Skip navigation.
Home kabah

Mswalieni Mtume

 

 

      Swaalih Suhayl 'Ubayd Bashamakh

       (Dubai, United Arab Emirates)

    

 

Kwa mapenzi na imani, salamu nawatumiya,

Popote ulimwenguni, zipate kuwafikiya,

Ndugu zangu zindukani, tumswaliye Nabiya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Isomeni Quraani, wazi mutashuhudiya,

Kuna Aya yabaini, Mola wetu amwombeya,  

Na Malaika mbinguni, wamswaliya Nabiya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Swala yake Rahamani, kwa waja wema jamiya,

Rehema kwa Waumini, na tena kuwaswifiya,             

Kwa Malaika mbinguni, wema wakashuhudiya,          

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

                                 

Ni amri Yake Manani, Mtume kumswaliya,

Na ndani ya Quraani, kuna Aya yatwambiya,

Enyi Mliyoamini, mswaliyeni Nabiya, (Al-Ahzaab : 56)

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Tuzidishe Ikhwani, Mtume kumswaliya,

Fadhila ziso kifani, aula kuziwaniya,

Ni neema kwa Manani, na nyingi thawabu piya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Hadithi zimebaini, bila shaka twazijuwa,

Kimswaliya Amini, na kumuombeya duwa,

Tunapewa na Manani, mara kumi kuswaliwa,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

   

Na hadithi vitabuni, Mtume kabashiriya,

Siku bora duniyani, Ijumaa katwambiya,

Siku hiyo zidisheni, dua na kuniswaliya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Pia kasema Amini, Mola hunirudishiya,

Roho hurudi mwilini, salamu kuitikiya,

Kwa yeyote Muumini, atakaye niswaliya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Na hadithi yanakili, nyengine yabashiriya,

Atakua ni bakhili, mtu kutoniswaliya,

Jina langu la Rasuli, muda akilisikiya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Pasina shaka ni njema, fadhila nalowambiya,

Jina wanapolisema, Mtume kumswaliya,

Ili tuyapate mema, Kutoka Kwake Jaliya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Twakuomba Mtukufu, huba za wetu Nabiya,

Tupe makao tukufu, Peponi kwako Jaliya,

Tuwe naye kwenye safu, Muhamadi Hashimiya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.

 

Mola uliye Mmoja, wasila mpe Nabiya,

Fadhila zako pamoja, baraka kumfikiya,

Na mfikishe daraja, takufu ‘lomwahidiya,

Mtume mswaliyeni, salamu kumtumiya.