104 - Al-Humazah

 

  الْهُمَزَة

 

104-Al-Humazah

 

104-Al-Humazah: Utangulizi Wa Suwrah

 

Alhidaaya.com

 

 

 

بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ

 

 

وَيْلٌ لِّكُلِّ هُمَزَةٍ لُّمَزَةٍ ﴿١﴾

1. Ole kwa kila mwenye kukashifu na kufedhehesha watu kwa ishara na vitendo, na kwa kila mwenye kusengenya na kufedhehesha kwa ulimi.[1]

 

 

 

الَّذِي جَمَعَ مَالًا وَعَدَّدَهُ ﴿٢﴾

2. Ambaye amekusanya mali na kuyahesabu.

 

 

 

يَحْسَبُ أَنَّ مَالَهُ أَخْلَدَهُ ﴿٣﴾

3. Anadhani kwamba mali yake itamdumisha milele.

 

 

 

كَلَّاۖ لَيُنبَذَنَّ فِي الْحُطَمَةِ ﴿٤﴾

4. Laa hasha! Atavurumishwa katika Al-Hutwamah[2] (moto mkali unaonyambua nyambua).

 

 

 

وَمَا أَدْرَاكَ مَا الْحُطَمَةُ ﴿٥﴾

5. Na nini kitakujulisha ni nini hiyo Al-Hutwamah?

 

 

 

نَارُ اللَّـهِ الْمُوقَدَةُ ﴿٦﴾

6. Ni moto wa Allaah uliowashwa.

 

 

 

الَّتِي تَطَّلِعُ عَلَى الْأَفْئِدَةِ ﴿٧﴾

7. Ambao unapanda nyoyoni.

 

 

 

إِنَّهَا عَلَيْهِم مُّؤْصَدَةٌ ﴿٨﴾

8. Hakika huo utafungiwa juu yao kila upande.

 

 

 

فِي عَمَدٍ مُّمَدَّدَةٍ ﴿٩﴾

9. Katika nguzo zilizonyooshwa.

 

 

 

 

[1] Maana Ya Al-Humazah Na Al-Lumazah:

 

‘Ulamaa wametofautiana katika maana za al-humazah na al-lumazah. Lakini wengi wao wamekubaliana kwamba al-humazah ni kukashifu, kufedhehesha, kudharau watu kwa ishara na vitendo. Na al-lumazah ni kusengenya, kukashifu na kufedhehesha kwa ulimi.  

 

Na katika Tarjama, maana zake zimetegemea muktadha zake. Na zimekuja maana zake mbalimbali kama ifuatavyo:  

 

Al-Humazah: Kudharau, kukashifu, kufedhehesha, kubeza n.k. Rejea Suwrah hii Al-Humazah (104:1), Al-Qalam (68:11).

 

Al-Lumazah: Kukosoa, kulaumu, kushutumu, kutukana, kukejeli, kufedhehesha na kuvunja heshima, kufanya tashtiti, n.k. Rejea Suwrah hii Al-Humazah (104:1), At-Tawbah (9:58), (9:79), Al-Hujuraat (49:11).

 

Na Allaah Mjuzi zaidi

 

[2] Al-Hutwamah Ni Miongoni Mwa Majina Ya Moto:

 

Moto wa al-hutwamah umetajwa sifa zake katika Aayah zinzofuatia kama alivyofasiri Imaam Ibn Kathiyr:

 

Thaabit Al-Bunaan amesema: “Utawachoma mpaka nyoyoni nao wangali wako hai.” Kisha akasema: “Kwa yakini adhabu imewafika.” Kisha akalia.  Muhammad Bin Ka’ba amesema: “Moto utakula kila kitu kwenye mwili wake mpaka moyo wake unapofika usawa wa koo lake, hurudi kwenye mwili wake.” [Tafsiyr Ibn Kathiyr]

 

Rejea Al-Muddath-thir (74:26) kwenye majina mengineyo ya moto.

 

 

 

Share