Skip navigation.
Home kabah

Kisa Katika Surat Yaasiyn



Imeandikwa na: Ummu Iyyaad

 



Kisa katika Sura hii kinaanza kuanzia Aya nambari  13 mpaka Aya 27

أَعُوذُ بِاللَّه مِنَ الشَّيْطاَنِ الرَّجِيم

وَاضْرِبْ لَهُم مَّثَلاً أَصْحَابَ الْقَرْيَةِ إِذْ جَاءهَا الْمُرْسَلُونَ ﴿13﴾ إِذْ أَرْسَلْنَا إِلَيْهِمُ اثْنَيْنِ فَكَذَّبُوهُمَا فَعَزَّزْنَا بِثَالِثٍ فَقَالُوا إِنَّا إِلَيْكُم مُّرْسَلُونَ ﴿14﴾ قَالُوا مَا أَنتُمْ إِلاَّ بَشَرٌ مِّثْلُنَا وَمَا أَنزَلَ الرَّحْمن مِن شَيْءٍ إِنْ أَنتُمْ إِلاَّ تَكْذِبُونَ ﴿15﴾ قَالُوا رَبُّنَا يَعْلَمُ إِنَّا إِلَيْكُمْ لَمُرْسَلُونَ ﴿16﴾ وَمَا عَلَيْنَا إِلاَّ الْبَلاَغُ الْمُبِينُ ﴿17﴾ قَالُوا إِنَّا تَطَيَّرْنَا بِكُمْ لَئِن لَّمْ تَنتَهُوا لَنَرْجُمَنَّكُمْ وَلَيَمَسَّنَّكُم مِّنَّا عَذَابٌ أَلِيمٌ ﴿18﴾ قَالُوا طَائِرُكُمْ مَعَكُمْ أَئِن ذُكِّرْتُم بَلْ أَنتُمْ قَوْمٌ مُّسْرِفُونَ ﴿19﴾ وَجَاء مِنْ أَقْصَى الْمَدِينَةِ رَجُلٌ يَسْعَى قَالَ يَا قَوْمِ اتَّبِعُوا الْمُرْسَلِينَ ﴿20﴾ اتَّبِعُوا مَن لاَّ يَسْأَلُكُمْ أَجْرًا وَهُم مُّهْتَدُونَ ﴿21﴾ وَمَا لِي لاَ أَعْبُدُ الَّذِي فَطَرَنِي وَإِلَيْهِ تُرْجَعُونَ ﴿22﴾ أَأَتَّخِذُ مِن دُونِهِ آلِهَةً إِن يُرِدْنِ الرَّحْمَن بِضُرٍّ لاَّ تُغْنِ عَنِّي شَفَاعَتُهُمْ شَيْئًا وَلاَ يُنقِذُونِ ﴿23﴾ إِنِّي إِذًا لَّفِي ضَلاَلٍ مُّبِينٍ ﴿24﴾ إِنِّي آمَنتُ بِرَبِّكُمْ فَاسْمَعُونِ ﴿25﴾ قِيلَ ادْخُلِ الْجَنَّةَ قَالَ يَا لَيْتَ قَوْمِي يَعْلَمُونَ ﴿26﴾ بِمَا غَفَرَ لِي رَبِّي وَجَعَلَنِي مِنَ الْمُكْرَمِينَ ﴿27﴾  

 

13.       Na wapigie mfano wa wakaazi wa mji walipo wafikia walio tumwa.

14.      Tulipo watumia wawili, wakawakanusha. Basi tukawazidishia nguvu  

           kwa wingine wa tatu. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwenu.

15.      Wakasema: Nyinyi si chochote ila ni watu kama sisi. Na Mwingi wa      

           Rehema hakuteremsha kitu. Nyinyi mnasema uwongo tu.

16.      Wakasema: Mola wetu Mlezi anajua kwamba hakika sisi tumetumwa   

           kwenu.

17.      Wala si juu yetu ila kufikisha ujumbe ulio wazi.

18.      Wakasema: Sisi tumeagua kuwa nyinyi ni wakorofi. Ikiwa hamtaacha

          basi kwa yakini tutakupigeni mawe, na mtapata adhabu chungu

          kutoka    kwetu.

19.     Wakasema: Ukorofi wenu mnao wenyewe! Je! Ni kwa kuwa       

          mnakumbushwa? Ama nyinyi ni watu walio pindukia mipaka.

20.     Na akaja mtu mbio kutokea upande wa mbali wa mjini, akasema:

          Enyi watu wangu! Wafuateni hawa walio tumwa.

21.     Wafuateni ambao hawakutakini ujira, hali ya kuwa wenyewe     

          wameongoka.

22.     Na kwa nini nisimuabudu yule aliye niumba na kwake mtarejeshwa?

23.     Je! Niishike miungu mingine badala yake? Arrahmani, Mwingi wa         

         Rehema, akinitakia   madhara uombezi wa hao hautanifaa kitu, wala      

         hawataniokoa.

24.    Basi hakika mimi hapo nitakuwa katika upotovu ulio dhaahiri.

25.    Hakika mimi nimemuamini Mola wenu Mlezi, basi nisikilizeni

26.   Akaambiwa: Ingia Peponi! Akasema: Laiti kuwa watu wangu wangeli jua

Allaah سبحانه وتعالى Ametupa mifano mingi katika Qur'aan, mifano yenye hikma ya hali ya juu kabisa kama alivyosema:

((وَلَهُ الْمَثَلُ الأَعْلَى فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ))

((Naye ndiye mwenye mfano bora katika mbingu na ardhi)) Ar-Ruum  27

Kisha Akasema: 

((وَلَقَدْ ضَرَبْنَا لِلنَّاسِ فِی هَذَا الْقُرْآنِ مِن کُلِّ مَثَلٍ لَّعَلَّهُمْ یَتَذَکَّرُونَ  ((

((Na bila ya shaka tumewapigia watu mifano ya kila namna katika hii Qur'ani ili wapate kukumbuka))

( Az-Zumar 27)

Lau kama watu wangelitafakari  mifano hiyo wangeliweza kusawazisha nafsi zao na kuzidisha imani katika kutekeleza amri za Mola wao. 

((وَلَقَدْ صَرَّفْنَا فِی هَذَا الْقُرْآنِ لِلنَّاسِ مِن کُلِّ مَثَلٍ وَکَانَ الْاِنسَانُ اَکْثَرَ شَیْءٍ جَدَلاً  ((

((Na bila ya shaka tumewaelezea watu katika hii Qur'ani kila namna ya mfano. Lakini mwanaadamu amezidi kuliko kila kitu kwa ubishi))

Al-Kahf: 54

Katika kisa hiki vile vile Allaah سبحانه وتعالى  Ametuanzia kwa kutupigia mfano  kama ilivyo desturi Yake  سبحانه وتعالى kufanya hivyo  sehemu mbali mbali  katika Qur'an .

((وَاضْرِبْ لَهُم مَّثَلاً أَصْحَابَ الْقَرْيَةِ إِذْ جَاءهَا الْمُرْسَلُونَ))

((Na wapigie mfano wa wakaazi wa mji walipo wafikia walio tumwa))

Ibn Ishaq amepokea  usemi  kutoka kwa Ibn Abbas, Ka'ab Al-Ahbar na Wahb bin Munabbih  kwamba mji huo ni  wa Antakiya  (Antioch) palipokuwa na mfalme jina lake  Antiochus, mwana wa , Antiochus mwana wa Antiochus ambae alikuwa akiabudu masanamu.  

Allaah سبحانه وتعالى  Aliwatumia wajumbe watatu  wakiitwa  Sadiq, Saduq na Shalum  ambao huyo mfalme aliwakanusha. (At-Tabari 20:500)

Kwa usemi mwingine  kutoka  kwa Ibn Juraij kwamba majina  ya watume wawili wa mwanzo ni  Shamun na Yuhanna na watatu ni  Bulus na huo  mji ni mji wa Antakiya (Antioch).  {At-Tabari 20: 500)

Usemi mwingine vile vile kutoka kwa Qatada bin Diama kasema kwamba wajumbe hao ni wajumbe kutoka kwa Isa عليه السلام    (Zama hizo ilikuwa ni zama za Utume wa Isa )

Lakini hawakutumwa wote pamoja, bali walitumwa mwanzo wawili kisha  walipowakadhibisha akatumwa wa tatu wao ili wawe na nguvu ya kutimiza huo ujumbe.  

((إِذْ أَرْسَلْنَا إِلَيْهِمُ اثْنَيْنِ فَكَذَّبُوهُمَا فَعَزَّزْنَا بِثَالِثٍ فَقَالُوا إِنَّا إِلَيْكُم مُّرْسَلُونَ))

((Tulipo watumia wawili, wakawakanusha. Basi tukawazidishia nguvu kwa mwingine wa tatu. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwenu ))

Waliwaambia kuwa wao ni wajumbe wa  Mwenyeezi Mungu Aliyewaumba wao Ambaye Anawaamrisha wamuabudu Yeye pekee  bila ya kumshirikisha. 

Lakini ilikuwa kawaida ya watu  walipokuwa wanapelekewa mitume ambao ni binaadamu kama wao  kutokuamini na kutaka mitume hao wawe Malaika kama walivyojibu kwenye aya ifuatayo:

((قَالُوا مَا أَنتُمْ إِلاَّ بَشَرٌ مِّثْلُنَا وَمَا أَنزَلَ الرَّحْمن مِن شَيْءٍ إِنْ أَنتُمْ إِلاَّ تَكْذِبُونَ))  

((Wakasema: Nyinyi si chochote ila ni watu kama sisi. Na Mwingi wa Rehema hakuteremsha kitu. Nyinyi mnasema uwongo tu))

 Kushangaa kwao kuwa vipi mitume wawe binaadamu kama wao ilikuwa ni kama kawaida ya umma zingine zikipelekewa   mitume nao wakisema hivyo hivyo:

((ذَلِكَ بِأَنَّهُ كَانَت تَّأْتِيهِمْ رُسُلُهُم بِالْبَيِّنَاتِ فَقَالُوا أَبَشَرٌ يَهْدُونَنَا))

((Hayo ni kwa kuwa walikuwa wakiwajia Mitume wao kwa hoja zilizo wazi, nao wakasema: Hivyo binaadamu ndio atuongoe?)) (At-Taghaabun 6)

Kutokuwaamini kwao mitume ambao walikuwa ni binaadamu kama wao, Allaah سبحانه وتعالى amewapa hoja kuwa lau kama wangelikuwa wao ni malaika basi Angeliwapelekea vile vile malaika kama wao:

((وَمَا مَنَعَ النَّاسَ اَن يوْمِنُواْ اِذْ جَاءهُمُ الْهُدَی اِلاَّ اَن قَالُواْ اَبَعَثَ اللّهُ بَشَرًا رَّسُولاً ((

)) قُل لَّوْ کَانَ فِی الاَرْضِ مَلآئِکَةٌ يمْشُونَ مُطْمَئِنِّينَ لَنَزَّلْنَا عَلَيهِم مِّنَ السَّمَاء مَلَکًا رَّسُولاً))

((Na nini kilicho wazuilia watu kuamini ulipo wajia uwongofu isipo kuwa walisema: Je! Mwenyezi Mungu humtuma mwanaadamu kuwa ni Mtume?))

((Sema: Ingeli kuwa duniani wapo Malaika wanatembea kwa utulivu wao, basi bila ya shaka tungeli wateremshia Malaika kuwa ni Mtume wao.))  

 (Al-Israa 94 – 95)

Vile vile katika kushangaa kwao walitaka japo wawe wamekuja pamoja na malaika kutuma ujumbe.

((وَقَالُوا مَالِ هَذَا الرَّسُولِ يَأْكُلُ الطَّعَامَ وَيَمْشِي فِي الْأَسْوَاقِ لَوْلاَ أُنزِلَ إِلَيْهِ مَلَكٌ فَيَكُونَ مَعَهُ نَذِيرًا ((

((Na wakasema: Ana nini Mtume huyu? Anakula chakula, na anatembea masokoni! Mbona hakuteremshiwa Malaika akawa mwonyaji pamoja naye?))

(Al-Furqan 7)

Wajumbe wakawajibu kuwa wao wamekuja kutimiza ujumbe wa Allaah سبحانه وتعالى  .

((قَالُوا رَبُّنَا يَعْلَمُ إِنَّا إِلَيْكُمْ لَمُرْسَلُونَ))  

((Wakasema: Mola wetu Mlezi anajua kwamba hakika sisi tumetumwa kwenu))

Wala hawana haja yoyote  kutoka kwao, na kama wanaongopa  basi wasingeliwajia kwa upole bali kwa ugomvi, 

 )) وَمَا عَلَيْنَا إِلاَّ الْبَلاَغُ الْمُبِينُ  ((

((Wala si juu yetu ila kufikisha ujumbe ulio wazi))

Na wao hawana wasiwasi  kwani Allaah سبحانه وتعالى  yuko nao, na ushindi utakuwa wao (wajumbe)  kama si wa duniani basi wa akhera (yaani watalipwa pepo). Na wao (watu wa mji) wakitii amri vilevile watapata maisha mema ya duniani na akhera na wakikanusha basi watakuwa na maisha mabaya duniani na akhera.

Watu hao wakaendelea na ukaidi wao kwa kuwasingizia kuwa wameleta ukorofi na kuwapa onyo la kuwafukuza kwa kuwapiga mawe.

 )) قَالُوا إِنَّا تَطَيَّرْنَا بِكُمْ لَئِن لَّمْ تَنتَهُوا لَنَرْجُمَنَّكُمْ وَلَيَمَسَّنَّكُم مِّنَّا عَذَابٌ أَلِيمٌ))  

((Wakasema: Sisi tumeagua kuwa nyinyi ni wakorofi. Ikiwa hamtaacha basi kwa yakini tutakupigeni mawe, na mtapata adhabu chungu kutoka kwetu))

((إِنَّا تَطَيَّرْنَا بِكُمْ))

((Sisi tumeagua kwa nyinyi ni wakorofi ))

Ibn Qatada  kasema wamemaanisha kuwa "ikiwa jambo baya likitufika  basi itakuwa ni kwa sababu yenu (wajumbe).  (At-Tabari 20:502)

Usemi mwingine walisema hivyo kuwa wamepata ukorofi kwa vile mvua ilikatika kwa muda (Aysarut-tafasiir  :  4:369)

Hakuna 'Ukorofi' (mkosi, nuksi) (superstition)  katika Uislamu

Haifai  katika Uislamu kusema kuna ukorofi (imani ya dhana, nuksi au mkosi) (au superstition)  ni mambo ya itikadi mbaya ambayo ni shirki.

Wakati wa jahiliya Waarabu walikuwa wakichukua ndege  (طير) na humtumilia kuonyesha ishara nzuri au mbaya, mfano wanapotaka kusafiri humrusha ndege yule, akiruka upande wa kulia basi wanaamini kuwa ni safari ya salama na kama akiruka upande wa kushoto basi huwa hawasafiri. Uislamu umekuja na kuondoa shirki kama hiyo kama alivyotukataza Mtume صلى الله عليه وسلم  katika hadithi sahihi ifuatayo:

)) لا طيرة، وخيرها الفأل . قالوا : وما الفأل يا رسول الله؟ قال : الكلمة الصالحة يسمعها أحدكم (( (البخاري )
 

((Hakuna ukorofi,  na ni bora tegemea heri (matumaini mema). Wakauliza  nini matumaini mema (matarajio ya kufanikiwa) ewe mjumbe wa Allaah? Akasema:  'ni neno jema alisikialo mmoja wenu'))  (Al-Bukhari)

Tafsiir inaendelea;

((لَئِن لَّمْ تَنتَهُوا لَنَرْجُمَنَّكُمْ))

((Ikiwa hamtaacha basi kwa yakini tutakupigeni mawe))

Jambo hili vile vile ilikuwa ni kawaida ya umma nyingine walipowajia watume yalikuwa makemeo yao kama hayo.  Hata Ibrahiim عليه السلام  alikemewa na baba yake 'Aazar' alipomnasihi kwa upole kabisa asiaubudu masanamu:

وَاذْكُرْ فِي الْكِتَابِ إِبْرَاهِيمَ إِنَّهُ كَانَ صِدِّيقًا نَّبِيًّا ﴿41﴾ إِذْ قَالَ لِأَبِيهِ يَا أَبَتِ لِمَ تَعْبُدُ مَا لَا يَسْمَعُ وَلَا يُبْصِرُ وَلَا يُغْنِي عَنكَ شَيْئًا ﴿42﴾ يَا أَبَتِ إِنِّي قَدْ جَاءنِي مِنَ الْعِلْمِ مَا لَمْ يَأْتِكَ فَاتَّبِعْنِي أَهْدِكَ صِرَاطًا سَوِيًّا ﴿43﴾ يَا أَبَتِ لَا تَعْبُدِ الشَّيْطَانَ إِنَّ الشَّيْطَانَ كَانَ لِلرَّحْمَنِ عَصِيًّا ﴿44﴾ يَا أَبَتِ إِنِّي أَخَافُ أَن يَمَسَّكَ عَذَابٌ مِّنَ الرَّحْمَن فَتَكُونَ لِلشَّيْطَانِ وَلِيًّا ﴿45﴾ قَالَ أَرَاغِبٌ أَنتَ عَنْ آلِهَتِي يَا إِبْراهِيمُ لَئِن لَّمْ تَنتَهِ لَأَرْجُمَنَّكَ وَاهْجُرْنِي مَلِيًّا ﴿46﴾

((Na mtaje katika Kitabu Ibrahim. Hakika yeye alikuwa mkweli, Nabii)).

((Alipo mwambia baba yake: Ewe baba yangu! Kwa nini unaabudu visivyo sikia, na visivyo ona, na visivyo kufaa chochote?))

((Ewe baba yangu! Kwa yakini imenifikia ilimu isiyo kufikia wewe. Basi nifuate mimi, nami nitakuongoza Njia Iliyo Sawa)).

((Ewe baba yangu! Usimuabudu Shet'ani. Hakika Shet'ani ni mwenye kumuasi Mwingi wa Rehema))

((Ewe baba yangu! Hakika mimi naogopa isikupate adhabu inayo toka kwa Mwingi wa Rehema ukaja kuwa mwenziwe Shet'ani))

(((Baba) akasema: Unaichukia miungu yangu, ewe Ibrahim? Kama huachi, basi lazima nitakupiga mawe. Na niondokelee mbali kwa muda!))  

(Sura Maryam  41 – 46)

Wajumbe wakawajibu:

  ))قَالُوا طَائِرُكُمْ مَعَكُمْ أَئِن ذُكِّرْتُم بَلْ أَنتُمْ قَوْمٌ مُّسْرِفُونَ))

((Wakasema: Ukorofi wenu mnao wenyewe! Je! Ni kwa kuwa mnakumbushwa? Ama nyinyi ni watu walio pindukia mipaka))

Qatada kasema :  Hii inamaanisha kwamba "kwa sababu tumekukumbusheni  kuhusu Mola wenu ndio mmeona ukorofi kwetu.  Sio hivyo! Bali nyinyi ndio  watu wapotovu"   (At-Tabari 20:504)

Ibn Ishaq ulimfikia  usemi huu kutoka kwa Ibn Abbas, Ka'ab Al-Ahbar na Wahb bin Munabbih kwamba watu wa mji huo walitaka kuwauwa hao wajumbe,.  Akaja mtu kutoka sehemu ya mbali ya huo mji  huku anakimbia. Mtu huyo alikuwa akifanya kazi ya kamba, alikuwa mgonjwa wa ukoma, na alikuwa mkarimu sana akitoa nusu ya kipato chake sadaka. (At-Tabari 20:504)

Shahib bin Bishir kasema usimulizi kutoka 'Ikrimah kutoka Ibn Abbas رضي الله عنهما   kwamba huyo mtu alikuwa anaitwa Habib An-Najjaar na aliuliwa na watu wake.

((وَجَاء مِنْ أَقْصَى الْمَدِينَةِ رَجُلٌ يَسْعَى))

((Na akaja mtu mbio kutokea upande wa mbali wa mjini))

(( قَالَ يَا قَوْمِ اتَّبِعُوا الْمُرْسَلِينَ))

  ((akasema: Enyi watu wangu! Wafuateni hawa walio tumwa)).

Usemi mwingine ni kuwa huyo Habib aliponyeshwa na Isa عليه السلام   ukoma akamuamini   na aliposikia kuwa hawa watu wanawakanusha wajumbe akawakimbilia mbio kuwanasihi ili nao wawaamini hao wajumbe.

(Aysarut-tafasiir 4:371 )

((اتَّبِعُوا مَن لاَّ يَسْأَلُكُمْ أَجْرًا وَهُم مُّهْتَدُونَ))

((Wafuateni ambao hawakutakini ujira, hali ya kuwa wenyewe wameongoka))

Maana kwamba,  fuateni  ujumbe wanaokuleteeni  na wao ni watu waliongoka katika yale wanayokuiteni kumuabudu Allaah سبحانه وتعالى  peke Yake bila ya mshirika.

((وَمَا لِي لاَ أَعْبُدُ الَّذِي فَطَرَنِي وَإِلَيْهِ تُرْجَعُونَ))  

((Na kwa nini  nisimuabudu yule aliye niumba na kwake mtarejeshwa?))

Ina maana kwamba  " na kitu gani  kinachonizuia  kumuabudu Yule ambaye  kaniumba?  Na kumuabudu Yeye pekee bila ya kumshirikisha?"

((وَإِلَيْهِ تُرْجَعُونَ))

((na kwake mtarejeshwa?))

 Siku ya Kiyama  Atakapokupimeni kwa vitendo vyenu, na kuvihesabu  vikiwa vizuri  mtalipwa mema na vikiwa vibaya mtaadhibiwa.

 )) أَأَتَّخِذُ مِن دُونِهِ آلِهَةً إِن يُرِدْنِ الرَّحْمَن بِضُرٍّ لاَّ تُغْنِ عَنِّي شَفَاعَتُهُمْ شَيْئًا وَلاَ يُنقِذُونِ ((

((Je! Niishike miungu mingine badala yake? Arrahmani, Mwingi wa Rehema, akinitakia madhara uombezi wa hao hautanifaa kitu, wala hawataniokoa)).

  Miungu hiyo mnayoiabudu  badala ya Allaah سبحانه وتعالى  haina nguvu wala uwezo wowote wa kuzuwia madhara Aliyotaka Allaah سبحانه وتعالى yanifikie.

((إِنِّي إِذًا لَّفِي ضَلاَلٍ مُّبِينٍ  ((

((Basi hakika mimi hapo nitakuwa katika upotovu ulio dhaahiri))

Ikiwa mimi nitaichukua hiyo miungu yenu ndio mungu wangu nitakuwa mpotofu. 

((إِنِّي آمَنتُ بِرَبِّكُمْ فَاسْمَعُونِ))

((Hakika mimi nimemuamini Mola wenu Mlezi, basi nisikilizeni!))

 Ibn Ishaq kapokea usimulizi  uliomfikia kutoka kwa Ibn Abbas رضي الله عنهما , Ka'ab  na Wahb kwamba; Habib aliposema hivyo walimgeukia  wote na kumuuwa  naye hakupata mtu wa kumsaidia au kumhifadhi (At-Tabari 20:508) 

Qatada kasema; "Wameanza kumpiga mawe mpaka  huku  yeye anasema "Ewe Mwenyeezi Mungu  Wahidi (Waongoe)  watu wangu kwani wao hawajui" lakini wameendelea kumpiga  mpaka kifo kimedhihiri na huku bado anaomba "Ewe Mwenyeezi Mungu Wape Rahma Yako"  (At-Tabari 20:501)

((قِيلَ ادْخُلِ الْجَنَّةَ قَالَ يَا لَيْتَ قَوْمِي يَعْلَمُونَ))  

((Akaambiwa: Ingia Peponi! Akasema: Laiti kuwa watu wangu wangeli jua))

Muhammad  bin Ishaq kapata  usimulizi kutoka baadhi ya sahaba kutoka kwa Ibn Mas'ud رضي الله عنه    kwamba walimkanyaga mpaka matumbo yake  yalitokeza nyuma yake. Na hapo Allaah سبحانه وتعالى  Akamwambia;

((قِيلَ ادْخُلِ الْجَنَّةَ))

((Akaambiwa: Ingia Peponi!))

Kwa vile kauliwa katika kufanya daawa ya Allaah سبحانه وتعالى  kifo chake ni kifo cha Shahiid ambaye  hubashiriwa pepo wakati anatoka roho yake.

Habib aliyaona mema ya pepo wakati anatoka roho, hivyo akawatamania watu  wake yale aliyoyaona.

Bushra ya pepo pia humfikia Muumini mwema kama alivyosema Allaah سبحانه وتعالى

إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا تَتَنَزَّلُ عَلَيْهِمُ الْمَلَائِكَةُ أَلَّا تَخَافُوا وَلَا تَحْزَنُوا وَأَبْشِرُوا بِالْجَنَّةِ الَّتِي كُنتُمْ تُوعَدُونَ ﴿30﴾ نَحْنُ أَوْلِيَاؤُكُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَفِي الْآخِرَةِ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَشْتَهِي أَنفُسُكُمْ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَدَّعُونَ ﴿31﴾ نُزُلًا مِّنْ غَفُورٍ رَّحِيمٍ ﴿32﴾

((Hakika walio sema: Mola wetu Mlezi ni Mwenyezi Mungu! Kisha wakanyooka sawa, hao huwateremkia Malaika wakawaambia: Msiogope, wala msihuzunike; nanyi furahini kwa Pepo mliyo kuwa mkiahidiwa))

((Sisi ni vipenzi vyenu katika maisha ya dunia na katika Akhera, na humo mtapata kinacho tamaniwa na nafsi zenu, na humo mtapata mtakavyo vitaka))

((Ni takrima itokayo kwa Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu))

 (Fusswilat  30 – 32)  

Habib akaingia peponi  na kupata neema zote baada ya Allaah سبحانه وتعالى  kumuondoshea magonjwa, huzuni na machofu ya dunia. 

Alipoyaona mema hayo akasema:

((يَا لَيْتَ قَوْمِي يَعْلَمُونَ))

((Laiti kuwa watu wangu wangeli jua))

Qatadah kasema; Hutomuona Muumini  isipokuwa ni mkweli  (mwenye moyo msafi) na hutomuona kuwa sio mkweli. Kwani alipoona kwa macho yake vipi Allaah سبحانه وتعالى  kamkirimu  kasema

((يَا لَيْتَ قَوْمِي يَعْلَمُونَ))

((Laiti kuwa watu wangu wangeli jua))

Alitamani watu wake wangelijua yale aliyoyaona kwa macho yake  karama ya Allaah سبحانه وتعالى .  (At-Tabari 20:509)

 Ibn Abbas kasema; Alikuwa mkweli kwa watu wake katika maisha yake kwa kuwaambia:

((يَا قَوْمِ اتَّبِعُوا الْمُرْسَلِينَ))

((Enyi watu wangu! Wafuateni hawa walio tumwa))

Na baada kufa kwake kwa kusema :

((يَا لَيْتَ قَوْمِي يَعْلَمُونَ  بِمَا غَفَرَ لِي رَبِّي وَجَعَلَنِي مِنَ الْمُكْرَمِينَ ))

((Jinsi Mola wangu Mlezi alivyo nisamehe, na akanifanya miongoni mwa walio hishimiwa)) 

Kwa yale aliyoghufuriwa na Allaah سبحانه وتعالى , kukirimiwa  pamoja na  Malaika, Mitume, Mashuhadaa na Swalihiin (Watu wema kabisa) .

MAFUNDISHO TUNAYOPATA KATIKA KISA HIKI

1.     Kuwa na Tawhiyd ya Allaah سبحانه وتعالى, kufundishana na kukumbushana

        baina yetu na kujiepusha na shirki.

2.     Haifai kuwa na itikadi zenye shirki  kama (superstition), ukorofi, kisirani, mkosi (bad omen) .  Mifano michache iliyomo katika mujtamaa wetu inayosemekana  kama hayo  ambayo inatupasa tuepukane nayo:

 

a) Jicho likimpiga mtu upande wa kushoto  husema nishari  hiyo inakuja.

b) Akimuona mtu paka mweusi basi siku hiyo itakuwa ni ya ukorofi.

c) Mkono umkimuwasha mtu anasema pesa.

d) Ukifagia usiku unaondoa baraka.

e) Akipaliwa mtu husema kuwa mtu anamtaja.

f) Ukikata kucha zote pamoja (ya mikono na miguu) ina

    maana kwamba shida zikija zitakuja zote pamoja.

 Na mengi mengineyo.

3. Wajibu wa kila mtu kufanya daawa (kunasihi wenzetu)  bila     ya khofu na mateso tutakayoyapata.

4. Ukarimu wa Allaah سبحانه وتعالى Atakaotukarimu  pepo.

5. Bishara kwa Muumini mwema anayekufa shahidi kuwa ataipata pepo wakati inatoka  roho yake .

6. Mwisho lakini muhimu ya yote hayo ni kuwa visa katika Qur'aan ni maburudisho ya nyoyo, mafundisho, uongofu na Rahma kwetu.


 

 

لَقَدْ كَانَ فِي قَصَصِهِمْ عِبْرَةٌ ِلأُوْلِي الأَلْبَابِ مَا كَانَ حَدِيثًا يُفْتَرَى وَلَكِن تَصْدِيقَ الَّذِي بَيْنَ يَدَيْهِ وَتَفْصِيلَ كُلَّ شَيْءٍ وَهُدًى وَرَحْمَةً لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ

Kwa hakika katika visa vyao yamo mazingatio kwa wenye akili. Si maneno yaliyo zuliwa, bali ni ya kusadikisha yaliyo kabla yake, na ufafanuzi wa kila kitu, na ni uwongofu na rehema kwa kaumu yenye kuamini.

 

 


Allaahumma Tujaaliye katika wale uliowakirimu pepo Yako Amiin.