151-Aayah Na Mafunzo: Miongoni Mwa Aliyopewa Nabiy Ni Kutiwa Kizaazaa Maadui Ili Waislamu Wapate Nusra

 

Aayah Na Mafunzo

Aal-‘Imraan

 

Miongoni Mwa Aliyopewa Nabiy Ni Kutiwa Kizaazaa Maadui Ili Waislamu Wapate Nusra

 

Alhidaaya.com

 

 

Anasema Allaah (سبحانه وتعالى):

 

سَنُلْقِي فِي قُلُوبِ الَّذِينَ كَفَرُوا الرُّعْبَ بِمَا أَشْرَكُوا بِاللَّـهِ مَا لَمْ يُنَزِّلْ بِهِ سُلْطَانًا ۖ وَمَأْوَاهُمُ النَّارُ ۚ وَبِئْسَ مَثْوَى الظَّالِمِينَ ﴿١٥١﴾

151. Tutavurumisha kizaazaa katika nyoyo za waliokufuru kwa sababu ya kumshirikisha Allaah na ambayo Hakuyateremshia mamlaka. Na makazi yao ni moto, na ubaya ulioje maskani ya madhalimu

 

Mafunzo:

 

Pindi Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) alipopigana vita pamoja na Swahaba zake dhidi ya makafiri, na idadi ya makafiri ilikuwa ni wengi mno kulikoni idadi ya Waislamu, Allaah (سبحانه وتعالى)  Aliwateremshia Waislamu miujiza kadhaa kuwasaidia waweze kupambana na makafiri na wapate ushindi. Mfano wa muujiza mmojawapo ni pale Allaah (سبحانه وتعالى) Alipowafanya makafiri wawaone Waislamu katika macho yao kuwa ni wa idadi kubwa ilhali ni wachache mno. Anasema Allaah (سبحانه وتعالى):

 

قَدْ كَانَ لَكُمْ آيَةٌ فِي فِئَتَيْنِ الْتَقَتَا ۖ فِئَةٌ تُقَاتِلُ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَأُخْرَىٰ كَافِرَةٌ يَرَوْنَهُم مِّثْلَيْهِمْ رَأْيَ الْعَيْنِ ۚ وَاللَّـهُ يُؤَيِّدُ بِنَصْرِهِ مَن يَشَاءُ ۗ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَعِبْرَةً لِّأُولِي الْأَبْصَارِ ﴿١٣﴾

Kwa hakika ilikuwa ni Aayah (ishara) kwenu katika makundi mawili; yalipokutana (vita vya Badr). Kundi linapigana katika njia ya Allaah na jingine ni makafiri ambao wanawaona (Waislamu) mara mbili yao kwa mtazamo wa macho. Na Allaah Humsaidia kwa nusura Yake Amtakaye. Hakika katika hayo bila shaka ni zingatio kwa wenye utambuzi. [Aal-‘Imraan: 13]

 

Hali kadhalika muujiza mwenginewe ni kutiwa kiwewe, kizaazaa, khofu kubwa nyoyoni mwa makafari, waogope na iwafanye wawe dhaifu na hivyo ushindi upatikane kwa Waislamu:

 

Abuu Huraryah (رضي الله عنه) amehadithia kwamba Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Nimefadhilishwa juu ya Manabii kwa mambo sita: nimepewa; ‘Jawaami’al-Kalimi’ (mukhtasari unaojumuisha maneno mengi) na nimenusuriwa kwa (kutiwa) kizaazaa (katika nyoyo za maadui) na nimehalalishiwa ghanima na nimefanyiwa ardhi kuwa kitwaharishi na Masjid (mahali pa kuswali) na nimetumwa kwa viumbe wote, na Manabii wamekhitimishwa kwangu.” [Muslim].

 

 

 

 

 

 

 

Share