Ametubia Baada Ya Kuzini Na Mwanamke Je Kumsaidia Na Mzazi Wake Atakuwa Anaharibu Toba Yake?

 SWALI

 

Asalam allaykum,

Ama baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu mtukufu na kumuombea mema mtume wetu Muhammad salallah allaih wasalam, naomba taaluma juu ya swala hili lifuatalo 

Imetokea mtu alikuwa na uhusiano wa kimapenzi (kuzini) na mwanamke ambaye sio muislam.  Mwanamme akaamua kuishi nchi nyengine tafauti ambayo anaishi mwanamke. Mwanamme alishatubu wala hana nia tena ya kurudia uovu huu. Siku kadhaa zimepita, mwanamme amesikia hali ya yule mwanamke na mzee wake sio nzuri kiuchumi (umaskini). Katika hali, je mwanamme atapata dhambi au ataharibu toba yake iwapo ataamua kumsaidia huyu mwanamke na mzee wake kiuchumi (kifedha), lakini sio kwa nia ya kimapenzi ila ni kwa huruma ya umasikini wao.


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako zuri kuhusu kumsaidia aliyezini naye.

Tunamtakia kila la kheri mtu huyo aliyetubia baada ya kuzini na tunamuombea kwa Allaah Aliyetukuka asirudie tena tendo hilo ovu.

 

Msaada unatakikana kwa Muislamu yeyote yule mwenye kuhitajia. Na ikiwa wako Waislamu wenye kuhitajia ni muhimu sana kuwasaidia.

Ama ikiwa huyo mtu anataka kumsaidia huyo mwanamke aliyezini naye

Pamoja na mama yake kwa sababu ya ule uhusiano wao na kujuana kwao, hiyo inaweza kupelekea kuendelea kuunganisha mahusano yao na kuzidi kuwaweka karibu na ukaribu huo ukapelekea wao kwa njia moja au nyingine kurudi au kukaribia maharamisho na makatazo ambayo Shari'ah haiwataki wao kuwa nayo. Kadhalika hali hiyo ya kusaidiana inaweza kuibua upya mapenzi kutokana na msaada huo haswa kwa upande wa mwanamke na kumfanya yeye bado akawa ana hisia na huyo mwanaume kwa kuona jinsi alivyo na huruma na kuwasaidia.

 

Katika hali kama hiyo pamoja na kuwa msaada ni jambo muhimu kwa wanaadamu lakini linaweza kuwarejesha tena kwenye maasi kwa njia moja au nyingine, hivyo ni bora kuepuka hilo na inshaAllaah watapata msaada kwa njia nyingine kwa uwezo wa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala).

Kuna kanuni inayosema, 'Kuzuia madhara kunatangulizwa kuliko kuleta maslaha'.

 

Na swali la kujiuliza, msaada kama huo anautoa kwa Waislam wenzake na wasio na uwezo au ni kwa huyo tu mwanamke asiye Muislamu kwa sababu ya historia yao?

 

Ajitahidi huyo mwanaume kusaidia mambo ya kheri na Waislamu wenye matatizo yao kwanza maadam ana uwezo wa kusaidia, na ikibidi sana kuwasaidia hao ima kwa hali yao kuzidi kuwa mbaya, basi asisaidie kwa njia ya moja kwa moja yeye, bali msaada ufikishwe na mtu mwengine na pia uambatane na nasaha za kurudi katika dini ya Allaah kweli na afundishwe Uislam na pia ajulishwe umuhimu wa kujilinda na maasi na kuwa mbali na ya haraam na awapelekee vitabu vya dini na mawaidha mbalimbali ya kuujua Uislam. Kwa upande mwengine kufanya hivyo pia kunaweza kuwavuta katika Uislamu na wakasalimika na kupata uongofu inshaAllaah.

  

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share