Skip navigation.
Home kabah

Maafa

 

‘Abdun-Naaswir Hikmany

 

Maafa ya Tsunami yalipoikumba dunia, hawakuacha wataalamu kutuambia kwamba yametokana na mtetemeko baharini. Sasa ni vyema nigeuke kwa walio wengi ambao wamepata kuiona bahari imetulia tuli kabisa. Linganisha utulivu huo kwa kuvuta fikra zako vizuri ili uchore picha ya namna bahari ilivyonyanyuka ikaja juu hadi ikagharakisha nyumba za chini mpaka ghorofa, sehemu za pwani mpaka barani. Mwisho malizia na kauli ya: Allaahu Akbar!

Wala tusibabaishane kwamba Tsunami ilitokana na mtetemeko au kukosa teknolojia ya kuizuia. Ni sawa tu na kusema mgonjwa amefariki kutokana na homa ya malaria, lakini ukweli unabaki kwamba mtoaji wa hiyo roho ni Izraili, na Aliyempatia ruhusa hiyo ni Allaah. Kwa hivyo, bado Mtoaji amri wa yote Anabaki kuwa ni Yeye tu Pekee. Vyengine vyote vyabaki kuwa ni sababu tu ya hilo tokeo.

Kwa bahati mbaya, wataalamu wanaotumiwa leo, wengi wao ni wasio na elimu ya Qur-aan wala Sunnah. Hata kama wanaielewa vizuri, wanaikanyaga chini ya viatu vyao, wakijidai kutoitambua. Ukweli ni kwamba, hayo yote yameshaelezwa ndani ya masomo hayo. Ukitaka usitake, huo ndio ukweli.

Nani kati yetu, anabisha ya kwamba, zinaa imetapakaa, udhalimu umeongezeka, mayatima wanadhalilishwa na mengineyo mengi tu. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametueleza kuwa; itakapofika zama za watu kujihalalishia madhambi kama vile ulevi na muziki, wajitayarishe na maafa yatakayokuja kwa kupokezana moja baada ya jengine. Hadiyth hiyo (kwa tafsiri) ni kama ifuatayo:

“…watakapojitokeza waimbaji wanawake wakiwa na ala zenye nyuzi, ulevi kunywewa, na wafuasi wa mwisho wa watu hawa wanawalaani wa mwanzo, angalia wakati huo kwa kutokea upepo mkali, mtetemeko wa ardhi, kumezwa na ardhi, badiliko la umbo, mvua kubwa mno, na alama zinazofuata moja baada ya nyengine kama vipande vya mkufu vinavyoanguka kimoja baada ya chengine pindi nyuzi zake zinapokatwa.” [at-Tirmidhiy]

Isome kwa kuzingatia vizuri, kisha tuiingize Hadiyth hiyo hapo juu ndani ya hali halisi ya mwaka 2008. Homa iitwayo ‘dengue’ imeikumba Brazil na kuua watu 80 tokea Januari hadi Aprili. Mafuriko yaliyoanza Texas hadi Pennsylvania – Marekani na kuua watu 13 mnamo Machi ya 17-19. Kimbunga kibaya chajeruhi watu 30 huko jimbo la Georgia na Atlanta – Marekani, mnamo Machi ya 14-15. Ndege yagonga mlima wa Andean huko Venezuela na kuua abiria wote 46 mnamo Februari ya 21. Mitetemeko miwili ya ardhi iliyo na nguvu yaikumba nchi ya Demokrasia ya Kongo na kuua watu 45 na kujeruhi zaidi ya 450, mnamo Februari ya 3. Mianguko mibaya ya theluji huko kusini mwa China imeacha watu 24 wakiwa wamefariki na kuathiri watu milioni 78, wakiwemo 827,000 waliohama nyumba zao., mnamo Januari ya 28. Takriban nusu ya majimbo yameachwa bila ya umeme, ambao umesababisha gari moshi za abiria kusimamisha usafiri, na kiasi cha viwanja vya ndege 19 kufungwa. Athari ya uchumi nchini China kutokana na maafa hayo yalikisiwa kufikia dola bilioni 3.2[1]

Ewe ndugu yangu, basi kaa kitako ufikirie wapi ulipotoka, wapi ulipo na wapi unaelekea. Kumbuka ulikuwa hupo duniani na itafika wakati utakuwa hupo tena. Ukiambiwa soma Qur-aan na Sunnah, zingatia uzisome kwa makini bila ya kuzua. Waislamu wanapokwenda darsa sahihi, jiunge nao. Achana na laghai za dunia hii ambazo hazitakusaidia kitu mbele ya Muumba zaidi ya maafa kama hayo na ghadhabu Zake Mola siku ya Qiyaamah.




[1] http://www.infoplease.com/world/disasters/2008.html

Asalam Alykum kwanza sina

Asalam Alykum

kwanza sina budi kushkuru uongozi wa saafu hii ambayo inatuletea faida kubwa sanaa sisi waumini wa DINI yetu hii ya KISLAMU. HERI KUBWA AKULIPENI JUU HILI. (ALLAH)

Mimi naomba ushauri tu juu ya jambo hili ambalo kila siku zikienda mbele
lina zidi ingawaje baadh ya wachache wao wanaona nijambo la maendeleo lakin sio hivyo. kwasababu tu hakaripiwi mtu, na malipo yake yako mbali sana kwa uwoni wa kibn-aadam. Haya masula ya simu za mikononi yaani "Mobile phone" hivi sasa ndani Miskit yetu imekuwa kama nisehemu nyengine yeyote, tumefanya bora Makanisa yamekuwa na Thaman kubwa mbele ya Mskiti! Hakuna tofauti tena. Waislam wanasali na FULL SYSTEMS YA MUSIC NA VIDEO CPLIS ZA NGONO. Tunangamia Waislam jamani.
JEE TUFANYEJE HAPA?

AHSANTE,
BY SALUM SULEIMAN NASSOR

Waalaykum salaam

Waalaykum salaam warahmatuLlaahi wabarakatuh Akhiy Saalum Sulayman Naaswir;

Nashkuru kwa juhudhi zako 'adhiym kabisa katika kutoa maoni ambayo bila ya shaka yatawasaidia wengi miongoni mwa wanaopitia mtandao huu.

Hili ni tatizo sugu miongoni mwetu na hata baadhi ya Waislamu wanapokatazwa kuhusu hili wanalichukulia kuwa ni jambo jepesi. Uhakika kwamba Muumini hawachi kuwa Muumini hadi aache hata yale yaliyo halali kwa khofu yake tu. Sasa hali imekuwa mbaya zaidi hadi Waislamu wanatenda maovu huku wakiwa wanavuta pumzi walizoruzukiwa na wananasihiwa kuwa hilo jambo halifai abadan.

La muhimu kama Muislamu anamukhofu kikweli kweli Allaah (Subhaanahu wa Ta'aala) basi hana budi kuachana kabisa na aina zote za muziki hata ikiwa ndani ya simu yake. Kuna milio ambayo ndani ya simu haina bughudha na yaweza kutumiwa bila ya kuudhi. Lakini hakuna budi kuchunga milio hata hiyo inayofaa Muislamu awapo msikitini kwa kutoa sauti.

Bila ya kusahau Waislamu wanaotumia picha zisizofaa ambazo ni kinyume na maadili ya Uislamu ndani ya simu hizo. Wengine wanaweka video clips halafu waenda kumsujudia Yule Ambaye Amekemea hayo mambo. Kama si kufanya istihzai ni nini?

Akhiy wangu, usivunjike moyo na wanasihi wengine insha Allaah wataiona njia na wewe utakuwa umetimiza wajibu wako wa kuamrisha mema na kukataza maovu. Halikadhalika, naomba uwe mfano kwa Waislamu wanaokuzunguka kwa kuweka milio ya simu isiyo kuwa na miziki hata chembe!

Naomba upitie pia suala ambalo limewahi kuulizwa ndani ya Alhidaaya

http://www.alhidaaya.com/sw/node/2145

Jazaaka Allaahu khayra wa bi Llaahi at-tawfiyq