Skip navigation.
Home kabah

Kutumia Dawa Za kuzuia Hedhi Wakati Wa Hija

SWALI  

Kuna uhalali gani kwa wanawake kuchelewesha au kusogeza mbele siku zao  za hedhi kwa kutumia dawa wakati wa hija? Hii inafanyika ili kutimiza ibada  nzima ya hija.

 

 

 



JIBU:   

Maulamaa wengi wametoa ruhusa mwanamke kutumia dawa za

kuzuia hedhi ikiwa anakwenda kutimiza nguzo ya Fardhi ya Hajj,

na hoja zao ni kama hivi:

Inafaa kutumia dawa kuzuwia hedhi ili mwanamke aweze

kukamilisha nguzo yake ya tano ya Kiislamu ikiwa atakhofu

kupatwa hedhi wakati yuko katika taratibu za Hajj, kwa sababu

 ya kutokana na umbali wa masafa wa kusafiri na gharama

zake nyingi ambazo pengine atashindwa tena kurudia  kuitimiza

nguzo yake miaka mingine.

 Hapa inafaa tutaje kuhusu wale wanaotaka kutumia dawa hizo kwa kuwawezesha kufunga mwezi mzima wa Ramadhani.

Rai za Ma'ulamaa kuhusu jambo hili zime ikhtilafiana, kuna

wachache waliokubali na wengi   wamepinga mwanamke

kutumia dawa hizo katika mwezi wa Ramadhani.

 Wale waliokubali wamesema kwamba shuruti za kutumia dawa hizo ni kwamba mwanamke apate ruhusa kwa Daktari kuwa akitumia dawa hizo hazitomfanyia madhara yoyote kwani sheria ya dini yetu haipendi madhara kwa mtu. 

 لا ضرر ولا ضرار

Hakuna kuleta madhara wala kudhuriana" "

 

 Wale  waliopinga kabisa kwa kusema kwamba hii na amri ya

Allaah aliyowaandikia  binaadamu, kwa hiyo sio sawa kubadilisha

 maumbile ya mwanamke kama alivyoambiwa bibi 'Aysha  رضي الله عنها   ilipomjia hedhi wakati wa Hajj kama ilivyo katika hadithi hii:

((Imetoka kwa Bibi 'Aishah na  Jaabir bin 'Abdillah kuwa katika

tarehe nane ya mwezi wa Dhul Hijjah siku ijulikanayo kuwa ni

ya 'Tarwiyah' walipokuwa wakielekea Minaa na Mtume صلى الله عليه وآله وسلم wakaleta talbiya ya Hijja, kisha Mtume  صلى الله عليه وآله وسلم  akaenda kwa Bi 'Aishah r.a. akamkuta analia, akamuuliza: ''una nini?''  akajibu (Bi 'Aishah r.a.) ''Nimepatwa na hedhi na watu

wamehirimia na wamefanya twawaaf nami sijafanya vyote

 hivyo! Na sasa watu wanaelekea kuhiji hivi sasa!!'' 

Mtume صلى الله عليه وآله وسلم    akamwambia:

 

 

فإن ذلك شيء كتبه الله على بنات آدم، فافعلي ما يفعل الحاج غير أن لا تطوفي بالبيت حتى تطهري

 

 "Hili ni jambo aliloliandika Mwenyeezi Mungu kwa wanawake

 (mabint Adam), basi nenda kaoge halafu kahirimie kisha Hiji

na fanya yale anayofanya Mwenye kuhiji isipokuwa kutufu

na kuswali". Bi 'Aishah akafanya matendo  yote ya Hajj

isipokuwa kufanya Twawaaf na Swalah.))

 

Vile vile  kwa Rahma ya Allaah سبحانه وتعالى  Ametusahilishia

dini yetu kwa kuturuhusu kuweza kulipa siku za Ramadhani

ambazo mtu akishindwa  kufunga ikiwa yuko safarini au ni mgonjwa na hali kama hii ya hedhi ya wanawake kwamba walipe siku zao miezi mingine baada ya kumalizika  Ramadhani.  Kwa hiyo ni bora zaidi mwanamke kukubali amri ya Allaah Aliyowaandikia kupata hedhi kwani kila majaaliwa ya Allaah juu ya binaadamu bila shaka yana hikma na manufaa makubwa kwetu. 

 

}}فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَى سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ

 يُرِيدُ اللّهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلاَ يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ وَلِتُكْمِلُواْ الْعِدَّةَ وَلِتُكَبِّرُواْ اللّهَ

 عَلَى مَا هَدَاكُمْ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ {{

 

{{Basi ataye kuwa mjini katika mwezi huu naafunge.

Na mwenye kuwa mgonjwa au safarini, basi atimize

hisabu katika siku nyengine. Mwenyezi Mungu anakutakieni

yaliyo mepesi wala hakutakieni yaliyo mazito, na mtimize

hiyo hisabu, na mumtukuze Mwenyezi Mungu kwa kuwa

amekuongoeni ili mpate kushukuru.}} Al-Baqarah 185

 

Wallaahu A'alam