25-Umuhimu Wa Tawhiyd Na Fadhila Zake: Ukitaka Mapenzi Ya Allaah, Thibitika Katika Tawhiyd

 

Umuhimu Na Fadhila Za Tawhiyd

 

25-Ukitaka Mapenzi Ya Allaah, Thibitika Katika Tawhiyd

 

 

 

Kumtii Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa kutekeleza amri Zake na kumpwekesha bila ya kumshirikisha ni katika dalili za kumpenda Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na kupata mapenzi Yake pia.

 

Waumini wa kikweli humpenda Allaah Pekee bila ya kumshirikisha yeyote katika mapenzi Yake. Kinyume chake ni kuelemeza mapenzi kwa wasiokuwa Allaah kama Anavyosema (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  

 

 وَمِنَ النَّاسِ مَن يَتَّخِذُ مِن دُونِ اللَّـهِ أَندَادًا يُحِبُّونَهُمْ كَحُبِّ اللَّـهِ ۖ وَالَّذِينَ آمَنُوا أَشَدُّ حُبًّا لِّلَّـهِ

Na miongoni mwa watu wako wenye kuchukua asiyekuwa Allaah na kuwafanya kuwa ni wanaolingana (na Allaah) wanawapenda kama kumpenda Allaah. Na wale walioamini wana mapenzi zaidi kwa Allaah. [Al-Baqarah: 165]

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Akaonya Waumini kwamba ikiwa watamkanusha na kuikanusha Dini Yake basi Anaweza kuwaleta wengineo ambao Atawapenda nao watampenda kikweli, Anasema hivyo katika kauli Yake:

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا مَن يَرْتَدَّ مِنكُمْ عَن دِينِهِ فَسَوْفَ يَأْتِي اللَّـهُ بِقَوْمٍ يُحِبُّهُمْ وَيُحِبُّونَهُ أَذِلَّةٍ عَلَى الْمُؤْمِنِينَ أَعِزَّةٍ عَلَى الْكَافِرِينَ يُجَاهِدُونَ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَلَا يَخَافُونَ لَوْمَةَ لَائِمٍ

Enyi walioamini! Yeyote atakayeritadi miongoni mwenu kutoka Dini yake, basi Allaah Ataleta watu (badala yao) Atakaowapenda nao watampenda; wanyenyekevu kwa Waumini, washupavu juu ya makafiri; wanafanya jihaad katika njia ya Allaah na wala hawakhofu lawama za mwenye kulaumu. [Al-Maaidah: 54]

 

 

Anayempenda Allaah kikweli hupenda yale Anayoyapenda Allaah kama humpwekesha kwa aina zote za Tawhiyd, na huchukia yale Anayochukia Allaah kama kumshirikisha, na hapo ndipo iymaan ya mtu inapothibitika. Na ndipo sharti mojawapo ya “laa ilaaha illa Allaah” ikawa ni: “Kupenda ambako kunaondowa kinyume chake”; yaani kutokupenda au kuchukia.” Ndio pia maana ya “Al-Walaa Wal-Baraa” (Kupenda na kuandamana na kuchukia na kutengana kwa ajili ya Allaah).

  

Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametaja hayo katika Hadiyth zifuatazo:

 

Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa):  

 

  ((أَوْثقُ عُرَى الإِيمان: الموالاَةُ في الله والمعاداةُ في الله، والحب في الله، والبغضُ في اللَّه عز وجل))   

Shikizo thabiti kabisa la iymaan ni kuwa na urafiki wa karibu kwa ajili ya Allaah na kujitenga kwa ajili ya Allaah, na kupenda kwa ajili ya Allaah, na kuchukia kwa ajili ya Allaah ‘Azza wa Jalla)) [Atw-Twabaraaniy katika Al-Kabiyr na ameisahihisha Al-Abaaniy katika Swahiyh Al-Jaami’ (2539))]

 

Hadiyth ya Anas bin Maalik (Radhwiya Allaahu ‘anhu):

 

 

عَنْ أَنَسِ بْنِ مَالِكٍ (رضي الله عنه) عَنْ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ: ((ثَلاَثٌ مَنْ كُنَّ فِيهِ وَجَدَ حَلاَوَةَ الإِيمَانِ: أَنْ يَكُونَ اللَّهُ وَرَسُولُهُ أَحَبَّ إِلَيْهِ مِمَّا سِوَاهُمَا، وَأَنْ يُحِبَّ الْمَرْءَ لاَ يُحِبُّهُ إِلاَّ لِلَّهِ, وَأَنْ يَكْرَهَ أَنْ يَعُودَ فِي الْكُفْرِ كَمَا يَكْرَهُ أَنْ يُقْذَفَ فِي النَّارِ)) متفق عليه

Amesimulia Anas bin Maalik (رضي الله عنه): Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Mambo matatu atakayekuwa nayo, atapata utamu wa imaan: Allaah na Rasuli Wake wawe vipenzi zaidi kwake kuliko wengineo, ampende mtu na wala asimpende isipokuwa kwa ajili ya Allaah, na achukie kurudi katika ukafiri baada ya Allaah kumwokoa kutoka huko kama anavyochukia kuingizwa motoni. [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

عَنْ أَبِي أُمَامَةَ ، قَالَ : قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ :  ((مَنْ أَحَبَّ فِي اللَّهِ وَأَبْغَضَ فِي اللَّهِ وَأَعْطَى لِلَّهِ وَمَنَعَ لِلَّهِ فَقَدِ اسْتَكْمَلَ الإِيمَانَ))  

Amesimulia Abuu Umaamah  (رضي الله عنه):  “Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم)  amesema: “Atakayependa kwa ajili ya Allaah, akachukia kwa ajili ya Allaah, akatoa kwa ajili ya Allaah, na akazuia kwa ajili ya Allaah, basi atakuwa amekamilisha imaan.”  [Abuu Daawuwd na ameisahihisha Al-Albaaniy (4681)]

 

 

عَنْ أَنَسٍ أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ (صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ) قَالَ: ((لاَ يُؤْمِنُ أَحَدُكُمْ حَتَّى أَكُونَ أَحَبَّ إِلَيْهِ مِنْ وَلَدِهِ وَوَالِدِهِ وَالنَّاسِ أَجْمَعِينَ)) أَخْرَجَاهُ

 

Amesimulia Anas (رضي الله عنه): Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Mmoja wenu hawi Muumini mpaka anipende mimi kuliko watoto wake na baba yake na watu wote.” [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

 

Mafanikio ya duniani na ya Aakhirah hayapatikani isipokuwa pale Muislamu atakapopenda kwa ajili ya Allaah na akachukia kwa ajili ya Allaah na akafuata maamrisho ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na Rasuli Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Hapo atakuwa miongoni mwa vipenzi vya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na watakuwa ni waliofadhilishwa kwa vyeo vya juu kabisa na kupewa nuru Siku ya Qiyaamah kama ilivyotajwa katika Hadiyth ifautayo inaelezea:

 

عَنْ عُمَرَ بْنَ الْخَطَّابِ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ قَالَ:قَالَ النَّبِىُّ صلى الله عليه وسلم: ((إِنَّ مِنْ عِبَادِ اللَّهِ لأُنَاسًا مَا هُمْ بِأَنْبِيَاءَ وَلاَ شُهَدَاءَ يَغْبِطُهُمُ الأَنْبِيَاءُ وَالشُّهَدَاءُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ بِمَكَانِهِمْ مِنَ اللَّهِ تَعَالَى)) قَالُوا: يَا رَسُولَ اللَّهِ تُخْبِرُنَا مَنْ هُمْ. قَالَ:  ((هُمْ قَوْمٌ تَحَابُّوا بِرُوحِ اللَّهِ عَلَى غَيْرِ أَرْحَامٍ بَيْنَهُمْ وَلاَ أَمْوَالٍ يَتَعَاطَوْنَهَا, فَوَاللَّهِ إِنَّ وُجُوهَهُمْ لَنُورٌ وَإِنَّهُمْ عَلَى نُورٍ, لاَ يَخَافُونَ إِذَا خَافَ النَّاسُ وَلاَ يَحْزَنُونَ إِذَا حَزِنَ النَّاس)) وَقَرَأَ هَذِهِ الآيَةَ: ((أَلَا إِنَّ أَوْلِيَاءَ اللَّـهِ لَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ))   

Kutoka kwa 'Umar bin Al-Khatwaab (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba Nabiy Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam amesema: ((Hakika miongoni mwa waja wa Allaah ni watu ambao si Manabii wala si mashahidi. Manabii na mashahidi watawaonea wivu kutokana na vyeo vyao vya juu mbele ya Allaah Ta’aalaa Siku ya Qiyaamah)) Wakasema: “Ee Rasuli wa Allaah! Tujulishe nani hao?” Akasema: ((Hao ni watu waliopendana kwa ajili ya Allaah bila ya kuwa na uhusiano wa damu, walahawakuungana kwa ajili ya mali. Naapa kwa Allaah! Nyuso zao zina nuru nao wako katika nuru. Hawaogopi wanapoogopa watu, wala hawahuzuniki wanapohuzunika watu)) Kisha akasoma Aayah hii: ((Tanabahi!  Hakika vipenzi wa Allaah hawana khofu juu yao, na wala hawatohuzunika.)) [Abu Daawuwd (3527) na ameisahihisha Al-Albaaniy (Aayah: Suwrat Yuwnus: 62)]

 

Tambua pia kwamba mapenzi ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) hayakamiliki bila ya kumfuata Rasuli Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kwa sababu Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:  

 

قُلْ إِن كُنتُمْ تُحِبُّونَ اللَّـهَ فَاتَّبِعُونِي يُحْبِبْكُمُ اللَّـهُ

Sema (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم): “Mkiwa mnampenda Allaah, basi nifuateni mimi, Atakupendeni Allaah  [Aal-‘Imraan: 31]

 

Kwa maana; kufuata Sunnah zake bila ya kuwenda kinyume na mafundisho yake na bila ya kuzusha mambo katika Dini.

 

 

Share