Skip navigation.
Home kabah

Nafasi Ya Mwanamke Katika Uislam

Ummu Iyyaad

 بسم الله والصلاة والسلام على رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم

 

Mwanamke wa Kiislamu amebahatika kuwa na umuhimu mkubwa katika Uislamu na si kama wanavyodai makafiri katika kumdhalilisha mwanamke. Kwa uoni wao, Uislamu umemnyima mwanamke wa Kiislamu  uhuru wake na kuharibu shani yake hiyo kwa kudai anahitaji kupata haki zake za kibinaadamu na kutaka kumweka sawa na mwanamme. 

Na ikiwa yuko mwanamke wa Kiislamu ambaye anahisi kuwa anahitaji haki hizo za kibinaadamu, bila shaka hakutambua bado umuhimu wake katika Uislamu. Kwa hivyo makala haya Insha-Allaah yatamuezesha mwanamke afahamu sehemu yake aliyojaaliwa na Mola wake akiwa ni kama Mama, dada na zaidi ni mwalimu wa kwanza katika kujenga mujtamaa (jamii)  ulio mzuri ulioimarika kutokana na mafunzo ya  Uislamu. 

Na tunaposema mafunzo ya  Uislamu, tunakusudia mwendo wake uwe ni wa kufuata  Qur'aan na Sunnah kwani hapo ndipo jamii itakuwa madhubuti na imeimarika katika misingi imara isiyotetereka. Na hapatokuwepo na khofu ya kuathirika na  mazingira yaliyotuzunguka na fitna zinazozidi kila siku. 

Kwa hivyo kutokana na vyanzo hivyo viwili vitukufu; Qur'aan na Sunnah, tutapata kujua umuhimu wake mwanamke wa kiislamu katika jamii, daraja yake na  haki zake alizopewa. 

Katika Qur'aan mwanamke ameelezewa katika njia ya aina tatu:

1)      Hali ya kimaumbile na kijamii.

2)      Hali ya  kuwa muuminah (mwenye kuamini)

3)      Shakhsiya na desturi yake kama tunavyoona katika visa vya Mitume.   

 

HALI YA MWANAMKE KATIKA UJAHILIYA

Kwanza kabisa inapasa tuonyeshe tofauti ya baina ya mwanamke alivyo katika Uislamu na kabla ya Uislam (wakati wa Ujaahiliya).     

 Katika ujaahiliyah ilikuwa mwanamke anaposhikwa na uchungu huchimbiwa shimo tayari  chini ya miguu ya kitanda cha kuzalia au godoro au mkeka.  Anapozaa mtoto mwanamume hupokewa kwa furaha na kusherehekewa.  Lakini akizaa mtoto wa kike  huambiwa, "mpige teke mwenyewe humo shimoni"  Basi huwa  hana la kufanya ila kumpiga teke humo na hapo hapo hufukiwa akesha.  

Wengine  walikuwa wanachukia kabisa anapozaliwa  mtoto wa kike, hata  baba hupatwa na  masikitiko makubwa na huwa baina ya kuchagua akae naye au amzike?  Hukaa siku nzima anajificha na habari mbaya na ya aibu kubwa hiyo. 

 Allaah سبحانه وتعالى  Aliyetuumba sote bila ya kumdhalilisha mwanamke au mwanamme,  hakupendezewa na dhulma hiyo na ndipo Ameielezea hukumu  hiyo kuwa ni mbovu  kabisa kwa kusema:

}}وَإِذَا بُشِّرَ أَحَدُهُمْ بِالأُنثَى ظَلَّ وَجْهُهُ مُسْوَدًّا وَهُوَ كَظِيمٌ{{

}}يَتَوَارَى مِنَ الْقَوْمِ مِن سُوءِ مَا بُشِّرَ بِهِ أَيُمْسِكُهُ عَلَى هُونٍ أَمْ يَدُسُّهُ فِي التُّرَابِ أَلاَ سَاء مَا يَحْكُمُونَ{{

{{Na mmoja wao akibashiriwa kwa msichana, uso wake unasawijika, naye kajaa chuki}}

{{Anajificha asionekane na watu kwa ubaya wa aliyo bashiriwa! Je, akae naye juu ya fedheha hiyo au amfukie udongoni? Tazama uovu wa wanavyo hukumu!}} An-Nahl: 58, 59

Na siku ya Kiyama ataulizwa kiumbe hicho kilichozikwa mzima mzima sababu ya kufanywa hivyo :

}}وَإِذَا الْمَوْؤُودَةُ سُئِلَت{{

{{Na msichana aliye zikwa hai atapo ulizwa}} At-Takwiiyr :8

Na kudharauliwa kwake mwanamke katika ujaahiliya kulikuwa ni kumfanya kama chombo cha mapambo tu cha kustareheya naye, akijipamba na kuvaa mavazi ya wazi yanayoonyesha mwili wake wote  na kucheza mbele ya mwanamme, na huku tayari ameshadhalilika kuwa yeye ni  kitu alichokimiliki mwanamme kisicho na thamani,  na yeye mwanamme ndio mwenye thamani na mwenye cheo kikubwa.  

Uislamu ukaja kuondosha dhulma hiyo na kumpa mwanamke hadhi yake ya kutulia na kubakia nyumbani kwake apate utulivu na alinde  heshima yake .

}}وَقَرْنَ فِي بُيُوتِكُنَّ وَلَا تَبَرَّجْنَ تَبَرُّجَ الْجَاهِلِيَّةِ الْأُولَى{{

{{Na kaeni majumbani kwenu, wala msijishauwe kwa majishauwo ya kijahilia ya kizamani}} Al-Ahzaab: 33

Vile vile katika kuondoa  dhulma na uovu huo Uislamu ukaja kumboresha mtoto wa kike akaweza kuishi na kupewa haki sawa tu na mwanamme, kwani wote ni viumbe vyake Allaah سبحانه وتعالى  ambavyo kaviumba kuwa  aina mbili hizo (mwanmke na mwanamume) kwa Rahma  yake kwa kuwa  kila mmoja ana manufaa na mahitajio kwa mwenzake.   

}}وَمِنْ آيَاتِهِ أَنْ خَلَقَ لَكُم مِّنْ أَنفُسِكُمْ أَزْوَاجًا لِّتَسْكُنُوا إِلَيْهَا وَجَعَلَ بَيْنَكُم مَّوَدَّةً وَرَحْمَةً إِنَّ فِي ذَلِكَ لَآيَاتٍ لِّقَوْمٍ يَتَفَكَّرُونَ{{

{{Na katika Ishara zake ni kuwa amekuumbieni wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao. Naye amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu wanao fikiri}} Ar-Ruum: 21

Nani zaidi ya Muumba wetu ni mbora wa kumtukuza kiumbe?   Katika kutaja uumbaji wake wa binaadamu,  Alivyowajaalia vizazi waja wake, Ametanguliza mwanzo kumtaja mtoto mwanamke kabla ya mwanamume

}}لِلَّهِ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ يَخْلُقُ مَا يَشَاء يَهَبُ لِمَنْ يَشَاء إِنَاثًا وَيَهَبُ لِمَن يَشَاء  الذُّكُورَ{{

{{Ufalme wa mbingu na ardhi ni wa Mwenyezi Mungu; anaumba apendavyo, anamtunukia amtakaye watoto wa kike, na anamtunukia amtakaye watoto wa kiume}} Ash-Shuura :49

Jambo muhimu zaidi ya yote ni kuwa Allaah سبحانه وتعالى  Hakuweka tofauti kabisa ya mahusiano baina Yake na viumbe Vyake vya kike na vya kiume katika kumuabudu Yeye, wote kawajaalia kupata malipo sawa sawa. Ni Uadilifu ulioje wa Muumba wetu  katika jambo muhimu kama hili' kwani sababu ya kutuumba sisi ni kumuabudu Yeye kama alivyosema:

}} وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ{{

{{Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi}}Adh-Dhariyaat :56

Kwa hiyo malipo ya ibada duniani na akhera yote ni malipo  yasiyo na tofauti kati ya mmoja na mwenzie:

}}مَنْ عَمِلَ صَالِحًا مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَى وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَلَنُحْيِيَنَّهُ حَيَاةً طَيِّبَةً وَلَنَجْزِيَنَّهُمْ أَجْرَهُم بِأَحْسَنِ مَا كَانُواْ يَعْمَلُون{{

{{Mwenye kutenda mema, mwanamume au mwanamke, naye akawa ni Muumini, tutamhuisha maisha mema; na tutawapa ujira wao kwa bora ya waliyo kuwa wakiyatenda}} An-Nahl:97

 }}وَعَدَ اللّهُ الْمُؤْمِنِينَ وَالْمُؤْمِنَاتِ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا وَمَسَاكِنَ طَيِّبَةً فِي جَنَّاتِ عَدْنٍ وَرِضْوَانٌ مِّنَ اللّهِ أَكْبَرُ ذَلِكَ هُوَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ{{

{{Mwenyezi Mungu amewaahidi Waumini wanaume na Waumini wanawake Bustani zipitazo mito kati yake, wadumu humo. Na makaazi mema katika Bustani za kudumu, na Radhi za Mwenyezi Mungu ndio kubwa kuliko yote. Huko ndiko kufuzu kukubwa}} At-Tawbah :72

}}فَاسْتَجَابَ لَهُمْ رَبُّهُمْ أَنِّي لاَ أُضِيعُ عَمَلَ عَامِلٍ مِّنكُم مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَى بَعْضُكُم مِّن بَعْضٍ{{

{{Mola Mlezi wao, akayakubali maombi yao akajibu: Hakika sipotezi kazi ya mfanya kazi miongoni mwenu, akiwa mwanamume au mwanamke, kwani ni nyinyi kwa nyinyi}}Al-Imraan :195

}}إِنَّ الْمُسْلِمِينَ وَالْمُسْلِمَاتِ وَالْمُؤْمِنِينَ وَالْمُؤْمِنَاتِ وَالْقَانِتِينَ وَالْقَانِتَاتِ وَالصَّادِقِينَ وَالصَّادِقَاتِ وَالصَّابِرِينَ وَالصَّابِرَاتِ وَالْخَاشِعِينَ وَالْخَاشِعَاتِ وَالْمُتَصَدِّقِينَ وَالْمُتَصَدِّقَاتِ وَالصَّائِمِينَ وَالصَّائِمَاتِ وَالْحَافِظِينَ فُرُوجَهُمْ وَالْحَافِظَاتِ وَالذَّاكِرِينَ اللَّهَ كَثِيرًا وَالذَّاكِرَاتِ أَعَدَّ اللَّهُ لَهُم مَّغْفِرَةً وَأَجْرًا عَظِيمًا{{

{{Hakika Waislamu wanaume na Waislamu wanawake, na Waumini wanaume na Waumini wanawake, na wat'iifu wanaume na wat'iifu wanawake, na wasemao kweli wanaume na wanawake, na wanao subiri wanaume na wanawake, na wanyenyekevu wanaume na wanawake, na watoao sadaka wanaume na wanawake, na wanao funga wanaume na wanawake, na wanao jihifadhi tupu zao wanaume na wanawake, na wanao mdhukuru Mwenyezi Mungu kwa wingi wanaume na wanawake, Mwenyezi Mungu amewaandalia msamaha na ujira mkubwa}} Al Ahzaab: 35

Wala mwanamke hakunyimwa haki katika ndoa baina yake na mumewe, kila mmoja ana haki fulani juu ya mwenzake ambazo ni wajibu wa kila mmoja kuzitimiza kwa mwenzake.     

}}وَلَهُنَّ مِثْلُ الَّذِي عَلَيْهِنَّ بِالْمَعْرُوفِ{{  

{{Nao wanawake wanayo haki kwa Sharia kama ile haki iliyo juu yao}}  Al-Baqarah :228

Na hii dhahiri kabisa kuwa mwanamke hakudharauliwa wala kudhalilishwa.       

 

Fadhila alizofadhiliwa mwanamke katika ndoa

Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alitoa nasaha kwa wanaume  kuhusu kuwafadhili wake zao, na katika fadhila hizo inamtosheleza mwanamke mwema kuwa na fahari kubwa kwa sifa aliyopewa ya kuwa yeye ni pambo bora kabisa katika dunia kama alivyosema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم   

))الدنيا كلها متاع ، وخير متاع الدنيا المرأة الصالحة((   رواه مسلم

((Dunia yote ni mapambo na mapambo bora kabisa ni mwanamke mwema))  Muslim.

Vile vile Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  alisisitiza mpaka katika khutba yake ya mwisho mwanamke kufanyiwa wema,

((واستوصوا بالنساء خيراً، فإنهن عندكم عوان لا يملكن لأنفسهن شيئاً، وإنكم إنما أخذتموهن بأمانة الله واستحللتم فروجهن بكلمة الله فاتقوا الله في النساء واستوصوا بهن خيراً))

((Wafanyieni wema wanawake kwani kwani wao hawana uwezo wa kuyasimamia mambo yao.  Na nyinyi mmewakubali na kuwapokea katika amana ya Allaah سبحانه وتعالى na wao wamefanywa ni halali kwenu, kwa hiyo mcheni Mungu katika wanawake na wafanyieni wema.))  

Mwanamke kwa kumtii mumewe basi kahakikishiwa pepo kwa njia nyepesi kabisa,

  (( عن عبد الرحمن بن عوف رضي الله عنه قال: قال رسول الله صلى الله عليه وسلم و إذا صلت المرأة خمسها وصامت شهرها ، وحفظت فرجها ، وأطاعت زوجها ، قيل لها: ادخلي من أي أبواب الجنة شئت )) رواه أحمد وابن حبان

 

((Kutoka kwa 'Abdur Rahmaan Bin 'Awf رضي الله عنه  ambaye kasema: Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  kasema, mwanamke akiswali Swalah zake tano, akafunga mwezi wake (Wa Ramadhaan), akajihifadhi  mwili wake, akamtii mume wake, ataambiwa "ingia katika milango yeyote ya pepo uitakayo))  Ahmad na Ibn Hibbaan

Fadhila anazozipata mtu kumlea mtoto wa kike malezi mema humuingiza peponi.

  ((عن أنس بن مالك -رضي الله عنه- قال: قال رسول الله  صلى الله عليه وسلم   ,من عال جارتين حتى تبلغا جاء يوم القيامة أنا وهو كهاتين وضم أصابع ))  مسلم

((Kutoka kwa Anas Bin Malik رضي الله عنه ambaye kasema: Mtume صلى الله عليه وآله وسلم kasema, atakayelea wasichana wawili mpaka wakabaleghe atakuja siku ya Kiyama mimi na yeye kama hivi viwili, akaambatanisha vidole vyake viwili )) Muslim

 

Baina ya wazazi wawili, mama ana daraja la juu kuliko baba.

)) عن أبي هريرة رضي الله عنه قال : جاء رجل إلى رسول الله صلى الله عليه وآله وسلم فقال يا رسول الله من أحق الناس بحسن صحابتي ؟ قال أمك ، قال ثم من ؟ قال أمك ، قال ثم من ؟ قال أمك قال ثم من ؟ قال أبوك))  بخاري و مسلم

((Inatokana na Abu Hurayrah رضى الله عنه kasema:  alikuja mtu kwa Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akamuuliza ewe Mjumbe wa Allaah, nani mwenye haki zaidi ya kumfanyia wema na wa kuwa  karibu yangu zaidi? Akasema “mama yako” akasema kisha nani? Akasema : “mama yako”, akasema kisha nani? Akasema “mama yako” akasema kisha nani? Akasema “baba yako”))   Al Bukhari na Muslim 

Huyu ndiye mwanamke Muislamu aliyekirimiwa na kufadhilishwa na Mola wake, basi naye mwanamke hana budi kufurahi na kuona fahari kwa umbile lake wala asiathirike na maneno ya uharibifu ya makafiri wanaotaka kuharibu mafunzo ya dini yetu yaliyo na thamani kubwa mno. 

Lakini kuzipata fadhila zote zote hizo na kuheshimika mwanamke huyo ni lazima awe mwanamke mwema, mwenye kumtii Mola kwa kufuata amri  na makatazo yake yaliyo katika Qur'aan na Sunnah. 

Mwanamke wa kiislamu awe na hima ya kuilinda heshima yake kutoka kila upande unaohusu kulinda heshima, ikiwa ni mwili wake, mavazi yake, tabia zake na atakapofunga ndoa  akajaaliwa kuwa na watoto aweze kuwalea watoto hao, nao wakue katika malezi ya Kiislamu ili iendelee hivyo kizazi baada ya kizazi kwani kama tulivyosema kuwa mwanamke ni mwalimu wa kwanza kabisa katika kuunda na kuimarisha mujtamaa wa Kiislamu. 

 

}}وَمَا تَوْفِيقِي إِلاَّ بِاللّهِ عَلَيْهِ تَوَكَّلْتُ وَإِلَيْهِ أُنِيبُ{{

((Na sipati kuwezeshwa haya ila na Mwenyezi Mungu. Kwake Yeye ninategemea, na kwake Yeye naelekea))  Huud: 88