Skip navigation.
Home kabah

Baina Ya Sheikh Na Shaytwaan

 

Swaleh Suheil Abeid Bashamakh

(Dubai, UAE)

 

 

Katika usiku sana,

Shekhe yuko kitandani

Kihamaki kapambana,

na shawishi za shetwani

Alo na nyingi laana,

aduwi wa Rahamani

Wakaanza ushindani

 

Na wakati washindana,

ilihali wako ndani

Ikasikika Adhana,

kutoka Msikitini

Shetwani mara kumwona,

Shekhe atoka chumbani

Kazidi kushika kani…

 

 

Sheikh

Wakati umewadiya,

wa kwenda Msikitini

Heri kukimbiliya,

niwe wa kwanza swafuni

Wajibu natiya niya,

ni amri yake Manani

Taswali Msikitini

 

 

Shaytwaan

Nini zako harakati,

zisokuwa na makini?

Ungali mwingi wakati,

usingizi wajikhini!

Lako kero huliwati,

rudi kwako kitandani!

Kheri uswali nyumbani!

 

 

Sheikh

Mimi huwa na maudhi,

nadhikika nafusini,

Fikira zanibughudhi,

najiona mashakani,

Kipitiwa na faradhi, siku kenda kaburini,

Kiulizwa tasemani?

 

 

Shaytwaan

Wajali nini kijana,

mbona nyingi tafishani?

Ni kama unavyo ona,

watu bado wako ndani,

Wakati mrefu sana,

wasiwasi ni wa nini?

Hebu jitulize ndani!

 

 

Sheikh

Sichoki kufikiriya,

daima n’napo kaa,

Kila mara hunuwiya,

nipate kujiandaa,

Swala inapowadiya,

niiswali ya Jamaa,

Nipate zote Rakaa!

 

 

Shaytwaan

Nakuona na mawazo,

wajitiya wahakani,

Usiifanye mikazo,

na kushika sana kani,

Kwa nini mifululizo,

ya kwenda Msikitini?

Swala itakufaani?

 

 

Shetwani akamuweza,

Shekhe hakutamakani,

Kabakiya kujilaza,

hakwenda Msikitini

Hadi jua kuchomoza,

akangiya hasarani,

Akashindwa na Shetwani

 

 

Shaytwaan

Haina haja kuwaza,

 wasiwasi ni wa nini?

Wakati wowote waweza,

asubuhi na jioni

Si haja kujihimiza,

swala haiwezekani

Taswali siku ya thani

 

 

Alipovuta nyiradi,

akaja tena shetwani,

Na kitabu maridadi,

cha kupamba fikirani

Kukawa hakuna budi,

wakaanza ubishani,

Shekhe hakujimakini

 

 

Sheikh

Nataka kukuuliza,

nipate kwako yakini

Kwa nini waniliwaza,

katu hunipi makini?

Dua sikuzimaliza,

za kumuomba Manani!

Wanizuwiya kwa nini?

 

 

Shaytwaan

Kuomba haikulazimu,

 ngojea hadi jioni

Tena sana si muhimu,

wajisumbua kwa nini?

Naona una wazimu,

Dua zitakufaliani?

Faida yake sioni!

 

 

Sheikh

Sasa nimeazimiya,

kujitowa madhambini

Nataka kwenda tubiya,

kumlekeya Manani

Niyepuke ya Duniya,

yasokuwa na thamani

Tamuomba Rahamani!

 

 

Shaytwaan

Wewe ungali kijana,

jipumbaze wangojani?

Tumiya wako ujana,

ishi uwe furahani

Duniya navyoiona,

ndiyo yako burudani

Sasa wangojeya nini?

 

 

Sheikh

Nayaogopa mauti,

na kutiwa kaburini

Naupoteza wakati,

kufwata ya Duniyani

Faida yake sipati,

narudi kwa Rahamani!

Niitakase imani!

 

 

Shekhe kutoka kazini,

akanuwiya moyoni

Atapofika nyumbani,

atakaa kwa makini,

Ahifadhi Quraani,

mara akaja shetwani

Ukaanza ubishani…….

 

 

Shaytwaan

Wapitwa ewe mwendani,

uko hivyo mpaka lini?

Fungua telivisheni,

kuna nyingi burudani!

Vipindi vya Merikani,

na nyimbo za Arabuni!

Ona kama huamini!

 

 

Sheikh

Nyimbo zote ni haramu,

faida yake sioni!

Kusikiza si muhimu,

zinanighasi moyoni,

Wamepinga Maimamu,

na wote Wanazuoni!

Nizisikize kwa nini?

 

 

Shaytwaan

Ni wengi Maulamaa,

waliyatowa maoni,

Na bado wanakataa,

kuimba si makosani,

Nyimbo zina manufaa,

huwatibu majununi!

Zapumbaza nafusini!

 

 

Sheikh

Kuna hadithi zilioko,

nyingi zimeharamisha,

Katika vitabu ziko,

waziwazi zaonesha,

Muziki kwangu ni mwiko,

sitaki naukomesha!

Nyimbo zanikirihisha!

 

 

Shaytwaan

Pulika nikuarifu,

utowe shaka moyoni

Naona wajikalifu,

wajitiya mashakani

Hadidhi hizo dhaifu,

mezisikiya zamani

Muziki ni burudani!

 

 

Na wakati washindana,

machoni kawatokeya

Alipita msichana,

shekhe hakumwangaliya

Na shetwani hapo tena,

uzuri kumswifiya,

Binti alowapitiya…

 

 

Shaytwaan

Mbona hukumwangaliya,

ni kwa nini hutaki?

Mwana yule avutiya,

amenitiya ashiki

Katu sijashuhudiya,

kwenye wote makhuluki!

Ni mzuri hawatiki!

 

 

Sheikh

Takuwa kwenye hatari,

kianza kumwangaliya

Namuogopa Qahari,

popote ashuhudiya

Daima natahadhari,

sije nikatumbukiya!

Haramu kumwangaliya!

 

 

Shaytwaan

Fikiri wake uzuri,

wala hufanyi vibaya

Ni halali kufikiri,

mara moja hata miya

Basi hakuna hatari,

sana ukimwangaliya!

Jito halina paziya!

 

 

Shekhe alipoamuwa,

Umra kutekeleza

Alipoanza khatuwa,         

shetwani kajitokeza

Akaja kumsumbuwa,

hakuwata kuuliza

Kaanza kumsemeza…

 

 

Shaytwaan

Nakuona hima hima,

kwa kuazimu safari

Hebu mwendani simama,

usende kwanza fikiri

Unipe jawabu njema,

ni kwa nini wasafiri?

Usende nakushauri!

 

 

Sheikh

Umra ibada njema,

ni swababu ya safari

Nalekeya nyumba njema,

nitubu kwa Qahari

Hivi sasa nishakoma,

kwake tasitaghafari

N’na madhambi chakari!

 

 

Shaytwaan

Wajitiya hatarini,

huna sababu ya sawa

Mimi n’navyo baini,

pesa nyingi utatowa

Kheri nyengine huoni,

 kwa nini wachachawa?

Umra huja jaliwa!

 

 

Sheikh

Lazima yetu amali,

vyema tuitekeleze

Na katika kula hali,

ovyo ovyo tusicheze

Tumuogope Jalali,

Mema yote tutimize,

Tuzipate Rehemaze!

 

 

Shaytwaan

Elewa uyapulike,

maneno yangu sikiya

Tena moyoni uyaweke,

ukae kuzingatiya

Mtu kwa vitendo vyake,

Peponi hataingiya!

Kama urongo nambiya!

 

 

Shekhe nyumbani katoka,

kwenda kuwatembeleya

Niya yake ni kutaka,

nasaha kuwatoleya

Waifahamu hakika,

waja alokusudiya

Shetwani akamwambiya…

 

 

Shaytwaan

Mbona wajibabaisha,

mwenzangu nakukhofiya

Mno wajihangaisha,

kwa mambo yaso na ndiya

Hebu kweli nijulisha,

lipi ulokusudiya?

Tafadhali niambiya!

 

 

Sheikh

Nasaha natakawapa,

wamuogope Jaliya

Waja wasiwe na pupa,

kuitapiya Duniya

Na Mola atanilipa,

haya nalokusudiya,

Ndiyo njema yangu niya!

 

 

Shaytwaan

Huko ni kudhoofisha,

 waipoteza afiya

Jambo lisonufaisha,

vipi walikimbiliya?

Wasije kufedhehesha,

Waja watakuchukiya!

Aibu watakutiya!

 

 

Sheikh

Ni jambo la manufaa,

iwapo wazingatiya

Tawandokeya balaa,

za akhera na duniya

Na ndipo hajiandaa,

Waja kuwalinganiya

Ni hakika nakwambiya!

 

 

Shaytwaan

Usijepata hasadi,

ikakufikiya shari

Niogopalo zaidi,

ni kwa wako ujabari

Kiini cha ufisadi,

ni mwingi umashuhuri

Waja watakuaziri!

 

 

Shekhe kawa na maswali,         

kumuuliza shetwani

Ajuwe zake amali,

za kushawishi nyoyoni,

Kuwapotozeya mbali,

Waja wema Waumini,

Kauliza kwa makini

 

 

Kwake ana rai gani,

kwa waliyo mashuhuri

Na atamwambiya nini,

kwa wasiyo mashuhuri

Shetwani hakumukhini,

kajibu kwa ujasiri

Kasema kwa uhodari…

 

 

Sheikh

Nakuomba tafadhali,

na mushikili usije

Unondolee muhali,

uambe wafikirije

Imamu wetu Hanbali,

wewe utamsemaje?

Nifahamishe yukoje?

 

 

Shaytwaan

Amenimaliza kweli,

naona hawezekani

Kaniuwa kwa kauli,

“Daima shikamaneni

Kwa Suna yake Rasuli,

na mwendo wa Quraani”

Amenishinda zamani!

 

 

Sheikh

Kizidi kuuliziya,

jengine talijibuje?

Na Ibni Taymiya,

hebu sema wamwonaje?

Vipi utaniambiya,

elimu yake ikoje?

Nangoja utasemaje?

 

 

Shaytwaan

Hajanipapo khatuwa,

kwake sikujimakini

Yeye amenisumbuwa,

meniroga akilini

Sana yamenisumbuwa,

mapigo yake kichwani

Nayeye siwezani!

 

 

Sheikh

Na hebu nipa khabari,

ilo kweli utamke

Kuna mwengine hodari,

anayo na sifa yake

Ndiye Imamu Bukhari,

tupashe khabari zake

Wazijuwa swifa zake?

 

 

Shaytwaan

Meichoma nyumba yangu,

kwa vile vyake vitabu

Walisoma watu wangu,

waaswi vikawatibu

Na wakarudi kwa Mungu,

dhambi zao wakatubu!

Meshindwa kumjaribu!

 

 

Sheikh

Vipi yule mujirimu,

Hajaaj utanambiya ?

Alivyoimwaga damu,

na kuwatesa raiya

Lau wewe ni hakimu,

nini ungemfanyiya?

Amua yako shariya!

 

 

Shaytwaan

Lau leo wangekuwa,

kama yeye humu mwetu

Elifu moja wakawa,        

kwenye ulimwengu wetu

Ingekuwa yetu dawa,

ya sera yake kwa watu

Yeye ndiye mtu wetu!

 

 

Sheikh

Hebu tena niambiya,

kumuhusu Firauni

Ni wengi twamtukiya,

alivyokuwa khaini

Mno kajikufuriya,

kuwa m’ngu Duniyani

Mbona kafa baharini?

 

 

Shaytwaan

Sisi twamshajiisha,

kumsaidiya mno

Alivyo tunufaisha,

kwa mambo mengi manono

Yote alokamilisha,

hakuna wake mfano

Ni kweli yangu maneno!

 

 

Sheikh

Sema wakumbuka nini,

kuhusu yule shujaa

Bwana Salah Uddini,

asokuwa na tamaa

Alolinganiya dini,

na kuondowa balaa

Kwa nini wamkataa?

 

 

Shaytwaan

Tuachane naye huyo,

katuvuruga zamani

Kachafuwa zetu nyoyo,