Skip navigation.
Home kabah

Mashairi - Du'aa Ya Rizki

Mtungaji: 'Aliy 'Umar 'Uthmaan

Ya Rabi tupe riziki,                  iso dhiki au tetesi

Uwezo na tudiriki,                   maisha yetu rahisi

Tuipate na taufiki,                   mazito yawe mepesi

 

Riziki iwapo mbali,                  tusongezee karibu

Uzifanye shughuli,                  ziwe pasi masaibu

Tumo liwe la halali,                 maishani tuswibu

 

Riziki ilo ardhini,                ujaalieyo itepuze

Na mvua situkhini,                  miti yetu ipendeze

Vuno bora shambani,              kula sisi na tuuuze

 

Ilo juu yetu ruzuku,                tini tuteremshie

Ulopiga marufuku,                  hivyo utuepushie

Tule mtana na usiku,              wendo tugawanyie

 

Fungu liwapo dogo,                 tuzidishie idadi

Vya shamba na mifugo,          uvilinde na hasidi

Yote yetu mipango,                uturidhie miradi

 

Riziki kiwa nyingi,                   ibariki mno idumu

Iweke mema misingi,             halali bila haramu

Vilo kheri na vingi,                       kwa ndugu tukasimu

 

Rabbi situpe mazito,                   tusoweza kuyabeba

Mizigo yawe matoto,              tusidhiki swahiba

Lijaalie letu pato,                    liwe jingi sio haba

 

Pasife kati yetu,                        illa we memrehemu

Safari kuja kwetu,                  nasi metulazimu

Tuwe na Mtume wetu,               mema uje tukirimu

 

Tusiugue maradhi,                  bila kutuonya dawa

Hapa kwenye aridhi,               tufuate yalo sawa

Maisha utuhifadhi,                  na wale wakupotoa

 

Utulinde na madeni,                kutushinda kulipa

Japo kuwa masikini,               tuweze wetu kuwapa

Tumuduvyo duniani,               visiwe vya kukopa