كِتَابُ اَلزَّكَاة
Kitabu Cha Zakaah
Abu Maalik Kamaal Bin As-Sayyid Saalim
Imetarjumiwa na 'Abdullaah Mu'aawiyah (Abu Baasim)
Alhidaaya.com
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
01-Taarifu Ya Zakaah
Alhidaaya.com [3]
الزكاة “Az-Zakaah” katika lugha, ni “maswdar” ya ((زكا الشيء)) yaani kitu kimekua na kimeongezeka. Hivyo Zakaah ni barakah, ukuaji, utwahara na utengefu. [Al Mu-’ujam Al-Wasiytw]
Ama kisharia (kiistilahi), Zakaah ni fungu lililokadiriwa toka mali maalum na katika wakati maalum, na hupewa watu maalum. Fungu hili linalotolewa toka kwenye mali limeitwa “Zakaah” kwa kuwa linaizidishia barakah mali ya asili lilikotolewa, linaistawisha na linailinda na majanga. [Al-Majmuw’u cha An Nawawiy (5/324)]
[Majmuw’u Fataawaa Ibn Taymiyah (8/35) kwa maana yake]
Ni kama Anavyosema Ta’aalaa:
((خُذْ مِنْ أَمْوَالِهِمْ صَدَقَةً تُطَهِّرُهُمْ وَتُزَكِّيهِم بِهَا وَصَلِّ عَلَيْهِمْ))
((Chukua katika mali zao Swadaqah, uwatakase na ziwazidishie kwazo na waombee du’aa (na maghfirah)). [At -Tawbah (9:103)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
02-Hukmu Ya Zakaah Na Hadhi Yake
Alhidaaya.com [3]
Zakaah ni Fardhi ‘Ayn kwa kila mtu ambaye zimekamilika kwake shuruti za kuwajibikiwa. Ufaradhi wake umethibiti katika Qur-aan, Sunnah na Ijma’a.
Katika Qur-aan, kuna Aayah nyingi zinazozungumzia uwajibu wa Zakaah na ulazima wa kulichukulia hima sana suala hili. Na kutokana na uzito wake, Zakaah imewekwa sambamba na Swalaah katika jumla ya Aayah 82. Kati ya Aayah hizo, ni Kauli Yake Ta’aalaa:
((فَأَقِيمُوا الصَّلَاةَ وَآتُوا الزَّكَاةَ))
((Basi simamisheni Swalaah na toeni Zakaah)). [Al-Hajj (22:78)]
Na Kauli Yake:
((خُذْ مِنْ أَمْوَالِهِمْ صَدَقَةً تُطَهِّرُهُمْ وَتُزَكِّيهِم بِهَا وَصَلِّ عَلَيْهِمْ))
((Chukua katika mali zao Swadaqah, uwatakase na ziwazidishie kwazo na waombee du’aa (na maghfirah)). [At-Tawbah (9:103)]
Aidha, makamio ni makubwa na mazito kwa mwenye kufanya ubakhili wa kuitoa. Allaah (Subhaanahuu wa Ta’aalaa Anasema:
(( وَالَّذِينَ يَكْنِزُونَ الذَّهَبَ وَالْفِضَّةَ وَلَا يُنفِقُونَهَا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ فَبَشِّرْهُم بِعَذَابٍ أَلِيمٍ • يَوْمَ يُحْمَىٰ عَلَيْهَا فِي نَارِ جَهَنَّمَ فَتُكْوَىٰ بِهَا جِبَاهُهُمْ وَجُنُوبُهُمْ وَظُهُورُهُمْ ۖ هَـٰذَا مَا كَنَزْتُمْ لِأَنفُسِكُمْ فَذُوقُوا مَا كُنتُمْ تَكْنِزُونَ))
((Na wale wanaorundika dhahabu na fedha [silver] na wala hawazitoi katika Njia ya Allaah, basi wabashirie adhabu iumizayo • Siku zitakapopashwa katika Jahannam, na kwazo vikachomwa moto vipaji vyao, na mbavu zao, na migongo yao (wakiambiwa): “Haya ndiyo mliyoyarundika kwa ajili ya nafsi zenu. Basi onjeni yale mliyokuwa mkiyarundika)). [At-Tawbah (9:34 na 35]
Imepokelewa kwa njia swahiyh toka kwa Ibn ‘Umar na Jaabir bin ‘Abdillaah kwamba wamesema: “Mali iliyotolewa Zakaah yake, haihesabiwi kuwa hazina ya mali [kanz]”.
Sunnah nayo imethibitisha wajibu wa Zakaah. Imepokelewa toka kwa Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) akisema:
((إنك تأتي قومًا أهل كتاب، فادعهم إلى شهادة أن لا إله إلا الله وأني رسول الله، فإن هم أطاعوا لذلك فأعلمهم أن الله عز وجل افترض عليهم خمس صلوات في كل يوم وليلة، فإن هم أطاعوا لذلك فأعلمهم أن الله تعالى افترض عليهم صدقة في أموالهم تؤخذ من أغنيائهم وتُرَدُّ إلى فقرائهم، فإن هم أطاعوا لذلك فإياك وكرائمَ أموالهم، واتقِ دعوة المظلوم؛ فإنه ليس بينها وبين الله حجابٌ))
“Kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipomtuma Mu’aadh bin Jabal (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwenda Yemen alimwambia: ((Hakika wewe unawaendea watu wa Ahlul Kitaab. Basi walinganie washahadie kuwa hapana mungu isipokuwa Allaah, na mimi ni Rasuli wa Allaah. Na kama watalitii hilo, basi wajulishe kuwa Allaah ‘Azza wa Jalla Amewafaradhishia Swalaah Tano kila mchana na usiku. Na kama watalitii hilo, basi wajulishe kuwa Allaah Ta’aalaa Amewafaradhishia Zakaah katika mali zao, huchukuliwa toka kwa matajiri wao na kurejeshwa kwa masikini wao. Na kama watalitii hilo, basi chunga usije kuchukua mali zao za thamani kubwa [wakati wa kukusanya Zakaah], na ogopa sana du’aa ya aliyedhulumiwa, kwani haina kizuizi kati yake na kati ya Allaah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1496) na Muslim (19)]
Ama Ijma’a, hii imekubaliana kwa sauti moja juu ya ufaradhi wa Zakaah. Hakuna aliyekwenda kinyume na hilo tokea enzi ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mpaka hivi leo.
Ama hadhi yake katika diyn, Zakaah ni nguzo kati ya nguzo tano za Uislamu, nayo ni nguzo ya tatu baada ya Shahadah Mbili na Swalaah. Nabiy (Swalla Allaahu alayhi wa ‘aalihii wa sallam) amesema:
((بُني الإسلام على خمس: شهادة أن لا إله إلا الله وأن محمدًا رسول الله، وإقام الصلاة، وإيتاء الزكاة، وصوم رمضان، وحج البيت لمن استطاع إليه سبيلا))
((Uislamu umejengwa juu ya (nguzo) tano: Kushahadia kwamba hapana mungu isipokuwa Allaah, na kwamba Muhammad ni Rasuli wa Allaah, kusimamisha Swalaah, kutoa Zakaah, kufunga Ramadhwaan, na kuikusudia Nyumba kwa atakayeweza kwenda)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (8) na Muslim (16)]
Na kwa ajili hiyo, Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akichukua kwa Maswahaba bay-‘a ya kwamba lazima wataitoa. Imepokelewa toka kwa Jariyr bin ‘Abdullaah akisema: ((Nilimpa bay-‘a Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kuwa lazima nisimamishe Swalaah, nitoe Zakaah na [nitoe] nasaha kwa kila Muislamu)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (57) na Muslim (56)]
Na Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliamuru kuwapiga vita wasiotoa Zakaah. Imepokelewa toka kwa Ibn ‘Umar kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((أمرت أن أقاتل الناس حتى يشهدوا أن لا إله إلا الله وأن محمدا رسول الله ، ويقيموا الصلاة، ويؤتوا الزكاة))
((Nimeamuriwa kuwapiga watu vita mpaka washahadie kuwa hapana mungu isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Rasuli wa Allaah, wasimamishe Swalaah na watoe Zakaah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (25) na Muslim (22)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
03-Fadhila Na Faida Za Kutoa Zakaah
Alhidaaya.com [3]
1- Zakaah ni kati ya sifa za watu wema wa Peponi. Allaah Anasema:
((إِنَّ الْمُتَّقِينَ فِي جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ • آخِذِينَ مَا آتَاهُمْ رَبُّهُمْ ۚ إِنَّهُمْ كَانُوا قَبْلَ ذَٰلِكَ مُحْسِنِين• كَانُوا قَلِيلًا مِّنَ اللَّيْلِ مَا يَهْجَعُونَ • وَبِالْأَسْحَارِ هُمْ يَسْتَغْفِرُونَ • وَفِي أَمْوَالِهِمْ حَقٌّ لِّلسَّائِلِ وَالْمَحْرُومِ))
((Hakika wenye taqwa watakuwa katika Jannaat na chemchemu • Wakichukua yale Atakayowapa Rabb wao • Hakika wao walikuwa kabla ya hapo ni wahisani • Walikuwa kidogo tu katika usiku wakilala kwa raha • Na kabla ya Alfajiri wakiomba maghfirah • Na katika mali zao kuna haki maalumu kwa mwenye kuomba na asiyeomba)). [Adh-Dhaariyaat (51:15-19)]
2- Zakaah ni miongoni mwa sifa za Waumini wenye kustahiki kuzipata Rahmah za Allaah. Allaah Anasema:
((وَالْمُؤْمِنُونَ وَالْمُؤْمِنَاتُ بَعْضُهُمْ أَوْلِيَاءُ بَعْضٍ ۚ يَأْمُرُونَ بِالْمَعْرُوفِ وَيَنْهَوْنَ عَنِ الْمُنكَرِ وَيُقِيمُونَ الصَّلَاةَ وَيُؤْتُونَ الزَّكَاةَ وَيُطِيعُونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ ۚ أُولَـٰئِكَ سَيَرْحَمُهُمُ اللَّـهُ ۗ إِنَّ اللَّـهَ عَزِيزٌ حَكِيمٌ))
((Na Waumini wanaume na Waumini wanawake ni marafiki wandani wao kwa wao, wanaamrisha mema na wanakataza munkari na wanasimamisha Swalaah na wanatoa Zakaah na wanamtii Allaah na Rasuli Wake. Hao Allaah Atawarehemu. Hakika Allaah ni Mwenye enzi ya nguvu Asiyeshindika, Mwenye hikmah wa yote)). [At Tawbah (9:71]
3- Allaah Huikuza na kuitunza kwa mtoaji wake. Anasema:
((لَّيْسَ عَلَيْكَ هُدَاهُمْ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يَهْدِي مَن يَشَاءُ ۗ وَمَا تُنفِقُوا مِنْ خَيْرٍ فَلِأَنفُسِكُمْ ۚ وَمَا تُنفِقُونَ إِلَّا ابْتِغَاءَ وَجْهِ اللَّـهِ ۚوَمَا تُنفِقُوا مِنْ خَيْرٍ يُوَفَّ إِلَيْكُمْ وَأَنتُمْ لَا تُظْلَمُونَ))
((Si juu yako kuwahidi, lakini Allaah Humhidi Amtakaye. Na chochote cha khayr mtoacho, basi ni kwa ajili ya nafsi zenu. Na hamtoi ila kutaka Wajhi wa Allaah. Na chochote mtoacho katika khayr mtalipwa kamilifu nanyi hamtodhulumiwa)). [Al-Baqarah (2:276)]
Na Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam amesema:
((من تصدق بعدل تمرة من كسب طيب - ولا يقبل الله إلا الطيب - فإن الله يتقبلها بيمينه ثم يربيها لصاحبها، كما يربي أحدكم فلوه حتى تكون مثل الجبل))
((Mwenye kutoa swadaqah ya thamani ya tende moja ya chumo safi la halali – na Allaah Hakubali isipokuwa kilicho safi –Allaah Huipokea kwa Mkono Wake wa kuume, kisha Huilea kwa mtoaji wake kama mmoja wenu anavyomtunza farasi wake mchanga mpaka inakuwa mithili ya mlima)). [Hadiyth Swahiyh: Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1410) na Muslim (1014)]
4- Allaah Mtukufu Atamwekea kivuli mtoaji kimkinge na joto la Siku ya Qiyaamah. Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((سبعة يظلهم الله في ظله يوم لا ظل إلا ظله ... ورجل تصدق بصدقة فأخفاها حتى لا تعلم شماله ما أنفقت يمينه...))
((Watu saba Allaah Atawaweka katika Kivuli Chake siku ambayo hakuna kivuli isipokuwa Kivuli Chake……na mtu aliyetoa swadaqah akaificha kiasi cha kushoto kwake kutojua kilichotolewa na kuume kwake…)). [Hadiyth Swahiyh: Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (660) na Muslim (1031)]
5- Zakaah huitakasa mali, huistawisha na humfungulia mtoaji wake milango zaidi ya rizki. Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((ما نقصت صدقة من مال...))
((Swadaqah haipunguzi chochote katika mali…)). [Hadiyth Swahiyh: Imekharijiwa na Muslim (2588)]
6- Zakaah ni sababu ya kushuka kheri na barakah, na kuizuia ni sababu ya kuzuilika kheri hizo. Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anasema:
((وما منع قوم زكاة أموالهم إلا منعوا القطر من السماء، ولولا البهائم لم يمطروا))
((Na watu hawazuilii Zakaah za mali zao, ila hunyimwa mvua toka mbinguni, na lau si wanyama, basi wasingelipata mvua)). [Ibn Maajah (4019) na wengineo. Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh katika Asw-Swahiyhah (105)]
7- Zakaah hufuta makosa na madhambi. Katika Hadiyth ya Mu’aadh bin Jabal, Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((..والصدقة تطفئ الخطيئة كما يطفئ الماء النار))
((…na swadaqah huzima makosa kama maji yanavyozima moto)). [At-Tirmidhiy (609), An-Nasaaiy katika Al-Kubraa (11394), Ibn Maajah (3973) na Ahmad (5/531). Ina uwezekano wa kufanywa Hadiyth Hasan]
8- Ni dalili ya ukweli wa iymaan ya mtoaji, kwa kuwa nafsi zinapenda mali, na kipendwacho hakitolewi ila kwa ajili ya kukitaka mfano wake au zaidi yake, bali hili ndilo litafutwalo zaidi. Na kwa ajili hiyo, Zakaah imeitwa swadaqah, kwa kuwa inaonyesha ukweli wa mtoaji wake katika kuzitafuta Radhi za Allaah ‘Azza wa Jalla. [Ash-Sharhu Al-Mumti’u]
9- Huitakasa tabia ya mtoaji, na hukikunjua kifua chake. Zakaah humwopoa mtoaji wake toka kwenye kundi la mabakhili na kumwingiza katika kundi la wakarimu, na hukikunjua kifua chake. Mtu anapotoa mali yake - kwa roho safi na ukwasi – basi huhisi ukunjufu ndani ya nafsi yake. [Angalia Zaad Al-Ma’aad cha Ibn Al-Qayyim (2/25)]
10- Huilinda na kuikinga mali kutokana na tamaa na uchu wa watu masikini na isifikiwe na mikono ya wahalifu.
11- Ni msaada kwa mafukara na wahitaji. Huwarejesha kuanza tena kazi na shughuli zao kama walikuwa wenye uwezo wakakwama, au huwasaidia kujijengea mazingira bora ya kuishi kama walikuwa hawajiwezi. Na hapa Zakaah inaikinga jamii kutokana na tatizo la umasikini, na huilinda dola isilemewe na majukumu zaidi na utendaji wake kuwa wa kusuasua. [Al–Fiqhu Al- Islaamiy Waadillatuh (2/732]
12- Ni mchango wa wajibu wa kujitolea wa Muislamu kwa jamii yake, na msaada kwa Dola Ya Kiislamu wakati wa dharura, kutayarisha majeshi, kukabiliana na uadui na kuwawezesha masikini wafikie upeo wa kujitosheleza. [Angalia iliyotangulia]
13- Ni shukrani kwa neema ya mali. [Adh-Dhakhiyrah cha Al-Quraafiy (3/7]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
04-Hukmu Ya Kuzuia Zakaah Na Adhabu Kwa Asiyetoa
Alhidaaya.com [3]
1- ‘Ulamaa wote wamekubaliana kuwa mwenye kukataa uwajibu wa Zakaah na akakanusha ufaradhi wake, basi huyo ni kafiri kwa Ijma’a. Kwa kuwa mtu huyo anaikadhibisha Qur-aan na Sunnah na anakanusha jambo ambalo linajulikana na wote katika diyn. [Al-Mughniy (2/572) na Al-Majmuw’u (5/334)]
2- Ama mwenye kukubali kuwa ni waajib lakini akakataa kutoa:
(a) Imesimuliwa toka kwa Ahmad kuwa amesema: “Mwenye kuacha kutoa kwa ubakhili wake, basi atakufurishwa kama mwenye kuacha Swalaah kwa uvivu”. Baadhi ya wafuasi wa Hanbali wameitilia nguvu riwaya hii. [Ash-Sharhu Al Kabiyr (3/43), Al-Mubdi’u (1/308) na Ash-Sharhu Al-Mumti’u].
Wameitolea dalili kwa Kauli Yake Ta’aalaa:
((فَإِن تَابُوا وَأَقَامُوا الصَّلَاةَ وَآتَوُا الزَّكَاةَ فَإِخْوَانُكُمْ فِي الدِّينِ ۗ وَنُفَصِّلُ الْآيَاتِ لِقَوْمٍ يَعْلَمُونَ))
((Wakitubu, na wakasimamisha Swalaah, na wakatoa Zakaah; basi ni ndugu zenu katika Dini. Na Tunafasili waziwazi Aayaat kwa watu wanaojua)). [At-Tawbah (9:11)]
Wamesema: “Udugu katika diyn haufutiki isipokuwa kama mtu atatoka kwenye diyn. Na Allaah Ameratibu uthibitisho wa udugu juu ya sifa hizi tatu: Kutubia na kuacha shirk, kusimamisha Swalaah na kutoa Zakaah”.
(b) Lakini Jumhuri ya ‘Ulamaa wanasema kuwa asiyetoa Zakaah kutokana na ubakhili wake tu na hapingi au kukataa kuwa ni waajib, basi huyo anafanya dhambi kubwa kati ya madhambi makubwa angamizi na kosa baya kabisa, na anaingia ndani ya duara la makamio makali ya kukabiliwa na adhabu kali Siku ya Qiyaamah. Na madhali anakiri na kukubali uwajibu wa kutoa Zakaah, basi hatoki nje ya diyn kwa kutoitoa.
Mwelekeo huu ndio sahihi. Unatiliwa nguvu na Hadiyth ya Abu Hurayrah ya kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipomtaja mzuiaji Zakaah ya dhahabu na fedha (silva), na akaelezea adhabu yake, alisema baada ya hapo:
((ثم يرى سبيله إما إلى الجنة وإما إلى النار))
((Kisha ataonyeshwa njia yake, ima kwenda Peponi au ima kwenda Motoni)). [Hadiyth Swahiyh: Imekharijiwa na Muslim (987)]
Na kama ni kafiri, basi hawezi kuwa na njia ya kuelekea Peponi. Allaah Ndiye Mjuzi zaidi.
Ama adhabu ya mzuiaji Zakaah hapa duniani, adhabu hiyo inakuwa ya kiqadari na kisharia. Ya kiqadari ni Allaah Ta’aalaa kumwonja kila mwenye kuifanyia ubakhili Haki ya Allaah na haki ya masikini katika mali yake kwa baa la njaa na ukame kama anavyosema Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((وما منع قوم الزكاة إلا ابتلاهم الله بالسنين))
((Na watu hawazuii Zakaah isipokuwa Allaah Huwaonja kwa ukame)). [Imekharijiwa na At-Twabaraaniy katika Al-Awsatw (4577), Al-Haakim (2/136) na Al-Bayhaqiy (3/346). Al-Albaaniy kasema ni Hadiyth Hasan]
Na katika riwaya:
((إلا حبس عنهم القطر))
((Isipokuwa Huwafungia mvua)).
Ama adhabu ya kisharia:
(a) Ikiwa mzuiaji Zakaah yuko ndani ya mamlaka na udhibiti wa mtawala, basi Zakaah itachukuliwa kutoka kwake kwa nguvu kutokana na neno la Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii sallam):
((أمرت أن أقاتل الناس حتى يقولوا: لا إله إلا الله محمد رسول الله، فإذا قالوها، عصموا مني دماءهم وأموالهم إلا بحقها وحسابهم على الله))
((Nimeamuriwa kuwapiga watu vita mpaka watamke: Laailaaha illa Allaahu Muhammadun Rasuwlul Laah. Wakilisema hilo, watazikinga damu zao na mali zao kutokana nami ila kwa haki yake na hisabu yao iko juu ya Allaah)).
Na kati ya haki zake ni Zakaah. Abu Bakri (Radhwiya Allaahu ‘anhu) alisema mbele ya kadamnasi ya Maswahaba:
((الزَّكَاةَ حَقُّ الْمَالِ، وَاَللَّهِ لَوْ مَنَعُونِي عَنَاقًا كَانُوا يُؤَدُّونَهَا إلَى رَسُولِ اللَّهِ - صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ - لَقَاتَلْتُهُمْ عَلَى مَنْعِهَا))
((Zakaah ni haki ya mali. Wa-Allaahi, lau watazuia kunipa mimi kondoo mchanga waliyekuwa wakimtoa kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), basi nitapambana nao kivita kwa kuzuia…..)). [Hadiyth Swahiyh: Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1399) na Muslim (20)
Na Jumhuri wanasema ikichukuliwa Zakaah kwa nguvu kwa aliyegoma kutoa, basi hakichukuliwi kingine cha ziada katika mali yake. Wanatolea dalili Hadiyth: ((Hakuna katika mali haki nyingine zaidi ya Zakaah)). [Ibn Maajah (1789) kwa Sanad Dhwa’iyf]
Ama Ash-Shaafi’iy katika madhehebu yake ya kale, Is-haaq na baadhi ya Maswahiba wa Ahmad, wanasema itachukuliwa Zakaah pamoja na nusu ya mali yake kama adhabu kwake. [Naylul Awtwaar (4/147), na Al-Mawsuw’atu Al-Fiqhiyyah (23/231).
Wametoa dalili kwa Hadiyth isemayo:
((ومن منعها فإنا آخذوها وشطر ماله))
((Na mwenye kuizuia, basi sisi ni wenye kuichukua pamoja na nusu ya mali yake)). [Abu Daawuwd (1560), An-Nasaaiy (5/15-17) na Ahmad kwa Sanad Hasan]
Waliotangulia wamejibu wakisema kuwa Hadiyth hii ni Mansuwkh, na kuongeza kuwa dai la naskh halikubaliwi kama tarehe na historia havijulikani.
(b) Kama mgomaji kutoa Zakaah yuko nje ya mamlaka na udhibiti wa mtawala, basi ni lazima apambane naye kivita, kwa kuwa Maswahaba walipambana kivita na waliokataa kutoa Zakaah.
Ama adhabu ya anayekataa kutoa Zakaah huko aakhirah, kuna Aayaat na Hadiyth kadhaa zilizozungumzia hilo. Kati yake ni:
1- Neno Lake Ta’aalaa:
((يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِنَّ كَثِيرًا مِّنَ الْأَحْبَارِ وَالرُّهْبَانِ لَيَأْكُلُونَ أَمْوَالَ النَّاسِ بِالْبَاطِلِ وَيَصُدُّونَ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ ۗ وَالَّذِينَ يَكْنِزُونَ الذَّهَبَ وَالْفِضَّةَ وَلَا يُنفِقُونَهَا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ فَبَشِّرْهُم بِعَذَابٍ أَلِيمٍ • يَوْمَ يُحْمَىٰ عَلَيْهَا فِي نَارِ جَهَنَّمَ فَتُكْوَىٰ بِهَا جِبَاهُهُمْ وَجُنُوبُهُمْ وَظُهُورُهُمْ ۖ هَـٰذَا مَا كَنَزْتُمْ لِأَنفُسِكُمْ فَذُوقُوا مَا كُنتُمْ تَكْنِزُونَ))
((Enyi walioamini! Hakika wengi katika Wanachuoni Marabai wa dini (zao) na Wamonaki wanakula mali za watu kwa batili, na wanazuia Njia ya Allaah. Na wale wanaorundika dhahabu na fedha [silva] na wala hawazitoi katika Njia ya Allaah, basi wabashirie adhabu iumizayo • Siku zitakapopashwa katika Jahannam, na kwazo vikachomwa moto vipaji vyao, na mbavu zao, na migongo yao (wakiambiwa): “Haya ndiyo mliyoyarundika kwa ajili ya nafsi zenu. Basi onjeni yale mliyokuwa mkiyarundika)). [At-Tawbah (9:34 na 35)]
2- Toka kwa Abu Hurayrah kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((مَنْ آتَاهُ اللَّهُ مَالاً فَلَمْ يُؤَدِّ زَكَاتَهُ، مُثِّلَ لَهُ يوم القيامة شُجَاعًا أَقْرَعَ، لَهُ زَبِيبَتَانِ يُطَوَّقُهُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ، ثم يَأْخُذُ بِلِهْزِمَتَيْهِ ـ يَعْنِي شِدْقَيْهِ ـ ثم يَقُولُ أَنَا كنزك أنا مَالُكَ)) . ثُمَّ تَلاَ هَذِهِ الآيَةَ {وَلاَ يَحْسِبَنَّ الَّذِينَ يَبْخَلُونَ بِمَا آتَاهُمُ اللَّهُ مِنْ فَضْلِهِ هُوَ خَيْرًا لَّهُم ۖ ... بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ))
((Mtu ambaye Allaah Amempa mali naye asiitolee Zakaah yake, basi ataundiwa kwa mali hiyo Siku ya Qiyaamah mfano wa joka lenye kichwa cheupe (upara), lina mabaka meusi juu ya macho yake, litamviringa Siku ya Qiyaamah. Kisha litambana kwa taya zake mbili liseme: Mimi ni hazina ya mali yako, mimi mali yako. Kisha akasoma Aayah hii:
((وَلَا يَحْسَبَنَّ الَّذِينَ يَبْخَلُونَ بِمَا آتَاهُمُ اللَّـهُ مِن فَضْلِهِ هُوَ خَيْرًا لَّهُم ۖ بَلْ هُوَ شَرٌّ لَّهُمْ ۖ سَيُطَوَّقُونَ مَا بَخِلُوا بِهِ يَوْمَ الْقِيَامَةِ ۗ وَلِلَّـهِ مِيرَاثُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۗ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ))
((Wala wasidhani kabisa wale wanaofanya ubakhili kwa yale Aliyowapa Allaah katika fadhila Zake kwamba hayo ni khayr kwao, bali ni shari kwao. Watafungwa kongwa yale waliyoyafanyia ubakhili Siku ya Qiyaamah. Na ni Wake Allaah Pekee urithi wa mbingu na ardhi. Na Allaah kwa yale myatendayo ni Mwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika)). [Al-Bukhaariy (1403)]
3- Toka kwa Abu Hurayrah amesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Hakuna yeyote mwenye hazina ya mali ambayo haitolei Zakaah, isipokuwa atapashiwa moto kwenye moto wa Jahannam, kisha ifanywe vipande vipana [vya metali], achomwe navyo mbavu zake na kipaji chake mpaka pale Allaah Atakapohukumu kati ya Waja Wake katika siku ambayo urefu wake ni miaka elfu khamsini. Halafu ataonyeshwa njia yake, ima ya kwenda Peponi, au ya kwenda motoni. Na hakuna yeyote mwenye kumiliki ngamia na asiwatolee Zakaah yake, isipokuwa atatandazwa kifudifudi mbele yao kwenye ardhi pana tambarare, wakiwa wakubwa kama walivyokuwa, watamkanyaga, kila wanapomaliza kumkanyaga wa mwisho wao, wa mwanzo wao watarejeshwa kumkanyaga tena mpaka Allaah Atakapohukumu baina ya Waja Wake katika siku ambayo urefu wake ni miaka elfu khamsini. Halafu ataonyeshwa njia yake, ima ya kwenda Peponi, au ya kwenda motoni. Na hakuna yeyote mwenye kumiliki mbuzi na kondoo na asiwatolee Zakaah yake, isipokuwa atatandazwa kifudifudi mbele yao kwenye ardhi pana tambarare, wakiwa wakubwa kama walivyokuwa, watamkanyaga kwa kwato zao, na watampiga kwa pembe zao, hakuna kati yao mwenye pembe zilizopinda wala asiye na pembe, kila wanapomaliza kumkanyaga wa mwisho wao, wa mwanzo wao watarejeshwa kumkanyaga tena mpaka Allaah Atakapohukumu kati ya Waja Wake katika siku ambayo urefu wake ni miaka elfu khamsini katika mnayohesabu. Halafu ataonyeshwa njia yake, ima ya kwenda Peponi, au ya kwenda motoni…)). [Muslim (987) na Abu Daawuwd (1642)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
05-Shuruti Za Uwajibu Wa Kutoa Zakaah
Alhidaaya.com [3]
Zakaah si waajib katika mali isipokuwa kwa shuruti. Ni katika Hikma ya Allaah ‘Azza wa Jalla katika kufaradhisha Sharia Zake kuwa Ameziwekea shuruti; yaani sifa maalumu ambazo sharia hizo haziwi waajib bila kuwepo shuruti hizo, ili sharia hizo ziwe sawa madhubuti. Na kama kusingelikuwepo shuruti, basi kila kitu kingeweza kubeba uwezekano wa kuwa waajib au si waajib. Lakini pia kuna vizuizi vinavyoondosha uwajibu wa Zakaah pamoja na kuwepo shuruti, na vitu vyote havitimu ila kwa kukamilika shuruti zake na kutokuwepo vizuizi vyake. [Ash-Sharhu Al-Mumti’u]
Shuruti hizi zina vigawanyo viwili. Shuruti kwa mwenye mali aliyewajibikiwa Zakaah, na shuruti katika mali yenyewe.
Masharti ambayo ni lazima yakamilike kwa mwenye mali ili Zakaah iwe wajibu kwake
Mwenye mali ambaye amewajibikiwa na Zakaah ana masharti mawili:
1- Awe huru (muungwana)
Zakaah si waajib kwa mtumwa, kwa kuwa mtumwa hamiliki, bali bwana wake ndiye anayemiliki mali zake. Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa Salllam) anasema:
((من باع عبدا له مال، فماله للذي باعه إلا أن يشترط المبتاع))
((Mwenye kumuuza mtumwa anayemiliki mali, basi mali yake ni ya mwenye kumuuza ila tu kama mnunuzi atashurutisha)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2379) na Muslim (1173)
Na kauli ya ‘Umar (Radhwiya Allaahu ‘anhu):
((ليس في مال العبد زكاة حتى يعتق))
((Mali ya mtumwa haina Zakaah mpaka aachwe huru)). [Al-Bayhaqiy (1/108) kwa Sanad Swahiyh. Angalia Al-Irwaa (3/252)].
Na toka kwa Kiysaan bin Abiy Sa’ad Al-Maqbariy amesema: ((Nilimwendea ‘Umar na dirham mia mbili ya Zakaah ya mali yangu– nami ni mtumwa niliyeandikishiana mkataba na bwana wangu–akaniuliza: Je, umeachwa huru? Nikamwambia: Na’am. Akasema: Nenda ukaigawe)). [Muswannaf Ibn Abiy Shaybah kwa Sanad Jayyid katika Al-Irwaa (2/252)]
2- Awe Muislamu
Zakaah si waajib kwa kafiri kwa Ijma’a kwa kuwa Zakaah ni ‘ibaadah takatifu, na kafiri hana utakaso madhali yupo kwenye ukafiri wake. Tunaposema Zakaah si katika mali yake, tunamaanisha kuwa hatumlazimishi aitoe ili awe salama au apate amani. Zakaah haikubaliwi toka kwa makafiri, na hakuna faida kuwalazimisha kuitoa. Allaah Ta’aalaa Anasema:
((وَمَا مَنَعَهُمْ أَن تُقْبَلَ مِنْهُمْ نَفَقَاتُهُمْ إِلَّا أَنَّهُمْ كَفَرُوا بِاللَّـهِ وَبِرَسُولِهِ ))
((Na haikuwazuilia ikubaliwe kwao michango yao isipokuwa kwa kuwa wao walimkufuru Allaah na Rasuli Wake)). [At-Tawbah (9:54)]
Lakini hii haina maana kuwa kafiri hatohisabiwa kwa kuacha kutoa, kwa kuwa makafiri wanasemeshwa na vipengele vya sharia kwa mujibu wa ilivyopitishwa katika taaluma ya Uswuwl. Allaah Ndiye Mjuzi zaidi.
Hukmu hii yote ni kwa kafiri wa kuzaliwa. Ama aliyeritadi –tunajilinda kwa Allaah na hilo-, ikiwa Zakaah ilikuwa imemwajibikia wakati bado ni Muislamu, basi haisameheki kwa kuritadi kwa mujibu wa kauli ya Ash-Shaafi’iy na Hanbali, kwa kuwa ni haki ambayo uwajibu wake ulithibiti. Kuritadi hakuipomoshi, na mfano wake ni kama faini ya kuharibu vitu. [Al-Mawsuw’at Al-Fiqhiyyah (23/233 Kuwait) na Fiqhu Az-Zakaah (1/115)]
Lakini Hanbali anasema inafutika kwa kuritadi.
Je, Zakaah ni waajib kwa mali ya mtoto mdogo na mwendawazimu?
‘Ulamaa wana kauli mbili mashuhuri katika suala hili:
Ya kwanza:
Si waajib, sawasawa kwa mali yote au sehemu ya mali. [Al-Mughniy (2/622), Badaai’u Asw-Swanaai’i (2/4-5), Al-Majmuw’u (5/329), Al-Muhallaa (5/205) na Fiqhu Az-Zakaah (1/125)]
Hili kalisema Abu Haniyfah, na limesimuliwa pia toka kwa baadhi ya Masalaf. Wamesema kuwa Zakaah ni ‘ibaadah halisia kama Swalaah ambayo inahitajia niya, na mtoto au mwendawazimu hawana niya.
Isitoshe, mtoto na mwendawazimu hawana taklifu, hivyo si lazima kwao. Na Zakaah pia ni kitwaharisho kwa mtoaji wake, na utwaharisho ni kwa uchafu wa madhambi, na wawili hawa hawana dhambi. Kadhalika, kutochukua Zakaah katika mali yao ni sawa na kuilinda, kwa kuwa hawana uwezo wa kuiwekeza kiuchumi.
Ya pili:
Ni waajib kutoa Zakaah katika mali ya mtoto na mwendawazimu. [Al-Muhallaa (5/201), Al-Majmuw’u (5/329), Majmuw’u Al-Fataawaa (25/17), Al-Mawsuw’at Al-Fiqhiyyah (23/232) na Ash-Sharh Al-Mumti’u (6/26)]
Hii ni kauli ya Jumhuri. Pia ni kauli ya ‘Umar, ‘Aliyy, ‘Abdullaah bin ‘Umar, ‘Aaishah, na Jaabir bin ‘Abdullaah. [Angalia Muswannaf wa ‘Abdul Razzaaq (6986-6992), Muswannaf Ibn Abiy Shaybah (3/149), Sunan Al-Bayhaqiy (4/107), Al-Muhallaa (5/208) na Al-Amwaal cha Abiy ‘Ubayd (uk 448)]
Na hakuna Swahaba yeyote anayejulikana kuwa alikwenda kinyume na kauli hii isipokuwa riwaya dhwa’iyf ya Ibn ‘Abbaas ambayo haiwezi kutolewa dalili.
Kauli hii inatiliwa nguvu na:
- Ujumuishi wa Aayaat na Hadiyth zinazohabarisha uwajibu usio ainishi wa Zakaah katika mali ya matajiri. Katika Aayaat na Hadiyth hizo, mtoto na mwendawazimu hawakutolewa nje ya duara la uwajibu.
- Yaliyopokelewa toka kwa ‘Umar bin Al-Khattwaab aliyesema: ((Wekezeni mali za mayatima katika biashara, ili zisiliwe na Zakaah)). [Dhwa’iyf: Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (641), Muwattwau Maalik, Ad-Daaraqutwniy (2/111) na ‘Abdul Razzaaq (2) kwa Sanad Dhwa’iyf. Angalia Al-Irwaa (788)]
- Makusudio ya Zakaah ni kuziba pengo la mahitaji ya masikini kwa mali ya matajiri kama shukrani kutoka kwao kwa Allaah Ta’aalaa na kutakasa mali zao. Na mali ya mtoto na mwendawazimu inaweza kuingia katika matumizi na kulipia faini, kwa hiyo isibanwe kwa kutotolewa Zakaah.
- Zakaah ni haki ya mwanadamu, hivyo wajibu wa kuitoa uko sawa kwa mukallaf na asiye mukallaf.
Kauli hii ndiyo yenye nguvu. Na juu ya msingi huu, msimamizi wa mali zao atawatolea Zakaah kutoka mali hizo, kwa kuwa ni waajib.
Shuruti za mali ili iwajibikiwe na Zakaah
Ili mali iwajibikiwe na Zakaah, ni lazima iwe na shuruti zifuatazo:
1- Iwe ni katika sampuli (aina) ambazo ni lazima kuzitolea Zakaah. Hili litachambuliwa mbeleni.
2- Ifikie kiwango, nacho ni kiasi ambacho kikitimia, Allaah Amekiwekea uwajibu wa kukitolea Zakaah. Mtu ambaye hana kiwango hicho na akamiliki kilicho chini yake, au kamwe hakumiliki chochote, basi hawajibikiwi na Zakaah. Na hili linatofautiana kwa mujibu wa aina ya mali kama tutakavyobainisha mbeleni.
3- Mali iwe inamilikiwa umiliki kamili usio na shaka. Na dalili ya sharti hii, ni kunasibishwa mali kwa wamiliki wake kwenye Qur-aan na Hadiyth. [Fiqhu Az-Zakaah cha Al-Qaradhwaawiy (1/150)]
Ni kama katika Kauli Yake Ta’aalaa:
((خُذْ مِنْ أَمْوَالِهِمْ صَدَقَةً تُطَهِّرُهُمْ وَتُزَكِّيهِم بِهَا وَصَلِّ عَلَيْهِمْ ۖ إِنَّ صَلَاتَكَ سَكَنٌ لَّهُمْ ۗوَاللَّـهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ ))
((Chukua katika mali zao Swadaqah, uwatakase na ziwazidishie kwazo na waombee du’aa (na maghfirah). Hakika du’aa yako ni utulivu kwao. Allaah ni Mwenye kusikia yote, Mjuzi wa yote.)). [At-Tawbah (9:103)]
Na Kauli Yake:
((وَالَّذِينَ فِي أَمْوَالِهِمْ حَقٌّ مَّعْلُومٌ ))
((Na wale ambao katika mali zao kuna haki maalumu.)). [Al-Ma’aarij (70:24)]
Na neno lake Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((إن الله فرض عليهم في أموالهم))
((Hakika Allaah Amewafaradhia katika mali zao)).
Hii ni kwa kuwa Zakaah ni umilikishaji wa mali kwa wastahiki wake, na umilikishaji ni sehemu itokanayo na milki, na kwa hivyo ni lazima Zakaah itoke kwenye milki ya mtoaji.
‘Ulamaa wamevutana: Je, milki ni ya kuhodhi (kuwa nayo mkononi)? Ya kuyasarifu (kuyatumia)? Au asili ya milki? [Angalia Majmuw’u Al-Fataawaa (25/45)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
06-Zakaah Ya Madeni
Alhidaaya.com [3]
Na juu ya vipengee hivi vitatu, ‘Ulamaa wamekhitalifiana katika Zakaah ya deni. Je itamlazimu mwenye kudai kutoa kwa kuwa ndiye mmiliki halisi wa mali ambayo ni deni? Au itamlazimu mdaiwa kutoa kwa kuwa ndiye mwenye kuisarifu mali na mwenye kunufaika nayo? Au wote wawili husameheka kwa kuwa milki ya kila mmoja wao si milki kamili?
Kauli yenye uwiano mzuri zaidi kuhusu Zakaah ya deni, ni kusema deni ni la aina mbili:
1- Deni lenye matumaini ya kulipwa. Hili ni deni lililo mkononi mwa mwenye uwezo anayekiri kudaiwa deni hilo. Huyu ataiwahisha Zakaah yake pamoja na mali yake anayoimiliki kila mwaka.
Kauli hii imesimuliwa na Abu ‘Ubayda katika Kitabu cha Al-Amwaal (uk. 432) toka kwa ‘Umar, ‘Uthmaan na Ibn ‘Umar ambao ni katika Swahaba na wengineo katika Taabi’iyna.
2- Deni lisilo na matumaini ya kulipwa kutokana na hali ngumu ya mdaiwa isiyotarajika kupata faraja, au deni lililo kwa mtu anayelikanusha na hakuna uthibitisho.
(Hapa ‘Ulamaa wamekhitalifiana). Kuna wanaosema litatolewa Zakaah kwa miaka yote iliyolipitia deni hilo. Haya ni madhehebu ya ‘Aliy. [Isnaad yake ni Swahiyh. Amesimulia kutoka kwake Abu ‘Ubayd katika Al-Amwaal (431/1220), na Al-Bayhaqiy (4/150) kwa Sanad Swahiyh)]
Pia Ibn ‘Abbaas. Isnaad yake ni Dhwa’iyf. Imesimuliwa na Abu ‘Ubayd katika Al-Amwaal, na Al-Albaaniy kasema ni Dhwa’iyf katika Al-Irwaa (786).
Wengine wamesema atalitolea Zakaah ya mwaka mmoja anapolipokea. Ni madhehebu ya Abu Haniyfah.
Wengine wa mwisho wamesema hapaswi kutoa Zakaah kwa deni lililopitiwa na miaka na hata kwa mwaka aliolipwa. Ni madhehebu ya Abu Haniyfah.
Sheikh wa Uislamu amesema (52/84): “Kauli iliyo karibu zaidi ni kauli ya wale wasiowajibisha chochote wakati ule ule anapopokea deni mpaka upite mwaka, au wale wenye kuwajibisha Zakaah ya mwaka mmoja tu anapolipokea deni. Kauli hii ina picha yake, na ile ina picha yake”.
Imepokelewa kwa njia swahiyh toka kwa ‘Uthmaan bin ‘Affaan kuwa amesema:
((هَذَا شَهْرُ زَكَاتِكُمْ، فَمَنْ كَانَ عَلَيْهِ دَيْنٌ فَلْيُؤَدِّ دَيْنَهُ، حَتَّى تَحْصُلَ أَمْوَالُكُمْ، فَتُؤَدُّونَ مِنْهَا الزَّكَاةَ))
((Huu ni mwezi wa Zakaah yenu. Basi anayedaiwa alipe deni lake, ili mali zenu zipate [kiwango] mzitolee Zakaah toka humo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Maalik (591), na kutoka kwake Ash-Shaafi’iy (1/237) na Al-Bayhaqiy (4/148). Ni Swahiyh kama ilivyo kwenye Al-Irwaa (789)]
‘Aaishah amesema: ((Hakuna Zakaah katika deni [mpaka alipokee])). [Imekharijiwa na Ibn Abiy Shaybah (4/32) kwa njia mbili ambayo kila moja ni dhwa’iyf. Al-Albaaniy kasema ni Hasan katika Al-Irwaa (784)]
Faida
Mtu mwenye mali mkononi ambayo imewajibikiwa Zakaah na wakati huo huo anadaiwa, na deni hilo likamomonyoa kiwango chake cha kutolewa Zakaah au likapunguza mali isifikie kiwango, basi haina Zakaah.
Na likiwa deni linapunguza mali lakini kiwango cha kutolewa Zakaah kikazidi, basi atalipa deni lake kamili na ataitolea Zakaah mali iliyobakia. Kwa mfano, ikiwa mali yake ni dinari 30, na anadaiwa dinari tano, ataitolea Zakaah dinari 25.
4- Mali ipitiwe na mwaka kamili wa Hijria (ikiwa mkononi mwa mmiliki).
Hili limeshurutishwa katika Zakaah ya dhahabu, fedha (silva) na mifugo. Ama mazao na matunda, sharti hili halipo. Mwaka wa mazao na matunda ni pale yanapokomaa vizuri na kuiva. Hili limekubaliwa na Fuqahaaul Amswaar. [Bidaayatul Mujtahid (2/261-262) na Majmuw’u Al-Fataawaa (14/25)]
Na hapa linakuja swali:
Nini hukmu ya mali inayotumika ndani ya mwaka?
Mali inayopatiwa manufaa ndani ya mwaka ina vigawanyo vitatu: [Al-Mughniy (2/626), (3/32), Fat-hul Qadiyr cha Ibn Al-Hamaam (1/510) na Al-Mawsuw’at Al-Fiqhiyyah (23/244)]
1- Ikiwa mali inayopatiwa manufaa imetokana na faida ya mali aliyonayo (ambayo haikuchanganyika na nyingine) kama faida ya mali ya biashara na zao la mifugo, basi mali hii (faida) ni lazima ijumuishwe kwenye asili yake (mtaji wa asili), na mwaka wake utahesabiwa sambamba na mwaka wa mali ya asili. Ibn Qudaamah amesema: “Hatujui mvutano wowote kwenye hili”. [Inaonyesha Ibn Hazm hakukubaliana na hili. Angalia Al-Muhallaa (6/82 na kurasa zinazofuatia]
2- Ikiwa mali inayopatiwa manufaa haitokani na aina ya mali aliyonayo kama mali yake kuwa ni ngamia, kisha akapata faida kutokana na dhahabu ya urithi au mfano wake, basi faida hii ya dhahabu itahesabiwa mwaka wake tokea siku alipoanza kuipatia manufaa kama itafikia kiwango (cha kutolewa Zakaah). Haitofungamanishwa na mwaka wa mali yake ya asili (ya ngamia).
3- Ikiwa mali inayopatiwa manufaa inatokana na mali ile ile aliyonayo -ambayo imefikia kiwango– lakini mali hii inayopatiwa manufaa haitokani na faida ya mali ya asili, na mfano wake ni kama mtu kuwa na mbuzi au kondoo arobaini waliopitiwa na sehemu ya mwaka, kisha akanunua wengine 100 au akapewa bure, basi hapa kuna madhehebu mawili:
La kwanza: Ataichanganya mali ya pili kwenye mali ya asili katika kiwango tu na si kwa mwaka, na kila moja ataitolea Zakaah yake kwa mwaka wake maalum. Ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na Hanbali.
Ya pili: Ataichanganya mali ya pili kwenye mali ya asili –atazitolea zote mbili Zakaah– ukitimia mwaka wa mali ya kwanza. Ni madhehebu ya Hanafiy.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
07-Aina Za Mali Ambazo Ni Waajib Kuzitolea Zakaah
Alhidaaya.com [3]
‘Ulamaa wamekhitilafiana kwa mapana na marefu kuhusu aina za mali ambazo ni lazima zitolewe Zakaah. Kuna waliobana na kushikilia aina zile zile tu zilizotajwa bayana kwenye Aayaat na Ahaadiyth. [Ni kama Ibn Hazm, kisha Ash-Shawkaaniy na Swiddiyq Khaan (Rahimahumul Laah)]
Wengine wametanua wigo na kuingiza kila mali inayostawi hata pia kutoshurutisha kufikia kiwango cha Zakaah kwa baadhi ya mali hizo. [Ni kama Abu Haniyfah (Rahimahul Laah)]
Wabanaji wanasemaje kuhusu mwelekeo wao huo?
Mwono wa Ibn Hazm na waliokubaliana na rai yake kuhusu wajibu wa Zakaah katika aina zile zile tu nane ambazo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alichukua Zakaah, uko juu ya mambo mawili: [Angalia Fiqhu Az-Zakaah (1/165)]
1- Uharamu uliothibiti kwa Hadiyth na Aayah juu ya mali ya Muislam. Haijuzu kuchukua chochote katika mali yake isipokuwa kwa maelekezo ya Aayah au Hadiyth.
2- Zakaah ni kalifisho la kisharia. Na dhima za watu kiasli hazina makalifisho isipokuwa yale tu yaliyokuja katika matini (Qur-aan au Hadiyth) ili tusije kuingiza sharia katika diyn ambayo Allaah Hakuiruhusu.
Ama Al-Qiyaas, hilo halijuzu kulitumia na hususan katika mlango wa Zakaah.
Waliotanua wigo wa mali za Zakaah wanasemaje kuhusu mwono wao?
Waliofungua milango zaidi ya aina za mali zinazolazimu kutolewa Zakaah, hawa njia yao imesimamia juu ya misingi ya uswuwl. Kati yake ni:
1- Kutoa dalili kwa kutumia ujumuishi wa Aayah za Qur-aan na Sunnah zinazosema kuwa kila mali ina haki ndani yake au swadaqah.
2- Matajiri wote na mali zao zote, wanahitajia kutakaswa na kutwaharishwa.
3- Kwa mazingatio ya ustawi na faida wamesema: “Mwenye kumiliki majengo na viwanda ambavyo vinamletea faida nyingi maradufu ya faida anayoipata kutokana na ardhi ya kilimo, ana haki zaidi ya kutoa Zakaah”.
4- Kuzingatia maslaha ya wote kwa kukidhi mahitaji ya masikini na fakiri na pia kuasisi maslaha jumuiya ya Waislamu wote.
Aina ambazo zimekubaliwa na wote kuwa ni lazima zitolewe Zakaah
‘Ulamaa kwa Ijma’a wamekubaliana kuwa ni waajib kuzitolea Zakaah aina tisa za mali:
1,2- Dhahabu na fedha (silver) [An-Naqdayn]
3,4,5- Ngamia, ng’ombe, mbuzi na kondoo (mifugo).
6,7,8,9- Ngano, shayiri (barley), tende na zabibu kavu (mazao na matunda). [Haikuthibiti Ibn Hazm kuzungumzia zabibu kavu, hakugusia, bali amezizungumzia sampuli nane nyingine. Angalia Al-Muhallaa (5/209)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
08-Zakaah Ya Dhahabu Na Fedha (Silver)
Alhidaaya.com [3]
Ikiwa masharti tuliyoyataja yatakamilika katika dhahabu na fedha pamoja na mmiliki wake, zikafikia kiwango, zikapitiwa na mwaka mmoja na mfano wa hivyo, basi hapo itabidi zitolewe Zakaah, na itakuwa mara moja tu kila mwaka.
Kiwango cha dhahabu na fedha na kiasi cha Zakaah ya kila kimoja
Imekuja katika Hadiyth ya ‘Aliyy bin Abiy Twaalib (Radhwiya Allaahu ‘anhu) toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akisema:
((إذا كانت لك مائتا درهم وحال عليها الحول، ففيها خمسة دراهم، وليس عليك شيء - يعني في الذهب- يكون لك عشرون دينارا، فإذا كانت لك عشرون دينارا، وحال عليها الحول ففيها نصف دينار))
((Ikiwa una dirham 200 na zikapitiwa na mwaka, basi kuna dirham 5 ndani yake, na hupaswi na chochote – yaani katika dhahabu – mpaka uwe na dinari 20. Kama una dinari 20 na zikapitiwa na mwaka, basi kuna nusu dinari ndani yake)). [Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (1558), At-Tirmidhiy (616), An-Nasaaiy (5/37), Ibn Maajah (1790) na Ahmad (1/121). Al-Bukhaariy kasema ni Swahiyh – kama alivyonukuu toka kwake At-Tirmidhiy – na Al-Haafidh ameifanya ni Hasan katika Al Fat-h. Na katika Swahiyh Abiy Daawuud (1391), Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh]
Na Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((ليس فيما دون خمس أواق من الورق صدقة))
((Hakuna Zakaah chini ya wakia (ounce) tano ya fedha [silver])). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1484) na Muslim (979)]
أواق ni wingi (plural) wa أوقية (singular) . Na wakia moja ni sawa na dirham 40 kwa makubaliano ya wataalamu. Hivyo wakia 5 zitakuwa sawa na dirham 200 (5×40)]
Tunajifunza kutokana na viwili hivi mambo kadhaa:
Kwanza: Ni kwamba:
- Kiwango cha fedha ya wakia (5) ambayo ni sawa na dirham 200 ya fedha safi, ni sawa na gram 595 za fedha.
- Kiwango cha dinari 20 za dhahabu ni sawa na mithqali 20, na mithqali 20 ni sawa na gram 85 za dhahabu krati 24, gramu 97 za dhahabu krati 21, na gramu 113 za dhahabu krati 18.
Pili: Ni lazima mwaka kamili wa Hijria ukipitie kiwango na zaidi ili Zakaah ipate uwajibu wa kutolewa.
Tatu: Kiasi cha Zakaah kwa dhahabu na fedha (silva) ni 2.5%= 1/40 (moja ya arobaini)
Mfano bainishi:
Mtu anamiliki nusu kilo ya dhahabu ya krati 24. Ni kiasi gani cha Zakaah atatoa ikipitiwa na mwaka?
Tunasema: Kwa kuwa kiasi cha dhahabu inayomilikiwa ni zaidi ya kiwango (gramu 85), hapa itabidi itolewe 2.5% (asilimia mbili na nusu). Kipimo cha wajibu kutolewa kitakuwa ni 500 gr X 1/40 = 12.5 gr
Itatolewa gramu 12.5 katika gramu 500 (ya dhahabu).
Je, dhahabu inaweza kuchanganywa na fedha ili kukamilisha kiwango?
Mtu akiwa na dhahabu isiyotimiza kiwango, na kiasi kingine cha fedha isiyotimiza kiwango, hapa ‘Ulamaa wana kauli mbili:
Ya kwanza:
Ataichanganya dhahabu na fedha ili kiwango kitimie halafu atatoa Zakaah. Ni madhehebu ya Jumhuri ya ‘Ulamaa (Abu Haniyfah na Maalik, na ni riwaya toka kwa Ahmad, na kauli ya Ath-Thawriy na Al-Awzaa’iy).
Dalili yao wanasema kuwa manufaa ya viwili hivyo ni mamoja, ni vitu vya thamani, na hukusudiwa kwavyo biashara. [Al-Mawsuw’at Al-Fiqhiyyah (23/267)]
Ya pili:
Hachanganyi kimoja na kingine. Ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy, riwaya toka kwa Ahmad, kauli ya Abiy ‘Ubayd, Ibn Abiy Laylaa, Abiy Thawr na Ibn Hazm. Kauli hii imekhitariwa na Al-Albaaniy na Ibn ‘Uthaymiyn, nayo ndiyo yenye nguvu In Shaa Allaah. [Ibn Hazm katika Al-Muhallaa (6/82), Al-Albaaniy katika Tamaam Al-Minnah (uk 360) na Ibn ‘Uthaymiyn katika Ash-Sharhu Al-Mumtií (6/107)]
Dalili zao:
1- Ujumuishi wa kauli yake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((ليس فيما دون خمس أواق من الورق صدقة))
((Hakuna Zakaah chini ya wakia tano ya fedha)). [Takhriyj yake imetajwa nyuma kidogo]
Na kauli yake:
((ليس عليك شيء –يعنني في الذهب- حنى يكون لك عشرون دينارا))
((Huwajibikiwi na chochote –yaani katika dhahabu – mpaka uwe na dinari 20)). [Takhriyj yake imetajwa nyuma kidogo]
Hadiyth hizi mbili zinadulisha kuwa mwenye kuchanganya dhahabu na fedha, anakuwa amewajibisha Zakaah ya kila kimoja ya viwili hivi chini ya kiwango chake.
2- Kuchukulia kipimo kwa ngómbe, mbuzi na kondoo, –uchambuzi wake utakuja– hawa kiwango cha mmoja hakikamilishwi kwa mwingine pamoja na kuwa lengo la kuwa nao ni moja, nalo ni kuwazalisha. Aidha, shayiri haichanganywi na ngano hata kwa wenye kusema dhahabu huchanganywa na fedha (silver). Aina moja haichanganywi na aina nyingine. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Faida
Mali ya wabadilishaji pesa (sarafu) hutolewa ndani ya duara hili. Hawa dhahabu na fedha huchanganywa ndani ya mali yao, na sio kuchanganya aina moja na nyingine. Na kwa vile lengo la viwili hivi ni biashara, basi vinakuwa ni mali ya biashara. [Ash-Sharhu Al-Mumtií (6/109). Angalia Al-Mughniy (3/2-3)]
Tukikubaliana na kauli ya kuchanganya, je huchanganywa sehemu au thamani?
Wenye kujuzisha kuchanganya dhahabu na fedha wamekhitalifiana juu ya kauli mbili:
1- Maalik, Abu Yuwsuf, Muhammad na Ahmad katika riwaya yake, wanasema uchanganyaji unakuwa ni kwa sehemu. [Al-Mawsuw’at Al-Fiqhiyyah (23/267)]
Maana ya hii ni kuwa mwenye nusu ya kiwango cha dhahabu na nusu ya kiwango cha fedha, Zakaah itamwajibikia. Vile vile, kama ana robo ya kiwango cha kimojawapo, na robo tatu ya kingine, au mfano wa hivyo. Kisha atatoa 2.5% kwa kila kimoja.
2- Ama Abu Haniyfah, yeye anaona kimoja kichanganywe na kingine kwa kutiwa thamani ya kimoja kwa kingine kwa namna ya kuwanufaisha zaidi masikini. Kwa maana nyingine, kingi kichanganywe kwenye kichache. [Angalia iliyotangulia]
Kwa mfano, ikiwa ana nusu ya kiwango cha fedha na robo ya kiwango cha dhahabu, na robo ya kiwango cha dhahabu ikawa thamani yake sawa na nusu ya kiwango cha fedha, hapo Zakaah itakuwa lazima kwake.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
09-Zakaah Katika Pesa Za Noti (Bank Note)
Alhidaaya.com [3]
Uoanisho (uendanishaji) wake wa Kifiqhi
Kutokana na uchache wa kuamiliana watu katika wakati wetu wa leo na dhahabu na fedha na badala yake kutumia zaidi sarafu za noti almaarufu kama (banknotes), Fuqahaa wamekumbana na changamoto ya “Uoanishaji wa Kifiqhi kwa sarafu za noti”, na ‘Ulamaa wa sharia wamepigana kufa na kupona ili kutohoa hukmu kwa aina hii mpya ya pesa kwa mujibu wa walivyoendanisha na kuiainisha nguvu ya pesa hii.
Katika suala hili, nimeziangalia kwa utaamuli kauli tano za ‘Ulamaa: [An-Nuquwd.. Wadhwaaifuhaa Al-Asaasiyya Waahkaamuhaa Ash-Shar-’iyyah cha ‘Alaaud Diyn Za’atariy (uk. 329 na zinazofuatia). Ni utafiti wenye faida kubwa sana]
1- Ni kuwa pesa hizi ni dhamana za madeni (debt securities) juu ya upande ulizozitoa
Wamekubali na kupitisha kuwa hii ndiyo hali yake halisi kwa mujibu wa muktadha wa tamko la kukiri deni lililosajiliwa katika kila noti ya sarafu. Na kwa ajili hiyo, wametumia juu yake hukmu za kuamiliana na dhamana za madeni. [Kati ya waliosema hili ni Baraza Kuu la ‘Ulamaa wa Al-Azhar na Al-‘Allaamah Ash-Shanqiytwiy katika Adhwaaul Bayaan (1/257)]
Kati ya tija hasi za uoanishaji huu ni kuwa pesa hizi zitaingia kwenye duara la mvutano tulioutaja nyuma kati ya ‘Ulamaa kuhusiana na Zakaah ya deni. Hivyo basi, ambaye haoni ulazima wa kutoa Zakaah ya deni, atazuia pia kuitoa katika pesa hizi.
Kadhalika, kama pesa hizi ni dhamana za madeni, basi haijuzu kuziuzia kama deni kutokana na Ijma’a isemayo kuwa haijuzu kuuza deni kwa deni. Ukiongezea na hilo, ikiwa dhamana za madeni zimechovywa dhahabu na fedha, basi haijuzu kamwe kununuliwa kwazo dhahabu na fedha, kwa kuwa sharti lililopo hapa ni kukabidhishana mkono kwa mkono, nalo halipo.
2- Ni kuwa pesa hizi ni mali kati ya mali ya biashara na bidhaa kati ya bidhaa [Kati ya waliosema hili ni As-Sa’adiyy (Rahimahul Laah) kama ilivyo katika kitabu cha Al-Fataawaa As-Sa’adiyyah (uk 338-339). Lakini mwanafunzi wake Ibn ‘Uthaymiyn (Rahimahul Laah) hakukubaliana naye]
Wamekubali kuielezea kama ni mali itiwayo thamani ambapo matashi hutofautiana kwayo, na huingia ndani ya kanuni ya ugavi na mahitaji (supply and demand). Hivyo basi, wamejaribu kutumia hukmu za kifiqhi zinazohusiana na mali za biashara katika sarafu hizi.
Kati ya tija hasi za uoanishaji huu ni kuwa unafungua mlango wa riba, kwani kuzizingatia pesa hizi kama mali za biashara, itajuzu kuziuza zenyewe kwa zenyewe kwa kuzidiana ubora hata kama ni za aina moja! Na hii ni haramu halisi.
Kadhalika, hazitowajibikiwa na Zakaah kwa kuwa ni mali za biashara ikiwa hazikutayarishwa kwa ajili ya biashara na kuzalishwa!
3- Ni kuwa pesa hizi zinafanana na “coins” zilizofuliwa kutokana na madini nyinginezo zisizo dhahabu au fedha kama shaba au nikeli
[Kati ya waliosema hili ni Mustwafaa Az Zarqaa kama Ibn Maniy’i alivyomnukuu katika kitabu cha Al-Waraq An-Naqdiy (uk 147)]
Wamesema: “Ni kama pesa zilizotengenezwa kwa karatasi, na thamani ya fedha hizi inategemea desturi na mazoea ya watu, na si thamani ya mada iliyotengenezewa”.
Pesa hizi zinaangaliwa kwa mazingatio mawili: (Kwanza), zingatio la asili yake ambayo ni (mali). Kwa kuwa asili ya shaba, nikeli na mfano wake, ni katika mali ambazo huuzwa na kununuliwa. (Pili), zingatio la maishilio yake ya kuwa kitu kingine ambacho ni (thamani).
Mwenye kuangalia asili yake, ataona kuna tija hasi zilizoelezewa katika mali za biashara. Na mwenye kuangalia mgeuko wake wa kuwa kitu kingine ambacho ni thamani, basi atabakiwa na mushkeli, nao ni kutofautiana pesa na sarafu hizi za karatasi kwa njia mbalimbali jambo linalozuia kuziweka pamoja sarafu za karatasi na pesa ambazo ziko chini yake kihadhi na kifanisi. [Angalia katika An-Nuquwd cha Az-Za-’atariy (uk. 346 na zinazofuatia)]
4- Ni kuwa pesa hizi zinachipukia kutoka kwenye dhahabu na fedha [Kati ya waliosema hili, ni Sheikh ‘Abdul Razzaaq ‘Afiyfiy (Rahimahul Laah) ambaye alikuwa mjumbe wa Bodi ya ‘Ulamaa Wakuu wa Saudia]
Wamesema: “Noti ni badala ya viwili hivi (dhahabu na fedha), na wakapitisha kuwa kutolesha noti kunahitajia kuichovya kwa dhahabu au fedha. Na kama mchovyo wa sarafu ni dhahabu, basi hukmu yake ni hukmu ya dhahabu, na kama ni fedha, basi hukmu yake ni fedha”.
Na kati ya tija hasi za uoanishaji huu ni kuwa kwa sasa hakuna ulimwenguni sarafu mbili zilizo sawa kithamani pamoja na kuwa zimetokana na tawi moja la dhahabu. Hivyo, kutokana na sababu hii, inalazimu kutojuzu kuzidiana wakati wa kubadili dinari ya Kuwait kwa dinari ya Libya –kwa mfano- bali ni lazima ziwe sawa –kwa msingi kwamba jinsi yao ni moja- huku tofauti kati yao ni kubwa!
Halafu kuftaridhi (assume) kuwepo mchovyo kamili wa dhahabu au fedha kwenye sarafu ya noti, kunatenguliwa na hukmu ya uhalisia wa hali unaothibitisha kwamba pesa zinategemea zaidi nguvu ya dola (nchi) na ushawishi wa mamlaka yake.
5- Ni kwamba noti ni sarafu inayojitegemea yenyewe
[Hili limesemwa na Bodi ya ‘Ulamaa Wakuu wa Saudia (azimio namba 10) lililopitishwa tarehe 17/4/1393 Hijria, Dk. Al-Qaradhwaawiy na wengineo]
Wamesema: “Kwa kuwa kila mali yenye kubeba thamani ambayo watu huitegemea katika kufanya kazi za sarafu, basi huchukua sifa ya uthamani. Na hivyo basi, inafaa kuwa sarafu na hususan pakizingatiwa kuwa katika sharia hakuna kinachoashiria kuwa ni dhahabu na fedha tu ndivyo vyenye thamani”.
Sheikh wa Uislamu Ibn Taymiyyah alidokeza kuwa ikiwa watu watakubaliana kukifanya kitu thamani, basi kitachukua hukmu ya thamani. Akasema: “Pesa zikiwa ni thamani na zikawa na jina, basi thamani haiuzwi kwa thamani kwa malipo ya mbeleni”. [Majmuw’u Al-Fataawaa (30/472)]
Akasisitiza kuwa uthamani hauishilii tu kwenye dhahabu na fedha (silver), bali marejeo katika hili ni mazoea na desturi ya watu na wanavyokubaliana wenyewe. Akasema: “Äma dirham na dinari, hakuna mpaka wa kikawaida au wa kisharia unaojulikana kuhusiana na sarafu hizi, bali marejeo yake ni kwa mazoea ya watu na wanavyokubaliana. Na hii ni kwa vile, kiasli, kuzikusudia hakufungamani nazo, bali lengo ni kuwa kipimo cha watu kuamiliana nacho..”[Majmuw’u Al-Fataawaa (19/251)]
Ninasema: “Huenda kauli hii ya mwisho inayosema kuwa sarafu za noti ni thamani ambayo hubeba hukmu za vitu vya thamani, ndiyo kauli sahihi. Kwayo, miamala tofauti ya kimali huratibiwa”.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
10-Kiwango Cha Zakaah Ya Noti (Bank Note)
Alhidaaya.com [3]
Kuna ‘Ulamaa wa enzi yetu ya leo ambao wanaona kuwa Zakaah ya “bank note” ikadiriwe kwa kiwango cha fedha, kwa kuwa ukadiriaji huu una manufaa zaidi kwa masikini.
Lakini wengine wanaona kuwa kiwango chake ni kiwango cha dhahabu, kwa kuwa thamani ya fedha ilibadilika baada ya enzi ya Nabiy na waliokuja baada yake mpaka ikapoteza thamani yake kabisa kinyume na dhahabu ambayo thamani yake kwa kiasi kikubwa inaonekana kutulia na kuimarika.
Halafu, kiwango cha dhahabu kiko karibu na viwango vyingine vya Zakaah kama ngamia watano, mbuzi au kondoo arobaini na kadhalika. Kwani vipi ikubalike na akili Uislamu usiwajibishe Zakaah kwa mwenye kumiliki ngamia wanne au kondoo 39 na kumzingatia kama masikini, halafu uje kuwajibisha Zakaah kwa mwenye kumiliki kiwango cha fedha ambacho hawezi hata kununulia mbuzi mmoja na kumzingatia kama tajiri?
Hakuna shaka kuwa madhehebu haya yako sawa zaidi. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Mfano bainishi:
Mtu mmoja ana pauni 2,000 na mwingine ana pauni 100,000. Ni kiasi gani cha Zakaah atatoa kila mmoja wao baada ya kupita mwaka?
Jibu:
Kwanza, tunahitaji kujua kiasi cha kiwango cha dhahabu kama ilivyotangulia ambazo ni gramu 85. Tukisema kwa mfano thamani ya gramu moja ya dhahabu ni sawa na pauni 30, kiwango kitakuwa: 85×30 = pauni 2,550. Na kwa kuwa anachokimiliki mtu wa kwanza ni chini ya kiwango, basi Zakaah si wajibu juu yake isipokuwa kama ataamua tu kutoa swadaqah.
Ama mtu wa pili, huyu anamiliki kiasi ambacho ni kikubwa kuliko kiwango. Huyu ni lazima atoe 2.5%. Zakaah yake itakuwa:
100,000 ÷ 40 = pauni 2,500 au 2.5 ÷ 100 × 100,000 = pauni 2,500
Hivyo atatoa pauni 2,500 kama Zakaah.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
11-Zakaah Ya Mapambo
Alhidaaya.com [3]
Wanachuoni wa Salaf na Khalaf wamekhitalifiana kwa kauli mbalimbali kuhusu Zakaah ya mapambo ya dhahabu na fedha. Kuna kauli mbili mashuhuri zaidi kati ya hizo:
Ya kwanza:
Hakuna Zakaah katika mapambo ya kawaida ya mwanamke ya dhahabu na fedha (anayoyavaa). Haya ni madhehebu ya Jumhuri ya ‘Ulamaa. [Ad-Durru Al-Mukhtaar (2/41), Bidaayatul Mujtahid (1/242), Al-Majmuw’u (6/29) na Al-Mughniy (3/9-17)]
Ni kauli ya Ibn ‘Umar, Jaabir, ‘Aaishah na Asmaa bint Abiy Bakr ambao ni katika Swahaba. Dalili zao ni:
1- Hadiyth:
((ليس في الحلي زكاة))
((Hakuna Zakaah katika vipambo)). [Ibn Al-Jawziy katika At-Tahqiyq. Al-Bayhaqiy na wengineo wameihukumu kuwa haifai. Angalia Al-Irwaa (817)]
Ni Hadiyth Baatwil Marfu’u, na la sawa ni iwe mawquwf kwa Jaabir.
2- Imepokelewa toka kwa Naafi’u kuwa Ibn ‘Umar alikuwa akiwapamba mabinti zake na vijakazi wake kwa dhahabu, na haitolei Zakaah. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Maalik (585) na Al-Bayhaqiy (4/138) kwa Sanad Swahiyh]
3- Kauli ya Ibn ‘Umar: ((Hakuna Zakaah katika vipambo)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na ‘Abdul Razzaaq (4/82), Ibn Shaybah (3/154) na Ad-Daaraqutwniy (2/109) kwa Sanad Swahiyh]
4- Kauli ya Jaabir bin ‘Abdillaah alipoulizwa kama kuna Zakaah katika vipambo, akasema: “Hakuna”. Akaulizwa: “Hata vikifikia dinari alfu?” Jaabir akasema: “Nyingi”. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na ‘Abdul Razzaaq (4/82) na Al-Bayhaqiy (4/138) kwa Sanad Swahiyh]
Na katika riwaya amesema: “Huazimwa na huvaliwa” . [Riwaya hii ni ya Ibn Abiy Shaybah (3/155)]
5- Toka kwa ‘Aaishah ya kuwa alikuwa akiwasimamia mabanati yatima wa kaka yake chini ya ulezi wake. Walikuwa na mapambo na hatoi Zakaah ya vipambo vyao. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Maalik (584) na ‘Abdul Razzaaq (4/83), nayo ni Swahiyh]
6- Toka kwa Asmaa kuwa alikuwa hatoi Zakaah ya vipambo. [Muswannaf Ibn Abiy Shaybah (3/155) kwa Sanad Swahiyh]
7- Wanasema: “Zakaah inakuwa katika mali inayozalika na kulindwa. Na vipambo vilivyoruhusiwa havizalishi kitu, ni kama nguo tu. Lakini ikiwa atavihifadhi na kuvifanya hazina ya mali, au akavitayarisha kwa biashara, basi vitatolewa Zakaah”.
Angalizo:
Wenye kauli hii wanashurutisha kipambo kiwe katika vyenye kuruhusika kisharia. Kama haviruhusiki kama mwanamume kujiwekea dhahabu, basi ni lazima atoe Zakaah.
Ya pili:
Mapambo yote ya dhahabu na fedha ni lazima yatolewe Zakaah kama yatafikia kiwango na kupitiwa na mwaka, ni sawa yakawa ya kuvaliwa, au ya kuwekwa akiba, au ya kutayarishwa kwa biashara. [Ni madhehebu ya Abu Haniyfah, riwaya toka kwa Ahmad na Ibn Hazm. Angalia Fat-hul Qadiyr (1/524), Ad-Durru Al-Mukhtaar (2/41) na Al-Muhallaa (6/78). Ni kauli ya Ibn Mas’uwd, ‘Umar, ‘Abdullaah bin ‘Amri na riwaya toka kwa ‘Aaishah]
Hoja za kauli hii ni: [Angalia Jaami’u Ahkaamin Nisaa (2/143) na yanayofuatia ya Sheikh wetu Mustwafaa bin Al-‘Adawiy]
1- Ujumuishi uliokuja kwenye Qur-aan Tukufu kama Neno Lake Ta’aalaa:
((وَالَّذِينَ يَكْنِزُونَ الذَّهَبَ وَالْفِضَّةَ وَلَا يُنفِقُونَهَا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ فَبَشِّرْهُم بِعَذَابٍ أَلِيمٍ))
((Na wale wanaorundika dhahabu na fedha (silver) na wala hawazitoi katika Njia ya Allaah, basi wabashirie adhabu iumizayo)). [At-Tawbah (9:34)]
2- Hadiyth jumla zilizopokelewa toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) zenye kuamuru kutoa Zakaah ya dhahabu na fedha kama neno lake:
((ما من صاحب ذهب لا يؤدي ما فيها إلا جعل له يوم القيامة صفائح من نار يكوى بها))
((Hakuna yeyote mwenye dhahabu ambayo haitolei yanayostahiki ndani yake, isipokuwa itatengenezwa kwa ajili yake Siku ya Qiyaamah vipande vya bati vya moto ababuliwe navyo.…)). [Imekharijiwa nyuma kidogo]
3- Hadiyth mahsusi zilizokuja kuhusiana na utoaji wa Zakaah ya vipambo na makamio kwa asiyetoa. Kati ya Hadiyth hizo:
(a) Hadiyth ya ‘Amri bin Shu’ayb toka kwa baba yake toka kwa babu yake: ((Kuwa mwanamke mmoja alimwendea Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akiwa na binti yake, na binti amevaa mkononi bangili mbili nzito za dhahabu. Akamwambia: ((Je, unatoa Zakaah ya hivi?)) Akasema: Hapana. Akasema: ((Je, utapenda Allaah Akuvalishe kwazo bangili mbili za moto Siku ya Qiyaamah?)) Akasema: Akazivua na kuzitupa kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: Ni za Allaah ‘Azza wa Jalla na Rasuli Wake)). [Swahiyh Lishawaahidihi. Imekharijiwa na Abu Daawuud (1563), An-Nasaaiy (5/38), At-Tirmidhiy (637) na Ahmad (2/178)]
(b) Hadiyth ya ‘Abdullaah bin Shaddaad aliyesema: ((Tuliingia kwa ‘Aaishah mke wa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akasema: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliingia kwangu akaona mkononi mwangu pete kubwa za fedha. Akauliza: Nini hii ee ‘Aaishah? Nikasema: “Nimezitengeneza ili nijipambie kwa ajili yako ee Rasuli wa Allaah”. Akauliza: ((Je, unazitolea Zakaah?)) Nikasema: “Hapana, au Maa Shaa Allaah”. Akasema: ((Hiyo itakutosheleza wewe na moto)). [Hasan Lishawaahidih. Imekharijiwa na Abu Daawuud (1565), Ad-Daaraqutwniy (2/105), Al-Haakim (1/389) na Al-Bayhaqiy (4/139). Katika Isnaad yake kuna maneno yanayoyaunga ya kabla yake]
(c) Hadiyth ya Asmaa binti Yaziyd aliyesema: ((Niliingia mimi na khalati yangu kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) naye [khalati] amevaa bangili za dhahabu. Akatuuliza: ((Je, mnazitolea Zakaah yake?)) Tukajibu: “Hapana”. Akasema: ((Hivi hamwogopi Allaah kuwavisheni kwazo bangili za moto? Toeni Zakaah yake)). [Hasan Lishawaahidihi. Imekharijiwa na Ahmad (6/461), na At-Twabaraaniy katika Al-Kabiyr (24/181). Sanad yake ni Hasan kwa nyingine zenye kuitilia nguvu zilizotangulia]
4- Athar zilizopokelewa toka kwa baadhi ya Swahaba kama:
(a) Athar ya Ibn Mas’uwd: ((Kuwa mwanamke mmoja alimuuliza kuhusu Zakaah ya vipambo naye akasema: “Vikifikia dirhamu 200 basi vitolee Zakaah”. Akasema: “Mimi ninawalea na kuwasimamia mayatima wangu, je niwape wao? Akasema: “Ndio”)). [Swahiyh Lighayrihi. Imekharijiwa na Abdur-Razzaaq (4/83) na At-Twabaraaniy (9/371) kwa Sanad Swahiyh Lighayrih]
(b) Athar ya ‘Umar: ((Ya kuwa aliandika kwa Abu Muwsaa Al-Ash-‘Ariy akimwambia: Waamuru wanawake wa Kiislamu walioko kwako watolee Zakaah vipambo vyao)). [Na katika riwaya: Vipambo vitolewe Zakaah] [Ibn Abiy Shaybah (3/153), Al-Bukhaariy katika At-Taariykh Al-Kabiyr (4/217) na Al-Bayhaqiy. Sanad yake ni Mursal]
(c) Athar ya ‘Abdullaah bin ‘Amri: ((Ya kuwa yeye alikuwa akimwandikia mweka hazina wake Saalim atoe Zakaah ya vipambo vya mabanati zake kila mwaka)). [Sunan Ad-Daaraqutwniy (2/107) kwa Sanad Hasan]
(d) Athar ya ‘Aaishah kuwa amesema: ((Hakuna ubaya kuvaa vipambo vikitolewa Zakaah yake)). [Ad-Daaraqutwniy (2/107) na Al-Bayhaqiy (4/139) na Sanad yake ni Hasan]
Madhehebu haya yamesemwa kuwa sahihi kwa Sa’iyd bin Al-Musayyib, Sa’iyd bin Jubayr, Ibraahiym An-Nakh’iy, ‘Atwaa bin Abiy Rabbaah, Az-Zuhriy, ‘Abdullaah bin Shaddaad, Sufyaan Ath-Thawriy na wengineo kama alivyonukuu hilo Sheikh wetu –Allaah Amhifadhi– katika kitabu cha Jaami’u Ahkaamin Nisaa (2/156-157).
Kauli yenye nguvu
Baada ya kuziweka bayana dalili za makundi mawili, ninaloliona lenye nguvu –kwa upande wangu- na ‘ilmu ya yote iko kwa Allaah Ta’alaa, ni kuwa kauli isemayo ni waajib kutoa Zakaah kwa mapambo ya dhahabu na fedha katika hali zote madhali yamefikia kiwango na kupitiwa na mwaka, ndio dalili imara zaidi, yenye kinga zaidi kuitumia, na kwayo mtu hutoka kwenye mvutano.
Zakaah si waajib katika mapambo ya lulu na vito vya thamani
Ukitoa dhahabu na fedha, Zakaah si waajib kwa lulu, marijani, zubarjad (aquamarine), yaquti (sapphire) na mfano wake kwa Ijma’a, kwa kuwa hakuna dalili juu ya hilo. [Angalia Muwattwa ya Maalik (1/250), Al-Ummu cha Ash-Shaafi’iy (2/36) na Al-Majmuw’u (6/6)]
Lakini zikiwa ni mali zilizotayarishwa kwa biashara, basi zitatolewa Zakaah kama mali nyinginezo. Hii ni kauli ya Jumhuri, na uchambuzi wake unakuja katika mlango wake, In Shaa Allaah.
Ikiwa mwanamke ana pete za dhahabu zenye stoni za vito, vipi atatoa Zakaah yake?
Kama ataweza kukitoa kito bila kuiharibu pete, basi atazitolea pete peke yake –bila vito vyake– kama zitafikia kiwango na kupitiwa na mwaka. Na kama hakuweza kuvitoa ila sharti pete iharibike, hapo atakadiria na kutoa Zakaah ya dhahabu tu. Na ikiwa pete hizi ni za biashara, basi atatoa Zakaah vile vile ya thamani ya vito kama mali za biashara kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri.
Je, vyombo na tuzo za kisanii au za kikale (Antiques) za dhahabu na fedha hutolewa Zakaah?
Kutumia vyombo vya dhahabu na fedha –na hususan katika kula, kunywa na mfano wake– ni haramu kwa neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((لا تشربوا في آنية الذهب والفضة، ولا تلبسوا الحرير والديباج، فإنها لهم في الدنيا ولكم في الآخرة))
((Msinywee katika vyombo vya dhahabu na fedha, wala msivae hariri na dibaji (hariri nzito), kwani hivyo ni vyao duniani, na vya kwenu aakhirah)). [Al-Bukhaariy (5633) na Muslim (2067)]
Na hakuna makhitalifiano kati ya ‘Ulamaa –hata wale wenye kusema kuwa si waajib kutoa Zakaah katika vipambo vya kuvaliwa na kutumiwa– ya kuwa kilichokatazwa kukitumia na kikiwa kimetengenezwa kwa dhahabu au fedha, basi ni lazima kitolewe Zakaah, ni sawa kwa mwanamume au mwanamke, kwa kuwa sababu iliyopelekea kuharamishwa inakigusa, nayo ni kuingia kwenye israfu, kibr, na kuzivunja nyoyo za masikini. Hivyo vinakuwa sawa katika uharamisho.
Na bila shaka wanawake wameruhusiwa kujipamba kwa kuwa wanalihitajia hilo kwa ajili ya waume zao, lakini si katika matumizi ya vyombo, uharamu wake unabakia palepale.
Na masanamu yameharamishwa. Na kama yametengenezwa kwa dhahabu na fedha, uharamu wake ni maradufu.
Yakithibiti haya, basi Zakaah ipo bila ya mvutano wowote kati ya ‘Ulamaa. Na hakuna Zakaah mpaka kiwango kifikie kwa uzani, au awe na kingine kilichofikia kiwango akichanganye pamoja (yaani cha aina yake). [Al-Mughniy cha Ibn Qudaamah]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
12-Zakaah Ya Mishahara Na Chumo La Kazi
Alhidaaya.com [3]
Mtumishi mwajiriwa au mfanyakazi anayepokea mshahara kila mwezi, au kila wiki, au mfano wa hivyo, haepukiki na moja ya mawili:
Kwanza: Atakuwa na pesa (za akiba) zilizofikia kiwango, na atautumia mshahara wake wa kila mwezi bila kuigusa akiba
Na hii ndio hali ya tatu –ambayo imetajwa nyuma- kati ya hali za mali inayopatiwa manufaa katika kipindi cha mwaka. [Rejea uangalie hukmu ya mali inayopatiwa manufaa]
Hivyo basi, mtumishi huyu atajiwekea rekodi ya hesabu ya mapato yake ambapo ataandika kila pesa inayobaki katika mshahara wake, halafu ataiingiza kwenye pesa zake za akiba, kisha kila pesa ataitolea Zakaah yake baada ya kupitiwa na mwaka kuanzia tarehe ya kuzipata pesa hizo.
Kama atataka kutojisumbua na kupita njia ya usamehevu, na nafsi yake ikaonelea vyema kuwapa kipaumbele masikini na wastahiki wengineo wa Zakaah kuliko maslaha yake binafsi, basi atatolea Zakaah pesa yote aliyonayo kinapopitiwa na mwaka kiwango cha kwanza alichokimiliki katika pesa hizo. Hii inakuwa na thawabu kubwa zaidi kwake, inamnyanyulia juu zaidi daraja yake, na inampumzisha zaidi.
Na hapo, pesa alizoziongeza kwenye akiba yake baada ya kukamilika kiwango cha kwanza, zinakuwa zimelipiwa Zakaah yake mapema kabla ya kutimiza mwaka. Na kutoa Zakaah mapema kabla ya mwaka kutimia kunajuzu na hususan kama kuna dharura au maslaha. [Ni Fatwaa iliyotolewa na Tume Ya Kudumu Ya Fatwaa, Fataawaa za Al-‘Allaamah Ibn Baaz (Rahimahul Laah), Fataawaa Islaamiyyah na Jam-’u Al-Musnad (uk. 76)]
Pia anaweza kufanya jambo la tatu. Atatoa Zakaah safi ya mwezi kila mwezi -baada ya kutoa matumizi yake yote na anaowakimu kimaisha-, halafu atakuja kuitolea Zakaah pesa yake ya akiba ikishatimiza mwaka. [Fiqhu Az Zakaah cha Al-Qaradhwaawiy]
Pili: Asiwe na pesa zilizofikia kiwango na anautumia mshahara wake wote wa kila mwezi
Kama kila mwezi anaweka kiasi fulani cha akiba, basi si waajib kutoa Zakaah mpaka pesa zifikie kiwango, au zifikie kiwango kwa kuchanganywa na pesa alizoweka akiba. Na hapo ataanza kuhesabia mwaka, na inakuwa kama hali iliyotangulia.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
13-Zakaah Ya Mahari
Alhidaaya.com [3]
Mahari ya mwanamke ni mali kama zilivyo mali nyinginezo, na hukmu yake ni hukmu ya mali nyinginezo.
1- Kama mwanamke amepokea mahari yake, na ikawa ni katika aina za mali zinazotolewa Zakaah na ikafikia kiwango au kikazidi, basi ataitolea Zakaah ikipitiwa na mwaka.
2- Ikiwa mahari ni ya kulipwa siku za mbeleni, basi itakuwa na hukmu ya deni ambayo tumeizungumzia nyuma. Ikiwa mume wake ana uwezo wa kifedha na ni mtu wa kuaminika, basi itambidi mwanamke atoe Zakaah ya mahari yake ambayo iko katika dhima ya mumewe, kwa kuwa matumaini ya kulipwa yapo. Lakini kama ni masikini, basi si lazima mwanamke huyo kutoa Zakaah ya mahari hiyo kwa mujibu wa kauli yenye nguvu. Na anapopokea mahari yake, ataitolea Zakaah ya mwaka mmoja tu.
3- Mwanamke akipokea mahari yake, halafu akatalikiwa kabla ya kuingiliwa, kisha mahari ikapitiwa na mwaka na ikafikia kiwango, basi yeye atatoa Zakaah ya nusu ya mahari, na mtalaka wake atatoa nusu nyingine. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi. [Angalia Al-Mughniy (3/52), Jaami’u Ahkaamin Nisaa (2/165) na Kitabu changu cha Fiqhu As-Sunnah Lin Nisaa (uk 217)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
14-Zakaah Ya Mifugo
Alhidaaya.com [3]
Aina Za Wanyama Ambao Hutolewa Zakaah
‘Ulamaa wote kwa pamoja wanasema kuwa Zakaah hutolewa kwa ngamia, ng’ombe, mbuzi na kondoo. Wametolea dalili hili kwa Hadiyth nyingi ambazo baadhi yake zitatajwa mahala pake husika, In Shaa Allaah.
Lakini wamekhitalifiana kwa upande wa farasi. [Al-Mughniy (2/620), Fat-hul Qadiyr (1/502), Sharhu Al-Minhaaj (2/3), na Al-Mawsuw’at Al-Fiqhiyyah (23/262]
Jumhuri, wakiwemo Maswahibu wawili wa Abu Haniyfah– wanaona kuwa farasi wasio wa biashara, hao hawatolewi Zakaah– (hata kama wanajilia majani yasiyogharamikiwa au wakafugwa ili wazaliane) ni sawa wakiwa wanafanyishwa kazi au hawafanyishwi.
Madhehebu yao haya yanatiliwa nguvu na Hadiyth ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) isemayo:
((ليس على المسلم في فرسه وغلامه صدقة))
((Si waajib juu ya Muislamu Zakaah kwa farasi wake na mtumwa wake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1464) na Muslim (628)]
Lakini Abu Haniyfah anaona kwa mbinde kuwa farasi ikiwa wanajilia majani yasiyogharamikiwa madume na majike, basi watatolewa Zakaah. Na kama ni madume tu, basi Zakaah hakuna kwa kuwa hawazaani, na kadhalika majike tu. Ametoa dalili Hadiyth ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) isemayo:
((الخيل لرجل أجر، ولرجل ستر، وعلى رجل وزر....[وفيه] ولم ينس حق الله في رقابها، ولا ظهورها))
((Farasi kwa mtu ni thawabu, kwa mtu ni sitara, na juu ya mtu ni dhambi…[Hadiyth ikaendelea kusema] na hakusahau haki ya Allaah katika shingo zake, wala migongo yake)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (2371) na Muslim (987)]
Amesema: “Haki ya shingo ni Zakaah”.
Ama wanyama wengineo kama nyumbu, punda na kadhalika, hao hawana Zakaah madhali si wa biashara. Ni kwa neno lake Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa Sallam) katika Hadiyth ya: ((Farasi kwa mtu ni thawabu…)) alipoulizwa kuhusu punda akasema: ((Sijateremshiwa chochote kuhusiana naye isipokuwa Aayah hii ya kipekee:
((فَمَن يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ خَيْرًا يَرَهُ))
((Basi yule atakayetenda kheri uzito wa chembe (atom) ataiona)). [Al-Zalzalah (7:99)]
Shuruti za kuwajibisha Zakaah kwa mifugo
1- Kiwango ambacho tutakibainisha mbeleni.
2- Kukamilika mwaka. Ni kwa Hadiyth: ((Hakuna Zakaah katika mali mpaka ipitiwe na mwaka)). [Hadiyth iliyotangulia]
3- Wachungwe na kulishwa muda mwingi wa mwaka kwenye malisho halali yasiyo na gharama.
Vigawanyo vya mifugo
Mifugo (ngamia, ng’ombe, mbuzi na kondoo) inaweza kugawanywa vigawanyo vinne:
1- Wenye kuchungwa na kulishwa kwenye malisho halali yasiyo na gharama muda mwingi wa mwaka, na wawe wametayarishwa kwa ajili ya maduhuli na kuzaana. Ni kama Alivyosema Ta’aalaa:
((وَمِنْهُ شَجَرٌ فِيهِ تُسِيمُون))
((na [mnaotesha] miti ambayo mnalishia)). [An-Nahl (16:10)]
Hawa wanalazimu kutolewa Zakaah.
2- Wenye kulishwa majani yanayogharamikiwa. Hawa hata kama wanafugwa kwa ajili ya maduhuli na kuzaana, lakini mmiliki wake anawanunulia majani au anawakatia, basi hawatolewi Zakaah.
3- Wenye kufanyishwa kazi. Ni kama ngamia ambao mmiliki wake anawakodishia watu ili kubeba mizigo au kupandwa, au ng’ombe wa kulima na kunyweshelea maji. Hawa hawana Zakaah kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri kinyume na Maalik. [Sharhu Fat-hil Qadiyr (1/509) na Al-Mughniy (2/576)]
4- Wenye kufugwa kwa lengo la biashara. Hawa watatolewa Zakaah kama mali za biashara. Ngamia mmoja anaweza kulazimu kutolewa Zakaah kama thamani yake itafikia kiwango, sawasawa akiwa anakula majani ya bure, au ya kununuliwa, au wa kupandwa.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
15-Zakaah Ya Ngamia
Alhidaaya.com [3]
Viwango Vya Zakaah Kwa Ngamia Na Kiasi Chake Cha Wajibu
Mwenye kumiliki chini ya ngamia watano –madume au majike, wadogo au wakubwa– basi hana Zakaah. Imepokelewa toka kwa Abu Sa’iyd Al-Khudriyy kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((ليس فيما دون خمس ذود من الإبل صدقة))
((Hakuna chini ya ngamia watano Zakaah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1447) na Muslim (979). Tushaitaja nyuma]
Ama waliozidi watano na kwenda mbele, Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa Sallam) amebainisha kiasi cha uwajibu wa kutolewa Zakaah katika Hadiyth ya Anas katika barua ya Abu Bakr aliyomtumia. Barua hiyo ni hii hapa kwa maandishi yake kutokana na umuhimu wake mkubwa tokea hapo:
Toka kwa Anas kuwa Abu Bakr (Radhwiya Allaahu ‘anhu) alimwandikia maelezo haya alipomtuma kwenda Bahrain:
“Bismil Laahi Ar-Rahmaan Ar-Rahiym. Hii ni fariydhwah ya Zakaah ambayo Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ameifaradhisha kwa Waislamu wote na ambayo Allaah Amemwamuru kwayo Rasuli Wake. Atakayetakwa katika Waislamu kwa njia ya sawa basi atoe, na atakayetakwa zaidi ya inavyostahiki, basi asitoe. Katika ngamia 24 na chini ya idadi hiyo (hadi watano), atatoa toka “ghanam”, mbuzi mmoja (au kondoo mmoja) kwa kila ngamia watano. Wakifika ngamia 25 hadi 35, basi atolewe binti makhaadhw jike, wakifika 36 hadi 45, basi atolewe binti labuwn jike. Wakifikia 46 hadi 60, atatolewa hiqqat aliye tayari kupandwa na dume, wakifikia 61 hadi 75, basi atatolewa jadha’a, wakifikia -yaani 76 hadi 90– basi atatolewa binti labuwn wawili. Wakifikia 91 hadi 120, basi watatolewa hiqqah wawili wanaopandwa na madume. Wakizidi zaidi ya 120, basi katika kila 40 atatolewa binti labuwn, na katika kila 50 atatolewa hiqqah. Na ambaye hana isipokuwa ngamia wanne tu, basi hana Zakaah ila tu kama mmiliki wake atataka. Wakifikia ngamia watano, basi atatoa mbuzi mmoja (au kondoo). Na katika Zakaah ya mbuzi na kondoo (ghanam) waliochungwa na kulishwa kwenye malisho halali yasiyo na gharama, wakiwa 40 hadi 120, atatolewa mbuzi mmoja (au kondoo). Wakipindukia 120 hadi 200, watatolewa mbuzi wawili (au kondoo wawili). Wakizidi zaidi ya 200 hadi 300, watatolewa mbuzi watatu (au kondoo watatu). Wakizidi zaidi ya 300, basi katika kila 100 mbuzi mmoja (au kondoo). Na ikiwa mbuzi wa mtu (au kondoo) aliowachunga na kuwalisha katika malisho halali yasiyo na gharama amepungua mmoja katika mbuzi 40, basi hakuna Zakaah hapo isipokuwa kama mmiliki wake atataka. Na katika fedha (silver) ni robo ya kumi, na kama hakuna isipokuwa 190, basi hakuna kitu humo ila kama mmiliki wake atataka”. [Hadiyth Swahiyh: Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1454), Abu Daawuwd (1567) na An-Nasaaiy (5/18)]
Na kwa mujibu wa Hadiyth hii, Zakaah ya ngamia hutolewa kwa mujibu wa jedwali ifuatayo:
Idadi ya ngamia wanaomilikiwa |
Kiasi cha wajibu kutolewa |
|
Kuanzia |
Hadi |
|
1 |
4 |
Hakuna Zakaah |
5 |
9 |
Mbuzi mmoja (au kondoo mmoja) |
10 |
14 |
Mbuzi wawili (au kondoo wawaili) |
15 |
19 |
Mbuzi watatu (au kondoo watatu) |
20 |
24 |
Mbuzi wanne (au kondoo wanne) |
25 |
35 |
Binti makhaadh mmoja. [Ni ngamia jike aliyetimiza mwaka mmoja na anaingia mwaka wa pili. Ameitwa hivi kwa kuwa mama yake amejiunga na makhaadh, nao ni ngamia wenye mimba]. Kama hakupatikana, itatosha kutoa ibni labuwn mmoja dume. |
36 |
45 |
Binti labuwn mmoja. [Ni ngamia jike aliyetimiza miaka miwili na kuingia mwaka wa tatu. Ameitwa hivi kwa kuwa mama yake amezaa vitoto vingine na kuwa na maziwa] |
46 |
60 |
Hiqqah mmoja. [Ni ngamia jike aliyetimiza miaka mitatu na kuingia mwaka wanne. Ameitwa hiqqah kwa kuwa anaweza kupandwa na dume] |
61 |
75 |
Jadha’a mmoja. [Ni ngamia jike aliyetimiza miaka minne na kuingia mwaka wa tano] |
76 |
90 |
Binti labuwn wawili |
91 |
120 |
Hiqqah wawili |
Ninasema: “Hii ndio idadi na kiasi kilichoelezewa katika Hadiyth ya Abu Bakr toka kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), na Ijma’a ya ‘Ulamaa imepitisha hilo”. [Al-Majmuw’u (5/400), Al-Amwaal cha Abiy Úbayd (uk.363) na Al-Mughniy (2/577)].
Ama idadi ya ngamia ikipita zaidi ya 120, linalofanywa na ‘Ulamaa wengi –kinyume na Hanafiy, An-Nakhíy na Ath-Thawriy– ni hili linalobainishwa na jedwali ifuatayo. [Hanafiy anasema kuwa faradhi inaanzia baada ya (120). Katika kila watano katika waliozidi, ni mbuzi mmoja kuongezea na hiqqah wawili].
Na ujumla wake ni kuwa kwa kila ngamia 50, atatolewa hiqqah, kwa kila 40, atatolewa binti labuwn, na hili limetajwa katika Hadiyth (ya Abu Bakri) iliyotangulia.
Idadi ya ngamia wanaomilikiwa |
Kiasi kilicho wajibu kutolewa |
|
Kuanzia |
Hadi |
|
121 |
129 |
Binti labuwn watatu |
130 |
139 |
Hiqqah mmoja + binti labuwn wawili |
140 |
149 |
Hiqqah wawili + binti labuwn mmoja |
150 |
159 |
Hiqqah watatu |
160 |
169 |
Binti labuwn wanne |
170 |
179 |
Binti labuwn watatu + hiqqah mmoja |
180 |
189 |
Binti labuwn wawili + hiqqah wawili |
190 |
199 |
Hiqqah watatu + binti labuwn mmoja |
200 |
209 |
Hiqqah wanne + binti labuwn watano |
Na hivi hivi kuendelea: Walio chini ya kumi msamaha (hakuna kitu). Na wakikamilika kumi, ufaradhi unahamia kati ya mahiqqah na mabinti labuwn juu ya msingi wa tuliyoyaeleza kuwa katika kila 50 hiqqah, na kila 40 binti labuwn. [Angalia Fiqhu Az Zakaah cha Dk. Yuwsuf Al-Qaradhwaawiy (1/195)]
Angalizo
Nambari zilizotajwa kwenye jedwali, zinakusanya aina zote za ngamia; “bukht” (wenye nundu mbili), “’iraab”wenye nundu moja na wengineo. Jina “Al-Ibil” linawahusu ngamia wote.
Aliyewajibikiwa kutoa ngamia wa umri fulani kwa mujibu wa ilivyobainishwa na asiwe naye, nini afanye?
Aliyewajibikiwa na umri fulani na asiwe naye kati ya ngamia wake, huyo anaweza kutoa ngamia mwenye umri wa chini yake anayefaa na kutosheleza kwa Zakaah. [Ni kwa mpangilio huu: binti makhaadh, kisha binti labuwn, kisha al-hiqqah, halafu jadha‘a]
Na kujazilia upungufu huo, atampa mkusanyaji Zakaah mbuzi wawili au dirhamu 20. Makusudio ya dirhamu hizi ni kujazilia thamani ya mbuzi wawili.
Au anaweza kutoa umri wa juu zaidi lakini atachukua kutoka kwa mkusanyaji Zakaah mbuzi wawili au dirhamu 20. Hii ni kwa kila mmoja aliyewajibikiwa na Zakaah.
Toka kwa Anas kuwa Abu Bakr (Radhwiya Allaah ‘anhu) alimwandikia fariydhwah ya Zakaah ambayo Allaah Alimwamuru Rasuli Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Aliyefikiwa na Zakaah ya kutoa jadha‘a katika ngamia wake, naye hana jadha‘a bali hiqqah, basi itakubaliwa atoe hiqqah, na watatolewa pamoja naye mbuzi wawili kama itakuwa wepesi kwake au dirhamu 20. Na aliyefikiwa na Zakaah ya kutoa hiqqah, naye hana hiqqah bali jadha‘a, basi itakubaliwa atoe jadha‘a lakini mkusanyaji Zakaah atampa dirhamu 20 au mbuzi wawili. Na aliyefikiwa na Zakaah ya kutoa hiqqah, naye hana bali binti labuwn, basi itakubaliwa atoe binti labuwn na atatoa juu yake mbuzi wawili au dirhamu 20. Na ambaye Zakaah yake imefikia binti labuwn naye hana, bali ana binti makhaadh, basi itakubaliwa atoe binti makhaadh na hutolewa pamoja naye dirhamu 20 au mbuzi wawili)). [Al-Bukhaariy (1453) na Ibn Maajah (1800)]
Inatoholewa kutokana na Hadiyth hii vile vile kuwa kama hakupata ngamia mwenye umri uliowajibikiwa Zakaah na badala yake akapata mkubwa zaidi kwa daraja mbili au mdogo zaidi kwa daraja mbili basi atamtoa, na tofauti ya ujazilio itakuwa dirhamu 40 na mbuzi wanne, na kuendelea.
Lakini inatolewa nje ya wigo wa qaaidah iliyotangulia katika hali hii: Ikiwa amewajibikiwa kumtoa binti makhaadh, na hakuwa na ibnati labuwn bali ana ibn labuwn dume, basi itamtosheleza kutoa binti makhaadh bila ya kutoa cha ziada au yeye kuchukua kitu. Na hii ni kutokana na Hadiyth ya Anas pia katika barua ya Abu Bakr kwa amri ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kuhusiana na Zakaah. Inasema:
((فإن لم يكن عنده بنت مخاض على وجهها، وعنده ابن لبون، فإنه يقبل منه وليس معه شيء))
((Kama hana binti makhaadh mwenye umri mwafaka lakini ana ibn labuwn, basi hukubaliwa na yeye hana chochote)). [Al-Bukhaariy (1448) na An-Nasaaiy (2447).
Je, itamtosheleza kutoa zaidi ya inavyomwajibikia?
Kutoa zaidi ya cha waajib kuna hali mbili:
Ya kwanza: Ni mtoaji Zakaah kujitolea tu kwa khiyari yake, akatoa ngamia mwenye umri mkubwa zaidi ya umri wa waajib. Ni kama kumtoa binti labuwn, au hiqqah, au jadha‘a badala ya binti makhaadh. Hili linajuzu bila mvutano wowote. [Al-Mughniy (2/582) na Naylul Awtwaar (4/161)]
Dalili yake ni Hadiyth ya Ubayya bin Ka’ab. Inasema kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimwambia aliyetoa ngamia jike mkubwa aliyenona, naye kawajibikiwa kutoa binti makhaadh katika ngamia wake- :
((ذاك الذي عليك، وإن تطوعن بخير قبلناه منك، وآجرك الله فيه))
((Yule ndiye unayepaswa kumtoa, lakini ukijitolea cha ziada kwa khiyari yako, basi tunakikubali kutoka kwako, na Allaah Atakulipa kwacho)). [Abu Daawuud (1583), na Ahmad (5/14 3) na Sanad yake ni Hasan]
Ya pili: Atoe ngamia jike badala ya mbuzi, na pia kwenye idadi iliyolazimu kutoa mbuzi (yaani ngamia walio chini ya 25). Hili lina mvutano:
Abu Haniyfah na Ash-Shaafi’iy, wanasema itamtosha. Maalik anasema hilo ndio sahihi zaidi. Lakini Hanbali anasema haimtoshelezi kwa kuwa amemtoa mwingine asiyetajwa kwenye Hadiyth na asiye wa kundi lake. [Al-Mughniy (2/578) na Rawdhwat At-Twaalibiyna (2/154)]
Na wengine wameunga mkono kauli ya Jumhuri ambayo pengine ndiyo yenye nguvu zaidi. [Al-Inswaaf (3/49)]
Sababu ni kuwa (Allaah) Mpangaji sharia Hakufaradhisha ngamia (kutolewa Zakaah) kwa idadi ya chini ya ngamia 25 ili kumfanyia takhfiyf mmiliki, kwani haikubaliki kiakili binti makhaadh atosheleze katika ngamia 25 na asitosheleze katika ngamia 20! [Ash-Sharhu Al-Mumtií]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
16-Zakaah Ya Ghanam (Mbuzi Na Kondoo)
Alhidaaya.com [3]
Viwango Vya Mbuzi Na Kondoo Na Kiasi Cha Wajibu Wake
‘Ulamaa kwa kauli moja wamekubaliana kuwa ni waajib kutoa Zakaah ya mbuzi na kondoo kwa mujibu wa Hadiyth ya Anas katika barua ya Abu Bakr iliyotangulia. Pia wamekubaliana kwa sauti moja kuwa “ghanam” ni mbuzi na kondoo, nao hujumuishwa kwa pamoja, kwa kuwa ni aina mbili za wanyama wa jamii moja. [Angalia Al-Majmuw’u (5/417) na Majmuw’u Al-Fataawaa (25/30-35)]
Na kwa mujibu wa Hadiyth ya Anas, Zakaah ya mbuzi na kondoo huchukuliwa kufuatana na jedwali ifuatayo:
Idadi ya mbuzi na kondoo |
Kiasi kilicho wajibu kutolewa |
|
Kuanzia |
Hadi |
|
1 |
39 |
Hakuna Zakaah |
40 |
120 |
Mbuzi mmoja |
121 |
200 |
Mbuzi wawili |
201 |
339 |
Mbuzi watatu |
400 |
499 |
Mbuzi wanne |
500 |
599 |
Mbuzi watano |
Na hivi hivi waliozidi 300, katika kila mbuzi 100, mbuzi mmoja kwa mujibu wa Jumhuri ya ‘Ulamaa.
Faida
Kondoo au mbuzi, jike au dume, anatosheleza kwa Zakaah. Ni kauli ya Hanafiy, Maalik na Ibn Hazm ambayo ndiyo yenye mwelekeo sawa zaidi. [Angalia Al-Muhallaa (5/268), Al-Majmuw’u (5/422) na Haashiyat ibn ‘Aabidiyna (2/19)]
Masuala jumla kuhusu Zakaah ya mifugo
Je, mifugo wadogo (wachanga) hutolewa Zakaah?
Wanachuoni wamekhitalifiana kuhusu Zakaah ya ngamia wachanga au ndama, au mbuzi na kondoo wachanga. [Badaai-‘u As-Swaanaai (2/31), Fat-hul Qadiyr (1/504), Ad-Durru Al-Mukhtaar (2/26), Al-Mughniy (2/602) na vinginevyo]
1- Baadhi yao wamesema: “Wanyama wachanga (vitoto) huhesabiwa sehemu ya kiwango cha Zakaat, na ni lazima wajumuishwe ndani ya Zakaah hata kama ni wachanga, na atamtoa mmoja kati yao”.
Wengine wamesema: “Atalazimika kununua mwenye umri wa wajibu kutoka kwengine”.
2- Wengine wamesema: “Wanyama wachanga huhesabiwa sehemu ya kiwango, na si lazima wajumuishwe ndani ya Zakaah isipokuwa kama wako na mama zao, ni sawa mama zao wakifikia kiwango peke yao au wasifikie”.
Makundi haya mawili yametolea dalili aliyoyasema ‘Umar kumwambia mkusanyaji Zakaah wake Sufyaan bin ‘Abdullaah Ath-Thaqafiy: ((Wajumlishe hesabuni kondoo na mbuzi wachanga…….)). [Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na Maalik (600) Ash-Shaafi’iy katika Al-Musnad (651) na Ibn Hazm kwa Sanad Hasan]
3- Wengine wamesema: “Mama wakifikia kiwango, basi vichanga vilivyozidi kiwango huhesabiwa”. Ni madhehebu ya Jumhuri. [Amenukulu haya kutoka kwao Sheikh wa Uislamu katika Al-Fataawaa (25/38)]
4- Ibn Hazm kasema: “Kichanga ambacho hakiwezi kuitwa mbuzi au kondoo, hakifai kuchukuliwa katika Zakaah ya wajibu, wala hakihesabiwi katika wanyama wanaochukuliwa Zakaah mpaka kitimize mwaka. Kikitimiza kitahesabiwa, na Zakaah yake itachukulika”. [Al-Muhallaa (5/274)]
Wengine wametolea dalili Hadiyth ya Suwayd bin Ghafalah aliyesema: ((Alitujia mkusanyaji Zakaah wa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), nikakaa kumsikiliza, nikamsikia akisema: Hakika katika niliyoyachukulia ahadi ni kuwa tusimchukue anayenyonya maziwa)). [Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (1579), An Nasaaiy (5/28) na Ahmad (4/315). Sanad yake ni Hasan].
Jumhuri wamechukulia muradi wa Hadiyth hii kuwa hachukuliwi, yaani mwenye kunyonya katika Zakaah, na hakuna kizuizi kuingizwa katika idadi ya kiwango.
Ibn Hazm ameihoji kauli yao akisema: “Ikiwa (Suwayd) anakusudia kuwa mwenye kunyonya asichukuliwe katika Zakaah angesema: Tusimchukue mwenye kunyonya maziwa, lakini alipozuia mwenye kunyonya maziwa asichukuliwe kwa Zakaah –na mwenye kunyonya maziwa ni nomino jumla (common noun)– imeruhusika kwa hilo wasihesabiwe wenye kunyonya katika wanyama wenye kuchukuliwa katika Zakaah”. [Al-Muhalla (5/278-279].
Sifa zinazochungwa kwa mnyama anayechukuliwa katika Zakaah ya mifugo
Mnyama anayechukuliwa katika Zakaah ya mifugo anatakiwa awe wa wastani, na hili linahitajia mambo mawili. La kwanza ni kwa mkusanyaji Zakaah ambaye ni mtumishi maalum aliyeteuliwa na mtawala kwa kazi hiyo, na la pili ni kwa mmiliki wa mifugo.
1- Mkusanyaji anatakiwa ajiepushe kuchukua mali ya thamani kubwa ya mtoaji Zakaah kama mwenyewe hakuitoa kwa roho safi. Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwambia Mu’aadh wakati alipomwamuru kuchukua Zakaah kwa watu wa Yemen:
((إياك وكرائمَ أموالهم، واتقِ دعوة المظلوم؛ فإنه ليس بينها وبين الله حجابٌ))
((Chunga usije kuchukua mali za watu za thamani kubwa, na ogopa sana du’aa ya aliyedhulumiwa, kwani haina kizuizi kati yake na kati ya Allaah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1496) na Muslim (19).
Imepokelewa toka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) akisema: ((Kondoo na mbuzi wa Zakaah walipitishwa kwa ‘Umar bin Al-Khattwaab. Akaona kati yao mbuzi aliyenona na vilembwe (chuchu) vimejaa maziwa. Akasema: Huyu mbuzi ni wa nini? Wakasema: Ni mbuzi wa Zakaah. Akasema: Watu wake hawakumtoa wakiwa wameridhika, msiwafitini watu (wakachukia Amri za Allaah), msichukue mali za thamani kubwa za Waislamu, waachieni cha kuwapa chakula)). [Hadiyth Swahiyh. Imefanyiwa ikhraaj na Maalik (602), na kutoka kwake Ash-Shaafi’iy katika Musnadi wake (654) na Sanadi yake ni Swahiyh].
2- Mmiliki asitoe mali mbovu. Kama kumtoa mnyama mwenye kasoro, au mwenye maradhi, au aliyevunjika, au kikongwe ambaye hana tena meno, au mwenye ila yenye kupunguza manufaa yake na thamani yake. Allaah Ta’alaa Amesema:
((وَلَا تَيَمَّمُوا الْخَبِيثَ مِنْهُ تُنفِقُونَ))
((Na wala msikusudie vibaya kutoka humo mkavitoa)). [Al-Baqarah 2:267]
Na Hadiyth ya ‘Abdullaah bin Mu’aawiyah inasema kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam amesema:
((ثلاث من فعلهن طعم طعم الايمان:...وأعطى زكاة ماله طيبة بها نفسه، راقدة عليه كل عام، ولا يعطي الهرمة ولا الدرنة، ولا المريضة، ولا الشرط اللئيمةـ ولكن من وسط أموالكم، فإن الله لم يسألكم خيره، ولم يأمركم بشره))
((Matatu mtu akiyafanya, ataonja ladha ya iymaan: …na akatoa Zakaah ya mali yake roho yake ikiwa safi, yenye kumsaidia kwa kipato kila mwaka, na asitoe mzee, wala mwenye pele, wala mgonjwa, wala asiyetamanika asiye na maziwa, bali toeni mali zenu za thamani ya wastani, kwani Allaah Hajawatakeni bora ya mali, wala Hakuwaamuruni mbovu yake)). [Abu Daawuud (1582), na wapokezi wake ni waaminifu]
Je, Zakaah ni waajib kwa mali yenyewe husika au kwa dhima ya mtoaji?
‘Ulamaa wana rai mbili katika suala hili:
Ya kwanza: Zakaah ni waajib kwa mali yenyewe husika. Hii ni kauli ya Jumhuri. Kati ya yanayozalikana na hili ni:
(a) Kuwa mali ikiharibika (ikiteketea) baada ya kuwajibikiwa na Zakaah, basi Zakaah itapomoka kwa kuteketea huko.
(b) Kuwa mwenye mbuzi 40 kwa mfano, atatoa mbuzi mmoja. Na kama hakutoa Zakaah ya mwaka (uliomwajibikia) na akabakiwa na mbuzi hao hao 40 (bila kuongezeka idadi), ni lazima amtoe mbuzi huyo mmoja, lakini hatowajibika kumtoa kwa mwaka unaofuatia, kwa kuwa mbuzi hao 40 wako katika hukumu ya mbuzi 39.
Ya pili: Zakaah ni waajib kwa dhima. Hii ni kauli ya Mahanbali na Ibn Hazm. Kauli yao inatotoa yafuatayo:
(a) Zakaah baada ya kuwa waajib, haiondoki kwa kuhiliki mali kwa kuwa imefungamana na dhima ya mwenye mali.
(b) Ambaye hakutoa Zakaah ya mbuzi 40 baada ya kupita mwaka wa kwanza, ni lazima atoe mbuzi wawili mwaka unaofuatia, kwa kuwa mbuzi wa kwanza amebakia katika dhima yake, na ni lazima amtoe mwingine kwa hao 40.
Ikiwa mifugo ni ya ushirika wa watu wawili, vipi Zakaah hutolewa?
Ushirika, -sawasawa ukiwa ni wa mifugo ya aina moja, au wa mifugo tofauti– unafanya mali mbili kuwa mali moja. Ni kwa Hadiyth:
((لا يجمع بين متفرق، ولا يفرق بين مجتمع، خشية الصدقة [وما كان من خليطين، فإنهما يتراجعان بينهما بالسوية]))
((Hawachanganywi kati ya waliotenganishwa, na wala hawatenganishwi kati ya waliochanganyishwa kwa kuogopa Zakaah [Na kwa wanyama wa washirika wawili, basi hao watarejesheana hesabu kati yao kwa usawa])). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (145), Ibn Maajah (1801) bila nyongeza, nayo iko kwa An-Nasaaiy (2447), Abu Daawuwd (1567) na At-Tirmidhiy (621)]
Na Zakaah ni waajib kwa mali ya shirika kama ilivyo waajib kwa mali ya mtu mmoja kwa masharti yafuatayo: [Angalia Al-Fiqhu Al-Islaamiy wa adillatuhu)]
1- Washirika wawili wawe na masharti ya kuwajibikiwa na Zakaah (kama kuwa Muislamu, muungwana, kuwa na umiliki kamili wa mali n.k).
2- Mali iliyochanganywa ifikie kiwango.
3- Ushirika wao upitiwe na mwaka kamili, na kama si hivyo, kila mmoja atatoa kivyake kwa mujibu wa mwaka wake.
4- Mali ya mmoja wao isitenganike na ya mwenzake katika mambo sita: machungio, boma la kulala, manyweo ya maji, sehemu ya kukamwa maziwa, mafahali na mchungaji. [Hanafiy na Ibn Hazm katika Al-Muhalla (6/51 na kurasa zinazofuatia) wanasema kuwa ushirika hauna athari yoyote, na ushirika haufanyi mali mbili kuwa moja]
Ama maana ya Hadiyth ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((لا يجمع بين مفترق، ولا يفرق بين مجتمع خشية الصدقة..))
((Hawachanganywi kati ya waliotenganishwa, wala hawatenganishwi kati ya waliochanganyishwa kwa kuogopa Zakaah)) ni kuwa:
1-Ushirika (unaozifanya mali mbili kuwa kama mali moja) unaweza kuwafaidisha washirika wawili kwa kuwapunguzia Zakaah. Ni kama kila mmoja wao kuwa na mbuzi 40 ambao wakichanganywa wanakuwa 80, na hapa watawajibika kutoa mbuzi mmoja tu, kinyume na kama si washirika, kila mmoja atatoa hapo mbuzi mmoja.
Na hapa ndipo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akakataza watu wawili kufanya hila, wakashirikiana kukwepa Zakaah na kuipunguza.
2- Ushirika unaweza kuongeza mzigo wa Zakaah kwa washirika wawili kama wote wawili kuwa na mbuzi 40. Hapa wote wawili ni lazima watoe mbuzi mmoja, kinyume na kama watatengana, hapo hawajibikiwi yeyote kati yao kutoa chochote. Na hapa washirika hawa wanakatazwa kutenganisha wanyama wao ili kukwepa Zakaah.
Je, ushirika una athari katika mali isiyo ya mifugo?
Madhehebu ya Hanbali yanasema kuwa hauathiri kwa mali nyinginezo zisizo wanyama wa kufugwa, kwa kuwa ushirika katika mifugo unakuwa na faida wakati fulani na hasara wakati mwingine. Ama mali isiyo mifugo, hiyo haidhaniwi jingine isipokuwa hasara tu kwa mwenye mali, kwa kuwa inampasa kuitolea Zakaah iliyozidi kiwango katika hesabu yake, na kuichanganya na mhisa wake hakusaidii kitu. Hivyo, ikiwa kila mmoja katika washirika wawili ana mali ambayo sio mifugo inayofikia nusu ya kiwango, basi hawawajibikiwi kutoa Zakaah. [Al-Inswaaf (3/83)]
Lakini madhehebu ya Ash-Shaafi’iy yanasema kuwa ushirika unaathiri katika mali isiyo ya mifugo vile vile kama mazao, matunda, dirhamu, dinari na mfano wake. [Mughnil Muhjtaaj (2/76)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
17-Zakaah Ya Ng’ombe
Alhidaaya.com [3]
Viwango Vya Ng’ombe Na Kiasi Cha Zakaah Yake
Toka kwa Mu’aadh bin Jabal (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alinituma kwenda Yemen, na akaniamuru nichukue katika kila ng’ombe arobaini musinnah, na katika kila thelathini tabiy dume au jike)). [Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (619), Abu Daawuwd (1561), An-Nasaaiy (5/26) na Ibn Maajah (1803)]
Idadi hii huwajumuisha nyati wa kufugwa pamoja na ng’ombe, kwa kuwa nyati hawa ni jamii ya ng’ombe kwa Ijma’a, na kwa hivyo hujumuishwa nao.
Na wewe unaona kuwa Hadiyth haikuainisha kiwango kidogo zaidi, lakini Jumhuri ya ‘Ulamaa wanasema kuwa hakuna Zakaah kwa ng’ombe chini ya 30. Wanapofikia 30, atatolewa tabiy dume au jike (jadha‘a dume au jike, na huyu ni mwenye mwaka mmoja), halafu kwa mujibu wa jedwali ifuatayo:
Idadi ya ng’ombe |
Kiasi kilicho wajibu kutolewa |
|
Kuanzia |
Hadi |
|
1 |
29 |
Hakuna Zakaah |
30 |
39 |
Tabiy mmoja dume au jike. (Tabiy ni ndama aliyetimiza mwaka). |
40 |
59 |
Musinnah mmoja. (Musinnah ni ng’ombe aliyetimiza miaka miwili). |
60 |
69 |
Tabiy wawili |
70 |
79 |
Tabiy mmoja na musinnah mmoja |
80 |
89 |
Musinnah wawili |
90 |
99 |
Tabiy watatu |
100 |
109 |
Tabiy wawili na musinnah mmoja |
Na hivi hivi kuendelea: kwa kila thelathini tabiy dume au jike, na kila arobaini musinnah.
Wakifikia 120, je wanakuwepo humo tabiy na musinnah? Inavyoonekana ni kuwa katika hali hii atachaguzwa baina ya kutoa tabiy wanne au musinnah watatu. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi. [Angalia Majmuw’u Al-Fataawaa]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
18-Zakaah Ya Mazao Na Matunda
Alhidaaya.com [3]
Zakaah ya mazao na matunda ni lazima katika ujumla wake. Ulazima wake umethibiti katika Qur-aan, Sunnah na Ijma’a, ingawa Fuqahaa wamekhitilafiana katika uchambuzi wake. [Badaai‘u As-Swanaai (2/54)]
Dalili kutoka katika Qur-aan na Sunnah zitakuja mbeleni tukiendelea kulichambua suala hili.
Mazao Na Matunda Ambayo Ni Lazima Yatolewe Zakaah
‘Ulamaa wamekubaliana wote kuwa ni lazima kutoa Zakaah katika aina ambazo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alizichukulia Zakaah ambazo ni ngano, shayiri, tende na zabibu kavu. Lakini wamekhitalifiana kuhusu aina zingine ambazo hazikugusiwa. Kauli zao kiujumla ni hizi zifuatazo:
1- Hakuna Zakaah isipokuwa katika aina hizi hizi nne, na zisizo hizi, hakuna Zakaah
[Al-Muhalla (5/209) na kurasa zinazofuatia, Naylu Al-Awtwaar (4/170), Al-Amwaal cha Abiy ‘Ubayd (469/1378), Tamaam Al-Minnah (uk. 372-373) na Fiqh Az Zakaah (1/377)]
Haya ni madhehebu ya Ibn ‘Umar([1]), Al-Hasan Al-Baswriy([2]), Ath-Thawriy, Ash-Sha’abiy, Ibn Siyriyn, Ibn Al-Mubaarak, Abu ‘Ubayd na Masalaf wengineo. Ni riwaya toka kwa Ahmad. Pia ni madhehebu ya Ibn Hazm isipokuwa Hadiyth ihusianayo na zabibu kavu, si swahihy kwa upande wake, na hakuizungumzia. Kadhalika, ni madhehebu ya Ash-Shawkaaniy kisha Al-Albaaniy.
Dalili za wenye kauli hii ni:
- Yaliyosimuliwa toka kwa Abu Burdah toka kwa Abu Muwsaa na Mu’aadh kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alipowatuma kwenda Yemen –ili kuwafundisha watu diyn yao –aliwaamuru wasichukue Zakaah isipokuwa kwa mazao haya manne tu: Ngano, shayiri, tende na zabibu kavu. [Al-Haakim (1/401) na Al-Bayhaqiy (4/125). Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh katika As-Swahiyhah (879)]
Na kwa vile mazao na matunda mengine yasiyo haya manne hayakutajwa na Aayah wala Hadiyth wala Ijma’a wala hata vinavyofanana navyo kwa ukaribu katika vyakula vinavyoliwa zaidi, uwepo wake na manufaa yake mengi, hivyo basi, haitofaa kuvifanyia vipimo juu ya mazao tajwa, wala kuvinasibisha nayo. Hivyo yanabakia katika asili yake.
Pia, Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) wakati alipoyaainisha mazao haya manne kwa Zakaah na kuyakataa mengine, alikuwa anajua kwamba watu wana vyakula vinginevyo na mali katika vinavyotolewa na ardhi. Hivyo kuviacha na kuvikataa ni msamaha kutoka kwake kama alivyosamehe Zakaah ya farasi na watumwa.
2- Zakaah hutolewa kwa kila kinacholiwa na kuhifadhiwa
[Al-Muwattwa (1/276 chapa ya Al-Halabiy), Al-Muhaddhab (5/493), na Fiqhu Az Zakaah (1/378)]
Ni madhehebu ya Maalik na Ash-Shaafi’iy. Vinavyoliwa ni vile ambavyo watu wanavitumia kwa utashi wao katika mazingira ya kawaida na si katika hali ya kulazimika. Ni kama ngano, shayiri, mahindi, mchele na mfano wake. Si lazima kutoa Zakaah ya jozi (walnut), lozi, fistiki (pistachio) na mfano wake. Hivi hata kama vinahifadhiwa, lakini si vyakula vya lishe na shibe kwa watu.
Dalili za wenye kauli hii ni Hadiyth ya Mu’aadh bin Jabal ikisema: ((Ama matango, matikiti maji, makomamanga, miwa na mboga, hivi amevisamehe Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam)). [Hadiyth Dhwa’iyf. Imekharijiwa na Al-Bayhaqiy (4/129), Al-Haakim (1/558) na Ad-Daaraqutwniy (2/97). Angalia At-Talkhiysw (837)]
Na kwa vile vyakula manufaa yake ni makubwa, vinakuwa kama wanyama wa mifugo.
3- Zakaah ni kwa kila kinachokauka, kinachobakia na kinachopimika [Al-Mughniy (2/690), Sharhu Muntahaa Al-Iraadaat (1/388) na Fiqh Az Zakaah (1/381).
Ni katika riwaya mashuhuri zaidi toka kwa Ahmad. Hapa zinaingia nafaka na matunda yanayopimwa na kuhifadhiwa, na nafaka zinazohifadhiwa nyumbani kama fuli (jamii ya maharagwe), njegere, adesi n.k. Pia tende, zabibu kavu, lozi, fistiki na kadhalika kwa kuwa zote zina sifa moja.
Hakuna Zakaah katika matunda mengineyo kama jozi, matufaha na mfano wake, au mboga mboga.
Dalili za wenye kauli hii ni:
1- Kauli ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((ليس فيما دون خمسة اوسق صدقة))
((Hakuna chini ya “wasq” tano [pishi 300] Zakaah)). [Al-Bukhaariy (1447) na Muslim (979)]
Wanasema kwenye Hadiyth pamezingatiwa ufunganyaji, hivyo inadulisha kuwa Zakaah inakuwa kwa vinavyofunganywa na kupimwa.
[Wasq 1 = pishi 60. Pishi 60 × wasq 5 = pishi 300. Pishi 1 = kilo 2.175. Hivyo, kiwango cha Zakaat ni takriban kilo 653 kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri. Wengine wanasema pishi moja ni sawa na kilo 3, na kiwango cha Zakaah ni kilo 900]
2- Kauli ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((ليس في حب ولا تمر صدقة حتى يبلغ خمسة أوسق))
((Hakuna Zakaah katika nafaka wala tende mpaka zifikie wasq tano)). [Muslim (979) na An-Nasaaiy ( 2485).
Wanasema: Hii inadulisha kuwa ni lazima kutoa Zakaah ya nafaka na tende, na si lazima kwa visivyo viwili hivyo. Ibn Taymiyyah amekhitari kuwa kinachozingatiwa ni kuhifadhika mazao na si vinginevyo, kwa kuwepo maana mwafaka ya kuwajibisha Zakaat ndani yake kinyume na mizani, kwani ni ukadiriaji tu na uzito katika maana yake.
4- Zakaah ni kwa kila kinachooteshwa na ardhi katika vinavyolimwa na mwanadamu [Al-Muhallaa (5/212), Al-Hidaayah (2/502), na ‘Aaridhwat Al-Ahwadhiy (3/135)]
Ni kauli ya ‘Umar bin ‘Abdul ‘Aziyz, na madhehebu ya Abu Haniyfah na Daawuwd Adh-Dhwaahiriy. Ibn ‘Arabiy ameitilia nguvu na amejikita sana katika kuiunga mkono, na Al-Qaradhwaawiy ameikhitari.
Hoja za mwelekeo wao huu ni:
1- Ujumuishi wa Kauli Yake Ta’aalaa:
((يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا أَنفِقُوا مِن طَيِّبَاتِ مَا كَسَبْتُمْ وَمِمَّا أَخْرَجْنَا لَكُم مِّنَ الْأَرْضِ))
((Enyi walioamini! Toeni katika vizuri mlivyochuma na katika ambavyo Tumekutoleeni kutoka katika ardhi)). [Al-Baqarah (2:267)]
Wamesema: Hakutofautisha kati ya vinavyotokana na chumo la mtu au vinavyotolewa na ardhi.
2- Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَآتُوا حَقَّهُ يَوْمَ حَصَادِهِ))
((na toeni haki yake (Zakaah) siku ya kuvunwa kwake)). [Al-An’aam (6:141)]
Na hii ni baada ya kutaja aina za vyakula vya mashamba, mitende, mimea, zaituni na makomamanga.
3- Kauli ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((فيما سقت السماء العشر، وفيما سقي بالنضح نصف العشر))
((Kwa yaliyonyeshelezewa na mvua 10%, na yaliyonyeshelezwa kwa mnyama 5%)).
Wamesema: “Hapa hakupambanua kati ya kinachofanywa chakula na kisichofanywa chakula, au kinacholiwa na kisicholiwa, au kinachohifadhika na kisichohifadhika”.
Ibn Al-‘Arabiy amesema: “Madhehebu yenye nguvu zaidi kwa upande wa dalili kuhusiana na suala hili, ni madhehebu ya Abu Haniyfah. Yamewatizama zaidi masikini, yanawezesha zaidi kuishukuru Neema ya Allaah, na yanadulisha ujumuishi wa Aayah na Hadiyth”.
Na hawa wameziponda Hadiyth zilizoifunga Zakaah ndani ya aina hizi nne tu wakisema kuwa ikiwa tutajaalia kuwa ni Hadiyth Swahiyh, basi zitafasiriwa kwa maana kuwa hakukuwa wakati huo na mazao mengine zaidi ya haya manne?
Zakaah ya mazao na matunda si lazima ipitiwe na mwaka
Hakuna sharti ya kupitiwa na mwaka katika Zakaah ya mazao na matunda kwa makubaliano ya ‘Ulamaa kutokana na Kauli Yake Ta’aalaa:
((وَآتُوا حَقَّهُ يَوْمَ حَصَادِه))
((na toeni haki yake (Zakaah) siku ya kuvunwa kwake)). [Al-An’aam (6:141)]
Kwa kuwa kinachovunwa ni barakah na kheri katika dhati yake, hapo imewajibika kutolewa Zakaah kinyume na mali nyinginezo za Zakaah. Mali hizo ni sharti zipitiwe na mwaka ili ziweze kuwekezwa. [Al-Mughniy (6/696)]
Ni wakati gani Zakaah ya mazao na matunda inakuwa waajib? Wakati gani hutolewa?
Zakaah inakuwa waajib wakati mazao yanapoonekana yamekomaa na punje kuwa ngumu, kwa kuwa katika hali hiyo, punje zinakuwa ni chakula. Punje kabla ya kufikia hali hii zinakuwa ni changa na haziliki. Ni waajib pia wakati mwaka unapokamilika, au tende (tamr) na zabibu kubadilika rangi, nazo kabla ya kugeuka rangi, zinakuwa ni tende mbichi “balah” au “haswram”, na zabibu mbichi.
Ama wakati wa kutolewa Zakaah yake, kwa nafaka, inakuwa ni baada ya kupukuchwa na kutolewa maganda. Ama kwa matunda, inakuwa ni baada ya kukaushwa, kwa kuwa huo ndio wakati wa ukomavu kamili na uwezekaniko wa kuhifadhiwa.
Na ikiwa mazao yataharibika kabla ya kuwajibikiwa na Zakaah, yaani kabla ya kukomaa, basi Zakaah husamehewa. Na kama yataharibika baada ya kukomaa lakini kabla ya kuhifadhiwa na kuwekwa ghalani, basi hakuna dhamana juu yake. [Al-Mughniy (2/702) na Sharhu Muntahaa Al-Iraadaat (1/390)]
Je, ni lazima mazao na matunda yafikie kiwango? Kiwango chake ni kiasi gani?
Ili Zakaah iwe waajib, ni lazima ifikie kiwango kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri. Kiasi chake ni “wasq”tano za nafaka safi zilizopembuliwa.
Hii ni kwa neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((ليس فيما دون خمسة اوسق صدقة))
((Hakuna chini ya wasq tano [pishi 300] Zakaah)). [Imesimuliwa na Al-Bukhaariy na Muslim]
Kipimo hiki ni sawa na “kaylah” 50 za Kimisri. [Fiqhu Az Zakaah (1/400)] Ni sawa na “irdabu” 4 1/6 . Ni sawa vile vile kujaza chombo chenye ujazo wa takriban kilo 647 za ngano.
Ikiwa mavuno yatapungua chini ya uzito huu, basi Zakaah si lazima kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri ya ‘Ulamaa. Kati yao ni maswahibu wawili wa Abu Haniyfah. Lakini Abu Haniyfah amewajibisha Zakaah kwa kidogo na kingi akitolea dalili ujumuishi wa Hadiyth isemayo:
(( فيما سقت السماء العشر))
((Kwa yaliyonyeshelezewa na mvua 10%)). [Takhriyj yake itakuja mbeleni kidogo]
Na kwa kuwa yeye hazingatii kupitiwa na mwaka, na hata kiwango pia hakizingatii.
Lakini Hadiyth: ((Hakuna chini ya wasq tano [pishi 300] Zakaah)), haijuzu ipingane na Hadiyth iliyotangulia [Kwa yaliyonyeshelezewa na mvua 10%], kwa kuwa hii ni khususi, muhkam (inafahamika bila utata) na iwazi, na ile ni jumuishi, ni mutashaabah (tata inayohitaji kubainishwa), na mujmal (yenye maana mchanganyo). Hii inabainisha kiwango, na ile bila shaka imekusudiwa kwayo kupambanua kati ya ambayo ni wajibu kutolewa asilimia 10 na ambayo ni wajibu kutolewa asilimia 5. Hivyo hakuna ukinzano kati yao. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
Vipi kinakadiriwa kiwango cha zao lisilopimika kwa wenye kuwajibisha Zakaah kwa zao hilo?
Zao lisilokadiriwa kwa kupimwa kama pamba mfano, -kwa wenye kusema ni wajibu litolewe Zakaah– ukadiriaji wa kiwango chake umekhitalifiwa kwa kauli mbalimbali: [Angalia Fiqh Az Zakaah (1/401)]
1- Itaangaliwa thamani. Ikiwa thamani yake itafikia karibu sana na kiwango cha mazao yanayofungashwa, basi Zakaah itatolewa. Kama haikukurubia, basi haitolewi.
2- Kitaangaliwa kiwango cha pesa.
3- Kiwango hakiangaliwi, bali Zakaah itatolewa kwa kichache chake na kingi chake.
4- Kitakadiriwa kwa uzito uliotajwa nyuma ambao ni kilo 647.
Kauli ya tano imetiliwa nguvu na Ibn Qudaamah katika Al-Mughniy (2/697). Amesema akiziandamiza kauli nyingine: “Sijui dalili yoyote wala asili yoyote ya kutegemewa juu ya kauli hizi. Zinanyamazishwa na kauli ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam): ((Hakuna chini ya wasq tano [pishi 300] Zakaah)).
Al-Qaradhwaawiy amekhitari kauli ya kuangalia thamani.
Je, mavuno yanaweza kuwekwa pamoja ili kukamilisha kiwango?
Kauli imara zaidi ya ‘Ulamaa inasema kuwa mazao ya jamii moja huwekwa pamoja yenyewe kwa yenyewe, lakini ya aina tofauti hayachanganywi. Ngano haichanganywi na shayiri na mfano wa hilo, wala nafaka zinazohifadhiwa nyumbani hazichanganywi pamoja. Dengu haichanganywi na adesi na mfano wa hilo. [Al-Majmu’u cha An-Nawawiy (5/511-513)]
Haya ni madhehebu ya Jumhuri ya Masalaf.
Ama aina mbalimbali za ngano, hizi huchanganywa zenyewe kwa zenyewe, pia shayiri hivyo hivyo, na tende kadhalika kwa aina zake tofauti na majina yake tofauti hata kama mashamba anayoyamiliki mtu yakawa yametengana huku na kule. [Al-Muhallaa cha Ibn Hazm (5/253)]
Kuna ‘Ulamaa waliojuzisha kuchanganya ngano na shayiri, na kuchanganya nafaka zinazohifadhiwa nyumbani kwa chakula kama fuli, dengu, adesi, njegere na mfano wake ili kukamilisha kiwango kutokana na mkusanyo wake. Haya ni madhehebu ya Maalik, riwaya toka kwa Ahmad, na Sheikh wa Uislamu ameikhitari kauli hii. [Al-Mughniy (2/560), Al-Mudawwanah (1/288), na Majmuw’u Al-Fataawaa (25/23-24)]
Ninasema: “Lakini, kauli hii, sijui dalili yoyote ya kuithibitisha. Yenye nguvu zaidi ni ya kwanza. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi”
Je, mavuno ya mwaka mmoja hukusanywa pamoja kukamilisha kiwango?
Ikiwa mtu ana shamba, na baadhi ya mazao yake huvunwa mapema na mengine baadaye, mazao haya yatachanganywa ili kukamilisha kiwango madhali ni mwaka huo huo. Ni chaguo la Sheikh wa Uislamu. [Majmu’u Al-Fataawaa (25/23). Angalia Al-Mughniy (2/733)]
Lakini hili tunalifungamanisha na masharti yaliyotangulia ya kuwa mazao yawe ya aina moja. Ama matunda ya miaka miwili, haya hayachanganywi.
Ukisiaji wa mavuno ya mitende na mizabibu
Matunda yanapoanza kukomaa, kiongozi wa nchi anatakiwa atume mtaalamu wa kukadiria kiasi cha mavuno baada ya kukauka matunda ili kiasi cha Zakaah kijulikane kwa wenye mashamba na kisha awajulishe. Atawakhiyarisha kati ya kuyahifadhi mpaka yakauke, au kula sehemu ya matunda hayo –yakiwa bado mabichi– na kuchunga haki ya masikini. Kama mwenye shamba atachagua kuyahifadhi mpaka yakauke, basi wakati huo atawajibikiwa Zakaah ya matunda aliyoyahifadhi yakiwa mengi au kidogo. Na kama atachagua –mwenye shamba- kula sehemu ya matunda hayo, basi atatoa fungu la masikini kwa mujibu wa hesabu ya makadirio.
Toka kwa Abu Hamiyd As Saa’idiy (Radhwiya Allaahu ‘anhu): ((Tulipigana vita vya Tabuk pamoja na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam). Alipofika Waadiy Al-Quraa, alimkuta mwanamke kwenye shamba lake. Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akawaambia Swahaba wake: Kisieni mavuno. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akakisia “wasq” kumi. Akamwambia: Dhibiti hesabu (ya mavuno) yatakayotoka humo…. Alipofika Waadiy Al-Quraa alimwambia mwanamke yule: Shamba lako limetoa mavuno kiasi gani? Akasema: Wasq kumi. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikisia mavuno)). [Al-Bukhaariy (1482) na Muslim (1392)]
Toka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa): ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anamtuma ‘Abdullaah bin Rawaaha kwenda kufanya makisio ya mitende wakati matunda yanapoanza kupata utamu kabla ya kuliwa, kisha huwakhiyarisha Mayahudi: (Ima) mitende (yote) iwe yao kwa mujibu wa makisio hayo [lakini wadhamini fungu la Waislamu], au wawaachie (yote Waislamu) kwa mujibu wa makisio hayo [lakini Ibn Rawaaha atawadhaminia kiasi cha fungu lao] ili aidhibiti Zakaah kabla matunda hayajaliwa na kutawanywa)). [Abu Daawuwd (1606), Abu ‘Ubayd katika Al-Amwaal (483/1438), Al-Bayhaqiy (4/123) na Ahmad (8/163). Ni Hadiyth Hasan Lishawaahidihii kama ilivyo katika Al-Irwaa (805)]
Je, inajuzu kula mazao kabla ya kuvuna? Je, yaliyoliwa hutiwa hesabuni?
Mwenye shamba anaruhusiwa kula chochote toka shambani mwake kiasi anachohitaji kabla ya kuvuna, na pia anaweza kutoa swadaqah kutoka humo wakati wa kuvuna, na haya hayatiwi hesabuni. Atakachotoa Zakaah ni kile kitakachopembuliwa baada ya hapo, kwa kuwa Zakaah haiwi waajib mpaka pale mazao yanapoweza kupimwa. Kwa hiyo, kilichotoka kabla ya hapo, kinakuwa kimetoka kabla ya kuwajibikiwa Zakaah.
Haya yamesemwa na Ash-Shaafi’iy, Al-Layth na Ibn Hazm. [Al-Muhallaa (5/259)]
Ni kiasi gani cha Zakaah ya mazao na matunda hutolewa kama yakifikia kiwango?
Kiasi cha Zakaah ya mazao na matunda hutofautiana kwa kutofautiana njia za umwagiliaji. Yaliyomwagiliwa bila kutumia zana za umwagiliaji (au wanyama), hayo yatatolewa moja ya kumi (yaani 10%). Ama yaliyomwagiliwa kwa zana, au kwa maji ya kununua, basi yatatolewa nusu ya kumi (moja ya ishirini au 5%).
Na dalili ya hili ni:
1- Hadiyth ya Ibn ‘Umar ya kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((فيما سقت السماء والعيون أو كان عثريا العشر، وفيما سقي بالنضح نصف العشر))
((Kwa yaliyomwagiliwa na mvua na chemchemu, au ikawa mitende iyfonzayo yenyewe maji toka chini, ni moja ya kumi [10%], na kwa yaliyomwagiliwa kwa mnyama ni nusu ya kumi [5%])). [Al-Bukhaariy (1483), Abu Daawuwd (1581), At-Tirmidhiy (635), An-Nasaaiy (5/41) na Ibn Maajah (1817)].
2- Hadiyth ya Jaabir toka kwa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
(( فيما سقت الأنهار والغيم: العشور، وفيما سقي بالسانية: نصف العشور))
((Kwa yaliyomwagiliwa kwa mito na mvua, ni moja ya kumi, na katika yaliyomwagiliwa kwa ngamia, ni nusu ya kumi)). [Muslim (981), Abu Daawuwd (1582) na An-Nasaaiy (5/42).
Na ikiwa shamba litamwagiliwa nusu yake kwa gharama na nusu yake nyingine bila gharama, basi Zakaah ni robo tatu ya kumi (7.5%) kwa makubaliano ya Jumhuri.
Na ikiwa eneo moja limemwagiliwa zaidi ya jingine, basi Jumhuri wanalizingatia lililomwagiliwa zaidi, na hukmu ya uchache huondoka. Wengine wamesema kila eneo kati ya mawili litaangaliwa kivyake.
Na kama hakujua kiasi kilichozidi, atatoa moja ya kumi kiakiba, kwa kuwa wajibu wa moja ya kumi ndio asili, nao hupomoka kwa kuwepo gharama. [Angalia Al-Mughniy (2/699)]
Je, gharama, masurufu ya ulimaji na madeni hutolewa kando kisha kinachobaki hutolewa Zakaah?
1- Madeni anayokuwa nayo mkulima wa mazao au matunda hayakosi moja ya mawili:
La kwanza:
Awe amekopa kwa ajili ya kugharamia shughuli ya ulimaji kama kununua mbegu, mbolea, malipo kwa vibarua na kadhalika. Madeni haya yatatolewa kando kutokana na kitakachopatikana shambani, na kinachobakia kitatolewa Zakaah. Haya ni madhehebu ya Ibn ‘Umar, na kundi la Masalaf akiwemo Sufyaan Ath-Thawriy, Yahyaa bin Aadam na Imaam Ahmad.
La pili:
Awe amekopa kwa matumizi yake binafsi na familia yake. Ibn ‘Umar anaona kuwa deni litalipwa, kisha kinachobakia atatoa Zakaah.
Ama Ibn ‘Abbaas, yeye anaona kuwa deni lake halitotolewa toka nje isipokuwa kama alilitumia kugharamia matunda yake kama ilivyotangulia.
Imepokelewa toka kwa Ibn ‘Umar akisema: ((Ataanza kwa alichokopa alipe, kisha atoe Zakaah kilichobakia)).
Ibn ‘Abbaas amesema: ((Atalipa alichotumia kugharamia matunda, kisha atatoa Zakaah kilichobakia)). [Abu ‘Ubayd amekhariji kutoka kwao wawili katika Al-Amwaal (uk. 509), na Yahyaa bin Aadam katika Al-Khuraaj (uk. 162) kwa Sanad Swahiyh]
Kuna riwaya mbili zimepokelewa toka kwa Imaam Ahmad.
Abu ‘Ubayd ametilia nguvu madhehebu ya Ibn ‘Umar na waliokubaliana naye ya kulipa kwanza madeni yote ya nje, kwa kuwa mwenye kudaiwa, mali yake huzingirwa na deni lake, na hapo anakuwa ni katika watu wanaostahiki kupewa swadaqah (Zakaah), basi vipi atoleshwe Zakaah na yeye ni katika watu wanaostahiki kupewa? Vipi awe tajiri na masikini kwa wakati mmoja? [Al-Amwaal cha Abu ‘Ubayd (uk. 510)]
Ninasema: “Kauli hii ndio yenye nguvu zaidi. Na kwa muktadha wake, ikiwa mtu shamba lake limetoa “wasq” 20 za ngano kwa mfano [pishi 1200], na anadaiwa pesa sawa na thamani ya “wasq” 17, basi atatoa “wasq” 17 kulipia deni na atabakiwa na “wasq” 3 ambazo zitakuwa hazina Zakaah, kwa kuwa ni chini ya kiwango. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi”.
2- Ama gharama za ukulima ikiwa hazitokani na deni
Ni kama gharama za mbegu, mbolea, kulima ardhi, uvunaj na mfano wake. ‘Ulamaa katika hili wana kauli mbili:
Ya kwanza:
Hazitolewi toka kwenye mazao yaliyopatikana kabla ya kuchukuliwa moja ya kumi au nusu yake. Ni madhehebu ya Hanafiy na Ibn Hazm. [Haashiyat Ibn ‘Aabidiyn (2/49), Fat-hul Qadiyr (2/8-9) na Al-Muhallaa (5/258)]
Wamesema kwa kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alichukulia tofauti ya cha wajibu (10% au 5%) toka tofauti ya gharama. Na kama gharama zitaondoshwa, basi cha wajibu kingekuwa kwa kiasi hicho hicho, kwa kuwa hakikuteremsha 10% hadi nusu yake isipokuwa gharama. Na fardhi ni chenye kubakia baada ya kutoa kiasi cha gharama, na si gharama zikiwa ndani.
Ya pili:
Hutolewa toka kwenye mazao yaliyopatikana na kinachosalia hutolewa Zakaah. Ni madhehebu ya Hanbali ambayo yameungwa mkono na Ibn Al-‘Arabiy. [Al-Mughniy (2/698), na ‘Aaridhwat Al-Ahwadhiy (3/143)]
Na hili ndilo lenye nguvu zaidi na lililo karibu zaidi na roho ya sharia, nalo linaungwa mkono kwa mambo mawili: [Fiqhu Az Zakaah (1/424)]
1- Ni kuwa gharama na matumizi yana athari. Gharama zinaweza kupunguza kiwango cha wajibu kama kumwagilia kwa mashine, na pia zinaweza kuzuia kabisa Zakaah kama kwa wanyama wanaolishwa majani kipindi kikubwa cha mwaka. Hivyo hakuna ajabu ya kupomosha kilicho mkabala wake katika kinachopatikana toka kwenye ardhi.
2- Ni kuwa ustawi wa kitu ni kuongezeka na kuzidi. Mali haiwezi kuhesabiwa kuwa imeongezeka na kuwa na faida ikiwa itatumiwa mfano wake ili kuipata.
Ardhi Ni Aina Mbili: “’Ushariyyah” (Ya Moja Ya Kumi) Na “Kharaajiyyah” (ya kodi)
“’Ushariyyah” ni ardhi ambayo wamiliki wake wamesilimu kwa khiyari yao wenyewe, au ni ardhi iliyokombolewa kwa nguvu (ya silaha) na kugawanywa kwa wakombozi, au ni ardhi ambayo Waislamu wameifufua.
Na “Kharaajiyyah” ni ardhi iliyokombolewa kwa nguvu kisha wakaachiwa wamiliki wake waendelee kuimiliki bila kugawanywa ngawira kwa wakombozi, au wamiliki hao wakakubalishwa wailipie kodi maalum kwa mkabala wa kuachiwa waitumie.
Kodi hii ni ya aina mbili:
1- Kodi Kazi: Ni kodi inayotoleshwa kwa ardhi, ni sawa mmiliki wake ameitumia kuzalisha au hakuitumia. ‘Umar (Radhwiya Allaahu ‘anhu) aliitolesha na kuitumia.
2- Kodi Mgawano: Ni kodi inayokatwa kutokana na mazao yaliyopatikana. Ni kama kuchukuliwa nusu ya mazao, au theluthi yake, au robo yake. Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alilifanya hilo alipoikomboa Khaybar.
Zakaah Ya Mazao Yanayotoka Kwenye “’Ardhi Kharaajiyyah”
Ardhi Kharaajiyyah ikitoa mazao yanayofikia kiwango cha waajib wa Zakaah, Jumhuri ya ‘Ulamaa wanasema kuwa italipwa kwanza kodi, kisha yaliyobakia yatatolewa Zakaah. Dalili zao ni:
1- Ujumuishi wa Aayaat na Hadiyth zilizotangulia zinazodulisha uwajibu bila kubagua kati ya ‘Ushariyyah na Kharaajiyyah.
2- Barua ya ‘Umar bin ‘Abdul ‘Aziyz aliyomwandikia ‘Abdullaah bin ‘Awf –aliyempa kazi ya kusimamia Palestina- kuhusiana na mwenye ardhi pamoja na jizya yake kati ya Waislamu: achukue jizya yake, kisha achukue kutoka humo Zakaah ya kilichobakia baada ya kutolewa jizya (yaani kodi). [Al-Amwaal cha Abu ‘Ubayd (uk. 88)]
3- Toka kwa Sufyaan Ath-Thawriy akisema kuhusu mazao yaliyotoka kwenye ardhi kharaajiyyah: ((Toa deni lako na kodi yako, na ikiwa itafikia “wasq” tano baada ya hapo, basi toa Zakaah)). [Al-Kharaaj cha Yahyaa bin Aadam (uk. 163)]
4- Ni kuwa kodi na moja ya kumi ni haki mbili zenye kutofautiana kidhati, kimahala, kisababu, kistahikivu na kidalili. Mahanafi wamekwenda kinyume katika hili, wakazuia kujumuika pamoja kodi na moja ya kumi katika ardhi moja. Wametoa dalili kwa Hadiyth baatwil isemayo:
((Moja ya kumi (‘ushru) na kodi (kharaaj) hazikutani katika ardhi ya Muislamu)). [Al-Kaamil cha Ibn ‘Uday (7/2155)].
Ibn Hibaan amesema Hadiyth hii si katika maneno ya Rasuli. Na Sheikh wa Uislamu amesema (25/55) ni uongo kwa makubaliano ya ‘Ulamaa wa Hadiyth.
Kauli ya Jumhuri ndiyo yenye nguvu Zaidi. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Vipi itatolewa Zakaah ya mazao yaliyopatikana toka ardhi iliyokodishwa? Nani atatoa, mwenye ardhi au mkodishiwa?
Jumhuri ya ‘Ulamaa (Maalik, Ash-Shaafi’iy, Hanbali na Maswahiba wawili wa Abu Haniyfah) wanasema kuwa aliyekodisha ardhi kisha akailima na kuipanda, yeye ndiye atakayetoa Zakaah.
Lakini Abu Haniyfah amesema kuwa mwenye ardhi atatoa moja ya kumi.
Nukta ya mzozano wao ni: Je, moja ya kumi ni haki ya ardhi au haki ya mazao? [Bidaayatul Mujtahid (1/239) na Majmu’u Al-Fataawaa (25/55)].
Ninasema: “Lililo bayana zaidi ni kuwa ‘ushru hiyo ni haki ya ardhi. Ni waajib kwa mkodishiwa na si kwa mwenye ardhi –kama wanavyosema Jumhuri- lakini hii ni baada ya kutolewa kodi ya kukodisha ardhi toka kwenye mazao, kwa kuwa inafanana zaidi na kodi ya ardhi”.
Kwa mfano, ikiwa kukodi ardhi ni pauni 20, na ardhi ikazalisha “irdabu” 10 za ngano, na kila irdabu moja ni sawa na pauni 5. Thamani ya mazao yaliyopatikana hapa itakuwa ni (10 × 5 = pauni 50). Hapa atatolea Zakaah irdabu sita tu (= pauni 30), na irdabu nyingine nne zitawekwa kando kulipia kodi ya ardhi. Na ikiwa irdabu sita zilizobakia hazikufikia kiwango, basi hazina Zakaah. [Fiqh Az Zakaah (1/430)]
Ama mmiliki wa ardhi, yeye atatoa Zakaah ya kodi ya ardhi yake kwa mujibu wa maelezo ya nyuma kuhusu Zakaah ya mishahara ya mwezi na mapato ya kazi.
Al-Qaradhwaawiy amekhitari mmiliki wa ardhi alipie Zakaah kile anacholipwa, nayo ni kodi anayoipokea kwa sharti ifikie kiwango kutokana na mazao yaliyopo.
Je, Asali Inatolewa Zakaah?
Katika suala hili, makundi mawili ya ‘Ulamaa yamekhitalifiana kati ya kutowajibisha na kuwajibisha, na kundi jingine limechukua msimamo wa kati na kati.
1- Jumhuri ya ‘Ulamaa akiwemo (Maalik, Ash-Shaafi’iy, Ibn Abiy Laylaa na Ibn Al-Mundhir) wanasema asali haina Zakaah kwa sababu mbili:
(a) Hakuna khabar yoyote wala Ijma’a inayothibitisha uwajibu wa Zakaah kwa asali. Hadiyth ziko wazi kwa vitolewavyo Zakaah, na asali haimo.
(b) Asali ni kimiminika kitokacho kwa mdudu mfano wa maziwa. Na maziwa hayana Zakaah kwa Ijma’a.
2- Hanafi na Ahmad wanasema asali hutolewa Zakaah, na dalili yao ni mambo mawili:
(a) Baadhi ya athar zinazozungumzia hili. Ni kama Hadiyth ya ‘Amri bin Shu’ayb toka kwa baba yake toka kwa babu yake toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kuwa: ((Alichukua ‘ushru ya asali)). [Hadiyth Dhwa’iyf. Imekharijiwa na Ibn Maajah, (1824) na Abu ‘Ubayd katika Al-Amwaal (497/1489). Sanad yake ni Dhwa’iyf].
Pia, imepokelewa toka kwa ‘Amri bin Shu’ayb toka kwa baba yake toka kwa babu yake amesema: ((Hilaal -Ahad Baniy Mut’aan- alikwenda kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) na moja ya kumi ya nyuki wake (asali yake). Alikuwa amemwomba (Rasuli) amlindie bonde lijulikanalo kama Salabah, na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akamlindia bonde hilo. Na ‘Umar bin Al-Khattwaab alipotawala, Sufyaan bin Wahab aliandika kwa ‘Umar bin Al-Khattwaab akimuuliza kuhusiana na hilo. ‘Umar (Radhwiya Allaahu anhu) akaandika: Kama atakupa kama alivyokuwa anatoa kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) moja ya kumi ya nyuki wake (asali yake), basi mlindie Salabah lake, na kama si hivyo, basi hao ni nyuki wa mvua anaila (asali yao) yeyote atakaye)). [Abu Daawuwd (1600), An-Nasaaiy (1/346) na wengineo kwa Sanad Swahiyh. Angalia Al-Irwaa (810)]
Ninasema: “Linalonibainikia mimi ni kuwa riwaya ya pili ndiyo iliyo sawa. Riwaya hii inaitia doa riwaya ya kwanza. Riwaya hii ya kwanza imepitia kwa Ibn Lahiy’ah na nyingine kwa njia ya ‘Amri bin Al-Haarith (anayeaminika, faqiyh na haafidh), na makhraji ni mamoja. Ibn Al-Qayyim –Rahimahul Laah- ameshangaza aliposema: Athar hizi zinatiana nguvu zenyewe kwa zenyewe, na makhraji zake ni nyingi. Njia zake zimetofautiana, mursali yake inatiliwa nguvu na musnadi yake?. [Zaad Al-Ma’aad (1/312].
Na hii tukijua kwamba kuna makhitalifiano katika riwaya nyingine kuhusu waswl yake na irsaal yake.
Na tukiftaridhi (assume) kuwa imethibiti na ni mawsuwlah, basi hakuna la kusema hapo, kwa kuwa linaloonekana ni kuwa moja ya kumi iliyochukuliwa toka kwenye asali haikuwa ni Zakaah, bali ilikuwa ni kwa mkabala wa lindo. Na kama ingekuwa ni Zakaah ya waajib, basi ‘Umar; Faqihi na Mweledi wa Hadiyth asingeikhiyarisha. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi. [Al-Haafidh ameliashiria hili katika Al Fat-h (3/348), na kabla yake Ibn Zanjawiyya katika Al-Amwaal (1095), halafu Al-Khattwaabiy katika Ma’aalim As-Sunan (1/208), halafu nilimwona Al-Albaaniy katika Tamaam Al-Minnah (uk. 374) amekinaika na hili].
(b) Wamesema: “Asali inazalikana kutokana na maua ya miti, hupimwa na huhifadhika. Hivyo ni lazima kuitolea Zakaah kama nafaka na tende. Kwa kuwa pia gharama zake ziko chini kulinganisha na gharama za mazao na matunda”. [Zaad Al-Ma’aad]
Na hawa waliowajibisha Zakaah katika asali, wamewajibisha kutoa moja ya kumi. Mahanafi wameshurutisha kwenye asali inayotolewa Zakaah isiwe inatoka kwenye ardhi kharaajiyyah, na iwe inamilikiwa, lakini pia hawakuainisha kiwango chake, bali wanaona Zakaah itolewe kwa asali nyingi au kidogo.
Lakini Mahanbali wanasema kuwa kiwango cha asali ni “afraaq” kumi ambazo ni sawa na kilo 46.67.
Na Al-Qaradhwaawiy ametilia uzito kiwango kiwe ni “wasq” tano sawa na kilo 647.
3- Abu ‘Ubaydah amechukua msimamo wa kati na kati kama anavyoeleza katika Kitabu cha Al-Amwaal (uk. 506):
“Njia inayoshabihiana zaidi katika jambo lake, yaani asali, ni kuwa wamiliki wake wanaamuriwa kutoa Zakaah yake, na wanahimizwa juu ya hilo, na ni makruhu kwao kuzuia kuitoa, na hakuna dhamana kwao ya kutopata madhambi ikiwa wataficha bila ya hilo kuwa ni faradhi kwao kama ulivyo uwajibu wa Zakaah ya ardhi na mifugo, kwa vile hakuna Hadiyth Swahiyh iliyothibiti kuhusu asali kama ilivyothibiti kwa ardhi na mifugo”.
Ninasema: “Hili ndilo lenye nguvu zaidi kuwa Zakaah si wajibu katika asali lakini kheri haikosekani ikiwa itatolewa. Na kama ni waajib, basi mtu atakuwa ametekeleza wajibu wake na kusafisha dhima yake, na kama si waajib, basi ni swadaqah”.
Na kwa ajili hiyo, Ibn Muflih ambaye ni mtaalamu mbobezi zaidi wa Fiqh ya Sheikh wa Uislamu, alikuwa anaona kuwa hakuna Zakaah katika asali. [Al-Furuu (2/450)]
[1] Abu ‘Ubayd amesimulia kwa Sanad Swahiyh (469/1378) toka kwa Ibn ‘Umar. Amesema kuhusu Zakaah ya mazao na matunda: “Ni ile inayotokana na tende, au zabibu kavu, au ngano, au shayiri”. Na mfano wa hivyo katika Musnad Ash-Shaafi’iy (656) kwa Sanad Swahiyh.
[2] Abu ‘Ubayd ameisimulia kutoka kwake (469/1379-1380), Ibn Zanjawiyyah (1030/1899) kwa Sanad zilizo Swahiyh kutoka kwake.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
19-Zakaah Ya Mali na Bidhaa Za Biashara
Alhidaaya.com [3]
Mali na bidhaa za biashara ni bidhaa zote isipokuwa dhahabu na fedha (silver). Ni kama mizigo, ardhi, viwanja na majumba (real estate), wanyama wa aina tofauti, mazao, mavazi, vyombo, vito vya thamani na mfano wake ambazo ni kwa ajili ya biashara.
Wengine wamezifasili bidhaa kama ni kila kilichotayarishwa kwa ajili ya kuuza na kununua kwa lengo la kupata faida.
Hukmu Ya Zakaah Katika Mali Na Bidhaa Za Biashara
‘Ulamaa wamekhitalifiana kuhusu Zakaah hii katika kauli mbili: [Angalia Fiqhu Az Zakaah (1/340) na baada yake, na vitabu vingine vilivyoashiriwa baadaye]
Kauli ya kwanza:
Ni lazima zitolewe Zakaah. Ni kauli ya Jumhuri ya ‘Ulamaa. Na wengine wameeleza kuwa ni Ijma’a ya Swahaba na Taabi’iyna kama tutakavyokuja kueleza mbeleni. Wametolea dalili Qur-aan, As-Sunnah, Athari za Swahaba na Taabi’iyna pamoja na Qiyaas.
(a) Kutoka kwenye Qur-aan ni Kauli Yake Ta’aalaa:
((يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا أَنفِقُوا مِن طَيِّبَاتِ مَا كَسَبْتُمْ وَمِمَّا أَخْرَجْنَا لَكُم مِّنَ الْأَرْضِ))
((Enyi walioamini! Toeni katika vizuri mlivyochuma na katika ambavyo Tumekutoleeni kutoka katika ardhi)). [Al-Baqarah (2:267)]
Al-Bukhaariy amelihusishia suala hili mlango maalum katika Kitaab Az Zakaah katika Swahiyh yake akisema: (Mlango Wa Zakaah Ya Chumo Na Biashara). Na maana ya Kauli Yake (مَا كَسَبْتُمْ) ni biashara. [Angalia Tafsiyr At-Twabariy (5/555), Ahkaamul Qur-aan cha Ibn ‘Arabiy (1/235) na wengineo]
(b) Na kutoka kwenye As-Sunnah:
Ni Hadiyth ya Samrah bin Jundub aliyesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa akituamuru tutoe Zakaah ya vitu tunavyoviandaa kwa kuuza)). [Hadiyth Dhwa’iyf. Imekharijiwa na Abu Daawuud (1562), na kutoka kwake Al-Bayhaqiy (1/97), Ad-Daaraqutwniy (uk. 214) na wengineo kwa Sanad Dhwa’iyf. Angalia Al-Irwaa (827)]
Na kwa Hadiyth Marfuw’u ya Abu Dharri:
((في الإبل صدقتها، وفي الغنم صدقتها، وفي البز صدقته))
((Katika ngamia kuna Zakaah yake, katika mbuzi na kondoo kuna Zakaah yake, na katika nguo kuna Zakaah yake)). [Hadiyth Dhwa’iyf. Imekharijiwa na Ahmad (5/179), Al-Bayhaqiy (4/147) na Ad-Daaraqutwniy. Angalia Adh-Dhwa’iyfah (1178)]
Nguo hapa ni pamoja na vitambaa, mashuka, matandiko, vyombo na mfano wake. Na vitu hivi vikiwa vya matumizi binafsi, basi havina Zakaah bila mvutano wowote. Hivyo, muradi wa kutolewa Zakaah ni kuwa tu viwe vinatumika kwa faida na biashara.
Tatizo hapa ni kuwa Hadiyth hizi mbili ni Dhwa’iyf. Lakini dalili ya kupasa kutoa Zakaah kwa mali na bidhaa za biashara inapatikana katika ujumuisho wa maneno ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kwa Mu’aadh:
((أعلمهم أن الله افترض عليهم صدقة من أموالهم))
((Wajulishe kuwa Allaah Amewafaradhishia Zakaah kutokana na mali zao..)). [Takhriyj yake ishadokezwa nyuma]
Bidhaa za biashara ni mali bila shaka yoyote, na hii ni kwa kuingia ndani ya mjumuisho wa kauli yake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam): ((Hakika amali ni kwa niya….)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1), na Muslim (1907)]
Kwani hakika, mfanyibiashara akiulizwa: “Unataka nini kwa biashara?” Atasema: “Dhahabu na fedha (silver)?!” [Imenukuliwa toka Ash-Sharhu Al-Mumti’u (6/141)]
Na hili linatolewa dalili vile vile na Hadiyth ya Abu Hurayrah kuhusiana na Khaalid bin Al-Waliyd kukataa kutoa Zakaah na watu kulilalamikia hilo. Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasema:
((وأما خالد، فإنكم تظلمون خالدا، قد احتبس أدراعه وأعتده في سبيل الله...))
((.. ama Khaalid, hakika nyinyi mnamdhulumu Khaalid, hakika yeye amezifungia ngao zake na zana zake za vita katika Njia ya Allaah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1468) na Muslim (983)]
Ni kana kwamba walidhani kuwa ngao na zana hizo ni kwa ajili ya biashara, wakamtaka atoe Zakaah kwa thamani zake. Na Rasuli (‘alayhis Swalaat was salaam) akawajulisha kuwa hakuna Zakaah kwa Khaalid kwa kile alichokifungia. [Angalia Fat-hul Baariy (3/392). Na amesema: Na hii inahitaji nukuu maalum ili iwe na hujja]
(c) Na kutoka kwenye aathaar za Swahaba na Watangu Wema:
1- Ibnu ‘Abdil Qaariy amesema: ((Nilikuwa mweka hazina wa Baytul Maal enzi za ‘Umar bin Al-Khattwaab. Alikuwa unapowadia wakati wa watu kutoa Zakaah, anakusanya mali za wafanyibiashara na kuzipiga hesabu; mali taslimu na mali zisizo taslimu [mifugo, mashamba n.k]. Kisha anachukua Zakaah ya mali taslimu na mali isiyo taslimu)). [Al-Amwaal, Muswannaf Ibn Abiy Shaybah na Al-Muhallaa. Ibn Hazm kasema ni Swahiyh na ameiawilisha]
2- Ibn ‘Umar kasema: ((Hakuna Zakaah katika vitu isipokuwa kwa vile vya biashara)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Ash-Shaafi’iy ameikhariji katika Al-Ummu (2/68), ‘Abdur Raaziq (4/97), na Al-Bayhaqiy (4/147) kwa Sanad Swahiyh]
3- Ibn ‘Abbaas amesema: ((Hakuna ubaya kufuatilia na kusubiri mpaka amalize mauzo, na Zakaah ni waajibu ndani yake)). [Al-Amwaal (uk. 426), na Ibn Hazm katika Al-Muhallaa (5/234). Isnaad Yake kasema ni Swahiyh lakini kaiawilisha]
4- ‘Atwaa amesema: ((Hakuna Zakaah katika lulu, wala zubarjad (aquamarine), wala yakuti (ruby), wala vistoni vya vito, wala bidhaa, wala kitu kisichofanyiwa biashara. Na ikiwa kuna chochote katika hivyo kinafanyiwa biashara, basi kuna Zakaah ndani yake katika thamani yake wakati kinapouzwa)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na Abdur Razzaaq (7061) na Ibn Abiy Shaybah (3/144) kwa Sanad Swahiyh]
5- ‘Umar bin ‘Abdul ‘Aziyz alimwandikia Zurayq akimwambia: ((Angalia waliopita kwako kati ya Waislamu. Chukua kinachoonekana katika mali zao katika vitu wanavyovifanyia biashara dinari moja katika kila dinari 40..)). [Isnaad yake ni Swahiyh. Imekharijiwa na Maalik (594) na Ash-Shaafi’iy katika Al-Ummu (2/68)]
Na hakikunukuliwa kutoka kwa yeyote katika Swahaba chochote chenye kukhalifiana na kauli ya ‘Umar, mwanaye na Ibn ‘Abbaas, bali kazi na fatwaa ziliendelea juu ya hilo katika enzi ya Taabi’iyna na enzi ya ‘Umar bin ‘Abdul ‘Aziyz. Aidha, Fuqahaa wa Taabi’iyna na waliofuatia baada yao, wameitafikiana juu ya kauli inayowajibisha Zakaah katika mali za biashara.
Hata Ibn Al-Mundhir na Abu ‘Ubaydah wamenukuu Ijma’a juu ya hilo isipokuwa kauli moja tu ambayo Abu ‘Ubaydah ameitaja na hakuinasibisha kwa msemaji yeyote. Kisha ‘Uqbah akasema: “Ama kauli nyingine, si katika madhehebu ya ‘Ulamaa kwetu sisi”.
(d) Ama Qiyaas:
Ni kuwa bidhaa zenye kufanyiwa biashara, ni mali zinazokusudiwa kuzalisha faida. Hivyo zinafanana na aina tatu ambazo ni lazima zitolewe Zakaah (dhahabu na fedha, mifugo na mazao).
(e) Ama kwa upande wa kinadhari na kimazingatio:
- Ni kuwa bidhaa za biashara zinazoingia kwenye mzunguko wa soko kwa ajili ya kuuzwa, zinakuwa ni pesa kimaana. Hakuna tofauti kati yake na dirhamu na dinari ambazo ni thamani zake, isipokuwa katika kuwa kiwango kinapanda na kushuka na kubadilika kati ya thamani ambayo ni pesa na kinachotiwa thamani ambacho ni bidhaa. Na lau kama Zakaah si waajib katika mali za biashara, basi matajiri wote au wengi wao wangeliweza kufanya biashara kwa kutumia pesa zao, na wangelipania kiwango cha dhahabu na fedha kisipitiwe kamwe na mwaka, na hivyo Zakaah ingelikwama kwao katika viwili hivyo. [Tafsiyr Al-Manaar ya Rashiyd Ridhwaa (10/591)]
- Watu wanaohitajia zaidi kujitakasa wenyewe pamoja na mali zao na kuzisafisha, ni wafanyibiashara, kwani njia zao za uchumaji mali hazisalimiki na ghushi na ufisadi.
Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) anasema:
(( يا معشر التجار، إن البيع يحضره اللغو والحلف، فشوبوه بالصدقة))
((Enyi jumuiya ya wafanyabiashara! Hakika biashara inaingiliwa na upuuzi na uapaji, basi yachanganyeni hayo kwa Zakaah)). [Abu Daawuwd (3326), At-Tirmidhiy (1208), An-Nasaaiy (3797) na Ibn Maajah (2145). Ni Hadiyth Swahiyh]
Faida
Ibn Al-Mundhir, Abu ‘Ubayd, na kundi la ‘Ulamaa wamenukuu Ijma’a juu ya uwajibu wa Zakaah kwa bidhaa za biashara. Hili linahitajia kuhakikiwa upya, kwa kuwa mvutano katika suala hili ni wa kale –kama alivyoeleza Ash-Shaafi’iy na wengineo- lakini Adh-Dhwaahiriyyah wamesema kinyume na hayo kama itakavyokuja kuelezwa mbeleni. [Al-Ijma’a (14) na Al-Amwaal (429). Angalia pia Al-Majmuw’u (6/47), Bidaayatul Mujtahid (1/254), Ar-Rawdhwatu An Naddiyyah (1/286) na Muswannaf Ibn Abiy Shaybah (3/36,44) chapa ya Al-Fikr]
Kauli ya pili:
Si lazima zitolewe Zakaah. Ni madhehebu ya Adh-Dhwaahiriyyah na walioungana nao kama Ash-Shawkaaniy, Swiddiyq Khaan, kisha Al-Albaaniy. Ibn Hazm katika kitabu chake cha Al-Muhalla ameienzi kauli yao na kuwatetea, na akakamia katika kutengua madhehebu ya Jumhuri.
Kati ya dalili zao ni:
1- Hadiyth
(( ليس على مسلم في عبده ولا فرسه صدقة))
((Hakuna Zakaah kwa Muislamu katika mtumwa wake wala farasi wake)). [Al-Bukhaariy (1464) na Muslim (628)]
Udhahiri wake ni kuwa hakuna uwajibu wa Zakaah sawasawa ikiwa ni kwa biashara au kwa jinginelo.
Jumhuri wamewajibu wakisema kuwa kusudio ni kukanusha Zakaah kwa mtumwa wake anayemtumikia na farasi wake anayempanda, na hao wawili ni katika mahitajio ya asili yanayosamehewa Zakaah kwa Ijma’a.
2- Mali ya Muislamu kiasili haibebeshwi wala kufungamanishwa na makalifisho yoyote, na uasili huu unabakia kama ulivyo ikiwa hakuna dalili ya kuubadilisha. Na nyuma tushasema kuwa Ijma’a ya Swahaba imethibitisha uwajibu wa Zakaah kwa bidhaa za biashara.
3- Hadiyth ya Qays bin Abiy Gharazah aliyesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alitoka kutufuata na sisi tunauza watumwa tukiitwa madalali. Akasema: ((Enyi jumuiya ya wafanyabiashara! Hakika mauzo yenu haya yanachanganyika na upuuzi na uapaji, basi yachanganyeni na Zakaah, au na kitu kidogo cha swadaqah))”. [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Ahmad (4/6), An-Nasaaiy (7/14), Abu Daawuud, At-Tirmidhiy (1208), Ibn Maajah (2154) na wengineo]
Ibn Hazm amesema: “Na hii ni swadaqah ya faradhi isiyo na mpaka, lakini kwa ambazo roho zao zimeridhia, na inakuwa ni kafara kwa yale yanayochanganyika ndani yake katika mambo yasiyofaa kama upuuzi na kuapa”.
Na mengineyo kati ya pingamizi na migogoro ambayo Ibn Hazm ameiibua kwenye Al-Muhalla (5/233) na kurasa zinazofuatia. Na kauli ya Jumhuri ndiyo sahihi. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Shuruti za Zakaah katika mali ya biashara
Ili mali iliyoandaliwa kwa ajili ya kupata faida na biashara iwajibikiwe na Zakaah, ni lazima iwe na shuruti zifuatazo:
1- Mali isiwe kiasili ni katika zinazolazimu Zakaah kama mifugo, dhahabu, fedha na mfano wake, kwa kuwa kwa mujibu wa Ijma’a, Zakaah mbili hazikusanyiki pamoja. [Angalia Al-Majmuw’u (6/50) na Al-Mughniy (3/34)]
2- Ifikie kiwango, nacho ni thamani ya gramu 85 za dhahabu.
3- Ipitiwe na mwaka.
Ni wakati gani kiwango cha mali ya biashara kinaangaliwa?
Kuna kauli tatu kuhusiana na hili:
1- Mwisho wa mwaka (Ni kauli ya Maalik na Ash-Shaafi’iy).
2- Mwaka wote, kwa maana, kiwango kikipungua muda mchache, basi mwaka unakatika (Ni madhehebu ya Jumhuri).
3- Mwanzo wa mwaka na mwisho wake (Ni madhehebu ya Abu Haniyfah).
Vipi mfanyabiashara anaitolea Zakaah mali yake ya biashara?
Unapofika muda wa Zakaah, mfanyabiashara atazikusanya mali zake zote. Mali hizi ni:
1- Mtaji, faida, akiba na thamani ya bidhaa zake.
2- Madeni anayotarajia kulipwa.
Atakokotoa thamani ya bidhaa zilizopo, kisha ataijumlisha na pesa zilizopo pamoja na madeni ambayo ana uhakika mkubwa wa kulipwa, halafu atatoa kando madeni anayodaiwa.
Baada ya kufanya hivi, atatolea vyote hivyo robo ya kumi (2.5%) kwa mujibu wa bei ya wakati wa kutoa Zakaah, na si kwa bei ya kununulia bidhaa.
Hii ndio rai ya Jumhuri ya Fuqahaa. Maalik ameungana nao katika hili kwa mfanyabiashara mwenye kuendesha shughuli za ununuzi na uuzaji.
Lakini amesema kuhusu mfanyabiashara (mlanguzi) ambaye ananunua bidhaa au viwanja, kisha anaziweka, anasubiri na anafuatilia mwenendo wa soko mpaka bei ipande ndipo auze, amesema kwamba huyu hatoi Zakaah isipokuwa kama atauza bidhaa. Bidhaa hiyo ataitolea Zakaah ya mwaka mmoja tu hata kama alibaki nayo kwa miaka mingi.
Je, ni bidhaa zenyewe zinazotolewa kwa Zakaah au thamani yake?
Jumhuri wanasema ni waajib kutoa thamani, na haijuzu kutoa bidhaa yenyewe, kwa kuwa kiwango cha Zakaah hutathminiwa kwa thamani, na Zakaah kutokana na thamani hiyo imekuwa ni kama kitu katika mali nyinginezo.
Lakini Abu Haniyfah na Ash-Shaafi’iy –katika moja ya kauli zake- wanaona kuwa mfanyabiashara ana khiyari ya kutoa bidhaa au thamani ya bidhaa. [Al-Badaai (2/21) na Al-Mughniy (3/31)]
Ama Sheikh wa Uislamu, yeye amekhiyari kuwa pande zote mbili ni sawa kwa mujibu wa unafuu kwa mpewa Zakaah. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/80)]
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
20-Zakaah Ya Rikaaz Na Madini
Alhidaaya.com [3]
Maana ya الركاز “Rikaaz” katika lugha ya kawaida ni kitu kilichohifadhiwa chini ya ardhi kama madini au mali au kinginecho.
Ama kisharia (kiistilahi), ni hazina ya mali iliyofukiwa chini enzi ya kale ambayo hutolewa bila gharama zozote wala kazi kubwa ikiwa ni dhahabu, au fedha au vinginevyo.
Ama madini katika lugha ya kawaida, ni kutokana na neno la Kiarabu العدن kwa maana ya kukaa mahala muda mrefu, na pia ina maana ya kiini cha kitu.
Ama kiistilahi, ni kila kinachotoka ardhini ambacho kimeumbwa humo kutokana na mada nyinginezo, na kina thamani.
Kuna madini magumu ambayo huyeyushwa na kuchakatwa kwa moto kama dhahabu, fedha, chuma, shaba, risasi na zebaki. Pia yapo madini miminika kama petrol, lami na mfano wake.
Rikaaz na madini ina maana moja kwa Mahanafi lakini Jumhuri ya ‘Ulamaa wametofautisha kati ya viwili hivi kutokana na Hadiyth ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((...والمعدن جبار، وفي الركاز الخمس))
((Na madini [atakayeumia au kudhurika kwenye mgodi] hakuna fidia, na katika rikaaz ni khumsi [moja ya tano = 20%])). [Al-Bukhaariy (1499) na Muslim (1710)]
Hapa Rasuli ametofautisha kati ya madini na rikaaz.
Atakayegundua (okota) hazina ya mali, nini afanye?
Atakayeokota au kugundua hazina ya mali, hakosi kuwa na moja ya hali tano:
[1] Aipate kwenye ardhi ambayo haikuguswa na mtu au ambayo haina mmiliki
Itakuwa ni halali yake. Atatoa Zakaah khumsi yake (moja ya tano), na nne zilizobaki atachukua yeye.
Imepokewa na ‘Amri bin Shu’ayb toka kwa baba yake toka kwa babu yake kuwa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema – kuhusu hazina ya mali ambayo mtu mmoja aliipata kwenye magofu ya enzi ya ujahili -:
((إن وجدته في قرية مسكونة أو في سبيل ميتاء فعرفه، وإن وجدته في خربة جاهلية، أو في قرية غير مسكونة، ففيه، وفي الركاز الخمس))
((Ikiwa umeipata kwenye kijiji chenye watu, au katika njia inayopitwa sana na watu, basi itangazie. Na kama umeipata kwenye magofu ya enzi za ujahili, au katika kijiji kisicho na watu, basi ichukue, na katika rikaaz khumsi)). [Abu Daawuwd (1710), Ash-Shaafi’iy katika Musnadi wake (674), Ahmad (2/207), na Al-Bayhaqiy (4/155)]. Sanad yake ni Hasan.
[2] Aipate kwenye barabara inayopitwa na watu au kijiji chenye watu
Huyu ataitangazia. Akipatikana mwenyewe basi atamkabidhi, na kama hakupatikana, basi ni haki ya mgunduaji kwa mujibu wa Hadiyth iliyotangulia.
[3] Aipate kwenye milki ya mtu mwingine. Hapa ‘Ulamaa wana kauli tatu:
Ya kwanza:
Itakuwa ni ya mmiliki wa ardhi. Ni kauli ya Abu Haniyfah, Muhammad bin Al-Hasan, Qiyaas ya kauli ya Maalik, na riwaya toka kwa Ahmad.
Ya pili:
Itakuwa ya mgunduaji. Ni riwaya nyingine toka kwa Ahmad, na Abu Yuwsuf ameiridhia. Wamesema: Sababu ni kuwa hazina haimilikiwi kwa kumiliki nyumba, hivyo inakuwa ni mali ya aliyeigundua.
Ya tatu:
Ni kwa uchanganuzi huu: Ikiwa mmiliki wa ardhi au nyumba atakiri ni yake, basi itakuwa mali yake, na kama akisema si yake, basi itakuwa haki ya mmiliki wa kwanza. Ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy.
[Al-Mabsuwtw (2/214), Fat-hul Qadiyr (2/183), Al-Mughniy (3/49), Al-Ummu (2/41) na Al-Majmuw’u (6/40)]
[4] Aikute ndani ya mali iliyohamia kwake kwa kununua au mfano wake. Hapa kuna kauli mbili:
Ya kwanza:
Itakuwa ya aliyeipata baada ya kumiliki mali ikiwa mmiliki wa kwanza hakuidai. Ni madhehebu ya Maalik, Abu Haniyfah na mashuhuri toka kwa Ahmad.
Ya pili:
Itakuwa ya mmiliki wa kabla yake kama atasema ni yake, na kama hakusema itakuwa ni ya wa nyuma yake na kuendelea. Na kama mmiliki wake hakujulikana, basi itakuwa ni kama mali iliyopotea. Hii ni kauli ya Ash-Shaafi’iy.
[Al-Mabsuwtw (2/212), Al-Mudawwanah (1/290), Al-Mughniy (3/49), Al-Ummu (2/44), na Al-Majmuw’u (6/40)]
[5] Aikute kwenye eneo la vita
Ikiwa ataipata kwa mbinde akisaidiana na kundi la Waislamu, basi itakuwa ni ngawira na itabeba hukmu ya ngawira. Na kama aliweza mwenyewe kuipata bila kusaidiwa, hapa ‘Ulamaa wana kauli mbili:
Ya kwanza:
Ni ya alieipata. Ni madhehebu ya Ahmad, kwa kufananisha na kilichopatikana kwenye ardhi ambayo haikuguswa na mtu.
Ya pili:
Mmiliki wa ardhi akijulikana na akawa adui anayeupiga vita Uislamu, basi atazuiliwa ardhi, na ardhi itakuwa ghanima. Na kama hakujulikana na ardhi haikuzuiliwa, basi itakuwa ni rikaaz. Ni madhehebu ya Maalik, Abu Haniyfah na Ash-Shaafi’iy kwa uchanganuzi kati yao.
[Al-Mughniy (3/50), Al-Mudawwanah (1/291), Al-Mabsuwtw (2/215) na Al-Majmuw’u (6/40)]
Si sharti kiwango kitimie au mwaka ukamilike kwa rikaaz
Kiwango na mwaka havishurutishwi katika rikaaz, bali hulazimu kutolewa Zakaah mara tu inapopatikana. Atatoa khumsi (moja ya tano = 20%) kutokana na kauli yake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((في الركاز الخمس))
((Katika rikaaz khumsi)). [Muttafaqun ‘alayhi]
Hii ni kauli ya Jumhuri ya ‘Ulamaa.
Nani atapewa khumsi ya Rikaaz?
‘Ulamaa wamekhitalifiana katika kubainisha watu wa kupewa khumsi katika kauli mbili:
Ya kwanza:
Khumsi hutolewa kwa wastahiki wale wale wa Zakaah. Ni kauli ya Ash-Shaafi’iy na Ahmad ingawa amesema kuwa ikiwa ataitoa swadaqah kwa masikini itamtosheleza.
Dalili yao ni yaliyosimuliwa toka kwa ‘Abdullaah bin Bishr Al-Khath-’amiy ambaye alipokea toka kwa mtu wa jamii yake akiitwa Hajamah akisema: ((Niliangukiwa na gudulia kwenye parokia la kale huko Kufa kwenye makaburi ya Bishr, ndani yake kuna dirham elfu nne. Nikaenda nalo kwa ‘Aliy bin Abiy Twaalib, akaniambia nizigawanye mafungu matano, nami nikazigawa. ‘Aliy akachukua fungu moja (moja ya tano) kati yake, halafu akanipa nne ya tano. Nilipompa mgongo kuondoka aliniita na kuniuliza: Je, una majirani mafukara au masikini? Nikamwambia na’am. Akasema: Basi lichukue uwagawanyie kati yao)). [Imekharijiwa na ‘Abdur Razzaaq (7179), At-Twahaawiy katika Sharhul Ma’aaniy (3/304), na Al-Bayhaqiy (4/157) kwa Sanad Dhwa’iyf]
Na kwa vile rikaaz inanufaikiwa toka ardhini, imefananishwa na mazao ya kilimo.
2- Hutolewa kwa wastahiki wa “fay-u” (mali inayochukuliwa toka kwa makafiri bila mapigano). Ni kauli ya Abu Haniyfah, Maalik, na riwaya katika madhehebu ya Ahmad, na Ibn Qudaamah amesema ni kauli swahiyh.
Dalili yao ni yaliyosimuliwa toka kwa Ash-Sha’abiy akisema: ((Mtu mmoja alikuta dinari 1000 zimezikwa akitokea Madiynah. Akaenda nazo kwa ‘Umar bin Al-Khattwaab (Radhwiya Allaahu ‘anhu), na ‘Umar akachukua khumsi yake dinari 200, na zilizobaki akamwachia mwenyewe. ‘Umar akaanza kuzigawa dinari 200 kwa Waislamu waliokuwepo kwake mpaka akabakisha baki. Akauliza: Yuko wapi mwenye dinari? Akasimama na kumwendea, na ‘Umar akamwambia: Chukua dinari hizi, ni zako)). [Al-Amwaal cha Abu ‘Ubayd (874) kwa Sanad Dhwa’iyf]
Ushahidi hapa ni kuwa lau zingelikuwa ni Zakaah, basi angezihusisha na wastahiki wake tu, na asingezirudisha tena kwa aliyezipata.
Wamesema: Na kwa vile “fay-u” ni waajib kwa Dhimmiy (kafiri anayeishi nchi ya Kiislamu kwa kulipa kodi, na anapatiwa himaya na haki zote za nchi), na Zakaah si waajib kwake, na kwa vile pia ni mali inayogawanywa mafungu matano, mkono wa kafiri unaondoshwa [kwa mazingatio kuwa ilizikwa enzi ya ujahili], hivyo inafanana na khumsi ya ngawira.
Ninasema: “Dalili hizi mbili hazifai kutolea hoja. Hata Al-Albaaniy (Allaah Amrehemu) amesema: “Hakuna kwenye Sunnah lolote lenye kutoa ushahidi wa wazi kwa kauli moja juu ya nyingine. Na kwa ajili hiyo, nimekhitari katika (hukmu ya rikaaz) kuwa pa kupelekwa kutaachiwa kiongozi wa Waislamu aamue anavyoona yeye; ataiweka pale anapoona kuna maslaha zaidi ya nchi. Na hili pia ndilo alilolikhitari Abu ‘Ubayd katika Al-Amwaal”. [Tamaam Al-Minnah uk. 378]
Je, madini yanaingia kwenye hukmu ya Rikaaz?
Maalik na Ash-Shaafi’iy wanaona kuwa madini hayapaswi kutolewa chochote isipokuwa dhahabu na fedha.
Ama Jumhuri, wao wanasema kuwa madini kwa aina zake zote; dhahabu, fedha (silver), shaba, chuma, risasi, petroli na mengineyo, ni kama rikaaz ambayo ni lazima haki yake itolewe, ingawa wamekhitalifiana katika kiasi chake cha kutolewa. [Al-Mabsuwtw (2/295), Al-Mudawwanah (1/292), Al-Ummu (2/45) na Al-Mughniy (3/50)]
Kauli hii ndiyo yenye nguvu zaidi kutokana na ujumuishi wa Kauli Yake Ta’aalaa:
يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا أَنفِقُوا مِن طَيِّبَاتِ مَا كَسَبْتُمْ وَمِمَّا أَخْرَجْنَا لَكُم مِّنَ الْأَرْضِ ۖ وَلَا تَيَمَّمُوا الْخَبِيثَ مِنْهُ تُنفِقُونَ وَلَسْتُم بِآخِذِيهِ إِلَّا أَن تُغْمِضُوا فِيهِ ۚ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ غَنِيٌّ حَمِيدٌ
((Enyi walioamini! Toeni katika vizuri mlivyochuma na katika ambavyo Tumekutoleeni kutoka katika ardhi. Na wala msikusudie vibaya kutoka humo mkavitoa na hali nyinyi wenyewe si wenye kuvichukuwa isipokuwa kwa kuvifumbia macho. Na jueni kwamba hakika Allaah ni Mkwasi, Mwenye kustahiki kuhimidiwa)). [Al-Baqarah (2:267)]
Na hakuna shaka kuwa mafuta (petrol) yanayojulikana kama dhahabu nyeusi, ni katika madini yenye thamani kubwa zaidi. Hivyo basi, haiswihi kutolewa nje ya hukmu hii. Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
Kiasi cha uwajibu katika madini
Abu Haniyfah na maswahibu wake, Abu ‘Ubayd na wengineo, wanaona kuwa kiasi cha uwajibu katika madini ni khumsi kama rikaaz.
Lakini Jumhuri wanasema ni robo ya kumi (2.5%) kwa kufanyia Qiyaas na kiwango cha dhahabu na fedha.
Kiini cha makhitalifiano kati ya makundi haya mawili, ni kutofautiana kwao katika ufahamu wa maana ya rikaaz. Je, madini yanaingia kwenye rikaaz au hayaingii?
Baadhi ya Fuqahaa wamefafanua wakisema: “Ikiwa kinachopatikana ni kingi kulinganisha na kazi na gharama, basi hapo wajibu ni khumsi (20%). Na kama ni kidogo kulinganisha na kazi na gharama, basi wajibu ni robo ya kumi (2.5%)”. [Angalia Fiqhu Az Zakaah (1/471) na kurasa zinazofuatia]
Na mtu ana haki ya kusema kuwa madini hayana Zakaah –isipokuwa dhahabu na fedha- kutokana na Hadiyth inavyosema:
((والمعدن جبار، وفي الركاز الخمس))
((Na madini [atakayeumia au kudhurika kwenye mgodi] hakuna fidia, na katika rikaaz ni khumsi [moja ya tano = 20%])).
.. ambapo maana ya (المعدن جبار) ni kwamba hakuna Zakaah kwenye madini kwa dalili ya kukutanika kwake na neno ((و في الركاز الخمس)) Isitoshe, rikaaz ni mali iliyotayari ambayo huchukuliwa bila gharama wala tabu yoyote kinyume na madini ambayo yanahitaji gharama na kazi kubwa ya kuyatoa, na kwa ajili hiyo Zakaah imeondoshwa kwa madini.
Ingawa yamkinika pia muradi wa neno lake (المعدن جبار) kuwa kwa maana ya mwenye kumkodi mtu wa kumchimbia madini, mgodi ukamfunika akafa, basi hakuna fidia. Inatiliwa nguvu na kukutanishwa na neno lake:
((البئر جبار، والعجماء جبار))
((Kisima hakina fidia, na mnyama hana fidia)). [Kwa maana kuwa mtu akianguka kwenye kisima cha mtu akaumia au mtu akamkodi kumchimbia kikamwangukia, basi hakuna kulipwa fidia. Au mnyama wa mtu akaharibu mali au akamdhuru mtu bila ya uzembe wa mmiliki wake, basi hakuna fidia].
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
21-Hukmu Kiujumla Katika Zakaah
Alhidaaya.com [3]
Je, Yatosheleza Kutoa Thamani (pesa) Badala Ya Kitu Chenyewe Kilichowajibikiwa Zakaah?
‘Ulamaa wana madhehebu mawili katika kutoa thamani katika Zakaah:
La kwanza: Hilo halijuzu. Ni madhehebu ya Maalik, Ash-Shaafi’iy, Ahmad na Daawuwd. [Al-Mudawwanah (1/258), Al-Majmuw’u (5/428-429) na Al-Mughniy (2/565)]
Hoja yao ni:
1- Sharia imeeleza na kuainisha cha waajib katika Zakaah, hivyo haijuzu kutoka nje ya kiainishwa, kama isivyojuzu katika wanyama wa kudhwahi [kuchinja wasiotajwa kama paa], wala katika manufaa, wala katika kafara.
2- Kauli ya Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((في خمس وعشرين من الإبل بنت مخاض، فإن لم تكن بنت مخاض فابن لبون))
((Katika ngamia ishirini na tano [atolewe] binti makhaadh, na kama hakuna binti makhaadh, basi [atolewe] ibn labuwn)). [Imekharijiwa nyuma]
Wamesema: Kama thamani ingejuzu, basi angebainisha.
3- Neno lake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kwa yule ambaye amewajibikiwa kumtoa jadha‘a:
((تقبل منه الحقة ويجعل معها شاتين أو عشرين درهما))
((Hukubaliwa toka kwake hiqqah na aongeze juu yake mbuzi wawili, au dirhamu ishirini)). [Imekharijiwa nyuma]
Wamesema: Lau thamani ingelikuwa inatosheleza, basi asingemkadiria, bali amewajibisha tofauti kwa mujibu wa thamani.
4- Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((فرض زكاة الفطر صاعا من تمر، أو صاعا من شعير..))
((Amefaradhisha Zakaatul Fitwr pishi ya tende, au pishi ya shayiri..)). [Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1504) na Muslim (984)]
Wamesema: Hapa hakutaja thamani, na kama thamani ingejuzu, basi angeeleza, kwani haja inaweza kupelekea hilo.
5- Pale Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alipomwambia Mu’aadh wakati alipomtuma kwenda Yemen:
((خذ الحب من الحب، والشاة من الغنم، والبعير من الإبل، والبقرة من البقر))
((Chukua nafaka kutoka nafaka, na mbuzi kutoka ghanam, na ngamia kutoka ngamia, na ng’ombe kutoka ng’ombe)). [Imekharijiwa na Abu Daawuwd (1099), Ibn Maajah (1814), Al-Haakim (1/546), Al-Bayhaqiy (4/112) na Ad-Daaraqutwniy (2/99). Kuna ulaini katika Sanad yake]
6- Zakaah ni waajib kwa ajili ya kuondosha dhiki ya masikini, na kutoa shukurani kwa neema ya mali. Na dhiki ziko nyingi, hivyo basi, inatakikana uwajibu uanuwaike ili umfikie masikini kwa aina zote ambazo zitaondosha dhiki yake, na kuishukuru neema kupatikane kwa faraja itokanayo na kile kile ambacho Allaah Amemneemesha mtu.
La pili: Inajuzu kutoa thamani (pesa). Ni madhehebu ya Abu Haniyfah, Ath-Thawriy katika madhehebu ya Al-Bukhaariy, kauli ya nguvu katika madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na riwaya toka kwa Ahmad. Hoja yao ni: [Al-Mabsuwtw (2/156) na Al-Majmuw’u (2/429)]
1- Yaliyosimuliwa toka kwa Mu’aadh bin Jabal (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba aliwaambia watu wa Yemen: ((Nileteeni vitambaa vya vazi la khamiysw au nguo za kuvaliwa badala ya shayiri na mahindi nichukue kutoka kwenu, kwani hilo ni jepesi zaidi kwenu na lenye kuwafaa zaidi Muhaajiriyna Madiynah)). [Al-Bukhaariy kasema ni Mu’allaq (3/336), na Al-Haafidh kasema ni Mawswuwl katika At-Taghliyq (3/12) kwa Sanad Dhwa’iyf kutokana na kukatika kwake]
2- Wametoa dalili ya kutosheleza ibn labuwn badala ya binti makhaadh, na kutosheleza hiqqah na juu yake dirhamu 20 badala ya jadha‘a. (Na hizi ni dalili mbili; ya pili na ya tatu ya madhehebu ya kundi la kwanza).
Wamesema, katika hili thamani inachukulika.
3- Makusudio ya kutoa Zakaah ni kumkidhia masikini mahitaji, na kumkidhia ni kwa kumpatia pesa, na pia kumpatia kitu. Na huenda kumwondoshea dhiki ya uhitaji kwa pesa kukawa na manufaa zaidi.
Kila kundi limejitahidi kuzijibu dalili za kundi jingine na kutilia nguvu mwelekeo wake. Ninaloliona lina nguvu zaidi kwa upande wangu ni lile lililokhitariwa na Sheikh wa Uislamu Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah), nalo ni kuchukulia ukati na kati katika mlango huu. Hakujuzisha ikawa ndio mwisho, wala hakuzuia ikawa ndio basi. Anaona inajuzu kutoa pesa (thamani) lakini kujuzu huko kufungamane na haja, maslaha na haki.
Na kama hakuna haja wala maslaha muhimu, basi lenye nguvu kwake ni kuwa hairuhusiwi kutoa pesa. Mwelekeo wake huu ni qaaidah ya kukusanya kati ya dalili tofauti. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/80-82)]
Nini hukmu ya kuwahisha Zakaah kabla ya kupitiwa na mwaka?
Umejua kwamba mali ikifikia kiwango, basi si waajib kuitolea Zakaah mpaka mwaka ukamilike. Lakini ikiwa mwenye mali anataka kuitolea Zakaah kabla ya kutimia mwaka, hapa ‘Ulamaa wana kauli mbili:
Ya kwanza: Inajuzu. Ni madhehebu ya Abu Haniyfah, Ash-Shaafi’iy, Ahmad na kundi la Masalaf. [Al-Mabsuwtw (2/176), Al-Ummu (2/20), Al-Majmuw’u (6/86) na Al-Mughniy (2/470)]
Dalili zao ni:
1- Yaliyosimuliwa ya kuwa Al-‘Abbaas alimuuliza Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kuhusu kuwahisha Zakaah yake kabla ya muda wake. ((Rasuli akamruhusu hilo)). [Abu Daawuwd (1624), At-Tirmidhiy (678), Ibn Maajah (1795) na wengineo. Al-Albaaniy kasema ni Hadiyth Hasan katika Al-Irwaa (857)].
2- Yaliyosimuliwa kuwa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwambia ‘Umar:
((إنا كنا تعجلنا صدقة العباس لعامنا هذا عام أول))
((Hakika sisi tulikuwa tumeiwahisha Zakaah ya Al-‘Abbaas katika mwaka wetu huu, mwaka wa kwanza)). [Angalia iliyotangulia]
3- Huo ni uwahishaji wa mali ambayo sababu ya uwajibu wake imeshapatikana (nayo ni kukamilika kiwango), kabla ya uwajibu wake wa kiwakati. Ni kama kuharakisha kulipa deni kabla ya kufika muda wake, kutoa kafara ya kiapo baada ya kuapa na kabla ya kuvunja kiapo, na kafara ya kuua baada ya kujeruhi kabla ya roho kutoka.
Ya pili: Ni marufuku. Ni madhehebu ya Maalik (lakini amelijuzisha kama zimebakia siku chache za kukamilika mwaka). Pia ni kauli ya Rabiy-‘a, Daawuwd na Ibn Hazm. [Al-Mudawwanah (1/284), Bidaayatul Mujtahid (1/232) na Al-Muhallaa (6/95)]
Dalili zao ni:
1- Hadiyth Marfuw’u ya Ibn ‘Umar: ((Hakuna Zakaah katika mali mpaka yapitiwe na mwaka)). [At-Tirmidhiy (631), Abu Daawuwd (1573), Ibn Maajah (1792), Ad-Daaraqutwniy (198) na Al-Bayhaqiy (4/104). Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh katika Al-Irwaa (787)]
2- Hadiyth ya Abu Bakr As-Swiddiyq: ((Ni kuwa alikuwa hachukui katika mali Zakaah mpaka yapitiwe na mwaka)). [Muswannaf ‘Abdur Razzaaq (7024)]
3- Ni kwamba mwaka ni sharti katika kuwajibika Zakaah. Hivyo haijuzu kutolea Zakaah mapema kama kiwango.
4- Ni kuwa Zakaah ina wakati wake. Hivyo haijuzu kuitanguliza kabla ya wakati kama ilivyo kwa Swalaah.
Kauli yenye nguvu
Inajuzu kutoa Zakaah kabla ya kupita mwaka kwa kuwa hakuna dalili ya kuzuia hilo. Ama Hadiyth (ya Ibn ‘Umar) “Hakuna Zakaah katika mali mpaka yapitiwe na mwaka”, ni kuwa Hadiyth inafahamisha tu kwamba si wajibu kutoa Zakaah kabla ya mwaka kutimilia, na hakuna ndani yake kinachozuia kuiwahisha.
Ama wanaposema: “Zakaah ina wakati wake maalum na haijuzu kuitanguliza kabla ya wakati huo”, basi sisi tunawaambia kuwa wakati unapoingia kwenye kitu, na ukanasibiana na kumfariji mtu, basi inatakikana (mhusika) auharakishe (kumfariji) badala ya kujifariji yeye binafsi. Ni kama deni la muda. Ama kupimia na Swalaah, hilo halijuzu kwa kuwa ‘ibaadah hazifanyiwi vipimo zenyewe kwa zenyewe, na kufananishia nyakati za Swalaah haiwezekaniki, na hivyo ni lazima zisivuke zaidi ya hapo. Allaah Ndiye Mjuzi zaidi”.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
22-Maswaarif Za Zakaah (Wastahiki Wa Kupewa Zakaah)
Alhidaaya.com [3]
Maswaarif za Zakaah zimeainishwa katika aina nane tu, na aina hizi nane zimetajwa na Al-Qur-aan Al-Kariym katika Kauli Yake Ta’aalaa:
((إِنَّمَا الصَّدَقَاتُ لِلْفُقَرَاءِ وَالْمَسَاكِينِ وَالْعَامِلِينَ عَلَيْهَا وَالْمُؤَلَّفَةِ قُلُوبُهُمْ وَفِي الرِّقَابِ وَالْغَارِمِينَ وَفِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَابْنِ السَّبِيلِ ۖ فَرِيضَةً مِّنَ اللَّـهِ ۗ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ))
((Hakika Zakaah ni kwa ajili ya mafakiri na masikini na wanaozitumikia, na wanaotiwa nguvu nyoyo zao (katika Uislamu) na kuwakomboa mateka, na wenye deni na katika Njia ya Allaah na msafiri (aliyeharibikiwa). Ni faradhi itokayo kwa Allaah. Na Allaah ni Mjuzi wa yote, Mwenye hikmah wa yote)). [At-Tawbah (9:60)]
انما Ambayo imeanziwa kwayo Aayah, ni neno la kudhibiti kitajwa kisiingie kingine, hivyo basi haijuzu kupewa Zakaah yeyote ambaye hayumo ndani ya aina hizi.
Je, Ni Lazima Aina Hizi Nane Wapewe Wote, Au Inajuzu Kupewa Baadhi Yao Tu?
Jumhuri ya ‘Ulamaa (Abu Haniyfah, Maalik, Hanbali na kundi la Masalaf akiwemo ‘Umar na Ibn ‘Abbaas) wanaona si lazima aina hizi nane kupewa wote katika mali ya Zakaah, bali yajuzu kupewa mmoja tu kati yao, na kumpa swadaqah pamoja na kuwepo wengine.
Wametoa hoja kwa yafuatayo:
1- Kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((تاخذ من أغنيائهم فترد على فقرائهم))
((Huchukuliwa toka kwa matajiri wao na hurejeshwa kwa mafakiri wao)). [Muttafaqun ‘Alayhi. Imetajwa nyuma mara nyingi]
Wamesema: Mafakiri ni aina moja kati ya aina za wastahiki nane wa Zakaah.
2- Yaliyosimuliwa kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliwapa watu Zakaah kama Hadiyth ya Qabiyswah bin Makhaariq alipokopa deni kubwa (la kudhamini suluhu kati ya watu) na akamjia Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kumwomba Zakaah, na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akamwambia:
((أقم حتى تأتينا الصدقة فنأمر لك بها))
((Kaa mpaka itujie Zakaah, kisha tuamuru upewe)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1044)]
Kuna matukio mengine ambayo baadhi yake yametajwa nyuma.
Lakini Ash-Shaafi’iy na kundi jingine wanasema kuwa ni lazima mgawo wa Zakaah uwaenee wote wa aina hizi nane. Abu Thawr na Abu ‘Ubayd wamesema: Ikiwa kiongozi mhusika atagawa Zakaah, basi ni lazima agawe kwa aina zote, lakini mmiliki wa mali akitoa, basi inajuzu kuitoa kwa aina moja tu. [Al-Majmuw’u (6/185), Al-Mughniy (2/668) na Al-Amwaal cha Abu ‘Ubayd (uk. 692)]
[1,2] Mafukara na masikini
Mafukara na masikini ni watu wahitaji wasiopata cha kuwatosheleza. Linapotajwa neno mafukara peke yake, basi huingia pamoja nao masikini, na pia kinyume chake. Na kama yatatajwa yote mawili katika sentensi moja kama katika Aayah ya wastahiki, basi kila moja litakuwa na maana tofauti na mwenzake.
‘Ulamaa wamekhitalifiana kuhusu nani kati ya wawili ni mhitaji zaidi kuliko mwingine. Ash-Shaafi’iy na Hanbali wanasema kuwa fakiri ni mhitaji zaidi kuliko masikini. Dalili yao wanasema kuwa Allaah Amewataja kwanza wao katika Aayah, na hii ni dalili kuwa wao ndio muhimu zaidi. Pia kwa Neno Lake Ta’aalaa:
((أَمَّا السَّفِينَةُ فَكَانَتْ لِمَسَاكِينَ يَعْمَلُونَ فِي الْبَحْرِ))
((Ama jahazi, ilikuwa ya masikini wanaofanya kazi baharini)). [Al-Kahf (18:79)]
Hapa Amewathibitishia sifa ya umasikini pamoja na kuwa wanamiliki jahazi na wanapata nauli.
Kadhalika, wamejiridhisha na hilo pia kutokana na mnyambuliko (wa neno). “Al-Faqiyr” (الفقير)katika lugha liko katika wazni wa “Fa’iyl” (فعيل) kwa maana ya mtendwa, naye ni mtu aliyeondolewa baadhi ya pingili za uti wake wa mgongo, na mgongo wake ukakatika. Na “Al-Miskiyn” (المسكين) liko katika wazni wa “Mif-‘iyl” (مفعيل) kutokana na neno “As-Sukuwn” (السكون) [kutulia]. Na mtu ambaye uti wake wa mgongo umevunjika anakuwa mhitaji zaidi kuliko “As-Saakin” (aliyetulia).
Lakini Hanafiy na Maalik wanaona kuwa masikini ni mhitaji zaidi kuliko fakiri. Dalili yao wanasema kuwa Allaah Mtukufu Anasema:
(( أَوْ مِسْكِينًا ذَا مَتْرَبَةٍ))
((Au maskini aliye hohehahe)). [Al-Balad (90:16]
Huyu ni masikini aliyetupwa juu ya udongo kutokana na njaa kali. Pia wanasema vigogo wa lugha wamesema hilo akiwemo Al-Farraai, Tha-‘alab na Ibn Qutaybah. Aidha, kutokana pia na mnyambuliko, kwani masikini linatokana na neno “As-Sukuwn” (kutulia) kana kwamba ameshindwa kusogea na kubakia pale alipo. Ad-Dusuwqiy amenukulu kauli isemayo kuwa fakiri na masikini ni mtu huyo huyo mmoja, naye ni ambaye hana chakula cha mwaka wake, sawasawa akiwa hana kitu kabisa, au ana chakula kidogo cha kumtosheleza mwaka mzima.
Fuqahaa wamekhitalifiana kuhusu mpaka (wa kipato) kwa masikini na fakiri
[Al-Mawsuw-’at Al-Fiqhiyyat (23/312)]
Ash-Shaafi’iy na Hanbali wanasema kuwa fakiri ni mtu asiye na mali wala kipato kinachokidhi mahitaji yake. Ni kama mtu ambaye anahitajia kumi na hapati chochote kabisa, au yule ambaye kwa mali yake, kipato chake na anachokipata kutokana na ardhi yake na kinginecho, anaweza kupata chini ya nusu ya mahitaji yake. Na ikiwa anapata nusu au zaidi lakini hapati kumi kamili, basi huyo ni masikini.
Hanafy na Maalik kwa upande wao wanasema masikini ni yule ambaye hana kitu asilani akahitajia kuomba, na huyu kuomba ni halali kwake. Lakini kwa upande wa fakiri wametofautiana. Hanafiy anasema: Fakiri ni yule mwenye kitu kidogo ambacho hakifikii kiwango (cha Zakaah). Ikiwa atamiliki kiwango kutoka mali yoyote ya Zakaah, basi huyo ni tajiri hastahiki kupewa chochote katika Zakaah. Na akimiliki chini kidogo ya kiwango, basi si mstahiki. Vile vile akimiliki kiwango ambacho hakiongezeki, nailhali ametingwa na mahitaji ya kimsingi (atapewa), na kama hakutingwa atazuiliwa. Ni kama mwenye nguo zenye thamani sawa na kiwango (cha Zakaah) ambazo hazihitajii, basi Zakaah ni haramu kupewa. Na ikiwa thamani ya anavyovimiliki itafikia kiwango, basi hilo halizuii yeye kuwa katika wastahiki wa Zakaah ikiwa thamani itatosheleza mahitaji asili. Ni kama mwenye vitabu anavyovihitaji kufundishia, au zana za kazi na mfano wa hivyo.
Maalik amesema: Fakiri ni yule ambaye anamiliki kitu ambacho hakimtoshi kwa chakula chake cha mwaka.
Utajiri unaozuia kupewa Zakaah kwa mujibu wa picha ya ufakiri na umasikini:
Haijuzu kiasli tajiri kupewa Zakaah. Hii ni itifaki ya ‘Ulamaa kutokana na neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((لا حظ فيها لغني))
((Hakuna fungu ndani yake kwa tajiri)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (1633) na An-Nasaaiy (2598)]
Lakini wamekhitalifiana kwa upande wa utajiri wenye kuzuia mtu kuchukua Zakaah. Jumhuri ya ‘Ulamaa wa madhehebu ya Maalik na Ash-Shaafi’iy, na riwaya ya Ahmad ambayo maswahibu zake waliofuatia baadaye waliikadimisha, wamesema: “Jambo linazingatiwa kwa kujitosha. Atakayepata pesa au kinginecho kinachomtosha na kuwatosha anaowakimu, basi huyo ni tajiri ambaye Zakaah si halali kwake. Na kama hakupata hilo, Zakaah itakuwa ni halali kwake hata kama alichonacho kitafikia viwango vya Zakaah. Na juu ya msingi wa haya, haizuii kuwepo mtu ambaye anawajibika kutoa Zakaah na wakati huo huo akawa mstahiki wa kupewa Zakaah”.
Mahanafiy wamesema: “Huo ni utajiri wenye kuwajibisha Zakaah. Hivyo, anayewajibikiwa Zakaah, si halali kwake achukue Zakaah kutokana na neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam): ((Hakika Allaah Amewafaradhia Zakaah, inachukuliwa toka kwa matajiri wao ikarudishwa kwa mafukara wao)).
Na mwenye kumiliki kiwango katika mali yoyote ya kutolewa Zakaah, basi huyo ni tajiri, haijuzu kupewa Zakaah hata kama alichonacho hakimtoshi kwa mwaka. Na ambaye hamiliki kiwango kamili, basi huyo ni fakiri au masikini inajuzu kumpa Zakaah kama ilivyotangulia”.
Na katika riwaya nyingine ya Mahanbali ambayo ina nguvu zaidi katika madhehebu yao ni kuwa akipata cha kumtosha, basi huyo ni tajiri, na kama hakupata na akawa na dirhamu 50, au thamani yake katika dhahabu, basi huyo ni tajiri hata kama haimtoshi. Na hii ni kwa Hadiyth isemayo:
((من سأل الناس وله ما يغنيه جاء يوم القيامة ومسألته في وجهه خموش أو خدوش أو كدوح. قالوا يا رسول الله وما يغنيه؟ قال: خمسون درهما أو قيمتها من الذهب))
((Mwenye kuomba watu naye anacho kinachomtosheleza, atakuja Siku ya Qiyaamah na (athari ya) ombaomba zake. Katika uso wake makovu, au mikwaruzo au mabaka”. Wakasema: Ee Rasuli wa Allaah! Ni kipi kinamtosheleza? Akasema: Dirhamu 50 au thamani yake ya dhahabu)) [Kuna mvutano katika Sanad yake. Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (650) na Ibn Maajah (1840)]
Na bila shaka wamepambanua kati ya thamani na vinginevyo kufuata Hadiyth.
Je, inajuzu kumpa Zakaah fakiri au masikini mwenye uwezo wa kufanya kazi na kulipwa?
Mtu yeyote fakiri au masikini mwenye kuweza kupata kipato cha kumtosha yeye na kuwatosha anaowakimu, au kuwatosheleza na kuzidi, basi si halali kwake kuchukua Zakaah. Ni kwa neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
(( لا حظ فيها لغني ولا لقوي مكتسب))
((Hakuna fungu ndani yake kwa tajiri wala kwa mwenye nguvu mwenye kuweza kupata kipato)). [Abu Daawuwd (1617) na An-Nasaaiy (5/99). Al-Albaaniy kasema Swahiyh]
Na kauli yake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
(( لا تحل الصدقة لغني ولا لذي مرة سوي))
((Si halali Zakaah kwa tajiri wala kwa mwenye nguvu mzima wa afya)). [At-Tirmidhiy (647) na Abu Daawuwd (1618). Angalia Swahiyh Al-Jaami’i (7251)]
Haya ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na Hanbali, nayo ndiyo yenye nguvu.
Lakini Hanafiy na Maalik, wao wanasema kuwa inajuzu kupewa madhali ni fakiri na masikini. Wametoa dalili kutoka kwenye mnasaba wa kisa cha Hadiyth tuliyoitaja. ((Ni kuwa watu wawili walimwomba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) Zakaah, naye akawapindulia macho yake kuwakagua, akawaona mashupavu. Akasema: Mkitaka nitawapeni, na hakuna fungu ndani yake kwa tajiri wala kwa mwenye nguvu mwenye kipato)). [Imekharijiwa nyuma kidogo]
Wamesema: Hapa amejuzisha kuwapa. Na neno lake (..hakuna fungu..) maana yake ni: “Hakuna haki wala fungu kwenu katika kuomba”. [Fat-hul Qadiyr (2/28), Al-Mughniy (6/423), Al-Majmuw’u (6/190) na Al-Mawsuw’at Al-Fiqhiyyah (23/316)]
Ninasema: “Hayafichikani yaliyomo ndani ya taawiyl hii. Lenye kuonekana bayana ni kuwa neno lake “Mkitaka nitawapeni” halimaanishi kujuzisha kupewa Zakaah, bali ni tahadharisho. Ni kama Kauli Yake Ta’aalaa:
((فَمَن شَاءَ فَلْيُؤْمِن وَمَن شَاءَ فَلْيَكْفُرْ))
((Basi anayetaka aamini, na anayetaka akufuru)). [Al-Kahf (18:29)]
Kiasi anachopewa fakiri na masikini katika Zakaah
Kwa mujibu wa Jumhuri ya ‘Ulamaa, fakiri na masikini hupewa Zakaah ya kumtosha au iliyokamili kwake yeye na anaowakimu kwa muda wa mwaka mzima, na haiongezwi zaidi ya hapo.
Wameweka mpaka wa mwaka mmoja kwa kuwa Zakaah hukariri aghlabu kila mwaka, na kwa kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam): ((Alikuwa anahifadhi kwa wakeze chakula cha mwaka mzima)). [Al-Bukhaariy (5357) na Muslim (1757)]
Baadhi yao wamesema: “Kama ni mtu wa kazi za mikono, basi atapewa cha kununulia vifaa vya kazi yake kwa namna ya kuweza kupata faida ya kumtosheleza takriban mahitaji yake”. [Al-Majmuw’u (6/194)]
[3] Wenye kuitumikia Zakaah (Wakusanyaji)
Inajuzu kuwapa Zakaah wenye kuitumikia (wakusanyaji). Mkusanyaji anayepewa Zakaah ni lazima awe na masharti yaliyofafanuliwa nyuma, na mwenye kupewa katika wakusanyaji hao si lazima awe fakiri, kwa kuwa anapewa kutokana na kazi yake, na si kutokana na ufakiri. Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amesema:
((لا تحل الصدقة لغني إلا لخمسة.. قذكر منهم العامل عليها))
((Si halali Zakaah kwa tajiri ila kwa watano…Akataja miongoni mwao mwenye kuitumikia Zakaah)). [Imekharijiwa na Abu Daawuwd (1635) na Ibn Maajah (184)]
Hanafiy amesema: “Mkusanyaji atalipwa kwa mujibu wa kazi yake. Atapewa cha kumtosheleza yeye na kuwatosheleza wasaidizi wake bila kukadiriwa kwa thamani, wala haongezewi zaidi ya nusu ya alichokusanya hata kama kazi yake ni kubwa zaidi”.
Ash-Shaafi’iy na Hanbali wamesema: “Kiongozi anatakiwa amwajiri mkusanyaji ajira rasmi kwa malipo maalumu, ima kwa muda maalumu au kwa kazi maalum”.
Kisha Ash-Shaafi’iy akasema: “Mkusanyaji hapewi kutoka kwenye (mali jumla ya) Zakaah zaidi ya thumni, na ikiwa malipo yake yatapindukia zaidi ya thumni, basi atakamilishiwa toka Baytul Maal”.
Wengine wamesema atakamilishiwa toka fungu lililobaki. Kadhalika, kiongozi anaweza kumpa malipo yake toka Baytul Maal, na anaweza kumtuma kama kibarua kisha akaja kumlipa malipo sawa na kazi aliyoifanya. Na ikiwa kiongozi atabeba jukumu la kukusanya Zakaah na ugawaji wake, au Mkuu wa Jimbo, au Kadhi au mfano wao ambao wameteuliwa na kiongozi, basi haitojuzu wachukue chochote toka kwenye Zakaah, kwa kuwa wanachukua mishahara yao toka Baytul Maal. Kazi za hawa hazina mpaka maalum.
[4] Wenye kuzoeshwa nyoyo
Wenye kuzoeshwa nyoyo wako aina mbili: Makafiri na Waislamu, na hawa wote ni vigogo waheshimiwa wenye kutiiwa na kusikilizwa na watu wao na koo zao.
Waislamu katika hawa wako aina nne:
1- Waheshimiwa wenye sauti mbele ya watu wao ambao wamesilimu lakini nyoyo zao bado dhaifu. Hawa hupewa ili kuwaweka imara ki-iymaan.
2- Watu watukufu wenye madaraka ambao wamesilimu. Hawa hupewa kwa ajili ya kuwaraghibisha wenzao katika makafiri ili wasilimu.
3- Wanaopewa kwa lengo la kuwazoesha huko kuwe kwa ajili ya kupambana na makafiri walio jirani nao, na kuwahami Waislamu walio karibu nao.
4- Wanaopewa kwa lengo la kuwashajiisha wasiotoa Zakaah wapate kutoa.
Ama makafiri, wao wako aina mbili:
1- Anayetarajiwa kusilimu. Huyu hupewa ili nafsi yake ipondokee kwenye Uislamu.
2- Anayehofiwa shari yake, na kwa kumpa hutarajiwa kuzuia shari yake na kuwazuia wengine pamoja naye. [Al-Mughniy cha Ibn Qudaamah (2/498)]
Je, fungu la wenye kuzoeshwa nyoyo limekatika baada ya kufariki Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) au bado lipo?
‘Ulamaa wamekhitalifiana katika suala hili katika kauli mbili: [Sharhu Fat-hil Qadiyr]
Ya kwanza:
Fungu la wenye kuzoeshwa nyoyo bado lipo kama zilivyo aina nyinginezo zilizotajwa katika Kitabu cha Allaah. Haya ni madhehebu ya Ahmad, na ni kauli inayotegemewa kwa Maalik na Ash-Shaafi’iy. Pia ni kauli ya Al-Hasan na Az-Zuhriy.
Ya pili:
Fungu lao limekatika baada ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam). Ni madhehebu ya Maalik, Ash-Shaafi’iy na Abu Haniyfah. Hoja yao ni kuwa Allaah Ameshautia Uislamu nguvu na uimara na Ameutosheleza na suala la watu kuzoeshewa. Wamelitolea hili dalili kwa kusema kuwa ‘Umar bin Al-Khattwaab hakutoa fungu hili kwa watu waliokuwa wanapewa, na akasema: ((Ni kitu ambacho Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alikuwa anawapeni ili awazoeshe, na sasa Allaah Ameshautia nguvu Uislamu na Hawahitajieni..)). [Sunan Al-Bayhaqiy (7/20)]
“Kiukweli ni kuwa ‘Umar hakulifuta fungu hili, bali hakuwapa kwa kuwa hawakuwa tena na sifa inayowafanya kuitwa (wazoeshwa nyoyo). Na hii ni kwa upande wa kufanya ijtihaad kwa kuwepo vigezo vya kuitumia matini, na si kwa upande wa kufuta hukmu ya matini, na hili liko wazi. Na kwa msingi huu, ikiwa itatokea haja ya kuwapa wenye maana na sifa ya (wazoeshwa nyoyo), basi hapo mtawala atawapa kutoka fungu hili kwa mujibu wa maslaha ya Waislamu, na hususan nguvu ya Waislamu ikiwa imepinduka na kuwa udhalili, na maadui zao kuwa juu yao.” [Al-Mafswal cha ‘Abdul Kariym Zaydaan (1/433-434) kwa mabadilisho kidogo]
[5] Watumwa
Hawa wako makundi matatu:
La kwanza.
Ni watumwa Waislamu walioandikishiana mkataba na mabwana zao. Hawa inajuzu kuwapa Zakaah kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri ya ‘Ulamaa kwa ajili ya kuwasaidia wajikomboe. Maalik hakujuzisha hilo, na pia hakujuzisha kutoa chochote katika Zakaah katika kumkomboa mtumwa ambaye ana njia ya kuachiliwa bila kuandikishiana mkataba kama kuwepo mkakati (wa kukomboka), kutwaa (mamlaka) na kuwa sehemu (ya bwana mmiliki).
Na kwa mujibu wa kauli ya Jumhuri ya ‘Ulamaa ni kuwa aliyeandikishiana mkataba husaidiwa kama hawezi kulipa sehemu ya malipo ya mkataba wake. Na kama hana kitu kabisa, basi atalipiwa malipo yote anayohitaji kumaliza mkataba.
La pili.
Kumkomboa Muislamu. Maalik na Ahmad katika riwaya yake wamejuzisha kutolewa Zakaah kwa ajili ya hili. Na kwa msingi huu, ikiwa Zakaah iko mkononi mwa mtawala au mkusanyaji Zakaah, basi itajuzu wao kumnunua mtumwa au watumwa na kisha kuwaacha huru, na muamana wao utakuwa kwa Waislamu. Na hivyo hivyo, ikiwa Zakaah iko mkononi mwa mwenye mali na akataka kumwacha huru mtumwa kikamilifu kutokana na Zakaah hiyo, basi hilo litajuzu kutokana na ujumuishi wa Aayah ((وفي الرقاب)) na muamana wake utakuwa kwa Waislamu kwa mujibu wa Maalik.
Hanafiy, Ash-Shaafi’iy na Ahmad katika riwaya nyingine wanasema hakombolewi kutokana na Zakaah, kwa kuwa hilo linakuwa kama kutoa Zakaah kwa mtumwa hohehahe, na mtumwa hapewi Zakaah, na kiuhalisia, bwana wake ndiye atakayeihodhi. Hanafiy anasema kukomboa ni kufuta umiliki, na si kumilikisha, lakini ikiwa Zakaah yake itasaidia kukomboa mtumwa, basi hilo litajuzu kwa mujibu wa Mahanbali wenye kauli hii.
La tatu:
Kumkomboa mateka wa Kiislamu anayeshikiliwa na Mapagani. Mahanbali, Ibn Habiyb na Ibn Al-Hakam wamesema hili linajuzu, kwa kuwa ni kumkomboa mtu matekani, na hili linaingia kwenye ujumuishi wa Aayah, bali ni muhimu zaidi kuliko kumwacha huru mateka tunayemshikilia. Maalik amelikataa hilo.
[6] Wenye madeni
Wadaiwa wenye kustahiki Zakaah ni wa aina tatu:
Aina ya kwanza:
Anayedaiwa deni la kibinafsi. Huyu ‘Ulamaa wote kiujumla wamekubaliana kuwa anastahiki. Masharti ya kumpa Zakaah mdaiwa huyu ni haya yafuatayo:
1- Awe Muislamu.
2- Asiwe wa kutoka Aalil Bayt (ukoo wa Rasuli). Lakini Hanbali anasema inajuzu kumpa Aalil Bayt Zakaah kama anadaiwa.
3- ‘Ulamaa wa Kimaalik wameshurutisha asiwe amekopa ili apewe Zakaah. Ni kama mtu kuwa na cha kumtosha, halafu akatanua matumizi katika fedha za deni ili achukue Zakaah kinyume na fakiri aliyekopa kwa dharura kwa nia ya kuchukua toka kwenye Zakaah.
4- Pia wameshurutisha deni liwe la mdaiwa ambaye mali yake inaweza kushikiliwa. Linaingia hapa deni analomdai mtoto baba yake na deni analodaiwa mtu mwenye hali ngumu. Haliingii hapa deni la kafara na Zakaah.
5- Kwa sharti la Mashaafi’iy, deni liwe la kulipwa wakati uliopo. Wamesema: Ikiwa deni ni la kulipwa mbeleni, basi kuna kauli tatu katika suala hili, ya tatu yake ni kuwa ikiwa muda wa mbeleni wa kulipwa ni mwaka huo huo, basi atapewa, na kama si hivyo hatopewa Zakaah za mwaka huo.
6- Asiweze kulipa kutokana na mali aliyonayo ya Zakaah au isiyo ya Zakaah iliyozidi toshelezo lake. Ikiwa thamani ya nyumba anayoishi ni sawa na mia, naye anadaiwa mia, ilhali nyumba ya hamsini inamtosha, basi hatopewa mpaka iuzwe, na kinachozidi kitalipwa kwenye deni lake kwa mujibu wa kauli ya Maalik. Na kama atapata cha kujazilia sehemu ya deni lake, basi atapewa kilichobakia tu. Na ikiwa ataweza kulipa deni kamili baada ya muda kwa kufanya kazi, basi itajuzu kumpa Zakaah kwa mujibu wa kauli mbili za Ash-Shaafi’iy.
Aina ya pili:
Aliyekopa kwa sababu ya kusuluhisha watu. Asili ya hili ni Hadiyth ya Qubayswah aliyesema: ((Nilikopa fedha nikazitumia kusuluhishia watu, kisha nikamwendea Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kumwomba anisaidie akaniambia: ((Kaa mpaka itujie Zakaah, tuamuru upewe)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1044), Abu Daawuwd (1624) na An-Nasaaiy (5/96)]
Ash-Shaafi’iy na Maalik wanasema mdaiwa wa aina hii hupewa Zakaah ni sawa akiwa tajiri au fakiri, kwa kuwa lau ingeshurutishwa mtu awe fukara (ndio apewe), basi utashi ungepungua katika kazi hii ya kutukuka na kuthaminiwa. Na picha yake ni kuwepo mzozo kati ya makabila mawili au mitaa miwili na watu wakawa wanauana au kuharibiana mali, hapo akakopa fedha kwa ajili ya kusuluhisha kati yao. Huyu atapewa Zakaah ili alipe deni lake hilo.
Mahanafiy wamesema: “Mwenye deni hilo hapewi Zakaah isipokuwa tu kama hamiliki kiwango cha ziada ya deni lake kama wadaiwa wengineo”.
Maalik katika kumpekua kwetu, hakuzungumza lolote kuhusu hukmu ya kundi hili.
Aina ya tatu:
Anayedaiwa kwa sababu ya deni la kudhamini. Ash-Shaafi’iy kaielezea aina hii. Lenye kuzingatiwa hapa ni kuwepo hali ngumu ya kipesa kwa mdhamini na mdhaminiwa. Ikiwa mmoja wa wawili hao anajiweza kifedha, basi kuna makhitalifiano na uchambuzi kati yao kuhusu kupewa mdhamini Zakaah. [Al-Mawsuw’atu Al-Fiqhiyyah (23/322)].
Maiti Mdaiwa
Akifa mtu anayedaiwa na hakuna cha kulipa deni lake katika alichokiwacha, basi haijuzu kulipa deni lake kwa Zakaah kwa mujibu wa rai ya Jumhuri.
Lakini Maalik amesema deni lake litalipwa kutoka kwenye Zakaah hata kama amekufa. Wengine wamesema: Ana haki zaidi ya kulipiwa kwa vile hakuna kabisa tamaa ya yeye kulilipa, nayo ni moja ya kauli mbili za Ash-Shaafi’iy.
[7] Fiy Sabiylil Laah
Kundi hili lina aina tatu:
Aina ya kwanza:
Ni wapiganaji katika Njia ya Allaah Ta’aalaa ambao hawana fungu lolote kwenye hazina ya dola, bali wanajitolea tu kushiriki katika Jihaad. Fuqahaa wote kiujumla wamekubaliana kuwa inajuzu kundi hili kupewa Zakaah kiasi cha kuwawezesha kujiandaa kwa vita kwa kupata kipando, silaha, matumizi na yote anayoyahitajia mpiganaji katika kipindi chote cha vita hata kama vita vitachukua muda mrefu. Na si sharti mpiganaji awe masikini, bali inajuzu kumpa tajiri kwa mujibu wa rai ya Jumhuri, kwa kuwa hachukui Zakaah hiyo kujinufaisha nafsi yake, bali ni kwa maslaha ya Waislamu wote.
Hanafiy kasema: Ikiwa mpiganaji ni tajiri, naye ni yule anayemiliki dirhamu 50 au thamani yake kwa dhahabu kama ilivyotangulia katika kundi la mafakiri, basi hapewi Zakaah. Na kama hana, basi atapewa hata kama ana kazi ya kumpatia kipato, kwa kuwa kazi itamzuia asishiriki Jihaad. Na kwa mujibu wa Muhammad, yeye anasema الغازي ni mtu aliyeshindwa kufuatana na Mahujaji (kwenda kuhiji) na si yule aliyeshindwa kuungana na wapiganaji (kwenda Jihaad).
Maalik ameeleza kuwa ni sharti mpiganaji awe mwenye kuwajibikiwa na Jihaad kama kuwa Muislamu, mwanamume, aliyebaleghe, mwenye uwezo na asiwe katika Aalul Bayt.
Ama askari jeshi wenye mishahara toka hazina ya dola, hawa hawapewi Zakaah. Ash-Shaafi’iy anasema katika moja ya kauli zake mbili kuwa ikiwa itashindikana kupatiwa mishahara toka Baytul Maal kutokana na ukata wa fedha, basi itajuzu kuwapa Zakaah.
Aina ya pili:
Ni miundo mbinu ya vita. Wanachuoni wa Kimaalik wameitaja aina hii. Sahihi kwao ni kuwa inajuzu kutumia mali ya Zakaah kwa maslahi mengine ya Jihaad kando na malipo ya wapiganaji kama kujenga ngome za kuhami mji (nchi) usivamiwe na maadui, au kutengenezea vipando vya kivita, au kumlipa jasusi wa kupeleleza habari za adui akiwa Muislamu au kafiri.
Baadhi ya Wanachuoni wa Kishaafi’iy wamejuzisha kununua silaha na zana za vita kwa mali ya Zakaah, na silaha hizo zifanywe waqf ambapo wapiganaji watazitumia kisha watazirejesha. Mahanbali hawakulijuzisha hili, na ndilo lililofanywa na Fuqahaa wengine ambapo wamelihusisha fungu la Fiy Sabiylil Laah kwa wapiganaji tu, au wapiganaji na Mahujaji tu. Fuqahaa hao wamesema kuwa haijuzu kutolewa Zakaah katika aina hii, kwa kuwa hakuna umilikishaji, au upo lakini si kwa wastahiki wa Zakaat. Au kama alivyosema Ahmad kuwa hakuna aliyepewa Zakaat, na Zakaah imeamuriwa itolewe.
Aina ya tatu:
Mahujaji. Jumhuri ya ‘Ulamaa (Hanafiy, Maalik, Ash-Shaafi’iy, Ath-Thawriy, Abu Thawr na Ibn Al-Mundhir, nayo ni riwaya toka kwa Ahmad, na Ibn Qudaamah kasema ni swahiyh) wanaona kuwa haijuzu kutoa Zakaah kwa ajili ya Hijjah, kwa kuwa Sabiylil Laah katika Aayah ni mutwlaq, na itwlaaq imelenga kwenye “Jihaad tu” Fiy Sabiylil Laah Ta’aalaa (na si vinginevyo). Kwa kuwa mengi yaliyotajwa katika Kitabu cha Allaah Ta’aalaa yamekusudiwa Jihaad.
Ahmad anaona Hajji ni katika Njia ya Allaah (Sabiylil Laah), hivyo hutolewa Zakaah, na hii ni kutokana na simulizi isemayo: “Mtu mmoja alimtoa ngamia wake katika Njia ya Allaah, na mkewe akataka kuhiji. Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akasema: ((Ama hakika wewe, lau utamhijisha kwa kumpandisha ngamia huyu, itakuwa ni katika Njia ya Allaah)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (1974), Al-Haakim (1838) na Al-Bayhaqiy (6/164)]
Kwa msingi wa kauli hii, hapewi Zakaah mwenye mali ya kumtosha kuhijia, na asiye na mali ya kumtosha hupewa kwa Hajji ya faradhi tu. Mahanbali wanasema: Inajuzu hata kwa Hajji ya Sunnah.
Imenukuliwa toka kwa baadhi ya Fuqahaa wa Kihanafiy kuwa mstahiki wa kupewa katika (Fiy Sabiyli Laah) ni yule aliyeshindwa kwenda na Mahujaji (kwa kuwa hana kitu). Isipokuwa anayetaka kuhiji kwa mujibu wa Fuqahaa wa Kishaafi’iy hupewa Zakaah kwa mazingatio kuwa ni msafiri kama itakayobainishwa mbeleni.
[8] Ibnus Sabiyl (Msafiri)
Ameitwa “Ibnus Sabiyl” kwa kutoachana kwake na njia, na kutokuwepo nchini kwake kupata hifadhi ya makazi.
Ibn As Sabiyl ni wa aina mbili:
Wa kwanza:
Aliyeko ughaibuni mbali na nchi yake na hana nauli ya kumrejesha. Huyu bila makhitalifiano ni katika watu wa kupewa Zakaah, atapewa cha kumfikisha kwao. Kauli dhwa’iyf ya Ash-Shaafi’iy inasema hapewi, kwa kuwa hilo linakuwa katika hukmu ya kuhamisha Zakaah toka nchi yake (ya asili).
Mghaibu huyu hapewi Zakaah isipokuwa kwa masharti yafuatayo:
La kwanza: Awe Muislamu lakini si Aalul Bayt.
La pili: Asiwe na mali wakati huo ya kumwezesha kurudi kwao hata kama ni tajiri nchini kwake. Na kama ana fedha ambazo atazipata baadaye, au zipo kwa mtu ambaye hayupo, au mwenye hali ngumu ya kifedha, au mwenye kukanusha deni, basi hayo hayazuii kupewa Zakaah kwa kauli ya Hanafiy.
La tatu: Safari yake isiwe ya maasia. Sharti hili limetolewa na Maalik, Ash-Shaafi’iy na Hanbali. Inajuzu kumpa ikiwa safari yake ni kwa ajili ya twa’a ya waajib kama Hajji ya faradhi, kuwatendea wema wazazi, au ya twa’a ya sunnah kama kuwazuru ‘Ulamaa na watu wema, au ya mubaaha kama kutafuta maisha na kufanya biashara. Na kama safari yake ni ya maasi’a, basi haijuzu kumpa Zakaah kwa kuwa itakuwa ni kumsaidia maasi’a yake ila tu kama atatubu. Ama ikiwa safari ni ya matembezi tu, hapa Hanbali ana miono miwili: na wenye nguvu zaidi ni kuwa haijuzu kupewa kwa kuwa safari hii hakuwa na ulazima nayo.
La nne: Asipate wa kumkopesha (ughaibuni) kama ni tajiri kwao. Sharti hili limetolewa na Maalik peke yake.
Watu wa fungu hili hawapewi Zakaah zaidi ya kinachowatosha kurejea makwao. Hanbali amesema: Kama ana nia ya kwenda nchi nyingine, basi atapewa cha kumfikisha huko, kisha na cha kumrejesha nchini kwake.
Maalik amesema: Kama atakaa nchi ya ughaibuni baada ya kupewa Zakaah, basi atapokonywa kama si fakiri nchini kwake. Na ikiwa kitabaki cha kubaki baada ya kurejea nchini kwake, basi kitachukuliwa kwa mujibu wa kauli ya Hanbali. Kisha Hanbali amesema: (Msafiri) mwenye uwezo wa kulipa deni, basi ni bora akope badala ya kuchukua Zakaah.
Wa pili:
Aliyeko nchini kwake na anataka kufanya safari. Jumhuri ya ‘Ulamaa wamekataza kupewa Zakaah watu wa aina hii, lakini Ash-Shaafi’iy amejuzisha kupewa kundi hili kwa sharti msafiri huyo asiwe na masurufu ya safari, na safari isiwe ya ma’asia.
Kwa msingi huu, inajuzu kumpa Zakaah anayetaka kuhiji kama hana fedha za kuhijia katika mji wake anakoanzia safari ya Hajji.
Mahanafiy hawaoni kuwa inajuzu kupewa Zakaah aina hii, lakini wanaona kuwa mtu aliyeko mjini kwake na hana fedha zozote za matumizi lakini anazo fedha mji mwingine ambao hawezi kwenda, basi atazingatiwa ni Ibn As Sabiyl. [Al-Mawsuw’at Al-Fiqhiyyah (23/324)]
Je, inajuzu mtoto au baba kupewa Zakaah?
Inajuzu mtu kuwapa Zakaah wazazi wake, au wanawe -ambao hawamtegemei kwa matumizi ya maisha– kama wana madeni, au wameandikishiana mkataba wa kujikomboa, au wapiganaji. [Majmu’u Al-Fataawaa cha Ibn Taymiyyah (25/90-92) na Al-Muhallaa (6/151-152)]
Ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy [Al-Majmuw’u cha An-Nawawiy (6/229]
Lakini kama ni mafukara na yeye hana uwezo wa kuwakimu kimaisha, Jumhuri wanasema ni marufuku kuwapa Zakaah. Sheikh wa Uislamu –Allaah Amrehemu- amekhitari kujuzu kuwapa Zakaah akishindwa mtu kuwakimu. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/90-92)].
Hili ndilo lenye nguvu zaidi, kwa kuwa Jumhuri kuzuia mtu kuwapa Zakaah anaowakimu kimaisha kumetokana na sababu mbili. Ya kwanza, kwa kuwakimu, yeye anakuwa ni mwenye kujitosheleza. Ya pili, kwa kumpa Zakaah, yeye mwenyewe anajinufaisha, na manufaa hayo ni kuzuia uwajibu wa kuwakimu.
Na ikiwa mtu hawezi toka mwanzoni kuwakimu, au hakuwa akilazimika kuwakimu, basi sababu mbili zitakuwa hazipo tena pamoja na uwepo wa muktadha. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
[Ninasema: “Huenda kujuzu kunatiliwa nguvu na Hadiyth ya Mu’an bin Yaziyd aliyesema: ((…na baba yangu –Yaziyd- alikuwa ametoa dinari kadhaa za swadaqah (Zakaah). Akaziweka kwa mtu msikitini, nami nikaenda, nikazichukua, halafu nikaenda nazo kwake. Akasema: Wallaah, si wewe niliyekusudia kumpa, nikaenda kumshtakia kwa Rasuli. Rasuli akasema: Umepata uliyoyakusudia ee Yaziyd, na ni haki yako uliyochukua ee Mu’an)). [Imesimuliwa na Al-Bukhaariy (1422)]
Na hapa iko ihtimali kuwa Mu’an baba yake Yaziyd alikuwa akimkimu kimaisha. Hivyo inakuwa ni hoja ya kujuzu kuwapa watoto Zakaah bila pingamizi, au anaweza kuwa anajitegemea mwenyewe na hahitaji matumizi toka kwa baba yake, na hii inakuwa hoja ya kujuzu kuwapa Zakaah watoto ambao baba hawakimu kimaisha. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Je, inajuzu mke kumpa Zakaah yake mumewe kama ni mstahiki wa Zakaah?
‘Ulamaa wamekhitalifiana katika suala hili katika kauli mbili:
Ya kwanza: Haijuzu kumpa. Ni madhehebu ya Abu Haniyfah, Maalik na riwaya toka kwa Ahmad. [Al-Mudawwanah (1/298), Sharhu Fat-hil Qadiyr (2/209) na Al-Mughniy (2/484)]
Hoja yao katika hili ni:
- Mume ni jozi ya wanandoa wawili. Haifai mmoja wao kumpa mwenzake Zakaah yake kama mtu wa kando.
- Mke atanufaika na Zakaah hiyo hiyo kwa kumpa mumewe.
Ya pili: Inajuzu kumpa. Ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na riwaya nyingine toka kwa Ahmad. [Al-Majmuw’u (6/138) na Al-Mughniy (2/484)]
Ni kauli yenye nguvu zaidi kwa kuwa inawafikiana na dalili.
Ni kwa Hadiyth ya Abu Sa’iyd isemayo kuwa Zaynab mke wa Ibn Mas-‘uwd alisema: ((Ee Nabiy wa Allaah! Hakika wewe umeamuru leo swadaqah (Zakaah). Na mimi nilikuwa na mapambo yangu nikataka kuyatoa Zakaah. Ibn Mas-‘uwd akadai kuwa yeye na mwanaye wana haki zaidi ya kupewa Zakaah hiyo nami. Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) akasema:
((صدق ابن مسعود، زوجك وولدك أحق من تصدقت به عليهم))
((Amesema kweli Ibn Mas-‘uwd. Mumeo na mwanao wana haki zaidi wewe kuwapa Zakaah kuliko wengine)). [Al-Bukhaariy (1462), Muslim (1000) na Ibn Maajah (1834)]
Na kwa vile mke si waajib wake kutoa matumizi kwa mumewe, basi hazuiliwi kumpa mumewe Zakaah kama mtu wa kando.
Ama mume, yeye Zakaah yake haijuzu kumpa mke wake, kwa kuwa pesa za matumizi ya mke wake yako juu yake. Pesa hizo zitamkidhi na kuzuia asichukue Zakaah. Ibn Al-Mundhir amenukulu Ijma’a juu ya hili. [Al-Mughniy (6/649) na Al-Badaai’u (2/49)]
Je, ndugu akraba wa damu hupewa Zakaah?
Ndugu akraba ikiwa wanastahiki Zakaah inajuzu kuwapa. Wao ni bora zaidi kupewa kuliko wengineo. Ni kutokana na neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
(( صدقتك على ذي الرحم صدقة وصلة))
((Swadaqah [Zakaah] yako kwa ndugu wa damu, ni swadaqah na ni kuunga [udugu])). [Imekharijiwa na At-Tirmidhiy (658), An-Nasaaiy (2582) na Ibn Maajah (1844). Kuna udhwa’iyf ndani yake]
Linalototewa ushuhuda ni yaliyomo kwenye Hadiyth ya Zaynab: “Je, Zakaat inawatosheleza wao wawili kwa waume zao na kwa mayatima walio chini ya ulezi wao?” Akasema (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((نعم، ولها أجران: أجر القرابة، وأجر الصدقة))
((Na’am, na yeye ana ajri mbili: ajri ya ukaraba, na ajri ya Zakaat)). [Al-Bukhaariy (1466) na Muslim (998)]
Na Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwambia Abu Twalha alipomjia na swadaqah yake:
((وإني أرى أن تجعلها في الأقربين...))
((..na hakika mimi naona uitoe kwa akraba zako…..)). [Al-Bukhaariy (1461) na Muslim (998)]
Je, inajuzu kupewa Zakaah mtu faasiq, mtu wa bid-’a, au mtu atakayeitumia kufanyia maasia?
Picha ya wenye kunasibishwa na Uislamu –na ambao wanaweza kuwa ni wenye kustahiki Zakaah -haikosi hali tatu:
1- Waislamu watiifu wenye kusimamisha shariy’ah. Hawa hupewa Zakaah -ikiwa wanastahiki- bila makhitilafiano yoyote kati ya ‘Ulamaa.
2- Waislamu wa bid’a za kuwakufurisha. Hawa watazuiliwa Zakaah bila makhitilafiano yoyote kati ya ‘Ulamaa. Kwa kuwa kwa bid’a zao hizi, wanakuwa wametoka nje ya Diyn, na makafiri hawapewi Zakaah kwa Ijma’a ya ‘Ulamaa.
3- Waislamu wa bid’a na maasia. Hawa, ikiwa dhana ya mtoaji itatopea kuwa wataitumia katika maasia, basi haijuzu kuwapa Zakaah. Hii ni kauli ya Ash-Shaafi’iy na Hanbal.
Hili kaligusia Sheikh wa Uislamu katika Kitabu cha Al-Fataawaa (25/87) akisema:
“Inatakikana mtu awahakiki wastahiki wa Zakaah yake miongoni mwa mafakiri, masikini, wenye madeni na wengineo kati ya Waislamu wenye kufuata shariy’ah. Na mwenye kudhihirisha bid-’a au fujuwr (ufasiki wa kupinga haki), basi huyo anastahiki adhabu ya kutengwa na jamii au nyingineyo na kutubishwa. Basi vipi asaidiwe kwa hilo? Aidha, haijuzu kupewa Zakaah mtu ambaye haimsaidii katika kumtii Allaah, kwani Allaah Ameifaradhisha ili iwe msaada wa kumtii Yeye. Asiyeswali hapewi mpaka atubie na awajibike kutekeleza Swalaah. Na atakayekuwa katika hawa ni mnafiki, au anadhihirisha bid-’a inayokhalifiana na Qur-aan na Sunnah katika bid-’a za masuala ya kiitikadi na ki’ibaadah, basi huyo anastahiki adhabu. Na kati ya adhabu hizo ni kunyimwa Zakaah mpaka atubie”.
Ama ikiwa hawaitumii mali ya Zakaah katika kumwasi Allaah, Sheikh wa Uislamu anaona pia kuwa wasipewe. Lakini wengine wanaona kuwa watapewa kwa kuwa wanaingia kwenye ujumuishi wa Aayah ya kundi la wanaopewa Zakaah ambayo haikubagua kati ya mtendaji maasia au mtiifu wa maamrisho.
Alaa kulli haal, lililo bora ni kutangulizwa watu walioshika Diyn na waliolingamana sawa katika itikadi na utendaji kabla ya wengine wakati wa kugawa Zakaah. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Ninasema: Kati ya yaliyosimuliwa katika mlango huu:
1- Toka kwa Qaz’ah amesema: ((Nilimwambia Ibn ‘Umar: Mimi nina mali, nani nimpe Zakaah yake? Akasema: Itoe kwa watu hawa –yaani Maamiyr- Nikasema: Basi watanunulia kwayo nguo na manukato. Akasema: Hata wakinunulia kwayo nguo na manukato, lakini katika mali yako kuna haki (nyingine) zaidi ya Zakaah)). [Al-Amwaal cha Abu ‘Ubayd (1798) kwa Sanad Swahiyh na mfanowe Ibn Abiy Shaybah (4/28)]
2- Toka kwa Suhayl bin Abiy Swaaleh toka kwa baba yake amesema: ((Nilimwendea Sa’ad bin Abiy Waqqaasw nikamwambia: Nina mali nataka kuitolea Zakaah yake, na watu hawa hali yao kama unavyoiona. Akasema: Wape hiyo Zakaah. Nikawaendea Ibn ‘Umar, Abu Hurayrah na Abu Sa’iyd, nao wakasema hivyo hivyo)). [Al-Amwaal (1789) na Al-Bayhaqiy (4/115) kwa Sanad Swahiyh.
Linaloonekana kutokana na konteksi ya athar hizi ni kuwa muradi wa watu –ambao hupewa Zakaah pamoja na maasia yao- ni Maamiri na viongozi ambao ni lazima kuwatii. Hivyo hakuna ukinzani katika yale tuliyoyatilia nguvu katika madhehebu ya Sheikh wa Uislamu. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Je, Baniy Haashim wanapewa Zakaah?
Baniy Haashim kwa kauli yenye nguvu, ni ukoo wa ‘Aliyy, ukoo wa ‘Aqiyl, ukoo wa Ja-’afar, ukoo wa ‘Abbaas, ukoo wa Al-Haarith na pia ukoo wa Al-Muttwalib. [Ni kwa neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) -kama ilivyo kwa Al-Bukhaariy (3/40) na wengineo-:
((إنا وبني المطلب لا نفنرق في جاهلية ولا إسلام، وإنما نحن وهم شيء واحد)) وشبك بين أصابعه
((Hakika sisi na Baniy Al-Muttwalib, hatutengani katika ujahilia wala katika Uislamu, bali hakika sisi na wao ni kitu kimoja)). Akapachanisha kati ya vidole vyake]
Hawa, si halali kwao kuchukua Zakaah ya faradhi bila makhitilafiano yoyote kati ya ‘Ulamaa kutokana na neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((إن الصدقة لا تنبغي لآل محمد، وإنما هي أوساخ الناس))
((Hakika Zakaah haifai kwa ukoo wa Muhammad. Hakika si jinginelo, Zakaah ni takataka za watu)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1072) na An-Nasaaiy (1609)]
Maana ya (takataka za watu) ni kuwa Zakaah ni utwaharisho wa mali zao na nafsi zao. Zakaah ni mashine ya kusugua na kuondosha uchafu. Na kwa neno lake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((إنا لا تحل لنا الصدقة))
((Hakika sisi si halali kwetu swadaqah [Zakaah])). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Muslim (1069) na Abu Daawuwd (1650)]
Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimwambia Al-Hasan bin ‘Aliyy alipochukua tende moja kati ya tende za swadaqah:
((كخ كخ (ليطرحها) أما شعرت أنا لا نأكل الصدقة))
((Wacha hii, wacha hii! (tema): Je hujui kuwa sisi hatuli swadaqah [Zakaah])). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1491) na Muslim (1069)]
Sheikh wa Uislamu amekhitari kuwa inajuzu kwa Baniy Haashim kuchukua Zakaah ya Mahaashim na si Zakaah ya watu wengineo. Haya yamesimuliwa toka kwa Abu Haniyfah na Abu Yuwsuf. [Fat-hul Qadiyr cha Ibn Al-Hamaam (2/272). Angalia Al-Jaami’u Lil-Ikhtibaaraat Al-Fiqhiyyah cha Ibn Taymiyyah. Dk. Ahmad Muwaafiy (1/400)]
Kupelekwa Zakaah Mji Mwingine
Asli ya mambo ni kuwa, Zakaah huchukuliwa toka kwa matajiri wa mji na kurejeshwa kwa mafakiri wao, haihamishwi ikapelekwa mji mwingine. Ni kwa neno lake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) katika Hadiyth ya Mu’aadh:
((أخبرهم أن الله قد فرض عليهم صدقة تؤخذ من أغنيائهم وترد إلى فقرائهم))
((Waeleze kuwa Allaah Amewafaradhia Zakaah, huchukuliwa toka kwa matajiri wao na kurejeshwa kwa mafukara wao)). [Imeripotiwa na Al-Bukhaariy na Muslim]
Lakini kama wakazi wa mji wa mtoaji Zakaah si wahitaji wa Zakaah, au watu wa eneo jingine wakawa wanaihitajia zaidi, au wakawa ni akraba wa mtoaji Zakaah wenye kustahiki Zakaah, au mengineyo kati ya manufaiko yenye uzito, basi hakuna ubaya kuihamisha Zakaah na kuipeleka mji mwingine. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Swahiyh Fiqh As-Sunnah
Mlango Wa Zakaah
23-Zakaatul Fitwr
Alhidaaya.com [3]
Zakaatul Fitwr kiistilahi, ni Zakaah inayolazimu (kutolewa) kwa kumalizika Ramadhwaan.
Hikma Ya Kufaradhishwa Zakaatul Fitwr
Ni kuwafariji mafukara kwa kuwatosheleza wasiombe katika siku ya ‘Iyd, kuwapa furaha katika siku hii ambayo Waislamu hufurahi kwa kuingia ‘Iyd, na kumtakasa aliyewajibikiwa kuitoa baada ya Mwezi wa Swawm kutokana na upuuzi na “rafath” (matamanio ya jimai, mazungumzo yake, vitangulizi vyake na jimai yenyewe). [Al-Mughniy (3/56)]
Imepokelewa toka kwa Ibn ‘Abbaas akisema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amefaradhisha Zakaatul Fitwr, kwa ajili ya kumtakasa mfungaji kutokana na upuuzi na “rafath” (matamanio ya jimai, mazungumzo yake, vitangulizi vyake na jimai yenyewe), na kuwalisha masikini. Na atakayeitoa kabla ya Swalaah, basi hiyo ni Zakaah yenye kukubaliwa, lakini atakayeitoa baada ya Swalaah, basi hiyo ni swadaqah kati ya swadaqah nyinginezo)). [Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (1609), Ibn Maajah (1827) na wengineo kwa Sanad Hasan]
Hukmu Yake
Zakaatul Fitwr ni waajib kwa kila Muislamu kutokana na Hadiyth ya Ibn ‘Umar (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) aliyesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amefaradhisha Zakaatul Fitwr pishi ya tende, au pishi ya shayiri, kwa mtumwa na muungwana, mwanamume au mwanamke, na mdogo na mkubwa katika Waislamu. Ameamuru itolewe kabla ya watu kutoka kwenda kuswali)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1503), Muslim (984) na wengineo]
Sa’iyd bin Al-Musayyib na ‘Umar bin ‘Abdul ‘Azizy wamesema kuhusu Kauli Yake Ta’aalaa:
قَدْ أَفْلَحَ مَن تَزَكَّىٰ
((Hakika amefaulu ambaye amejitakasa)),
kwamba makusudio ni Zakaatul Fitwr.
Ibn Al-Mundhir kasema: “Wote tunaowajua vyema katika ‘Ulamaa wamesema kwa sauti moja kuwa Zakaatul Fitwr ni fardhi”. [Al-Ijma’a cha Ibn Al-Mundhir (uk.9)]
Ni waajib kwa nani?
Zakaatul Fitwr ni waajib kwa mwenye masharti yafuatayo:
[1] Awe Muislamu
Kwa kuwa Zakaatul Fitwr ni ‘amali katika ‘amali za kujikurubisha mtu kwa Allaah, na ni kitwaharisho kwa mfungaji kutokana na “rafath” na upuuzi –kama ilivyotangulia- na kafiri hahusiki na haya bali ataadhibiwa Aakhirah kwa kuacha kutoa. Na kwa ajili hiyo, amesema katika Hadiyth iliyotangulia ya Ibn ‘Umar “katika Waislamu”. Uislamu ni sharti kwa Jumhuri ya ‘Ulamaa kinyume na Mashaafi’iy ambao la sahihi kwao ni kuwa ni lazima kwa kafiri aitoe kuwapa jamaa zake Waislamu. [Ad-Durru Al-Mukhtaar (2/72) na Mughnil Muhtaaj (1/402)]
[2] Awe na uwezo wa kuitoa
Mpaka wa uwezo huu ni mtu kuwa na ziada katika mlo wake na mlo wa anaowakimu kimaisha usiku wa ‘Iyd na mchana wake kwa mujibu wa Jumhuri ya ‘Ulamaa (Maalik, Ash-Shaafi’iy na Hanbali). [Mughnil Muhtaaj (1/403, 628) na Al-Mughniy (3/76)]
Hii ni kwa vile mtu ambaye hali yake iko hivi, anakuwa ni mwenye kujitosheleza, kwani Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii amesema:
((من سأل وعنده ما يغنيه فإنما بستكثر من النار)) فقالوا يا رسول الله، وما يغنيه؟ قال: ((أن يكون له شبع يوم وليلة))
((Mwenye kuomba naye ana [chakula] cha kumtosha, basi hakika anajikusanyia moto)). Wakasema: Ee Rasuli wa Allaah! Ni kipi kinamtosha?Akasema: Awe na mlo wa kumshibisha mchana na usiku)). [Hadiyth Hasan. Imekharijiwa na Abu Daawuwd (1629) kwa Sanad Hasan]
Abu Haniyfah na wenzake wamelikhalifu hili wakisema kuwa Zakaah haipasi isipokuwa kwa yule anayemiliki kiwango cha dhahabu na fedha (silver) au thamani yake mbali na nyumba yake. [Sharhu Fat-hil Qadiyr (2/218) na Haashiyatu Ibn ‘Aabidiyna (2/360)]
Wametoa dalili kwa kauli yake Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam):
((لا صدقة إلا عن ظهر غنى))
((Hakuna swadaqah [iliyo kamili] isipokuwa inayotokana na mtu kuwa amejitosheleza)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1426)]
Wamesema: Fakiri hana cha kujitosheleza, hivyo si waajib kwake, na kwa kuwa Zakaah ni halali yeye kupewa, inakuwa si waajib kwake kutoa kama asiye na uwezo wa kuitoa.
Ninasema:
Rai ya Jumhuri ina uzito zaidi kwa mambo haya:
1- Kufaradhishwa Zakaatul Fitwr kumekuja kwa wote bila uainisho; kwa mdogo, mkubwa, mwanamume, mwanamke, muungwana na mtumwa. Haikufunganishwa na utajiri au umasikini kama ilivyofunganishwa Zakaatul Maal kwa neno lake Rasuli: ((Huchukuliwa toka kwa matajiri wao ikarejeshwa kwa mafukara wao)).
2- Zakaatul Fitwr haiongezeki kutokana na wingi wa mali ya mtu, hivyo uwajibu wa kiwango haupo ndani yake kama kafara.
3- Wao kutoa dalili kwa Hadiyth: ((Hakuna swadaqah [iliyo kamili] isipokuwa inayotokana na mtu kuwa amejitosheleza)) hakukubaliwi, na sisi tunasema pamoja nao: Asiyeweza kuitoa hawajibikiwi, bali tumeleta Hadiyth inayosema kuwa mwanadamu kinamtosheleza chakula cha kumshibisha mchana wake na usiku wake.
Faida
Zakaatul Fitwr ni waajib kwa kila Muislamu mwenye uwezo wa kuitoa hata kama ni mtumwa anayemilikiwa –kama walivyosema Mahanbali- kinyume na Jumhuri ya Fuqahaa. Fuqahaa hawa wameshurutisha mtu awe muungwana ili awajibikiwe na Zakaah. Wamesema kuwa si waajib kwa mtumwa, kwa kuwa mtumwa hamiliki kitu.
Lililo sahihi ni kuwa ni waajib kwa Muislamu anayemiliki mtumwa amtolee Zakaatul Fitwr mtumwa wake kwa Hadiyth ya Ibn ‘Umar aliyesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amefaradhisha Zakaatul Fitwr pishi ya tende au pishi ya shayiri kwa kila mtumwa na muungwana, mdogo au mkubwa)). [Hadiyth Swahiyh. Imeshatajwa nyuma]
Kwa Muhtasari
Zakaatul Fitwr ni waajib kwa kila Muislamu aliye huru –anayemiliki chakula chake na chakula cha watoto wake mchana au usiku- ajitolee yeye mwenyewe na wale anaowakimu kimaisha kama mke wake, watoto wake na watumishi wake walio Waislamu. Imepokelewa toka kwa Ibn ‘Umar amesema: ((Rasuli wa Allaah Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam ameamuru Zakaatul Fitwr kwa mdogo na mkubwa, muungwana na mtumwa katika mnaowalisha)). [Hadiyth Hasan Lighayrih. Imekharijiwa na Ad-Daaraqutwniy (220), na kwa njia yake Al-Bayhaqiy (4/161). Angalia Al-Irwaa (835)]
Ibn Hazm anaona kuwa Zakaatul Fitwr haimlazimu mtu kumtolea mwingine, si baba yake wala mama yake, wala mke wake, wala yeyote kati ya anaowalisha isipokuwa ajitolee yeye mwenyewe. Na hawa (wanaolishwa) ni waajib kila mmoja wao ajitolee mwenyewe kwa pesa zake kwa mujibu wa Hadiyth ya Ibn ‘Umar iliyokubaliwa na wote.
Fawaaid
1- Si lazima mtu kumtolea Zakaatul Fitwr mkewe ambaye bado hajamwingilia kwa kuwa bado hajawajibikiwa kumlisha.
2- Ikiwa mke atamwasi mumewe katika wakati wa kutoa Zakaatul Fitwr, basi mke atajitolea Zakaah mwenyewe, na si mume.
3- Ikiwa mke ni Ahlul Kitaab (Myahudi au Mnaswara), basi hatolewi Zakaatul Fitwr.
Aina za vyakula vinavyotolewa katika Zakaatul Fitwr
Zakaatul Fitwr hutolewa kwa vyakula vinavyoliwa na Waislamu, si tu vile vilivyotajwa kwenye Hadiyth (shayiri, tende na zabibu), bali hutolewa mchele, mahindi, na mfano wake katika mazao yanayotumika kama vyakula.
Hii ni kauli swahiyh zaidi ya ‘Ulamaa, nayo ni madhehebu ya Ash-Shaafi’iy na Maalik. [Lakini wao wameshurutisha vyakula viwe katika mazao yanayotolewa 10% (moja ya kumi) ya Zakaah]
Na Sheikh wa Uislamu ameikhitari. Ama Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) kufaradhisha pishi ya tende au pishi ya shayiri, ni kuwa hivi ndivyo vilivyokuwa vyakula vikuu vya watu wa Madiynah. Na kama hivi visingekuwa vyakula vyao bali wanakula vingine, basi asingeliwakalifisha watoe wasichokila. Kama ambavyo hakuamuru hilo katika malipo ya kafara. Allaah Ta’aalaa Amesema kuhusu kafara:
مِنْ أَوْسَطِ مَا تُطْعِمُونَ أَهْلِيكُمْ
((chakula cha wastani mnachowalisha ahli zenu)). [Al-Maaidah (5:89)]
Na Zakaatul Fitwr ni kundi moja na malipo ya kafara, zote mbili zina mahusiano na kiwiliwili kinyume na Zakaatul Maal. Zakaatul Maal ni lazima kwa sababu ya mali itokanayo na aina ile ile ambayo Allaah Amemruzuku mtu. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/69)]
Ama Mahanbali, wao wamesema kuwa haitoshelezi isipokuwa tende, shayiri na burri.
Ni kiasi gani cha uwajibu anachotolewa kila mtu katika Zakaatul Fitwr?
‘Ulamaa wako katika madhehebu mawili kuhusiana na kiasi cha uwajibu anachotolewa kila mtu. [Al-Mudawwanah (1/358), Al-Majmuw’u (6/48), Al-Mughniy (3/81) na Sharhu Fat-hil Qadiyr (2/225)]
La kwanza: Wajibu ni pishi ya aina yoyote (ya chakula)
Hii ni kauli ya Jumhuri –kinyume na Abu Haniyfah na Maswahibu wake- na dalili zao ni:
1- Hadiyth ya Abu Sa’iyd Al-Khudriy aliyesema: ((Tulikuwa tunatoa Zakaatul Fitwr wakati Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) yuko pamoja nasi, pishi ya chakula, au pishi ya shayiri, au pishi ya tende, au pishi ya zabibu kavu au pishi ya samli kavu ya maziwa. Na hatukuacha kuitoa (hivyo) mpaka alipokuja Mu’aawiyah Madiynah, akazungumza. Na kati ya aliyoyazungumzia kwa watu ni: Hakika mimi naona kwa uyakini vibaba viwili vya ngano ya Sham ni sawa na pishi ya tende, na watu wakalifuata hilo. [Abu Sa’iyd akasema]: Ama mimi, bado naendelea kuitoa kama nilivyokuwa naitoa)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1505), Muslim (985), Abu Daawuwd (1616) na At-Tirmidhiy na An-Nasaaiy]
2- Hadiyth ya Ibn ‘Umar: ((Kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alifaradhisha Zakaatul Fitwr pishi ya tende, na pishi ya shayiri, na watu wakageuza na kutoa nusu pishi ya burri)). (Kutokana na ubora wa ngano ya Sham kulinganisha na ya Hijaaz). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1511) na Muslim (984)]
La pili: Wajibu ni pishi isipokuwa katika burri ambayo inatosha nusu pishi
Haya ni madhehebu ya Abu Haniyfah na Maswahibu wake. Zabibu kavu ni kama burri kwa Abu Haniyfah katika riwaayah. Na dalili zao ni:
1- Yaliyosimuliwa toka kwa Tha’alabah toka kwa Abiy Swu’ayr toka kwa baba yake toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) aliyesema:
((صاع من بر أو قمح على كل اثنين))
((Pishi ya burri au ngano kwa kila wawili)). [Hadiyth Dhwa’iyf. Abu Daawuwd (1619) kwa Sanad Swahiyh]
2- Toka kwa ‘Amri bin Shu’ayb toka kwa baba yake toka kwa babu yake kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) alimtuma mpiga mbiu kwenye barabara za Makkah atangaze:
((ألا إن صدقة الفطر واجبة على كل مسلم ذكر أو أنثى أو عبد، صغير أو كبير، مدان من قمح، أو سواهما صاع من طعام))
((Jueni kuwa Zakaatul Fitwr ni waajib kwa kila Muislamu; mwanaume au mwanamke, au mtumwa, mdogo au mkubwa, vibaba viwili vya ngano, au kama si vibaba viwili [vya ngano] pishi ya chakula)). [Hadiyth Dhwa’iyf. At-Tirmidhiy (669) kwa Sanad Layyin. Kuna makhitalifiano, angalia Tuhfat Al-Ahwadhiy (3/348)]
Al-Haafidh katika Al-Fat-h (3/437) amesema: “Ibnul Mundhir amesema: Hatujui habari yakini ya kutegemewa kuhusiana na ngano toka kwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam), na burri haikuwepo Madiynah wakati huo isipokuwa kiasi kidogo tu. Na ilipokuwa nyingi enzi ya Swahaba, waliona kuwa nusu pishi ya burri ni sawa na pishi moja ya shayiri, nao ndio Maimamu. Hivyo basi haijuzu kuiacha kauli yao ila tu kama mtu ataiacha na kuifuata kauli ya wengine mfano wao. Kisha imepokewa kwa Sanad Swahiyh toka kwa ‘Uthmaan, ‘Aliy, Abu Hurayrah, Jaabir, Ibn ‘Abbaas, Ibn Az Zubayr, na mama yake Asmaa bint Abiy Bakr kwamba wao wanaona ni nusu pishi ya ngano katika Zakaatul Fitwr….mpaka mwisho wa maneno”. [Maneno ya Ibn Al-Mundhir] Hatima hii imemfanya akhitari mwelekeo wa Hanafiy. Lakini Hadiyth ya Abu Sa’iyd Al-Khudriy inaonyesha kuwa yeye hakukubaliana na hilo, na pia Ibn ‘Umar, hivyo hakuna Ijma’a katika suala hili …. (nukuu toka Kitabu cha Al-Fat-h)
Faida
Pishi moja ni sawa na vibaba vinne, na vibaba vinne ni sawa na 1/6 ya “Kaylah” (chombo cha kupimia nafaka) ya Misri ya Kale ambayo ni sawa na kilo 2.157 (kwa mizani takriban).
Ni wakati gani Zakaatul Fitwr hutolewa?
Ni lazima Zakaatul Fitwr itolewe kabla ya Swalaatul ‘Iyd. Ni haramu kuichelewesha mpaka baada ya Swalaah. Imepokelewa toka kwa Ibn ‘Umar akisema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) ameamuru Zakaatul Fitwr itolewe kabla hawajatoka watu kwenda katika Swalaah)). [Hadiyth Swahiyh. Al-Bukhaariy (1509) na Muslim (986) na wengineo]
Toka kwa Ibn ‘Abbaas amesema: ((Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihii wa sallam) amefaradhisha Zakaatul Fitwr, kwa ajili ya kumtakasa mfungaji kutokana na upuuzi na “rafath” (matamanio ya jimai, mazungumzo yake, vitangulizi vyake na jimai yenyewe), na kuwalisha masikini. Na atakayeitoa kabla ya Swalaah, basi hiyo ni Zakaah yenye kukubaliwa, na atakayeitoa baada ya Swalaah, basi hiyo ni swadaqah kati ya swadaqah nyinginezo)). [Takhriyj yake imetajwa nyuma kidogo]
Ama mwanzo wa wakati wa uwajibu kwa mujibu wa ‘Ulamaa wa Kishaafi’iy, Kihanbal na Kimaalik, ni pale jua linapokuchwa siku ya mwisho ya Ramadhwaan. Ama kwa Mahanafiy na kauli ya Maalik, ni pale inapochomoza alfajiri ya siku ya ‘Iyd. [Al-Mawsuw’atu Al-Fiqhiyyah (23/340)]
Na faida ya makhitilafiano haya kuhusu mwanzo wa wakati wa uwajibu, inapatikana kwa mtu aliyekufa baada ya kuchwa jua siku ya mwisho ya Ramadhwaan. Kwa msingi wa kauli ya kwanza, atatolewa Zakaatul Fitwr kwa kuwa alikuwa hai wakati wa uwajibu, lakini kwa msingi wa kauli ya pili, hatotolewa.
Kadhalika, mtoto aliyezaliwa baada ya kuchwa jua siku ya mwisho ya Ramadhwaan. Kwa kauli ya kwanza hatotolewa Zakaah, na kwa ya pili atatolewa.
Je, inajuzu kutoa Zakaatul Fitwr kabla ya wakati wa Uwajibu?
Inajuzu kutoa Zakaatul Fitwr mapema kabla ya wakati wake kwa siku moja au siku mbili.
Toka kwa Naafi’u amesema: ((Ibn ‘Umar alikuwa anawapa wale wanaoikubali, na walikuwa wanaitoa kabla ya kuisha mfungo kwa siku moja au kwa siku mbili)). [Hadiyth Swahiyh. Imekharijiwa na Al-Bukhaariy (1511) na Muslim (986)]
Je, Zakaatul Fitwr husameheka kwa kutoka wakati wake?
‘Ulamaa wote wamekubaliana kuwa Zakaatul Fitwr haisameheki kama wakati wake utatoka, kwa kuwa ni dhima inayomganda mtu kwa watu wanaostahiki kupewa. Ni deni wanalolidai wastahiki hao, halisameheki ila kwa kuwalipa, na deni hilo ni haki ya watu. Ama Haki ya Allaah katika kuichelewesha ukatoka wakati wake, hii haiondoki isipokuwa kwa kuomba maghfirah na kujuta. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Je, inatosha kutoa pesa katika Zakaatul Fitwr badala ya chakula?
Tushazungumza nyuma kuhusu hukmu ya kutoa pesa katika Zakaah mbalimbali kiujumla. Tumesema asli, ni kuitoa kwa namna ilivyobainishwa na Hadiyth, na mtu asitoke nje ya Hadiyth akatoa pesa isipokuwa kwa dharura, au haja, au maslaha nyeti muhimu, hapo itatosheleza kutoa pesa. Allaah Ndiye Mjuzi Zaidi.
Wanaopewa Zakaatul Fitwr
‘Ulamaa wamekhitalifiana katika kauli mbili kuhusu watu wa kupewa Zakaatul Fitwr:
Ya kwanza: Wanaopewa ni watu wanane (waliotajwa kwenye Aayah)
Ni madhehebu ya Jumhuri ya ‘Ulamaa kinyume na Maalik. [Ad-Durru Al-Mukhtaar (2/369) na Al-Majmuw’u (6/144)]
Ya pili: Wanapewa wahitaji (mafukara na masikini tu)
Ni madhehebu ya Maalik, na yamekhitariwa na Sheikh wa Uislamu. [Majmuw’u Al-Fataawaa (25/73)].
Ni kauli yenye nguvu zaidi kwa kunasibiana kwake na ufaradhisho wa Zakaatul Fitwr, kwa kuwa kwake ni (lishe kwa masikini). [Hadiyth Hasan. Takhriyj yake imeelezwa nyuma]
Na kwa kuwa pia Zakaatul Fitwr inafanana na kafara, hivyo haijuzu kumlisha isipokuwa yule anayestahiki kafara.
Links
[1] https://www.alhidaaya.com/sw/taxonomy/term/284
[2] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10434&title=04-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20%D9%83%D9%90%D8%AA%D9%8E%D8%A7%D8%A8%D9%8F%20%D8%A7%D9%8E%D9%84%D8%B2%D9%91%D9%8E%D9%83%D9%8E%D8%A7%D8%A9%20-%20Kitabu%20Cha%20Zakaah%20
[3] http://www.alhidaaya.com
[4] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10439&title=01-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Taarifu%20Ya%20Zakaah
[5] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10440&title=02-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Hukmu%20Ya%20Zakaah%20Na%20Hadhi%20Yake
[6] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10441&title=03-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Fadhila%20Na%20Faida%20Za%20Kutoa%20Zakaah
[7] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10442&title=04-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Hukmu%20Ya%20Kuzuia%20Zakaah%20Na%20Adhabu%20Kwa%20Asiyetoa
[8] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10443&title=05-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Shuruti%20Za%20Uwajibu%20Wa%20Kutoa%20Zakaah
[9] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10554&title=06-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaa%20Ya%20Madeni
[10] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10555&title=07-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Aina%20Za%20Mali%20Ambazo%20Ni%20Waajib%20Kuzitolea%20Zakaah
[11] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10556&title=08-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Dhahabu%20Na%20Fedha%20%28Silver%29
[12] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10557&title=09-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Katika%20Pesa%20Za%20Noti%20%28Bank%20Note%29
[13] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10558&title=10-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Kiwango%20Cha%20Zakaah%20Ya%20%20Noti%20%28Bank%20Note%29
[14] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10559&title=11-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Mapambo
[15] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10560&title=12-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Mishahara%20Na%20Chumo%20La%20Kazi
[16] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10561&title=13-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Mahari
[17] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10562&title=14-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaa%20Ya%20Mifugo
[18] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10563&title=15-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Ngamia
[19] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10564&title=16-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Ghanam%20%28Mbuzi%20Na%20Kondoo%29
[20] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10565&title=17-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Ng%E2%80%99ombe
[21] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10566&title=18-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Mazao%20Na%20Matunda
[22] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10567&title=19-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaah%20Ya%20Mali%20na%20Bidhaa%20Za%20Biashara
[23] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10568&title=20-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20%20Zakaah%20Ya%20Rikaaz%20Na%20Madini
[24] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10569&title=21-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Hukmu%20Kiujumla%20Katika%20Zakaah%20
[25] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10570&title=22-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Maswaarif%20Za%20Zakaah%20%28Wastahiki%20Wa%20Kupewa%20Zakaah%29
[26] https://www.addtoany.com/share#url=https%3A%2F%2Fwww.alhidaaya.com%2Fsw%2Fnode%2F10571&title=23-Swahiyh%20Fiqh%20As-Sunnah%3A%20Mlango%20Wa%20Zakaah%3A%20Zakaatul%20Fitwr%3A