Skip navigation.
Home kabah

Duaa Ya Mtume صلى الله عليه وآله وسلم Baada Ya Kutoka Twaaif Matamshi Na Maana Yake

Du'aa hii 'adhiym ni Du'aa ya kipenzi chetu Mtume صلى الله عليه وآله وسلم Alipotoka Twaaif baada ya kufukuzwa na kupigwa mawe na watu Wa Twaaif.  Na kabla ya hapo Mtume صلى الله عليه وآله وسلم Alikuwa Makkah na kabla ya kwenda Twaaif alipatwa na msiba wa kufiwa na watu wawili waliokuwa muhimu sana katika maisha yake ya da'awa ya utume alipokuwa Makkah. 

Kifo cha   'Ammi yake Abu Talib ambaye   ingawa hakuingia uislamu lakini alikuwa   akimhifadhi kutokana na maudhi ya maquraysh wa Makkah. Kisha  kikafuata kifo cha  mke wake mpenzi Bibi Khadija رضي الله عنها   ambaye alikuwa akimliwaza sana anapopata mashaka na maudhi kutoka kwa maquraysh. Kwa hiyo Mtume صلى الله عليه وآله وسلم Alikuwa katika huzuni kubwa  sana na maudhi ya makafiri yalizidi. Kisha akaamua  kuondoka Makkah na kuelekea Twaaif   kuwaita watu wa huko katika uislamu na kutegemea kupokelewa kwa vizuri, lakini matokeo yake ilikuwa ni kufukuzwa na kupigwa mawe hadi kuchuruzikwa na damu.   Ikambidi akimbie na kurudi akiwa ana   dhiki,  maumivu na machofu ambayo yalimfikisha kupumzika njiani.  Akapumzika katika ukuta wa shamba la mzabibu na ndipo    alipomtegemea Mola wake kwa kumkabili   kumuomba du'aa hii  yenye masikitiko makubwa. 

Du'aa hii inatupa mafundisho makubwa kuwa tunapofikwa na maudhi  ya kutokana na watu jambo muhimu ni kumkabili Mola Mtukufu na kumshtakia Yeye Pekee na muhimu zaidi ni kutaka Radhi Zake Mola. 

Baada ya kuomba Du'aa hii akaendelea kurudi Makkah na alipofika Qarn Al-Manaazil Allaah سبحانه وتعالى  Alimtumia Jibriyl    عليه السلام pamoja na malaika wa majabali na kumuuliza kama atapenda waifukie Makkah na waangamizwe watu baina ya 'Akhshabayn' (majabali mawili)  lakini  Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  kwa upole na khuluq (tabia) yake njema   alikataa na kujibu maneno haya yenye kutia moyo kabisa na kutuzidishia imani na mapenzi ya Mtume wetu   صلى الله عليه وآله وسلم .

Alisema:

((بل أستأني بهم . لعل الله أن يخرج من أصلابهم من يعبده لا يشرك به شيئا))

((Nitasubiri nao (nitastahmili nao) Pengine Allaah Atatoa katika migongo yao (vizazi vyao) watakaomuabudu na bila ya kumshirikisha Naye kitu))

(Al-Bukhaariy na Muslim)

DU'AA

 

اَلَّلهُمَّ إِنِّي  أَشْكُو إِلَيْكَ ضَعْفَ قُُوَّتِي, وَقِلَّةَ حِيْلَتِي, وَهَوَانِي عَلَى النَّاسِ,  يَا أَرْحَمَ الرَّاحِمِين, أَنْتَ رَبُّ الْمُسْتَضْعَفِينَ وَاَنْتَ رَبّي إِلَى مَنْ تَكِلْنِي؟ إِلَى بَعِيدٍ يَتَجَهَّمُنِي أَمٍ إِلَى عَدُوٍ مَلَّكْتَهُ أَمْرِي؟ إِنْ لَمْ يَكُنْ بِكَ غَضَبٌ عَلَىَّ فَلاَ أُبَاِلي، وَلَكِنَّ عَافِيَتَكَ أَوْسَعُ لِي مِنْ ذُنُوبِي,  أَسْأَلُكَ بِنُورِ وَجْهِكَ الَّذِي أَشْرَقَتْ لَهُ الظُّلُمَاتُ، وَصَلَحَ عَلَيْهِ أَمْرُ الدُّنْيَا وَالأَخِرَةِ مِنْ أَنْ يُنْزِلَ عَلَيَّ غَضَبُكَ أَوْ يَحِلُّ عَلَىَّ سَخَطُُكَ   وَلاَ حَوْلَ وَلاَ قُوَّةَ إِلاَّ بِكَ      

Allaahumma Inniy Ashkuu Ilayka Dha'fa Quwwatiy, Wa Qillata HiylatiyWa Hawaaniy 'Alan-Naas.  Yaa Arhamar-Raahimiyn.  Anta Rabbul-Mustadhw'afiyn, Wa Anta Rabbiy  Ilaa Man Takilniy?  Ilaa Ba'iydin Yatajahhamuniy? Am Ilaa 'Aduwwim-Mallaktahu Amriy?  In-lam Yakun Bika Ghadhwabun 'Alayya Falaa UbaaliyWa Laakin 'Aafiyataka Awsa'u Liy Min Dhunuubiy.  As-aluka Binuuri Wajhika-lladhiy Ashraqat Lahudh-Dhwulumaat, Wa  Swalaha 'Alayhi Amrud-Duniyaa Wal-Aakhiratiy Min Ay-yunzila 'Alayya Ghadhwabuka Aw Yahillu 'Alayya Sakhatwuka, Wa Laa Hawlaa Walaa Quwwata Illaa Bik.   

Ya Allaah , Kwako peke Yako nalalamika udhai'fu wa nguvu zangu, na uchache  wa uwezo wangu na unyonge wangu (wa kukabili adha) za watu.  Wewe Ndiye Mwenye  wingi wa Rehma na wingi wa Huruma na Upole.

Wewe  ni Mola wa wasiojiweza na wadhaifu.  Nawe ni Mola Wangu.  Unanitupa kwenye mikono ya nani (atakayenisaidia)?  Kwenye mikono ya jamaa  yangu aliye mbali na asiye na huruma na mimi?  Ambaye ananihamakia  kwa chuki na kunidharau?  Au kwenye adui aliyepewa utawala juu ya mambo yangu?  Lakini kama ghadhabu Yako  haitoanguka kwangu au haitonifikia basi hakuna kitu nitakachojali.  Na hakika msamaha Wako ni mkubwa kuliko dhambi zangu.     

Nakuomba  kutokana na Nuru ya Wajihi wako, ambayo inaangazia mbingu na inaondoa kiza na kutawala  mambo yote ya dunia na akhera ili hasira Yako isinifikie au ghadhabu Yako isiniangukie.  Na hakuna mamlaka wala nguvu na uwezo ila Wako peke yako.