Skip navigation.
Home kabah

Mzazi Kumuuzia Nyumba Mtoto Mmoja

SWALI:

ASSALAM ALEIKUM.

SWALI LANGU NI: 

TUNA NYUMBA YA FAMILIA KUBWA KWA MAJINA YETU YAANI NDUGU SOTE ISIPOKUA JINA LA BABA NA MAMA.  NA IKIWA BABA AMA MAMA ANA NYUMBA YAKE MWENYEWE  NA ANATAKA KUMUUZIYA MMOJA WA WATOTO WAO KISHERIA INAWEZEKANA ? AMA ATAKUWA AMEWADHULUMU WATOTO WENGINE KWA KUWA HAKUWAGAWIYA? TAFADHALI NAOMBA JIBU.

 

 



JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani kubwa na za dhati kwa ndugu yetu kuhusu swali lako hilo. Hakika ni kuwa mas-ala ya kuuza na kununua yamo katika Dini yetu tukufu. Kuuza na kununua ni kazi na biashara ambayo hutiliwa baraka na Mwenyewe Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala).

Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anasema: “Hayo ni kwa sababu wamesema: ‘Biashara ni kama ribaa’, hali Allaah Amehalalisha biashara na kuiharamisha ribaa” (2: 275).

Biashara katika Uislamu kama kazi nyenginezo ina kanuni zake. Mambo kama kughushi, kuficha, kuongeza bei na haja yoyote ile, utovu wa uaminifu, uongo na kadhalika. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Msihusudiane, wala msiongezeane bei pasi na kuwa na haja ya kununua wala msichukiane wala msipeane nyongo wala wasinunue baadhi yenu kilichokwisha kuuziwa wenzenu, lakini kuweni enyi waja wa Allaah ndugu” (al-Bukhaariy, Muslim na Abu Daawuud).

Na Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anasema: “Enyi mlioamini! Msiliane mali zenu kwa batili, isipokuwa iwe biashara kwa kuridhiana baina yenu. (Hiyo inajuzu) wala msijiue (wala msiue wenzenu)” (4: 29).

Ayah tuliyoinukuu hapo juu (4: 29) inatuweka sisi wazi katika mas-ala ya kuuza (au biashara) kwa kuridhiana. Kwa hiyo, msingi mkubwa na mahusiano ya kidamu baina ya wanaouziana bali ni maelewano. Katika Uislamu inajuzu mzazi kumuuzia kitu kilicho miliki yake mtu yeyote hata akiwa mtoto wake. Vile vile inajuzu kwa mtoto kuuza bidhaa yake kwa mtu yeyote hata akiwa ni mzazi wake. Hii nyumba aliyonayo baba bado ni yake na kwa hiyo ana uhuru wa kumuuzia mtoto wake aliye tayari kuinunua kutoka kwake kwa pesa watakazokubaliana.

Jambo ambalo halifai ni kwa baba kumrithisha mmoja na kuwaacha wengine. Mas-ala haya yamekatazwa na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Jambo la urithi tayari Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) keshagawa na mtu kaachiwa thuluthi ya kumtunikia anayemtaka ambaye kisheria si yule mwenye kurithi. Kwa hivyo, baba kumuuzia nyumba mtoto wake inawezekana na hakuna dhulma yoyote kwani yeye yuko huru.

Sentensi ya kwanza katika swali lako hatukuifahamu pale uliposema, “Tuna nyumba ya familia kubwa kwa majina yetu yaani ndugu sote isipokuwa jina la baba na mama”. Je, hii nyumba ambayo mzazi ameiuza kwa mmoja wenu ni hii yenu au vipi? Ikiwa jibu ndio, je, ilikuwaje kwa majina yenu, mlinunua au mlikabidhiwa au vipi? Ikiwa mmeimiliki tayari basi itakuwa haifai kwa mama au baba kuiuza nyumba hiyo kwani yeye hayumo katika shirika ya nyumba hiyo. Na ikiwa yumo katika shirika pia hatoweza kuiuza peke yake mpaka washirika wote wawe ni wenye kukubali.

 Na Allaah Anajua zaidi