Al-Baqarah
Kutoa Swadaqah Hata Riyali Moja Ni Kheri
Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):
الَّذِينَ يُنفِقُونَ أَمْوَالَهُم بِاللَّيْلِ وَالنَّهَارِ سِرًّا وَعَلَانِيَةً فَلَهُمْ أَجْرُهُمْ عِندَ رَبِّهِمْ وَلَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ﴿٢٧٤﴾
274. Wale wanaotoa mali zao usiku na mchana, kwa siri na kwa dhahiri; watapata ujira wao kwa Rabb wao, na wala hakuna khofu juu yao na wala wao hawatohuzunika.
Mafunzo:
Abuu Hurayrah (رضي الله عنه) amehadithia kwamba Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Mtu alisema: Nitatoa swadaqah usiku. Alitoka usiku na swadaqah yake ikamfikia mkononi mwa mzinzi mwanamke (bila ya kujua). Asubuhi, watu wakahadithia: Mzinzi amepewa swadaqah! Yule mtu akasema: Allaahumma Himdi ni Zako, kwa (kumpa swadaqah) mzinzi mwanamke. Leo usiku nitatoa swadaqah tena. Akatoa swadaqah yake na (bila kujua) ikafika mikononi mwa tajiri. Asubuhi yake (watu) wakahadithia: Usiku uliopita tajiri kapewa swadaqah! Akasema: Allaahumma Himdi ni Zako kwa (kumpa swadaqah) tajiri. Usiku nitatoa swadaqah. Hivyo alitoka na swadaqah yake (na bila ya kujua) ikamfikia mikononi mwa mwizi. Siku ya pili yake wakahadithia watu: Usiku uliopita mwizi alipewa swadaqah! Akasema: Allaahumma Himdi ni Zako, (nimempa swadaqah) mzinzi mwanamke, tajiri na mwizi. Kisha alimjia mtu na kumwambia: Swadaqah ulizotoa zimekubaliwa. Ama kuhusu mwanamke mzinzi, inaweza kumfanya kuacha uzinifu. Ama kuhusu tajiri, itamfanya kujifunza na kumfanya kutumia utajri wake aliopewa na Allaah. Ama mwizi inaweza kumfanya kuacha wizi.” [Al-Bukhaariy na Muslim]
Links
[1] http://www.alhidaaya.com
[2] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F8058&title=274-Aayah%20Na%20Mafunzo%3A%20Kutoa%20Swadaqah%20Hata%20Riyali%20Moja%20Ni%20Kheri