Soma Kwa Jina La Mola Wako Aliyekuumba
‘Abdun-Naaswir Hikmany
Assalamu ‘alaykum wa Rahmatullaahi wa Barakatuh;
Dakika zinakatika
Mali unaitafuta
Wiki zinaanguka
Elimu hutaikuta
Miezi inayeyuka
Nafsi unaifuata
Miaka inachomoka
Huna unachopata
Umri umemaliza
Fadhila hujazipata
Ewe mwenye macho ona
Ona yanayopasia
Ona mafunzo ya maana
Yayakayokusaidia
Ona ya kuonekana
Yasiyokuwa na doa
Dini mukikamatana
Atakupenda Jalia
Upate kukutana
Mola Kakufurahikia
Hapana uficho wowote kwa Muislamu ambaye moyo wake umesalimika na fikira zilizonyooka, kwamba utukufu wa elimu haupingwi, na yaliyopokelewa katika fadhila zake hiyo elimu, katu hayadhibitiki. Allaah (Subhaanahu Wataala) Anasema:
{{Je wanalingana wale wanaojua na wale wasiojua?}} [Az-Zumar: 9]
Allaah pia Anaelezea daraja ya wale waliopata elimu:
{{Atawainua Mwenyezi Mungu wale walioamini miongoni mwenu, na wale waliopewa elimu wana daraja kubwa}} [Al-Mujaadilah: 11]
Tusiache kukumbuka kwamba kutafuta elimu ni faradhi kama ilivyo ‘Ibaadah ya Swalaah. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Kutafuta elimu ni faradhi juu ya kila Muislamu.” Ibn Maajah na at-Tirmidhiy
Fadhila za kutafuta elimu ni kurahisishiwa njia nyepesi ya kuingia Peponi. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anasema: “Mwenye kufuata njia katika kutafuta ndani yake elimu, Allaah Atamrahisishia njia ya Peponi.” Al-Bukhaariy
Waislamu tunajiona tumetosheka na elimu, kushughulishwa sana na pumbazo za dunia kama vile sinema, mipira, miziki n.k. Wengine wanafurutu ada kwa kudharau tu elimu kama ilivyo ibada ya Swalaah. Imaam ash-Shaafi’i (Radhiya Allaahu ‘Anhu) anasema: “Kujishughulisha na elimu ni bora zaidi kuliko Swalah za Sunnah.” Imaam anaendelea kusema kwamba; “Hapana baada ya faradhi kitu kilicho bora zaidi kuliko kutafuta elimu.”
Ajabu zaidi, elimu kwa siku za leo inapatikana kwa urahisi na uwepesi zaidi. Alhamdulillaah kuna mitandao ya kila aina kuhusu masuala ya Kiislamu. Wapo baadhi ya wanaharakati wanatumia wakati wao bila ya malipo kuwatumia wenziwao barua pepe kuhusu elimu hii. Lakini ni wachache wanaotumia rasilimali hizi. Baadhi yao, hufikia kuzifuta tu barua pepe zinazoletwa kwao bila hata kuzipitia.
Tambua ya kwamba, utukufu wa elimu ulio na cheo na ufakhari kuisoma, ni Elimu ya Fiqhi yenye kuchimbuliwa katika Qur-aan na Sunnah. Iko dhamana kwa mwenye kupita njia hiyo kuingia Peponi. Kwa elimu hii, ndio Muislamu huweza kupambanua halali kutokana na haramu.
Akili zimetekwa nyara kutafuta rizki zaidi na anasa, hadi kufikia kuidharau elimu ya Kiislamu.
Basi tunamwomba Mwenyezi Mungu Atuzindushe katika Diyn na Atufungulie ufunguzi wa wenye kujua, Atupe hekima na busara mfano wa mbora wa Mitume Anbiyai na Mitume Mursaliyna, na ziwe pia juu ya ‘ali zake na Swahabah zake wote. AAMIYN
»
- Login or register to post comments
- Email this page
- Chapisha


