Skip navigation.
Home kabah

Kulipa Deni La Ramadhaan Na Sita Shawwaal

 

SWALI

As-salaam alaykum Warahmatullah Wabarakatuh

Naomba fatwa kwa masuala yangu yafuatayo:
Suali: 1
Je inawezekeana kwa mwanamke aliyeingia kwenye siku zake (hedhi) katika mwezi wa ramadhani, baada ya ramadhani kumalizika, kufunga ( kulipa ) ramadhani na wakati huo huo(sambamba) kufunga sitatul shawwal? yaani kama piriadi yake ni siku 5 na sitatul shawwal siku 6, akafunga siku 6 kwa kutia nia mbili pamoja?
a) kama inawezekana atatia nia vipi?
b) kama haiwezekani, ni funga ipi aianze kwanza ? yaani siku alizozikosa ramadhani au anaweza kuanza na sitatul shawwal, badae ndio akalipa ramadhani

suali: 2
Je ikiwa mwanamke alijifungua(kazaa) yaani kapata mtoto kabla ya ramadhani na ramadhani ikamkutia bado hajakooga arubaini(siku 40 baada ya kujifungua) na ikawa siku ya edi-el fitri ndio siku yake ya mwisho, na akamua kuwa siku inayofuata aanza kulipa (yaani mwezi pili mfunguo mosi)ramadhani na wakati huo huo anataka afunge sitatul shawwali, na iwapo kama atafunga ramadhani siku 29 au 30, ataikosa sitatul shawwal je anaweza kuanza sitatul shawwal, badae ndio akanza kufunga ramadhani? na je ni lazima akianza kufunga ramadhani  azifuatanishe zote siku 29/30 au anaweza kufunga taratibu taratibu?

Natunguliza shukurani kwa majibu, na nitafurahi kama nitapata majibu kabla ya ramadhani kwisha, kwani hiyo kesi nakabiliana nayo nikiwa nje ya nchi (Uchina)

AS-SALAAM ALAYKUM

 



 

   

JIBU:

 

Wa 'Alaykumus salaam WarahmatuLLahi Wabarakaatuh,

 

Kwanza tunaomba samahani kuchelewa kukujibu swali lako ambalo uliomba lijibiwe haraka kutokana na  maswali mengi yanayomiminika huwa vigumu kuyajibu yote kwa haraka.

Jibu la Swali la kwanza

Haiwezekani kufunga deni na Sita Shawwaal kwa nia moja.  Rai iliyosahihi ni kwamba, kufunga Sita Shawwaal kunawezekana tu baada ya kumaliza deni kwanza la Ramadhaan. Hii ni kutokana na  Hadiythi ya Mtume صلى الله عليه وآله وسلم

 

 ((من صام رمضان ثم أتبعه بست من شوال))

 

((Atakayefunga Ramadhaan, kisha akafuatia na Sita za Shawwal…)) [Muslim, Abu Daawuud, At-Tirmidhiy, Ibn Maajah, Ahmad, ad-Daarimiy].

 

Kiunganisho cha neno 'kisha' katika Hadiythi hii kinaonyesha kuwa kufunga huko lazima kutimizwe kwa mpango, yaani kwanza kukamilisha funga Ramadhaan pamoja na deni lake kama mtu analo, kisha kufunga Sita Shawwaal ili kupata hizo fadhila zilizotajwa katika Hadiythi.  Aliyefunga Ramadhaan bila ya kuikamilisha hatambuliki kuwa ni yule aliyefunga Ramadhaan kamili.

 

Kwa hiyo kutia Nia moja katika funga hii ya Sita Shawwaal haiwezekani, bali ikiwa atafunga mtu deni lake katika siku za kufunga Sunnah yoyote kama Jumatatu na Alkhamiys, au siku za Ayaamul-Biydh (tarehe 13, 14, 15), au siku ya 'Ashuraa au 'Arafat  ndio inawezekana kutia nia pamoja na Swawm hizo na huweza kupata thawabu za fadhila zote.  

 

Kwa maelezo zaidi ya Swala hili soma  katika Fataawa iliyokuwepo katika kiungo hiki kifuatacho:

 

Fataawa Mbali Mbali Kuhusu Kulipa Deni Na Kufunga Sita Shawwaal

 

Nia haitajwi Kwa Matamshi:

 

Nia ya kufanya jambo lolote la ibada huwekwa moyoni na huwa haitajwi nia kwa matamshi kama wengi wanavyofahamu.

 

Na kutajwa nia kwa matamshi ni jambo la bid'ah (uzushi) kwani nia mahali pake ni moyoni.  Haikuthibitika kutoka kwa Mtume صلى الله عليه وآله وسلم wala  Maswahaaba wala Maimaamu wakubwa wote kwamba walikuwa wakitaja nia kwa kusema. Kwa hiyo inatosha kuiweka moyoni.

Jibu la Swali la pili 

 

 

Ikiwa ni hali kama hiyo uliyoitaja basi atakuwa ana 'udhuru wa kumchelewesha kufunga Sita Shawwaal, kwa hiyo hukumu yake ni vile vile kwamba kwanza amalize deni la Ramadhaan mpaka alimalize, na atakapomaliza deni na ukaingia mwezi wa pili yaani Dhul-Qaada basi afunge Swawm za Sita Shawwaal katika mwezi huo na atapata fadhila zake.    Lakini atakayeuwacha mwezi wa Shawwaal kupita bila ya kufunga na bila ya 'udhuru wowote, basi hatopata thawabu za Sita Shawwaal ikiwa atazifunga katika mwezi wa Dhul-Qaadah.

 

 

Sheikh Ibn 'Uthaymiyn alipoulizwa kuhusu mas-ala haya , alimalizia kujibu   kwa kusema : "Ikiwa mfano mwanamke aliyetoka katika uzazi amelipa deni lake lote katika mwezi wa Shawwaal, kisha ukaingia mwezi wa Dhul-Qaadah na yeye anataka kufunga Sita Shawwaal apate fadhila zake, basi afunge Sita Shawwaal katika mwezi huo wa Dhul-Qaadah ili apate thawabu zake, kwa sababu amezichelewesha (funga za Sita Shawwaal) kutokana na 'udhuru (sababu) muhimu.[Majmu'u ya Fataawa 20/19] 

 

Kuhusu utaratibu wa kufunga, kama tulivyosema hapo juu kwamba ikiwa mtu ana nia ya kufunga na Sita Shawwaal na yeye ana deni la mwezi mzima, basi  afunge deni lake katika mwezi wa Shawwaal bila ya kuziwacha siku kupita ili aunganishe na Sita Shawwaal hata kama umeingia mwezi wa pili.  Lakini kama mtu hana nia ya kufunga Sita Shawwaal, basi sio lazima kulipa deni lake kwa mfululizo, bali anaweza kufunga na kupumzika na anaweza pia kumalizia deni lake katika miezi mingine.

 

 

Na Allaah Anajua Zaidi