07-Kitaab At-Tawhiyd: Shirki Kuva Kikuku cha Chuma, Uzi n.k Kwa Ajili Kuondosha Au Kuzuia Balaa

Mlango Wa 7

بَابٌ مِنَ الشِّرْكِ لُبْسُ الْحَلْقَة وَالْخَيْطِ وَنَحْوِهِمَا لِرَفْعِ الْبَلَاءِ أَوْ دَفْعِهِ

Ni Shirki Kuva Kikuku cha Chuma Na Uzi Na Vitu Kama Hivyo Kwa Ajili Ya Kuondosha Au Kuzuia Balaa

 


 

وَقَوْلُ اللهِ تَعَالَى:

Na kauli Yake Ta’aalaa:

قُلْ أَفَرَأَيْتُم مَّا تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ إِنْ أَرَادَنِيَ اللَّـهُ بِضُرٍّ هَلْ هُنَّ كَاشِفَاتُ ضُرِّهِ أَوْ أَرَادَنِي بِرَحْمَةٍ هَلْ هُنَّ مُمْسِكَاتُ رَحْمَتِهِ ۚ قُلْ حَسْبِيَ اللَّـهُ ۖ عَلَيْهِ يَتَوَكَّلُ الْمُتَوَكِّلُونَ ﴿٣٨﴾

((Sema: “Je, mnaonaje wale mnaowaomba badala ya Allaah; ikiwa Allaah Atanikusudia dhara; je, wao wataweza kuondosha dhara Yake? Au Akinikusudia rahmah; je wao wataweza kuizuia rahmah Yake?” Sema: “Ananitosheleza Allaah”, Kwake watawakali wenye kutawakali)) [Az-Zumar (39: 38)]

 

عَنْ عِمْرَانَ بْنِ حُصَيْن (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) أَنَّ النَّبِيَّ (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ) رَأَى رَجُلاً فِي يَدِهِ حَلَقَةٌ مِنْ صُفْرٍ، فَقَالَ: ((مَا هَذِهِ؟))  قَالَ: مِنَ الْوَاهِنَةِ فَقَالَ: ((انْزَعْهَا؛ فَإِنَّهَا لاَ تَزِيدُكَ إِلاَّ وَهَنًا، فَإِنَّكَ لَوْ مِتَّ وَهِيَ عَلَيْكَ؛ مَا أَفْلَحْتَ أَبَدًا))  رَوَاهُ أَحْمَدُ بِسَنَدٍ لا بَأْسَ بِهِ.

Imepokelewa kutoka kwa ‘Imraan bin Huswayn (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) kwamba Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) alimwona mtu amevaa kikuku cha chuma mkononi mwake, akamuuliza: ((Nini hiki?)) Akajibu: “Kuzuia udhaifu wa uzee.” Akasema: ((Ivue, kwani haizidishi ila udhaifu. Na pindi ukifa ukiwa nacho, hutofaulu kamwe)) [Imekusanywa na Ahmad katika Musnad (4/445) kwa isnaad nzuri]

 

وَلَهُ عَنْ عُقْبَةَ بْنِ عَامِرٍ (رضي الله عنه) مَرْفُوعًا: ((مَنْ تَعَلَّقَ تَمِيمَةً؛ فَلَا أَتَمَّ اللهُ لَهُ، وَمَنْ تَعَلَّقَ وَدَعَةً؛ فَلَا وَدَعَ اللهُ لَهُ))

Ahmad amepokea pia kutoka kwa ‘Uqbah bin ‘Aamir  (رضي الله عنه) Hadiyth Marfuw’ kwamba Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Atakayetundika talasimu[1] hatopata kuona haja yake kutimizwa na Allaah. Na atakayeitundika kombe la pwani hatopata amani na utulivu kutoka kwa Allaah [yaani Allaah Hatomkhafifishia anayoyaogopea])) [Ahmad katik Musnad (4/154)]

 

وَفِي رِوَايَةٍ: ((مَنْ تَعَلَّقَ تَمِيمَةً؛ فَقَدْ أَشْرَكَ))

Na katika riwaayah nyingine: ((Atakayetundika talasimu kwa yakini ameshirikisha)) [Ahmad katika Musnad (4/156)]

 

وَلإِبْنِ أَبِي حَاتِمٍ عَنْ حُذَيْفَةَ (رضي الله عنه) أَنَّهُ رَأَى رَجُلاً فِي يَدِهِ خَيْطٌ مِنَ الْحُمَّى، فَقَطَعَهُ وَتَلا قَوْلَهُ : وَمَا يُؤْمِنُ أَكْثَرُهُم بِاللَّـهِ إِلَّا وَهُم مُّشْرِكُونَ ﴿١٠٦﴾

Ibn Haatim ameripoti kutoka kwa Hudhayfah (رضي الله عنه) kuwa alimuona mtu amevaa talasimu (kwa ajili ya kukinga homa) akaikata kisha akasoma kauli Yake Allaah ((Na wengi kati yao hawamwamini Allaah isipokuwa wao ni wenye kufanya shirki)) [Yuwsuf (12: 106)] [Yaani wanamuamini Allaah, lakini huku wanamshirikisha]

 

 

 

Masuala Muhimu Yaliyomo:

 

1-Haramisho la kuvaa vikuku vya chuma nyuzi na mfano wake.

 

 

2-Ikiwa mvaaji atafariki akiwa ameivaa hatofaulu (Aakhirah). Hii inaunga mkono kauli ya Maswahaba kuwa shirki ndogo ni mbaya kuliko madhambi makubwa.

 

 

3-Kutokujua si udhuru.

 

 

4-Kuvaa vitu kama hivyo, havitonufaisha humu duniani bali vitadhuru kama alivyosema Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم): ((haizidishi ila udhaifu)).

 

 

5-Kemeo kali kwa mwenye kufanya jambo kama hili.

 

 

6-Inaeleza kuwa mmojawapo anapovaa vitu hivi anakuwa ameachwa alindwe na hivyo vitu (badala ya ulinzi wa Allaah (سبحانه وتعالى) na hivyo hana ulinzi wowote.

 

 

7-Maelezo kuwa mwenye kuvaa hirizi amefanya shirki.

 

 

8-Kuvaa kamba (kitambaa au uzi) kwa ajili ya homa ni sawa na hayo ya kuwa ni shirki.

 

9-Hudhayfah   (رضي الله عنه)kusoma Aayah ya Qur-aan  ni dalili ya wazi kwamba Maswahaba walikuwa wakinukuu Aayah inayohusu shirki kubwa kwa ajili ya kukanusha shirki ndogo, kama alivyofanya Ibn ‘Abbaas   (رضي الله عنهما) kuisoma Aayah ya Al-Baqarah namba (2: 165).

 

 

10-Kuvaa hirizi kwa ajili ya kujilinda na jicho baya kunaangukia katika kundi hilohilo.

 

 

11-Du’aa (ya kumlaani) mwenye kuvaa hirizi, kuwa Allaah (سبحانه وتعالى) Hatomtimizia maombi yake. Na anayejifunga na kombe (la kiumbe wa baharini), hatokuwa katika amani na utulivu yaani Allaah (سبحانه وتعالى) Hatomjali.

 

 

 

 

 

[1] Hirizi: Karatasi inayotundikwa ukutani kwa ajili ya kinga au kuvaliwa shingoni au mikononi.

Share