Vipi Aweze Kufanya Biashara Ya Nguo Kwa Misingi Ya Dini?

SWALI:

 

WAllaahi m/mungu atawalipa kwa juhudi zenu kwetu mimi ningali pendekeza kunifundisha upishi wa vileja vya mayai na vileja vya mafuta (bila ya yai) pia nna swali naomba munisaidie mimi ni mfanya kazi ktk campuni moja ya mafuta lakini bado sijaajiriwa na mwenyewe nataka kujiendeleza kimaisha nimeamua nitafute njia moja ya kufanya biashara ya nguo swali lipo hapa: Jee nitumie njia ipi kwa misingi ya kiislamu ili biashara yangu iniendeleze vizuri na nipate kutoa msaada kwa wenzangu?


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu kufanya biashara ya nguo.

 

Mafanikio baada ya tawfiki ya Allaah Aliyetukuka hutegemea na juhudi ya mtu mwenyewe. Ikiwa umeweka azma ya kufanya biashara, biashara ni kazi moja ambayo ina baraka sana swali Swalaah ya Istikhaarah kumtaka shauri Allaah Aliyetukuka kama biashara hiyo ni muafaka au la.

 

Pindi unapoanza biashara mafanikio yatatokana na wewe kujiweka katika:

 

1.     Dini, ushikamane nayo barabara katika hali zote wala usiache Ibaadah zako kama Swalaah na nyinginezo.

2.     Uwe mkweli na mwaminifu katika kazi yote, hivyo usidanganye wala usiseme uongo.

3.     Usiwe ni mwenye kuapa yamini katika biashara na haswa yamini ya uongo kwani hilo litakuweka mahali pabaya.

4.     Na ikiwa utakuwa na mtu wa kukusaidia unatakiwa usimfanyie khiyana kabisa.

5.     Muombe sana Allaah Aliyetukuka katika nyakati ambazo du’aa inakubaliwa kama baina ya Adhana na Iqaamah, unapoamka usiku wakati wa Tahajjud, unapofunga na kadhalika.

 

Na tunakuombea kwa Allaah Aliyetukuka Akufanyie sahali jambo hilo ulitakalo na liwe kheri kwako katika Dini yako, amali yako na hatima yako.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share