Madhara Ya Ghiybah (Kusengenya) 1-Kutunza Ulimi
Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
وَلَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ وَنَعْلَمُ مَا تُوَسْوِسُ بِهِ نَفْسُهُ وَنَحْنُ أَقْرَبُ إِلَيْهِ مِنْ حَبْلِ الْوَرِيدِ
((Na hakika Tumemuumba mtu, nasi tunayajua yanayompitikia katika nafsi yake. Na Sisi tuko karibu naye kuliko mshipa wa shingoni mwake))
((Wanapopokea wapokeaji wawili, [Malaika] wanaokaa kuliani na kushotoni))
((Hatamki neno ila karibu yake yupo mwangalizi tayari [kuandika])) [Qaaf:16-18]
Kila binaadamu ana Malaika wawili wanaokaa mmoja upande wa kulia na mmoja upande wa kushoto nao ni, Raqiyb na 'Atiyd.
Na kazi zao ni kuandika mema ya mtu na maovu yake; ikiwa ni makubwa au madogo hata kama chembe cha khardali (uwele) basi huandikwa na Malaika hao, hata kama binaadam atatamka neno dogo mno vipi basi litaandikwa. Hakuna kitakachokosekana kuandikwa na Malaika hao, wala binaadamu hawezi kuwakwepa kwani wao wamewekwa kwa ajili hiyo kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
وَإِنَّ عَلَيْكُمْ لَحَافِظِينَ
((Na hakika bila ya shaka wapo walinzi juu yenu))
((Waandishi wenye heshima))
((Wanayajua mnayoyatenda)) [Al-Infitwaar: 10-12]
Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ametuumba katika umbo bora kabisa na Amepanga kila kiungo mahali pake panapostahiki. Kwa Hikma Yake, Ameviumba viungo viwili muhimu katika mwili wa binaadamu katika sehemu zilizofichika ili vihifadhike visidhihirike nje ya mwili wake. Navyo ni: ulimi na sehemu za siri. Ni viungo ambavyo pindi binaadamu atakapovichunga basi vitampeleka Peponi kama Anavyosema Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):
عَنْ سَهْلِ بْنِ سَعْدٍ رضي الله عنه ، عَنْ رَسُولِ اللَّهِ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ: (( مَنْ يَضْمَنْ لِي مَا بَيْنَ لَحْيَيْهِ وَمَا بَيْنَ رِجْلَيْهِ ، أَضْمَنْ لَهُ الْجَنَّةَ)) متفق عليه
Sahli bin Sa'd (Radhiya Allaahu 'anhu) amesema: Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Atakayenidhaminia kilichomo baina ya taya zake (yaani ulimi) na kilichomo baina ya miguu yake (yaani tupu au sehemu za siri) nami nitamdhamini Pepo)) [Al-Bukhaariy na Muslim]
وعن عقبة بن عامر رضي الله عنه قال : قلت : يا رسول الله ما النجاة ؟ قال : ((أمسك عليك لسانك ، وليسعك بيتك ، وأبك على خطيئتك)) رواه الترمذي وقال حديث حسن
Na 'Uqbah bin 'Aamir (Radhiya Allaahu 'anhu) amesema: "Nilimuuliza Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) "Ewe Mjumbe wa Allaah, ni kupi kuokoka? Akajibu: ((Uzuie ulimi wako, utosheke na nyumba yako na ulie juu ya dhambi zako))' [At-Tirmidhiy na amesema: Hadiyth hii ni Hasan]
وعَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِي اللَّه عَنْه قَالَ : قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ : (( مَنْ كَانَ يُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ ، فَلْيَقُلْ خَيْرًا أَوْ لِيَصْمُتْ)) [ متفق عليه ] .
Na kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allahu 'anhu) ambaye amsema: Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Mwenye kumuamini Allaah na siku ya Mwisho basi aseme mema au anyamaze)) [Al-Bukhaariy na Muslim]
************
- Login or register to post comments
- Email this page
- Chapisha


