Skip navigation.
Home kabah

Nini Baada Ya Ramadhaan?

   

Ummu Iyyaad

بسم الله الرحمن الرحيم  الحمد لله رب العالمين  والصلاة و السلام على سيدنا محمد وعلى آله وأصحابه أجمعين وبعد

Tumeshauga mwezi wa Ramadhaan Mtukufu, mwezi wa Baraka na Rahma, tumeziaga siku zake za  mchana tukiwa katika subira ya Swawm, na siku zake za usiku zenye ladha ya ‘Ibaadah.  Tumeuaga mwezi wa Qur-aan, mwezi wa Taqwa, mwezi wa Jihaad, mwezi wa Maghfirah, Mwezi wa Du'aa kutakabaliwa,  na mwezi wa kuepushwa na moto.   Amefaulu aliyetimizia Swawm ilivyopaswa akachuma mema mengi na akajitahidi kufanya ‘Ibaadah zaidi na amekhasirika aliyepuuza Swawm na sheria zake na asichume mengi, na akafanya uvivu asiyejitahidi kufanya ‘Ibaadah zaidi.

Kama Alivyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) katika Aayah zilizotufaridhisha kufunga Ramadhaan kuwa lengo la Swawm ni kuingia katika Taqwaaa.

 ((يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ كُتِبَ عَلَيْكُمُ الصِّيَامُ كَمَا كُتِبَ عَلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكُمْ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ)) 

((Enyi mlioamini! Mmeandikiwa Swawm, kama waliyoandikiwa waliokuwa kabla yenu ili mpate kumcha Mungu)) [Al-Baqarah: 183]

Kwa hiyo kila Muislamu aliyeingia katika mwezi wa Ramadhaan atakuwa ameingia katika madrasa ya Taqwa. Na mtu anapoingia katika madrasa yoyote hutoka humo akiwa amepata shahada yake ya lile somo alilolisoma, na baada ya hapo huitumia ile elimu aliyoisoma aidha kuifanyia kazi au kumsaidia katika kuendesha maisha yake yamuongoze katika uhusiano wa tabia yake pamoja na familia yake, mujtamaa wake na watu wote kwa ujumla.

Na huendelea kuitumia hiyo elimu katika maisha yake yote hadi kufa kwake. Na ni hivyo hivyo ndivyo shahada ya Taqwa inayopatikana katika mwezi huu, elimu yake humuongoza Muislamu katika uhusiano wake pamoja na Mola wake, familia yake na watu wote kwa ujumla. Kwa hiyo inampasa Muislamu aendelee kuitumia elimu hii ya Taqwa hadi atakapoonana na Mola wake kama Alivyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):     

(( وَاعْبُدْ رَبَّكَ حَتَّى يَأْتِيَكَ الْيَقِينُ))

((Na muabudu Mola wako Mlezi mpaka ikufikie Yakini [Maana yake hadi yakufukie mauti]))  [Al-Hijr: 99]

Na hii ndio maana ya Istiqaamah (kunyooka au kuendelea kuthibiti) kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):   

((فَاسْتَقِمْ كَمَا أُمِرْتَ وَمَن تَابَ مَعَكَ وَلاَ تَطْغَوْاْ إِنَّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ))

((Basi, simama sawa sawa kama ulivyoamrishwa, wewe na wale wanaoelekea kwa Allaah pamoja nawe; wala msikiuke mipaka. Hakika Yeye anayaona yote myatendayo)) [Huud: 112]

((فَاسْتَقِيمُوا إِلَيْهِ وَاسْتَغْفِرُوهُ))

((Basi nyookeni sawa kumwendea Yeye, na mumtake msamaha)) [Fusswilat: 6]

 Kunyooka katika ‘Ibaadah vile vile ametufundisha Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika Hadiyth ifuatayo:

 عن أبي عَمْرو، وَقِيلَ: أبي عَمْرَةَ، سُفْيَانَ بْنِ عَبْدِ اللهِ الثّقَفيِّ رَضيَ اللهُ عَنْهُ قَال: قُلْتُ: يا رَسُولَ الله، قُلْ لي في الإِسْلاَمِ قَوْلاً، لاَ أَسْأَلُ عَنْهُ أَحَداً غَيْرَكَ. قَال: (("قُلْ: آمَنْتُ باللهِ ثُمَّ اسْتَقِمْ")).

Kutoka kwa Abu 'Amr, vile vile (anajulikana kama) Abu 'Amra Sufyaan bin Abdillaah (Radhiya Allaahu 'anhu) ambaye amesema: Nilisema: Ewe Mjumbe wa Mwenyeezi Mungu, niambie kitu kuhusu Uislamu ambacho siwezi kumuuliza mtu yeyote ila wewe.  Akasema (Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): ((Sema; Namuamini Allaah, kisha kuwa mwenye kunyooka. (kwa kuendelea kufanya ibada na kuwa na msimamo madhubuti katika dini)) [Imesimuliwa na Muslim]

Kuthibitika katika  ‘ibaadah ya Ramadhaan au msimu wowote wa ‘ibaadah ni alama ya kukubaliwa vitendo vya ‘ibaadah alivyovifanya Muislamu humo na kupotoka na kuingia katika maasi baada ya kutoka kwenye Taqwa ni alama ya kuviharibu vitendo vyake vyema. Na inampasa Muislamu anapotoka katika mwezi wa Ramadhaan, hali yake ya twa'a na Mola wake iwe bora zaidi kuliko ilivyokuwa kabla. Na kuhakikisha hali hii, jiulize na ujibu maswali haya:

1.       Je, Umekufikia mchana mmoja kama mchana wa Ramadhaan ukiwa katika Swawm?      

2.       Je, Umekufikia usiku mmoja kama usiku wa Ramadhaan ukiwa katika Qiyaamul-Layl?

3.       Je, Umeburudika na kusoma Qur-aan kama ulivyoburudika katika Ramadhaan?

4.       Je, Umeuburudisha moyo wako kwa dhikr, istighfaar, du'aa kama ilivyokuwa hali yako katika Ramadhaan?

5.       Je umetokwa na machozi kwa kukumbuka madhambi yako na kumkumbuka Mola Mtukufu na adhabu Zake?

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anapenda vitendo vya mwanaadamu anavyoviendeleza japokuwa kama ni kidogo vipi, kuliko vitendo vingi kisha asiviendeleze:

قال رسول الله صلى الله عليه وسلم : (( أحب الأعمال إلى الله أدومها وإن قل))  متفق عليه

Amesema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ((Vitendo Anavyovipenda Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) zaidi (kuliko vyote) ni vile vinavyodumishwa japokuwa ni vidogo)).  [Al-Bukhaariy na Muslim]

Kwa hiyo nyooka ewe ndugu Muislamu kwa kujiendeleza kufanya vitendo vyema na ibada katika miezi mingine yote kama ulivyokuwa ukifanya katika mwezi wa Ramadhaan nazo ni: 

Swawm:

Funga siku sita za mwezi wa Shawwaal ili ujipatie thawabu za kufunga mwaka mzima kama alivyosema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):    

 ((من صام رمضان ثم أتبعه ستاً من شوال كان كصيام الدهر)) رواه مسلم و الترمذي وابن ماجه, أبو داود و أحمد 

((Yeyote atakayefunga mwezi wa Ramadhaan, kisha akafuatia kwa kufunga siku sita za mwezi wa Shawwaal, basi atapata ujira wa aliyefunga mwaka mzima)). [Imepokewa na Maimaam Muslim, At-Tirmidhy, Ibn Maajah, Abu Dawuud na Ahmad]  

Vile vile kuna Swawm za Jumatatu na Alkhamiys, siku tatu katika mwezi, (Ayaamul-Biydh), Swawm ya Arafat, Swawm ya 'Ashuraa na zote zimetajwa fadhila zake katika mada inayopatikana katika AL HIDAAYA kwenye kiungo hiki kifuatacho:

 Swawm Baada Ya Ramadhaan 

Qiyaamul-Layl (kisimamo cha kuswali usiku)

Ni Swalah ya Sunnah iliyo bora kabisa baada ya Swalah ya Fardh kama ilivyo katika Hadiyth ifuatayo:

((أفضل الصلاة بعد الفريضة صلاة الليل))  رواه مسلم.

((Swalah iliyo bora kabisa baada ya Fardh ni Swalah ya usiku)) [Muslim]

Na fadhila zake zimetajwa nyingi sana, ingia katika vitengo vifuatavyo utambue fadhila zake:

 Fadhila Za Qiyaamul-Layl - 1 (Kusimama Kuswali Usiku)

Faida za Qiyaamul-Layl -2 (Kusimama Kuswali Usiku) 

Sadaka: 

Ikiwa ulikuwa ukitoa sadaqa katika Ramadhaan kwa wingi, basi endelea kutoa sadaka japo kidogo kidogo miezi mingine katika milango mingi ya Jihaad fiy Sabiyli-LLaah (Jihaad katika njia ya Allaah). Sadaka ni kinga kubwa ya kumuepusha Muislamu na maovu mengi, kama uhasidi, huwa ni kinga hata kwa adui zake, na pia ni kumtoharisha mtu moyo wake na kuuweka uwe safi kutokana na maradhi ya moyo kama uhasidi, chuki, ufidhuli n.k.  Na juu ya hivyo humzidisha kheri na baraka nyingi katika mali yake, umri wake, humpa mtu siha nzuri, na ni kumuepusha na moto pia.  

Kulisha Masikini:

Ni jambo Analolipenda Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) na Amelisisitiza katika Qur-aan na kuwasifu wenye kulisha maskini na wengineo kwamba ni waja wema na jaza yao ni Pepo:

((إِنَّ الْأَبْرَارَ يَشْرَبُونَ مِن كَأْسٍ كَانَ مِزَاجُهَا كَافُورًا   ((عَيْنًا يَشْرَبُ بِهَا عِبَادُ اللَّهِ يُفَجِّرُونَهَا تَفْجِيرًا ))

(( يُوفُونَ بِالنَّذْرِ وَيَخَافُونَ يَوْمًا كَانَ شَرُّهُ مُسْتَطِيرًا))    ((وَيُطْعِمُونَ الطَّعَامَ عَلَى حُبِّهِ مِسْكِينًا وَيَتِيمًا وَأَسِيرًا))

 (( إِنَّمَا نُطْعِمُكُمْ لِوَجْهِ اللَّهِ لَا نُرِيدُ مِنكُمْ جَزَاء وَلَا شُكُورًا ))  (( إِنَّا نَخَافُ مِن رَّبِّنَا يَوْمًا عَبُوسًا قَمْطَرِيرًا ))

 (( فَوَقَاهُمُ اللَّهُ شَرَّ ذَلِكَ الْيَوْمِ وَلَقَّاهُمْ نَضْرَةً وَسُرُورًا ))  (( وَجَزَاهُم بِمَا صَبَرُوا جَنَّةً وَحَرِيرًا ))  

5. Hakika watu wema watakunywa katika vinywaji vilivyochanganyika na kafuri,

6. Ni chemchem watakaoinywa waja wa Allaah wakiifanya imiminike kwa wingi.

7. Wanatimiza ahadi, na wanaiogopa siku ambayo shari yake inaenea sana,  

8. Na huwalisha chakula, juu ya kukipenda kwake, masikini, na yatima, na wafungwa.  

9. Hakika sisi tunakulisheni kwa wajihi wa Allaah. Hatutaki kwenu malipo wala shukrani.  

10. Hakika sisi tunaiogopa kwa Mola wetu Mlezi hiyo siku yenye shida na taabu.  

11. Basi Allaah Atawalinda na shari ya siku hiyo, na atawakutanisha na raha na furaha.

12. Na atawajazi Bustani za Peponi na maguo ya hariri kwa vile walivyosubiri. [Al-Insaan: 5-12]

 

Kutenda Wema Na Ukarimu:

Ikiwa Ramadhaan ilikubadilisha tabia yako ukawa unatenda wema kwa wazazi, ndugu, jamaa, jirani na marafiki, basi kutenda wema huko kuendelee miezi yote mingine.

Na vitendo vingi vyenginevyo inampasa Muislamu aendelee navyo siku zote wakati wote.     

Tunatoa Nasiha za dhati kwa ndugu Waislamu waliofunga Ramadhaan ipasavyo, kuendelea kuthibiti katika Taqwa na kumshukuru na kumuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Akusaidie kuwa katika hali hiyo bila ya kurudi nyuma.  Wala usiwe kama yule aliyeshona nguo yake akaipenda sana kisha akaiharibu kwa kuivuta uzi bila ya sababu kama mfano wa mwanamke mmoja aliyekuwa Makkah ambaye alikuwa akifuma uzi na kuufanya madhubuti kisha kila ukiwa madhubuti huufumua, naye Amemtaja Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):     

((وَلاَ تَكُونُواْ كَالَّتِي نَقَضَتْ غَزْلَهَا مِن بَعْدِ قُوَّةٍ أَنكَاثًا))

((Wala msiwe kama mwanamke anayeuzongoa uzi wake baada ya kwisha usokota ukawa mgumu)) [An-Nahl: 92]

Hii ni kama hali ya mwenye kurudia katika maasi baada ya kutoka katika Ramadhaan na akaacha kuwa na twa'a na kufanya mema, akawa badala ya kuitumia neema ya kuwasiliana na Mola wake na kuwa karibu Naye, akarudi katika madhambi. Waovu walioje watu wanaomtambua Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) katika Ramadhaan pekee. 

Alipofariki Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam), Maswahaba walikuwa katika vilio  na huzuni kubwa za ajabu hadi wengine walipigwa  na bumbuwazi, na 'Umar (Radhiya Allaahu 'anhu) alifika hadi kusema "Atakayesema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amefariki nitamuua". Walivunjikwa moyo sana hadi hali ikawa sio ya kupendeza, ndipo Abu Bakar (Radhiya Allaahu 'anhu) akawaambia:

"من كان يعبد محمد فمحمد قد مات ومن كان يعبد الله فان الله باقي حي لا يموت"

"Yeyote aliyekuwa anamuabudu Muhammad, basi Muhammad amefariki na yeyote aliyekuwa anamuabudu Allaah, basi Allaah Anabakia, Yu hai Hafi"

Hali kadhalika tunasema 'aliyekuwa anaabudu Ramadhaan, basi Ramadhaan inapita na aliyekuwa anamuabudu Allaah, basi Allaah Anabakia, Yu hai Hapiti kuondoka (Hafi)"

Kutokuwa katika istiqaamah baada ya Ramadhaan kunadhihirika kwa njia kama zifuatazo:

 

Kupuuza Swalah:

Kutokuswali Swalah za Fardhi, au kutokuziswali kwa wakati wake au kutokuziswali kwa kwa utulivu kama ipasavyo.

 

Kuacha Kuswali Jamaa'h Misikitini:

Swalah ya Jama'ah ni jambo liliosisitizwa sana na Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) sio Ramadhaan tu, bali siku zote za kawaida. Lakini utaona misikiti inajaa watu siku za Ramadhaan khaswa katika Swalah ya Tarawiyh ambayo ni Sunnah, wakati Swalah za fardhi ndizo muhimu zaidi. Na fadhila nyingi zimetajwa katika Sunnah anazozipata Muislamu kuswali Jama'ah.

Kuacha Kusoma Qur-aan Na Kujua Maana Yake:

Wengine  huijua Qur-aan katika Ramadhaan tu, ikimalizika Ramadhaan, misahafu inarudishwa katika kabati ijae vumbi hadi Ramadhaan nyingine, wakati Qur-aan ni uongofu kamili wetu, na ina manufaa makubwa sana katika maisha yetu kwa kila upande kwani imekusanya neema zote humo zenye manufaa kwetu kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):    

((يَا أَيُّهَا النَّاسُ قَدْ جَاءتْكُم مَّوْعِظَةٌ مِّن رَّبِّكُمْ وَشِفَاء لِّمَا فِي الصُّدُورِ وَهُدًى وَرَحْمَةٌ لِّلْمُؤْمِنِينَ))

((قُلْ بِفَضْلِ اللّهِ وَبِرَحْمَتِهِ فَبِذَلِكَ فَلْيَفْرَحُواْ هُوَ خَيْرٌ مِّمَّا يَجْمَعُونَ))

((Enyi watu! Yamekujieni mawaidha kutoka kwa Mola wenu Mlezi, na poza kuponyesha yaliyomo vifuani, na uongofu, na Rehma kwa Waumini))

((Sema: Kwa fadhila ya Allaah na Rehma Yake! Basi nawafurahi kwa hayo. Haya ni bora kuliko hayo wanayoyakusanya) [Yuunus: 57-58]

Vile vile ni muhimu sana Muislamu ajue maana ya maneno ya Mola wake ili atambue maamrisho na makatazo yake, sheria zake anazozihitaji katika maisha yake, na vile vile Qur-aan ni kipumbazo cha moyo kwani humo kuna visa vya Mitume na watu wa kale ambavyo vina mafundisho mazito kwetu na masimulizi ya kuburudisha nyoyo.

Kurudia Katika Mambo Ya Upuuzi:

Inampasa Muislamu aendelee kujiepusha na mambo ya upuuzi kama kutazama michezo ya televisheni, kusikiliza nyimbo, kukaa barazani kupiga soga, kusengenya katika simu, kusoma vitabu visivyo vya elimu na haswa elimu ya dini ya Kiislamu na kadhalika, na badala yake anatakiwa ajitahidi autumie wakati wa thamani katika kutafuta elimu ya dini yake tukufu na kuutumia wakati wake wote katika yale yenye kumridhisha Mola wake tu. Kujiepusha na mambo ya upuuzi ni moja wa sababu ya kumrithisisha Muislamu Pepo ya Firdaws kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) katika Aayah ifuatayo:

          ((وَالَّذِينَ هُمْ عَنِ اللَّغْوِ مُعْرِضُونَ))

 ((Na ambao hujiepusha na mambo ya upuuzi))  [Al-Muuminuun: 3]

Ndugu Muislamu, endelea kunyooka katika Taqwa siku zote, wakati wote, kwani hujui lini Malaika wa kuchukua roho atakuwa mgeni wako. Jihadhari kukutana naye wakati uko katika maasi na jitayarishe uwe katika wale ambao wanapofikiwa na Malaika wa roho uambiwe:

((يَا أَيَّتُهَا النَّفْسُ الْمُطْمَئِنَّةُ))   ((ارْجِعِي إِلَى رَبِّكِ رَاضِيَةً مَّرْضِيَّةً))     ((فَادْخُلِي فِي عِبَادِي))    ((وَاد ْخُلِي جَنَّتِي))

   ((Ewe nafsi iliyotua))  ((Rejea kwa Mola wako Mlezi umeridhika, na umemridhisha))  ((Basi ingia miongoni mwa waja wangu))       ((Na ingia katika Pepo yangu)) [Al-Fajr: 27- 30]

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Atutakabalie amali zetu zote tulizozifanya katika Ramadhaan na Atuhidi kutuendeleza kunyooka katika Taqwa na wenye kuzidisha kufanya vitendo vyema siku zote, wakati wote hadi tutakapokutana Naye Mola wetu Mtukufu tuwe miongoni mwa wale walioamini na Atuingize Peponi kama Alivyotuahidi katika kitabu chake Kitukufu:

((إِنَّ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ أُوْلَئِكَ هُمْ خَيْرُ الْبَرِيَّةِ))

 ((جَزَاؤُهُمْ عِندَ رَبِّهِمْ جَنَّاتُ عَدْنٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا أَبَدًا رَّضِيَ اللَّهُ عَنْهُمْ وَرَضُوا عَنْهُ ذَلِكَ لِمَنْ خَشِيَ رَبَّهُ))

 ((Hakika walioamini na wakatenda mema, hao ndio bora wa viumbe))

((Malipo yao kwa Mola Wao Mlezi ni Bustani za daima, zipitazo mito kati yake. Wakae humo milele. Allaah Yu radhi nao, na wao waradhi Naye. Hayo ni kwa anaye mwogopa Mola wake Mlezi)) [Al-Bayyinah: 7-8]

Du'aa ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ya kututhibitisha nyoyo zetu katika Dini yetu tukufu.

 اَللَّهُمَّ يَا مُقَلِّبَ الْقُلُوبِ ثَبِّتْ قَلْبِي عَلَى دِينِك

Allaahuuma Yaa Muqallibal-Quluub Thabbit Qalbiy 'Alaa Diynik

(Allaahuumma, Ewe Mgeuza nyoyo, thibitisha  moyo wangu katika Dini Yako(

اّللَّهُمَّ ياَ مُصَرِّفَ الْقُلُوب صَرِّف  قُلُوبَناَ عَلَى طَاعَتِك         

Allaahuumma Ya Muswarrifal-quluub Swarrif Quluubana 'Alaa Twaa'atik

(Allaahumma, Ewe Muelekezaji wa nyoyo, Elekeza nyoyo zetu katika Twa'aa Yako) 

Na Allaah Anajua Zaidi