Mirungi Ni Haraam? Vipi Mtu Aweze Kuacha Kutumia?

 

Mirungi Ni Haraam? Vipi Mtu Aweze Kuacha Kutumia?

 

www.alhidaaya.com

 

SWALI:

 

Naimani wewe ni mzima wa afya na mimi ni mzima nashukuru Allah kwa kunipatia Pumzi siku ya leo.  

swali langu ni je mirungi ni haramu? Na je nifanyeje ili ndugu yangu aache kutumia? Wabillah tawfiq. 

 

 

JIBU: 

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Mwanzo kabisa ni kuwa mirungi ni haramu katika Dini yetu ya Kiislamu kwa madhara yake maovu sana katika nyanja tofauti. Miongoni mwazo ni: Kufuja pesa kwa kitu kisichokuwa na manufaa, kuharibu afya ya mlaji pamoja na magonjwa na madhara mengi ambayo yanatokana nayo kama kuvunja nyumba kwa kuleta talaka baina ya wanandoa, kuleta uhalifu na wizi na maovu mengine mengi.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

 

وَلَا تُلْقُوا بِأَيْدِيكُمْ إِلَى التَّهْلُكَةِ ۛ وَأَحْسِنُوا ۛ إِنَّ اللَّـهَ يُحِبُّ الْمُحْسِنِينَ ﴿١٩٥﴾

wala msijitupe katika maangamizi kwa (kuzuia) mikono yenu isitoe. Na fanyeni ihsaan Hakika Allaah Anapenda wafanyao ihsaan. [Al-Baqarah: 195]

 

  

Uislamu umekuja kuyathibiti maslahi ya wana Aadam wote na kitu chochote ambacho kina madhara basi huwa kimekatazwa kwa kuchunga ule msingi wa kuihifadhi nafsi 'Hifdhwun-Nafs'. Na kwa madhara yote hayo basi shariy’ah imejitokeza moja kwa moja kukataza ulaji wa mirungi. Taabu na tatizo linatokea kwa ma-Shaykh ambao ima kwa maslahi yao kwa sababu ya uhaba wa elimu wanahalalisha lakini kufanya hivyo kwao hakuwezi kufanya jambo haraam kuwa halaal. 

 

Ama kumtoa ndugu yako katika ulaji wa majani hayo inategemea anakula kiasi gani. Je, yeye ni mlaji wa starehe tu au ni yule ambaye ni lazima apate kila siku? Katika hali zote inatakiwa juhudi za juu kwa upande wako ili umwokoe na maafa makubwa yanayomkumba. Ushauri wetu ni kuwa ufuate mfumo ufuatao nasi twakuombea tawfiki katika hilo: 

 

1-Kumfahamisha uharamu wake:

 

Mara nyingi Waislamu hufanya kitu cha haramu kwa kutojua uharamu wake. Hivyo, ni juu yako kumfahamisha hilo. Uharamu wake umetajwa na Shaykh al-Amiyn Mazrui katika Qur-aan Tukufu, juzuu ya kwanza. Pia zipo kaseti za wataalamu wa Kiislamu katika nyanja ya sayansi na udaktari ambao wametoa madhara yake.

 

 

2- Umauti:

 

Zungumza naye kuhusu suala hilo la kuwa sote tutakuwa ni wenye kuaga dunia na kwenda kuhukumiwa na Aliye Muadilifu. Je, sisi tumejiandaa vipi kwa suala hilo? Tupo tayari kukutana na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)? Mweleze umuhimu wa kuweza kuihesabu nafsi yake kwa yote ambayo nafsi inafanya mazuri na maovu na ajaribu kuyapima yepi ni mengi. Hilo linaweza kumsaidia.

 

3-Kielelezo Chema:

 

Jaribu kumpatia mawaidha kutumia ruwaza njema za watangu wema na jinsi gani walikuwa na ari ya kuitafuta haki na kufanya juhudi kuifuata pindi wanapoipata. Mueleze jinsi gani Maswahaba (Radhwiya Allaahu 'Anhum) walivyokuwa ni wanywaji vileo (ulevi) kwa kupindukia lakini pindi Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  Alipoteremsha Aayah ya 90 hadi 91 katika Suwratul-Maaidah walivyoacha papo hapo bila kusita. Tafuta vitabu vya maisha ya watu wema vilivyo sahihi na ujaribu kumuelimisha katika hayo.

 

4-Marafiki:

 

Urafiki na uchaguzi wa rafiki au marafiki ni muhimu sana. Mara nyingi utakuta mtu ameingia katika wema au uovu kwa sababu ya urafiki. Ndio kwa ajili hiyo Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika Hadiyh iliyonukuliwa na Al-Bukhaariy na Muslim akafananisha urafiki mwema na muuzaji manukato ambayo anaweza ima akakupa hadiya au akakupaka na rafiki muovu ni kama kusuhubiana na mfua chuma. Huyu ima ataunguza nguo yako au utatoka kwake na harufu mbaya. Hivyo, jaribu wewe kama ndugu mwema kusuhubiana naye na kumtoa katika magenge na mabaraza ambayo hayafaidishi. 

 

Mbali na yote hayo itategemea yeye mwenyewe ataka kuwaje. Je, anataka kubadilisha maisha yake au anataka kubaki kama alivyo? Lakini letu sisi ni kufikisha ujumbe kama ulivyo na kutia juhudi pamoja na kupanga mikakati na kumwachia mengine Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa). Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

  إِنَّ اللَّـهَ لَا يُغَيِّرُ مَا بِقَوْمٍ حَتَّىٰ يُغَيِّرُوا مَا بِأَنفُسِهِمْ ۗ  

  Hakika Allaah Habadilishi yale yaliyoko kwa watu mpaka wao wenyewe wabadilishe yale yaliyomo katika nafsi zao.  [Ar-Ra’d: 11]

 

Mpatie Makala zifuatazo:

 

 

Kokeni, Hiroini, Bangi, Mirungi - Haramu

Mirungi - 1

Mirungi - 2 (Historia, Madhara Na Mikasa)

Mirungi - 3 (Mwisho) - Fataawa Za Wanachuoni

Mirungi Ni Jamii Moja Na Bangi

Mirungi - Majani ya Mashetani

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share