007-Lu-ulu-un-Manthuwrun: Kumwamini Allaah Na Kuwa Na Istiqaamah

 

 

 

(Mkusanyiko Wa Hadiyth Mbali Mbali Na Mafunzo Yake)

 

Hadiyth Ya 7  

Kumwamini Allaah Na Kuwa Na Istiqaamah

 

www.alhidaaya.com

 

عَنْ أبي عَمْرَةَ سُفْيَانَ بْنِ عَبْدِ اللَّهِ (رضي الله عنه)  قَالَ: قُلْتُ يَا رَسُولَ اللَّهِ قُلْ لِي فِي الإسْلاَمِ قَوْلاً لاَ أَسْأَلُ عَنْهُ أَحَدًا غَيْرَكَ)) قَالَ:  ((قُلْ آمَنْتُ بِاللَّهِ  ثُمَّ َاسْتَقِمْ)) رواه مسلم

Imepokelewa kutoka kwa Abu ‘Amrah Sufyaan bin ‘Abdillaah (رضي الله عنه) amesema: Nilisema: “Ee Rasuli wa Allaah! Niambie neno katika Uislamu ambalo sitomuuliza yeyote badala yako”. Akasema: ((Sema: Nimemwamini Allaah kisha uwe na istiqaamah [msimamo])) [Muslim]

 

Mafunzo Na Mwongozo:

 

 

1. Hadiyth hii ni miongoni mwa ‘Jawaami’ul-Kalim’ (Mjumuisho wa maana nyingi katika maneno machache) aliyopewa Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم). Na thawabu za Istiqaamah (kuthibitika, msimamo katika Dini) zimetajwa katika kauli za Allaah (سبحانه وتعالى):

 

 

إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّـهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا تَتَنَزَّلُ عَلَيْهِمُ الْمَلَائِكَةُ أَلَّا تَخَافُوا وَلَا تَحْزَنُوا وَأَبْشِرُوا بِالْجَنَّةِ الَّتِي كُنتُمْ تُوعَدُونَ﴿٣٠﴾

Hakika wale waliosema: “Rabb wetu ni Allaah.” Kisha wakathibitika imara; Malaika huwateremkia: (kuwaambia): “Msikhofu, na wala msihuzunike, na pokeeni bishara njema ya Jannah ambayo mlikuwa mkiahidiwa.”

 

نَحْنُ أَوْلِيَاؤُكُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَفِي الْآخِرَةِ ۖ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَشْتَهِي أَنفُسُكُمْ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَدَّعُونَ﴿٣١﴾

 “Sisi ni rafiki zenu walinzi katika uhai wa dunia na katika Aakhirah. Na mtapata humo yale yanayotamani nafsi zenu, na mtapata humo yale mtakayoomba.

 

نُزُلًا مِّنْ غَفُورٍ رَّحِيمٍ﴿٣٢﴾

 “Ni mapokezi ya takrima kutoka kwa Mwenye kughufuria, Mwenye kurehemu.”[Fusw-swilat 41: 30-32].

 

Na pia: 

 

إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّـهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا فَلَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ﴿١٣﴾

Hakika wale waliosema: “Rabb wetu ni Allaah.” Kisha wakathibitika imara, basi hakutokuwa na khofu juu yao, na wala hawatohuzunika.

أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ خَالِدِينَ فِيهَا جَزَاءً بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ﴿١٤﴾

Hao ndio watu wa Jannah, ni wenye kudumu humo, jazaa kwa yale waliyokuwa wakitenda.  [Al-Ahqaaf 46: 13-14]

 

2. Umuhimu wa tawhiyd, kumpwekesha Allaah bila ya kumshirikisha.

 

Rejea: Al-An’aam (6: 102), Al-Baqarah (2: 163), Twaahaa (20: 14), Al-Qaswas (28: 88), Ghaafir (40: 65-66).

 

 

Na Hadiyth:

 

عَنْ عبد الله بن مسعود رضي الله عنه قال: لَمَّا نَزَلَتْ هَذِهِ الآيَةُ: الَّذِينَ آمَنُوا وَلَمْ يَلْبِسُوا إِيمَانَهُمْ بِظُلْمٍ، شَقَّ ذَلِكَ عَلَى النَّاس وَقَالُوا: أَيُّنَا لَمْ يَظْلِمْ نَفْسَهُ؟! فَقَالَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ: ((إنَّه لَيْسَ كَمَا تَعنُون! ألَمْ تَسْمَعوا ما قال الْعبْد الصَّالح؟  يَا بُنَيَّ لا تُشْرِكْ بِاللَّهِ إِنَّ الشِّرْكَ لَظُلْمٌ عَظِيمٌ - إنَّما هُو الشِّرْك))

Imepokelewa kutoka kwa ‘Abdullaah bin Mas‘uwd (رضي الله عنه)    ambaye amesema: Ilipoteremshwa Aayah hii: Wale walioamini na hawakuchanganya iymaan zao na dhulma [An-An’aam: 82] Iliwatatiza watu  wakasema: “Nani katika sisi hajadhulumu nafsi yake?” Akasema Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم)  ((Si kama vile mnavyomaanisha! Hamsikii pale mja mwema aliposema: “Ee mwanangu! Usimshirikishe Allaah, hakika shirki ni dhulma kuu!” [Luqmaan: 13] Hakika hiyo ni shirk.)) [Ahmad na riwaaya zinazofanana katika Al-Bukhaariy na wengineo]

 

Pia rejea Hadiyth namba (11), (12), (48), (125).

 

3. Kuwa na msimamo kunapeleka kufikia cheo cha juu na ukamilifu wa Iymaan.

 

Amesema ‘Umar bin al-Khattwaab (رضي الله عنه): “Istiqaamah ni kutekeleza amri na kuacha yaliyokatazwa, wala msimili na kugeuka geuka mgeuko wa fisi.”

 

 

4. Hii inaashiria kuwa Istiqaamah ina fadhila kubwa mpaka imekuja baada tu ya Iymaan. Na bila shaka Iymaan yenyewe haiwezi kusimama bila ya Istiqaamah.

 

Share