Vidokezo Muhimu Kwa Wazazi Wenye Wasichana Na Wavulana

 

Vidokezo Muhimu Kwa Wazazi Wenye Wasichana Na Wavulana

 

Imetarjumiwa na: Ummu 'Abdil-Wahhaab

 

 

Wazazi wafanye nini ili vijana wao wawe ni Waislamu wenye kutekeleza Uislamu wao kwa matendo? 

 

 

1-Yatilie Bidii Malezi Kuliko Hata Kazi Yako Ya Kutwa Nzima

Hii ina maana kwamba wazazi wote wawili ni lazima waelewe kuwa watoto wao ni wa kweli kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala), na baba atakuja kuulizwa vipi kawalea watoto wake.  Ikiwa watoto wao hawatokulia katika kuutekeleza Uislamu kwa sababu ya mapuuza ya wazazi wao, halitokuwa ni jambo la kukubalika kwa maisha ya hapa duniani na hata ya baadae.

 

2-Punguza Au Badilisha Masaa Ya Kazi Kwa Ajili Ya Kupata Muda Wa Kuwa  Pamoja Na Familia Yako

Ni bora kuwa na kazi moja yenye muda wa kudumu, anasa chache katika nyumba (yaani sio magari mengi, nguo za gharama nyingi, nyumba kubwa ya fakhari, televisheni kila pahali), na muda zaidi wa kuwa pamoja na familia, kuliko kuwa na mambo mengi ya anasa na kukakosekana malezi. Haya yote yanawahusu mababa na mamama. Wazazi hawawezi kuwafunza watoto wao bila ya wao kuwepo nao kikawaida.  Acha kazi za ziada kwenye siku za mwisho wa wiki au kazi za jioni na badala yake nenda na watoto Msikitini kwa ajili ya Halaqah (darsa za dini) na shughuli nyenginezo. Au tilia maanani kugeuza nyakati za kazi ili uwe nyumbani wakati ambao watoto wapo.

 

3-Soma Qur-aan, Ifahamu Maana Yake, Angalau Kwa Dakika Tano Kila Siku

Angalau dakika tano. Inawezekana ikawa kwenye gari wakati (umesimama kwa ajili) ya msongamano wa magari, mapema baada ya Swalah ya alfajiri, au mara tu kabla ya kulala, soma Qur-aan pamoja na maana au tafsiri.  Baadae angalia umuhimu wa taathira yake.  In shaa Allaah utajikurubisha kwa Allaah, na baada ya muda mrefu, utakuwa mfano bora wa kuigwa na kuisaidia familia nzima kujikurubisha kwa Allaah vile vile.

 

4-Hudhuria Halaqah Kila Wiki

Acha michezo ya karata na kuangalia televisheni siku za jumapili na badala yake hudhuria Halaqah (darsa duara za dini; ima misikitini au majumbani au kwenye kumbi za kukodishwa). Ikiwa (katika Msikiti) hakuna utaratibu uliowekwa tayari kwa wakati huo, basi msaidie Imamu ili auweke. Hudhuria kwa uangalifu Natija ya kufanya haya ni kule watoto kuwaona wazazi wao wanafanya bidii ya kuusoma Uislamu, na wao kwa namna yoyote ile watapata hamu ya kufanya vile vile (wafanyavyo wazazi wao).

 

5-Waheshimu Watoto Wako

Kuwaheshimu watoto wako ina maana usiwafanye kama wapumbavu, bali ni kuwachukulia kama wao ni watu wazima, usiseme nao kitoto au kuwafedhehesha na kuwatukana.  Wajumuishe kwenye shughuli za nyumbani zenye manufaa na waombe ushauri kwenye maamuzi ya mambo muhimu. 

 

6-Kuwa Na Hamu Ya Kushiriki Katika Mambo Wanayoyafanya

Hudhuria michezo yake kikawaida pindi ikiwezekana na harakaat mbalimbali wazifanyazo.

 

7-Yatambue Matatizo Yaliyopo Na Wajulishe Wazi Wazi

Kwa kadiri unavyotumia wakati wako kuwa pamoja na vijana wako, utakuwa na uwezo zaidi wa hisia ya kugundua kitu gani kinawakera Usifagilie hisia hii chini ya zulia (usiufiche ukweli). Ujulishe kwa uwazi. Lakini usifanya kwenye mkutano wa familia au mbele ya wengine. Fanya hivyo wakati wa fikra inayofuata.

 

8-Weka Miadi Ya Kuonana Na Kijana Wako

Kwa vile mara nyingi uwekaji wa miadi ya kuonana inahusishwa na kukutana kwa msichana na mvulana, wazo hili linaweza kutumiwa kwa aina yoyote ya mkutano baina ya watu wawili wanaotaka kutambuana vyema.

Ni muhimu sana kuweka miadi ya kuonana na vijana wako katika kiwango tofauti mara wanapoingia kwenye umri wa usichana/uvulana kwa sababu wao si watoto wadogo tena. Unaweza kuweka miadi na Sumayyah wakati anapomaliza masomo yake ya sekondari (badala ya kwenda kwenye sherehe za ngoma), Yaasir naye wakati anapopata leseni yake ya kuendesha gari au ikiwa unahisi kuna kitu kinawakera na unataka kuwajulisha peke yao ili kuwasaidia kutatua mashaakil yao. 

 

9-Usiwe Tu Ni Mzazi Kwa Mtoto Bali Uwe Pia Ni Rafiki Kwake

Kujenga urafiki nae ina maana ya kuwapa majukumu katika familia. Mpe mvulana wako wa miaka 16, 'Uthmaan, ambaye ana leseni ya gari, majukumu ya kumsaidia mama yake siku za jumamosi anapokwenda madukani kununua vyakula.  Mpe msichana wako wa miaka 15, Khadiyjah, ambaye anapenda maua, kuwa ni mwangalizi wa bustani pamoja na kukatakata majani. Kwa njia hii vijana watajihisi kuwa na wao ni sehemu ya familia, wanajumuishwa na wanahitajiwa.

 

10- Jenga Msikiti Katika Nyumba Yako (Tenga Sehemu  Maalum Ya  Kuswalia Ikiwezekana)

Chagua sehemu ya chini ya nyumba yako au katika ukumbi wako uwe ni Msikiti wa nyumbani. Itayarishe hiyo sehemu kwa kuweka miswala, misahafu na iwe sehemu khaswa ya kuswaliwa.

Fanya Msikiti huu kuwa waangalizi wake ni watoto tu peke yao. Muweke mkubwa wao kuwa ni msimamizi na mpangaji wa majukumu kwa wadogo zake. Majukumu hayo yawe ni pamoja na kuuweka Msikiti uwe safi, kuwaamsha watu Alfajiri, kuadhini, na kadhalika.

 

11-Usijenge (Fikra Kuwa) “Uislamu Ni Kwa Wanaume Tu”

Hii ina maana usibague wake zako na wasichana kwenye Swalah. Wakati wanaume wanaposwali Swalah ya jama'ah, hakikisha wanawake wapo nyuma yao au wanaswali Swalah ya Jama'aah (sehemu nyengine) na wao.  Vile vile hakikisha Imaam anasoma kwa sauti kiasi ya kusikika na wanawake ikiwa wapo sehemu nyengine ya nyumba.  Vile vile wahimize wanawake waswali Swalah ya Jama'Aah pindi ikiwa wanaume hawapo nyumbani.

 

12- Anzisha Maktaba Ya Kiislamu Na Chagua Muangalizi Wake

Iandae nyumba yako yenye maktaba ya Kiislamu kwa vitabu, kanda za kusikiliza zenye maadili ya Kiislamu, mpatie kila mmoja kwa mujibu wa umri na hamu yake. Ikiwa 'Abdullaah mwenye umri wa miaka 13 anapenda vitabu vya hadithi za hatari, kwa mfano, hakikisha unavyo vitabu vya Kiislamu vya kila aina vyenye hadithi za aina hiyo.

Mfanye mmoja katika vijana wako kuwa ni mwangalizi wa maktaba. Aipangilie na kuiweka katika hali nzuri. Kitu chochote kinachotakiwa kuingizwa kwenye maktaba ni lazima kipitishwe kwake. Mpe msimamizi wa maktaba bajeti ya kila mwezi ya kununulia vitabu, kanda za kusikiliza na kadhalika.

 

13-Wachukue kwenye shughuli za Kiislamu

Badala ya kwenda kwenye Mgahawa (Restaurant) kwa ajili ya vyakula vya kila aina, hifadhi pesa zako kwa ajili ya kumchukua kila mmoja katika chakula au shughuli za jamii ya Kiislamu. Fanya bidii kwenda kwenye matukio ambayo vijana wengine wa Kiislamu watahudhuria na kutakuwa na msemaji atakayetoa ujumbe kwenye mkusanyiko (huo).

Ni muhimu vile vile  kufanya mazoea ya kumchukua 'Abdur-Rahmaan na 'Aaishah kwenye kambi za  Kiislamu na mikutano ambayo watakutana na watoto wenzao wa Kiislamu kwa wingi na wenye umri unaolingana na wao.

 

14-Hamia Kwenye Maeneo Yenye Waislamu Wengi

Wazo hili limekusudiwa haswa kwenye eneo lilo karibu na Msikiti. Hatua hii ni muhimu kwa kuwa watoto wako ili wawe wanaambatana na watoto wengine wa Kiislamu wenye umri ulio chini, sawa au zaidi na wao, katika mambo yao ya kimsingi ya kila siku.

 

15-Wasaidie Vijana Wako Ili Waanzishe Wao Wenyewe Kikundi Cha Vijana

Baada ya kuwa unaishi kwenye eneo la Waislamu na unahudhuria shughuli za Kiislamu kikawaida, vijana wako katika mambo mengi wataukuza urafiki na  Waislamu wengine wenye umri unaolingana na wao.  Usiyaachie haya yakaishia hapo.

Wasaidie kuanzisha kikundi cha vijana, sio tu kwa ajili ya kusoma Uislamu bali pia kutembea pamoja kwenye viwanja vya kupendeza, kuogelea, na kadhalika.  Kihusishe kikundi hichi kwenye kazi muhimu kama za kusafisha takataka Msikitini au kuhudhuria nyumba zinazolelewa wazee.  Kikundi hiki  ni lazima kiwe na uangalizi wa wazazi, ijapokuwa maamuzi ya vijana yasiingiliwe mpaka ionekane kikweli kweli upo umuhimu/haja ya kufanya hivyo.

 

16-Kuwepo Mikutano Ya Familia Kwa Kila Wiki

Madhumuni  ni kutafuta kinachoendelea katika maisha ya kila mmoja wao na kutoa ushauri wa mambo muhimu katika familia. Hafswah ameanza kuhudhuria Halaqah, Hasan naye amerejea kutoka kwenye kambi ya Kiislamu, na Husayn amekaribia jaribio lake la mwisho katika hesabu za algebra.  Sio tu kutoa taarifa kwa mfumo wa muhtasar, bali ni kujadiliana na kuwasiliana baina ya kila mmoja, na kuweka taarifa mpya kabisa kwa kila kinachoendelea katika maisha ya kila mmoja wao, ambapo inakuwa ni vigumu (kuyafanya haya) pale watoto wanapokuwa wanakaribia kuingia kwenye umri wa ujana.

Huu vile vile ni wakati wa kuishauri familia na kuamua juu ya mambo makubwa  yanayomuathiri  kila mmoja kati yao kama kuhamia mji mwengine, harusi ya mmoja kati yao, iwapo yupo mwenye wakati mgumu skuli kwa sababu ya wanao mbughudhi, na kadhalika.

Tafadhali kumbuka: Mashauriano katika familia haimaanishi kwamba maamuzi ya walio wengi ndio yafuatwe kuhusu hali inayojadiliwa.  Bali wazazi watabaki kuwa ndio wenye dhamana, fikra na rai za vijana na watoto wadogo, wazazi watayazingatia kwenye kufanya maamuzi yao ya mwisho.

 

17-Weka Kigezo Cha Majukumu - Nini Abu Bakr Kafanya?

Mbali ya kuwa wewe mwenyewe ni kigezo juu ya kuutekeleza Uislamu kwa vitendo, hakikisha unawawekea vijana wako vifaa vya kusoma kuhusu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa Sallam) na Maswahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum), wote wanawake na wanaume, la sivyo, huenda watoto wako wakaiga wahusika wa vipindi vya televisheni ambavyo watoto wako wanaangalia na wakawa ndio Maswahaba wao. 

Jadiliana nao nini Maswahaba walikuwa wakifanya katika kukabiliana na maisha ya vijana. Swahaba Abu Bakr asw-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ‘anhu) angelifanya nini pindi angelimuona mtu anauza majawabu ya mtihani wa mwisho ya hesabu za darasa la saba au darasa la kumi na mbili (form IV)? Na 'Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anha) angelifanya nini pindi angelikabiliana na mtu mwenye kudanganya wazazi wake?

 

18-Soma Vitabu Kwa Ajili Ya Malezi Ya Uhakika

Hivi vinaweza kuwa ni vitabu vilivyoandikwa na Waislamu, lakini vitabu vilivyoandikwa na wasiokuwa Waislamu pia vinaweza kusaidia.  Hata hivyo, jitayarishe na pia hakikisha kuwa unao uwezo wa kugundua ni vitabu vipi vinakubalika Kiislamu dhidi ya visivyokubalika.

 

19-Waache Waoe / Waolewe Mapema

Fitna kutoka nchi za Magharibi zimeeneza picha za ngono kwenye televisheni, mabango ya matangazo, mitaani, kwenye mabasi, katika filamu za maigizo, na kadhalika, nazo zinapatikana wazi katika baadhi ya nchi zetu.  Inakuwa ni ngumu kwa kijana wa Kiislamu kuyakabili haya bila ya kuwa na matamanio na kushindwa kujizuia na maovu hayo. Ni jambo la maana kuwaacha waoe/waolewe mapema (Soma baadhi ya vidokezo vinavyowahusu wazazi juu). Hii itarahisisha shinikizo, na hapana haja ya kukatisha masomo yao kwenye suala hili.

Kumbuka, kama ni mzazi utabeba jukumu ikiwa mvulana au msichana wako atataka kuoa au kuolewa na wewe ukamkataza na akaishia kwenye kufanya uzinifu. Vile vile ni lazima ukumbuke kuwa unapotekeleza hatua hii usimlazimishe mvulana au msichana wako kuoa au kuolewa na mtu asiyempenda.

 

20-Mwisho Lakini Pia Muhimu - Omba Du'aa

Omba Dua. Ni Yeye Allaah Pekee Anayeongoa au Kutoongoa, lakini ikiwa umetekeleza wajibu wako kama ni mzazi kuwafanya watoto kuwa ni wenye kuutekeleza Uislamu kwa vitendo, In shaa Allaah, ni rahisi kuwalea kuliko kulipuuza jukumu hili. Pia waombee Du'aa vijana wako mbele yao. Kufanya hivyo kutawakumbusha wao jinsi gani unavyowapenda na kujihusisha nao.

 

Du'aa Mojawapo Katika Qur-aan

رَبَّنَا هَبْ لَنَا مِنْ أَزْوَاجِنَا وَذُرِّيَّاتِنَا قُرَّةَ أَعْيُنٍ وَاجْعَلْنَا لِلْمُتَّقِينَ إِمَامًا

((Rabb wetu Tupe katika wake zetu na wenetu yaburudishayo macho, na Utujaalie tuwe waongozi kwa wenye taqwa)) [Al-Furqaan: 74]

 

 

 

 

Share