50-Kitaab At-Tawhiyd: Kuharamishwa Majina Yanayoabudiwa Badala Ya Allaah

Mlango Wa 50

باب: فَلَمَّا آتَاهُمَا صَالِحًا جَعَلَا لَهُ شُرَكَاءَ فِيمَا آتَاهُمَا

Kuharamishwa Majina Yanayoabudiwa Badala Ya Allaah


 

 

قَوْلُ اَللَّهِ تَعَالَى:

Kauli ya Allaah Ta’aalaa:

 

فَلَمَّا آتَاهُمَا صَالِحًا جَعَلَا لَهُ شُرَكَاءَ فِيمَا آتَاهُمَا ۚ فَتَعَالَى اللَّـهُ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿١٩٠﴾

((Basi Anapowapa (mtoto) mwema asiyekuwa na kasoro, wanamfanyia (Allaah) washirika katika kile Alichowapa. Basi Ametukuka Allaah kwa Uluwa kutokana na yale yote wanayoshirikisha)) [Al-A’raaf (7: 190)]

 

 قَالَ اِبْنُ حَزْمٍ:  اِتَّفَقُوا عَلَى تَحْرِيمِ كُلِّ اِسْمٍ مُعَبَّدٍ لِغَيْرِ اَللَّهِ كَعَبْدِ عَمْرِوٍ وَعَبْدِ الْكَعْبَةِ وَمَا أَشْبَهَ ذَلِكَ، حَاشَا عَبْدِ الْمُطَّلِبِ.

Ibn Hazm amesema: Wamekubaliana (huenda imekusudiwa Ijmaa’ - ’Ulamaa) kuharamisha kila jina linalomaanisha kuabudiwa kinyume na Allaah; mfano ‘Abd-‘Umar (mja wa ‘Umar), ‘Abdul-Ka’bah (mja wa Ka’bah), na kama hivyo isipokuwa ‘Abdul-Muttwalib – hili limeruhusiwa.

 

وَعَنِ اِبْنِ عَبَّاسٍ قَالَ: ((لِمَا تَغَشَّاهَا آدَمُ حَمَلَتْ، فَأَتَاهُمَا إِبْلِيْسُ فَقَالَ: إِنِّي صَاحِبُكُمَا اَلَّذِي أَخْرَجَكُمَا مِنَ الْجَنَّة، لَتُطِيعَانِّنِي أَوْ لأَجْعَلَنَّ لَهُ قَرْنَيْ إِيِّلٍ فَيَخْرُجُ مِنْ بَطْنِكَ فَيَشُقُّهُ وَلأَفْعَلَنَّ - يُخَوِّفُهُمَا - سَمِّيَاهُ عَبْدَ الْحَارِثِ،

 فَأَبَيَا أَنْ يُطِيْعَاهُ فَخَرَجَ مَيِّتًا. ثُمَّ حَمَلَتْ فَأَتَاهُمَا فَذَكَرَ لَهُمَا فَأَدْرَكَهُمَا حُبُّ الْوَلَدِ فَسَمَّيَاهُ عَبْدَ الْحَارِثِ فَذَلِكَ قَولُهُ: ((جَعَلَا لَهُ شُرَكَاءَ فِيمَا آتَاهُمَا))   رَوَاهُ اِبْنُ أَبِي حَاتِمٍ

Na Imepokelewa kutoka kwa Ibn ‘Abbaas(رضي الله عنهما)  katika kuifafanua Aayah hiyo, amesema: “Aadam alipombashiri Hawaa alishika mimba. Ibliys akawaendea na kusema: “Mimi ndiye mwenzenu niliyekusababisheni kutolewa Jannah. Mtanitii au sivyo nitamfanya mtoto wenu aote pembe mbili kama swala tumboni mwa mama yake ambazo zitapasua tumbo lake wakati wa kumzaa, na hakika nitafanya hivyo!”  Akawatisha - na kusema: “Muiteni ‘Abdul-Haarith” (mja wa mkulima). Lakini walikataa kumtii, akazaliwa mtoto akiwa amekufa. Kisha Hawaa aliposhika mimba mara ya pili, Ibliys akawaendea tena akakariri kauli yake (kuwataka wafanye vile na kuwatisha). Wakakataa tena kumtii. Akazaliwa mtoto akiwa amekufa. Kisha Hawaa akashika mimba tena, Ibliys akawaendea akawakumbusha yaliyotokea awali, wakajazwa mapenzi ya mtoto na wakamwita mtoto ‘Abdul-Haarith. Na hivyo ndio maana ya kauli ya Allaah: ((wanamfanyia (Allaah) washirika katika kile Alichowapa))

 

وَلَهُ بِسَنَدٍ صَحِيْحٍ عَنْ قَتَادَة:  قَالَ: شُرَكَاءُ فِي طَاعَتِهِ وَلَمْ يَكُنْ فِي عِبَادَتِهِ

Naye (Ibn Haatim) amepokea kwa isnaad Swahiyh kutoka kwa Qataadah: Amesema: “Washirika katika kumtii Kwake, na si katika kumwabudu kinyume Naye.”

 

وَلَهُ بِسَنَدٍ صَحِيحٍ عَنْ مُجَاهِدٍ فِي قَوْلِهِ ((لَئِنْ آتَيْتَنَا صَالِحًا))  قَالَ: أَشْفَقَا أَلاَّ يَكُونَ إِنْسَانًا. وَذَكَرَ مَعْنَاهُ عَنْ الْحَسَنِ وَسَعِيدٍ وَغَيْرِهِمَا.

Naye (Ibn Haatim) amesimulia kutoka kwa Mujaahid kuhusu kauli Yake Allaah: ((Ukitupa (mtoto) mwema asiyekuwa na kasoro)) [Al-A’raaf (7:189)] Amesema: (Aadam na Hawaa) waliogopa mtoto asije kuwa si bin Aadam.  Maana kama hiyo imetajwa na Hasan, Sa’iyd na wengineo.

 

 

Masuala Muhimu Yaliyomo:

 

1-Jina lolote lenye maana ya kumwabudu asiye Allaah (سبحانه وتعالى) limeharamishwa.

 

2-Tafsiri ya Aayah katika Suwrah Al-A’raaf (7: 189).

 

3-Shirki hii inahusiana katika kulipa jina tu japokuwa haikukusudiwa maana yake, yaani kuabudiwa huyo mtoto. 

 

4-Neema kubwa ya Allaah (سبحانه وتعالى) kumruzuku mtu mtoto mwema kamili asiye na kasoro. 

5-As-Salaf wametofautisha baina ya shirki katika kutii na shirki katika kuabudu.   

 

 

Share