Skip navigation.
Home kabah

Tusikiapo Adhaana

 

 

Swaleh Suheil Abeid Bashamakh

(Dubai, UAE)

 

 

Bisimilahi naanza, Kwa jina lako Jaliya

Mola wa kila uweza, wa milele kubakiya

Ilahi naomba jaza, nasaha kuhubiriya

Niwezeshe kuwajuza, uma wapatesikiya.

 

Rabi swala na salamu, zitume kwake Nabiya

Na Swahabaze kiramu, na jamaze twasaliya

Tupate pepo adhimu, pamoja nao kungiya

Tunusuru ya Karimu, dua twakulinganiya.

 

Baada kukamilisha, dua nalolinganiya

Hamu ni kuwajulisha, waja wapatesikiya

Wale wanaopuzisha, Adhana wakisikiya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya

 

Mtume metufundisha, sharuti katupangiya

Adhana inapokwisha, natumuombe Jaliya

Kazi kuzisimamisha, misikitini kungiya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya.

 

Nawakumbusha Kaumu, Mwadhini kitunadiya

Tujuwe yatulazimu, nyoyoni kunuwiliya

Kutawadha ni muhimu, tuswali sote jamiya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya

 

Adhana yatuarifu, kuwa swala mewadiya

Ni Ibada ya Raufu, upesi kukimbiliya

Tuunge mwanzo wa swafu, Iqama kuingojeya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya.

 

Mtume wetu kanena, lau watashuhudiya

Watu ndani ya Adhana, na swafu ya awaliya

Wangefanya hima sana, wasibaki kusaliya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya.

 

Ama Swala bila shaka, kwa Isilamu jamiya

Wakati wake kifika, haraka kuiqimiya

Ni amri ya Rabuka, Quraani metwambiya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya.

 

Tumkumbuke Bilali, ni swahaba wa Nabiya

Alikua wa awali, Uma kuwaadhiniya

Alipendwa na Rasuli, kwa sauti kuvutiya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya.

 

Madukani twawaona, wale wenye tijariya

Wasikiapo Adhana, hamunazo hujitiya

Makini huwa hawana, hawawahi kutikiya

Wasikiapo Adhana, wapuza kuitikiya.

 

Wangapi barabarani, wengi twawashuhudiya

Simu zao mikononi, wakati zinapoliya

Huwa hawadirikani, upesi kuzitikiya

Bali kiwa ni Adhana, wapuza kuitikiya.

 

Na wenye tarikilishi, muda wakizitumiya

Swala hawasimamishi, kwa nyakatize kingiya

Shetwani huwashawishi, hasarani wakangiya

Wasikiapo Adhana, wapuza kuitikiya.

 

Na walo maofisini, kazi zisowaishiya

Mwadhini akiadhini, hawajali kutikiya

Huwa wamo shughulini, waghurika na Duniya

Wasikiapo Adhana, wapuza kuitikiya.

 

Na wenye telivisheni, ashiki huwazidiya

Vipindi vya Merikani, na mpira wa Ulaya

Hughurika na shetwani, Swala zikawapitiya

Wasikiapo Adhana, wapuza kuitikiya.

 

Wenzangu jitahidini, tuzifuate shariya

Tuilinganiye Dini, haki kuitangaziya

Tuheshimu Waadhini, Swala wakitunadiya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya.

 

Watamati ikhiwani, tosha nalohubiriya

Tumengiya hasarani, na sote ni masuliya

Tutakwenda sema nini, tufikapo kwa Jaliya?

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya.

 

Kitaka lolinakili, shairi kuwatungiya

Ni Swalehe wa Suheli, Hadhirami asiliya

Kijana msema mkweli, Dini kuitumikiya

Tusikiapo Adhana, twapuza kuitikiya.