbukie kidogo ndani ya maana hii na tujue nini maana ya  'illah? (kusudio la amri). 'Illah ni  madhumuni (au kusudio) ya amri inayotolewa katika ayah ambayo ni hukumu au sheria ya Allaah سبحانه وتعالى .

Hivyo baada ya kujua  nini maana ya 'illah, tunaweza kuelezea kuwa kuhifadhika wanawake wasiudhiwe katika aya kuwa si 'illah (kusudio la amri), bali ni faida au matokeo ya kufuata amri. 

Kuna baadhi ya maneno fulani yenye kuonyesha kuwepo 'illah (kusudio la amri) mfano  مِنْ أَجْلِ ذَلِكَ    (Min Ajli Dhaalika )  (kwa sababu ya hayo) Kama katika aya ifuatayo:

}}مِنْ أَجْلِ ذَلِكَ كَتَبْنَا عَلَى بَنِي إِسْرَائِيلَ أَنَّهُ مَن قَتَلَ نَفْسًا بِغَيْرِ نَفْسٍ أَوْ فَسَادٍ فِي الأَرْضِ فَكَأَنَّمَا قَتَلَ النَّاسَ جَمِيعًا وَمَنْ أَحْيَاهَا فَكَأَنَّمَا أَحْيَا النَّاسَ جَمِيعًا{{

{{Kwa sababu ya hayo tuliwaandikia Wana wa Israili ya kwamba aliyemuua mtu bila ya yeye kuua, au kufanya uchafuzi katika nchi, basi ni kama amewaua watu wote. Na mwenye kumuokoa mtu na mauti ni kama amewaokoa watu wote}} Al-Maaidah:32

Au كَيْ  (Kay) (ili)

Mfano:

}}مَّا أَفَاء اللَّهُ عَلَى رَسُولِهِ مِنْ أَهْلِ الْقُرَى فَلِلَّهِ وَلِلرَّسُولِ وَلِذِي الْقُرْبَى وَالْيَتَامَى وَالْمَسَاكِينِ وَابْنِ السَّبِيلِ كَيْ لَا يَكُونَ دُولَةً بَيْنَ الْأَغْنِيَاء مِنكُمْ{{

{{Mali aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwa watu wa hivi vijiji ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na kwa ajili ya Mtume, na jamaa, na mayatima, na masikini, na msafiri, ili yasiwe yakizunguka baina ya matajiri tu miongoni mwenu}} Al-Hashr: 7

Katika mas-ala mengine kunakuweko maelezo baada ya amri kuonyesha  kuweko 'illa (kusudio la amri) Mfano katika aya Suratul-Anfaal Aya ya 60  neno la  تُرْهِبُونَ   turhibuuna (ili kuwatisha) limefuatia baada ya amri kwamba:

}}وَأَعِدُّواْ لَهُم مَّا اسْتَطَعْتُم مِّن قُوَّةٍ وَمِن رِّبَاطِ الْخَيْلِ تُرْهِبُونَ بِهِ عَدْوَّ اللّهِ وَعَدُوَّكُمْ{{

{{Basi waandalieni (wawekeeni tayari) nguvu kama muwezavyo (silaha)  na kwa farasi walio fungwa tayari-tayari, ili kuwatishia maadui wa Mwenyezi Mungu na maadui zenu}} Al-Anfaal:60

Kwa hiyo "ili kuwatisha" ndio kusudio la amri ya kujiandaa kwa kutumia silaha na farasi, ama katika aya ya Hijaab maneno yamekuja kwa ujumla bila ya 'illah.

Badala ya kuweko 'illah (kusudio la amri) katika aya hii ya Hijaab, 

}}ذَلِكَ أَدْنَى أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ{{  

{{Hivyo ni karibu zaidi kuweza kutambulikana wasiudhiwe}}

kumekuwepo na matokeo ya kitendo cha kuvaa hijaab, na sio sababu. Kujiteremshia nguo zao (kuvaa hijaab zao) kutawapa wao utambulisho na kuwalinda na maudhi na bughudha. Kwa hiyo, kulindika wao na maudhi na bughudha kunasababishwa na kujisitiri kwao kama Alivyoamrisha Allaah سبحانه وتعالى

 }}يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ وَبَنَاتِكَ وَنِسَاء الْمُؤْمِنِينَ يُدْنِينَ عَلَيْهِنَّ مِن جَلَابِيبِهِنَّ ذَلِكَ أَدْنَى أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ وَكَانَ اللَّهُ غَفُورًا رَّحِيمًا{{

{{Ewe Nabii! Waambie wake zako, na binti zako, na wake za Waumini wajiteremshie nguo zao. Hivyo ni karibu zaidi kuweza kutambulikana wasiudhiwe. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu}}. Al Ahzaab: 59

Ili kuonyesha na kufahamisha zaidi tofauti ya 'illah (makusudio) na matokeo (results), tuchukue mfano mwengine katika Suratul Ankabuut'  

}}اتْلُ مَا أُوحِيَ إِلَيْكَ مِنَ الْكِتَابِ وَأَقِمِ الصَّلَاةَ إِنَّ الصَّلَاةَ تَنْهَى عَنِ الْفَحْشَاء وَالْمُنكَرِ وَلَذِكْرُ اللَّهِ أَكْبَرُ وَاللَّهُ يَعْلَمُ مَا تَصْنَعُونَ{{

{{Soma uliyofunuliwa katika Kitabu, na ushike Sala. Hakika Sala inazuilia mambo machafu na maovu. Na kwa yakini kumdhukuru Mwenyezi Mungu ndilo jambo kubwa kabisa. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayo yatenda}} Al 'Ankabuut: 45

Hapa kuzuilika na mambo machafu na maovu sio 'illah' (kusudio la amri)  bali ni matokeo (results ) ya kitendo cha Swalah. Hii ni kwa sababu katika 'illah, sheria au hukumu inaambatana na 'illah, maana kwamba ikiwa'illah ipo basi na sheria/hukumu itakuwepo na ikiwa haipo basi pia sheria/hukumu haitokuwepo. Tujiulize Je, ina maana kwamba mtu asiswali ikiwa  ameepukana na mambo machafu na maovu? 

Tunajua kwamba kutokana na aya na hadithi nyingi kuwa Swalah ni fardhi kwa kila mtu hata kwa yule aliye mcha Mungu mbora kabisa ambaye ni Mtume صلى الله عليه وآله وسلم . Na pia mtu anayeswali huenda akawa anafanya mambo machafu na maovu, ambayo inatuonyesha kuwa "kujiepusha na mambo machafu na maovu"  sio 'illah (yaani kusudio la amri la Swalah)  bali ni matokeo ya Swalah.

Na hivi ndivyo vile ilivyo katika aya ya Hijaab, kuwa mwanamke anaweza kuudhiwa japo akivaa hijaab. Au je, ina maana kwamba mwanamke akiwa haudhiwi ndio basi asivae hijaab?  Hivi sivyo kabisa ilivyokusudiwa.

Mwisho tujue kwamba Ma'ulamaa wanaposoma ayah au hadiyth na kutoa sheria/hukumu hawatazami dalili fulani tu pekee bali wanatazama dalili inayoambatana na mas-ala  yenyewe yote.   Kutokana na dalili nyingine zinazotujulisha kuwa hijaab ni fardhi kwa kila Mwanamke Muislamu na kutokana na sababu hii Mafuqahaa hawakuona kuwa "kutokuudhiwa' ni kusudio la amri

Lazima tukumbuke kuwa haipasi kufuata rai ya mtu yeyote ambaye hakuambatanisha maneno yake na hukumu ya maneno ya Muumba, hata kama ni mtaalamu au mwanafalsafa au kiongozi. Hii ni kama kuchagua na kukubali jambo lisilo la Kiislamu ambalo limekatazwa kabisa na sheria ya Allaah سبحانه وتعالى  Ambaye Ametuamrisha tuchague na tukubali yale aliyotufundisha Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  na sio kutoka kwa mtu yeyote mwingine kwani Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  kasema:

((Allaah سبحانه وتعالى hatokunyimeni elimu baada ya kukupeni, lakini itanyakuliwa kutokana na vifo vya Ma'ulamaa walio na elimu.  Kisha kutabakia watu wajinga ambao wakitakiwa ushauri  watatoa hukumu kutokana na rai zao ambazo zitawapoteza wengineo na wao pia watapotoka))      

Na ndio maana watu kama hawa hutoa Fatawa kutokana na rai zao bila ya kufikiria dalili za hukumu. Rai hizi hazina thamani yoyote kwa Muislamu kuzifuata

 Pili : Sababu ya kufanya hivyo kama alivyoamrishwa mwanake wa Kiislam na Muumba Mwenye Hekima, ni kuhifadhika na kulindika na maudhi, bughudha na kudhalilishwa. Na maudhi hayo yanaweza kuja kwa aina mbalimbali na sababu nyingi, mojawapo ambayo ameghafilika nayo Dr. Badawi, ni kubughudhiwa kijinsia ambako kunatokana zaidi na mwanamke kutembea waziwazi na bila stara ya kisheria! Akidhani ametoa suluhisho upande mmoja lakini akiwa amesahau pande mia zingine!

Tatu: Yote anayoamrisha Muumba Mtukufu Mwenye Hekima za Juu, tunapaswa tuyafuate kwa kuitikia na kutii bila falsafa wala miono wala lakini lakini, kwani akili zetu na uerevu tunaozidhania nazo, kwa kujihisi ni Ma-Dr. n.k. haziwezi kufikia chembe ya za Yule Aliyetuumba na kutujaalia akili hizo! Na tutakapojifanya tunaweza kuwa na muono juu ya Maamuzi ya Muumba, basi hapo ndipo penye Maangamizi na Msiba juu ya Msiba.

Anasema Allaah سبحانه وتعالى Kutufungia kabisa milango ile ya rai, miono, mitazamo, na ijtihaad baada ya Yeye au Mtume wake صلى الله عليه وآله وسلم kuamua jambo:

}} وَمَا كَانَ لِمُؤْمِنٍ وَلَا مُؤْمِنَةٍ إِذَا قَضَى اللَّهُ وَرَسُولُهُ أَمْرًا أَن يَكُونَ لَهُمُ الْخِيَرَةُ مِنْ أَمْرِهِمْ وَمَن يَعْصِ اللَّهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا مُّبِينًا{{

{{Haiwi kwa Muumini mwanamume wala Muumini mwanamke kuwa na khiari katika jambo, Mwenyezi Mungu na Mtume wake wanapo kata shauri katika jambo lao. Na mwenye kumuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake basi hakika amepotea upotofu ulio wazi}} Al Ahzaab:36

Suluhisho lingine alilolisahau Dr. Badawi ni aya nyingine katika surah hiyo hiyo ambayo Muumba Mtukufu kaishatoa? Nayo ni:

}}وَقَرْنَ فِي بُيُوتِكُنَ{{

{{Na kaeni majumbani kwenu}}  Al Ahzaab: 33:33

Mbona asitoe ufumbuzi kama huu ambao ni bora zaidi na uliowekwa na Mola wetu?Bila shaka yeye ni miongoni mwa wale Aliowauliza Allaah سبحانه وتعالى : 

}}أَفَتُؤْمِنُونَ بِبَعْضِ الْكِتَابِ وَتَكْفُرُونَ بِبَعْضٍ{{

{{Je! Mnaamini baadhi ya Kitabu na mnakataa baadhi yake}}  Al-Baqarah :2:85

Au ni mwenye kufuata yale yanayompendesha yeye aidha kwa kutafuta maslahi ya nchi anayoishi au kuwaridhisha wenye nchi badala ya kumridhisha Mola wake.

}}فَأَمَّا الَّذِينَ في قُلُوبِهِمْ زَيْغٌ فَيَتَّبِعُونَ مَا تَشَابَهَ مِنْهُ ابْتِغَاء الْفِتْنَةِ وَابْتِغَاء تَأْوِيلِهِ{{

{{Ama wale ambao nyoyoni mwao umo upotovu wanafuata zile za mifano kwa kutafuta fitna, na kutafuta maana yake; na wala hapana ajuaye maana yake ila Mwenyezi Mungu}} Al ‘Imraan:7

Ndugu Waislamu, je, tumefikiria nini madhara ya Fatwa kama hii? Na matokeo yake yatakuwa nini?  

Kuna hatari kubwa watakapoanza wanawake walio dhaifu au wale waliokuwa hawako tayari kuvaa Hijaab, au wale waliokuwa bado hawajakinai nafsi zao kuvaa vazi hilo, kuelekea katika kukhalifu amri ya Mola wao na kujikuta wametekeleza amri ya kiumbe! Na ndio mwanzo wa kuachwa Kitabu cha Mwenyeezi Mungu na kupuuzwa na kufuatwa rai za wanaoonekana ni Wanachuoni!!

Vile vile kwa sababu tayari fitna za wanawake zilikuwa zimeshashamiri katika zama zetu hizi, kuna hatari kuwa fitna zitazidi kuenea na heshima ya mwanamke itapotea tena kabisa na atakuwa hana tofauti na mwanamke wa kikafiri katika mavazi yake, maadili yake, na mengine mengi, mwanzo ni huu wa kuvua hijaab, kisha pole pole yatafuata mengi ya kuwaiga makafiri ili tukubalike katika jamii zao na ndipo yatathibiti zaidi yale maneno maarufu ya Mtume  ambayo tayari yashathibiti, nayo ni:  

 ((عن ابي سعيد الخضري رضي الله عنه عن النبي صلى الله عليه وآله وسلم  قال: لتتبعن سنن من كان قبلكم شبراً شبراً، وذراعاً بذراع، حتى لو دخلوا جحر ضب تبعتموهم قالوا: يا رسول الله اليهود والنصارى؟ قال: فمن؟))  رواه البخاري  ومسلم

 ((Imetoka kwa Abu Sa'iyd Al-Khudhriy رضي الله عنه   - Kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم    kasema: “Mtafuata nyendo  za wale waliokuja  kabla yenu kiganja kwa kiganja, dhiraa kwa dhiraa, mpaka itafika hadi wakiingia katika shimo la kenge, na nyinyi mtaingia pia.” Wakasema (Maswahaba): “Ewe Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  (je, unamaanisha) Mayahudi na Wakristo? Akasema صلى الله عليه وآله وسلم hivyo nani basi mwengine?)) Al Bukhari na Muslim

Lakini amri hiyo haitofuatwa na wanawake wote bali wale walio dhaifu katika imani zao, wenye kukhofu binaadamu zaidi ya Mola wao na wale walio kama bendera fuata upepo, kama Alivyosema Allaah سبحانه وتعالى

}}وَمِنَ النَّاسِ مَن يَقُولُ آمَنَّا بِاللَّهِ فَإِذَا أُوذِيَ فِي اللَّهِ جَعَلَ فِتْنَةَ النَّاسِ كَعَذَابِ اللَّهِ وَلَئِن جَاء نَصْرٌ مِّن رَّبِّكَ لَيَقُولُنَّ إِنَّا كُنَّا مَعَكُمْ أَوَلَيْسَ اللَّهُ بِأَعْلَمَ بِمَا فِي صُدُورِ الْعَالَمِينَ }}  {{وَلَيَعْلَمَنَّ اللَّهُ الَّذِينَ آمَنُوا وَلَيَعْلَمَنَّ الْمُنَافِقِينَ{{

{{Na katika watu wapo wanao sema: Tumemuamini Mwenyezi Mungu. Lakini wanapo pewa maudhi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, wanayafanya mateso ya watu kama ni adhabu ya Mwenyezi Mungu. Na inapo kuja nusura kutoka kwa Mola wako Mlezi husema: Hakika sisi tulikuwa pamoja nanyi. Kwani Mwenyezi Mungu hayajui yaliomo vifuani mwa walimwengu.

{{Na hapana shaka Mwenyezi Mungu atawatambulisha walio amini, na atawatambulisha wanaafiki}} Ankabuut:10,11

Au vile vile kama mfano wengine wanaokuwa na imani wakati wa kheri tu, na wakati wakipata misukosuko kidogo huwa dhaifu katika imani zao na kumsahau Mola wao kuwa Ndiye mwenye uwezo wa Kuwaondoshea hiyo misukosuko, nayo hii ni kukosa Tawakkul kwa Allaah سبحانه وتعالى :

}}وَمِنَ النَّاسِ مَن يَعْبُدُ اللَّهَ عَلَى حَرْفٍ فَإِنْ أَصَابَهُ خَيْرٌ اطْمَأَنَّ بِهِ وَإِنْ أَصَابَتْهُ فِتْنَةٌ انقَلَبَ عَلَى وَجْهِهِ خَسِرَ الدُّنْيَا وَالْآخِرَةَ ذَلِكَ هُوَ الْخُسْرَانُ الْمُبِينُ{{

{{Na katika watu wapo wanao muabudu Mwenyezi Mungu kwa ukingoni. Ikimfikia kheri hutulia kwayo, na ukimfikia msukosuko hugeuza uso wake. Amekhasiri dunia na Akhera; hiyo ndiyo khasara iliyo wazi}} Al Hajj: 11

Misukosuko, tabu, dhiki na kila aina ya shida ni katika kumpa mitihani mwanadamu kumtazama vipi atapokea mitihani hiyo. Je, atakuwa na subira? Au ataterereka na kuyumba?

Na hivi ndivyo Allaah سبحانه وتعالى Anavyotaka Kutupima katika mitihani hiyo:

}}وَلَنَبْلُوَنَّكُمْ حَتَّى نَعْلَمَ الْمُجَاهِدِينَ مِنكُمْ وَالصَّابِرِينَ وَنَبْلُوَ أَخْبَارَكُمْ{{

{{Na bila ya shaka tutakujaribuni mpaka tuwadhihirishe wapignao Jihadi katika nyinyi na wanao subiri. Nasi tutazifanyia mtihani khabari zenu}} Muhammad:31

Vile vile ni mojawapo ya sababu ya kuwatambulisha wale waliothibitika na imani zao na wale walio dhaifu, kama vile kuchambua mchele na pumba:

}}مَّا كَانَ اللّهُ لِيَذَرَ الْمُؤْمِنِينَ عَلَى مَآ أَنتُمْ عَلَيْهِ حَتَّىَ يَمِيزَ الْخَبِيثَ مِنَ الطَّيِّبِ{{

{{Haiwi kwa Mwenyezi Mungu kuwaacha Waumini katika hali mliyo nayo mpaka apambanue wabaya na wema}} Al ‘Imraan 179

Kwa hivyo Muislamu Mu'min aliyethibitika imani yake hawezi kusumbuliwa na mitihani ya Mola wake, bali huipokea  na kuikabili bila ya khofu yoyote, kuwa na tawakkul na kuamini kuwa hakuna lolote litakalomsibu ila lile tu alilokidhiwa na Mola wake hata kama kuna nguvu kubwa vipi mbele yake inayomkabili kama alivyosema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم katika hadithi hii sahihi:

((عَنْ أَبي العَبَّاسِ عَبْدِ اللهِ ابْنِ عَبَّاس رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُمَا  قَال :َ كُنْتُ خَلْفَ النَبيِّ صلى الله عليه وآله  وسلم     يَوْمًا فَقَالَ :( يَا غُلَامُ إِنِّي أُعَلِّمُكَ كَلِمَاتٍ : احْفَظِ اللَّهَ يَحْفَظْكَ احْفَظِ اللَّهَ تَجِدْهُ تُجَاهَكَ إِذَا سَأَلْتَ فَاسْأَلِ اللَّهَ وَإِذَا اسْتَعَنْتَ فَاسْتَعِنْ بِاللَّهِ وَاعْلَمْ أَنَّ الْأُمَّةَ لَوْ اجْتَمَعَتْ عَلَى أَنْ يَنْفَعُوكَ بِشَيْءٍ لَمْ يَنْفَعُوكَ إِلَّا بِشَيْءٍ قَدْ كَتَبَهُ اللَّهُ لَكَ وَإِنْ اجْتَمَعُوا عَلَى أَنْ يَضُرُّوكَ بِشَيْءٍ لَمْ يَضُرُّوكَ إِلَّا بِشَيْءٍ قَدْ كَتَبَهُ اللَّهُ عَلَيْكَ رُفِعَتْ الْأَقْلَامُ وَجَفَّتِ الصُّحُفُ ))  رَوَاهُ التِّرْمِذِيُّ  وَقَالَ: حَدِيثٌ حَسَنٌ صَحِيحٌ.

((Kutoka kwa Abul ‘Abbaas Abdullah Ibn ‘Abbaas رضي الله عنهما  ambaye alisema: Siku moja nilikuwa nyuma ya Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akaniambia: Kijana nitakufundisha maneno (ya kufaa); Mhifadhi Allaah سبحانه وتعالى (fuata maamrisho Yake na chunga Mipaka Yake) Atakuhifadhi.  Muhifadhi Allaah سبحانه وتعالى na utamkuta mbele yako.  Ukiomba, muombe Allaah سبحانه وتعالى, ukitafuta msaada tafuta kwa Allaah سبحانه وتعالى. (lazima) ujue kuwa ikiwa taifa zima litaungana kukunufaisha wewe kwa kitu, basi hutonufaika ila tu kwa kile alichokwishakuandikia Allaah سبحانه وتعالى na wakikusanyika kukudhuru kwa chochote, hotodhurika ila tu kwa kile Allaah سبحانه وتعالى alichokwishakuandikia (kuwa kitakudhuru). Kwani Kalamu zimeshanyanyuliwa (kila kitu kishaandikwa) na sahifa zimeshakauka (Hakuna kupangwa tena wala kupanguliwa) Imesimuliwa na At Tirmidhy na kasema ni hadiyth Hasan Sahihi.

Naam, ndugu Waislamu, hii ndiyo tawakkul hasa inayotupasa sote tuwe nayo kwa kuthibitika na maamrisho ya Mola wetu mahma itakavyokuwa mitihani wenyewe, na mwenye kutawakkal kwa Mola wake basi Anamtosheleza kabisa katika mambo yake yote: 

}}وَمَن يَتَوَكَّلْ عَلَى اللَّهِ فَهُوَ حَسْبُه{{ُ

{{Na anaye mtegemea Mwenyezi Mungu Yeye humtosha}}At-Twalaaq: 65:3

Mwisho mfano mzuri kabisa tunao wa masahaba wetu Al-Kiraam walipofikwa na mtihani mbali mbali kutokea mwanzo kabisa walivyokuwa wakiingia katika Uislamu walivumulia adhabu za makafiri na hivyo ndivyo Alivyotaka Allaah سبحانه وتعالى Kuwatazama imani zao kama Alivyosema:

 }}الم {{

}}   أَحَسِبَ النَّاسُ أَن يُتْرَكُوا أَن يَقُولُوا آمَنَّا وَهُمْ لَا يُفْتَنُونَ{{

}}  وَلَقَدْ فَتَنَّا الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ فَلَيَعْلَمَنَّ اللَّهُ الَّذِينَ صَدَقُوا وَلَيَعْلَمَنَّ الْكَاذِبِين{{

{{Alif Lam Miym}}

{{Je! Wanadhani watu wataachwa kwa kuwa wanasema: Tumeamini. Nao wasijaribiwe?}}

{{Hakika tuliwajaribu walio kuwa kabla yao, na kwa yakini Mwenyezi Mungu atawatambulisha walio wa kweli na atawatambulisha walio waongo}} Ankabuut 29:1-3

Na hata baada ya imani zao kuwa zimethibitika, mitihani iliendelea na matokeo yalikuwa ni vile vile kuthibitika imani zao japokuwa walikabiliwa na khofu za ajabu. 

}}الَّذِينَ قَالَ لَهُمُ النَّاسُ إِنَّ النَّاسَ قَدْ جَمَعُواْ لَكُمْ فَاخْشَوْهُمْ فَزَادَهُمْ إِيمَاناً وَقَالُواْ حَسْبُنَا اللّهُ وَنِعْمَ الْوَكِيلُ{{

}} فَانقَلَبُواْ بِنِعْمَةٍ مِّنَ اللّهِ وَفَضْلٍ لَّمْ يَمْسَسْهُمْ سُوءٌ وَاتَّبَعُواْ رِضْوَانَ اللّهِ وَاللّهُ ذُو فَضْلٍ عَظِيم{{ٍ

{{Walio ambiwa na watu: Kuna watu wamekukusanyikieni, waogopeni! Hayo yakawazidishia Imani, wakasema: Mwenyezi Mungu anatutosha, naye ni mbora wa kutegemewa}}

{{Basi wakarudi na neema na fadhila za Mwenyezi Mungu. Hapana baya lilio wagusa, na wakafuata yanayo mridhi Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila kuu}} Al-'Imraan 3:173-174

Tulipokuwa tukitazama habari kwenye BBC leo hii  tarehe 05 August, 2005,    tukasikia tena matangazo hayo ya hiyo Fatwa ya Dr Badawi, na wakaletwa wanawake wa Kiislam wakitoa maoni yao kuhusu Fatwa hiyo, alhamduliLLaah bado kuna kheri nyingi, wanawake wengi walipinga Fatwa hiyo na mmoja wao aliyevaa miwani akasema, “Hijaab ni jambo wajibu tuliyoamrishwa nayo, Hijaab si kama miwani unayovaa machoni, ukipenda unavaa na ukipenda unavua”.

Dr. Badawi hakuanza fikra zake hizi za kupinga Hijaab leo au siku za karibuni, wanafunzi wanaosoma katika Chuo chake wanasema kuwa hata masekretari wake hawavai Hijaab tangu siku nyingi!

Vilevile kwa kutaka kukubalika katika jamii ya kiingereza, na kama anavyosifiwa na vyombo vya habari vya Uingereza kuwa ni Sheikh au Mwanachuoni mwenye msimamo 'laini' au wa 'kati na kati', amekuwa akilegeza sheria nyingi za dini na hata kuzipinga nyingine. Anajulikana kwa misimamo ya kutetea wanawake au 'kudai haki za wanawake' n.k.[kama kwamba wanawake walikuwa hawana haki!!] )

Fatwa kama hizi za Masheikh kama hawa ndugu waislam si ngeni katika zama hizi zetu za fitna na mitihani. Masiku ya nyuma tulimsikia aliyekuwa Mufti wa Misri na sasa ni Sheikh Mkuu wa Azhar, Sheikh Muhammad Sayyid Twantawiy, aliyeunga mkono nchi ya Ufaransa kupiga marufuku Hijaab!

Vilevile tulimsikia mwanamke Amina Waduud, aliyeswalisha wanaume huko Marekani na mifano kama hiyo ni mingi ndugu waislam, na inazidi kutupambanulia na kutuchujia walio wema miongoni mwetu na wale waharibifu.

Miongoni mwa Fadhila za Hijaab ni:

-Hijaab ni UtiifuMola Mtukufu na Mtume wake.

-Hijaab ni Stara

-Hijaab ni Ucha Mungu

-Hijaab ni Imani

-Hijaab ni Twahara

-Hijaab ni Hayaa

-Hijaab ni Kinga

 

Na Miongoni mwa madhara ya kujiacha wazi na kutojistiri kisheria:

-Ni Maasi, kumuasi Mwenyeezi Mungu na Mtume wake

-Ni madhambi makubwa yenye kuangamiza

-Ni kuvuta laana na kufukuza Rahma za Mwenyeezi Mungu

-Ni katika sifa za watu wa motoni

-Ni kiza na kukoseshwa nuru siku ya Kiyama

-Ni Unafiki

-Ni Fedheha

-Ni Uchafu

-Ni Sunnah ya Ibilisi

-Ni mwendo wa Kiyahudi

-Ni Ujahiliya wenye Uvundo

-Ni Upotofu uliyojivuruga

-Ni Mlango wa shari uendeleao

Yote haya ndugu waislam, yana dalili kutoka katika Qur’an na Sunnah, tumeacha kunukuu ayah na hadiyth kwa kufupisha makala hii.

Allaahuma Tuthibitishe Imani zetu na Uturuzuku Tawakkul daima.  Amiyn.