Utaratibu Sahihi Wa Kufanya Ruqya - 2 Tiba Ya Jicho la Husda Na Uchawi
(Na Fat-hi Al-Jundii)
Imefasiriwa na Ummu Ashraf
Tiba Ya Jicho La Husda
Uwezo wa kuwadhuru wengine kwa kuwatazama au kuonea kijicho ambao hujulikana kama “kijicho” kweli upo. Ibn Abbas kasimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kasema: “madhara ya Kijicho (al-ayn) kweli yapo. Kwani kama kungelikuwa na jambo la kuitangulia kadari basi lingekuwa ni dhara la kijicho” (Muslim).
Ili kuzuwia madhara ya kijicho, mtu akiona mtu au jambo la kumpendeza machoni na akachelea atashidwa kuizuwia nafsi kulihusudu au kulionea kijicho, basi aseme “maa shaa-Allaah (akitakacho MwenyeziMungu kiwe ndicho huwa!) na kisha amuombe MwenyeziMungu amjaalie kheri mtu huyo aliyemtazama au akijaalie kheri kitu alichokitazama.
Tiba ya kijicho yaweza kufanyika bila kujali kama mtu aliyemtazama mwenziwe kwa kijicho kajulikana au hakujulikana. Ikiwa mtu aliyemuonea mwenziwe kijicho kajulikana basi ushahidi wa jinsi ya kufanya tiba unapatikana katika Hadith ifuatayo:
Abu Umamah ibn Sahl ibn Hunayf kasimulia hivi: “Baba yangu, Sahl ibn Hunayf, alifanya josho (ghusl) pale al-Kharrar. Akavua juba alilokuwa amelivaa huku Amir ibn Rabia akimtazama, na Sahl alikuwa na ngozi nyororo nyeupe.
Amir akasema: “Sijapata kuona (ngozi) mfano wa hii ambayo nimeiona leo, haifanani hata na ngozi ya mwanamwali.” Papo hapo Sahl akawa mgonjwa na hali yake ikawa mbaya sana.
Mtu mmoja akaenda kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na kumwambia kuwa Sahl ni mgonjwa na asingeweza kujimudu kuja pale kwa Mtume. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akaja pale alipokuwa Sahl. Sahl akamsimulia kilichotokea wakati alipokuwa na Amir.
Mtume wa Allaah akasema, “kwa nini mmoja wenu anamuua nduguye? Kwa nini (wewe Amir) hukusema ‘Tabarak-Allaah’ (MwenyeziMungu Akujaalie kheri)? Kijicho kipo kweli.”
Kisha Mtume akamwambia Amir, ‘tia udhu kwa ajili ya mwenzio’. Amir akatia udhu. Baada ya Amir kutia udhu, Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akanyunyiza maji ya udhu ya Amir kichwani na mwilini mwa Sahl. Halafu Sahl akaondoka pamoja na Mtume na hakuwa na ugonjwa tena”. (Ahmad).
Endapo mtu aliyemuonea kijicho mwenziwe hajulikani, basi tiba inaweza kufanywa kwa ruqyah, duwa zinazoswihi za Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) zikiambatana na unyenyekevu uliojaa ikhilasi kwa Allaah.
MwenyeziMungu daima huitikia maombi ya wenye shida.kama isemavyo Qur’an, “Au yule anayemjibu anayedhikika amwombapo na kuondoa dhiki (yake)..?” (27:62).
Ibn Qayyim kasema: “miongoni mwa njia za kuomba ulinzi wa MwenyeziMungu na zile zinazojumuisha ruqya ni: usomaji wa mara kwa mara wa Surat al-Falaq, surati An-Nasi, surati Al-Fatiha na Ayatul Kursiyu.
Mtu pia asome dua za Mtume kama hizi:
*Kwa maneno haya thabiti ya Allaah, najikinga Kwake na shari aliyoiumba.
*Kwa maneno thabiti ya Allaah, naomba Ulinzi Kwake dhidi ya kila shetani, kila mnyama hatari na kila jicho baya.
*Kwa maneno thabiti ya Allaah ambayo si Muumini wala si muovu anayeweza kuyakhalifu, najikinga Kwake na shari ya alivyoviumba, akavipa uhai na akavizalisha.
*Allaah Anatutosheleza na ndiye Mlinzi bora kabisa. Allaah Ananitosha. Hakuna mungu isipokuwa Yeye. Kwake Yeye nategemeza imani yangu, Naye ndiye Mola wa Arshi kuu.
Watu ambao wamejitahidi kuomba dua hizi kwa hakika wamepata manufaa makubwa na kukidhiwa haja shida zao kubwa kubwa kwani duwa hizi zinazuwia na kuondosha madhara ya kijicho kutegemeana na imani ya mtu anayezisoma.
Kadri imani yake inavyokuwa na nguvu ndivyo utegemezi wake kwa MwenyeziMungu unavyokuwa mkubwa. Kwa hakika hii ndizo silaha (za kupambana na uovu)” (Atti An-Nabawii).
Huwa inasemwa kuwa Kinga ni bora kuliko Tiba. Kwa hiyo basi, mtu ajikinge na madhara ya uchawi kabla haujatokea. Pamoja na mambo mengine, kinga hii hupatikana kwa kumtii na kumuabudia Allaah pekee, kuamini Qudra na Qadari Yake, kuomba ulinzi Wake kwa kumdhukuru mara kwa mara na kusoma dua za Mtume katika nyakati zinazofaa.
Kula tende Ajwah ni njia nyingine ya kuzuia madhara ya uchawi kama ilivyobainishwa katika Hadith iliyosimuliwa na Sa’ad ambapo Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kasema, “mtu akila tende Ajwah kila asubuhi, hatadhurika kwa sumu au uchawi kwa siku hiyo.” (Bukhari na Muslim).
Ni muhimu kutambua kuwa wale wanaostahili kunufaika na Hadith hii ni wale tu wanaoamini kikwelikweli haya aliyoyasema mtume na wanaoamini kwa dhati kabisa kuwa kila alichosema ni ukweli, ama wathibishe ukweli wake au la. Na kuhusu tiba ya uchawi, mtu aliyerogwa aoneshe subira na airidhie kudra ya Allaah. Pia ni jambo la msingi kwake kujirudi kwa dhambi yoyote ambayo ameitenda na afanye toba ya kweli kwa dhambi hiyo.
Anapotafuta tiba, aepuke kabisa tiba za “kitekero” au”kisangoma” zinazotolewa na waganga magirini. Kama ikibidi, basi anaweza kushirikiana na watu wachaMungu kumuomba msaada Allaah kwa utaratibu anaouridhia Allaah.
Inaendelea ..../3
- Login or register to post comments
- Email this page
- Chapisha



God bless you all this is a
God bless you all this is a very educative website for muslim thank you and keep it up.