02-Jihaad: Ni Waajib

Jihaad Ni Waajib

 

Jihaad imefaridhishwa katika mwaka wa pili wa Hijra aliposema Allaah:

 

كُتِبَ عَلَيْكُمُ الْقِتَالُ وَهُوَ كُرْهٌ لَّكُمْ وَعَسَى أَن تَكْرَهُواْ شَيْئًا وَهُوَ خَيْرٌ لَّكُمْ وَعَسَى أَن تُحِبُّواْ شَيْئًا وَهُوَ شَرٌّ لَّكُمْ وَاللّهُ يَعْلَمُ وَأَنتُمْ لاَ تَعْلَمُونَ

 

“Mumelazimishwa kupigana vita (kwa ajili ya dini). Nalo ni jambo zito kwenu. Lakini huenda mkachukia kitu nacho ni kheri kwenu. Na huenda mkapenda kitu nacho ni shari kwenu. Na Allaah ndiye anayejua, (lakini) nyinyi hamjui.”

Al-Baqarah: 216

 

Kupigana Jihaad ni Fardhi Kifaayah na wakati mwingine inakuwa Fardhi ‘Ayn.

 

 

Fardhi ‘Ayn

 

‘Fardhi ‘Ayn’ ni yale ambayo kila Muislamu analazimika kuwa nayo au kuyatenda, na hasameheki asiyetenda hata kama kundi la watu wengine watalisimamia jambo hilo na kulikamilisha, kwa mfano; Imani, Swalah, Twahara, Kutoa Zakaah, Kufunga, Kuhiji n.k. Haya yanaitwa Fardhi ‘Ayn na kila Muislamu analazimika kuwa nayo au kuyatenda na si halali kwa mtu yeyote kutoyapa umuhimu.

 

 

Maana Ya Fardhi Kifaayah

 

 

Ama ‘Fardhi kifaayah’ ni yale matendo ambayo Waislamu wanalazimika kuyatenda ingawaje si lazima litendwe na Waisalmu wote, kwani linapotendwa na kundi miongoni mwao, basi waliobaki wanasameheka, kwa mfano,

 

KATIKA DINI:

Kujifunza elimu ya dini kwa ajili ya kuwasomesha wengine, Kumswalia maiti, Kuadhini n.k.

 

KATIKA MAISHA:

Kulima, Utabibu, Ufundi na yaliyo na mfano wake, mambo ambayo yakikosekana, maisha ya wanaadamu yanakuwa hatarini.

 

 

Yanayomhusu Kiongozi

 

Kama vile kuamrisha mema, kukataza mabaya, Kuitisha Jihaad, na Kuyapiga vita maovu na yale yaliyoharamishwa nk.

 

Jihaad inaingia katika Fardhi Kifaayah ambayo haimwajibikii kila mtu iwapo litatokea kundi la watu miongoni mwao litakaloweza kuwapiga vita maadui na kuiondoa shari yao bila kuhitajia msaada wa waliobaki.

 

Katika kutafuta elimu, Allaah Anasema:

 

وَمَا كَانَ الْمُؤْمِنُونَ لِيَنفِرُواْ كَآفَّةً فَلَوْلاَ نَفَرَ مِن كُلِّ فِرْقَةٍ مِّنْهُمْ طَآئِفَةٌ لِّيَتَفَقَّهُواْ فِي الدِّينِ وَلِيُنذِرُواْ قَوْمَهُمْ إِذَا رَجَعُواْ إِلَيْهِمْ لَعَلَّهُمْ يَحْذَرُون

 

“Wala haiwapasi Waislamu kutoka wote (katika miji yao wakaja Madiynah wakaiwacha miji yao mitupi). Lakini kwa nini halitoki kundi (tu) katika kila taifa miongoni mwao (lende Madiynah kwa Mtume) kujitalimisha vyema dini na (kisha wakaja) kuwaonya weziwao (waliosalia makwao) watakapowarudia, ili wapate kujihadharisha (na wao na mabaya).”

At-Tawbah: 122

 

 

Ama kuhusu Jihaad, Allaah Anasema:

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ خُذُواْ حِذْرَكُمْ فَانفِرُواْ ثُبَاتٍ أَوِ انفِرُواْ جَمِيعًا

 

“Enyi Mlioamini! Shikeni hadhari yenu (juu ya maadui zenu msikhadaike). Tokeni (kwenda vitani) makundi moja moja au tokeni nyote pamoja (kama atakavyokuambieni Mtume).”

An-Nisaa: 71

 

Na Akasema:

 

لاَّ يَسْتَوِي الْقَاعِدُونَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ غَيْرُ أُوْلِي الضَّرَرِ وَالْمُجَاهِدُونَ فِي سَبِيلِ اللّهِ بِأَمْوَالِهِمْ وَأَنفُسِهِمْ فَضَّلَ اللّهُ الْمُجَاهِدِينَ بِأَمْوَالِهِمْ وَأَنفُسِهِمْ عَلَى الْقَاعِدِينَ دَرَجَةً وَكُـلاًّ وَعَدَ اللّهُ الْحُسْنَى وَفَضَّلَ اللّهُ الْمُجَاهِدِينَ عَلَى الْقَاعِدِينَ أَجْرًا عَظِيمًا

 

“Hawawi sawa Waislamu wanaokaa wasende vitani, isipokuwa wenye dharura. (Hawawi sawa) na wale wapiganao katika njia ya Allaah kwa mali zao na kwa nafsi zao. Allaah amewafadhilisha katika cheo wale wapiganao katika njia ya Allaah kwa mali zao na kwa nafsi zao kuliko wakaao (wasende kupigana). Ingawa Allaah ameahidi wote (kupata) wema. Lakini Allaah amewafadhilisha – wale wapiganao kuliko wakaao – kwa ujira mkuu.”

An-Nisaa: 95

 

 

Na katika Sahihi Muslim kutoka kwa Abu Sa’iyd Al Khudry (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema kuwa; Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alituma ujumbe kwenda kwa watu wa kabila la Hudhayl kuwaambia:

“Atoke (kwenda vitani) katika kila wawili mtu mmoja na ujira watapata wote wawili.”

Sahihi Muslim Kitab al-Imaara – mlango wa Fadhail I’aanat al-ghazi fiy sabili Llaah – Hadiyth nambari 38

 

Na hii ni kwa sababu ikimwajibikia kila mtu, basi mambo mengi ya kidunia yenye maslahi kwa wanaadamu yataharibika, ndiyo maana ikawajibika kwa baadhi yao tu.

 

 

Jihaad Inapokuwa Fardhi

 

Jihaad inakuwa Fardhi ‘Ayn katika sehemu tatu:

 

Ya kwanza – ni pale mwenye kuwajibika kupigana anapokuwa vitani keshasimama katika msitari pamoja na wenzake, hapo analazimika kupigana.

 

Allaah Anasema:

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ إِذَا لَقِيتُمْ فِئَةً فَاثْبُتُواْ

 

 “Enyi mlioamini! Mkutanapo na jeshi (la makafiri) kazaneni barabara (wala msikimbie).”

Al-Anfaal: .45

 

Na Anasema:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ إِذَا لَقِيتُمُ الَّذِينَ كَفَرُواْ زَحْفاً فَلاَ تُوَلُّوهُمُ الأَدْبَارَ

Enyi Mlioamini! Mkikutana na waliokufuru vitani msiwageuzie mgongo.”

Al-Anfaal: 15

 

 

Ya pili – Adui anapoingia katika nchi ya Kiislamu, wanalazimika watu wote wa nchi hiyo kwa pamoja kutoka na kupambana naye, na si halali kwa mtu yeyote kurudi nyuma asitimize wajibu wake huo wa kupigana na adui, na hii ikiwa haiwezekani kumtoa adui huyo bila kushirikiana wote kwa pamoja.

 

Allaah Anasema:

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ قَاتِلُواْ الَّذِينَ يَلُونَكُم مِّنَ الْكُفَّارِ وَلِيَجِدُواْ فِيكُمْ غِلْظَةً وَاعْلَمُواْ أَنَّ اللّهَ مَعَ الْمُتَّقِينَ

 

“Enyi mlioamini! Piganeni na wale makafiri walio karibu yenu (kwanza kwani ndio wenye madhara na nyinyi zaidi), na wakute ugumu kwenu. Na jueni ya kwamba Allaah yu pamoja na wacha- Mungu.”

At-awbah: 123

 

 

Ya tatu – Mwenye kuhukumu anapotangaza Jihaad analazimika kila mwenye kuwajibika kupigana kuuitikia mwito huo, na haya yanatokana na Hadiyth iliyosimuliwa na Ibn ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhu) aliposema kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amesema:

 

لا هجرة بعد الفتح ولكن جهاد ونية وإذا استنفرتم فانفروا

 

“Hapana kuhajir tena (kutoka Makkah kwenda Madiynah) baada ya Waislamu kuuteka (mji wa Makkah) isipokuwa (kilichokuwepo ni) Jihaad na nia (ya kupigana Jihaad), na mnapoitwa muitikie (mwito).”

Swahiyh al-Bukhaariy – juzu ya 2 Mlango wa ‘Fadhila za Jihaad.’ Hadiyth nambari 2631.

 

Na maana yake ni kuwa mnapotakiwa kwenda kupigana Jihaad, basi lazima muitikie mwito huo.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema:

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ مَا لَكُمْ إِذَا قِيلَ لَكُمُ انفِرُواْ فِي سَبِيلِ اللّهِ اثَّاقَلْتُمْ إِلَى الأَرْضِ أَرَضِيتُم بِالْحَيَاةِ الدُّنْيَا مِنَ الآخِرَةِ فَمَا مَتَاعُ الْحَيَاةِ الدُّنْيَا فِي الآخِرَةِ إِلاَّ قَلِيلٌ

 

“Enyi mlioamini! Mna nini mnapoambiwa “Nendeni (kupigana) kwa ajili ya dini ya Allaah” mnajitia uzito katika ardhi? Je, mumekuwa radhi na maisha ya dunia kuliko ya Akhera? Lakini starehe za maisha ya dunia kwa (mkabala wa maisha ya) Akhera ni kidogo tu.”

At-Tawbah: 38.

 

 

Wanaowajibika Kupigana

 

Anawajibika kupigana Jihaad kila Muislamu mwanamume, mwenye akili timamu, aliyekwishabaleghe, mwenye afya njema mwenye uwezo wa kuwaachia watu wake kiasi cha mali inayowatosha mpaka pale atakaporudi.

 

Kwa hivyo haimwajibikii asiyekuwa Muislamu, mwanamke, mtoto mdogo, mwenda wazimu na mgonjwa, na kwa ajili hiyo hana lawama yeyote katika hawa asipoutikia mwito wa Jihaad kutokana na udhaifu wao au umasikini wao au umri wao au kutokuwa na akili zao ambao huenda kuwepo kwao katika uwanja wa mapambano kukasababisha madhara zaidi kuliko manufaa.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema:

 

لَّيْسَ عَلَى الضُّعَفَاء وَلاَ عَلَى الْمَرْضَى وَلاَ عَلَى الَّذِينَ لاَ يَجِدُونَ مَا يُنفِقُونَ حَرَجٌ إِذَا نَصَحُواْ لِلّهِ وَرَسُولِهِ مَا عَلَى الْمُحْسِنِينَ مِن سَبِيلٍ وَاللّهُ غَفُورٌ رَّحِيمٌ

“Hapana lawama kwa wanyonge, wagonjwa, na wasiopata cha kutumia, maadamu wanamsafia nia Allaah na Mtume Wake. Hapana njia ya kuwalaumu wanao fanya wema. Na Allaah ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu.”

At-Tawbah: 91.

 

Na Anasema:

لَيْسَ عَلَى الأعْمَى حَرَجٌ ولا عَلَى الأَعْرَجِ حَرَجٌ وَلا عَلَى الْمَرِيضِ حَرَجٌ

 

“Kipofu hana lawama, wala kiguru hana lawama, wala mgonjwa hana lawama.”

Al-Fat-h: 17.

 

Na kutoka kwa ‘AbdullAah bin ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa amesema:

“Nilipelekwa kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) siku ya Uhud (aniruhusu nikapigane) na wakati huo nilikuwa na umri wa miaka kumi na nne lakini hakuniruhusu.”

Fat-hul Baariy – Sharh ya Swahiyh al-Bukhaariy Juz. 5 Kkitabu cha ‘Ushahidi’, mlango wa ‘kubaleghe kwa watoto na ushahidi wao’.

 

Swahiyh Muslim – Kitabu cha ‘Imaarah’ mlango unaobainisha kubaleghe – Hadiyth nambari 1868

Na hii ni kwa sababu Jihaad ni ibada na haimwajibikii isipokuwa aliyebaleghe.

 

Imeelezwa na Maimam Ahmad na al-Bukhaariy kutoka kwa Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha) kuwa amesema:

 

“Nilisema (Nilimuuliza) - ewe Mtume wa Allaah; wanawake wanawajibika kupigana Jihaad?” akanijibu: “Jihaad (yao ni ile) isiyokuwa na kuuana ndani yake -  Hija na ‘Umrah.”

Musnad ya Imam Ahmad juz. 6 – Hadiyth za Bibi ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha)

Fat-hul Baariy – Sharh ya Swahiyh al-Bukhaariy Juz. 4 mlango wa Hija ya wanawake.

 

Na katika riwaya nyingine kuwa alisema:

“Lakini Jihaad iliyo bora ni Hija iliyokubaliwa.”

 

Imesimuliwa na Al-Waahidiy na As-Suyuutiy katika ‘Ad-Dur al-Manthuur’ kuwa Mujaahid amesema; “Ummu Salamah (Radhiya Allaahu ‘anha) alisema:

“Ewe Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), (kwa nini) wanaume (tu) wanateka miji (wanapigana Jihaad) na sisi hatuteki na sisi tunapata nusu ya urithi (tu)?”

 

Allaah Akateremsha kauli Yake:

 

وَلاَ تَتَمَنَّوْاْ مَا فَضَّلَ اللّهُ بِهِ بَعْضَكُمْ عَلَى بَعْضٍ لِّلرِّجَالِ نَصِيبٌ مِّمَّا اكْتَسَبُواْ وَلِلنِّسَاء نَصِيبٌ مِّمَّا اكْتَسَبْنَ وَاسْأَلُواْ اللّهَ مِن فَضْلِهِ إِنَّ اللّهَ كَانَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمًا

“Wala msitamani alicho wafadhili Allaah baadhi yenu kuliko wengine. Wanaume wana fungu katika waliovichuma, na wanawake wana fungu katika waliovichuma. Na muombeni Allaah fadhila Zake. Hakika Allaah ni Mjuzi wa kila kitu.”

An-Nisaa: 32.

 

Imepokelewa pia kutoka kwa Ikrimah (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa  alisema:

"Wanawake waliuliza juu ya Jihaad wakasema: “Tunatamani lau Allaah angejaalia na sisi pia tuwe tunapigana Jihaad ili tupate cho chote katika ujira (mwema) kama wanavyopata wanaume.” Ndipo Allaah Alipoiteremsha aya hiyo.

 

Hata hivyo hapana ubaya ikiwa wanawake watatoka kwa ajili ya kuwatibia walioumia au kwa ajili ya shughuli za mfano wake.

 

Kutoka kwa Anas (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema:

“Siku ya (vita vya) Uhud Waislamu walishindwa wakiwa na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), nilimuona (siku hiyo) Bibi ‘Aaishah binti Abi Bakr na Ummu Sulayum wakiwa wamekunja mikono ya kanzu zao nikiviona visigino vya miguu yao (huku wakiwa wanakwenda mbio) huku (na kule) wakibeba viriba vya maji migongoni mwao na kuwanywesha watu, kisha wanarudi na kuvijaza tena kisha wanarudi kuwanywesha watu (tena).”

Al-Bukhaariy juz. 2 – Kitabu cha Jihaad, mlango wa ‘Kupigana Jihaad wanawake pamoja na wanaume.’ Hadiyth nambari 2724.

Muslim juz. 3 Mlango wa ‘Kupigana Jihaad wanawake pamoja na wanaume.’ Hadiyth nambari 1811.

 

Kutoka kwa Anas pia anasema:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alikuwa akipigana vita akiwa pamoja na Ummu Sulayum na wanawake wengine katika watu wa Madiynah, waliokuwa wakiwanywesha watu maji na kuwatibia majeruhi.”

Muslim juz. 3 Mlango wa ‘Kupigana Jihaad wanawake pamoja na wanaume.’ Hadiyth nambari 1810.

Abu Daawuud juz. 3 mlango wa ‘Wanawake wanapigana vita’. Hadiyth nambari 2529.

 

At-Tirmidhiy juz. 3 mlango wa ‘Wanawake kwenda vitani’ Hadiyth nambari 1623.

 

 

Ruhusa Ya Wazee

 

Jihaad iliyowajibika haihitajii ruhusa ya wazee, ama Jihaad ya kujitolea lazima ipatikane ruhusa ya wazee wawili au ya mmoja wao.

 

Amesema Ibn Mas’uud (Radhiya Allaahu ‘anhu):

“Nilimuuliza Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam); ‘Amali (ibada) ipi inayopendwa zaidi na Allaah?

Akasema:

“Swala katika wakati wake”.

Nikamuuliza (tena):

“Kisha ipi?”

Akaniambia:

“Kuwatii wazee wawili.”

Nikamuuliza (tena):

“Kisha ipi?”

Akaniambia:

 “Jihaad katika njia ya Allaah.”

Swahiyh Al-Bukhaariy juz.1 Kitabu cha ‘Nyakati za Swalah’, mlango wa ‘Fadhila za kusali katika wakati wake’, Hadiyth nambari 504.

Swahiyh Muslim – juz. 1 Kitabu cha ‘Imani’, mlango wa ‘Imani juu ya Allaah ndiyo ‘amali bora kupita zote’, Hadiyth nambari 85

 

Na Ibn ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema:

“Alikuja mtu kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na kumuomba amruhusu kwenda kupigana Jihaad, akamuuliza; ‘Wazee wako wahai?’ Akasema; ‘Ndiyo’, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia: ‘Basi Jihaad yako iwe katika (kuwahudumia) wao’.

Abu Daawuud na An-Nasaaiy na At-Tirmidhiy aliyeisahihisha.

 

Na katika kitabu kiitwacho ‘Shar-atul Islaam’, (imeandikwa):

‘Na haijuzu kwenda kupigana Jihaad isipokuwa yule tu asiyekuwa na matatizo ya kuwahudumia wanawe na wazee wake, kwa sababu hayo ni bora kuliko kupigana Jihaad, bali ndiyo Jihaad iliyo bora.’

(Bila shaka hii ni katika Jihaad isiyowajibika, ama katika Jihaad ya ‘Fardh ‘Ayn’ yaani Jihaad iliyowajibika, basi hapana haja ya kuomba ruhusa kwa mtu yeyote kama ilivyotangulia kuelezwa).

 

 

Kumuomba Ruhusa Mwenye Deni

 

Haruhusiwi kwa anayedaiwa kwenda katika Jihaad isiyowajibika isipokuwa baada ya kumuomba ruhusa mwenye kumdai au aweke rahani mali inayotosheleza kulipa deni hilo au aweke mdhamini, kwa sababu katika Hadiyth ya Abu Qataadah (Radhiya Allaahu ‘anhu) iliyomo ndani ya kitabu cha Imam Ahmad na pia katika Swahiyh Muslim (aliulizwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam)):

‘Unaonaje nikiuliwa katika (Jihaad) katika njia ya Allaah, nitasamehewa madhambi yangu yote?’

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akasema:

“Ndiyo (utasamehewa) ikiwa utauliwa ukiwa katika subira huku ukitegemea ujira mwema (kutoka kwa Allaah), isipokuwa (kama una) deni, hakika Jibril ameniambia hayo (hivi punde).”

Ahmad na Muslim

 

Kutoka kwa ‘Abdullaah bin ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amesema:

“Allaah anamghufiria aliyekufa shahiyd madhambi yake yote isipokuwa deni.”

Pamoja na deni zinaingia pia dhulma alizowadhulumu watu, kama vile kuua na kula mali za watu pasipo haki na mfano wake.

 

 

Msaada Wa Makafiri

 

Inajuzu kutaka msaada wa wanafiki na wavunjao amri katika vita dhidi ya makafiri, na hii ni kwa sababu ‘Abdullaahi bin Ubay na wanafiki wenzake walikuwa wakienda vitani pamoja na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), na pia kisa cha Abu Muhjan ath-Thaqafi aliyekuwa mlevi, aliyepigana katika vita dhidi ya dola ya Kifursi ni mashuhuri sana.

Ama kutaka kupigana vita pamoja na makafiri, jambo hili lina khitilafu ndani yake miongoni mwa Maulamaa wa Kiislamu.

 

Ma Imaam Maalik na Ahmad wanasema:

“Haijuzu kutaka msaada wao, wala kusaidia katika jambo lolote.”

 

Imam Maalik akaongeza:

‘Isipokuwa kama watakuwa wakiwahudumia Waislamu tu, hapo inajuzu.’

 

Imam Abu Haniyfah yeye amesema:

“Inawezekana kutaka msaada wao na wanaweza kutoa msaada wowote ule sharti uwe Uislamu ndio wenye nguvu, ama ikiwa ushirikina ndio wenye nguvu, basi inachukiza.”

 

Imam ash-Shaafi’iy yeye anasema:

“Inajuzu kwa masharti mawili;

Kwanza – Waislamu wawe wengi na washirikina wawe wachache.

Pili – Wawe wanajulikana washirikina hao kuwa wana fikra nzuri na muelekeo mzuri juu ya Uislamu. Na watakapotakiwa msaada wao, wasipewe katika sehemu ya ngawira, bali wapewe malipo maalum bila kushirikishwa katika ngawira.”

 

 

Msaada Wa Watu Dhaifu

 

Kutoka kwa Mus'aab bin Sa’ad bin Abi Waqaas amesema:

“Baba yangu alidhani kuwa ana fadhila zaidi kuliko waliokuwa chini yake, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia:

“Kwani mungepata ushindi na kupata riziki bila ya (du’aa za) madhaifu miongoni mwenu?”

Al-Bukhaariy na An-Nasaaiy.

 

Katika An-Nasaaiy imeandikwa kwa lafdhi ifuatayo:

“Hakika Allaah huwanusuru umma huu kwa madhaifu wao, kwa Dua zao na Swala zao na ikhalsi yao.”

 

Na kutoka kwa Abu ad-Darda-a (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema:

“Nilimsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akisema:

“Niitieni masikini wenu, kwa hakika mnapata rizki na mnapata ushindi kwa (dua) za madhaifu wenu.”

Maimamu wote wa Ahlus Sunnah

 

Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) amesema:

“Huenda mwenye nywele zilizotimka (kwa umasikini), anayefukuzwa milangoni (kwa kudharauliwa) anapomuomba Allaah Atamkubalia (du’aa yake).”

Ahmad na Muslim

 

 

 

 

Share