09 - Mambo ya Haramu Kwa Vinyozi: Baadhi Ya Saluni Vinyozi Huwanyoa Nywele Wanawake

Mambo ya Haramu yanayofanyika katika kazi ya Unyozi:

 

9. Baadhi Ya Saluni Vinyozi Huwanyoa Nywele Wanawake

 

Mwanamke kunyoa nywele zake kipara au kunyolewa ni jambo lililokatazwa na shariy’ah. Kadhaalika mwanamke kukata nywele zake kimitindo kama makafiri.

Kutoka kwa ‘Aliy (Radhwiya Allaahu ‘anhu) anaeleza kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amekataza wanawake kunyoa nywele zao. [At-Tirmidhiy na An-Nasaaiy]

Kadhaalika, Al-Khallaal (Rahimahu Allaah) anasimulia kutoka kwa Qataadah (Rahimahu Allaah) naye kutoka kwa ‘Ikrimah (Rahimahu Allaah) ambaye amesema: “Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amekataza wanawake kunyoa nywele zao.”

Vilevile Hadiyth iliyohadithiwa na Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Kunyoa nywele si jukumu lililowekewa wanawake; kukata kidogo ndivyo inavyotakiwa.” [Abuu Daawuwd].

Na Hadiyth nyingine kutoka kwa Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) ni kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Wanawake (mahujaji) hawafai kunyoa (vichwa vyao); wanaweza tu kupunguza nywele zao.” [Abuu Daawuwd].

Ibn al-Mundhir amesema: “Yapo maafikiano miongoni mwa Wanachuoni kuhusu hili, kwa kuwa kunyoa nywele za kichwa cha mwanamke ni aina ya adhabu.”

Kwa hali ya dharura kama maradhi ya kichwa au wadudu wa kichwani, hapo ndipo tu mwanamke anaporuhusiwa kunyoa kipara.

Ee kinyozi wa Kiislamu, mche Mola wako na jiepushe kunyoa wanawake nywele. Kumbuka kuwa, katika kumnyoa mwanamke nywele, mbali na makatazo yaliyo hapo juu, vilevile kunahusisha kutazama maeneo ya wazi ya mwanamke yasiyoruhusiwa kishariy’ah na kadhaalika kumgusa mwanamke na kumshika. Yote hayo ni haramu ya wazi.

 

 

Share