Ni Kweli Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) Alimtangazia Urithi ‘Aliy (رضي الله عنه)?

 

SWALI:

 

Wa alaykumusalaam,

 

ALHAMDULILLAHI RABBI L 'ALAMIN. ASSWALAT  WA SALAAM 'A LAA MUHAMAD WA ALAA AALI HII WA SAHBI HII WA SALLIM..Ahsante sana wa kwa majibu mazuri, na pia nashukuru kwa maelezo mlionipa ALLAH (SUB HAANA HUU WA TAALA) atawalipa mema.

 

Naomba msinichoke: Nina swali jengine. Ni kweli MTUME MUHAMAD (SWALLA LLAHU ALAIHI WA SALLAM) alimtangaza urithi Sayyidna ALI (RADHIA LLAHU ANHU)?

 


 

 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu kutangazwa kwa ‘Aliy kuwa Khaliyfah na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Hakika ni kuwa hakuna nasw (andiko) ya wazi kuhusu suala hilo. Na jambo hilo ni la kila moja kutumia akili yake barabara basi atapata jibu mara moja lisilokuwa na utata wa aina.

 

Kila Muislamu anafahamu kuwa Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) walikuwa ni watu wacha Mngu, waadilifu, wakweli, wenye tabia nzuri na msitari wa mbele kuitetea haki. Je, yamkinika kwa watu wenye maadili hayo kuweza kukiuka agizo la Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)? Jibu ni kuwa haiyumkiniki kabisa kwa wao kufanya hivyo. Kisha Allaah Aliyetukuka Amewasifu kwa sifa zilizo wazi, kama Alivyosema:

Muhammad ni Mtume wa Allaah. Na walio pamoja naye ni wenye nyoyo thabiti mbele ya makafiri na wenye kuhurumiana wao kwa wao. Utawaona wakiinama kwa kurukuu na kusujudu pamoja, wakitafuta fadhila za Allaah na radhi Yake” (48: 29).

Na tena:

Kwa hakika Allaah Amewaridhia Waislamu walipofungamana nawe chini ya mti; na alijua yaliyomo nyoyoni mwao” (48: 18).

Na pia:

Na wale waliotangulia wakawa wa kwanza katika Uislamu – Muhajiri na Answari, na wale waliowafuata kwa mwendo mzuri – Allaah Atawapa radhi, nao wamridhie na Amewaandalia mabustani yapitayo mito mbele yake, wakae humo milele” (9: 100).

 

Hizi ni baadhi ya Aayah ambazo zinatuonyesha kuwa Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) waliridhiwa na Allaah Aliyetukuka, Anajua yaliyo nyoyoni mwao na Amewaandalia Pepo. Je, watu wenye sifa hiyo wanaweza kufanya khiyana? Hilo ni jambo lisilowezekana.

 

Kisha wale walioshika hatamu za uongozi baada ya kuaga dunia kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) walikuwa wamebashiriwa Pepo wakiwa hai. Pia ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) mwenyewe aliwazungumzia waliomtangulia kwa kusema:

“Mbora wa Ummah huu baada ya Mtume wake ni Abu Bakr, kisha ‘Umar, na kama ningalitaka ningalimtaja wa tatu – anakusudia ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhum” (Kanzul Umal).

 

Na kauli ya Ibn ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhuma): “Tulikuwa tunasema na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) bado yu hai: Abu Bakr, kisha ‘Umar, kisha ‘Uthmaan, kisha ‘Aliy. Yakamfikia hayo Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) naye hakuyapinga” (Abu Daawuud). Na hakika fadhila za Abu Bakr (Radhiya Allaahu ‘anhu) zilikuwa juu ya Maswahaba wote, na ndiye Swahaba wa pekee aliyepewa ruhusa na kuwakilishwa na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kuwaswalisha Maswahaba wakati Mtume yuko hai na yuko Madiynah.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share