Skip navigation.
Home kabah

Mashairi - Mke Bora



Mtungaji: 'Aliy 'Umar 'Uthmaan 

 

1.     Tupunguze mahari,              mabanati waolewe

        Ili tuepuke shari,         wenetu wasitiriwe

        Tuwatoe kwa fahari,            tuombe wabarikiwe

 

2.     Mke alivyoamriwa,               dini yetu tuisome

        Kwake mefaradhiwa,            sheria aziandame

        Lau mja husujudiwa,             mke angeabudu mume  

 

3.     Akae nyumbani kwake, amlekee Mola pekewe

        Atimize wajibu wake,           ibada kwa wakatiwe

        Jihadi ya mwanamke,           ni kumtwii mumewe

 

4.     Binti jikalie kwako,              upate kusifika

        Mume ni rafiki yako,            kumliwaza yataka

        Mume ni moshi wa koko,       usipowaka hufuka

 

5.     Husitiri siri yake,         hampi labuda maiti

        Katu usiteteleke,        usiwe yako hufiti

        Mtu hafui demu lake,           katikati ya umati

 

6.     Siku zote vumilia,                mambo ngakusonga

        Nyumbayo shikilia,              maisha vyema panga

        Mwana elewa dunia,            ni pepo ya wajinga

 

7.     Ufanye uvumilivu,                uandame ule wakati

        Jikoni japo kukavu,              ulimi wako dhibiti

        Asokujua alie wivu,             aone una mno bahati

 

8.     Waepuke wavundifu,            tunga wako muamala

        Hali japo ni dhaifu,              sitamauke kwa Mola

        Mtu haandami lufufu,           ni matumizi na kula

 

9.     Mja hujua atokako,              dhiki nana usione

        Katu hujui wendako             muatie Mola sinene

        Siri za nyumba yako,            zisikeuke kuta nne

 

10.    Hutopata utakacho,             pepo tanga uandame

        Siwe nanga ubwiacho,  ni hilo hilo siseme

        Shukuru upawacho,              simkalifishe mume

 

11.    Mwana soma upishi,            hebu wata kukoroga

        Upike mule freshi,               vyakula na maboga

        Basi hapo mutaishi,             ya kweli sio soga

 

12.    Uwe bora muandazi,            uwalishe vya tiba

        Wape wanayo malezi,          shirikiana na baba

        Waonyeshe mapenzi,           japo riziki ni haba

 

13.    Kupunguza gharama,           na uipinge isirafu

        Huwa nusu ya kutuma,          kujiwekea halafu

        Kuyafuja mali koma,            kuna maji kuwa mafu

 

14.    Pale mukiruzukiwa,              ukumbuke na ukame

        Na dini tumeusiwa,              muonee utungu mume

        Usipike visoliwa,         mwana israfu ukome

 

15.    Tunga mali ya mumeo,        ni akibayo usivuju-usifujeni 

        Siri ziweke pekeyo,              sinene hata iweje

        Saza simalize leo,               kesho shida zisije

 

16.    Jilinde na machafu,              umakinike uolewe

        Uepuke na uvundifu,            wendapo usitahiwe

        Sifa ya mke ni upofu,            asoona illa mumewe

 

17.    Mke mwema ni kiziwi,  haoni wala hasikii

        Asowasikiza wawi,               raha mume kumtwii

        Na waovu hahadawi,            uchafu hafikirii

 

18.    Mke mwema ni kiduko, uzito kutiwa chuki

        Huviepuka vituko,                hamtii mume dhiki

        Katu hana papatiko,            mumewe hambanduki

 

19.    Mke mwema huwa bubwi,     asonena illa kheri

        Si umbile la lumbwi,            kisema hutafakari

        Kinyume na chubwi,             aolea juu ya bahari

 

20.    Mke sawa awe kiwete,         hakeuki kizingiti

        Katu hendi kokote,              akikatzwa huketi

        Wa nidhamu saa zote,         haupotezi wakati

 

21.    Mwana siwe kirango,            buibui kuwa ruhusa

        Katu sinene urongo,            hilo ni kubwa kosa

        Lituze lako bongo,               waume wawapi sasa?

 

22.    Mwana guu silivute,             bila ruhusa ya mume

        Kikatazwa usitete,              shatani usiandame

        Radhi ya Mngu upate,          katu nawe silalame

 

23.    Utunge sana ulimi,              siyanene yakaraha

        Hututongea ndimi,               tukazikosa na raha     

Kama kweli umneni,            basi nena ya furaha

 

24.    Na mumeo mukiteta,           sio mbele ya watoto

        Suluhu nawe tafuta,            wala usione uzito

        Msamaha kishapata,            ndio ulifumbe jito

 

25.    Usimuinulie sauti,               kimzungumzia mume

       Ikitokea tafauti,          siropokwe jipime

        Alozalikana binti,                ni mtele uso ndume

 

26.    Saa zote jieke safi,             japo ni kopo la maji

        Husifika mwanamke,            upambe kiwa kipaji

        Mume hata atosheke,          awe nde si mwendaji

 

27.    Pale jito lifikapo,         pawe swafi mwilini

        Kila nyote mukaapo,            utumie lugha laini

        Hata kenda endapo,            roho iwe nyumbani

 

28.    Nguo japo tambara,             uchachage lazima

        Bora upate sitara,               dhikizo kutosema

        Usimame sana imara,          usitikisike daima

 

29.    Simnukishe uvundo,             aingiapo nyumbani

        Ayaone kwa vitendo,            ustaarabu wa pwani

        Umuoneshe na pendo,         akiwa nde na ndani

 

30.    Ujifukize na nyudi,              jikwatue ndio ada

        Ujiweke maradadi,               kwa viluwa na poda

        Mumeo roho iburudi,            nakuusia ewe dada

 

31.    Mama imekulazimu,             una wajibu duniani

        Ulichozaa muhimu,              yatie sana akilini

        Mama ndiwe mwalimu,        wa wanayo nyumbani

 

32.    Walee wanayo vyema, kwa misingi ya dini

        Waonee sana huruma,         siwatese masikini

        Uhusiano uwe mwema,        watakufaa mbeleni

 

33.    Mpendee mume nduze,        ulitunge na jinale

        Mume usimpeleleze,            yuwatoa ngapi kule

        Muhimu atakeleze,              katu haramu musile

 

34.    Mtie mume urafiki,         hata nde kusimueke

        Ili waja wanafiki,            mabega yawashuke

        Ni wajibu yako haki,            mtu kuzatiti chake

 

35.    Marafikizo kwanda,              watuje kwa makini

        Watague kama tunda,          pale wendapo sokoni

        Uepuke asokupenda,            kumjaza nyumbani

 

36.    Watunge sana watu,            usije matozi kulia

        Kuna wasojali kitu,              na wenye mbaya nia

        Kitanda asisubutu,              mwengineo kulalia

 

37.    Linda faragha yako,             wasione watu wote

        Uwe na mema mashiko,       uyafuate kwa kite

        Mke chumbani kwako,  mamnuu kwa yoyote

 

      38.     kama una uzuri- kama una uzuri bora,      hutomshinda Hawa

           Wapili mrembo Sara,                    Ibrahimu alomkewa

            Vipusa walo na sura,                    na radhi za Moliwa

 

39.    Mwana usiteteleke,             usiwe nawe kama hao

        Jikaze mno umueke,            mume ubora alonao

        Wele wao wanawake,          wasotwii waume zao