Maiti Anapokujia Katika Ndoto Huwa Anakumbuka Ya Duniani?

SWALI:

 

NATOA SHUKRANI ZANGU ZA DHATI KWA WALE WOTE WAHUSIKA WA WEBSITE HII MWENYEZI AWAJAALIE KILA LA KHERI HAPA DUNIANI NA AKHERA. SWALI LANGU NI, MTU ANAPOFARIKI HUWA ANAYAKUMBUKA YA DUNIANI? KAMA VILE MTOTO, MKE, NA MENGINEYO NA ANAPOKUJIA NDOTONI ANAYOKWAMBIA HUWA YA KWELI?


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu ndoto. Na shukurani nyingi kwa du’aa zako nzuri ambazo kwazo tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Azitakabali kwetu na kwenu kadhalika.

 

Mwanadamu mara nyingi huwa anaota kwa sababu moja au nyingine. Na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametueleza kuwa zipo ndoto aina mbili. Ndoto nzuri na ile ambayo ni mbaya. Wakati unapolala unaweza kuota yoyote kati ya hizi.

 

Ndoto njema inatoka kwa Allaah Aliyetukuka na mbaya inatoka kwa Shetani. Ukiota ndoto ambayo ni nzuri usimzungumzie yeyote ila yule unayempenda. Ama ndoto ikiwa ni mbaya unatakiwa upulize kushotoni mwako mara tatu, kisha uombe hifadhi kutoka kwa Allaah Aliyetukuka kwa ulichokiona, na kukulinda na Shetani mara tatu. Baada ya hapo hutakiwi kumwambia yeyote na ugeuze ubavu wako. Na ukitaka utasimama uswali rakaa mbili.

 

Ikiwa ndoto ni mbaya ukaingiwa na hofu basi inafaa usome du’aa ifuatayo: “A‘udhu bikalimaati LLaahi at-Tammaati min ghadhwabihi wa ‘iqaabihi wa sharri ‘ibaadihi wa min hamazaati ash-Shayaatwiyn wa an yahdhwuruun – Najilinda na maneno ya Allaah yaliyotimia, kutokana na hasira Zake, na adhabu Yake, na shari ya waja Wake, na vioja vya Mashetani na kunijia kwao” (Abu Daawuud na at-Tirmidhiy).

 

Kumuota aliyekufa inaweza ikatokana na kuwa umemfikiria sana siku ile au siku za karibu. Au unakumbuka ihsani aliyokuwa akikufanyia au muliishi naye kwa njia ambayo ni nzuri. Ama yale anayokwambia si kweli na huenda Shetani anataka kukughuri kwa njia moja au nyingine. Kile ambacho unaweza kufanya ni kumuombea maghrifa kwa Allaah Aliyetukuka au ikiwa ni mtu wa karibu basi umtolee sadaka.

 

Ingia katika kiungo kifuatacho upate maelezo zaidi kuhusu ndoto:

 

Ndoto Anazoota Zinatokea Kweli Hadi Zinamtia Khofu

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share