كِتَابُ اَلصِّيَامِ
Kitabu Cha Swiyaam
Abu Maalik Kamaal Bin As-Sayyid Saalim
Imetarjumiwa na 'Abdullaah Mu'aawiyah (Abu Baasim)
Alhidaaya.com
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
01-Taarifu ya Swawm
Alhidaaya.com [3]
[Al-Lubaab (1/162), Al-Majmuw’u (6/248) na Al-Mughniy (3/84)]
الصيام و الصوم “Swiyaam” na “HAJJ” katika lugha ya kawaida ina maana ya kujishika na kujizuia na kitu, na hutumiwa katika kujizuia kwa aina zote. Allaah Ta’aalaa Akimzungumzia Maryam (‘Alayhas Salaam) Amesema:
(( إِنِّي نَذَرْتُ لِلرَّحْمَـٰنِ صَوْمًا))
((Hakika mimi nimeweka nadhiri ya swawm [ya kutozungumza] kwa Ar-Rahmaan)). [Maryam (19: 26)]
Yaani, kunyamaza, kujishika na kujizuia na kunena.
Ama kisharia, ni kujizuia na vyenye kufunguza Swawm toka kuchomoza Alfajiri hadi jua kuchwa pamoja na niya ya kumfanyia ‘ibaadah Allaah Ta’aalaa.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
02-Fadhila Za Swiyaam Na Faida Zake
Alhidaaya.com [3]
(a) Swiyaam ni katika twa’a adhwimu za kujikurubisha kwazo kwa Allaah Ta’aalaa ambazo Muumini hulipwa thawabu zisizo na mipaka. Kwa ‘ibaadah hii, dhambi alizozifanya mtu nyuma hufutwa, hubaidishwa kati ya uso wake na kati ya moto, hustahiki mja kuingia Peponi kupitia mlango maalumu ulioandaliwa kwa ajili ya wafungaji, na mja atafurahi kwayo atakapokutana na Mola wake.
1- Toka kwa Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu Anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((قال الله عز وجل: كل عمل ابن آدم له إلا الصيام فإنه لي وأنا أجزي به، والصيام جنة، فإذا كان يوم صوم أحدكم فلا يرفث ولا يصخب ولا يجهل، فإن شاتمه أحد أو قاتله قليقل: إني صائم –مرتين- والذي نفس محمد بيده لخلوف فم الصائم أطيب عند الله يوم القيامة من ريح المسك، وللصائم فرحتان يفرحهما: إذا أفطر فرح بفطره، وإذا لقي ربه فرح بصومه))
((Allaah ‘Azza wa Jalla Amesema: Kila ‘amali ya mwanadamu ni yake, isipokuwa Swiyaam, hakika Swiyaam yanihusu Mimi tu, na Mimi Ndiye Ninasimamia malipo yake. Na Swiyaam ni ngao, na itakapokuwa siku ya Swiyaam ya mmoja wenu, basi asitamke maneno machafu, wala asipayuke na kupaza sauti, wala asifanye mambo ya ovyo. Na ikiwa mtu atatafuta sababu ya kutukanana naye, au kupigana naye basi aseme: Hakika mimi niko kwenye Swiyaam –mara mbili-. Naapa kwa Ambaye nafsi ya Muhammad iko Mkononi Mwake, hakika harufu mbaya ya kinywa cha mfungaji, itanukia vizuri zaidi kwa Allaah Siku ya Qiyaamah kuliko harufu ya misk. Na mfungaji ana furaha mbili anazozifurahia: anapofungua hufurahi kwa kufuturu kwake, na atakapokutana na Mola wake atafurahi kwa Swawm yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1904) Muslim (1151) na wengineo]
2- Toka kwa Abu Hurayrah amesema: “Amesema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((من صام رمضان إيمانا واحتسابا، غفر له ما تقدم من ذنبه))
((Atakayefunga Ramadhwaan kwa iymaan na kutarajia malipo [toka kwa Allaah], hughufiriwa dhambi zake zilizotangulia)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1900) Muslim (760) na wengineo]
3- Toka kwa Sa’iyd Al-Khudriy amesema: “Amesema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘ alayhi wa aalihii wa sallam):
((لا يصوم عبد يوما في سبيل الله إلا باعد الله بذلك اليوم وجهه عن النار سبعين خريفا))
((Hafungi mja siku yoyote katika Njia ya Allaah isipokuwa Allaah Ataubaidisha uso wake kwa siku hiyo na moto miaka 70)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2840), Muslim (1153) na wengineo]
4- Toka kwa Sahl bin Sa’ad kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((إن في الجنة بابا يقال له الريان يدخل منه الصائمون يوم القيامة لا يدخل منه أحد غيرهم يقال: أـين الصائمون؟ فيقومون لا يدخل منه أحد غيرهم، فإذا دخلوا أغلق فلم يدخل منه أحد))
((Hakika Peponi kuna mlango uitwao Ar-Rayyaan,, wataingia kupitia kwao wafungaji Siku ya Qiyaamah, haingii yeyote kupitia kwao zaidi yao. Patanadiwa: Wako wapi wafungaji? Watasimama, haingii kupitia kwao yeyote zaidi yao. Wanapoingia, utafungwa, na hatoingia yeyote kupitia kwao)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1896), Muslim (1152) na wengineo]
(b) Swiyaam ni chuo cha tabia na mwenendo ambapo Muumini anajifunza humo mambo mengi. Swiyaam ni Jihaad ya nafsi, ni mapambano dhidi ya hawaa na vishawishi viovu vya Shaytwaan ambavyo vinaweza kumtokezea. Pia mtu hujizoesha kwayo kuwa na tabia ya subra kwa vitu ambavyo hawezi kuvipata, na anapokabiliwa na matukio ya kutisha na kuogofya na misukosuko. Kadhalika, hufundisha nidhamu na utiifu, hukuza kwa mtu mhemko wa huruma na udugu, na hisia ya mshikamano na ushirikiano unaowaunganisha Waislamu. [Al-Fiqhu Al-Islaamiy wa Adillatuh (2/566-568)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
03-Vigawanyo Vya Swiyaam
Alhidaaya.com [3]
Jua kwamba Swiyaam ina vigawanyo viwili:
1- Swiyaam ya Waajib
2- Swiyaam ya Sunnah
1- Vigawanyo Vya Swiyaam Ya Waajibu
Swiyaam ya Waajib ina vigawanyo vitatu: [Bidaayatul Mujtahid (1/422)]
(a) Ni ya waajib katika wakati wake husika. Hii ni Swawm ya Mwezi wa Ramadhwaan wenyewe, na ndiyo ambayo ahkaam zake tunazizungumzia hapa.
(b) Ni ya waajib kutokana na sababu. Hii ni Swiyaam ya Kafara.
(c) Ni ya waajib kutokana na mtu kujiwajibishia mwenyewe hilo. Hii ni Swiyaam ya Nadhiri.
Vigawanyo hivi viwili (Swiyaam ya Kafara na Nadhiri) tutavifafanua kila kimoja peke yake katika mahala pake.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
04-Swiyaam ya Ramadhwaan Hukmu Yake
Alhidaaya.com [3]
Swiyaam ya Ramadhwaan ni waajib kwa kila Muislamu aliyebaleghe, mwenye akili timamu, mzima wa afya na mkazi. Ni nguzo kati ya nguzo za Uislamu, na uwajibu wake umedulishwa na Qur-aan, Sunnah na Ijma’a ya Ummah.
Kutoka Qur-aan ni Kauli Yake Ta’aalaa:
((يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا كُتِبَ عَلَيْكُمُ الصِّيَامُ كَمَا كُتِبَ عَلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكُمْ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ • أَيَّامًا مَّعْدُودَاتٍ ۚ فَمَن كَانَ مِنكُم مَّرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ ۚ وَعَلَى الَّذِينَ يُطِيقُونَهُ فِدْيَةٌ طَعَامُ مِسْكِينٍ ۖ فَمَن تَطَوَّعَ خَيْرًا فَهُوَ خَيْرٌ لَّهُ ۚ وَأَن تَصُومُوا خَيْرٌ لَّكُمْ ۖ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ • شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِي أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَىٰ وَالْفُرْقَانِ ۚ فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ ۖ وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ ۗ يُرِيدُ اللَّـهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلَا يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ وَلِتُكْمِلُوا الْعِدَّةَ وَلِتُكَبِّرُوا اللَّـهَ عَلَىٰ مَا هَدَاكُمْ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ))
((Enyi walioamini! Mmefaridhishwa Swiyaam kama ilivyofaridhishwa kwa walio kabla yenu mpate kuwa na taqwa • (Swiyaam ni) Siku za kuhesabika. Lakini atakayekuwa mgonjwa miongoni mwenu, au yuko safarini, basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. Na kwa wale wanaoiweza lakini kwa mashaka na kutaabika watoe fidia; kulisha masikini. Na atakayefanya kwa khiari yake jema lolote, basi hilo ni bora kwake. Na mkifunga Swiyaam ni bora kwenu mkiwa mnajua • Mwezi wa Ramadhwaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan ili iwe mwongozo kwa watu na hoja bayana za mwongozo na pambanuo (la haki na batili). Basi atakayeshuhudia miongoni mwenu mwezi na afunge. Na atakayekuwa mgonjwa au safarini basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. Allaah Anakutakieni mepesi na wala Hakutakieni magumu; na ili mkamilishe idadi na ili mumkabbir Allaah kwa kuwa Amekuongozeni na ili mpate kushukuru)). [Al-Baqarah (2:183-185)]
Na kutoka kwenye Sunnah:
1- Hadiyth ya Talha bin ‘Ubaydillaah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba bedui mmoja alikuja kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) ilhali nywele zake zimevurugika, zimejaa vumbi (kutokana na safari) akasema: “Nieleze Aliyonifaradhia Allaah katika Swiyaam”. Akasema:
((شهر رمضان إلا أن تطوع شيئا))
((Mwezi wa Ramadhwaan isipokuwa kama utafanya kitu cha ziada [cha Sunnah])). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (46) na Muslim (11)]
2- Hadiyth ya Ibn ‘Umar (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) amesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((بني الإسلام على خمس: شهادة أن لا إله إلا الله وأن محمدا رسول الله، وإقام الصلاة، وإيتاء الزكاة، والحج، وصوم رمضان))
((Uislamu umejengwa juu ya (nguzo) tano: Kushahadia kuwa hapana mungu isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Rasuli wa Allaah, kusimamisha Swalaah, kutoa Zakaah, Kuhiji na kufunga Ramadhwaan)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (8) na Muslim (16)]
3- Hadiyth mashuhuri ya Jibriyl isemayo: Akasema (Rasuli):
((الاسلام أن تعبد الله ولا تشرك به، وتقيم الصلاة، وتؤتي الزكاة المفروضة، وتصوم رمضان...)) الحديث
((Uislamu ni (wewe) umwabudu Allaah na wala usimshirikishe, usimamishe Swalaah, utoe Zakaah iliyofaradhishwa, na ufunge Ramadhwaan..)). Hadiyth [Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (50) na Muslim (9)]
Waislamu wote wanakubaliana kuwa Swawm ni nguzo kati ya nguzo za Uislamu zinazojulikana kwa ulazima katika Diyn ambapo mwenye kuikanusha anakuwa kafiri, na kwamba nguzo hii haipomoki kwa mukallaf (aliyebaleghe) isipokuwa kwa udhuru kati ya nyudhuru za kisharia zinazokubalika ambazo tutakuja kuzielezea. [Al-Ifswaah cha Ibn Habiyrah (1/232), Al-Mughniy (3/285) na Al-Majmuw’u (6/252)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
05-Kati Ya Fadhila Za Ramadhwaan Na Kufanya ‘Ibaadah Ndani Yake
Alhidaaya.com [3]
1- Toka kwa Abiy Bakrah (Radhwiya Allaahu Anhu) toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((شهران لا ينقصان، شهرا عيد: رمضان وذو الحجة))
((Miezi miwili haipungui, miezi miwili ya ‘Iyd: Ramadhwaan na Dhul Hijjah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1912) na Muslim (1089)]
Hadiyth hii inafidisha kuwa Ramadhwaan na Dhul Hijjah iko sawa katika fadhwiylah, na kwamba yote yaliyogusiwa kuhusu fadhwaail za miezi hii miwili, malipo yake na thawabu zake, yanapatikana kwa ukamilifu wake hata kama mwezi ni siku 29. [Fat-hul Baariy (4/150), Al-Majmuw’u (6/253) na Swahiyh Ibn Hibaan (8/218)]
2- Toka kwa Abu Hurayrah kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((إذا دخل شهر رمضان فتحت أبواب السماء، وغلقت أبواب جهنم، وسلسلت الشياطين))
((Unapoingia Mwezi wa Ramadhwaan milango ya mbingu hufunguliwa ikawa wazi, milango ya Jahannamu hufungwa ikakomewa, na Mashaytwaan hufungwa minyororo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1899) na Muslim (1079)]
3- Na toka tena kwa Abu Hurayrah kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((من صام رمضان إيمانا واحتسابا، غقر له ما تقدم من ذنبه))
((Atakayefunga Ramadhwaan kwa iymaan na kutarajia malipo [toka kwa Allaah], hughufiriwa dhambi zake zilizotangulia)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (38), na (4/157) na Ibn Maajah (1641)]
Abu Haatim bin Hibaan amesema: "إيمانا" kwa kuamini ufaradhi wake, na "احتسابا" kwa kutakasia niya.
4- Na toka kwa huyo huyo Abu Hurayrah kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((الصلوات الخمس، والجمعة إلى الجمعة، ورمضان إلى رمضان، مكفرات لما بينهن إذا اجتنبت الكبائر))
((Swalaah Tano, na Ijumaa hadi Ijumaa, na Ramadhwaan hadi Ramadhwaan, ni zenye kufuta yaliyo baina yao ikiwa madhambi makubwa yataepukwa)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (233)]
5- Ndani yake yapo Masiku Kumi ya Mwisho na Laylatul Qadr. Tutazielezea fadhiylah zake na kufanya ‘ibaadah ndani yake.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
06-Ni Kwa Jambo Gani Kunakuwa Wajibu Kufunga Ramadhwaan?
Alhidaaya.com [3]
Ni waajib kufunga Ramadhwaan kwa kuthibiti mwezi, nao huthibiti kwa moja ya mawili:
1- Kuona Mwezi Mwandamo Wa Ramadhwaan
Allaah Ta’aalaa Anasema:
((فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ))
((Basi atakayeshuhudia miongoni mwenu mwezi, na aufunge)). [Al-Baqarah (2:185)]
Na toka kwa Ibn ‘Umar kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((إذا رأيتموه فصوموا، وإذا رأيتموه فأفطروا، فإن غم عليكم فاقدروا له))
((Mkiuona basi fungeni, na mkiuona basi fungueni. Na kama mawingu yatawakingeni, basi ukadirieni [kutimia siku 30])). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1900) na Muslim (1080)]
Na toka kwa Ibn ‘Umar pia kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((الشهر تسع وعشرون ليلة، فلا تصوموا حتى تروه، فإن غم عليكم فأكملوا العدة ثلاثين))
((Mwezi ni masiku 29, basi msifunge mpaka muuone. Na kama mawingu yatawakingeni, basi kamilisheni hisabu thalathini)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1907)]
Kuthibitisha Mwezi Mwandamo (Mbalamwezi) ni kwa kuuona na si kwa hisabu [za kifalaki]
Njia ya kuthibitisha Mwezi Mwandamo ni kwa kuuona na si kwa njia nyingine, na haiswihi kuainisha mahala pa kuonekana kwake kwa hesabu (za kifalaki). Sisi tunajua kwa njia ya lazima kupitia Diyn yetu ya Uislamu kuwa kuangalia ndiko kunakotumika kuutafuta Mwezi Mwandamo wa Swawm ya Ramadhwaan na Mwezi wa Hajji (Dhul Hijjah), na pia kwa eda, au kiapo cha kutomwingilia mke, au ahkaam nyinginezo zenye mafungamano na mwezi, na haijuzu kwa habari ya hesabu za mtaalamu wa falaki. Zipo Hadiyth lukuki za Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) zinazogusia hili. Kati yake ni neno lake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((إنا أمة أمية لا نكتب ولا نحسب، الشهر هكذا وهكذا))
((Sisi ni umma usio jua kusoma na kuandika, hatuandiki wala hatuhesabu. Mwezi ni hivi na hivi)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1913), Muslim (1080) na wengineo]
Yaani, mara unakuwa siku 29 na mara nyingine unakuwa siku 30. Waislamu wote wamekubaliana juu ya hilo. Hakuna asilani makhitalifiano ya kale wala ya sasa yanayojulikana kuhusiana na jambo hili. Isipokuwa hivi leo, baada ya kupita miaka 300 ya utulivu wa makubaliano hayo, wamedhihiri wanaojinasibisha na taaluma ya Fiqh ambao wamejuzisha kutumia hesabu za kifalaki. Ni jambo la ajabu ambalo limeshatanguliwa na Ijma’a inayopingana nalo. [Angalia Majmuw’u Al-Fataawaa (25/113, 132, 146), Haashiyatu Ibn ‘Aabidiyna (2/393), Al-Majmuw’u (6/279) na Bidaayatul Mujtahid (1/423)]
Kuona Mwezi Mwandamo wa Ramadhwaan kunathibiti kwa ushahidi wa mtu mwadilifu aliyeuona
Anapouona mtu mmoja mwadilifu anayeaminiwa Mwezi Mwandamo wa Ramadhwaan, basi taarifa yake itakubaliwa na itafanyiwa kazi kwa mujibu wa ‘Ulamaa wengi kama Abu Haniyfah, Ash-Shaafi’iy, Ahmad na Ahlu Adh-Dhwaahir. Ibn Al-Mundhir ameukhitari msimamo huu.
Ama Maalik, Al-Layth, Al-Awzaa’iy, Ath-Thawriy na Ash-Shaafi’iy katika kauli yake nyingine, wameshurutisha wauone watu wawili waadilifu wakilifananisha hilo na utoaji ushahidi (ambao unahitaji mashahidi wawili).
Kauli ya kwanza (ya kutosha kuuona mtu mmoja) ndiyo yenye nguvu zaidi, kwa kuwa kumfananisha mwenye kuuona na msimulizi wa Hadiyth ni sawa zaidi kuliko kumfananisha na mtoa ushahidi. Katika sharia inajuzu kukubali habari ya mtu mmoja, kisha inashadidia zaidi kwenye mali na haki za watu kinyume na inavyoshadidia katika habari za kidini.
Kutosheka na taarifa ya mtu mmoja kunatolewa dalili na Hadiyth ya Ibn ‘Umar aliyesema: ((Watu walikusanyika kuangalia Mwezi Mwandamo, nami nikauona. Nikampa taarifa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), akafunga (siku ya pili) na akaamuru watu waufunge)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2342) Ad-Daaramiy (2/4) na Ibn Hibaan (3447). Angalia Al-Irwaa (908)]
Taarifa kuhusu hili inakubaliwa kwa ngazi sawa toka kwa mwanamume au mwanamke katika kauli mbili sahihi za ‘Ulamaa. [Ni madhehebu ya Mahanbali kama ilivyo katika Sharhu Al-Muntahaa (1/440) na Ibn Hazm katika Al-Muhallaa (6/350)]
Ama Mwezi Mwandamo Wa Shawwaal
Fuqahaa wameitafikiana kuwa ushahidi wa mtu mmoja hautoshi katika kuthibitisha Mwezi Mwandamo wa Shawwaal, bali unaokubaliwa ni ushahidi wa watu wawili waadilifu. Ash-Shawkaaniy ameliunga hili mkono, na Ibn Rushdiy anaonyesha kama anaegemea huko. Lakini Abu Thawr na Ibn Hazm wamelikhalifu hilo wakisema kuwa ushahidi wa mtu mmoja unatosha, kwa kuwa ushahidi ni ule ule wa sehemu mbili za Mwezi wa Ramadhwaan, mwanzo wake wa kuingia na kutoka kwake.
Ninasema: “Hoja ya Jumhuri ni Hadiyth ya ‘Abdul Rahmaan bin Zayd bin Al-Khattwaab ya kuwa Swahaba wa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) walimweleza kuwa (Rasuli) kasema:
((صوموا لرؤيته، وأفطروا لرؤيته، وانسكوا لها، فإن غم عليكم فأكملوا ثلاثين، فإن شهد شاهدان فصوموا وأفطروا))
((Fungeni kwa kuuona, na fungueni kwa kuuona, na jikurubisheni kwao [kwa Allaah kwa Swiyaam], na kama mawingu yatawakinga msiuone, basi kamilisheni thelathini. Na kama watashuhudia mashahidi wawili, basi fungeni na fungueni)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na An-Nasaaiy (1/300), na Ahmad (4/321). Angalia Al-Irwaa (909)]
Hadiyth hii inadulisha kutokujuzu ushahidi wa mtu mmoja katika kufunga na kufungua. Hivyo funga (kwa ushuhuda wa mtu mmoja) kwa mujibu wa Hadiyth ya Ibn ‘Umar iliyotangulia, inatoka nje (ya duara la kujuzu). Kisha kunabakia kufungua (kumalizika mfungo) ambapo hakuna dalili ya kujuzu kwa ushuhuda wa mtu mmoja. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi.
Atakayeuona Mwezi Mwandamo peke yake
[Al-Badaai’u (2/80), Al-Mudawwanah (1/193), Al-Mubdi’u (3/10), Al-Majmuw’u (6/280), Al-Muhallaa (6/350) na Majmuw’u Al-Fataawaa (25/114)]
Atakayeuona Mwezi Mwandamo peke yake na taarifa yake ikakataliwa, basi ‘Ulamaa wana kauli tatu kuhusiana na kufunga kwake na kufungua kwake kwa mujibu wa kuona kwake mwezi.
Ya kwanza: Atafunga akiuona Mwezi Mwandamo wa Ramadhwaan, na atafungua kwa siri kwa Mwezi Mwandamo wa Shawwaal ili asikhalifiane na Jamaa. Hii ni kauli ya Ash-Shaafi’iy, riwaya toka kwa Ahmad, na madhehebu ya Ibn Hazm. Ni kwa Neno Lake Ta’aalaa:
((فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ))
((Basi atakayeshuhudia miongoni mwenu mwezi, na aufunge)). [Al-Baqarah (2:185)]
Ya pili: Atafunga kwa yeye kuuona, lakini hatofungua isipokuwa pamoja na watu. Ni madhehebu ya Abu Haniyfah, Maalik na mashuhuri toka kwa Ahmad.
Ya tatu: Hatofanya lolote kwa kuuona, bali atafunga pamoja na watu na atafungua pamoja nao. Ni riwaya toka kwa Ahmad na limekhitariwa hili na Sheikh wa Uislamu. Ni kutokana na neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((صومكم يوم تصومون، وفطركم يوم تفطرون، وأضحاكم يوم تضحون))
((Swawm yenu ni siku mnafunga, na kufungua kwenu ni siku mnafungua, na Adhwhaa yenu ni siku mnachinja)). [Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2324) na wengineo. Angalia Al-Irwaa (905)]
Maana ya Hadiyth ni kuwa kufunga na kufungua kunakuwa pamoja na Jamaa.
Ninasema: “Lenye nguvu ni kuwa atafunga na kufungua kwa siri kwa mujibu wa yeye alivyouona mwezi kama atapishana na watu. Muhimu Swawm yake isizidi siku 30. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi.”
2- Kukamilika Hisabu Ya Sha’abaan Siku Thelathini
Kwa kuwa Mwezi Mwandamo haupungui chini ya siku 29 na hauzidi zaidi ya siku 30. Na kama hawakuuona Mwezi Mwandamo usiku wa kuamkia thelathini ya Sha’abaan –anga ikiwa safi bila mawingu au kizuizi chochote cha kuzuia kuona-, basi watakamilisha Sha’abaan siku thelathini na wataamka bila kufunga, ima kwa njia ya waajib au kwa njia ya Sunnah kama tutakavyokuja kufafanua kuhusu kufunga siku ya shaka.
Mawingu Au Mfano Wake Yakifunga Watu Wasiweze Kuuona Mwezi Mwandamo Usiku Wa Kuamkia Thalathini Ya Sha’abaan
Katika suala hili, ‘Ulamaa wana kauli nyingi. Zilizo mashuhuri zaidi ni nne: [Al-Badaai’i (2/78), Al-Khurshiy (2/238), Al-Majmuw’u (6/269), Al-Inswaaf (2/269), Majmuw’u Al-Fataawaa (25/124) na Zaadul Ma’aadi (2/46-49)]
Ya kwanza: Haijuzu kuifunga, si kwa njia ya Waajib wala kwa njia ya Sunnah.
Ni madhehebu ya Jumhuri ya ‘Ulamaa na riwaya toka kwa Ahmad. Dalili yao ni:
1- Hadiyth ya Ibn ‘Umar kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((الشهر تسع وعشرون ليلة، فلا تصوموا حتى تروه، فإن غم عليكم فأكملوا العدة ثلاثين))
((Mwezi ni masiku 29, hivyo msifunge mpaka muuone, na kama mawingu yatawatatizeni, basi kamilisheni hisabu thalathini)). [Hadiyth Swahiyh. Imetajwa nyuma kidogo]
2- Hadiyth ya Abu Hurayrah ya kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((لا يتقدمن أحدكم رمضان بصوم يوم أو يومين، إلا أن يكون رجل كان يصوم صومه، فليصم ذلك اليوم))
((Asiitangulie kamwe mmoja wenu Ramadhwaan kwa kufunga siku moja au siku mbili, isipokuwa awe mtu alikuwa anafunga Swawm yake, basi na aifunge siku hiyo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1914) na Muslim (1082)]
3- Hadiyth ya ‘Ammaar bin Yaasir amesema:
((من صام اليوم الذي شك فيه فقد عصى ابا القاسم صلى الله عليه وسلم))
((Mwenye kufunga siku ambayo amefanya shaka ndani yake, basi hakika amemwasi Abal Qaasim (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2317), At-Tirmidhiy (681), An-Nasaaiy (4/153) na Ibn Maajah (1645). Angalia Al-Irwaa (961)]
4- Ni kuwa kufunga siku hii kwa njia ya hadhari ya kiakiba ni ushadidiaji, uchupaji mipaka na uzushi katika diyn. Kwa kuwa hadhari inakuwa kwa jambo ambalo asili yake ni waajib. Ama lile ambalo asili yake si waajib, basi hakuna hadhari ya kiakiba katika kuliwajibisha, na Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam ashasema:
((هلك المتنطعون))
((Wameangamia washadidiaji wachupao mipaka)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (2670) na Abu Daawuwd (4608) toka Hadiyth ya Ibn Mas’ uwd]
Ya pili: Ni lazima kuifunga kwa msingi wa kuwa ni sehemu ya Ramadhwaan
Kauli hii ni mashuhuri katika madhehebu ya Hanbali. Pia ni kauli iliyosemwa na kundi katika Swahaba akiwemo ‘Aliy, ‘Aaishah na Ibn ‘Umar pamoja na kundi la Masalaf. Dalili yao ni:
1- Kuwa Ibn ‘Umar (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) alikuwa unapokuwa usiku wa kuamkia thalathini ya Sha’abaan na mawingu yakazuia kuona au mvua, anaamka akiwa amefunga)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2320) na Ahmad (2/5). Angalia Al-Irwaa (904)]
Wamesema: “ Na Ibn ‘Umar ndiye msimulizi wa Hadiyth:
((فإن غم عليكم...))
Hivyo kitendo chake ni tafsiyr ya Hadiyth”.
2- Kuwa kauli ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((فإن غم عليكم فاقدروا له))
.. maana yake ni (ضيقوا له) , yaani ubaneni, na kuibana idadi ni kwa kufanywa Sha’abaan siku ishirini na tisa.
3- Kuwa maana ya neno lake:
((فإن غم عليكم فاقدروا له))
((Na kama mawingu yatawakingeni, basi ukadirieni [kutimia siku 30]))..ni kama anga litakuwa safi bila mawingu wala vumbi. Ama katika hali ya kutanda mawingu, hapo hukmu inakuwa nyingine.
4- Kuwa Mwezi Mwandamo inawezekana ukawa umetoka lakini umezuiwa na mawingu, hivyo anafunga kiakiba.
Ya tatu: Ni kuwa watu wanamfuata Imamu (Kiongozi), akifunga nao watafunga, na asipofunga watakula
Ni riwaya toka kwa Ahmad kutokana na neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((الفطر يوم يفطر الناس، والأضحى يوم يضحي الناس))
((Kufungua [‘Iyd El Fitwr] ni siku watu wote wanafungua, na [Siku ya ‘Iyd] Adhwhaa ni siku watu wanachinja)). [Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh. Imetajwa nyuma kidogo]
Ninasema: “Kauli ya Jumhuri ya ‘Ulamaa ya kuzuia kufunga ina nguvu zaidi kutokana na dalili zilizotangulia. Ama kitendo cha Ibn ‘Umar, hakuna ndani yake kinachodulisha kuwa yeye alikuwa akiitakidi uwajibu wake mpaka hili lizingatiwe kuwa ni lenye kufasiri yale aliyoyasimulia. Na linalodulisha hilo ni kuwa lau kama lingekuwa ni waajib, basi angeliwaamuru watu kulitenda japokuwa mkewe na wanawe. Upeo wa tunaloweza kusema kuhusu hili ni kuwa yeye alifunga kwa njia ya Sunnah au kwa njia ya kiakiba. Na hii ndio kauli ya nne, nayo ndiyo ambayo Ibn Taymiyah na Ibn Al-Qayyim wameichagua. Ukiongezea na hayo, imethibiti kupokewa kauli ya Ibn ‘Umar akisema: ”Lau ningelifunga mwaka mzima, basi ningelikula siku ambayo inafanyiwa shaka.” [Isnaad Yake ni Swahiyh. Ameinukulu Ibn Al-Qayyim katika Az Zaad (2/49) toka kwa Hanbal katika Masaail yake kwa Sanad Swahiyh]
Ninasema: “Kisha kitendo hiki cha Ibn ‘Umar kinakhalifiana na kitendo cha Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) ambaye ‘Aaishah amemsimulia aliposema:
((كان رسول الله صلى الله عليه وسلم يتحفظ عن شعبان ولا يتحفظ من غيره، ثم يصوم لرؤية رمضان، فإن غم عليه عد ثلاثين يوما ثم صام))
((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa akiuchunga sana [Mwezi wa] Sha’abaan [kwa kuhifadhi na kuyahesabu masiku yake] na hachungi sana miezi mingineyo, kisha anafunga kwa kuonekana Ramadhwaan. Na kama mawingu yatamtinga, huhesabu siku thelathini, kisha hufunga)). [Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2325), Ahmad (6/149) na Al-Bayhaqiy (4/206) na Sanad Yake ni Muqaarib]
Ikibainika katika siku ya shaka kuwa ni Ramadhwaan
Ni kama kuwa yule ambaye ameuona Mwezi Mwandamo hakufika kwa Kadhi (kutoa taarifa) isipokuwa mchana, au watu wakauona mwezi mchana –kabla jua halijapinduka- na mfano wa hivi.
1- Awe mtu amefunga siku ya shaka kwa niya ya kuwa ni siku ya Ramadhwaan –kama yalivyo madhehebu ya Hanbal-, huyu swawm yake hiyo itamtosheleza bila makhitilafiano yoyote.
2- Awe amefunga siku hii kwa niya ya Sunnah au kwa niya ya kutofungamana na upande wowote. Hapa Jumhuri wanasema kuwa Swawm yake hiyo haimtoshelezi, kwa kuwa ni lazima aainishe niya na aitakidi kuwa anafunga Ramadhwaan. [Al-Khurashiy (2/238), Al-Majmuw’u (6/270), Ar-Rawdhwah (2/353) na Al-Mughniy (3/27)]
Abu Haniyfah amesema inamtosheleza –kwa mujibu wa asili yake ya kutoshurutisha niya katika kufunga Ramadhwaan- Na kutosheleza ni riwaya toka kwa Ahmad, nalo ni chaguo la Sheikh wa Uislamu. [Al-Mabsuwtw (3/60) na Al-Mughniy (3/27)]
Ninasema: “Kauli ya kwanza ina nguvu zaidi kwa upande wa dalili”.
3- Aamke akiwa na niya ya kula, kisha wakati wa mchana –kabla hajala au kunywa chochote- apate habari yakini kuwa Ramadhwaan ishaingia. Hapa Ash-Shaafi’iy amesema: Atakamilisha Swawm yake, lakini lazima ailipe, kwa kuwa hakutia niya usiku. [Fat-hul Maalik Fiy Tartiyb At-Tamhiyd cha Ibn ‘Abdul Barri (5/97).
Abu Haniyfah kasema inamtosheleza.
4- Aamke akiwa si mwenye kufunga (mlaji), kisha wakati wa mchana apate habari yakini kuwa Ramadhwaan ishaingia baada ya kuwa amekula na kunywa. Huyu ni wajibu kwake ajizuie kula na kunywa mchana wake wote uliosalia bila makhitilafiano yoyote. Na hii ni kutokana na Hadiyth ya Salamah bin Al-Akwa’a aliyesema: ((Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwamuru mtu mmoja aliyesilimu awatangazie watu aseme: “Aliyekula, basi na afunge siku yake iliyobakia, na ambaye hakuwa amekula, basi na afunge, kwani leo ni Siku ya ‘Aashuwraa)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2007) na Muslim (1129)].
Siku hii ilikuwa ni waajib wakati huo. Kisha ni waajib juu yake ailipe siku hii kwa kuwa hakutia niya usiku. Haya ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na Hanbali. [Al-Ummu (2/95), na Al-Kaafiy cha Ibn Qudaamah (1/350)]
Lakini Sheikh wa Uislamu Ibn Taymiyah amesema kuwa haimlazimu kuilipa, kwa kuwa kulipa kunahitajia dalili –na hususan pamoja na kutokuwepo uzembe. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/110), Ash-Sharhu Al-Mumti’u (6/342) na Al-Ikhtiyaaraat (uk. 107)]
Ama kutokunuwia, amejibu akisema kuwa niya inaambatana na kulijua jambo, na kwamba Allaah Hamkalifishi mtu kulinuwia jambo ambalo hakulijua, na kulijua jambo hakujatokea isipokuwa wakati wa mchana. Huu ni mwelekeo murua kabisa, lakini la akiba zaidi ni kuilipa. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Ikiwa Mwezi Mwandamo umeonekana nchi fulani, je ni lazima nchi nyinginezo zifuate?
‘Ulamaa wana kauli tatu katika suala hili:
Ya kwanza: Watu wa nchi fulani wakiuouna mwezi, ni lazima nchi nyinginezo nazo zifunge bila kuangalia tofauti ya mionekano ya mwezi.
Kauli hii ndiyo inayotegemewa kwa Mahanafiy, ni madhehebu ya Maalik na baadhi ya ‘Ulamaa wa Shaafi’iy, na ni mashuhuri kwa Mahanbali. [Haashiyatu Ibn ‘Aabidiyna (2/393), Ash-Sharhul Kabiyr (1/510), Al-Majmuw’u (6/273) na Al-Inswaaf (3/273)]
Wamesema:
- Kwa kuwa ni Waislamu wote wanaosemeshwa katika neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((إذا رأيتموه فصوموا))
((Mnapouona, basi ufungeni)).
- Hili li karibu zaidi katika kuungana Waislamu na kuwa wamoja katika neno lao, na pia kutokana na wepesi wa mawasiliano kati ya pande zote za dunia katika wakati wetu wa sasa kwa njia ya satelaiti.
Ya pili: Kila nchi – iliyo chini ya mamlaka moja- ina mwezi wake
Kauli hii imenukuliwa na Ibn Al-Mundhir toka kwa‘Ikrimah, Al-Qaasim, Saalim na Is-Haaq. [Al-Mughniy (3/289) na Al-Majmuw’u (6/274)]
Dalili yao ni:
- Hadiyth ya Kurayb – mwachwa huru wa Ibn ‘Abbaas- aliyesema: ((Niliwasili Sham, na Mwezi Mwandamo wa Ramadhwaan ukanidhihirikia nami niko Sham, tukauona Mwezi Mwandamo usiku wa kuamkia Ijumaa. Kisha nikawasili Madiynah mwishoni mwa mwezi, na Ibn ‘Abbaas akaniuliza. Kisha akaukumbuka Mwezi Mwandamo akauliza: Lini muliuona Mwezi Mwandamo? Nikasema: Tuliuona usiku wa kuamkia Ijumaa. Akasema: Wewe uliuona usiku wa kuamkia Ijumaa? Nikasema: Na’am, na watu waliuona, wakafunga, na akafunga Mu’aawiyah. Akasema: Lakini sisi tuliuona usiku wa kuamkia Jumamosi, na bado tunaendelea na Swiyaam mpaka tukamilishe thelathini au tuuone. Nikauliza: Je hutosheki kwa kuuona Mu’aawiyah na kufunga kwake? Akasema: Hapana, hivi ndivyo alivyotuamuru Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1087), Abu Daawuwd (2332), An-Nasaaiy (4/131) na At-Tirmidhiy (693)]
- Kauli Yake Ta’aalaa:
((فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ))
((Basi atakayeshuhudia miongoni mwenu mwezi, na aufunge)). [Al-Baqarah (2:185)]
Mafhumu yake ni kuwa ambaye hakuuona hafungi mpaka auone, au akamilishe hesabu ya Sha’abaan.
Ya tatu: Ni lazima zifunge nchi ambazo hazitofautiani mwonekano wa mwezi
Huu ni mwelekeo sahihi zaidi kwa Mashaafi’iy, ni madhehebu ya baadhi ya ‘Ulamaa wa Kimaalik na Kihanafiy, na ni chaguo la Sheikh wa Uislamu. [Al-Qawaaniynu Al-Fiqhiyyah (103) na vitabu rejea vilivyotangulia]
Na hii ndio kauli ya kati na kati (wastani) katika suala hili, kwani miandamo ya mwezi inatofautiana kwa makubaliano ya wataalamu. Na kama miandamo itakuwa sawa kote, basi ni lazima kufunga, na kama inatofautiana, basi si lazima.
Ama kauli ya kwanza ya kutozingatia tofauti ya miandamo, kauli hii inakwenda kinyume na lile ambalo limethibiti kiulazima la kutofautiana nyakati. Kwa maana kuwa, ikiwa jua limekuchwa mashariki, basi watu wa magharibi hawawezi kufungua kwa makubaliano ya wote.
Ama Hadiyth ya Kurayb, Hadiyth hii inadulisha kuwa wao hawafungui kutokana na kauli ya Kurayb peke yake, -nasi tunaisema- bali mvutano ni kuhusiana na uwajibu wa kuilipa siku ya kwanza, na hili haliko katika Hadiyth. [Al-Mughniy (3/289). Angalia Naylul Awtwaar (4/231)]
Kisha hilo halipindukii zaidi ya kuwa ni ufahamu wa Ibn ‘Abbaas wa agizo la Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) la kufunga na kufungua kwa kuuona Mwezi Mwandamo. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
07-Shuruti Za Kuswihi Swiyaam
Alhidaaya.com [3]
Ili Swiyaam iswihi, lazima yawepo mambo mawili:
1- Kutwaharika na hedhi na nifasi
Hili ni sharti la wajibu wa kutenda na kuswihi kwa pamoja. [Fat-hul Qadiyr (2/234) na Haashiyatu Ad-Dusuwqiy (1/509)]. Tutakuja kulizungumzia hili muda si mrefu.
2- Niya
Swawm ya Ramadhwaan ni ‘ibaadah, hivyo haiswihi isipokuwa kwa niya kama ‘ibaadah nyinginezo. Allaah Ta’aalaa Anasema:
((وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّـهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ حُنَفَاءَ))
((Na hawakuamrishwa isipokuwa wamwabudu Allaah wenye kumtakasia Dini, wenye kujiengua na upotofu kuelemea Dini ya haki)). [Al-Bayyinah (98:5)]
Na Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((إنما الأعمال بالنيات))
((Hakika si jinginelo, matendo ni kwa niya)). [Hadiyth Swahiyh. Imetajwa sehemu nyingi nyuma]
Na kwa vile kujizuia kunaweza kuwa kwa sababu ya mazoea, au kukosa hamu ya kula, au ugonjwa, au mazoezi au mengineyo, hivyo hakuwajibiki ila kwa niya. An-Nawawiy amesema: “Swawm haiswihi ila kwa niya, na mahala pake ni moyoni”. [Rawdhwat At Twaalibiyn (2/350)]
Ili Niya Itosheleze Ni Lazima Iwe Na Masharti Manne
(a) Kukata shauri na kudhamiria kikweli: Kunashurutishwa ili kuondosha kabisa mbabaiko, hata lau akinuwia usiku wa shaka kufunga kesho, na kesho ikawa Ramadhwaan, basi haitomtosheleza. [Kwa kuwa ni niya ya nusu nusu]
(b) Kuainisha: Ni lazima kuainisha niya katika Swawm ya Ramadhwaan, au Swawm ya Faradhi au Swawm ya Wajibu. Haitoshi uainisho wa Swawm bila jina, wala uainisho wa Swawm fulani isiyo Ramadhwaan kwa mujibu wa Jumhuri kinyume na Abu Haniyfah. [Al-Hidaayat (2/248), Ar-Rawdhwah (2/353) na Kash-Shaaful Qinaa (2/315)]
(c) Kuilaza niya: Nako ni kuitia niya usiku, na wakati wake ni kati ya jua kuchwa hadi kuchomoza Alfajiri. Sharti hili ni la madhehebu ya Maalik, Shaafi’iy na Hanbal. Ni kwa Hadiyth ya Ibn ‘Umar toka kwa Hafswah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((من لم يجمع الصيام قبل الفجر، فلا صيام له))
((Ambaye hakunuwia na kuazimia Swiyaam kabla ya Alfajiri, basi hana Swiyaam)). [Imetiwa kasoro kwa Waqf. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2454), At-Tirmidhiy (730), An-Nasaaiy (4/196) na Ibn Maajah (1700) kwa Sanad Swahiyh, lakini imetiwa doa kwa Waqf. Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh katika Swahiyhul Jaami’i (6538)]
Je, ni lazima kutia niya usiku kwa Swiyaam ya Sunnah?
Tumeshaitaja Hadiyth isemayo:
((من لم يجمع الصيام قبل الفجر، فلا صيام له))
((Ambaye hakunuwia na kuazimia Swiyaam kabla ya Alfajiri, basi hana Swiyaam)).
Na imepokelewa toka kwa ‘Aaishah akisema: ((Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliingia kwangu siku moja akauliza: ((Je, mna chochote?)) Tukasema: Hapana. Akasema: ((Basi kwa hivyo mimi nafunga)). Kisha akatujia siku nyingine tukamwambia: Ëe Rasuli wa Allaah! Tumeletewa zawadi ya “hays” [Chakula cha mchanganyo wa samli na tende]. Akasema: Nionyeshe. Hakika niliamka nikiwa nimefunga)) Akaila. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1451)]
‘Ulamaa wamekhitalifiana kuhusu kutia niya usiku katika Swiyaam ya Sunnah kutokana na Hadiyth hizi mbili. Jumhuri wamepita njia ya kukusanya, wakaichukulia Hadiyth ya Hafswa kuwa inahusiana na Swiyaam ya Faradhi, na Hadiyth ya ‘Aaishah kuwa inahusiana na Swiyaam ya Sunnah. Na niyah ya Swawm ya Sunnah ni kuanzia mchana kabla jua halijapinduka, na wengine wamesema hata baada ya jua kupinduka. Sheikh wa Uislamu amesema baada ya Hadiyth ya ‘Aaishah: “Na hii inadulisha kwamba yeye (Rasuli) aliizindua Swawm mchana, kwa kuwa alisema: فإني صائم ((Basi kwa hivyo mimi nafunga)), na الفاء hii inadulisha sababu, na maana inakuwa: Mimi nafunga kwa sababu hakuna chochote kwenu. Na inajulikana kuwa lau angenuwia na kuazimia Swawm tokea usiku, basi Swawm yake isingelikuwa kwa sababu hii. Vile vile, neno lake: فإني إذن لصائم ((Basi kwa ajili hiyo nafunga)), na إذن ni bayana zaidi kuelezea sababu kuliko الفاء “ [Sharhu Al-‘Umdah (1/86)]
Wametilia vigezo utoaji dalili wao kwa kusema kuwa hili ndilo walilolifahamu Swahaba (Radhwiya Allaahu ‘anhum) kutokana na kitendo cha Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam). Kwani imethibiti uzindushi wa niya ya Swawm ya Sunnah kuanzia mchana toka kwa Ibn Mas’uwd, Ibn ‘Abbaas, Abu Ayyuwb, Abu Ad-Dardaai, Hudhayfah na Abu Twalha (Radhwiya Allaahu ‘anhum).
Kadhalika, wametolea dalili agizo la Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kwa watu la kufunga Siku ya ‘Aashuwraa. Ilikuwa imefaradhishwa kabla ya Fardhi ya Ramadhwaan.
((من أكل فليصم بقية يومه، ومن لم يكن أكل فليصم))
((Aliyekula, basi na afunge siku yake iliyobakia, na ambaye hakuwa amekula, basi na afunge)). [Hadiyth Swahiyh. Imetajwa nyuma kidogo]
Maalik, Al-Layth, na Ibn Hazm ambaye Ash-Shawkaaniy ameungana naye, hawa wameshika msimamo wa kulalia penye uzito zaidi (At-Tarjiyh), wakaichukua Hadiyth ya Hafswah. Hawakufarikisha kati ya Swawm ya Sunnah wala Faradhi katika kushurutisha kutia niya usiku. Wakasema: “Neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) – katika Hadiyth ya Hafswah- ((لا صيام)) siainishi, na ni kanushi, hivyo linazihusu Swiyaam zote, na haitoki humo isipokuwa ile ambayo imethibiti kwa dalili kuwa haishurutishwi kutiliwa niya usiku. [Naylul Awtwaar 4/233]
Wamejibu kuhusu Hadiyth ya ‘Aaishah kuwa hakuna ndani yake linalogusia kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) hakuwa amenuwiya kufunga kuanzia usiku, wala kuwa aliamka asubuhi akiwa hakufunga, kisha akanuwia kufunga baada ya hapo. Lakini linaloelezwa ni kuwa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa akiamka na Swiyaam ya Sunnah, kisha anafungua, na hili linaruhusika. Hivyo yamkinika alinuwiya tokea usiku na akataka kufungua. Na hilo linadulishwa na neno lake katika Hadiyth ya ‘Aaishah: ((فلقد أصبحت صائما)). Na haijuzu kuacha la yakini katika Hadiyth ya Hafswah kwa la dhana imkinikayo katika Hadiyth ya ‘Aaishah. [Al-Muhallaa (6/72)]
Na wamejibu kuhusu Hadiyth ya ‘Aashuwraa ya kuwa niya bila shaka imeswihi katika mchana wa ‘Aashuwraa kwa kuwa kurejea usiku hakuwezekaniki tena, na mvutano ni kwa linalowezekanika likakhusu kujuzu katika picha kama hii.
Ninasema: “Kila dhehebu katika mawili linabebwa na dalili, na kushurutisha kutia niya usiku katika Swiyaam ya Sunnah ni jambo la akiba zaidi. Allaah Ndiye Mjuzi zaidi”.
(d) Kujadidisha niya kila usiku wa Ramadhwaan
Ni lazima kutia niya ya kufunga kila usiku katika nyusiku za Ramadhwaan –kwa mujibu wa Jumhuri ya ‘Ulamaa- kutokana na ujumuishi wa Hadiyth ya Hafswah iliyotangulia, na kwa kuwa kila siku ni ‘ibaadah kando, na siku hizi hazifungamani zenyewe kwa zenyewe na haziharibiki kwa kuharibika baadhi yake, nazo zinaingiliwa na yanayokwenda kinyume nayo, nazo ni nyusiku ambazo yanaruhusika ndani yake yaliyoharamishwa mchana.
[Raddu Al-Muhtaar (2/87), Al-Majmuw’u (6/302) na Kash-Shaaful Qinaa (2/315)]
Ama Zafr na Maalik –nayo ni riwaya toka kwa Ahmad- wao wanaona kwamba niya moja inatosheleza kwa mwezi wote mwanzoni mwake kama Swalaah, na pia katika kila Swawm ya kufunga siku mfululizo kama kafara ya Swawm na Dhwihaar. [Al-Qawaaniynu Al-Fiqhiyyah (uk. 80) na Ash-Sharhul Kabiyr (1/521)]
Ninasema: “Kauli ya kwanza (ya kutia niya kila usiku) ndio yenye nguvu zaidi kutokana na ujumuishi wa Hadiyth. Ibn ‘Abdul Hakam –ambaye ni katika ‘Ulamaa wa Maalik-amepondokea kwenye usawa na kukubaliana na madhehebu ya Jumhuri ya ‘Ulamaa”.
Faida
Niya inafanyika kwa picha iliyotangulia kwa kuamka saa za mwisho wa usiku na kula na kunywa katika wakati huo na hususan kwa yule ambaye si ada yake kufanya hivyo katika masiku yasiyo ya Ramadhwaan. Kwa kuwa niya ni kukikusudia kitu au kukitaka, na hili lishapatiwa makusudio yatakiwayo. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
08-Nguzo Ya Swiyaam
Alhidaaya.com [3]
Ni kujizuia na yenye kufunguza toka kuchomoza Alfajiri hadi Magharibi. Allaah Ta’aalaa Amesema:
((فَالْآنَ بَاشِرُوهُنَّ وَابْتَغُوا مَا كَتَبَ اللَّـهُ لَكُمْ ۚ وَكُلُوا وَاشْرَبُوا حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَكُمُ الْخَيْطُ الْأَبْيَضُ مِنَ الْخَيْطِ الْأَسْوَدِ مِنَ الْفَجْرِ ۖ ثُمَّ أَتِمُّوا الصِّيَامَ إِلَى اللَّيْلِ))
((Basi sasa waingilieni na tafuteni Aliyokuandikieni Allaah kwenu. Na kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu uzi mweupe (mapambazuko) wa Alfajiri kutokana na uzi mweusi (wa kiza cha usiku). Kisha timizeni Swiyaam mpaka usiku)). [Al-Baqarah (2:187)]
Allaah Ta’aalaa Ameruhusu idadi hii ya mambo yenye kufunguza usiku wa Swiyaam, kisha Akaamuru kujizuia nayo mchana wake. Hivyo basi, Ametutaarifu kuwa uhalisia wa Swawm na mhimili wake ni kujizuia. [Tuhfat Al-Fuqahaa (1/537)na Badaai’u As-Swanaai’ i (2/90)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
09-Sunnah Za Swawm Na Adabu Zake
Alhidaaya.com [3]
1- Kula daku
Toka kwa Anas bin Maalik (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((تسحروا، فإن في السحور بركة))
((Kuleni daku, kwani katika daku kuna barkah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1923) na Muslim (1095)]
Na toka kwa ‘Amri bin Al-‘Aaswiy amesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((فصل ما بين صيامنا وصيام أهل الكتاب أكلة السحور))
((Tofauti kati ya Swiyaam yetu na Swiyaam ya Ahlul Kitaab ni mlo wa daku)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1096), Abu Daawuwd (2343), At-Tirmidhiy (709) na An-Nasaaiy (4/46)]
Daku inakidhi lengo lake hata japo kwa funda la maji. Toka kwa ‘Abdullaah bin ‘Amri kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((تسحروا ولو بجرعة ماء))
((Kuleni daku japokuwa kwa funda la maji)). [Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na Ibn Hibaan (3476). Ina Hadiyth mwenza kwa Ahmad (3/12) na Abiy Ya’alaa (3340) toka kwa Anas]
Na lau tende italiwa kwa daku, basi ni bora zaidi. Ni kwa Hadiyth ya Abu Hurayrah kwamba Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((نعم سحور المؤمن التمر))
((Daku bora zaidi kwa Muumini ni tende)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2345) na Ibn Hibaan (3475). Ina Hadiyth wenza]
2- Kuchelewesha daku
Ni kwa Hadiyth ya Anas toka kwa Zayd bin Thaabit (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) amesema:
((Tulikula daku pamoja na Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), kisha akasimama kwenda kwenye Swalaah. Nikauliza: Ni muda gani kati ya adhana na daku? Akasema: ((Kiasi cha Aayah 50)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1921), Muslim (1097) na wengineo]
Toka kwa Unaysah bint Habiyb amesema: “Amesema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) :
((إذا أذن ابن أم مكتوم، فكلوا واشربوا، وإذا أذن بلال فلا تأكلوا ولا تشربوا. فإن كانت الواحدة منا ليبقى عليها الشيء من سحورها، فنقول لبلال: أمهل حتى أفرغ من سحوري))
((Akiadhini Ibn Ummi Maktuwm, basi kuleni na kunyweni. Na akiadhini Bilaal, basi msile wala msinywe)). “Na kama mmoja wetu imebaki sehemu ya daku yake hajaimaliza, tunamwambia Bilaal: Subiri kidogo mpaka nimalize daku yangu”. [Isnaad yake ni Swahiyh. An-Nasaaiy ameikhariji kwa tamko hili (2/10), Ahmad (6/433) na Ibn Hibaan (3474)]
Na kama mtu atasikia adhana ya Alfajiri nailhali chakula chake au kinywaji chake kiko mkononi, basi anaweza kumalizia tonge lake na kinywaji chake. Ni kwa Hadiyth ya Abu Hurayrah aliyesema: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((إِذَا سَمِعَ أَحَدُكُمُ النِّدَاءَ وَالْإِنَاءُ عَلَى يَدِهِ، فَلَا يَضَعْهُ حَتَّى يَقْضِيَ حَاجَتَهُ مِنْهُ))
((Akisikia mmoja wenu adhana, na chombo kiko mkononi mwake, basi asikitue mpaka amalize haja yake toka humo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2333) na Al-Haakim (1/426). Angalia Swahiyh Al-Jaami’i(607)]
3- Kuwahisha kufuturu
Toka kwa Sahl bin Sa’ad kwamba Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((لا يزال الناس بخير، ما عجلوا الفطر))
((Watu wataendelea kuwa kwenye kheri, madhali wanaharakia kufungua)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1957) na Muslim (1098)]
Na toka kwa ‘Abdullaah bin Abiy Awfaa amesema: ((Tulikuwa pamoja na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) katika safari –na yeye amefunga- na jua lilipokuchwa, aliwaambia baadhi ya watu: Ee fulani, simama utukorogee chakula. Akasema: Ee Rasuli wa Allaah! Ikiingia jioni. Akasema: Shuka, utukorogee chakula…(×3). Akateremka na kuwakorogea. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akanywa, kisha akasema:
((إذا رأيتم الليل قد أقبل من ها هنا فقد أفطر الصائم))
((Mkiuona usiku umeingia kutokea hapa, basi mfungaji ameshafungua)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1955) na Muslim (1101)]
4- Kufungulia kwa rutwab (tende laini) au tamr (tende kavu) -zikipatikana- au maji
Toka kwa Anas amesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa akifungulia kwa rutwab kabla ya kuswali, na kama si rutwab, basi kwa tamr, na kama hakupata, hunywa mafundo ya maji)). [Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2356) na At-Tirmidhiy (692). Angalia Al-Irwaa (822) na Asw-Swahiyha (2065)].
“Kwani kuupa mwili kitu tamu tumbo likiwa tupu, kunalifanya likipokee haraka zaidi na mwili unanufaika nacho vizuri zaidi na kupata nguvu. Ama maji, ini kutokana na Swawm, hupatwa na ukavu hivi, na linapopata unyevu kwa maji, basi hunufaika kikamilifu na chakula kinacholiwa halafu. Na kwa ajili hiyo, inakuwa ni vizuri zaidi kwa mwenye kiu na njaa, aanze kunywa maji kidogo kabla ya kula, kisha ale baada ya kunywa. Hii ukiongezea na faida mahususi zilizopo kwenye tamr na maji ambazo husaidia sana katika kuweka moyo wa mtu katika hali imara ya afya. Faida hizi hawazijui isipokuwa madaktari wa moyo”. [Zaadul Ma’aad (2/50 na 51]
5- Kuomba du’aa wakati wa kufungua kwa yafuatayo:
Toka kwa Ibn ‘Umar amesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anapofungua husema:
((ذهب الظمأ وابتلت العروق، وثبت الأجر إن شاء الله))
((Kiu kimeondoka, mishipa ya damu imelowana, na ajri imethibiti In Shaa Allaah)). [Al-Albaaniy kasema Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2357), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (10131-3329) na Ibn As-Sunniy (472). Angalia Al-Irwaa (920)]
6, 7- Utoaji kwa ukwasi, kuisoma Qur-aan na kuidurusu
Toka kwa Ibn ‘Abbaas amesema: ((Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa mkwasi zaidi wa watu kwa kheri. Alikuwa mwingi wa ukwasi zaidi katika Ramadhwaan wakati Jibriyl anapokutana naye. Jibriyl alikuwa anakutana naye kila usiku wa Ramadhwaan mpaka inamalizika, na Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) anamsomea Qur-aan. Na Jibriyl anapokutana naye, alikuwa mkwasi zaidi wa kheri kuliko upepo uvumao)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (6) na Muslim (2308)]
8- Kujiweka mbali na yenye kubomoa thawabu za Swiyaam kati ya maaswiya ya dhahiri na yasiyo dhahiri
Ni lazima mfungaji auchunge ulimi wake kutokana na maneno yasiyo na faida, kubwabwaja, kuongopa, kusengenya, kufitini, maneno machafu, maneno ya karaha, mizozano na mijadala. Na avizuie viungo vyake kutokana na aina zote za matamanio na maharamisho, kwani hii ndio siri halisi ya Swawm kama Alivyosema Ta’aalaa:
((يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا كُتِبَ عَلَيْكُمُ الصِّيَامُ كَمَا كُتِبَ عَلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكُمْ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ))
((Enyi walioamini! Mmefaridhishwa Swiyaam kama ilivyofaridhishwa kwa walio kabla yenu mpate kuwa na taqwa)). [Al-Baqarah (2:183)]
Na kwa ajili hiyo, Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((مَنْ لَمْ يَدَعْ قَوْلَ اَلزُّورِ وَالْعَمَلَ بِهِ، فَلَيْسَ لِلَّهِ حَاجَةٌ فِي أَنْ يَدَعَ طَعَامَهُ وَشَرَابَهُ))
((Ambaye hatoacha kusema ya haramu na kuyatenda, basi Allaah Hana haja ya [mtu huyo] kuacha chakula chake na kinywaji chake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1903), Abu Daawuwd (2345) na At-Tirmidhiy (702)]
Na toka kwa Abu Hurayrah kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((إذا كان يوم صوم أحدكم فلا يرفث ولا يصخب ولا يجهل، فإن شاتمه أحد أو قاتله قليقل: إني صائم))
((Itakapokuwa siku ya Swiyaam ya mmoja wenu, basi asitamke maneno machafu, wala asipayuke akipaza sauti, wala asifanye mambo ya ovyo. Na ikiwa mtu atatafuta sababu ya kutukanana naye au kupigana naye basi aseme: Hakika mimi nimefunga)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1904) na Muslim (1151)]
Tunapata funzo kutokana na Hadiyth hizi mbili kuwa ubaya wa maasia haya huzidi katika mfungo wa Ramadhwaan kuliko katika miezi mingineyo, na kuwa maasia haya hudhuru usalama wa Swiyaam, bali yanaweza kumfanya mfungaji akose kabisa thawabu.
9- Aseme kama atatukanwa: “Mimi nimefunga”
Ni kwa Hadiyth ya Abu Hurayrah iliyotangulia. Inakuwa ni vizuri kwa aliyetukanwa amwambie aliyemtukana wakati wa Swiyaam: “Mimi nimefunga”. Na ni vizuri aseme hivyo kwa sauti ya kusikika sawasawa kwa Swawm ya Faradhi au Swawm ya Sunnah. Katika hili kuna faida mbili:
Ya kwanza: Ni kumjuvya mtukanaji kuwa anayetukanwa hakuacha kukabiliana naye kwa kuwa hamwezi, bali ni kwa kuwa amefunga.
Ya pili: Ni kumkumbusha mtukanaji kuwa mfungaji hatukanani na yeyote, hivyo inakuwa ni kama kumkataza asiendelee kutukana.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
10-Mambo Yenye Kubatilisha Swiyaam
Alhidaaya.com [3]
Swawm kiujumla inabatilika kwa kukosekana sharti moja kati ya shuruti zake, au kuharibika nguzo kati ya nguzo zake. Na mizizi ya mambo haya yenye kufunguza ni mitatu ambayo Allaah ameitaja katika Kitabu Chake:
((فَالْآنَ بَاشِرُوهُنَّ وَابْتَغُوا مَا كَتَبَ اللَّـهُ لَكُمْ ۚ وَكُلُوا وَاشْرَبُوا حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَكُمُ الْخَيْطُ الْأَبْيَضُ مِنَ الْخَيْطِ الْأَسْوَدِ مِنَ الْفَجْرِ ۖ ثُمَّ أَتِمُّوا الصِّيَامَ إِلَى اللَّيْلِ))
((Basi sasa waingilieni na tafuteni Aliyokuandikieni Allaah kwenu. Na kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu uzi mweupe (mapambazuko) wa Alfajiri kutokana na uzi mweusi (wa kiza cha usiku). Kisha timizeni Swiyaam mpaka usiku)). [Al-Baqarah (2:187)]
‘Ulamaa wote bila makhitalifiano wanasema kuwa ni lazima mfungaji ajizuie wakati wa Swawm na vyakula, vinywaji na kujimai. Kisha wakakhitalifiana katika hilo katika masaail, baadhi yake yamenyamaziwa na mengine yamezungumziwa.
Yenye Kubatilisha Yanagawanyika Vigawanyo Viwili
(a) Yenye kubatilisha Swiyaam na kuwajibisha kulipa
Ni kula na kunywa kwa makusudi huku mfungaji akikumbuka kuwa amefunga. Ikiwa atakula au kunywa kwa kusahau, basi atatimiza Swawm yake na wala hatoilipa siku. Ni kwa Hadiyth ya Abu Hurayrah kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((من نسي -هو صائم- فأكل أو شرب، فليتم صومه، فإنما أطعمه الله وسقاه))
((Aliyesahau –naye amefunga- akala au akanywa, basi aitimize Swawm yake, kwani hakika Allaah Amemlisha na Amemnywesha)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1423) na Muslim (1155)]
Hukmu ni moja katika hili kwa Swawm ya Faradhi au ya Sunnah kutokana na ujumuishi wa dalili kwa Jumhuri kinyume na Maalik. Yeye ameihusisha hukmu hii kwa Swawm ya Ramadhwaan tu. Anasema ikiwa mtu amesahau katika Swawm isiyo ya Ramadhwaan, akala au akanywa, basi ni lazima ailipe. Lakini lililo sahihi ni kuwa hakuna tofauti.
Na kula ni kuingiza kitu hadi tumboni kwa njia ya mdomo, na kiujumla huhusisha vyenye manufaa na vyenye madhara, na visivyo na manufaa wala madhara.
Ikiwa mtu amekula au amekunywa au ameingilia akidhani jua limekuchwa au alfajiri bado haijachomoza, kisha ikamdhihirikia kinyume chake
‘Ulamaa katika hili wana madhehebu mawili:
La kwanza: Ni lazima alipe. Ni dhehebu la Jumhuri ya ‘Ulamaa wakiwemo Maimamu wanne. [Al-Bahru Ar-Raaiq (2/292), Al-Muntaqaa cha Al-Baajiy (2/292), Mughnil Muhjaat (1/432), Ash-Sharhul Kabiyr (2/31) na Al-Mughniy (3/354)]
La pili: Hana cha kulipa. Ni dhehebu la Is-Haaq, na riwaya toka kwa Ahmad, Daawuwd, na Ibn Hazm. Limenasibishwa kwa Jumhuri ya Salaf. Ni chaguo la Sheikh wa Uislamu Ibn Taymiyah. [Al-Muhalla (6/220,229), Al-Majmuw’u (6/311) na Majmuw’ul Fataawaa (25/231)]
Dhehebu hili ndilo lenye nguvu kutokana na yafuatayo:
1- Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَلَيْسَ عَلَيْكُمْ جُنَاحٌ فِيمَا أَخْطَأْتُم بِهِ وَلَـٰكِن مَّا تَعَمَّدَتْ قُلُوبُكُمْ ۚوَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا))
((Na wala hakuna dhambi juu yenu katika yale mliyoyakosea, lakini isipokuwa katika yale yaliyoyakusudia nyoyo zenu; na Allaah daima ni Mwingi wa kughufuria, Mwenye kurehemu)). [Al-Ahzaab (33:5)]
2- Kauli Yake Ta’aalaa:
((رَبَّنَا لَا تُؤَاخِذْنَا إِن نَّسِينَا أَوْ أَخْطَأْنَا))
((Rabb wetu Usituchukulie tukisahau au tukikosea)). [Al-Baqarah (2:286)]
Na Allaah –kama ilivyo kwenye Hadiyth Akasema- : “Na’am”. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (135)]
3- Hadiyth ya Asmaa bint Abiy Bakr aliyesema: ((Tulikula enzi ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) siku ambayo mawingu yalitanda, kisha jua likachomoza. Hishaam (msimulizi toka kwa mama yake Faatwimah toka kwa Asmaa) akaulizwa: Wakaamuriwa kulipa? Akasema: Ni lazima kulipa. Na Mu’ammar akasema: “Nimemsikia Hishaam akisema: Sijui kama walilipa au la)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1959)]
Hadiyth hii ya Asmaa haionyeshi uthibitisho wala ukanushi wa kulipa. Ama maneno ya Hishaam, hayo kayasema kwa rai yake. Hilo linadokezwa na swali aliloulizwa na Mu’ammar.
Kwa picha hii, tunapata kufahamu kuwa hawakuamuriwa kulipa, na kama wangewajibikiwa kulipa, basi hilo lingehifadhiwa. Na kwa kuwa halikuhifadhiwa toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), jukumu la dhima linakuwa halipo, na kulipa hakuna.
4- Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَكُلُوا وَاشْرَبُوا حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَكُمُ الْخَيْطُ الْأَبْيَضُ مِنَ الْخَيْطِ الْأَسْوَدِ مِنَ الْفَجْرِ))
((Na kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu uzi mweupe (mapambazuko) wa Alfajiri kutokana na uzi mweusi (wa kiza cha usiku)). [Al-Baqarah (2:187)]
Kuanza Swawm hapa kumefungamanishwa na kudhihiri wazi Alfajiri na si tu kuchomoza.
5- Asiyejua jambo husamehewa. Katika Hadiyth ya ‘Uday toka kwa Haatim amesema: ((Ilipoteremka (حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَكُمُ الْخَيْطُ الْأَبْيَضُ) nilichukua kamba nyeusi na kamba [iqaal] nyeupe, nikaziweka chini ya mto. Nikaanza kulitaamuli giza, na sikuweza kuona chochote. Nikarauka mapema kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) na nikamweleza hilo [akacheka], akasema:
((إنما ذلك سواد الليل والنهار))
((Hakika hilo ni weusi wa usiku na [weupe wa] mchana)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (4509) na Muslim (1090)]
Rasuli hakumwamuru kulipa kwa kuwa hajui, na hakukusudia kukaidi Amri ya Allaah na Rasuli Wake, bali yeye aliona kuwa hiyo ndiyo Hukmu ya Allaah na Rasuli Wake, na hivyo akasamehewa. [Sharhu Al-Mumti’i (6/403)]
Kauli hii ndiyo yenye nguvu kwa kuwa inawafikiana sambamba na dalili. Lakini yafuatayo ni lazima yachungwe:
1- Mwenye kufungua kabla jua halijazama, kisha ikambainikia kuwa bado halijazama, basi ni lazima aendelee kujizuia, kwa kuwa amefungua kwa msingi wa kuwepo sababu, kisha akagundua kuwa haipo.
2- Akila huku ana shaka ya kuchomoza Alfajiri, basi Swawm yake ni sahihi, kwa kuwa asili ni kuendelea usiku mpaka Alfajiri idhihiri kihakika au dhana yake itopee. Na akila huku ana shaka ya kuchwa jua, basi Swawm yake ni baatwil, kwa kuwa asili ni kubakia mchana. Hivyo haijuzu kula pamoja na shaka, na ni lazima alipe madhali hakujua kuwa amekula baada ya kuchwa jua. Akijua amekula baada ya kuchwa jua, basi hakuna kulipa hapo. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
Kula na kunywa kwa makusudi kunawajibisha kulipa tu
[Sharhu Fat-hil Qadiyr (2/70), Al-Mudawwanah (1/219), Al-Majmuw’u (6/329), Al-Mughniy (3/130) na vAl-Muhallaa (1/185)]
Yamesemwa haya na Ash-Shaafi’iy, Ahmad –kwa iliyo mashuhuri kwake-, Ahlu Adh-Dhwaahir na ‘Ulamaa wengi. Na hii ni kutokana na kutokuwepo Aayah au Hadiyth yenye kuwajibisha kafara isipokuwa katika jimai tu kama itakavyokuja mbeleni. Kafara ni kwa jimai tu na haivuki zaidi ya hapo kwenda kwenye mengineyo, kwa kuwa jimai ni ukiukaji mbaya wa utukufu wa Mwezi, na mtu anaweza kujikaza asiikaribie hadi usiku kinyume na alivyozoea katika kula na kunywa, na kwa kuwa pia haja ya kuikataza ni kubwa zaidi na hukmu ya kuikiuka ni ya usisitizo zaidi.
Lakini Maalik, Abu Haniyfah, Is-Haaq na baadhi wengineo, wanasema kuwa kula na kunywa kwa makusudi kunawajibisha kulipa na kutoa kafara, kwa kuwa kipimo chao ni kimoja na jimai, na vyote vinashirikiana katika kukiuka utukufu wa Swawm.
Kauli ya kwanza ndio sahihi zaidi kwa kuwa hakuna dalili thabiti, na asli ni kuwa kafara hazifanyiwi kipimo. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
3- Kujitapisha kwa makusudi
Ikiwa matapishi yatamshinda yakatoka yenyewe, basi halipi wala hatoi kafara bila makhitalifiano yoyote. Ni kwa Hadiyth ya Abu Hurayrah ya kuwa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((من ذرعه القيء فليس عليه قضاء، ومن استقاء عمدا فليقض))
((Aliyelemewa na matapishi basi halipi, na aliyejitapisha kwa makusudi basi alipe)). [Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd 2380), At-Tirmidhiy (716), Ibn Maajah (1676), Ahmad (2/468) na wengineo. Al-Bukhaariy na Ahmad wameitia kasoro kama ilivyo katika Naswbur Raayah (2/448). Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh katika Al-Irwaa (923) na Swahiyh Al-Jaami’i (6243)]
4, 5- Hedhi na nifasi
Mwanamke akipata hedhi au nifasi ijapokuwa katika dakika za mwisho za mchana, basi Swawm yake itatenguka, na ni lazima ailipe siku hii kwa ‘Ijma’a ya ‘Ulamaa.
6- Kujichua (kupiga punyeto) kwa kukusudia
Ni kufanya kusudi kuyatoa manii kwa njia isiyo ya jimai kama kuyatoa kwa kuichezea dhakari kimahaba kwa mkono au kujigusisha gusisha au mfano wa hayo kwa lengo la kuyatoa kwa ashiki. Na ikiwa manii yatamtoka kwa kufanya hayo kimakusudi huku anakumbuka kuwa amefunga, basi Swawm yake itabatilika na ni lazima ailipe kwa mujibu wa Jumhuri ya ‘Ulamaa. [Ad-Durar Al Mukhtaar (2/104), Al-Qawaaniynu Al-Fiqhiyyah (81), Rawdhwat At-Twaalibiyna (2/361), Al-Ummu (2/86), Al-Mughniy (3/48) na Kash-Shaaful Qinaa (2/352)]
Lakini Ibn Hazm anaona kuwa ikiwa atajitoa manii –bila kujamii-, basi Swawm yake haiharibiki hata kama amefanya makusudi. Amesema: “Haikuja kwa hilo matini yoyote wala Ijma’a wala kauli ya Swahaba wala Qiyaas”. [Al-Muhallaa (6/203-205]
Ninasema: “Madhehebu ya Jumhuri ndiyo yenye uzito zaidi. Yanatolewa dalili kwa Kauli Yake Ta’aalaa katika Al-Hadiyth Al-Qudsiy kuhusiana na mfungaji:
((يدع طعامه وشرابه وشهوته من أجلي))
((Anaacha chakula chake, kinywaji chake na matamanio yake kwa ajili Yangu)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1984) na Muslim (1151) toka kwa Abu Hurayrah)]
Na kujitoa manii ni matamanio, na pia kutoka manii yenyewe. Na linalothibitisha kuwa manii huitwa matamanio ni kauli yake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((وفي بضع أحدكم صدقة))
((Na katika kumwingilia mmoja wenu mke wake ni swadaqah)). Wakasema: Ee Rasuli wa Allaah! Mmoja wetu anafanya matamanio yake na anapata ajri? Akasema:
((أرأيتم لو وضعها في الحرام))
((Nielezeni, lau angeyaweka katika haramu [si angepata dhambi?])). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1006) toka kwa Abu Hurayrah]
Kile kinachowekwa ni manii, na yeye ameyaita matamanio (shahwah).
Ama kama atafikiria, au akaangalia akamwaga, na wala hakukusudia kwa kufikiria huko au kumwangalia mwanamke na mfano wa hivyo kumwaga manii, basi Swawm yake haiharibiki.
7- Niya ya kuvunja Swawm
[Al-Muhallaa 6/175), Al-Majmuw’u (6/314), Al-Mughniy (3/35) na Al-Mabsuwtw 3/87)]
Ikiwa atanuwiya kuvunja Swawm yake (na yeye amefunga), na akaazimia kwa kukata shauri kufungua kwa makusudi na huku anakumbuka kuwa yuko katika Swawm, basi Swawm yake itaharibika hata kama hakula au hajanywa kwa kuwa kila mtu ni kwa lile alilolinuwiya ((لكل امرئ ما نوى)) . Na kwa kuwa kuingia katika Swawm hakuhitajii kitendo isipokuwa niya ya Swawm, na hivyo hivyo kutoka hakuhitajii kitendo isipokuwa niya. Na kwa vile niya ni sharti ya kutekeleza Swawm, na yeye ameibadili kwa kinyume chake, na bila sharti, ‘ibaadah haitekelezeki.
Haya ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy, Dhwaahir, Ahmad, Abu Thawr, Adh-Dhwaahiriyyah na Asw-haab Ar-Raay, isipokuwa Asw-haab Ar-Raay wamesema ikiwa atarudi akanuwia kabla ya kufika nusu ya mchana, basi kutamtosheleza kwa mujibu wa asili yao ya kufaa kutia niya mchana.
8- Kuritadi
[Al-Mughniy (3/25) na Kash-Shaaful Qinaa (2/309)]
Hatujui baina ya ‘Ulamaa mvutano wowote kuwa mwenye kuritadi wakati wa Swawm, basi Swawm yake inabatilika, na atalazimika kuilipa kama atarudi tena katika Uislamu, ni sawasawa alirudi siku hiyo hiyo au baada ya kumalizika. Ni kwa Neno Lake Ta’aalaa:
((لَئِنْ أَشْرَكْتَ لَيَحْبَطَنَّ عَمَلُكَ وَلَتَكُونَنَّ مِنَ الْخَاسِرِينَ))
((Ukifanya shirki bila shaka zitaporomoka ‘amali zako na bila shaka utakuwa miongoni mwa waliokhasirika)). [Az-Zumar (39:65)]
Na kwa kuwa Swawm ni ‘ibaadah ambayo sharti yake ni niya, hivyo kuritadi kunaiharibu.
(b) Yenye Kubatilisha Swiyaam Na Kuwajibisha Kulipa Na Kafara
Ni jimai peke yake na si jingine zaidi. Toka kwa Abu Hurayrah amesema: ((Tulipokuwa tumekaa mbele ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), mara ghafla alimjia mtu na kumwambia: Ee Rasuli wa Allaah! Nimeangamia. Akamwambia: Una nini? Akasema: Nimemwingilia mke wangu na mimi nimefunga. Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akamuuliza: Je, una mtumwa umwache huru? Akasema hapana. Akamuuliza: Basi je unaweza kufunga miezi miwili mfululizo? Akasema hapana. Akamuuliza: Je unaweza kuwalisha masikini sitini? Akasema hapana. Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa salaam) akanyamaza. Na wakati sisi tuko katika hali hiyo, Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliletewa tenga lenye tende kavu. Akauliza: Yuko wapi muulizaji? Akasema: Mimi hapa. Akamwambia: Chukua hizi uzitoe swadaqah. Mtu yule akasema: Kwa walio mafukara zaidi kuliko mimi ee Rasuli wa Allaah? Naapa wal Laah! Kati ya pande mbili za Madiynah, hakuna watu wenye nyumba iliyo masikini zaidi kuliko watu wa nyumba yangu. Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akacheka mpaka chonge zake zikaonekana, kisha akamwambia: Basi walishe watu wako)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1936) na Muslim (1111)]
Jumhuri ya ‘Ulamaa wanaona kuwa kujamii mfungaji katika mchana wa Ramadhwaan kwa makusudi na kwa khiyari kwa kukutana tupu mbili na kukizamisha kichwa cha dhakari katika moja ya njia mbili (mbele au nyuma kuliko haramishwa), kunafunguza, na ni lazima kuilipa siku na kutoa kafara, ni sawa amemwaga manii au hakumwaga.
Ninasema (Abu Maalik): “Kigezo cha Jumhuri katika kuwajibisha kulipa kwa mwenye kujimai katika Mwezi wa Ramadhwaan, ni ziada iliyokuja katika baadhi ya Asaaniyd za Hadiyth hii, nayo ni kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam alisema mwishoni:
((وصم يوما مكانه))
((Na funga siku moja mahala pake)), nayo ni ziada dhwa’iyf haithibiti. [Hadiyth ya Abu Hurayrah iliyotangulia imesimuliwa kupitia Az-Zuhriy toka kwa Humayd bin ‘Abdul Rahmaan toka kwa Abu Hurayrah bila kutaja kulipa]
Na kwa ajili hiyo, Ibn Hazm –Rahimahul Laah- anaona kuwa ni waajib kwake kutoa kafara tu bila kulipa. Na hili lina nguvu na mwelekeo sahihi zaidi, na linaendana na yaliyozungumziwa nyuma kuhusiana na kulipa Swalaah, na yatakayokuja kuzungumziwa kuhusiana na kulipa Swiyaam- ya kuwa hakuna usharia wa kulipa kwa mtu aliyeacha ‘ibaadah –bila ya udhuru- isipokuwa kwa dalili mpya. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi”.
Je, ni waajib kafara kwa mwanamke kama ilivyo kwa mwanaume?
Katika Hadiyth ya Abu Hurayrah iliyotangulia ni kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwamuru mwanaume kafara, na akanyamaza kuhusu mwanamke. Na kwa hili, ‘Ulamaa wamekhitalifiana kwa kauli kadhaa kuhusu mwanamke aliyeingiliwa na mumewe; je atoe kafara au asitoe?
Ya kwanza: Si waajib kwa mwanamke kutoa kafara yoyote. Ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy, na kauli ya Ahmad isemayo kuwa kafara moja inawatosheleza wote wawili, na ni waajib kwa mwanamume tu pasina mwanamke. Na hii ni kwa yafuatayo:
1- Ni kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) hakumwamuru mwanamke kutoa kafara pamoja na kuwa mumewe amemjimai, na tendo limefanyika kutokana na wote wawili pamoja, yeye na mumewe. Hii inadulisha kuwa lau Rasuli angeliona kuwa ni lazima kafara juu yake, basi angemlazimisha, na wala asingelinyamazia hilo.
2- Hiyo ni haki ya mali iliyohusishwa na jimai, hivyo imehusishwa na mwanamume tu kama mahari.
Ya pili: Ni waajib kafara kwa mwanamke kama ilivyo kwa mwanamume. Ni kauli ya Jumhuri; Abu Haniyfah, Maalik, na kauli ya Ash-Shaafi’iy na Ahmad katika moja ya riwaya mbili swahiyh toka kwake. Kuna makhitalifiano na changanuzi kati yao kuhusu mwanamke muungwana, kijakazi, mwanamke aliyeridhia tendo na aliyelazimishwa. Wamesema:
1- Kwa sababu mwanamke amevunja hadhi ya Swawm ya Ramadhwaan kwa jimai, hivyo ni lazima naye atoe kafara kama mwanamume. Na sharia haikubagua usawa kati ya watu katika ahkaam isipokuwa katika maeneo maalum yaliyoainishwa na dalili. Na kama itamlazimu kulipa kwa kuwa amevunja Swawm kwa jimai ya kukusudia kama ilivyo wajibu kwa mwanamume, basi ni wajibu kwake vile vile kafara sawa na mwanamume kutokana na sababu hii.
2- Ama Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kutomwamuru mwanamke kutoa kafara, hapa tukio linazingatiwa kuwa ni hali maalum na si hali ya wote. Inawezekana mwanamke (wa Swahaba yule) alikuwa hajafunga kwa udhuru wa maradhi au safari, au alikuwa amelazimishwa, au amesahau kuwa kafunga, au mfano wa hivyo.
3- Mwanamke hakumuuliza Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) hukmu ya hilo kama alivyouliza mumewe, na mume kukiri alilolifanya mkewe hakumwajibishii hukmu madhali hakukiri.
4- Inawezekana kuwa sababu ya Rasuli kunyamazia hukmu ya mwanamke ni maneno aliyoyafahamu ya mumewe kuwa mkewe hana uwezo wa chochote.
Ya tatu: Inawatosha wote wawili kafara moja isipokuwa kama kafara itakuwa ni kwa kufunga, hapo itawabidi wote wawili wafunge. Haya ni madhehebu ya Al-Awzaa’iy.
Ninasema: “Madhehebu ya Jumhuri ndiyo yenye nguvu zaidi, na kauli ya Ash-Shaafi’iy haiko mbali pia. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi”.
Angalizo
Mwanamke akilazimishwa, au akisahau, au akiwa hajui, basi halipi wala hatoi kafara kwa mujibu wa kauli swahiyh. Pia mwanamume akisahau au akiwa hajui. Haya ni madhehebu ya Abu Haniyfah, Ash-Shaafi’iy na Ahmad. [Al-Mughniy (3/27) chapa ya Ihyaau At-Turaath Al-‘Arabiy]
Je, ni lazima kafara iwe kwa mpangilio?
Jumhuri wanasema kuwa ni lazima kafara iwe kwa mpangilio. Asihamie kufunga miezi miwili isipokuwa baada ya kushindwa kumwacha huru mtumwa, na asihamie kuwalisha masikini sitini ila baada ya kushindwa kufunga kwa mujibu wa inavyoonyesha Hadiyth iliyotangulia ya Abu Hurayrah. [Al-Mughniy (3/344), Bidaayatul Mujtahid (1/451) na Fat-hul Baariy (4/198)]
Lakini Maalik anasema kuwa mtu hukhiyarishwa kutokana na riwaya ya Muslim kuhusiana na Hadiyth toka kwa Abu Hurayrah: ((Kwamba mtu mmoja alifungua katika Ramadhwaan, na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akamwamuru atoe kafara kwa kumwacha huru mtumwa, au afunge miezi miwili mfululizo, au alishe masikini sitini)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1111)]
Wamesema: “Hailazimu mpangilio kutokana na riwaya ya Al-Bukhaariy kwa Hadiyth, kwani mfano wa swali kama hili linaweza kutumika kwa jambo la kukhiyarishwa. Hivyo inachukulika Rasuli kumwelekeza Swahaba huyo kumwacha huru mtumwa kuwa hilo anaweza kulitekeleza kulipia kafara yake [pengine alikuwa anamiliki watumwa wengi]. Wengine wameuchukulia mpangilio kama ni wa kupewa kipaumbele, na kuchaguzwa mtu lipi la kutoa fidia kama suala linalojuzu”.
Ama Jumhuri, wao wamepita mkondo wa kughilibisha (tarjiyh), wakatilia nguvu riwaya ya mpangilio kuliko riwaya ya kuchaguzwa wakisisitiza kuwa waliosimulia Hadiyth ya mpangilio ni wengi zaidi na Asaaniyd zao zinakutana zote kwa Imamu (msimulizi) mmoja, na pia msimulizi wa Hadiyth ya kuchaguzwa amecheza na maneno ya Hadiyth. Hivyo mpangilio ni salama na akiba zaidi na unatosheleza. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
Je, kafara hutolewa kwa idadi ya jimai?
[Bidaayatul Mujtahid (1/453), Al-Mughniy (3/341) na Al-Majmuw’u (6/370)]
1- Mwenye kujimai mchana wa Ramadhwaan kisha akatoa kafara, halafu akajimai siku nyingine, basi ni lazima atoe kafara nyingine kwa Ijma’a ya ‘Ulamaa.
2- Mwenye kujimai katika siku moja mara kadhaa, basi hawajibikiwi isipokuwa na kafara moja tu kwa Ijma’a ya ‘Ulamaa.
3- Mwenye kujimai katika mchana wa Ramadhwaan na hakutoa kafara, kisha akajimai siku nyingine, hapa kuna kauli mbili:
Ya kwanza: Ataitolea kafara kila siku, kwa kuwa kila siku ni ‘ibaadah kando, na kafara ikilazimu kwa kuiharibu Swawm moja, basi kafara haziingiliani. Ni kauli ya Maalik, Ash-Shaafi’iy na Al-Jamaa’ah.
Ya pili: Atatoa kafara moja tu madhali bado hajaitolea kafara jimai ya kwanza. Ni kauli ya Abu Haniyfah, Maswahibu zake, Al-Awzaa’iy na Az-Zuhriy kwa kulinganishia na adhabu ya kisharia (hadd).
Kauli ya kwanza ina nguvu zaidi. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
11-Mambo Ambayo Hayabatilishi Swiyaam
Alhidaaya.com [3]
1- Kuamka na janaba siku ya Swiyaam
Aliyelala –naye amefunga- kisha akaota, Swawm yake haiharibiki, bali ataendelea nayo kwa Ijma’a. [Raddu Al-Muhtaar (2/98) na Al-Qawaaniyn Al-Fiqhiyyah (81)]
Vile vile, aliyepata janaba usiku kisha akaamka na janaba yake asubuhi, Swawm yake ni sahihi na wala hatolipa kwa mujibu wa Jumhuri. Ni kwa Hadiyth ya ‘Aaishah na Ummu Salamah: ((Kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anaingiliwa na Alfajiri na yeye ana janaba kutokana na wakeze, kisha anaoga na kufunga)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1926) na Muslim (1109)]
2- Kumbusu mke na kugusana naye ngozi kwa ngozi kama atadhamini kuwa hawezi kumwaga manii
Toka kwa ‘Aaishah amesema: ((Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa akibusu na kukumbatia naye amefunga, na alikuwa mwenye kudhibiti zaidi matamanio yake kuliko yeyote kati yenu)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1927) na Muslim (1106)]
Pia amesema ‘Aaishah: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa ananibusu, yeye amefunga, na mimi nimefunga)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2384) na ‘Abdul Razzaaq)]
Ibn Hazm amesema (6/208): “Wakati alipokufa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), ‘Aaaishah alikuwa binti wa miaka 18. Kwa hilo, imebatilika kauli ya aliyetofautisha katika hilo kati ya mzee na kijana (kuwa mzee inafaa na kijana haifai), na kauli ya aliyesema kuwa busu ni makruhu wakati ambapo kisahihi, busu ni jambo zuri, lililo stahabiwa, ni Sunnah katika Sunan na kurubisho la mtu kwa Allaah Ta’aalaa kwa kumfuata Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam)”.
Ninasema: “Na wala haisemwi kuwa kujuzu kubusu kwa mfungaji ni mahususi kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kutokana na haya yafuatayo:
1- Toka kwa ‘Umar bin Abiy Salamah kuwa alimuuliza Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam): Je, mfungaji anapiga busu? Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akamwambia: Muulize huyu (akimnyooshea) Ummu Salamah. Akamweleza kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) anafanya hilo. Akasema: Ee Rasuli wa Allaah! Umeshasamehewa dhambi zako zilizopita na zijazo. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akamwambia:
((أما والله إتي لأتقاكم لله وأخشاكم له))
((Ama wal Laah. Hakika mimi ndio mchaji zaidi wenu kwa Allaah na mwenye kumwogopa zaidi wenu)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1108). Angalia Sharhu An-Nawawiy]
2- Toka kwa Jaabir kuwa ‘Umar bin Al-Khattwaab (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema: ((Nilijawa na furaha na hamu siku moja, nikakisi na mimi nimefunga. Nikamjia Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) nikamwambia: Hakika nimefanya jambo kubwa sana leo. Akauliza: Ni lipi? Nikasema: Nimebusu na mimi nimefunga. Akasema: Unasemaje lau umesukutua kwa maji? Nikasema: Hivyo haina ubaya. Akasema: Kwa lipi?)). [Hadiyth Swahiyh Lighayrih. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2382), Ahmad (1/53), ‘Iyd bin Humayd katika Al-Muntakhab (21), nayo ni Swahiyh Lighayrihii kama alivyosema Sheikh wetu Allaah Amhifadhi]
المباشرة ni kugusana ngozi ya mwanamume na mwanamke bila kufikia maeneo ya kujimai kama kubusu. Toka kwa Masruwk amesema: ((Nilimuuliza ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa: Ni lipi linaruhusiwa kwa mwanamume aliyefunga kwa mkewe? Akasema: Kila kitu isipokuwa jimai)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na ‘Abdul Razzaaq (8439)]
Na toka kwa ‘Amri bin Sharhabiyl: ((Kwamba Ibn Mas’uwd alikuwa akimchezea mkewe katikati ya mchana naye amefunga)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na ‘Abdul Razzaaq (8442) na Ibn Abiy Shaybah (3/63)]
Na toka kwa ‘Ikrimah amesema: ((Sa’ad bin Maalik aliisugua tupu yake (mkewe) kwa mkono wake na yeye amefunga)). [Swahiyh Lighayrihii. Imekharijiwa na ‘Abdul Razzaaq (8444), na ina Hadiyth mwenza kwa Ibn Abiy Shaybah (3/63)]
Ninasema: “Lililo sahihi ni kuwa si makruhu kupiga busu au kugusa. Ikiwa atapiga busu au akagusa madhii yakamtoka yeye au mkewe, basi hakuna kitu juu yao. Lakini ikiwa yeye anajijua kuwa atamwaga manii kwa kufanya hivyo, basi haitojuzu kufanya. Na kama atafanya akamwaga manii yeye au mkewe, basi aliyemwaga kati yao ndiye ambaye Swawm yake itabatilika, na ni lazima ailipe. [Al-Majmuw’u (6/323). Angalia Jaami’u Ahkaamin Nisaa (2/361)]
3- Kuoga na kujimwagia maji kichwani ili kujipooza na joto
Ni kwa yaliyotangulia nyuma kidogo ((kuwa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa Alfajiri inamwingilia na yeye ana janaba kutokana na wakeze, kisha huoga na kufunga)).
Baadhi ya Swahaba wa Nabiy (Swalla Allaahu ‘al;ayhi wa aalihii wa sallam) wamesema: ((Hakika nilimwona Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) huko Al-‘Arj anamimina maji juu ya kichwa chake naye amefunga kutokana na kiu au kutokana na joto)). [Al-Albaaniy kasema ni Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2348)]
4- Kusukutua na kupaliza bila kupandisha sana maji
Toka kwa Laqiytw bin Swabrah amesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((وبالغ في الاستنشاق إلا أن تكون صائما))
((Na yavute sana maji juu katika kupaliza isipokuwa kama umefunga)). [Hadiyht Swahiyh. Tumeitaja katika mlango wa twahara]
Hakuna ubaya kwa mfungaji kusukutua hata kama si katika wudhuu au ghusl, na wala unyevu wa maji unaobakia kinywani baada ya kusukutua hauharibu Swawm akiumeza pamoja na mate, kwa kuwa haiwezekani kujikinga nao. [Raddu Al-Muhtaar (2/98)]
Na ikiwa atasukutua au akapaliza maji puani na maji yakamponyoka yakafika kooni bila kukusudia wala kuzembea, basi haina neno kwake kwa mujibu wa kauli mbili swahiyh za ‘Ulamaa. Hili limesemwa na Al-Awzaa’iy, Is-Haaq na Ash-Shaafi’iy katika moja ya kauli zake mbili kinyume na kauli ya Abu Haniyfah na Maalik kuwa hilo linafunguza.
5- Kuonja chakula kwa haja mradi tu kisifike ndani
Toka kwa Ibn ‘Abbaas amesema: ((Hakuna ubaya kuonja siki au kitu maadamu hakikuingia kwenye koo yake na yeye amefunga)). [Hasan Lighayrihi. Imekharijiwa na Ibn Abiy Shaybah (3/47). Ina Hadiyth mwenza kwa Al-Bukhaariy (4/153) ikiwa Mu’allaq na Al-Bayhaqiy (4/261)]
Sheikh wa Uislamu amesema: “..na kuonja chakula ni makruhu bila haja lakini hakufunguzi. Ama kwa haja, basi ni kama kusukutua”. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/266). Angalia Al-Mabsuwtw (3/93)]
Na inaingia kwenye maana ya kuonja, kutafuna chakula kwa haja. Toka kwa Yuwnus toka kwa Al-Hasan amesema: “Nilimwona akimtafunia mtoto chakula –na yeye amefunga- anakitafuna kisha anakitoa toka kinywani mwake na kukiweka mdomoni mwa mtoto”. [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na ‘Abdur Razzaaq (7512). Ina mwenza kwa Ibn Abiy Shaybah (3/47)]
Faida
Ni makruhu kwa mfungaji kutafuna ubani mkali kama hautotoa utomvu wowote wa kuingia ndani na haukuwa na ladha inayosikika kooni, kwa kuwa ubani hukausha koo na kuleta kiu. Na kama unatoa utomvu unaoingia hadi kooni, basi unafunguza kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri. [Al-Mughniy (3/109), Al-Majmuw’u (6/353) na Fat-hul Baariy (4/160)]
6- Kuumika (الحجامة) na kuchangia damu kwa asiyechelea kudhoofu mwili
"الحجامة" kuumika, ni kufyonza damu kwa kikombe kidogo baada ya kuchanja ngozi. Ufyonzaji huu unaweza kuwa mkavu bila damu. [Kamusi ya Al-Wajiyz]
Imepokelewa toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kwa Asaaniyd tofauti kuwa amesema:
((أفطر الحاجم والمحجوم))
((Amefungua muumikaji na muumikwa)). [Swahiyh kwa Asaaniyd zake. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (774), Abu Daawuwd (2367) na wengineo. Angalia Al-Irwaa (931)]
Na imethibiti toka kwa Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) ya kuwa:
((أن النبي صلى الله عليه وسلم احتجم وهو صائم))
((Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) aliumika na yeye amefunga)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1939), Abu Daawuuwd (2372) na At-Tirmidhiy (776)]
Lakini madhehebu ya Ahmad, Ibn Siyriyn, ‘Atwaa, Al-Awzaa’iy, Is-Haaq, Ibn Al-Mundhir na Ibn Khuzaymah na ambayo yamekhitariwa na Ibn Taymiyah, yanasema mwenye kuumikwa hufungua kwa kufanyiwa hijaamah. Ni kauli pia ya ‘Aliy, Abu Hurayrah na ‘Aaishah. Hoja ya madhehebu haya ni:
[Al-Inswaaf (3/302), Al-Furuw’u (3/48), na Majmuw’u Al-Fataawaa (25/255)]
1- Hadiyth:
((أفطر الحاجم والمحجوم))
((Amefungua muumikaji na mwenye kuumikwa)).
2- Imaam Ahmad amesema kuwa Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas iliyotangulia ni Dhwa’iyf, nayo ipo kwa Al-Bukhaariy?!
3- Wamesema: Hata tukisema kuwa ni Swahiyh, lakini hata hivyo ni Mansuwkh.
Ibn Taymiyah ameongeza –toka kwa ‘Ulamaa wa Hanbal- kuwa muumikaji hufungua vile vile kama ataifyonza chupa.
Ama Jumhuri; Abu Haniyfah, Maalik, Ash-Shaafi’iy na wengineo, wao wanasema kuwa kuumika hakumfunguzi muumikaji wala mwenye kuumikwa. Haya yamesemwa pia na Ibn Mas’uwd, Ibn ‘Umar, Ibn ‘Abbaas, Anas, Abu Sa’iyd Al-Khudriyy na kundi la Masalaf. Hoja zao ni: [Al-Mabsuwtw (3/56), Al-Qawaaniyn Al-Fiqhiyyah (105), Al-Majmuw’u (6/349) na Fat-hul Baariy (4/209)
1- Kuwa Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas imethibiti na ni Swahiyh. Wamejibu madai ya Imaam Ahmad anayesema kuwa ni Dhwa’iyf kwa kutumia kauli ya Muhannaa aliyesema: “Nilimuuliza Ahmad kuhusu Hadiyth hii akasema kuwa hakuna ndani yake neno ((صائم)) mfungaji, bali lililopo ni ((محرم)) aliyehirimia, kisha akaziweka bayana Asaaniyd zake toka kwa Ibn ‘Abbaas lakini hakuna ndani yake Sanad ya Ayuuwb iliyoko kwa Al-Bukhaariy”.
Al-Haafidh amesema: “Hadiyth ni Swahiyh, haina shaka kabisa”.
2- Wamesema: Hadiyth ya ((أفطر الحاجم والمحجوم)) ((Amefungua muumikaji na mwenye kuumikwa)), ni Mansuwkh, na An-Nawawiy amezungumza sana kuhusu hilo. Kauli hii wameisema akina Ash-Shaafi’iy, Al-Bayhaqiy, Ibn ‘Abdul Barri na wengineo.
3- Wamesema Hadiyth ((أفطر الحاجم والمحجوم)) ni Dhwa’iyf.
Ninasema: “Uhakika ni kuwa hakuna uthibitisho wa madai ya kuwepo naskh toka kwa makundi mawili na hususan hilo likiambatana na kutojua historia. Kisha Hadiyth mbili ni Swahiyh, na hakuna yoyote iliyokosolewa kati yao. Na hizi hapa njia mbili ambazo ni lazima kuishilia kwenye moja kati yao:
(a) Ima isemwe kuwa kufungua muumikaji na mwenye kuumikwa kumenasikhiwa na Hadiyth nyingine, nayo ni Hadiyth ya Abu Sa’iyd Al-Khudriyy (Radhwiya Allaahu ‘anhu) aliyesema: ((Nabiy Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam ameruhusu kuumika kwa mfungaji)). [Swahiyh Lighayrih. Imekharijiwa na An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (3241), Ad-Daaraqutwniy (2/182) na Al-Bayhaqiy (4/264). Angalia Al-Irwaa (4/74)]
Ibn Hazm (6/204) amesema: “Isnaad yake ni Swahiyh, hivyo ni wajibu kuitumia, kwa kuwa ruksa inakuwa baada ya kuazimia. Hivyo imedulisha kuwa kubatwilika Swiyaam kwa kuumika kumenasikhiwa sawasawa kwa muumikaji au mwenye kuumikwa.
(b) Au isemwe kuwa katazo la kuumika kwa mfungaji si la kuharamisha, hivyo Hadiyth ya ((Amefunga muumikaji na mwenye kuumikwa)) itachukuliwa kimajazi, kwa maana kuwa kitendo chao kitapelekea kufungua. Hili linatiliwa nguvu na Hadiyth iliyosimuliwa na ‘Abdul Rahmaan bin Abiy Laylaa toka kwa mtu mmoja katika Swahaba wa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kuwa Rasuli wa Allaah: ((Amekataza kuumika na kuendelea na Swiyaam bila kufungua- lakini hakuyaharamisha mawili haya- kwa ajili ya kulinda afya za Swahaba Wake..))”. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2374) na ‘Abdur Razzaaq (7535). Swahaba kutojua jambo hakudhuru].
Hivyo inaduilisha kuwa yeye alilichukia hilo kwa yule ambaye alikuwa anadhoofika kwa kufanya hayo. Linatiliwa nguvu na Hadiyth iliyothibiti ya kuwa yeye alimwambia Anas bin Maalik: ((Je mlikuwa mnaifanya hijaamah makruhu kwa mfungaji enzi ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam? Akasema hapana, isipokuwa kutokana na kudhoofu mwili)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1940)]
Ninasema: “Na hili ndilo bora zaidi kukubalika, na hivyo madhehebu ya Jumhuri yanakuwa na nguvu zaidi ya kuwa hijaamah haitengui Swawm, lakini inakuwa makruhu kuifanya kwa mtu ambaye inamdhoofisha, na inakuwa ni haramu ikiwa udhoofu huo utakuwa sababu ya mtu kufungua. Na kutoa damu ni sawa na kufanya hijaamah, na yaliyosemwa kuhusu hijaamah ndiyo hayo hayo kuhusu kutoa damu. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi”.
7-10 – Kutia wanja, kupigwa bomba mapitio ya haja kubwa (mkunduni), kutia matone ya dawa puani na kunusa manukato
[Madhehebu ya Hanafiy, Shaafi’iy na baadhi ya Maalik, yanasema kuwa wanja haufunguzi sawasawa mtu akihisi ladha yake kooni au la. Na hili limesimuliwa toka kwa Ibn ‘Umar, Anas na Ibn Ubayya Awfaa. Lakini madhehebu ya Maalik na Ahmad yanasema kuwa wanja unabatwilisha Swawm ukifika kooni. Angalia Al-Bidaayah (1/126), Al-Majmuw’u (6/348), Al-Qawaaniyn Al-Fiqhiyyah (104) na Al-Inswaaf (3/299)]
[Jumhuri wanasema kupigwa bomba mkunduni kunafunguza. Lakini Daawuwd, Al-Hasan bin Swaaleh na Maalik, wanasema hakufunguzi. Angalia Al-Hidaayah (1/115), Al-Majmuw’u (6/320), Al-Qawaaniyn (104) na Al-Inswaaf (3/299)]
Sheikh wa Uislamu Ibn Taymiyah amesema: “Ama wanja na sindano , na matone ya dawa yananayotiwa kwenye mrija wa mkojo (urethra), na kutibu jeraha kwenye ubongo au jeraha la ndani ya mwili, haya ni katika mambo ambayo ‘Ulamaa wamevutana. Baadhi yao wamesema hakuna chochote katika hayo kinachofunguza, wengine wamesema yote yanafunguza isipokuwa wanja, wengine wamesema yote isipokuwa matone, na wengine wamesema wanja na matone havifunguzi lakini vinginevyo vyote vinafunguza.
Na lililo dhahiri zaidi ni kuwa hakuna chochote katika hayo kinachofunguza Swawm, kwani Swawm ni jambo ambalo anahitaji kulijua kila mtu katika Diyn ya Uislamu. Na lau kama Allaah na Rasuli Wake wameyaharamisha katika Swawm na yanaiharibu, basi ingelikuwa ni waajib kwa Rasuli kuyabainisha. Na kama angelieleza hilo, basi Swahaba wangelijua na wangelifikisha kwa umma kama walivyofikisha sharia nyinginezo. Na kwa vile hakuna yeyote katika ‘Ulamaa aliyenukulu hilo toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) si kwa Hadiyth Swahiyh, wala Dhwa’iyf wala Mursal, inajulikana kuwa hakueleza chochote katika hilo, na Hadiyth iliyozungumzia wanja ni Dhwa’iyf”. [Ni Hadiyth isemayo: ((Ya kuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliamuru aletewe ithmud ya miski wakati wa kulala. Akasema: ((Aiepuke mfungaji)), nayo ni Munkar. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2377)]. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/233-234)]
Na akasema: [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/242)] “Inavyojulikana ni kuwa wanja na mfano wake ni katika vitu ambavyo ni vigumu kuepukana navyo kwa watu wote kama ilivyo kwa mafuta, kuoga, bukhuri na mafuta mazuri. Na kama haya yangekuwa yanafunguza, basi Rasuli angebainisha kama alivyobainisha mengine yanayofunguza kwa kuyafanya. Na kwa kuwa hakubainisha hilo, itajulikana kuwa wanja ni katika aina za manukato, bukhuri na mafuta. Na bukhuri inaweza kupanda hadi puani ikafika kwenye ubongo, na mwili ukazimuka. Na mafuta hufyonzwa na mwili na kuingia ndani yake, na mtu hupata msisimko. Pia mafuta mazuri humfanya ajihisi yuko imara. Na kwa kuwa mfungaji hakukatazwa hayo, inadulisha kuwa anaruhusiwa kujitia manukato, kujifukiza udi, kujipaka mafuta mazuri na kujitia wanja. Baadhi ya Waislamu katika enzi yake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) waliwahi kujeruhiwa majeraha ya kwenye ubongo au ya kufika ndani ya mwili katika Jihaad au katika harakati nyingine. Na kama hali hiyo ingekuwa inafunguza, basi Rasuli angebainisha”.
Na akasema (Rahimahu-Allaah) - [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/235). Angalia Al-Muhalla (6/215)] : “Na waliosema kuwa mambo haya yanafunguza, hawana dalili yoyote toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), bali wamelisema hilo kwa kutegemea Qiyaas. La nguvu zaidi walilolitolea hoja ni kauli yake Rasuli:
((وبالغ في الاستنشاق إلا أن تكون صائما))
((Na yavute sana maji juu katika kupaliza isipokuwa kama umefunga))”. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa nyuma]
Akaendelea kusema [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/244)]: “Nacho ni Qiyaas dhwa’iyf kwa kuwa anayepaliza maji kwa tundu za pua yake, maji hayo huteremka hadi kwenye koo yake na kisha tumboni. Na kwa hilo, linatokea lile linalotokea kwa mwenye kunywa kwa mdomo wake ambapo kwa kufanya hivyo, maji huupa lishe mwili wake, huondosha kiu na chakula tumboni mwake husagwa kama inavyofanyika kwa kunywa maji. Na lau isingelikuja Hadiyth kuhusu hilo, ingejulikana kuwa hii ni katika namna ya unywaji, kwani hakuna tofauti kati yao isipokuwa katika kuingia maji kupitia mdomoni, na hilo si la kuzingatiwa, bali kuingia maji kwenye kinywa tu hakufunguzi, hili si lenye kufunguza wala si sehemu ya lenye kufunguza kwa kuwa halina athari, bali ni njia kuelekea kwenye lenye kufunguza. Mambo hayako hivyo kwa wanja, bomba la kwenye haja kubwa na kutibiwa ugonjwa wa kwenye ubongo na majeraha ndani ya mwili, kwani wanja hautoi lishe kabisa, na hakuna yeyote anayeingiza wanja ndani ya mwili wake si kwa mdomo wala kwa pua. Pia bomba la mapitio ya haja kubwa halitoi lishe, bali hupakua na kuvitoa vilivyoko mwilini mfano wa kama lau amenusa kitu katika viharishi au akashtuka mshtuko mkubwa uliosababisha mkorogeko mkali wa tumbo, na bomba hili halifiki tumboni. Na dawa inayofika tumboni katika kutibu jeraha la ndani ya mwili au kwenye ubongo haifanani na chakula kinachoingia humo”.
Ibn Taymiyah – (Rahimahu-Allaah) - amezungumza kwa urefu sana katika kutengua Qiyaas hiki, na tunachoweza kufaidika nacho kwa ufupi ni:
- Ni kuwa Hadiyth imethibitisha kuharibika Swawm kwa kula na kunywa lakini mambo haya hayaitwi kula au kunywa wala hayakusudiwi kwayo kula au kunywa. Na kwa msingi huo, sindano ya bomba na sindano kwa aina zake zote hazifunguzi ila tu kama itakuwa ni ya kulishia, hili ni la kutafitiwa.
- Linalopatikana kwa linalopatikana kwa kula na kunywa hujumuishwa nalo.
- Sababu ya kutenguza Swawm kutokana na kula au kunywa inaweza isiwe tu kula, bali inaweza kuwa mchanganyo wa kupata lishe na kuburudika kwa chakula na kinywaji. Linalothibitisha hili ni kuwa mgonjwa ambaye analishwa kwa mpira kwa masiku kadhaa, anakuwa anatamani sana chakula. [Kayaeleza haya Al-‘Allaamah Ibn ‘Uthaymiyn (Rahimahu-Allaah)- katika Al-Mumti’u (6/381)]
Basi ikiwa ni hivi, sindano zote hazitengui Swawm hata kama ni za kulishia. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
11- Kupiga mswaki
Kupiga mswaki ni jambo lililosuniwa kisharia –kama ilivyotangulia- na hakuna naswi yoyote inayomzuia mfungaji, bali kuna Hadiyth zilizopokelewa ambazo baadhi yake zinathibitisha uhalali wa kupiga mswaki kwa mfungaji, na nyingine zinamhimiza kufanya hivyo wakati wa Swiyaam, lakini ni Dhwa’iyf hazina mashiko. Na asli ni kuwa mswaki unaruhusiwa, na kama ungekuwa unaharibu Swawm, basi Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa sallam) angetueleza hilo na Swahaba wangelinukulu kutokana na ugumu wa kuepukana nao kwa watu wote.
Fuqahaa wote wamekubaliana kuwa inajuzu mfungaji apige mswaki, ijapokuwa ‘Ulamaa wa Kishaafi’iy na Kihanbali wamependelea kuacha kupiga kwa mfungaji baada ya jua kupinduka ili kuibakisha harufu mbaya ya kinywa ambayo inanukia vizuri zaidi kwa Allaah kuliko harufu ya miski.
Ninasema: “Lililo wazi zaidi ni kuwa hakuna ubaya kupiga mswaki nyakati zote. Allaah Ndiye Mjuzi zaidi”.
Je, inajuzu kutumia dawa ya meno (tooth paste) kwa mfungaji?
Kwa mujibu wa yaliyotangulia, inajuzu kutumia mswaki wa brashi na dawa kwa mfungaji kama atahakikisha haipenyi kufika kooni. Ni bora kuitumia usiku na kuacha mchana. Allaah Ndiye Mjuzi zaidi.
12- Kumeza kohozi النخامة
"النخامة" Ni kile kinachotoka kupitia tundu mbili za pua wakati wa kujikohoza (kamasi), au kohozi linalopanda toka kifuani. Kohozi haliharibu Swawm kwa mujibu wa Madhehebu ya Hanafiy, Maalik na riwaya toka kwa Ahmad, kwa kuwa umezaji wake ni wa ndani ya kinywa usiohusiana na kinachotoka nje, hivyo ni sawa na mate. [Raddu Al-Muhtaar (2/101), Al-Mughniy (2/43) na Jawaahir Al-Ikliyl (1/149)]
Ama Ash-Shaafi’iy na Hanbal, wao wanasema inafaa kuyameza kama hayakufika kinywani (toka kifuani au kooni), na kama yatafika kinywani mwake akayameza, basi atakuwa amefungua. [Rawdhwat At-Twaalibiyn (2/360) na Kash-Shaaf Al-Qinaa (2/329)]
Ninasema: “Lililo dhahiri zaidi ni kuwa hakuna ubaya kuyameza hata kama yako ndani ya kinywa chake madhali si kwa niya mbaya, au akakusudia kuyala au kuyanywa”.
13- Kuyameza yasiyowezekana kujikinga nayo kama:
(a) Mabaki ya chakula yaliyoganda kwenye meno kama ni kidogo kwa kuwa haiwezekani kuzuia yasichanganyike na mate. Ni sharti asikusudie kuyameza, au akashindwa kuyaengua apate kuyatema. [Radd Al-Muhtaar (2/98), Ar-Rawdhwat (2/359) na Kash-Shaaf Al-Qinaa (2/329)]
(b) Damu kidogo toka kwenye fizi na meno. Lau fizi zake zitatoa damu, na mate yake yakaingia kooni mwake yakiwa yamechanganyika na damu bila kufika tumboni, basi Swawm yake haibatiliki kwa mujibu wa kauli ya Mahanafiy, kwa kuwa hilo haliepukiki isipokuwa damu ikiyazidi mate, hapo itabatilika.
Ama Mashaafi’iy, wao wanasema kuwa Swawm yake itabatilika kwa kumeza mate yaliyochanganyika na damu. Wao wanaizingatia damu kuwa najisi na haifai kuimeza. [Raddu Al-Muhtaar (2/98), Ar-Rawdhwat (2/359) na Kash-Shaaf Al-Qinaa (2/329).
Ninasema: “Lililo dhahiri ni kuwa haifai kufanya kusudi kumeza damu kwa kuwa imeharamishwa. Na ikiwa kuimeza kutamshinda au ikawa vigumu kwake kujizuia asiweze kuimeza au hakujua, basi Swawm yake haibatiliki”.
(c) Vumbi la njiani, unga, poda na mfano wa hayo katika ambavyo haiwezekani kujikinga navyo.
14, 15, 16- Kula, kunywa na kujimai kwa kusahau
17- Kutapika bila kujitapisha
Nyuma kidogo tumezielezea dalili za kutofisidika Swawm kwa mambo haya.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
12-Wasiofunga (Swawm) Na Hukmu Zinazowahusu
Alhidaaya.com [3]
Wasiofunga katika Mwezi wa Ramadhwaan wako katika makundi matatu: [Bidaayatul Mujtahid (1/438)]
(a) Wanaoruhusiwa kufunga au kutofunga
(b) Wasioruhusiwa kufunga (lazima wale)
(c) Ambao ni lazima wafunge
[a] Kundi La Wanaoruhusiwa Kufunga Au Kutofunga Swawm
1- Mgonjwa
Maradhi ni kila lile linalomtoa mtu toka kwenye mpaka wa afya yake kutokana na hitilafu mwilini. [Al-Miswbaah Al-Muniyr, kidahizo (maradhi)]
‘Ulamaa kwa kauli moja wameruhusu mgonjwa kula kisha alipe anapopona. [Al-Mughniy pamoja na sharh (3/16)]
Na asli ya hili, ni Kauli ya Allaah Ta’aalaa:
((وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ))
Na atakayekuwa mgonjwa au safarini, basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo [Al-Baqarah (2:185)]
Toka kwa Salamah bin Al-Akwa’a (Radhwiya Allaah ‘anhu) amesema: “Ilipoteremka Aayah hii
((وَعَلَى الَّذِينَ يُطِيقُونَهُ فِدْيَةٌ طَعَامُ مِسْكِينٍ))
((Na kwa wale wanaoiweza lakini kwa mashaka na kutaabika watoe fidia; kulisha masikini)). [Al-Baqarah (2:184)]
ilikuwa anayetaka kula hula na hutoa fidia mpaka ilipoteremshwa Aayah inayoifuatia”. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (4507) na Muslim (1145)]
Yaani Neno Lake Ta’aalaa:
((شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِي أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَىٰ وَالْفُرْقَانِ ۚ فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ ۖ وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ ۗ))
Mwezi wa Ramadhwaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan ili iwe mwongozo kwa watu na hoja bayana za mwongozo na pambanuo (la haki na batili). Basi atakayeshuhudia miongoni mwenu mwezi na afunge. Na atakayekuwa mgonjwa au safarini, basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. [Al-Baqarah: 185]
Mgonjwa ana hali tatu: [Al-Mughniy (3/364) na Al-Muhallaa (6/228)]
1- Awe anaumwa ugonjwa hafifu ambao haumuumizi kwa kufunga na wala kufungua hakumletei afueni. Ni kama mafua mepesi, maumivu ya mbali ya kichwa, maumivu ya gego na mfano wa hayo. Huyu haijuzu kufungua.
2- Ni mwenye ugonjwa unaoshitadi au unaokawia kupona, na Swawm inakuwa nzito kwake lakini haimdhuru. Huyu imesuniwa afungue, ni makruhu kufunga.
3- Swawm kuwa nzito kwake na kumsababishia madhara yanayoweza kupelekea kifo. Huyu ni haramu kimsingi kwake kufunga kwa Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَلَا تَقْتُلُوا أَنفُسَكُمْ))
((Wala msijiue)). [An-Nisaa (4:29)]
Mtu mzima wa afya anayehofia ugonjwa kwa kufunga anaruhusiwa kufungua, kwa kuwa ni sawa na mgonjwa anayehofia kuzidi maradhi yake au Swawm kukawiza kupona. Allaah Ta’aalaa Amesema:
((وَلَا تَقْتُلُوا أَنفُسَكُمْ))
((Wala msijiue)). [An-Nisaa (4:29)]
Na Amesema:
((يُرِيدُ اللَّـهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلَا يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ))
((Allaah Anakutakieni mepesi na wala Hakutakieni magumu)). [Al-Baqarah (2:185)]
Pia Kasema:
وَمَا جَعَلَ عَلَيْكُمْ فِي الدِّينِ مِنْ حَرَجٍ ۚ
Na Hakukufanyieni ugumu wowote ule katika Dini [Al-Hajj: 78]
Na Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((إذا أمرتكم بأمر فائتوا منه مااستطعتم))
((Nikiwaamuruni jambo lolote, basi lifanyeni kiasi muwezavyo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (7288) na Muslim (1337)]
2- Msafiri
Sharia inamruhusu msafiri –wa safari ya kupunguza Swalaah- afungue kwa Kauli Yake Ta’alaa:
((وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ))
Na atakayekuwa mgonjwa au safarini, basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. [Al-Baqarah (2:185)]
Na kama msafiri atafunga, basi Swawm yake itaswihi. Ni madhehebu ya Swahaba wengi, Taabi’iyna na Maimamu wanne wanaosema kuwa kufunga safarini ni swahiyh na kunatosheleza. Lakini imesimuliwa toka kwa Abu Hurayrah, Ibn ‘Abbaas na Ibn ‘Umar (Radhwiya Allaah ‘anhum) –nayo ni madhehebu ya Ibn Hazm- kuwa Swawm si swahiyh na msafiri ni lazima alipe kama atafunga safarini. Kuna kauli nyingine inayosema kuwa ni makruhu kufunga, lakini madhehebu ya Jumhuri yana nguvu zaidi kama tutakavyokuja kubainisha mbeleni.
Lipi bora kwa msafiri, kufunga au kutofunga Swawm?
‘Ulamaa wamekhitalifiana kuhusu hili. Suala hili likifanyiwa uhakiki katika pale ambapo nusuus zinakutania, basi tunaweza kusema:
Msafiri ana hali tatu:
1- Swawm kumwelea ugumu au ikamzuia asiweze kufanya jambo la kheri, hapa kufungua itakuwa ni bora kwake. Hili linapatikana katika Hadiyth ya Jaabir aliyesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa safarini akaona msongamano na mtu amewekewa kivuli akauliza: Ana nini huyu? Wakasema: Amefunga. Akasema:
((ليس من البر الصوم في السفر))
((Si katika wema kufunga safarini)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1946) na Muslim (1115)]
Na Hadiyth ya Anas aliyesema: ((Tulikuwa pamoja na Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) safarini, baadhi yetu wamefunga na wengine hawakufunga. Tukashukia mahala katika siku ya joto, mwenye kivuli zaidi kati yetu ni mwenye guo, na baadhi yetu wanakinga jua kwa mkono. Anasema: Waliofunga wakaanguka na wasiofunga wakasimama, wakafunga mahema na wakawanywesha wasafiri. Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasema:
((ذهب المفطرون اليوم بالأجر))
((Wasiofunga wameondoka na thawabu leo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1119)]
Na katika Hadiyth ya Abu Sa’iyd Al-Khudriy ni kwamba Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliwaambia Swahaba wake–walikuwa vitani-
((إنكم مصبحو العدو غدا والفطر أقوى لكم))
((Hakika nyinyi mtawapambaukia maadui kesho, na kufungua kutawapeni nguvu zaidi)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1120)]
2- Swawm isimwelee uzito na isimzuie kufanya jambo la kheri, hapa kufunga itakuwa ni bora kwake kutokana na ujumuishi wa Neno Lake Ta’aalaa:
((وَأَن تَصُومُوا خَيْرٌ لَّكُمْ ۖ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُون))
((Na mkifunga Swiyaam ni bora kwenu mkiwa mnajua)). [Al-Baqarah (2:184)]
Toka kwa Abud Dardaai amesema: ((Tulitoka pamoja na Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) katika baadhi ya safari zake katika siku ya joto kufikia mpaka wa mtu kuweka mkono wake kichwani kutokana na joto kali, na hakuna kati yetu aliyefunga isipokuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) na Ibn Rawaahah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1945) na Muslim (1122)]
Na toka kwa ‘Aaishah kwamba Hamzah bin ‘Amri Al-Aslamiy alimuuliza Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa sallam): “Je nifunge safarini?”(Alikuwa mwingi wa kufunga). Akamwambia:
((إن شئت فصم، وإن شئت فأفطر))
((Ukitaka funga, na ukitaka kula)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1943) na Muslim (1121)]
Kwa kuwa Swawm –kama haina uzito- inatakasa haraka zaidi dhima na ni nyepesi zaidi kwa mfungaji na hususan anapofunga na watu kuliko kuja kulipa na watu wengine wanakula.
3- Swawm kumletea uzito mkubwa mno usiostahamilika unaoweza kusababisha kifo, na hapa ni lazima ale na ni haramu kufunga. Ni kama ilivyo katika Hadiyth ya Jaabir: ((Kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alitoka mwaka wa ukombozi kuelekea Makkah. Akaenda mpaka akafika Kuraa’al Ghamiym, kisha akaitisha gilasi ya maji, akainyanyua mpaka watu wakaiona, kisha akanywa. Baada ya hapo aliambiwa kuwa baadhi ya watu wamefunga, akasema:
((اولئك العصاة، اولئك العصاة))
((Hao ni waasi, hao ni waasi)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1114), na mfano wake kwa Al-Bukhaariy (1948) toka kwa Ibn ‘Abbaas]
Wakati wa kujuzu kufungua Swawm kwa msafiri
Kuna hali kadhaa kuhusiana na wakati wa kujuzu kufungua kwa msafiri:
Ya kwanza:
Aanze safari yake kabla ya alfajiri, au alfajiri imkute akiwa njiani safarini, na anuwie kutofunga. Huyu inajuzu kwake kufungua kwa Ijma’a ya ‘Ulamaa, kwa kuwa yeye ashapata sifa ya kuwa msafiri wakati wa kuwepo sababu ya uwajibu. [Al-Qawaaniyn Al-Fiqhiyyah cha Ibn Jaziy (82)]
Ya pili:
Aanze safari yake baada ya alfajiri (mchana). Jumhuri ya ‘Ulamaa; (Abu Haniyfah, Maalik, Ash-Shaafi’iy na riwaya toka kwa Ahmad) wanasema hatoruhusiwa kufungua siku hiyo, kwa kuwa Swawm ni ‘ibaadah ambayo inatofautiana kwa ukazi na safari, na viwili hivi vikichanganyika (ukazi na safari), basi hukmu ya ukazi inakuwa juu, mfano wa Swalaah. [Haashiyat Ibn ‘Aabidiyna (2/431), Al-Qawaaniyn Al-Fiqhiyyah (106) na Al-Majmuw’u (6/261)]
Lakini Ahmad, Is-Haaq na Hasan –nalo ni chaguo la Ibn Taymiyah, nayo ndio rai yenye nguvu katika suala hili- wanasema inajuzu kufungua katika siku hiyo. [Al-Inswaaf 3/289) na Majmuw’u Al-Fataawaa (25/212)]
Na hii ni kwa ujumuisho wa Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ))
Na atakayekuwa mgonjwa au safarini, basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. [Al-Baqarah (2:185)]
Na kwa Hadiyth ya Jaabir tuliyoitaja nyuma kidogo ya kutoka Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kwenda Makkah mwaka wa ukombozi ambayo kipande chake kinasema: ((…akaitisha gilasi ya maji baada ya Al-‘Asr, akanywa na watu wanamwangalia)). [Hadiyth Swahiyh. Imeelezwa nyuma kidogo]
Na mfano wake ni Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas ambayo kipande chake kinasema: ((..kisha akaitisha maji, akayanyanyua kwa mkono wake ili watu wayaone, akafungua mpaka akawasili Makkah, na hiyo ni katika Ramadhwaan…)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1948)]
Madhehebu haya yanatiliwa nguvu vile vile na Hadiyth ya Muhammad bin Ka’ab anayesema: ((Nilimwendea Anas bin Maalik –katika Ramadhwaan- na yeye anajiandaa kwa safari, na ngamia wake ameshaandaliwa. Akavaa nguo za safari, akaitisha chakula akala. Nikamwambia: Ni Sunnah? Akasema: Ni Sunnah, kisha akapanda)). [Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (799), Al-Bayhaqiy (4/247), Ad-Daaraqutwniy (2/187), Adh-dhwiyaa Fil Mukhtaara (2602) na wengineo. Al-‘Allaaamah Al-Albaaniy ana tasnifu katika Twaswhiyh yake, ipitie]
Toka kwa ‘Ubayd bin Jubayr amesema: ((Nilipanda jahazi na baba yangu Baswrah Al-Ghaffaariy toka Fustat wakati wa Ramadhwaan. Jahazi likan’goa nanga na kuanza safari, halafu akatengewa chakula chake akaniambia jongea tule. Nikamwambia: Je, si bado unayaona majumba [ya Fustat]? Akasema: Je, umeachana na Sunnah ya Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam)?)). [Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2412), Ahmad (6/398), Ad-Daaramiy (1713) na Al-Bayhaqiy (4/246). Angalia tasnifu iliyodokezewa kabla yake]
Angalizo
Katika Hadiyth hizi mbili za mwisho kuna dalili kuwa msafiri anatakikana ale kabla hajatoka mji aliopo. Ibn Al-‘Arabiy kasema: “Hadiyth ya Anas ni Swahiyh. Inadokeza kujuzu kula safari inapokuwa tayari”. [Naylul Awtwaar (4/271)]
Lakini Jumhuri ya ‘Ulamaa wamekataza msafiri kula kabla hajaondoka mji wake, kwa kuwa kabla hajaondoka hawi safarini, bali anakuwa ni mwenye kukusudia safari.
Ya tatu:
Anuwie kufunga –naye ni msafiri- kisha akaona bora asifunge, huyu inajuzu kula –kama ataona hilo ni bora kwake- kutokana na dalili zilizotangulia katika hali ya pili. Hili limesemwa na Jumhuri kinyume na Maalik na Hanafiy. [Al-Mughniy (3/19), Al-Majmuw’u (6/260), Al-Qawaaniynul Fiqhiyyah (82) na Radd Al-Muhtaar (2/122)]
Kutenguka ruksa ya kufungua kwa msafiri
Ruksa ya kufungua inatenguka kwa msafiri kwa mambo mawili:
La kwanza: Akinuwia kukaa bila kuainisha muda, au muda wa kukaa kisharia [Muda wa kukaa ambao anaruhusiwa kula kwa kauli ya Maalik na Shaafi’iy ni siku nne, kwa Hanbali zaidi ya siku nne, na kwa Hanafiy siku kumi na tano. Maainisho haya ya siku hayana dalili. Angalia Al-Muhallaa (6/244)]
Toka kwa Ibn ‘Abbaas: ((Kuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alipigana vita vya ukombozi (wa Makkah) katika Ramadhwaan na akafunga, mpaka alipofika Al-Kadiyd –nayo ni maji yaliyopo kati ya Qudayd na ‘Usfaan- [alifungua]. Aliendelea kula mpaka Mwezi ukamalizika)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (4275)]
Ni maarufu kwamba ukombozi ulikuwa ni tarehe 20 Ramadhwaan. Hivyo basi, Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alifungua akiwa Makkah siku kumi au siku kumi na moja kwa mujibu wa kutofautiana riwaya. Na hakuna shaka kuwa kufungua kwake katika muda huu, hakukanushi kufungua zaidi ya hapo.
Kiufupi ni kuwa aliyenuwia kukaa katika mji ukazi usiojulikana idadi ya siku zake, huyo atafunga na hatokula. Na kama hakunuwia kukaa bali amekaa ili kufuatilia haja yake bila kuwa na niya ya kukaa na hajui lini haja yake ataimaliza, basi huyo anaweza kula. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi.
La pili: Akirudi mjini kwake
Akirudi anakoishi usiku, na kesho yake ni Ramadhwaan, basi ni lazima afunge bila makhitalifiano. Ama lau kama amewasili mchana, je atajizuia kula hadi Magharibi? Hapa kuna kauli mbili. Yenye nguvu zaidi ni isemayo kuwa halazimiki kujizuia bali ataendelea kula. Haya ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na Maalik. Imepokewa kwa njia swahiyh toka kwa Ibn Mas’uwd kwamba amesema: ((Mwenye kula mwanzo wa mchana, basi ale mwisho wake)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na Ibn Abiy Shaybah (9343)]
Abu Haniyfah na Maswahibu zake wanasema: Atajizuia sehemu iliyobaki ya siku kwa kuchukulia Qiyaas cha mtu aliyekula Siku ya shaka akaja kujua kuwa ni Ramadhwaan. Maneno haya yanahitaji kutafitiwa zaidi, kwa kuwa aliyekula Siku ya shaka, amekula kutokana na kutojua, na msafiri huyu amekula kwa sababu halali. [Bidaayatul Mujtahid (1/441-442)]
Kutokana na hili inazalikana faida nayo ni:
Msafiri ambaye hakufunga akiwasili nyumbani mchana wa Ramadhwaan na akamkuta mkewe ametwaharika na hedhi au nifasi, au amepona ugonjwa na hakufunga, anaweza kumwingilia na hana kafara. [Al-Majmuw’u (6/268), nayo ni kauli ya Ash-Shaafi’iy katika Al-Ummu (2/62) na Maalik katika Al-Mudawwanah (1/184)]
Swali: Mtu kazidiwa matamanio ya kimwili na ameshindwa kuvumilia –siku moja- kumjimai mkewe, je anaweza kusafiri naye ili afungue apate kumjimai? Inavyoonekana ni kuwa hakuna ubaya kufanya hivyo. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi.
3, 4- Mzee kikongwe, bibi kijizere na mgonjwa wa maradhi sugu
‘Ulamaa wote wanakubaliana kuwa mzee kikongwe na bibi kijizere wasioweza kufunga, inajuzu kwao kula bila kulipa. Halafu wakakhitalifiana kuhusu lipi litawalazimu kama watakula. Jumhuri wamesema watalisha maskini kwa kila siku moja, lakini Maalik anasema hawawajibikiwi kulisha masikini ila tu hilo ni zuri wakipenda. [Al-Qawaaniyn Al-Fiqhiyyah (82), Al-Majmuw’u (6/258), Al-Mughniy (3/79), Kash-Shaaf Al-Qinaa (2/309) na Bidaayatul Mujtahid (1/447)]
Kauli ya Jumhuri ina nguvu zaidi.
Na asli ya hili ni Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَعَلَى الَّذِينَ يُطِيقُونَهُ فِدْيَةٌ طَعَامُ مِسْكِينٍ))
((Na kwa wale wanaoiweza lakini kwa mashaka na kutaabika watoe fidia; kulisha masikini)). [Al-Baqarah (2:184)]
Toka kwa ‘Atwaa kuwa alimsikia Ibn ‘Abbaas akiisoma Aayah hii, na Ibn ‘Abbaas akasema: ((Si mansuwkhah (haikufutwa), ni kwa mzee kikongwe na bibi kijizere wasioweza kufunga. Walishe mahala pa kila siku masikini mmoja)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (4505). Lakini Ibn ‘Abbaas ameisoma:
(وعلى الذين يطوّقونه)
Na kwa wale wanaoiweza lakini kwa mashaka na kutaabika
nacho ni kisomo kisicho cha kawaida. Angalia Tafsiyr At-Twabariy (3/438)]
Na Jumhuri ya Swahaba –akiwemo Ibn ‘Abbaas kwa utafiti unaoendelea kama tutakavyoona mbeleni- wanaona kuwa Aayah hii ni mansuwkhah. Toka kwa Salamah bin Al-Akwa’a amesema: ((Ilipoteremka
وَعَلَى الَّذِينَ يُطِيقُونَهُ فِدْيَةٌ طَعَامُ مِسْكِينٍ
((Na kwa wale wanaoiweza lakini kwa mashaka na kutaabika watoe fidia; kulisha masikini)). [Al-Baqarah (2:184)]
mtu alikuwa (ana khiyari) akitaka anakula na kutoa fidia mpaka ilipoteremka Aayah inayoifuatia, ikafuta hukmu hii)). [Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (4507)]
Na tukichukulia kauli inayosema kuwa imefutwa, basi Aayah bado iko pale pale mahala pa kutolewa dalili, kwa kuwa ikiwa imeteremka kuhusiana na mzee mwenye umri mkubwa –kama walivyosema baadhi ya Masalaf- na hata ikiwa imeshuka kukhiyarisha, basi itabaki hivyo hivyo, kwa kuwa mzee anabakia katika haki ya mwenye kuweza kufunga, hivyo mzee huyu anabakia katika hali yake kama alivyokuwa. [Al-‘Inaayat ‘Alal-Hidaayat (2/227- pamoja na Fat-hul Qadiyr]
Kisha mzee kikongwe na bibi kijizere kufutiwa Swawm kunanasibiana na ujumla na ujumuishi wa kuondoshea watu uzito.
Na hukmu ya mgonjwa wa maradhi sugu ni kama ya wazee. [Radd Al-Mukhtaar (2/119), Al-Majmuw’u (6/258), Ar-Rawdh Al-Murabba’a (1/138)]
5,6- Mja mzito na mwenye kunyonyesha
Mwanamke mja mzito akikihofia kijusi chake tumboni, au mwenye kunyonyesha akahofia kichanga chake kutopata maziwa ya kutosha au kutopata kabisa na mfano wa hivyo, basi inajuzu kwao kula bila makhitalifiano yoyote kutokana na kauli yake Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((إن الله عز وجل وضع عن المسافر شطر الصلاة، وعن المسافر والحامل والمرضع الصوم))
((Hakika Allaah ‘Azza wa Jalla Ameondosha nusu ya Swalaah kwa msafiri, na Swawm kwa msafiri, mja mzito na mwenye kunyonyesha)). [Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na Ahmad (4/347) na ‘Abdu bin Humayd (Al-Muntakhab) (430). Sheikh wetu amesema ni Hadiyth Hasan]
Lakini ‘Ulamaa wamekhitalifiana kuhusiana na linalowalazimu kama wakila kwa kauli tano:
Ya kwanza:
Ni lazima walipe na walishe masikini mmoja kwa kila siku. Ni kauli ya Maalik, Ash-Shaafi’iy na Ahmad. [At-Tirmidhiy ameinukulu kutoka kwao (3/402 –At-Tuhfah. Angalia rejea zilizotangulia]
Na Wanazuoni wa Kishaafiíy na Kihanbali wanasema ikiwa watakula kwa kujiogopea wenyewe, basi watalipa tu!!
Ya pili:
Watalipa tu. Ni madhehebu ya Al-Awzaa’iy, Ath-Thawriy, Abu Haniyfah na Maswahibu Zake, Abu Thawr na Abu ‘Ubayd. [Bidaayatul Mujtahid (1/446) na Jaami’u Ahkaamin Nisaa (2/394)]
Hawa wameichukulia dalili ya kuwekwa kundi moja msafiri, mja mzito na mwenye kunyonyesha katika Hadiyth iliyopita, au wametumia Qiyaas cha mja mzito na mwenye kunyonyesha kwa mgonjwa au msafiri.
Kauli yao hii inajibiwa kwa kusema kuwa msafiri ni lazima alipe kutokana na naswi nje ya Hadiyth, nayo ni Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ))
((Na atakayekuwa mgonjwa au safarini)). [Al-Baqarah (2:185)]
Ama mjamzito na mwenye kunyonyesha, hakuna dalili ya kuwajibisha wao kulipa. Kisha kwa kuiangalia Hadiyth kwa kina, tunakuta kwamba msafiri akipunguza Swalaah safarini, hatakiwi –baada ya kurudi- kutimiza rakaa alizokuwa amepunguza, Basi na isemwe pia kuwa mjamzito na mwenye kunyonyesha hawalazimiki kulipa siku walizokula!! [Jaami’u Ahkaamin Nisaa (2/395)]
Ya tatu:
Watalisha tu bila kulipa. Ni kinyume na iliyopita. Ni kauli ya Ibn ‘Abbaas na Ibn ‘Umar. Ni madhehebu ya Is-Haaq, na ni chaguo la Al-‘Allaamah Al-Albaaniy (Rahimahumul Laah).
Toka kwa Ibn ‘Abbaas amesema: ((Mzee kikongwe na bibi kijizere waliruhusuwa katika hilo nailhali wanaweza kufunga, wakitaka wanakula na wanalisha kila siku masikini, na hawalipi. Kisha hukmu hiyo ikaondoshwa katika Aayah hii:
فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ
Basi atakayeshuhudia miongoni mwenu mwezi na afunge. [Al-Baqarah: 185]
na ikathibiti kwa mzee kikongwe na bibi kijizere kama hawawezi kufunga, na mjamzito na mwenye kunyonyesha wakihofia [nafsi zao au watoto wao], na walishe kila siku masikini)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Ibn Al-Jaaruwd (381), na Al-Bayhaqiy (4/239). Angalia Al-Irwaa (4/18)]
Na katika neno lake “ikathibiti” kuna ujulisho kuwa hukmu hii ilikuwa ni sharia kwa asiyeweza kufunga kama ilivyokuwa sharia kwa mwenye kuweza kufunga, na hii ikafutwa na nyingine ikaendelea. Na bila shaka Ibn ‘Abbaas ameujua usharia wake wote na kuendelea kwake toka kwenye Hadiyth, na si toka kwenye Qur-aan. [Al-Albaaniy (Rahimahul Laah amelielezea hili katika Al-Irwaa (4/24)]
Na hili linatiliwa nguvu na Ibn ‘Abbaas kuithibitisha hukmu hii kwa mjamzito na mwenye kunyonyesha kama wakihofia. Na ni wazi kabisa kuwa wawili hawa si kama mzee kikongwe na bibi kijizere katika kutokuwa na uwezo wa kufunga, bali wao wana uwezo wa kufunga. Na kwa ajili hiyo, alikuwa akimwamuru kijakazi chake mjamzito ale na kumwambia: ((Wewe ni sawa na mzee kikongwe asiyeweza kufunga, basi kula na ulishe kwa kila siku nusu pishi ya ngano)). [Isnaad Yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na ‘Abdul Razzaaq (7567) na Ad-Daaraqutwniy (2/206) na amesema ni Swahiyh]
Basi ni kutokea wapi Ibn ‘Abbaas amewapa wawili hawa hukmu hii na kusema kuwa Aayah hii ni mansuwkhah?! Hilo ni kutoka kwenye Sunnah bila shaka.
Toka kwa Naafi’i amesema: ((Binti wa Ibn ‘Umar alikuwa chini ya mwanamume wa Kikureshi, alikuwa mja mzito, kikampata kiu katika Ramadhwaan. Ibn ‘Umar akamwamuru ale na alishe kwa kila siku masikini)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na Ad-Daaraqutwniy (2/207). Angalia Al-Irwaa (4/20)]
Ya nne:
Mjamzito atalipa, na mwenye kunyonyesha atalipa na atalisha. Ni kauli ya Maalik, na ni kauli ya Wanachuoni wa Kishaafi’iy. [Al-Muhallaa (6/265), Bidaayatul Mujtahid (1/446) na Al-Majmuw’u (6/273)]
Ya tano:
Si lazima juu yao kulipa wala kulisha. Ni madhehebu ya Ibn Hazm [Al-Muhallaa (6/263)]
Amesema: “Swawm ikipomoka, basi kuwajibisha wao kuilipa ni sharia ambayo Allaah Hakuidhinisha, na Allaah Ta’aalaa Hakuwajibisha kulipa isipokuwa kwa mgonjwa, msafiri, mwenye hedhi, mwenye nifasi na mwenye kujitapisha kwa kusudi. Ama kuwakalifisha kulisha, bila shaka haijuzu kwa yeyote kulazimisha faini ambayo haikutajwa na Aayah, wala Sunnah wala Ijma’a”.
Ninasema: “Kauli yenye nguvu zaidi kati ya kauli hizi ni kuwa watakula na watalisha kwa kila siku masikini, na hakuna kulipa juu yao. Ni kauli ya Ibn ‘Abbaas na Ibn ‘Umar, na hakuna Swahaba yeyote aliyekwenda nao kinyume. Kisha Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas ina hukmu ya “Raf-’u”, kwa kuwa ni Hadiyth ya Swahaba iliyokuja katika kufasiri yanayohusiana na sababu ya kuteremka Aayah. Na hii ni Hadiyth Musnad kama inavyojulikana katika taaluma ya Mustwalah”. [Angalia Kitabu cha Tadriyb Ar-Raawiy (1/192-193) na ‘Uluwm Al-Hadiyth cha Ibn Swalaah (uk 24)]
[b] Kundi La Ambao Ni Lazima Wale Na Walipe
1,2- Mwenye hedhi na mwenye nifasi
‘Ulamaa wote bila makhitalifiano wanasema haiswihi kufunga kwa mwenye hedhi na mwenye nifasi, na si wajibu kwao, bali pia ni haramu, na baada ya kutwaharika ni lazima walipe. [Al-Mughniy (3/142) na Al-Majmuw’u (6/259)]
Toka kwa Abu Sa’iyd (Radhwiya Allaah ‘anhu) amesema: “Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((أليست إذا حاضت لم تصل ولم تصم؟ فذلك نقصان دينها))
((Je, si anapoingia hedhini haswali wala hafungi? Basi hilo ni upungufu wa diyn yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1951)]
Na toka kwa ‘Aaishah amesema: ((Tulikuwa tunapata hedhi wakati wa enzi ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) halafu tunaamuriwa kulipa Swawm na hatuamuriwi kulipa Swalaah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (335), Abu Daawuwd (259), At-Tirmidhiy (784) na An-Nasaaiy (4/191)]
Masuala Mbalimbali Kuhusu Swawm Na Mwanamke Mwenye Hedhi
Akitwaharika na hedhi wakati wa mchana
Ataendelea kujiachia atakavyo katika kula na kunywa, na kama mumewe atarudi kutoka safari akiwa hajafunga, anaweza kumjimai. Haitakikani ajizuie siku iliyobakia kwa niya ya kufunga.
Akitwaharika kabla ya Alfajiri
Akitwaharika kabla ya Alfajiri na akanuwia kufunga, Swawm yake itaswihi hata kama atakuja kuoga baada ya Al-Fajiri. Hii ni kauli ya Jumhuri.
Je, mwanamke anaweza kutumia dawa ya kukata hedhi katika Mwezi wa Ramadhwaan?
Hedhi ni jambo ambalo Allaah Amewaumbia nalo wanawake, na wanawake wakati wa enzi ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) hawakuwa wakijitaabisha kwa hilo ili waweze kufunga Mwezi kamili, hivyo hilo si jambo linalopendeza.
Lakini ikiwa mwanamke atafanya hilo –na dawa ikawa haina madhara kwake- basi hakuna ubaya. Na akiitumia na damu ikakatika, basi anakuwa na hukmu ya mwanamke aliye twahara, atafunga na wala hatolipa. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi.
Mwenye damu ya istihaadhwah
Hatojizuia kufunga wala kuswali, bali hayo yote mawili ni lazima ayafanye kwa Ijma’a ya ‘Ulamaa.
3- Mwenye kuhofia kufa akifunga
Huyu ni lazima ale. [Al-Muhallaa (6/228), Al-Majmuw’u (6/262), Ad-Durru Al-Mukhtaar (2/116) na Al-Qawaaniyn Al-Fiqhiyyah (82)]
[c] Kundi La Ambao Hawaruhusiwi Kula
Ni kila Muislamu aliyebaleghe, mwenye akili, mzima wa afya, mkazi asiye msafiri, na mwanamke aliyetwaharika kutokana na hedhi au nifasi.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
13-Kulipa Swiyaam Za Ramadhwaan
Alhidaaya.com [3]
1- Mwenye kufungua bila udhuru
‘Ulamaa wengi wanasema kuwa mwenye kufungua makusudi, ni lazima alipe sawasawa kwa udhuru au bila udhuru. Lakini wamekhitalifiana hawa katika haya:
Baadhi yao wamewajibisha kulipa na kutoa kafara kwa aliyekula au kunywa kwa kuliweka hilo kipimo kimoja na jimai!! [Tumegusia nyuma kidogo kuwa amri ya kulipa kwa mwenye kumjimai mkewe mchana wa Ramadhwaan haikuthibiti toka kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam).
Ni kauli ya Ibn Mubaarak, Ath-Thawriy, Is-Haaq, Abu Haniyfah, na Maalik. Ash-Shaafi’iy na Ahmad ambao wamesema ni lazima alipe bila kutoa kafara.
Ama Ibn Hazm, yeye anaona kuwa hakuna dalili ya kisharia ya kulipa akila makusudi bila udhuru, kwa kuwa ‘ibaadah ya muda ina mpaka wa kuanza na kumalizika, na kama itaachwa bila udhuru, basi hakuna sharia inayosema ilipwe ila kwa naswi (dalili) mpya. Hivyo kulazimisha Swiyaam isiyo Ramadhwaan –ambayo amefaradhishiwa kufunga- badala yake, ni wajibisho wa sharia ambayo Allaah Ta’aalaa Hakuiamuru. [Al-Muhallaa (6/180) na Mas-alah (735)]
Ninasema (Abu Maalik): “Haya ni madhehebu yenye nguvu zaidi kama ilivyozungumzwa nyuma kuhusiana na kulipa Swalaah zilizompita mtu. Na hapa yanatiliwa nguvu ya kuwa haikuthibiti kuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwamuru aliyejimai mchana wa Ramadhwaan alipe pamoja na kuthibiti kafara kama ilivyotangulia nyuma kidogo. Imepokelewa kwa njia swahiyh toka kwa Ibn Mas’uwd kuwa amesema: ((Mwenye kufungua siku moja ya Ramadhwaan bila ya udhuru wala ruksa, haitomfalia Swiyaam ya umri wake wote))”. [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na Ibn Abiy Shaybah (9784)]
Hadiyth kama hii imepokewa pia toka kwa Abu Hurayrah.
Ninasema: “Lakini katika yaliyotangulia, kujitapisha kwa kusudi kunatolewa nje, kwani mwenye kufanya hivyo atalipa kutokana na naswi inayogusia hilo kama ilivyozungumzwa katika sehemu yake husika. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi”.
1- Kulipa Ramadhwaan si lazima kufanyike kwa haraka
Kulipa siku zilizompita mtu katika Ramadhwaan kutokana na udhuru wa kisharia si lazima kuwe papo kwa hapo, bali wajibu wake ni wa wigo mpana na wakati mkunjufu. Ni kwa Hadiyth ya ‘Aaishah (Radhwiya Allaah ‘anhaa) aliyesema: ((Ilikuwa ninakuwa na Swawm ya kulipa ya Ramadhwaan, na siwezi kuilipa isipokuwa katika Sha’abaan)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1950) na Muslim (1146)]
Al-Haafidh kasema katika Al Fat-h (4/191): “Katika Hadiyth kuna dalili ya kujuzu kuchelewesha kulipa Ramadhwaan, sawasawa kukawa (kuchelewesha huko) kwa udhuru au bila udhuru”.
Lakini pamoja na hivyo, ni vizuri kufanya haraka kulipa kutokana na ujumuishi wa Kauli Yake Ta’aalaa:
((أُولَـٰئِكَ يُسَارِعُونَ فِي الْخَيْرَاتِ وَهُمْ لَهَا سَابِقُونَ))
((Hao wanakimbilia katika mambo ya khayr; na wao ndio wenye kuyatanguliza)). [Al-Muuminuwn (23:61)]
Faida
Ikiwa atachelewesha kulipa mpaka ikaingia Ramadhwaan nyingine, basi atafunga Ramadhwaan mpya ilioingia kama alivyoamuriwa. Kisha akila katika Shawwaal, atayalipa masiku anayodaiwa tu na wala hakuna la ziada ya hapo. Si wajibu kwake kulisha wala jingine lolote, kwa kuwa hakuna chochote chenye kuthibitisha hilo kilichorufaishwa kwa Nabiy (Swalla Allaah ’alayhi wa aalihii wa sallam). Haya ni madhehebu ya Abu Haniyfah na Ibn Hazm, nayo ndiyo yenye nguvu.
Maalik amesema kuwa atalisha katika kuilipa kila siku kibaba kwa kibaba kwa idadi ya masikini ikiwa alifanya kusudi kuacha kulipa. Ni kauli ya Ash-Shaafi’iy pia. [Al-Muhallaa (6/260, 261). Angalia Al-Majmuw’u (6/412)]
2- Si lazima kufululiza siku katika kulipa
Ni kwa Kauli Yake Ta’aalaa :
فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ
basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. [Al-Baqarah (2:184)]
Ibn ‘Abbaas amesema: ((Hakuna ubaya kama ataachanisha)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Al-Bukhaariy amesema ni Mu’allaq, na ‘Abdul Razzaaq kasema ni Mawsuwl (4/43), na Ad-Daaraqutwniy (2/192) na Al-Bayhaqiy (4/258) kwa Sanad Swahiyh]
Abu Hurayrah amesema: ((Azilipe kwa (hisabu) ya witri akipenda)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na Ad-Daaraqutwniy. Angalia Al-Irwaa (4/95)]
Na Anas kasema: ((Ukipenda ilipe Ramadhwaan siku mfululizo, na ukitaka achanisha siku)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na Ibn Abiy Shaybah (9115) na Al-Bayhaqiy (4/258)]
Ama Hadiyth Marfuw’u toka kwa Abu Hurayrah:
((من كان عليه صوم رمضان فليسرده ولا يقطعه))
((Anayedaiwa Swawm ya Ramadhwaan basi aandamishe wala asiikate))..
Hadiyth hii ni Dhwa’iyf haijasemwa na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam). [Imekharijiwa na Ad-Daaraqutwniy (2/191) na Al-Bayhaqiy (4/259). Angalia Al-Irwaa (4/95)]
Maimamu wanne wamekhiyarisha kati ya kufululiza au kuachanisha wakati wa kulipa. [Al-Muhallaa (6/261), Masaail Ahmad cha Abu Daawuwd (uk. 95), Al-Majmuw’u (6/412) na Al-Mughny (3/43)]
3- Aliyekufa na anadaiwa Swawm
‘Ulamaa wamekhitalifiana kuhusu mtu aliyekufa na anadaiwa Swawm. Je msimamizi wake atamfungia? Wana kauli tatu kuhusu hili:
Ya kwanza:
Hafungiwi, si kwa Swawm ya nadhiri wala qadwaa ya Ramadhwaan. Ni madhehebu ya Abu Haniyfah na Maswahibu zake, Maalik, Dhwaahir na madhehebu ya Ash-Shaaf’iy. [Tahdhiyb As Sunan (7/27), Al-Majmuw’u (6/412) na Fat-hul Qadiyr (2/360)].
Hoja yao ni:
1- Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَأَن لَّيْسَ لِلْإِنسَانِ إِلَّا مَا سَعَىٰ))
((Na kwamba insani hatopata (jazaa) isipokuwa yale aliyoyafanyia juhudi)). [An-Najm ( 53:39)]
2- Kauli ya Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam)
((إِذَا مَاتَ ابنُ آدم انْقَطَعَ عَنْهُ عَمَلُهُ إِلَّا مِنْ ثَلَاثٍ: صَدَقَةٍ جَارِيَةٍ، أو عِلْمٍ يُنْتَفَعُ بِهِ، أَوْ وَلَدٍ صَالِحٍ يَدْعُو لَهُ))
((Anapokufa mwanadamu ‘amali yake hukatika isipokuwa ya matatu: Swadaqah endelevu, au ‘ilmu inayopatiwa manufaa, au mtoto mwema anayemwombea)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy, Muslim (1631), At-Tirmidhiy (1376), Abu Daawuwd (3880) na An-Nasaaiy (3651)]
3- Yaliyosimuliwa toka kwa ‘Ubaadah bin Nassiy kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa sallam) amesema:
((من مرض في رمضان فلم يزل مريضا حتى مات لم يطعم عنه، وإن صح فلم يقضه حتى الموت أطعم عنه))
((Mwenye kuugua katika Ramadhwaan na akaendelea kuumwa mpaka akafa, basi hatolishiwa chakula, na kama atapona na hakulipa mpaka akafa, basi atalishiwa chakula)). Hadiyth hii haifai kutumika. [Isnaad yake ni Dhwa’iyf. Imekharijiwa na ‘ Abdul Razzaaq]
4- Hadiyth ya ‘Amrah: ((Kuwa mama yake alikufa akiwa anadaiwa Swiyaam ya Ramadhwaan, akamwambia ‘Aaishah: Je nimlipie? Akasema: ((Hapana, bali mtolee Swadaqah mahala pa kila siku nusu pishi kwa kila masikini)). [Isnaad yake ni Dhwa’iyf. Imekharijiwa na Atw-Twahaawiy katika Al-Mushkil (3/142) na Ibn Hazm katika Al-Muhallaa (4/7)]
Na imesimuliwa toka kwake akisema:
((لا تصوموا عن موتاكم وأطعموا عنهم))
((Msiwafungie maiti wenu bali walishieni chakula)). [Isnaad yake ni Dhwa’iyf sana. Imekharijiwa na ‘Abdul Razzaaq na Al-Bayhaqiy (4/256)]
Wamesema: Naye ndiye aliyesimulia neno lake Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa sallam):
((من مات وعليه صوم، صام عنه وليه))
((Mwenye kufa na anadaiwa Swawm, msimamizi wake atamfungia)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1952) na Muslim (1147)]
Hivyo, Hadiyth inajulisha kuwa lililoamuriwa (na Rasuli) ni kinyume na aliyoyahadithia Bibi ‘Aaishah.
5- Toka kwa Ibn ‘Abbaas amesema: ((Mtu asimswalie mtu, wala mtu asimfungie mtu)). [Isnaad Yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (2918), na kwa Sanad yake Ibn ‘Abdul Barri katika At-Tamhiyd (9/27), na At-Twahaawiy katika Al-Mushkil (6/176)]
Na Ibn ‘Abbaas huyu ndiye msimulizi wa Hadiyth ya kumfungia mama itakayokuja mbeleni.
6- Wameawilisha Hadiyth ya ((صام عنه وليه)) wakisema muradi wake ni kuwa atamfanyia linalowakilisha Swawm, nako ni kulisha chakula!!
An-Nawawiy amesema katika Al-Majmuw’u (6/419) kuwa hii ni taawiyl batilifu ambayo inajibiwa na Hadiyth nyingine.
7- ‘Ulamaa wa Kimaalik wamesema: Walivyofanya watu wa Madiynah ni kinyume ya hayo!!
Ya pili:
Hufungiwa nadhiri zake na hulipiwa Swawm zake bila kizuizi chochote. Ni madhehebu ya Abu Thawr na moja ya kauli mbili za Ash-Shaafi’iy –An-Nawawiy ameikhitari-, Ahlul Hadiyth na Ibn Hazm. [Al-Muhallaa (2/7) na kurasa zinazofuatia), Al-Majmuw’u (6/418) na Al-Fat-h (4/226)]
Dalili zao ni:
1- Hadiyth ya ‘Aaishah kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((من مات وعليه صيام صام عنه وليه))
((Mwenye kufa na anadaiwa Swawm, msimamizi wake atamfungia)). [Hadiyht Swahiyh. Imetajwa nyuma kidogo]
2- Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas ambaye amesema: ((Mtu mmoja alikwenda kwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasema: Ee Rasuli wa Allaah! Hakika mama yangu amekufa naye anadaiwa Swawm ya mwezi, [katika riwaya: Swawm ya nadhiri] je nimlipie? Akasema:
((نعم فدين الله أحق أن يقضى))
((Na’am, deni la Allaah lina haki zaidi kulipwa)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (9153) na Muslim (1148)]
3- Hadiyth ya Buraydah amesema: ((Wakati nilipokuwa nimekaa kwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam), mara akamjia mwanamke mmoja akamwambia: Ee Rasuli wa Allaah! Hakika mimi nilimpa mama yangu Swadaqah ya kijakazi, na yeye amefariki [je nimchukue nimmiliki tena?]. Akasema:
((وجب أجرك، وردها عليك الميراث))
((Ujira wako umethibiti [kwa kumuunga mama yako], na mirathi imemrejesha kwako [kijakazi])). Akasema: Ee Rasuli wa Allaah! Hakika yeye alikuwa anadaiwa Swawm ya mwezi, je nimfungie? Akasema:
((صومي عنها))
((Mfungie)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1149) na At-Tirmidhiy (667)]
4- Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas: ((Kwamba mwanamke mmoja alisafiri baharini, akaweka nadhiri kuwa ikiwa Allaah Atamfikisha salama safari yake, basi atafunga mwezi mzima. Allaah Ta’aalaa Akamfikisha salama safari yake, naye hakufunga mpaka akafariki. Binti yake au dada yake akaenda kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam), na Rasuli akamwamuru amfungie)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (3308) na An-Nasaaiy (3816)]
5- Wamejibu dalili za wenye kuzuia (kufungiwa au kulipiwa Swawm maiti) kwa Neno Lake Ta’aalaa:
((وَأَن لَّيْسَ لِلْإِنسَانِ إِلَّا مَا سَعَىٰ))
((Na kwamba insani hatopata (jazaa) isipokuwa yale aliyoyafanyia juhudi)). [An-Najm (53:39)]
..wakisema kuwa Aliyeiteremsha Aayah hii Ndiye Aliyeiteremsha Aayah:
((مِن بَعْدِ وَصِيَّةٍ يُوصِي بِهَا أَوْ دَيْنٍ))
((baada ya kutoa wasia aliousia (maiti) au kulipa deni)). [An-Nisaa (4:11)]
Na Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) ameiita Swiyaam deni, hivyo imejulikana kuwa muradi ni kwamba mwanadamu hana isipokuwa kile tu alichokifanyia juhudi mwenyewe, na kwa kile ambacho Allaah na Rasuli Wake Wamekihukumia kuwa anakipata pia kutokana na juhudi alizofanyiwa na mwingine, na Swawm ni katika jumla ya hayo.
6- Wameijibu Hadiyth:
((إذا مات ابن آدم انقطع عمله...))
((Anapokufa mwanadamu amali yake hukatika….))..kuwa haihusiana na suala letu hili bali inahusiana na kukatika amali ya maiti, lakini haigusii kukatika amali anayofanyiwa na mtu mwingine wala kukataza hilo.
7- Wamejibu fatwa ya Ibn ‘Abbaas na ‘Aaishah wakisema kuwa athar zilizopokelewa toka kwao zina mzozo, na kama zingekuwa ziko sawa, basi zingekuwa ni hoja kwa yale waliyoyasimuliwa yakiwa Marfuw’u bila haja ya fatwa zao kama ilivyopitishwa katika taaluma ya Uswuwl.
Ya tatu:
Hufungiwa nadhiri tu lakini halipiwi Ramadhwaan. Ni madhehebu ya Ahmad, Is-Haaq, Abu ‘Ubayd na Al-Layth. [Tahdhiyb As-Sunan (7/27) na Al Fat-h (4/228)]
Dalili zao ni:
1- Ni kuwa Hadiyth ya ‘Aaishah ni ya jumla na Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas ni mahususi, na hii ndiyo inayochukuliwa. Na muradi wake unakuwa Swawm ambayo anaifunga msimamizi wa maiti ni Swawm ya nadhiri.
2- Lililothibiti toka kwa ‘Aaishah kuhusu kukataza kwake kumfungia maiti, ni kuwa katazo hilo linahusiana na Swawm ya faradhi tu na si Swawm ya nadhiri kama ilivyotangulia katika athar ya ‘Amrah toka kwa ‘Aaishah isemayo: ((Kuwa mama yake alikufa akiwa anadaiwa Ramadhwaan…)). Inavyoonyesha hapa ni kuwa yeye hakatazi kumfungia maiti nadhiri kwa kutekeleza aliyoyasimulia kutokana na ujumla.
3- Lililothibiti toka kwa Ibn ‘Abbaas –naye ndiye msimulizi wa Hadiyth nyingine kuhusu kumfungia maiti- ni neno lake: ((Mtu akiumwa katika Ramadhwaan kisha akafa bila kufunga, atatolewa chakula na haitokuwa juu yake kulipiwa. Na kama anadaiwa nadhiri, msimamizi wake atamlipia)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2398) na Ibn Hazm (7/7)]
Na bila shaka yeye ndiye ajuaye zaidi maana ya simulizi yake.
4- Fardhi ya Swiyaam inapita mkondo wa Swalaah na kusilimu. Na kama ambavyo mtu hamswalii mtu wala mtu kumsilimia mwingine, ni hivyo hivyo kwa Swiyaam. Na muktadha wa dalili ni kuwa wanachomfanyia maiti baada ya kufa, hakiondoshi dhima yake, hakikubaliwi, na wala hanufaiki kwa kufanyiwa na wengine Fardhi za Allaah zinazompasa.
Ama nadhiri, ni kuwa Allaah kimsingi Hakumlazimisha, bali mtu mwenyewe kajilazimishia, hivyo inakuwa ni kama deni alilolikopa ambalo linaingiliwa na uniaba (kufanyiwa).
Ninasema (Abu Maalik): “Ambalo mimi naona lina nguvu ni kuwa maiti hufungiwa siku anazodaiwa pamoja na nadhiri bila mpaka wala shuruti, kwa kuwa ujumla (katika Hadiyth ya ‘Aaishah) haukhusishwi na mmoja wa watu wake (katika Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas) isipokuwa katika hali ya mkinzano –kama ilivyoelezwa katika taaluma ya Uswuwl-, na hapa hakuna ukinzano. Na kwa ajili hiyo, Al-Haafidh amesema katika Al-Fat-h (4/228): Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas ni picha inayojitegemea ambayo huulizwa kwayo mtu ambaye imemtokea. Ama Hadiyth ya ‘Aaishah, hiyo ni azimio la kanuni jumla”.
Mwisho wa yote haya, tunafahamu kuwa aliyekufa ilhali anadaiwa Swawm, haepukani na moja ya hali tatu:
1- Udhuru wake wa kuilipa Swawm uendelee mpaka afe akiwa hawezi kulipa. Huyu hatodaiwa chochote, wala warithi wake, wala katika mali aliyoiacha; hakuna kufungiwa wala kutolewa chakula. [Al-Majmuw’u (6/414)]
2- Udhuru wake kuondoka na aweze kulipa Ramadhwaan lakini hakulipa mpaka akafa. Huyu atafungiwa.
3- Afe ilhali anadaiwa nadhiri. Huyu atafungiwa na warithi wake.
Faida mbili:
1- Neno lake Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((من مات وعليه صيام، صام عنه وليه))
((Mwenye kufa na anadaiwa Swawm, msimamizi wake atamfungia)), ni habari isiyo kanushi wala amri, lakini ina maana agizi, na taqdiyr yake ni:
((فليصم عنه وليه))
((basi msimamizi wake amfungie)).
Na amri hii ni ya Sunnah si ya waajib kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri kinyume na Ahl Adh-Dhwaahir. [Fat-hul Baariy (4/228)]
Hili linatiliwa nguvu na riwaya ya Al-Bazzaaz isemayo:
((فليصم عنه وليه إن شاء))
((basi msimamizi wake amfungie akipenda)). [Hili lau riwaya hii ni swahiyh,
nayo ni nyongeza isiyopendeza. Angalia Tamaam Al-Minnah (uk. 427)]
Na hili ndilo lenye kuendana na qawaaid, kwani asli ya mambo ni mtu kutokuwa na dhima yoyote juu yake, na kwamba mukallaf halazimiki kufanya yanayohusu dhima ya mwingine isipokuwa kwa dalili bayana.
2- Aliyekufa ilhali anadaiwa Swawm, na akafungiwa na watu kwa idadi ya siku anazodaiwa, basi hilo litajuzu.
Ama kulisha chakula, ikiwa msimamizi wake atakusanya masikini kwa idadi ya siku anazodaiwa na akawashibisha, basi hilo pia litajuzu. Hivyo ndivyo alivyofanya Maalik (Radhwiya Allaah ‘anhu).
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
14-Swiyaam za Sunnah
Alhidaaya.com [3]
[Nimefaidika katika mlango huu kutokana na aliyoyakusanya ndugu yangu mfadhili Usaamah ‘Abdul ‘Aziyz –Allaah Amlipe jaza yake- katika Kitabu chake cha Swiyaamu At-Tatwawwu’i Fadhwaiilu wa Ahkaam]
Sharia imewapa watu utashi na kuwaraghibisha kufunga masiku yasiyo Ramadhwaan ambayo ni:
1- Siku Sita za Shawwaal
Imesuniwa Ramadhwaan ifuatishwe kwa Siku Sita za Shawwaal –si lazima kufuatanisha- kwa kuwa kufunga masiku haya ni sawa na Swiyaam ya mwaka. Toka kwa Abu Ayyuwb Al-Answaariy kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((من صام رمضان، ثم أتبعه ستا من شوال، كان كصيام الدهر))
((Aliyefunga Ramadhwaan, kisha akaifuatishia [siku] Sita za Shawwaal, inakuwa kama Swawm ya mwaka)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1164), Abu Daawuwd (2433), At-Tirmidhiy (759), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (2862) na Ibn Maajah (1716)]
Na bila shaka limekuwa hilo kama Swawm ya mwaka kwa kuwa jema moja hulipwa kwa kumi mfano wake. Na Ramadhwaan ni kwa miezi kumi (siku 300), na sita (za Shawwaal) ni kwa miezi miwili (siku 60). Ni kama inavyoeleza Hadiyth ya Thawbaan toka kwa Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa sallam):
((من صام رمضان، فشهر بعشرة أشهر وصيام ستة أيام بعد الفطر، فذلك تمام صيام السنة))
((Mwenye kufunga Ramadhwaan, basi mwezi ni kwa miezi kumi, na kufunga siku sita baada ya kufungua, basi huko ni kutimia Swiyaam ya mwaka)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Ahmad (5/280), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (2860) na Ibn Maajah (1715)]
‘Ulamaa wengi wakiwemo Ash-Shaafi’iy na Ahmad wamestahabisha kuifunga Sunnah hii. Lakini Abu Haniyfah, Abu Yuwsuf na Maalik, wao wanaona ni karaha kuifunga ili watu wasije kuamini kwamba ni waajib kuandamishia na Ramadhwaan. Ukaraha huu hauna mashiko kwa kuwa unakinzana na Hadiyth Swahiyh bayana. Kisha kuandamiza, bila shaka kumehofiwa mwanzoni mwa mwezi, ama mwishoni mwake, kunakuwa kumetenganishwa kati yake na siku nyingine na siku ya ‘Iyd ambayo haijuzu kufunga. [Sharhu Muslim cha An-Nawawiy (3/238), Sharh Al-‘Umdah (2/556), Al-Mughniy (4/438), Fat-hul Qadiyr (2/349) na Haashiyat ‘Aabidiyn (3/421).
Anayedaiwa siku za kulipa za Ramadhwaan, je afunge Sita Shawwaal kwanza kabla ya kulipa Ramadhwaan?
Linaloonekana kutokana na Hadiyth iliyotangulia ya Abu Ayyuwb ni kuwa kupata fadhila ya thawabu za Swawm ya mwaka, kumeshurutishiwa kuifunga Ramadhwaan (kwanza) kisha kuifuatilishia siku Sita za Shawwaal. Hivyo Swawm ya Sita Shawwaal haitangulizwi kabla ya kulipa Ramadhwaan. [Amelieleza hili Al-‘Allaamah Ibn ‘Uthaymiyn (Rahimahul Laah) kama ilivyo katika Al-Mumti’u (6/448)]
Ninasema: Isipokuwa kama itasemwa kuwa kauli yake (Rasuli):
((ثم أتبعه ستا)) imeendana na mazoea ya watu wengi kufanya hivyo (kufunga mfululizo), na si ilivyofahamika katika Hadiyth. Na kwa msingi huo, inajuzu kufunga Sita Shawwaal kabla ya kulipa Ramadhwaan na hususan kwa yule ambaye amebakiwa na siku chache kabla ya kumalizika Mwezi Shawwaal. Na Hadiyth ya Thawbaan ambayo haikutaja kuandamisha inabeba maana hii. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
2,3 - Swawm ya Muharram, na usisitizo zaidi tarehe tisa na kumi (‘Aashuwraa)
Imestahabiwa kukithirisha kufunga Mwezi wa Muharram kutokana na Hadiyth ya Abu Hurayrah kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((أفضل الصيام بعد رمضان شهر الله المحرم، وأفضل الصلاة بعد الفريضة صلاة الليل))
((Swiyaam bora zaidi baada ya Ramadhwaan ni Mwezi wa Allaah Al-Muharram, na Swalaah bora zaidi baada ya za Faradhi ni Swalaah ya Usiku)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1163) An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (605) na Ibn Maajah (1742)]
Stahabisho linasisitizika katika kufunga tarehe kumi ya Muharram (‘Aashuwraa). Toka kwa Abu Qataadah kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((صيام يوم عاشوراء أحتسب على الله أن يكفر السنة التي قبله))
((Funga Siku ya ‘Aashuwraa, ninataraji kwa Allaah Asamehe [madhambi ya] mwaka ulio kabla yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1162)]
Ibn ‘Abbaas aliulizwa kuhusu funga ya Siku ya ‘Aashuwraa akasema: ((Sikujua kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amefunga siku yoyote anatafuta fadhla zake kuliko masiku mengine yote isipokuwa Siku hii, wala mwezi wowote isipokuwa Mwezi huu, yaani Ramadhwaan)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2006) na Muslim (1132)]
Imestahabiwa kufunga kabla yake tarehe tisa ya Muharram kutokana na Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas aliyesema: ((Wakati Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alipofunga ‘Aashuwraa na akaamuru ifungwe walisema: Ee Rasuli wa Allaah! Hakika hiyo ni Siku ambayo Mayahudi na Manasara wanaitukuza. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasema:
((فإن كان العام المقبل –إن شاء الله- صمنا اليوم التاسع))
((Basi ikiwa mwaka ujao –Akipenda Allaah- tutafunga Siku ya Tisa)).
Akasema: Mwaka ujao haukuja mpaka Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘ alayhi wa aalihii wa sallam) akafariki)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1134)]
Maalik, Ash-Shaafi’iy na Ahmad wamestahabisha kukusanya kati ya Funga ya tarehe tisa na tarehe kumi ya Muharram ili kutojishabihisha na Mayahudi katika kuifunga tarehe Kumi pekee. [Sharh Az-Zarqaaniy (2/237) na Al-Majmuw’u (6/383)]
Angalizo
Baadhi ya ‘Ulamaa wamestahabisha kufunga tarehe kumi na moja kuunganisha na tarehe Tisa na Kumi wakitolea dalili kwa yaliyosimuliwa toka kwa Ibn ‘Abbaas kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((صوموا يوم عاشوراء وخالفوا اليهود، صوموا قبله يوما وبعده يوما))
((Fungeni Siku ya ‘Aashuwraa, na fanyeni kinyume na Mayahudi, fungeni kabla yake siku na baada yake siku)), lakini Hadiyth hii ni Dhwa’iyf sana, haina dalili ya kustahabisha kufunga tarehe kumi na moja. Watu walijue hili. Imekharijiwa na Ahmad (2418), Al-Humaydiy (485), Ibn Khuzaymah (2095) na wengineo.
4- Kukithirisha kufunga katika Mwezi wa Sha’abaan
Hakika Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa akiufunga Mwezi wote isipokuwa siku chache mno. Toka kwa ‘Aaishah amesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anafunga mpaka tunasema hatofungua, na hufungua mpaka tunasema hatofunga, na sikumwona Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amekamilisha kufunga mwezi isipokuwa Ramadhwaan, na sikumwona akifunga zaidi kuliko [anavyofunga] katika Sha’abaan)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1969) na Muslim (1156)]
Angalizo mbili
La kwanza: Kuifanya nusu ya Sha’abaan siku maalumu ya kufunga ni bid’a
Mtu ambaye si ada yake kukithirisha kufunga Sha’abaan, au kufunga Masiku Matatu Meupe, kisha akaja kuifanya tarehe kumi na tano ya Sha’abaan kuwa siku maalum ya kufunga akiitakidi kuwa siku hii ina fadhila maalum, basi kitendo chake hicho ni bid’a, kwa kuwa hakuna Hadiyth yoyote Swahiyh iliyopokelewa toka kwa Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) inayozungumzia fadhila za nusu ya Sha’abaan. Hadiyth zote zilizosimuliwa kuhusu hili ni ima Dhwa’iyf mno au ni za kutengenezwa kama Hadiyth Marfuw’u ya ‘Aliy:
((إذا كانت ليلة النصف من شعبان فقوموا ليلها وصوموا نهارها...))
((Utakapokuwa usiku wa nusu ya Sha’abaan, basi simameni usiku wake na fungeni mchana wake)). [Dhwa’iyf sana. Imekharijiwa na Ibn Maajah (1388)]
La pili: Hakuna katazo lililothibiti kuzuia kufunga baada ya nusu ya Sha’abaan
‘Ulamaa wamekhitalifiana kuhusiana na Swawm ya Sunnah baada ya tarehe kumi na tano ya Sha’abaan. Jumhuri wanasema inajuzu kufunga, lakini ‘Ulamaa wa Kishaafi’iy wanasema ni makruhu wakitolea dalili Hadiyth ya Abu Hurayrah kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((إذا انتصف شعبان فلا تصوموا))
((Ikiingia nusu ya Sha’abaan, basi msifunge)). [Munkar. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2337), At-Tirmidhiy (738), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (2911), Ibn Maajah (1651) na Ahmad (2/442). ‘Abdur Rahmaan bin Mahdiy, Ahmad, Yahyaa bin Mu’iyn, Abu Zar-’ah na wengineo wameikataa Hadiyth hii. Na mimi nimeikosoa katika maelezo yangu kuhusu Kitabu cha Sharhu Al-Bayquwniyyah cha Ibn ‘Uthaymiyn (uk. 22-24). Al-‘Allaamah Al-Albaaniy (Rahimahul Laah) kasema ni Hadiyth Swahiyh!!]
Hadiyth hii ni Dhwa’iyf kwa kauli yenye nguvu. Maimamu ambao kauli zao hazina shaka kuhusiana na jambo hili wameikataa. Hivyo basi, hakuna ubaya mtu kufunga baada ya kuingia nusu ya pili ya Sha’abaan, na hili linatiliwa nguvu na Hadiyth ambazo ni Swahiyh. Ni kama Hadiyth iliyotangulia ya Bi ‘Aaishah kuhusiana na Rasuli (Swalla Allah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kukithirisha sana kufunga Sha’abaan, na Hadiyth ya Abu Hurayrah ya kuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((لا يتقدمن أحدكم رمضان بصوم يوم أو يومين، إلا أن يكون رجل كان يصوم صومه فلبصم ذلك اليوم))
((Asiitangulie kabisa mmoja wenu Ramadhwaan kwa Swawm ya siku moja au siku mbili, isipokuwa awe mtu alikuwa anafunga Swawm yake, basi na aifunge siku hiyo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1914) na Muslim (1082)]
Katika Hadiyth hii, kuna katazo la kufunga siku moja au siku mbili tu za mwisho za Mwezi wa Sha’abaan kwa ajili ya kuchelea ziada katika mwezi mtu akabeba yasiyohusu isipokuwa kama itakuwa ni Swawm ambayo ni ada yake kuifunga, hapo hakuna ubaya. Toka kwa Ummu Salamah amesema: ((Sikumwona Nabiy wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) anafunga miezi miwili mfululizo isipokuwa Sha’abaan na Ramadhwaan)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (726), An-Nasaaiy (4/150), Ibn Maajah (1648) na Ahmad (6/293)]
5- Kufunga Siku ya ‘Arafah kwa wasiohiji
Imestahabiwa kwa asiyehiji afunge Siku ya ‘Arafah. Ni kwa Hadiyth ya Abu Qataadah aliyesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((صيام يوم عرفة أحتسب على الله أن يكفر السنة التي قبله، والسنة التي بعده))
((Swawm ya Siku ya ‘Arafah ninataraji kwa Allaah Asamehe [madhambi ya] mwaka wa kabla yake, na mwaka wa baada yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1162)]
Makusudio ya kusamehewa madhambi ya miaka miwili ni ima Allaah Ta’alaa Anamghufiria madhambi ya miaka miwili [kwa sharti ya kuepuka madhambi makubwa], au Allaah Anamlinda katika miaka hii miwili asifanye ma’asia. [Al-Majmuw’u cha An-Nawawiy (6/381)]
Haistahabiwi kwa Hujaji kufunga ‘Arafah. Hakika ulikuwa ni mwongozo mwema wa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) na Makhalifa wake Waongofu kutofunga Siku ya ‘Arafah huko ‘Arafah. Toka kwa Maymuwnah (Radhwiya Allaah ‘anhaa): ((Kwamba watu walifanya shaka kama Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amefunga Siku ya ‘Arafah. Nikampelekea gilasi ya maziwa –naye amesimama katika kisimamo- akanywa na watu wanaangalia)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1989) na Muslim (1124)]
Ibn ‘Umar aliulizwa kuhusu kufunga Siku ya ‘Arafah huko ‘Arafah akasema: ((Nilihiji pamoja na Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) naye hakuifunga, pamoja na Abu Bakri naye hakuifunga, pamoja na ‘Umar naye hakuifunga, pamoja na ‘Uthmaan naye hakuifunga, na mimi siifungi, na siamuru kuifunga, na wala sikatazi kuifunga)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (751), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (2826) na Ahmad (2/47)]
Ni bora zaidi kwa Hujaji asifunge Siku ya ‘Arafah kwa kufuata alivyofanya Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) pamoja na Makhalifa Wake. Kutofunga kutampa nguvu ya kuomba du’aa na kuleta adhkaar katika kisimamo hiki. Na haya ndiyo madhehebu ya Jumhuri ya ‘Ulamaa. [Al-Majmuw’u (6/380), At-Tamhiyd (21/158), na Sharh Al-‘Umdah cha Sheikh wa Uislamu (2/47)]
6- Swawm ya Jumatatu na Alkhamisi
Toka kwa ‘Aaishah amesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa akijitahidi sana asikose Swawm ya Jumatatu na Alkhamisi)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (745), An-Nasaaiy (2186) na Ibn Maajah (1739)]
Na Usaamah bin Zayd alimuuliza Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kuhusu funga ya Jumatatu na Alkhamisi, na Rasuli akasema:
((ذانك يومان تعرض فيهما الأعمال على رب العالمين ، وأحب أن يعرض عملي وأنا صائم))
((Hizo ni siku mbili ambazo huonyeshwa ‘amali kwa Mola wa walimwengu, nami napenda ‘amali yangu ionyeshwe nikiwa nimefunga)). [Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na An-Nasaaiy (2357), Ahmad (5/201) na Al-Bayhaqiy katika Ash-Shu’ab (3821]
7- Swawm ya Siku Tatu za Kila Mwezi
Toka kwa Abu Hurayrah amesema: ((Ameniusia Rafiki yangu kipenzi (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) [mambo] matatu: Kufunga Siku Tatu za kila Mwezi, rakaa mbili za Adh-Dhuhaa, na niswali Witr kabla ya kulala)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1981) na Muslim (721)]
Na Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwambia ‘Abdullaah bin ‘Amr:
((وصم من الشهر ثلاثة أيام، فإن الحسنة بعشر أمثالها، وذلك مثل صيام الدهر..))
((Na funga katika mwezi siku tatu, kwani hakika jema ni kwa kumi mfano wake, na hiyo ni kama Swiyaam ya mwaka..)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1976) na Muslim (1159)]
Na inastahabiwa yawe masiku Matatu Meupe, nayo ni tarehe 13, 14 na 15 ya kila mwezi kwa neno lake Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((صيام ثلاثة أيام من كل شهر، صبام الدهر، أيام البيض صبيحة ثلاث عشرة وأربع عشرة وخمس عشرة))
((Swiyaam ya Siku Tatu za kila Mwezi ni Swiyaam ya mwaka. Masiku meupe asubuhi ya kumi na tatu, kumi na nne na kumi na tano)). [Hadiyth Swahiyh Lishawaahidih. Imekharijiwa na An-Nasaaiy (2419), Abu Ya’alaa (7504) na At-Twabaraaniy katika Al-Kabiyr (2/2499) toka kwa Jariyj. Ina Hadiyth wenza toka kwa Abu Dharri na Qataadah bin Milhaan]
8- Kufunga siku moja na kula siku moja (Swawm ya Daawuwd ‘Alayhis Salaam)
Hii ndio Swawm bora zaidi, ya kiuwiano zaidi, na inayopendwa zaidi kwa Allaah ‘Azza wa Jalla. Toka kwa ‘Abdullaah bin ‘Amri amesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam amesema:
((أحب الصلاة إلى الله صلاة داود عليه السلام، وأحب الصوم إلى الله صيام داودـ، وكان ينام نصف الليل، ويقوم ثلثه، وينام سدسه، ويصوم يوما ويفطر يوما)) وفي رواية ((وهو أعدل الصيام))
((Swalaah inayopendwa zaidi kwa Allaah ni Swalaah ya Daawuwd ‘Alayhis Salaam, na Swawm inayopendwa zaidi kwa Allaah ni Swiyaam ya Daawuwd, na alikuwa analala nusu ya usiku, na anasimama theluthi yake na analala sudusi yake, na anafunga siku moja na anakula siku nyingine)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1131) na Muslim (1159)]
Na katika riwaya: ((Nayo ndiyo Swawm ya uwiano zaidi)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1976) na Muslim (1159)]
Lakini hili limeshurutishwa kwa ambaye hatopoteza Aliyomwajibishia Allaah kwa sababu ya kufunga, na kama atapoteza faradhi, au ikamshughulisha asiweze kukidhi mahitaji ya mkewe na watoto, basi itakuwa marufuku kwake. [Yamedondolewa haya toka Ash-Sharh Al-Mumti’u cha Ibn ‘Uthaymiyn -Rahimahul Laah- (6/474)]
Faida
Imestahabiwa mtu asiache mwezi kupita bila kufunga Swawm yoyote. Toka kwa ‘Abdullaah bin Shuqayq amesema: “Nilimuuliza ‘Aaishah: Je, Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anafunga mwezi maalum mbali ya Ramadhwaan? Akasema: ((Wal Laah, hakufunga mwezi maalum isipokuwa Ramadhwaan mpaka umalizike, na hakula [mwezi wowote] mpaka afunge sehemu yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1156)]
Hivyo ni mustahabu mtu asiuache mwezi ukapita bila kufunga Swawm yoyote, kwani Swawm za Sunnah hazihusishwi na wakati maalumu, bali mwaka wote unafaa kwa Swawm isipokuwa siku ambazo ni haramu kufunga, ijapokuwa lililo bora zaidi ni kufunga masiku ambayo yamekokotezewa na sharia. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
15-Masuala Kadhaa Kuhusiana Na Swawm Za Sunnah
Alhidaaya.com [3]
1- Kutia niya ya kufunga tokea usiku
Nyuma katika kuzungumzia masharti ya kuswihi Swiyaam, tumeona kwamba madhehebu ya Jumhuri yamejuzisha kuweka niya ya kufunga Swawm ya Sunnah wakati wa mchana kwa ambaye hakula au kunywa na akataka kufunga, na kwamba hakuna sharti ya kutia niya usiku kama ilivyo kwenye Swawm ya Faradhi. Lakini kutia niya hiyo kabla ya Alfajiri inakuwa akiba zaidi.
2- Mwenye kufunga Swawm ya Sunnah ni mfalme wa nafsi yake, akitaka atakamilisha Swawm, na akitaka atakula, na hatolipa.
Aliyeamua kufunga Swawm ya Sunnah, linalopendeza kwake ni kuikamilisha, lakini kama ataona ale, basi afanye hivyo na hatolipa. Yamesemwa haya na Ash-Shaafi’iy na Ahmad. [Al-Majmuw’u (6/393) na Sharhul ‘Umdah]
Wametolea dalili yaliyosimuliwa toka kwa Ummu Haaniy: ((Kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliingia kwangu Siku ya ukombozi wa Makkah, akaletewa kinywaji akanywa, kisha akanipa mimi nikamwambia: Mimi nimefunga. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasema:
((إن المتطوع أمير نفسه، فإن شئت فصومي، وإن شئت فأفطري))
((Mwenye kufunga Swawm ya Sunnah ni mfalme wa nafsi yake, hivyo ukitaka funga, na ukitaka kula)). [Hadiyth Dhwa’iyf. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (732), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (503) na Ahmad (6/341)]
Ninasema: “Hadiyth hii ni Dhwa’iyf, lakini maana yake inatolewa ushahidi na Hadiyth ya Abu Juhayfah aliyesema: ((Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliunga udugu kati ya Salmaan na Abud Dardaa,... Salmaan akamwandalia chakula na kumkaribisha. Akasema Mimi nimefunga. Akasema: Mimi sili mpaka ule, naye akala,… Salmaan akamwambia: Hakika Mola wako Ana haki Yake toka kwako, nafsi yako ina haki yake toka kwako, mke wako ana haki yake toka kwako, basi mpe kila mwenye haki haki (yake). [Abud Dardaai] akamwendea Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akamwelezea hilo. Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akamwambia: ((Salmaan kasema kweli)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy]
Hadiyth hii inatueleza kuwa Abud Dardaai alikula, na Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) hakumwamuru kulipa.
Na Hadiyth ya ‘Aaishah aliyesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliniambia siku moja: ((Ee ‘Aaishah! Je mna chochote? Nikasema: Ee Rasuli wa Allaah, hatuna kitu. Akasema: ((Basi kwa hivyo mimi nafunga)). Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam akatoka, tukaletewa zawadi., au alitujia mgeni. Na wakati aliporudi Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) nilimwambia: Ee Rasuli wa Allaah! Tumeletewa zawadi au ametujia mgeni [na zawadi], nami nimekufichia kidogo. Akauliza: ((Ni nini hicho?)) Nikamwambia ni “hays” [Chakula cha mchanganyo wa samli na tende]. Akasema: Ilete, nikamletea, naye akaila. Kisha akasema: ((Hakika niliamka nikiwa nimefunga)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1154) na imetajwa nyuma]
Na hii ni Hadiyth inayogusia kujuzu kufungua baada ya kutia niya ya kufunga. Na hili limethibiti kwa Asaaniyd Swahiyhah toka kwa Ibn ‘Abbaas, Ibn Mas’uwd, na Jaabir.
Lakini Abu Haniyfah na Maalik wanasema kuwa aliyeamka na Swawm ya Sunnah kisha akala kwa kusudi, basi ni lazima alipe. Wametoa dalili kwa yaliyosimuliwa toka kwa ‘Aaishah kwamba Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwambia yeye na Hafswah walipokuwa wamefunga halafu wakala:
((اقضيا يوما آخر مكانه))
((Lipeni siku nyingine mahala pake)), lakini ni Dhwa’iyf. [Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (735), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (3291) na Ahmad]
Pia wametoa hoja kwa ziada iliyokuja katika Hadiyth ya ‘Aaishah -kuhusiana na kufungua Rasuli baada ya kufunga-, na nyongeza hiyo ni:
((إني كنت أردت الصوم، ولكن أصوم يوما مكانه))
((Hakika mimi nilitaka kufunga, lakini nitafunga siku nyingine mahala pake)), lakini ni Shaadh. [Imekharijiwa na An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (3300), ‘Abdur Razzaaq (7793), Ad-Daaraqutwniy (2/177) na Al-Bayhaqiy (4/275). An-Nasaaiy kasema: Hili ni kosa. Na Al-Bayhaqiy kasema: Kwa ‘Ulamaa ni Hadiyth isiyohifadhiwa]
Wametoa ulinganishi (qiyaas) wa kutimiza Swawm ya Sunnah kwa kutimiza Hajji na ‘Umrah, lakini huu ni ulinganishi wa viwili vinavyotofautiana, kwani mwenye kuiharibu Swalaah yake au Swawm yake, anakuwa ni mwenye kuasi lau atabobea kwenye uharibifu huo. Ama katika Hajji, [ikiwa ataiharibu] basi anaamuriwa aendelee kuifisidi, na haijuzu kwake kutoka kwenye ‘ibaadah hiyo mpaka aitimize ikiwa imeshafisidika, kisha atailipa. Lakini kwa Swawm na Swalaah si hivyo, hazifanyiwi ulinganishi na Hajji. Halafu ulinganishi hapa ni kwa mkabala wa Hadiyth, hivyo hauzingatiwi. [Ameinukulu katika At-Tamhiyd (12/77) toka kwa Ash-Shaafi’iy]
Isitoshe hapa, Qiyaas ni kwa mkabala wa Hadiyth, hivyo haizingatiwi.
3- Je, inajuzu kufunga Swawm ya Sunnah kabla ya kulipa Ramadhwaan?
Tumeshatangulia kusema kuwa madhehebu ya Jumhuri ya Salaf na Khalaf imejuzisha kuchelewesha kulipa Ramadhwaan –kwa aliyekula kutokana na udhuru- bila kushurutisha kuharakia kuilipa mara anapoweza kufanya hilo.
Kisha wakakhitalifiana katika kujuzu kufunga Swawm ya Sunnah kabla ya kulipa Ramadhwaan. Mahanafii na riwaya toka kwa Ahmad wakajuzisha, Wamaalik wakasema ni makruhu, Mashaafi’iy wakastahabisha kulipa kabla ya kufunga Sunnah, na Ahmad kwa riwaya nyingine akasema haijuzu. [Al-Badaai’u (2/104), Mawaahibul Jaliyl (2/417), Al-Majmuw’u (6/375) na Al-Mughniy (4/401)]
Ninasema: “Dalili ya kuzuia kufunga Sunnah kabla ya kulipa Ramadhwaan haiswihi bali inaonyesha kuwa inajuzu. Kwa kuwa Allaah Ta’aalaa Hakuainisha mpaka ya kulipa kwa Neno Lake:
فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ
basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. [Al-Baqarah (2:184)]
Na Hadiyth ya ‘Aaishah inadulisha hilo vile vile aliposema: ((Ilikuwa ninakuwa nadaiwa Swawm ya Ramadhwaan, na siwezi kuilipa isipokuwa katika Sha’abaan)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1950), na Muslim (1146)]
Na hakuna shaka kuwa alikuwa anafunga Swawm za Sunnah katika masiku ya mwaka, na hili alilifanya na Rasuli anajua, na kujua huko ni kulikubali jambo. Kisha kulipa ni wajibu unaofungamana na wakati mkunjufu, hivyo imejuzu kufunga Sunnah katika wakati wake kabla ya kulipa. Ni kama Swalaah ya Sunnah anapoiswali mwanzoni mwa wakati wake [kisha akalipa faradhi]. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
4- Mwanamke humtaka mumewe idhni ya kufunga
Haijuzu kwa mwanamke kufunga Swawm ya Sunnah na mumewe yupo isipokuwa kwa idhini yake. Ni kwa Hadiyth ya Abu Hurayrah toka kwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliyesema:
((لا تصوم المرأة وبعلها شاهد إلا بإذنه))
((Hafungi mwanamke na mumewe yupo ila kwa idhni yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (5192) na Muslim (1026)]
Sababu ya katazo hili ni kuwa mume ana haki ya kustarehe naye nyakati zote, na haki hiyo ni lazima apatiwe haraka. Hivyo haki hiyo isimpite kwa Swawm ya Sunnah au ya Waajib ya kucheleweshwa. [Al-Badaai’u (2/107), Al-Mudawwanah (1/186) na Sharhu Muslim cha An-Nawawiy (3/65)]
Mwanamke mmoja alikwenda kwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasema: “Ee Rasuli wa Allaah! Hakika mume wangu Swafwaan bin Al-Mu’attwal ananipiga nikiswali, ananifunguzisha nikifunga, na haswali Alfajiri mpaka jua lichomoze. Swafwaan akasema: Ee Rasuli wa Allaah! Ama neno lake ananipiga nikiswali, hakika yeye anasoma Suwrah mbili na wewe umetukataza. Akasema (Rasuli): ((Lau ingelikuwa Suwrah moja, basi ingeliwatosha watu)). Ama neno lake ananifunguzisha, hakika yeye anakurupuka tu na kufunga, na mimi ni mtu kijana, siwezi kuvumilia. Siku hiyo Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasema:
((لا تصوم امرأة إلا بإذن زوجها))
((Hafungi mwanamke yeyote ila kwa ruksa ya mumewe)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2459), Ahmad (3/84) na Al-Bayhaqiy (4/303)]
Na ikiwa mumewe hayupo kabisa nyumbani, basi Swawm yake ya Sunnah inajuzu bila makhitalifiano kutokana na Hadiyth ilivyofahamika na kwa kuondoka sababu ya katazo. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi. [Al-Majmuw’u cha An-Nawawiy (6/392)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
16-Masiku Ambayo Imekatazwa Kufunga
Alhidaaya.com [3]
1,2- Siku Mbili Za ‘Iyd Mbili
‘Ulamaa wote bila makhitalifiano wameharamisha kufunga Siku ya ‘Iyd El-Fitwr na Siku ya ‘Iyd El-Adhwhaa kwa hali zote, sawasawa akifunga mtu kwa nadhiri, au Sunnah, au kafara au jinginelo. [Sharhu Muslim cha An-Nawawiy (3/207), Al-Mughniy (4/424) na Fat-hul Baariy (4/281)]
Ni kwa Hadiyth ya Abu ‘Ubayd mwachwa huru wa Ibn Azhar aliyesema: ((Nilishuhudia ‘Iyd pamoja na ‘Umar bin Al-Khattwaab (Radhwiya Allaah ‘anhu) akasema: Siku hizi mbili, Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amekataza kuzifunga: Siku ya kufungua kwenu kutokana na Swiyaam yenu, na Siku nyingine mnakula ndani yake kutokana na nusuki zenu [Hijja])). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1990) na Muslim (1137)]
Na toka kwa Abu Sa’iyd Al-Khudriy (Radhwiya Allaah ‘anhu): ((Kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amekataza kufunga siku mbili: Siku ya Al-Fitwr na Siku ya Kuchinja)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1991) na Muslim (1138)]
3- Masiku ya Tashriyq
[Ni masiku matatu baada ya Siku ya Kuchinja (Siku ya ‘Iyd Al-Adhwhaa), nayo ni Siku ya pili, ya tatu na ya nne ya ‘Iyd Al-Adhwhaa]
Haijuzu kuyafunga masiku haya Swawm ya Sunnah kwa kauli ya ‘Ulamaa wengi. Ni kwa Hadiyth ya Nubayshah Al-Hadhliy aliyesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam amesema):
((أيام التشريق أيام أكل وشرب))
((Masiku ya Tashriyq ni masiku ya kula na kunywa)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1141)]
Na toka kwa Abu Murrah mwachwa huru wa Ummu Haaniy: ((Ni kuwa yeye aliingia pamoja na ‘Abdullaah bin ‘Amri kwa baba yake ‘Amri bin Al-‘Aaswiy, akawasogezea chakula akisema: Karibu. Akasema mimi nimefunga. ‘Amri akasema: Kula, kwani haya ndio masiku ambayo Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anatuamuru tuyalie vyakula, na anatukataza kuyafunga)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2418) na Ahmad (4/197)]
Lakini, Hujaji ambaye hakupata mnyama wa kuchinja anaruhusiwa kufunga katika Masiku haya kama tutakavyoeleza mbeleni. Toka kwa ‘Aaishah na Ibn ‘Umar wamesema: ((Haikuruhusiwa katika Masiku ya Tashriyq kuyafunga ila kwa ambaye hakupata mnyama wa kuchinja)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1997-1998)]
4- Kufunga Siku ya Ijumaa pweke
Haijuzu kufunga Siku ya Ijumaa ila kwa mtu aliyefunga siku moja kabla yake, au siku baada yake, au alikuwa anafunga siku na anakula siku nyingine na Swawm yake ikasadifiana na Ijumaa, basi hakuna ubaya.
Toka kwa Abu Hurayrah (Radhwiya Allaah ‘anhu) amesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((لا يصم أحدكم يوم الجمعة إلا أن يصوم قبله أو يصوم بعده))
((Asifunge mmoja wenu Siku ya Ijumaa isipokuwa akifunga kabla yake au akifunga baada yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1985) na Muslim (1144)]
Na toka kwa Juwayriyah bint Al-Haarith (Radhwiya Allaah ‘anhaa): ((Kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliingia kwake Siku ya Ijumaa na yeye [Juwayriyah] amefunga akamuuliza: Je ulifunga jana? Akasema: Hapana. Akasema: Unataka kufunga kesho? Akasema: Hapana. Akasema: Basi fungua)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1984) na Muslim (1143)]
Na haya ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na Ahmad. Abu Haniyfah na Maalik wamekhalifu hili wakisema kuwa hakuna ukaraha. [Haashiyat Ibn ‘Aabidiyna (3/336), Al-Muwattwa (1/330), Sharhu Muslim (3/210) na Al-Mughniy (4/427)]
Mahanafii wametoa dalili kwa Hadiyth ya Ibn Mas’uwd: ((Kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anafunga siku tatu za mwanzo wa kila mwezi, na ni mara chache mno anafungua Siku ya Ijumaa)). [Isnaad yake ni laini. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2450), At-Tirmidhiy (742), An-Nasaaiy (2367), Ibn Maajah (1725) kupitia kwa ‘Aaswim toka kwa Zarr bin Hubaysh toka kwa Ibn Mas’uwd. Riwaya ya ‘Aaswim toka kwa Zarr ina maneno]
Dai hili linajibiwa na majibu mbalimbali. Kati ya majibu hayo ni kuwa linaloonekana zaidi ni kwamba Hadiyth hii ni Dhwa’iyf, na hata tukijalia kuwa ni Swahiyh, itachukulika kwamba Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anafunga siku moja kabla yake au baada yake pamoja nayo, na dalili haitimii kwa kuwepo uwezekaniko bali uhakika. [At-Talkhiysw (2/216) na Subulus Salaam (2/347)]
Isitoshe, hiki ni kitendo na ile ni kauli, na kauli inatangulizwa kabla ya kitendo kama kuna mgongano na kutowezekana kuoanishwa.
Ama Maalik, -Rahimahul Laah- yeye katazo halijamfikia, na aliyejua hujjah hutangulizwa kabla ya ambaye hakujua.
Faida
Siku ya Ijumaa ikisadiafiana na Siku ya ‘Arafah, basi hakuna ubaya kuipwekesha kwa Swawm, kwani katazo linahusiana na kuikusudia Siku yenyewe ya Ijumaa kwa Swawm. Allaah Ndiye Mjuzi zaidi. [Sharhu Al-‘Umdah (2/6532) na Az Zaad (2/86)]
5- Kufunga Siku ya Shaka
Haijuzu kupokelewa Ramadhwaan kwa kufunga siku moja au mbili kwa nia ya akiba kwa Ramadhwaan, lakini hii ni kwa yule ambaye hakusadifu ada yake, au akawa ameunganisha na siku za kabla yake. Kama hakuunganisha wala hakusadifu ada yake, basi ni haramu. [Ni kama kuwa ada yake kufunga siku moja na kula nyingine, au kufunga siku za jumatatu na alkhamisi na kadhalika]
Ni kwa Hadiyth ya Abu Hurayrah toka kwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliyesema:
((لا يتقدمن أحدكم رمضان بصوم يوم ولا يومين، إلا أن يكون رجل كان يصوم صومه، فليصم ذلك اليوم))
((Asiitangulie kamwe mmoja wenu Ramadhwaan kwa kufunga siku moja au siku mbili, isipokuwa awe mtu alikuwa anafunga Swawm yake, basi na aifunge siku hiyo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1914) na Muslim (1082)]
Na toka kwa ‘Ammaar bin Yaasir amesema: ((Aliyefunga siku ambayo ameifanyia shaka, basi amemwasi Abul Qaasim)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2334), At-Tirmidhiy (681), An-Nasaaiy (4/153) na Ibn Maajah (1645)]
6- Swawm ya Mwaka Mzima
Toka kwa ‘Abdullaah bin ‘Amri kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alipopata habari kuwa yeye anaandamisha Swawm bila kukatiza akamwambia:
((لا صام من ص
ام الأبد، لا صام من صام الأبد، لا صام من صام الأبد))
((Hakufunga aliyefunga siku zote, hakufunga aliyefunga siku zote, hakufunga aliyefunga siku zote)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1977) na Muslim (1159)]
Na katika Hadiyth ya Abu Qataadah: ‘Umar alisema: Ee Rasuli wa Allaah! Vipi kuhusu anayefunga mwaka mzima?: Akasema:
((لا صام ولا أفطر))
((Hakufunga wala hakula)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1162)]
Ni makruhu mtu kufunga mwaka mzima, hata kama hatohisi uzito au udhoofu, na hata kama hakufunga masiku yaliyokatazwa kuyafunga. Akiyafunga basi ni haramu pia. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
Je kuna uhalali wa kufunga Rajab?
Hakuna Hadiyth yoyote Swahiyh toka kwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) wala kwa Swahaba Wake inayozungumzia kuhusu fadhla ya kufunga Rajab. Hadiyth zote zinazozungumzia fadhla hizo ni Dhwa’iyf, bali ni za kutunga na za uongo. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/290), Latwaaiful Ma’aarif (uk. 228), na Subulul Jarraar (2/143)]
Hivyo, haijuzu kuweka azima maalum ya kufunga Rajab au kuufanya mwanzo wake spesheli kwa Swawm. ‘Umar alikuwa anawapiga watu wanaoifunga. Toka kwa Kharshah bin Al-Hurr amesema: ((Nilimwona ‘Umar anapiga viganja vya watu katika Rajab mpaka wanaviweka kwenye madeste, na anawaambia: Kuleni, hakika huu ni mwezi ambao watu wa ujahili walikuwa wanautukuza)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Ibn Abiy Shaybah (3/102) na Ibn Kathiyr katika Musnad Al-Faaruwk (1/285).
Na toka kwa Muhammad bin Zayd amesema: ((Ibn ‘Umar alikuwa anapowaona watu na wanayoyaandaa kwa ajili ya Rajab, basi anachukia hilo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Ibn Abiy Shaybah (3/102)]
Na toka kwa ‘Atwaa amesema: ((Ibn ‘Abbaas alikuwa anakataza kufunga Rajab yote ili isifanywe ‘Iyd)). [Hadiyth Swahiyh. Imekhatijiwa na ‘Abdul Razzaaq (7854)]
Na baadhi ya Wanachuoni wamestahabisha kufunga Rajab kwa kuwa ni katika Miezi Mitukufu. [Al-Majmuw’u (6/386), Muqaddimaat Ibn Rushd (1/242) na Nayl Al-Awtwaar (4/293)]
Ninasema: “Allaah Ta’alaa Ameitaja Miezi Mitukufu kimahususi na Amekataza kufanya dhulma ndani yake kutokana na utukufu wake ingawa dhulma imekatazwa nyakati zote. Allaah Ta’aalaa Anasema:
((إِنَّ عِدَّةَ الشُّهُورِ عِندَ اللَّـهِ اثْنَا عَشَرَ شَهْرًا فِي كِتَابِ اللَّـهِ يَوْمَ خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ مِنْهَا أَرْبَعَةٌ حُرُمٌ ۚذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ ۚ فَلَا تَظْلِمُوا فِيهِنَّ أَنفُسَكُمْ ۚ وَقَاتِلُوا الْمُشْرِكِينَ كَافَّةً كَمَا يُقَاتِلُونَكُمْ كَافَّةً ۚ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ مَعَ الْمُتَّقِينَ))
((Hakika idadi ya miezi mbele ya Allaah ni kumi na mbili katika hukmu ya makadirio ya Allaah, (tangu) siku Aliyoumba mbingu na ardhi. Kati ya hiyo iko minne mitukufu. Hivyo ndiyo Dini iliyo nyoofu. Basi msijidhulumu humo nafsi zenu, na piganeni vita na washirikina wote kama wao wanavyokupigeni vita nyote. Na jueni kwamba Allaah Yu Pamoja na wenye taqwa)). [At-Tawbah (9:36]
Basi hapa imekatazwa kufanya madhambi katika miezi hii kutokana na utukufu wake kwa Allaah Ta’aalaa, na kwamba adhabu inaweza kuwa maradufu kwa madhambi, kama ambavyo malipo huongezwa kwa ‘amali njema. Lakini je, hii ina maana kwamba Miezi hii tu ihusishwe kwa Swawm kati ya miezi mingine iliyobaki, na hasa tukizingatia kuwa hakuna kuhusiana na hili Hadiyth yoyote Swahiyh toka kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam), bali Hadiyth moja tu Dhwa’iyf isemayo kwamba Rasuli alimwambia mtu toka kabila la Baahil:
((صم من الحرم واترك))
((Funga katika Miezi Mitukufu na wacha))? [Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2428), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (2743) na Ahmad (5/28)]
Isitoshe, tafsiyr ya Aayah ina picha nyingine, nayo ni kuwa muradi wa Kauli Yake Ta’aalaa:
فَلَا تَظْلِمُوا فِيهِنَّ أَنفُسَكُمْ
Basi msijidhulumu humo nafsi zenu,
Msiyageuze ya haramu ya miezi hii kuwa halali, wala ya halali kuwa haramu. [Tafsiyr At-Twabariy (6/366)]
Hivyo tunasema, lililothibiti ni kufunga Mwezi wa Muharram kama tulivyobainisha nyuma. Ama Swiyaam ya Rajab na kuufanya mwezi huu kuwa mahsusi kwa funga –na hasahasa pamoja na kuitakidi ubora wake- basi haijuzu.
Lakini kama atafunga baadhi ya masiku ya mwezi huu bila kuwa mwenye kufanya matukuzo ya kijahiliya, na bila kulifanya kuwa hilo ni jambo la lazima, au akatenga mahususi baadhi ya siku zake akafululiza kuzifunga, au nyusiku zake akafululiza kusimama kuswali akiwa na uhakika kuwa hayo ni Sunnah, basi hakuna ubaya. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi. [Angalia Tabyiynul ‘Ajiyb bimaa warada fiy fadhwli Rajab cha Al-Haafidhw Ibn Hajar (uk 70)]
Hukmu ya kuipwekesha Jumamosi kwa Swawm tu
Toka kwa ‘Abdullaah bin Busri toka kwa dada yake kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((لا تصوموا يوم السبت إلا فيما افترض عليكم، وإن لم يجد أحدكم إلا لحاءـ عنبة أو عود شجرة فليمضغه))
((Msifunge Siku ya Jumamosi isipokuwa lile mlilofaradhishiwa, na kama mmoja wenu hakupata isipokuwa gome la mzabibu au kijiti cha mti, basi alitafune)). [Maimamu wamesema ina kasoro. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2421), At-Tirmidhiy (744), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (2762), Ibn Maajah (1726) na Ahmad (6/368). Maalik amesema ni Hadiyth ya uongo. Abu Daawuwd amesema ni Mansuwkh. Al-Haafidh kasema ni Mkorogeko (Mudhwtwarib) [Iliyoelezwa kwa riwaya mbili zinazogongana]. At-Twahaawiy kasema ni Shaadh [iliyoelezewa na mmoja mwenye kuaminika tofauti na wengi wenye kuaminika], na pia Sheikh wa Uislamu na wengineo. Nimeihakiki katika maelezo yangu kuhusu Sharhu Al-Mandhwuwmat Al-Bayquwniyyah cha Ibn ‘Uthaymiyn (uk 24)]
‘Ulamaa wametofautiana kuhusiana na fiqhi ya Hadiyth hii katika kauli mbili:
Ya kwanza:
Inajuzu kufunga Swawm ya Sunnah Siku ya Jumamosi hata kwa kuipwekesha. Ni madhehebu ya Maalik. Na inafahamiwa kutokana na maneno ya Ahmad, na imekhitariwa na Ibn Taymiyyah na Ibn Al-Qayyim. [Al-Inswaaf 3/347), Iqtidhwaau As-Swiraatw Al-Mustaqiym (2/575) na Mukhtaswar As-Sunan (3/298)].
Na hawa wamesema Hadiyth ni Dhwa’iyf na wakaleta badala yake Hadiyth Swahiyh zinazohimizia kufunga ‘Arafah, Sita Shawwaal, ‘Aashuwraa, Siku Tatu Nyeupe, na kufunga siku moja na kula siku nyingine. Hivyo ni lazima siku moja kati ya masiku haya isadifiane na Jumamosi!!
Vile vile Hadiyth ya kufunga siku moja kabla ya Ijumaa au siku moja baada yake, na kauli ya Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kwa Juwayriyyah alipofunga Siku ya Ijumaa:
((أتريدين أن تصومي غدا؟))
((Je wataka kufunga kesho?))… na yote haya tushayaeleza.
Ya pili:
Ni makruhu kuipwekesha Jumamosi kwa Swawm. Ni madhehebu ya Jumhuri; Hanafiy, Shaafi’iy na Hanbal. [Al-Majmuw’u (6/440), Al-Badaai’u (2/79) na Al-Mughniy (4/428)]
Wameichukulia Hadiyth hii kuwa inakataza kuipwekesha Jumamosi kwa Swawm kwa kuwa kufanya hivyo ni kujishabihisha na Mayahudi. Wamelitilia nguvu hili kutokana na yaliyosimuliwa toka kwa Ibn ‘Abbaas ya kwamba Ummu Salamah alisema: ((Hakika Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa akikithirisha zaidi kufunga kati ya masiku siku ya Jumamosi na siku ya Jumapili)). Alikuwa anasema:
((إنهما عيدان للمشركين وأنا أريد أن أخالفهم))
((Hakika siku hizi mbili ni sikukuu kwa Mapagani, na mimi nataka kwenda kinyume nao)). [Hadiyth Dhwa’iyf. Imekharijiwa na An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (2776), Ahmad (6/323) na wengineo kwa Sanad Dhwa’iyf]
Ninasema: “Ama Hadiyth ya ‘Abdullaah bin Busr, tumeona Maimamu wengi wameikosoa. Na juu ya msingi huo, hakuna ubaya kuifunga Jumamosi na hususan ikisadifiana na siku ambayo imesuniwa kisharia kuifunga. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi”.
Ni makruhu kufunga mfululizo bila kupumzika
Ni makruhu kuandamisha Swawm na kufululisha masiku bila kula au kula daku. Ni kutokana na neno lake Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((إياكم والوصال)) -قالها ثلاث- قالوا: إنك تواصل يا رسول الله؟ قال: ((إنكم لستم في ذلك مثلي، إني أبيت يطعمني ربي ويسقيني، فاكلفوا من الأعمال ما تطيقون))
((Hadharini na kufunga bila kufungua)) –alilisema mara tatu- Wakasema: Hakika wewe unafunga bila kufungua ee Rasuli wa Allaah? Akasema: ((Hakika nyinyi hamko kama mimi katika hilo. Hakika mimi ninalala na Mola wangu Ananilisha na Ananinywesha, basi bebeni katika ‘amali mnazoziweza)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1966) na Muslim (1103) toka kwa Abu Hurayrah]
Lakini, ikiwa hakuna tabu au uzito, basi hakuna ubaya kuendelea na Swawm mpaka wakati wa daku tu. Ni kwa neno lake (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((لا تواصلوا، فأيكم أراد أن يواصل فليواصل إلى السحر))
((Msiendelee na Swawm bila kufungua, na yeyote akipenda kuendelea na Swawm bila kufungua, basi aendelee hadi daku)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1967) na Abu Daawuwd (2344)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
17-Laylatul-Qadr Na Fadhila Zake
Alhidaaya.com [3]
Allaah Ta’aalaa Amesema:
بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ
إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةِ الْقَدْرِ ﴿١﴾
Hakika Sisi Tumeiteremsha Qur-aan katika Laylatil-Qadr (usiku wa Qadar).
وَمَا أَدْرَاكَ مَا لَيْلَةُ الْقَدْرِ ﴿٢﴾
Na nini kitakachokujulisha ni nini huo Laylatul-Qadr?
لَيْلَةُ الْقَدْرِ خَيْرٌ مِّنْ أَلْفِ شَهْرٍ ﴿٣﴾
Laylatul-Qadr ni mbora kuliko miezi elfu.
تَنَزَّلُ الْمَلَائِكَةُ وَالرُّوحُ فِيهَا بِإِذْنِ رَبِّهِم مِّن كُلِّ أَمْرٍ ﴿٤﴾
Wanateremka humo Malaika na Ar-Ruwh (Jibriyl) kwa idhini ya Rabb wao kwa kila jambo.
سَلَامٌ هِيَ حَتَّىٰ مَطْلَعِ الْفَجْرِ ﴿٥﴾
Amani mpaka kuchomoza Alfajiri. [Al-Qadr: 1-5]
Suwrat hii Tukufu imepangilia fungu la fadhwaail za Usiku huu kama ifuatavyo: [At Tas-hiyl litaawiyl At-Tanziyl cha Sheikh wetu Mustwafaa Al-‘Adawiy (Juz-u ‘Amma (2/448)]
1- Kwamba Allaah ‘Azza wa Jalla Ameiteremsha Qur-aan katika Usiku huu kama Alivyosema Ta’aalaa:
إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةٍ مُّبَارَكَةٍ ۚ إِنَّا كُنَّا مُنذِرِينَ﴿٣﴾
Hakika Sisi Tumeiteremsha (Qur-aan) katika usiku uliobarikiwa, hakika Sisi daima ni Wenye kuonya. [Ad-Dukhaan (44:3)]
2- Kwamba Allaah ‘Azza wa Jalla Ametukuza shani yake kwa kuutaja na kwa Neno Lake:
((وَمَا أَدْرَاكَ مَا لَيْلَةُ الْقَدْرِ))
Na nini kitakachokujulisha ni nini huo Laylatul-Qadr?
3- Kwamba ‘ibaadah ndani ya Usiku huu inashinda ‘ibaadah katika miezi elfu moja isiyo na Laylatul Qadr ndani yake.
4- Kwamba Malaika Huteremka makundi kwa makundi katika Usiku huu. Imesemwa: Wanateremka na rahmah nyingi, baraka nyingi na utulivu. Imesemwa: Wanateremka na kila jambo ambalo Allaah Amelihukumu na Amelikadiria kwa mwaka huo kama Alivyosema:
فِيهَا يُفْرَقُ كُلُّ أَمْرٍ حَكِيمٍ﴿٤﴾
Katika (usiku) huo hupambanuliwa kila jambo la hikmah.
أَمْرًا مِّنْ عِندِنَا ۚ إِنَّا كُنَّا مُرْسِلِينَ﴿٥﴾
Ni amri kutoka Kwetu, hakika Sisi ndio Wenye kutuma (Rusuli). [Ad-Dukhaan (44:4,5]
5- Kwamba amani na utulivu hutanda katika Usiku huu kwa watu wa iymaan, na salamu za Malaika huandamana juu yao ndani ya Usiku huu.
6- Toka kwa Abu Hurayrah toka kwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((من صام رمضان إيمانا واحتسابا غفر له ما تقدم من ذنبه، ومن قام ليلة القدر إيمانا واحتسابا غفر له ما تقدم من ذنبه))
((Mwenye kufunga Ramadhaan kwa iymaan na kutaraji malipo, hughufiriwa madhambi yake yaliyotangulia. Na mwenye kusimama [kufanya ‘ibaadah katika] Laylatul Qadr kwa iymaan na kutarajia malipo, hughufiriwa madhambi yake yaliyotangulia)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2014) na Muslim (759)]
Usiku Huu Ni Upi [Unakuwa Tarehe Ngapi]?
Hakuna shaka yoyote kwamba Laylatul Qadr iko katika Ramadhwaan kwa Neno Lake Ta’aalaa:
((إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةِ الْقَدْرِ))
((Hakika Sisi Tumeiteremsha [Qur-aan] katika Laylatil-Qadr [usiku wa Qadar])). [Al-Qadr (97:1)]
..pamoja na Kauli Yake Ta’aalaa:
((شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِي أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ ))
((Mwezi wa Ramadhwaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan)). [Al-Baqarah (2:185)]
Ama kuuainisha, Al-Haafidh Ibn Hajar amesema: “’Ulamaa hakika wamekhitalifiana makhitilafiano mengi sana kuhusu Laylatul Qadr, na tumepata katika hilo zaidi ya kauli 40 katika madhehebu zao”. [Kisha akazitaja kauli hizo na dalili walizotoa watu wake]. [Fat-hul Baariy (4/309 - Salafiyyah].
Na wengi wao wamesema unapatikana katika Kumi la Mwisho la Ramadhwaan kwa Hadiyth ya Abu Sa’iyd Al-Khudriyy kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘ alayhi wa aalihii wa sallam) amesema):
((....فابتغوها في العشر الأواخر))
((..basi upanieni katika Kumi la Mwisho)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2018) na Muslim (1167) toka kwa Abu Sa’iyd[
Na wengi wao pia wamesema unapatikana katika (hesabu ya) witri katika Kumi la Mwisho kutokana na neno lake Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((نحروا ليلة القدر في الوتر من العشر الاواخر))
((Itafuteni Laylatul Qadr katika witr ya Kumi la Mwisho)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2017)]
Na wengi wao kadhalika wamesema ni Usiku wa tarehe 27, na hii ni kauli ya kundi la Swahaba. Ubayya bin Ka’ab ameikata kauli hii kuwa haina shaka na ameiapia kama ilivyo katika Swahiyh Muslim. [Swahiyh Muslim (762) na At-Tirmidhiy (3351)]
Ninasema: “Ninaloliona mimi ni kuwa Laylatul Qadr hupatikana katika Kumi la Mwisho, na katika masiku ya witri inakuwa na uhakika zaidi, nayo huhama ndani ya masiku hayo, na haihusiani tu na Usiku wa tarehe 27, kwani yaliyosimuliwa toka kwa Ubayya kuwa ni Usiku wa tarehe 27, hilo ni katika mwaka mmoja tu na haina maana kuwa kila mwaka itakuwa ni 27. Lidulishalo hili ni kuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliisadifu Laylatul Qadr Usiku wa tarehe 21 kama ilivyo katika Hadiyth ya Abu Sa’iyd kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliwakhutubia na kuwaambia:
((إني أريت ليلة القدر ثم أنسيتها، فالتمسوها في العشر الأواخر في الوتر، وإني رأيت أني أسجد في ماء وطين))
((Hakika mimi nilionyeshwa Laylatul Qadr kisha nikasahaulishwa, basi itafuteni katika Kumi la Mwisho katika witr, na hakika mimi nimeona kwamba mimi nasujudu katika maji na udongo))… Abu Sa’iyd amesema: ((Tulipata mvua usiku wa ishirini na moja, na paa la Msikiti likatona maji sehemu anayoswalia Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam), nikamwangalia na yeye ametoka kwenye Swalaat As-Subh na uso wake umelowa udongo na maji)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2018) na Muslim (1167)]
Na hili ndilo linalodulishwa na jumla ya habari zilizokuja kuhusu hilo. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi”.
Kufichwa Laylatul Qadr
Bila shaka Laylatul Qadr imefichwa ili waja wajitahidi kufanya ‘ibaadah katika kila usiku wa Ramadhwaan kwa matarajio ya kuwa usiku wowote unaweza kuwa ndio wa Laylatul Qadr. Basi atakayekuwa na habari ya yakini katika usiku wowote, basi ataukeshea kwa ‘ibaadah, na anayetaka kuusadifu na kuupata kiuhakika, basi ni juu yake amshukuru Allaah kwa kujifaraghisha Kwake kwa ‘ibaadah katika Mwezi wote. Na hii ndio siri ya kutotajwa siku maalum ya kupatikana kwake. Na huenda hili linaashiriwa na neno lake Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((إني خرجت لأخبركم بليلة القدر، فتلاحى فلان وفلان، فرفعت [يعنى: رفع علمها]، وعسى أن يكون خيرا لكم، فالتمسوها...))
((Hakika mimi nilitoka niwahabarisheni [siku maalum ilioainishwa ya] Laylatul Qadr, fulani na fulani wakazozana, basi ikaondoshwa [yaani, kuijua kwake kukaondoshwa], na huenda ikawa kheri kwenu, basi utafuteni…)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2023)]
Vipi Muislamu anajitahidi kuipata Laylatul Qadr?
Mwenye kukoseshwa asiupate Usiku huu wa Baraka, basi amekoseshwa kheri yote, na hakoseshwi kheri yake isipokuwa mkoseshwa. Na kwa ajili hiyo, inatakikana kwa Muislamu mwenye pupa ya kumfanyia twa’a Allaah, aukeshe Usiku huo akiwa na iymaan na tamaa ya kupata malipo yake makubwa, na ajitahidi zaidi katika Kumi la Mwisho kufuata alivyofanya Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam). Toka kwa ‘Aaishah amesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anajitahidi asivyojitahidi katika masiku mengine)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1174)]
Anapaswa akithirishe Swalaah katika Usiku huu, ajitenge na wanawake na awahimize ahli wake kufanya twa’a ndani yake. Toka kwa ‘Aaishah amesema: ((Alikuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) linapoingia Kumi [la Mwisho], hujiandaa na kujitahidi ukomo wa jitihada, hukesha usiku wake, na huwaamsha wakeze)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2024) na Muslim (1174)]
Na haya yote ili awe na uhakika wa kupata yaliyoahidiwa na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliyesema:
((من صام رمضان إيمانا واحتسابا، غفر له ما تقدم من ذنبه))
((Atakayefunga Ramadhwaan kwa iymaan na kutarajia malipo [toka kwa Allaah], hughufiriwa dhambi zake zilizotangulia)). [Hadiyth Swahiyh. Imetajwa nyuma kidogo]
Du’aa katika Laylatul Qadr
Imestahabiwa kuomba du’aa katika Usiku huo na kukithirisha na hususan du’aa iliyokuja katika Hadiyth ya ‘Aaishah aliyesema:
((يا رَسُولَ اللهِ، أرَأيْتَ إنْ عَلِمْتُ أيُّ لَيْلَةٍ لَيْلَةُ الْقَدْرِ، مَا أقُولُ فِيها؟ قَالَ: ((قُولي: اللَّهُمَّ إنَّكَ عَفُوٌّ كَرِيمٌ تُحِبُّ العَفْوَ فَاعْفُ عَنِّي)).
((Ee Rasuli wa Allaah! Nieleze ikiwa nitajua usiku fulani ndio wa Laylatul Qadr, niseme nini?” Akasema: ((Sema:
اللَّهُمَّ إنَّكَ عَفُوٌّ كَرِيمٌ تُحِبُّ العَفْوَ فَاعْفُ عَنِّي
Ee Allaah! Hakika wewe ni Mwingi wa kufuta kabisa madhambi, Mwingi wa ukarimu, Unapenda kufuta kabisa madhambi, basi Nifutie kabisa dhambi zangu)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (3760) na Ibn Maajah (3850)]
Alama za Laylatul Qadr
Laylatul Qadr ina alama ambazo hujulikana kwazo. Kati ya alama hizo ni zile ambazo hupatikana katika Usiku wenyewe kama:
1- Anga kuwa safi na upepo kutulia. Toka kwa Ibn ‘Abbaas amesema: “Amesema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((ليلة القدر ليلة سمحة، طلقة لا حارة ولا باردة، تصبح الشمس صبيحها ضعيفة حمراء))
((Laylatul Qadr ni Usiku mtulivu mwangavu, si wa joto wala baridi, jua asubuhi yake hupambauka dhaifu jekundu)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na At-Twayaalsiy (349), Ibn Khuzaymah (3/231) na Al-Bazzaar (1034)]
2- Utulivu na ushwari ambao Malaika huteremka nao. Mwanadamu huhisi utulivu wa moyo, hukikuta kifua chake kikikunjuka, na huhisi ladha ya ‘ibaadah katika Usiku huu ambayo haipati katika masiku mengineyo.
3- Mtu anaweza kuiona usingizini kama ilivyotokea kwa baadhi ya Swahaba.
Kati ya alama ambazo huonekana baada ya Usiku huo kupita ni kama:
4- Jua kuchomoza asubuhi yake likiwa safi bila miale. Toka kwa Ubayya bin Ka’ab kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((صبيحة ليلة القدر تطلع الشمس لا شعاع لها، كأنها طست، حتى ترتفع))
((Asubuhi ya Laylatul Qadr jua huchomoza bila miale [umbo lake] mithili ya kikaangio mpaka linyanyuke)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1174)]
Angalizo
Watu wa kawaida wana visa vingi sana vya uongo vilivyojazwa chumvi kuhusiana na Laylatul Qadr pamoja na itikadi nyingi mbovu. Kati ya itikadi hizo ni kuwa katika Usiku huo miti husujudu, majengo hulala, maji chumvi hugeuka maji tamu, mbwa hawabweki na mengineyo yaliyo bayana ubovu wake na ubatilifu wake.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Swiyaam
18-I’tikaaf
Alhidaaya.com [3]
Maana Yake
Ni kulikalia jambo. Aliyejifungia Msikitini na kukaa humo kwa ajili ya ‘ibaadah hujulikana kama mkaaji I’tikaaf معتكف) au (عاكف [Al-Miswbaah Al-Muniyr (2/424) na Lisaan Al-‘Arab (9/252)]
Dalili ya uthibitifu wake
Imestahabiwa kukaa I’tikaaf katika Mwezi wa Ramadhwaan. Ni kwa Hadiyth ya Abu Hurayrah aliyesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anakaa I’tikaaf katika kila Ramadhwaan siku kumi, na ulipokuwa mwaka ambao alifariki, alikaa I’tikaaf siku ishirini)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2044).
I’tikaaf bora zaidi ni ya mwisho wa Ramadhwaan kutokana na yaliyothibiti toka kwa ‘Aaishah kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anakaa I’tikaaf Kumi la Mwisho la Ramadhwaan mpaka Allaah ‘Azza wa Jalla Alipomfisha. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2026) na Muslim (1172)]
Na imethibiti pia kuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikaa I’tikaaf siku kumi za mwisho za Shawwaal kwa ajili ya kulipa I’tikaaf ya Ramadhwaan, kwa kuwa hakukaa masiku hayo I’tikaaf katika Ramadhwaan. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2041) na Muslim (1174)]
Ikiwa mtu ameweka nadhiri ya kukaa I’tikaaf siku moja au zaidi, basi ni lazima atekeleze nadhiri yake. Toka kwa ‘Umar bin Al-Khattwaab kwamba alimwambia Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam): “Ee Rasuli wa Allaah! Hakika mimi nilikuwa nimeweka nadhiri enzi ya ujahilia ya kukaa usiku mmoja I’tikaaf ndani ya Al-Masjid Al-Haraam”. Rasuli akamwambia:
((فأوف بنذرك [فاعتكف ليلة]..))
((Basi tekeleza nadhiri yako [Akakaa I’tikaaf usiku mmoja]..)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2042) na Muslim (1656)]
I’tikaaf haifanywi ila ndani ya Msikiti
Ni kwa Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَلَا تُبَاشِرُوهُنَّ وَأَنتُمْ عَاكِفُونَ فِي الْمَسَاجِدِ))
((Na wala msiwaingilie hali ya kuwa nyinyi ni wenye kukaa i’tikaaf Misikitini)). [Al-Baqarah (2:187)]
Na kwa vile Msikiti ulikuwa ndio sehemu ambayo Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii sallam) alifanyia I’tikaaf na wakeze vile vile. Na kama ingekuwa inafaa kufanya I’tikaaf mahala pengine, basi wakeze Rasuli wasingefanya I’tikaaf kwenye Msikiti ambapo kuna uzito wa kuweka kambi humo. Na kama ingekuwa inafaa nyumbani, basi wangefanyia humo ijapokuwa mara moja.
Jumhuri ya ‘Ulamaa wanasema I’tikaaf inafaa katika Misikiti yote –ingawa wamekhitalifiana katika kushurutisha kama ni Msikiti Mkubwa "جامع" au mfano
wake- kutokana na ujumuishi wa Kauli Yake Ta’aalaa: فِي الْمَسَاجِدِ
Watu wamesema: Hakuna I’tikaaf isipokuwa katika Misikiti Mitatu: Al-Masjidul Haraam, Al-Masjid An-Nabawiy na Al-Masjid Al-Aqswaa. Hili limesemwa na Hudhayfah na Sa’iyd. [Bidaayatul Mujtahid (1/466)]
Madhehebu ya Jumhuri ndio yenye nguvu zaidi. Ama yanayosimuliwa kwa njia Marfu’u toka kwa Hudhayfah:
((لا اعتكاف إلا في المساجد الثلاثة))
((Hakuna I’tikaaf isipokuwa katika Misikiti Mitatu)). [Imekharijiwa na Al-Bayhaqiy (4/316), na Ismaa’iyl kama ilivyo katika Mu’ujamu Shuyuukhihii (3/721), Adh-Dhahabiy katika As-Siyar (5/81), Ibn Al-Jawziy katika At-Tahqiyq (1181) kupitia kwa Ibn ‘Uyaynah toka kwa Jaami’i bin Abiy Raashid toka kwa Abu Waail toka kwa Hudhayfah ikiwa Marfu’u. Ibn ‘Uyaynah amezozaniwa kwa kuisimulia kwa ‘Abdul Razzaaq (8016), na kupitia kwake At-Twabaraaniy (6/301-302) kwa Sanad yake toka kwa Hudhayfah ikiwa Marfuw’u. Ibraahiym ameifuatilia toka kwa Hudhayfah ikiwa Mawquwf kwa ‘Abdul Razzaaq (8014) na At-Twabaraaniy (9/301)]
‘Ulamaa wamekhitalifiana kuhusiana na kuwa Marfuw’u au Mawquwf.
Wanawake wanaruhusika kukaa I’tikaaf kwa masharti mawili:
Wanawake wanaruhusiwa kufanya I’tikaaf. Toka kwa ‘Aaishah kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alidokeza kuwa atafanya I’tikaaf Kumi la Mwisho la Ramadhwaan. ‘Aaishah akamwomba ruksa, naye akamruhusu. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2045) na Muslim (1172)]
‘Aaishah amesema tena: ((Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anakaa I’tikaaf katika Kumi la Mwisho la Ramadhwaan mpaka Allaah Ta‘aalaa Alipomfisha, kisha wakeze walikaa baada yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2026) na Muslim (1172)]
Kuna masharti mawili ya mwanamke kukaa I’tikaaf:
La kwanza: Apate ruksa ya mumewe
Kwa kuwa hatoki nyumbani kwake ila kwa idhini ya mumewe. Hadiyth ya ‘Aaishah iliyopita inaeleza kuwa alimwomba ruksa Rasuli kwa ajili ya I’tikaaf, pia Hafswah na Zaynab walifanya hivyo.
Faida
Mume akimruhusu mkewe kukaa I’tikaaf, je anaweza kumtoa asiendelee?
- Ikiwa I’tikaaf ni ya Sunnah, basi mume ana haki ya kumtoa, kwani Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa sallam) wakati ‘Aaishah alipomwomba ruksa ya kukaa I’tikaaf, kisha akamfuatia Hafswah halafu Zaynab, (Rasuli) alihisi kuwa hawana hasa niya ya kukaa I’tikaaf bali wanataka tu kuwa karibu naye kutokana na wivu wao kwake, akawatoa na kusema:
((...آلبر أردن؟ ما أنا بمعتكف..))
((..Je, wamekusudia [kweli] kupata thawabu? Mimi sikai I’tikaaf..)). [Hadiyth Swahiyh.]
- Ikiwa I’tikaaf yake ni ya waajib (kama ya nadhiri kwa mfano), na nadhiri ikawa ya kufatanisha siku (ameweka nadhiri I’tikaaf ya Kumi la Mwisho) na mumewe akamruhusu, basi hatokuwa na haki ya kumtoa. Na kama hakushurutisha kufuatanisha katika nadhiri yake, basi anaweza kumtoa kisha baadaye akakamilisha nadhiri yake. [Al-Majmuw’u cha An-Nawawiy (6/476)]
La pili: I’tikaaf yake isiwe sababu ya fitnah
Mwanamke atafanya I’tikaaf madamu hakuna fitnah. Na kama fitnah itamtokea yeye au kwa wanaume kutokana na I’tikaaf yake, basi atazuiwa na hatoruhusiwa, kwani Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliwazuia wakeze kukaa I’tikaaf kwa lisilo hilo kama ilivyotangulia katika Hadiyth ya ‘Aaishah.
Je ni sharti mtu afunge Swawm ndio akae I’tikaaf?
[Faida ya hili mahala pake: Akikaa I’tikaaf kwa isiyo Ramadhwaan kwa ajili ya nadhiri au mfano wake, au alikuwa akila Ramadhwaan kutokana na udhuru na akataka kukaa I’tikaaf]
‘Ulamaa wamekhitalifiana katika suala hili kwa kauli mbili:
Ya kwanza: I’tikaaf haifai bila Swawm
Ni madhehebu ya Abu Haniyfah, Maalik na Ahmad katika moja ya riwaya zake mbili, nayo imesimuliwa toka kwa ‘Aaishah, Ibn ‘Abbaas na Ibn ‘Umar. [Bidaayatul Mujtahid (1/470) na Tahdhiyb As-Sunan (7/104-109)]
Dalili zao ni:
1- Kuwa Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikaa I’tikaaf katika Mwezi wa Ramadhwaan, na uthibiti wa I’tikaaf haukujulikana ila kwa Swawm, na haikuthibiti toka kwa Nabiy wala kwa yeyote katika Swahaba Zake kuwa walikaa I’tikaaf bila Swawm.
2- Ni kutajwa kwa pamoja I’tikaaf na Swawm katika Aayah moja.
3- Ni Hadiyth ya ‘Aaishah aliyesema: ((Sunnah kwa mwenye kukaa I’tikaaf asimzuru mgonjwa, asiende kuzika, asimguse mwanamke wala asimwingilie, na wala asitoke kwa haja yoyote isipokuwa ya dharura, na hakuna I’tikaaf isipokuwa kwa Swawm, na hakuna I’tikaaf isipokuwa katika Msikiti Mkubwa)). Imesimuliwa toka kwake ikiwa Marfu’u lakini si Swahiyh. [Isnaad yake ni Jayyid. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (2473) na Al-Bayhaqiy (4/315). Kuna mvutano kuhusiana na kuthibiti neno lake “Sunnah”, bali Ad-Daaraqutwniy amekata kuwa tamko lote limeandikwa toka kwenye maneno ya Az-Zuhriy, lakini Al-Albaaniy amemjibu katika Al-Irwaa (4/140)]
Ya pili: Si sharti Swawm kwa ajili ya I’tikaaf bali imestahabiwa
Ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na Ahmad –katika kauli yake mashuhuri- nayo imesimuliwa toka kwa ‘Aliy na Ibn Mas’uwd. Dalili zao ni:
1- Kuwa ‘Umar alimwambia Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam): “Ee Rasuli wa Allaah! Hakika mimi nilikuwa nimeweka nadhiri enzi ya ujahilia ya kukaa usiku mmoja I’tikaaf ndani ya Al-Masjid Al-Haraam”. Rasuli akamwambia:
(فأوف بنذرك [فاعتكف ليلة]..))
((Basi tekeleza nadhiri yako [Akakaa I’tikaaf usiku mmoja]..)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2042) na Muslim (1656)]
Wamesema: Usiku si mahala pa Swawm, na (Rasuli) amejuzisha kufanya I’tikaaf wakati huo.
2- Katika riwaya ya Hadiyth ya ‘Aaishah iliyotangulia –kuhusiana na I’tikaaf za wakeze Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam)- akasema Rasuli alipoona vijihema vya wakeze:
((آلبر تردن))
((Je, mmekusudia [kweli] kupata thawabu?)). Akaamuru kijihema chake kivunjwe, akaacha I’tikaaf katika Mwezi wa Ramadhwaan, na akaja kuifanya mwanzoni mwa Mwezi wa Shawwaal)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim kwa tamko hili (1172)]
Wamesema: Na Shawaal mosi ni siku ya kula, si halali kufunga.
3- Yaliyosimuliwa Marfu’u toka kwa Ibn ‘Abbaas:
((ليس على المعتكف صيام إلا أن يجعله على نفسه))
((Si lazima kwa mwenye kukaa I’tikaaf Swawm ila tu kama atajilazimishia Swawm mwenyewe)). Hadiyth hii ni Dhwa’iyf. [Imekharijiwa na Al-Haakim (1/605), Al-Bayhaqiy (4/318) na Ad-Daaraqutwniy (2/199) kwa Sanad Dhwa’iyf]
4- I’tikaaf ni ‘ibaadah inayojitegemea yenyewe, hivyo si sharti Swawm iwe ndani yake kama ‘ibaadah nyinginezo.
5- I’tikaaf ni kubakia sehemu maalum kwa ajili ya kumfanyia twa’a Allaah, hivyo Swawm si sharti iwe kiunganishi chake.
Ninasema: “Linaloonekana kuwa na nguvu ni kwamba si sharti Swawm ili I’tikaaf ifanyike, bali imestahabiwa. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi”.
Muda wa chini zaidi wa I’tikaaf
[Bidaayatul Mujtahid (1/468) na Fat-hul Baariy (4/319)]
Jumhuri ya ‘Ulamaa wakiwemo Abu Haniyfah na Ash-Shaafi’iy wanasema kwamba hakuna mpaka wa chini wa muda wa kukaa I’tikaaf. Maalik kasema uchache wake ni mchana na usiku, na imepokewa toka kwake siku tatu, na imepokewa pia toka kwake siku kumi.
Linaloonekana ni kuwa mwenye kushikilia kwamba sharti ya I’tikaaf ni Swawm, basi haijuzu kwake kufanya I’tikaaf usiku. Hivyo hana cha uchache wa mchana na usiku kwa kuwa muda wake wa I’tikaaf ni mchana tu.
Ninasema: “Linaloonekana kuwa na nguvu ni kuwa uchache wake ni usiku mmoja kutokana na Hadiyth ya ‘Umar wakati Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alipomwamuru atekeleze nadhiri yake, akakaa usiku mmoja. Hili limeelezwa nyuma. Ama kauli ya Jumhuri isemayo kuwa inatosha chini ya usiku mmoja hata kitambo kidogo cha usiku na mchana, hili linahitaji dalili”.
Ni wakati gani anaingia mahala pa kufanyia I’tikaaf na wakati gani anatoka?
Mwenye kuweka nadhiri kukaa I’tikaaf siku za kuhesabika, au akataka kukaa I’tikaaf siku kumi za mwisho za Ramadhwaan, basi ni Sunnah aingie sehemu ya kufanyia I’tikaaf baada ya Swalaat Al-Fajr mwanzoni mwa masiku haya (ishirini na moja). Hivi ndivyo alivyofanya Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam). Katika Hadiyth ya ‘Aaishah (Radhwiya Allaah ‘anhaa): ((Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anakaa I’tikaaf katika Kumi la Mwisho la Ramadhwaan. Nilikuwa nikimfungia kijihema, akaswali As-Subhi, kisha akaingia ndani yake…)). [Hadiyth Swahiyh. Imetajwa nyuma]
Hii ni kauli ya Al-Awzaa’iy, Al-Layth na Ath-Thawriy.
Maimamu wanne na kundi jingine la ‘Ulamaa wanasema kuwa ataingia muda mchache kabla ya kuchwa jua (tarehe 20). Wameiawilisha Hadiyth kuwa na maana kwamba aliingia mwanzo wa usiku, kisha huingia akabakia peke yake mwenyewe ndani ya kihema baada ya Swalat As-Subh. Wamesema: Kwa kuwa kumi ni jina la idadi ya siku (nights), hivyo ni lazima aanze kabla usiku haujaanza.
Ninasema (Abu Maalik): “Hadiyth inalazimu moja kati ya mawili: Ima iwe imeweka sharia ya kukaa I’tikaaf kuanzia usiku –kama walivyosema- na yeye (Rasuli) aliingia ndani ya kijihema chake baada ya Alfajiri, na hii inaleta utata kwa waliozuia kutoka ndani ya ‘ibaadah baada ya kuingia ndani yake.
Au iwe imeweka sharia ya kuanza kukaa I’tikaaf baada ya Alfajiri. Na hili linatiliwa nguvu – kwa mimi ninavyoona- na Hadiyth ya Abu Sa’iyd Al-Khudriyy anayesema: ((Tulifanya I’tikaaf pamoja na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) katika Kumi la Kati la Ramadhwaan, tukatoka Asubuhi ya ishirini)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2036). Imetangulia nyuma]
Tunaelewa kutokana na Hadiyth hii kuwa Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alipokuwa anakaa I’tikaaf katika Kumi la Kati, alikuwa anatoka kwenye I’tikaaf asubuhi ya tarehe ishirini, na anaingia alfajiri ya tarehe kumi. Na hili linawafikiana na Hadiyth ya ‘Aaishah. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
Ama kutoka kwenye I’tikaaf, kwa mujibu wa kauli ya kwanza, atatoka baada ya Alfajiri ya Siku ya ‘Iyd kwenda sehemu ya kuswalia Swalaatul ‘Iyd, na hili limestahabiwa na Maalik. Na ama kwa mujibu wa kauli ya pili, atatoka baada ya kuchwa jua la siku ya mwisho ya Ramadhwaan. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi”.
Yenye kubatwilisha I’tikaaf
I’tikaaf hubatwilika kwa moja ya yafuatayo:
(a) Kutoka bila ya udhuru wa kisharia au kwa haja ya dharura
Asitoke Msikitini ila kwa jambo lisilo na budi kihisia au kisharia. Mfano wa kwanza (kihisia) ni kutoka ili kupata chakula, kinywaji na kwenda haja ikiwa hili litamwelea uzito kama hakutoka. Na mfano wa pili (kisharia) ni kutoka kwa ajili ya kuoga janaba au kutawadha kama itashindikana kufanya hayo ndani ya Msikiti. Hili halina budi kisharia.
Toka kwa ‘Aaishah amesema: ((Na hakika Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anaingiza kichwa chake –naye yuko Msikitini- nikamchana nywele zake, na alikuwa haingii nyumbani isipokuwa kwa haja anapokuwa yuko kwenye I’tikaaf)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2029) na Muslim (298)]
Na tamko lake lishatangulia nyuma lisemalo: ((Sunnah kwa mwenye kukaa I’tikaaf asimzuru mgonjwa, asiende kuzika, asimguse mwanamke wala asimwingilie, na wala asitoke kwa haja yoyote isipokuwa kwa jambo la lazima)).
Linatiliwa nguvu na Hadiyth ya ‘Amrah aliyesema: ((‘Aaishah katika I’tikaaf yake alikuwa anapotoka kwenda nyumbani kwake ni kwa ajili ya haja yake tu, humpitia mgonjwa akamjulia hali, naye hupita tu bila kukaa kumuuliza uliza)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na ‘Abdul Razzaaq katika Al-Muswannaf (8055)]
Akishurutisha katika niya yake kutoka kwa jambo maalum, kama kushurutisha kwamba atatoka kwenda kuzika au kwenda kazini kwake mchana –kama wafanyavyo baadhi ya wafanyakazi-, ‘Ulamaa wengi wamesema kuwa sharti yake haimfai, na kama atafanya basi I’tikaaf yake itabatilika.
Ath-Thawriy, Ash-Shaafi’iy na Is-Haaq –nayo ni riwaya toka kwa Ahmad- wanasema kuwa ikiwa ataweka sharti mwanzoni mwa I’tikaaf yake, basi haibatiliki kwa kitendo chake. Ni kama kushurutisha katika Hajji.
(b) Kujimai
‘Ulamaa wote kwa sauti moja wanasema mwenye kumwingilia mke wake katika utupu wake naye yuko katika I’tikaaf akikusudia hilo [akijua kuwa yuko I’tikaafni], basi I’tikaaf yake hubatilika. Ni kwa Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَلَا تُبَاشِرُوهُنَّ وَأَنتُمْ عَاكِفُونَ فِي الْمَسَاجِدِ))
((Na wala msiwaingilie hali ya kuwa nyinyi ni wenye kukaa i’tikaaf Misikitini)). [Al-Baqarah (2:187)]
Jimai imekatazwa kwa umahususi wake katika ‘ibaadah, hivyo kuifanya hubatilisha ‘ibaadah. [Ash-Sharh Al-Mumti’u]
Ama kugusana naye bila kufikia upeo wa kujimai, na bila matamanio, basi hakuna ubaya. Ni kama mke kuosha kichwa chake, au kumpa kitu. Na hili ni kwa Hadiyth ya ‘Aaishah aliyesema:
((Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anakiinamishia kichwa chake kwangu na yeye yuko jirani ndani ya Msikiti, nikamchana na mimi nina hedhi)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2029)]
Kama itakuwa kwa matamanio, basi hilo ni haramu kwa mujibu wa Aayah hii. Ikiwa atafanya na manii yakamtoka, I’tikaaf yake itaharibika, na kama hayakutoka, basi haitoharibika. Hili limesemwa na Abu Haniyfah na Ash-Shaafi’iy katika moja ya kauli zake mbili. Amesema katika kauli nyingine: Inaharibika katika hali zote mbili, na hii pia ni kauli ya Maalik, kwa kuwa huo ni mgusano ulioharamishwa, hivyo umeharibu I’tikaaf na kuwa sawa na kumwaga.
Ibn Qudaamah amesema: “Sisi kwa upande wetu huo ni mgusano, hauharibu Swawm wala Hijja, hivyo hauharibu I’tikaaf, kwa kuwa ni bila matamanio”. [Al-Mughniy (3/199)]
Yanayojuzu kwa mwenye kukaa I’tikaaf
(a) Kutoka kwa haja ya dharura
Ni kama kutoka kwenda kula, au kunywa, au kujisaidia kama itakuwa vigumu kufanya ndani ya Msikiti kama ilivyotangulia.
(b) Kujishughulisha na mambo yanayoruhusika
Ni kama kumsindikiza aliyemtembelea na kwenda naye hadi kwenye mlango wa Msikiti, au kuzungumza na mtu mwingine.
(c,d) Kutembelewa na mkewe, na kubaki naye faragha
Mambo matatu haya ya mwisho yamedondolewa toka kwenye Hadiyth ya mke wa Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) Bi Swafiyyah: ((Alikwenda kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kumtembelea Msikitini katika Kumi la Mwisho la Ramadhwaan. Akakaa na kuzungumza naye saa, kisha akasimama kuondoka. Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasimama pamoja naye na kumsindikiza mpaka alipofika mlango wa Msikiti kwenye mlango wa Ummu Salamah..)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2035) na Muslim (2175)]
(e) Kuoga na kutawadha ndani ya Msikiti
Toka kwa mtu aliyemhudumia Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema: ((Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alitawadha Msikitini wudhuu mwepesi)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Ahmad (5/364) kwa Sanad Swahiyh]
Tushaeleza ‘Aaishah kumwosha Rasuli kichwa na kumchana nywele zake.
(f) Kufunga hema lake la kukalia I’tikaaf mwisho wa Msikiti
Kwa kuwa ‘Aaishah alikuwa akimfungia Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kijihema anapokaa I’tikaaf. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2023)].
Na hilo lilikuwa ni kwa maagizo yake (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam).
[Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1173)]
(g) Kuleta tandiko lake au kitanda chake Msikitini
Toka kwa Ibn ‘Umar: ((Kwamba Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anapokaa I’tikaaf, hutandikiwa tandiko lake au huwekewa kitanda chake nyuma ya nguzo ya At-Tawbah)). [Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na Ibn Maajah (642)]
Hili linataarifiwa na yaliyomo ndani ya Hadiyth ya Abu Sa’iyd: ((…inapokuwa asubuhi ya ishirini, tunahamisha vitu vyetu…)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2040)]
(h) Kuposa na kufunga ndoa
[Al-Muwattwaa (1/318), Al-Muhallaa (5/192) na Al-Mughniy (3/205)]
Hili halina ubaya, kwa kuwa I’tikaaf ni ‘ibaadah isiyozuia kutumia manukato, na kwa hivyo haikuzuia ndoa kama Swawm. Lakini hili limeshurutishwa na kutojimai kama ilivyotangulia.
(i) Mwanamke mwenye damu ya istihaadhwah anaruhusiwa kufanya I’tikaaf
[Al-Majmuw’u (6/520) na Al-Mughniy (3/209)]
Lakini anatakikana ajichunge vizuri ili asije kuchafua Msikiti. Anaweza kutoka ili kubadili na kujisafisha kulinda usafi wa Msikiti.
Toka kwa ‘Aaishah amesema: ((Mwanamke mwenye damu ya istihaadhwah katika wakeze wa Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikaa pamoja naye I’tikaaf. Alikuwa anaona wekundu na unjano, na huenda tuliweka beseni chini yake naye anaswali)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2037) na Muslim (2476)]
Je, inafaa mwenye hedhi kukaa I’tikaaf?
Mwenye hedhi kukaa I’tikaaf kunasimamia juu ya masuala mawili.
La kwanza: Je, ni lazima I’tikaaf iambatane na Swawm? La pili: Je mwenye hedhi anaingia Msikitini?
Anayeona kuwa ni lazima I’tikaaf iambatane na Swawm, basi kwa msingi huo, mwanamke atazuiliwa asikae I’tikaaf kwa kuwa hafungi. Na mwenye kuona kuwa mwenye hedhi haruhusiwi kuingia Msikitini, basi atazuiliwa asifanye I’tikaaf humo. [Jaami’u Ahkaamin Nisaa (2/430)]
Masuala haya yamefafanuliwa kwa mapana katika milango yake katika kitabu hiki. Unaweza kurejea huko. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi.
Faida
Mwanamke akikaa I’tikaaf Msikitini atajiwekea uzio wa kumsitiri asionekane
Wakeze Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam) walipotaka kukaa I’tikaaf, waliamuru vijihema vyao vikafungwa ndani ya Msikiti. Kwa kawaida wanaume huhudhuria Msikitini, hivyo ni bora kwao na akina mama wasionane. Na kama wanawake watatengewa sehemu yao maalum Msikitini, basi ni bora zaidi. [Angalia kitabu changu cha Fiqhu As-Sunnah Lin Nisaa (uk 247) chapa ya At-Tawfiyqiyyah]
Kati ya adabu za I’tikaaf
Imestahabiwa kwa mwenye kukaa I’tikaaf ajishughulishe na amali za utiifu kwa Allaah kama kuswali, kusoma Qur-aan, kumdhukuru Allaah, kumwomba maghfirah, kuomba du’aa, kumswalia Nabiy (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihii wa sallam), kuitafsiri Qur-aan, kudurusu Hadiyth na mfano wa hayo.
Si jambo zuri kujishughulisha na maneno au vitendo visivyo na faida, au kupafanya mahala pake pa I’tikaaf kuwa baraza ya masuhubiano ya watu, au mkusanyiko wa watembeleaji, au kurefusha sana mazungumzo na wenzake anaofanya nao I’tikaaf. Hii ni aina, lakini I’tikaaf ya Rasuli ni nyingine kabisa.
Links
[1] https://www.alhidaaya.com/sw/taxonomy/term/284
[2] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10435&title=05-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20%D9%83%D9%90%D8%AA%D9%8E%D8%A7%D8%A8%D9%8F%20%D8%A7%D9%8E%D9%84%D8%B5%D9%91%D9%90%D9%8A%D9%8E%D8%A7%D9%85%D9%90%20-%20Kitabu%20Cha%20Swiyaam%20%20
[3] http://www.alhidaaya.com
[4] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10573&title=01-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Taarifu%20Ya%20Swawm
[5] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10574&title=02-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Fadhila%20Za%20Swiyaam%20Na%20Faida%20Zake
[6] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10575&title=03-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Vigawanyo%20Vya%20Swiyaam
[7] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10576&title=04-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Swiyaam%20ya%20Ramadhwaan%20Hukmu%20Yake
[8] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10577&title=05-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Kati%20Ya%20Fadhila%20Za%20Ramadhwaan%20Na%20Kufanya%20%E2%80%98Ibaadah%20Ndani%20Yake
[9] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10578&title=06-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Jambo%20Gani%20Kunakuwa%20Wajibu%20Kufunga%20Ramadhwaan%3F%20
[10] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10579&title=07-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Shuruti%20Za%20Kuswihi%20Swiyaam
[11] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10580&title=08-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Nguzo%20Ya%20Swiyaam
[12] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10581&title=09-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Sunnah%20Za%20Swawm%20Na%20Adabu%20Zake
[13] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10582&title=10-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Mambo%20Yenye%20Kubatilisha%20Swiyaam
[14] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10583&title=11-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Mambo%20Ambayo%20Hayabatilishi%20Swiyaam
[15] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10584&title=12-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20%20Wasiofunga%20%28Swawm%29%20Na%20Hukmu%20Zinazowahusu
[16] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10585&title=13-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Kulipa%20Swiyaam%20Za%20Ramadhwaan
[17] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10586&title=14-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Swiyaam%20za%20Sunnah
[18] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10587&title=15-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Masuala%20Kadhaa%20Kuhusiana%20Na%20Swawm%20Za%20Sunnah
[19] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10588&title=16-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Masiku%20Ambayo%20Imekatazwa%20Kufunga
[20] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10589&title=17-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20Laylatul%20Qadr%20Na%20Fadhila%20Zake
[21] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10590&title=18-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Swiyaam%3A%20I%27tikaaf