Masuala Kumi Yanayoeleweka Vibaya Katika Uislam - 03

 

Masuala Kumi Yanayoeleweka Vibaya Katika Uislaam - 03

 

Imefasiriwa na: Naaswir Haamid

 

Alhidaaya.com

 

 

Suala Nambari 3 Linaloeleweka Vibaya

 

Ndani ya Uislamu, wanawake ni duni kuliko wanaume kwasababu:

 

  • Mwanaume anaweza kuoa hadi wake wanne, mwanamke anaweza kuolewa na mwanamme mmoja tu.

 

  • Sehemu ya urithi wa mwanamme ni kubwa kuliko ya mwanamke.

 

  • Mwanamme anaweza kuoa mwanamke asiye Muislamu, mwanamke hawezi

 

  • Mwanamke ni lazima avae hijaab.

 

 

Jibu

 

Suala hili pana halielekei kufuatana kwa mnasaba wa hoja zinazotolewa. Tathmini ya mwanzo na muhimu zaidi ya kuifanya ni kuhusu suala maarufu “Je wanaume ni sawa na wanawake?”

 

Ni suala ambalo limetengenezwa vibaya, lisiloweza kujibika. Tatizo ambalo watu wengi wanatumia kuliepuka ni kutolitafsiri neno “usawa”. Hii ni nukta inayohitaji kuupambanua usawa ambao ni lazima uelezwe kwa hali inayopimika. Kwa mfano, wanawake kwa kiwango fulani wapo juu kuliko wanaume kama tutauliza nani ni mfupi kwa (kupambanisha na) urefu kuliko mwengine (“Ukuaji na Maendeleo” Encyclopaedia Britannica, 1992). Wanawake pia wapo juu kwa kiwango fulani kama tutauliza watoto wana mapenzi zaidi na nani, mama au baba? Wanawake pia wapo juu kwa kiwango fulani kama tutauliza nani ana tabia ya kujiweka kwenye jamii zaidi. Kwa upande mwengine, wanaume wapo juu kwa kiwango fulani kama tutauliza nani ni mrefu kwa (kupambanisha na) ufupi kuliko mwengine. Na mambo mengineyo: kila suala linaweza kugeuzwa upande mwengine, na muhimu zaidi ni kuwa hali hizi hazina mnasaba.

 

Je, kinachofuata, ni hali gani muhimu ambayo tuna wasiwasi nayo kuhusiana na usawa wa jinsia? Kiasili, kutokana na uoni wa Qur-aan na Sunnah, hali iliyokuwa muhimu zaidi ni nani aliyekuwa mtiifu kwa Allaah, wanaume au wanawake? Suala hili bila ya shaka linajibiwa ndani ya Qur-aan:

 

وَمَن يَعْمَلْ مِنَ الصَّالِحَاتِ مِن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَأُولَـٰئِكَ يَدْخُلُونَ الْجَنَّةَ وَلَا يُظْلَمُونَ نَقِيرًا ﴿١٢٤﴾

 

Na atakayefanya mema akiwa mwanamume au mwanamke hali yeye ni Muumini; basi hao wataingia Jannah na wala hawatodhulumiwa watu kadiri ya kitone cha kokwa ya tende.  [An-Nisaa: 124]

 

 Pia Amesema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

إِنَّ الْمُسْلِمِينَ وَالْمُسْلِمَاتِ وَالْمُؤْمِنِينَ وَالْمُؤْمِنَاتِ وَالْقَانِتِينَ وَالْقَانِتَاتِ وَالصَّادِقِينَ وَالصَّادِقَاتِ وَالصَّابِرِينَ وَالصَّابِرَاتِ وَالْخَاشِعِينَ وَالْخَاشِعَاتِ وَالْمُتَصَدِّقِينَ وَالْمُتَصَدِّقَاتِ وَالصَّائِمِينَ وَالصَّائِمَاتِ وَالْحَافِظِينَ فُرُوجَهُمْ وَالْحَافِظَاتِ وَالذَّاكِرِينَ اللَّـهَ كَثِيرًا وَالذَّاكِرَاتِ أَعَدَّ اللَّـهُ لَهُم مَّغْفِرَةً وَأَجْرًا عَظِيمًا ﴿٣٥﴾

 

Hakika Waislamu wanaume na wanawake, na Waumini wanaume na wanawake, na watiifu wanaume na wanawake, na wasemao kweli wanaume na wanawake, na wanaosubiri wanaume na wanawake, na wanyenyekevu wanaume na wanawake, na watoao swadaqah wanaume na wanawake, na wafungao Swawm wanaume na wanawake, wanaojihifadhi tupu zao wanaume na wanawake, na wanaomdhukuru Allaah kwa wingi wanaume na wanawake; Allaah Amewaandalia maghfirah na ujira adhimu. [Al-Ahzaab: 35]

 

Qur-aan na Sunnah zinarudia tena na tena kwamba Allaah Anampendelea mtu mmoja dhidi ya mtu mwengine kwa kigezo chake cha hamasa, unyenyekevu, khofu, mapenzi, na matarajio ya Allaah (neno la kiarabu la ‘Taqwa’ ‘Mcha Allaah’ ni gumu kulipatia tafsiri yake halisi). Sifa nyengine zote zimetenguliwa: jinsia, kabila, taifa, asili, n.k.

 

Kwa vile Allaah Hapendelei jinsia moja dhidi ya nyengine ndani ya matakwa Yake kwetu sisi (na inasaidia kukumbuka kwamba Allaah sio mwanamme wala mwanamke), na sasa tunaweza kuelezea tofauti baina ya jinsia ndani ya Uislaam.

 

Kwanza, wanaume na wanawake hawapo sawa kama tunavyoelewa. Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anaelezea ndani ya Qur-aan:

وَلَيْسَ الذَّكَرُ كَالْأُنثَىٰ ۖ 

Na mwanamme si kama mwanamke. [Al-‘Imraan: 36]

 

Wanaume na wanawake ni tofauti kwenye tabia, na kwenye majukumu yao ndani ya Uislaam. Hata hivyo, wote wana ulazima wa uwajibikaji kwa mwenziwe, hususan nukta hii muhimu inayofuata ambayo ni lazima ieleweke ndani ya mjadala wowote kuhusu wanaume na wanawake.

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

وَأَنكِحُوا الْأَيَامَىٰ مِنكُمْ وَالصَّالِحِينَ مِنْ عِبَادِكُمْ وَإِمَائِكُمْ ۚ إِن يَكُونُوا فُقَرَاءَ يُغْنِهِمُ اللَّـهُ مِن فَضْلِهِ ۗ وَاللَّـهُ وَاسِعٌ عَلِيمٌ ﴿٣٢﴾

 

Na waozesheni wajane miongoni mwenu na walio Swalihina kati ya watumwa wenu wanaume na wajakazi wenu. Wakiwa mafakiri Allaah Atawatajirisha katika fadhila Zake. Na Allaah Mwenye Wasaa, Mjuzi wa yote. [An-Nuwr: 32]

 

Ndani ya Aayah hii, Allaah Anatilia mkazo kwamba ndoa ni lazima ifungwe mapema na Waislamu: tabia ya kuwa pweke isikuwepo. Kwa kuwepo hili akilini, tunaweza kuanza kuelewa hoja nne zilizotajwa hapo juu kwa hitimisho lisilo na kosa lolote.

 

Wanaume na wanawake ni tofauti kwenye kuwajibika kwao kwa familia ambazo wanahimizwa sana kuzisimamisha. Wanawake hawawajibiki kufanya kazi, wakati wanaume wanalazimika. Mwanamme ni lazima atoe mahitaji kwa familia, lakini mwanamke hana haja ya kutumia pesa yake kwa ajili hiyo, ingawa anapata malipo kwa kufanya hivyo. Allaah Anasema ndani ya Qur-aan:

 

الرِّجَالُ قَوَّامُونَ عَلَى النِّسَاءِ بِمَا فَضَّلَ اللَّـهُ بَعْضَهُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ وَبِمَا أَنفَقُوا مِنْ أَمْوَالِهِمْ ۚ فَالصَّالِحَاتُ قَانِتَاتٌ حَافِظَاتٌ لِّلْغَيْبِ بِمَا حَفِظَ اللَّـهُ ۚ وَاللَّاتِي تَخَافُونَ نُشُوزَهُنَّ فَعِظُوهُنَّ وَاهْجُرُوهُنَّ فِي الْمَضَاجِعِ وَاضْرِبُوهُنَّ ۖ فَإِنْ أَطَعْنَكُمْ فَلَا تَبْغُوا عَلَيْهِنَّ سَبِيلًا ۗ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلِيًّا كَبِيرًا ﴿٣٤﴾

 

Wanaume ni wasimamizi juu ya wanawake kwa kuwa Allaah Amefadhilisha baadhi yao kuliko wengine na pia kwa ambayo wanatoa katika mali zao. Basi wanawake wema ni wale watiifu wenye kujihifadhi katika hali ya kutokuweko waume zao kwa kuwa Allaah Ameamrisha wajihifadhi. Na wale ambao mnakhofu uasi wao wa ndoa, basi wanasihini na wahameni katika malazi na wapigeni (kipigo kisichodhuru). Wakikutiini, basi msitafute njia dhidi yao (ya kuwaudhi). Hakika Allaah daima ni Mwenye Uluwa, Mkubwa wa dhati, vitendo na sifa [Al-Nisaa: 34]

 

Kutokana na Sunnah, hususan ndani ya somo la Sunnah linaloitwa [Swahiyh al-Bukhaariy], tunaona:

 

Amesimulia ‘Amr bin Al-Haarih: Zaynab, mke wa ‘Abdullaah alisema: “Nilikuwa Msikitini nikamuona Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: ‘Enyi wanawake! Toeni sadaka hata kama kutoka kwenye mapambo yenu’ Zaynab alikuwa akimpatia ‘Abdullaah na mayatima walio chini ya hifadhi yake. Hivyo alimwambia ‘Abdullaah, “Je unaweza kumuuliza Rasuli wa Allaah iwapo naweza kutumia sehemu ya Zakaat kwako na mayatima walio chini ya hifadhi yangu?” Alijibu “Je, utamuuliza mwenyewe Rasuli wa Allaah?” (Zaynab akaongeza): Hivyo nilienda kwa Nabiy na hapo nikamuona mwanamke wa ki-Aanswari aliyekuwa amesimama mlangoni (kwa Nabiy) aliyekuwa na tatizo lililo sawa na langu. Bilaal alipita mbele yetu na tukamuomba, “Muulize Rasuli wa Allaah iwapo naweza kutumia sehemu ya Zakaat kwa mume wangu na mayatima walio chini ya hifadhi yangu” Na tukamuomba Bilaal kutomtaarifu Nabiy kuhusu sisi. Hivyo Bilaal aliingia ndani na kumuuliza Nabiy kuhusiana na tatizo letu. Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliuliza, “Hao wawili ni kina nani?” Bilaal alijibu kwamba alikuwa ni Zaynab. Nabiy alisema, “Zaynab gani?” Bilaal alisema, “Mke wa ‘Abdullaah (bin Mas’uud)”. Nabiy akasema, “Ndio, (inawezekana kwake), na atapata malipo mara mbili yake (kwa tendo hilo): Kwanza kwa kusaidia jamaa zake, na pili kwa kutoa Zakaat.”

 

Kutokana na waume kulazimishwa kuwahudumia wake, na kwamba ndoa ni pendekezo lililotiliwa mkazo (sana) la Uislaam, ni rahisi kuona kwanini urithi wa wanawake ni nusu ya wanaume. Pia tunatambua kwamba, katika ndoa ni wanaume wanaolazimishwa kuwapatia wanawake mahari yaliyo muafaka. Ni kweli, na inafaa kwa sasa kuzungumza misamiati ya waume na wake kuliko wanaume na wanawake. Allaah Anasema ndani ya Qur-aan:

 

وَآتُوا النِّسَاءَ صَدُقَاتِهِنَّ نِحْلَةً ۚ فَإِن طِبْنَ لَكُمْ عَن شَيْءٍ مِّنْهُ نَفْسًا فَكُلُوهُ هَنِيئًا مَّرِيئًا ﴿٤﴾ 

 

Na wapeni wanawake mahari zao kwa maridhawa. Lakini wakitoa chochote wenyewe katika mahari yao kwa khiari zao, basi kuleni kwa kufurahia na kunufaika. [Al-Nisaa: 4]

 

Allaah Anasema ndani ya Qur-aan:

 

 وَبُعُولَتُهُنَّ أَحَقُّ بِرَدِّهِنَّ فِي ذَٰلِكَ إِنْ أَرَادُوا إِصْلَاحًا ۚ وَلَهُنَّ مِثْلُ الَّذِي عَلَيْهِنَّ بِالْمَعْرُوفِ ۚ وَلِلرِّجَالِ عَلَيْهِنَّ دَرَجَةٌ ۗ 

 

Nao wake wana haki kama ambayo (ya waume zao) iliyo juu yao kwa mujibu wa shariy’ah. Na wanaume wana daraja zaidi juu yao. [Al-Baqarah: 228]

 

Hali hii haimuathiri (hata chembe) wadhifa wa Allaah ambaye Ameeleza kwamba Hawaangalii wanawake kuwa ni bora kwake kuliko wanaume, au kinyume chake. Isipokuwa kwa njia nyepesi ya kugawa majukumu ndani ya nyumba yenye watu wazima wawili: mtu mmoja ni lazima awe na kauli ya mwisho katika masuala ya kila siku. Kama itakavyooneshwa hapa chini ndani ya sehemu kwenye masuala tofauti yanayoeleweka vibaya, ingawa kauli ya mwisho inaangukia kwa mume, ni kwa kupitia njia ya mashauriano kwamba amri zilizo nzuri zinafikiwa.

 

Wakati wanaume wanaruhusiwa kuoa hadi wake wanne, pia wanalazimika kabla yake kutimiza masharti ya kuweza kuwahudumia kifedha. Pia wamtumikie kila mke kwa haki na usawa pamoja na majukumu ya ndoa na uchumi. Allaah Anasema ndani ya Qur-aan:

 

وَإِنْ خِفْتُمْ أَلَّا تُقْسِطُوا فِي الْيَتَامَىٰ فَانكِحُوا مَا طَابَ لَكُم مِّنَ النِّسَاءِ مَثْنَىٰ وَثُلَاثَ وَرُبَاعَ ۖ فَإِنْ خِفْتُمْ أَلَّا تَعْدِلُوا فَوَاحِدَةً أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُكُمْ ۚ ذَٰلِكَ أَدْنَىٰ أَلَّا تَعُولُوا ﴿٣﴾

 

Na mkikhofu kuwa hamtoweza kufanya uadilifu kwa mayatima; basi oeni waliokupendezeni katika wanawake wengine; wawili au watatu au wanne. Lakini mkikhofu kuwa hamtoweza kufanya uadilifu, basi mmoja tu au ambao mikono yenu ya kulia imewamiliki. Hivyo ni karibu zaidi kwamba hamtoelemea kudhulumu. [Al-Nisaa: 3]

 

Juu ya hivyo, wanawake wanaruhusiwa kukataa posa yoyote iliyofanywa kwake na mposaji aliye tayari (kuoa), hivyo kama atahisi kwamba hawezi kutimiza kanuni za Qur-aan na Sunnah ikiwa ataolewa na mtu fulani, anaweza kukataa posa yake (mposaji). Ingawa (tuhuma hizi) si sahihi kwa Uislamu, ni vyema ikabainishwa kwamba dini zote mbili; Uyahudi na Ukristo unakubali ndoa ya mke zaidi ya mmoja. Fikra hii sio kwamba ni ngeni kwa wasiokuwa Waislamu kama inavyodaiwa.

 

Mwisho, uvaaji wa hijabu kwa wanawake ni jambo lisilo na mantiki kudai kwamba wanawake wapo chini kuliko wanaume. Ni bora kuikemea jamii inayokubali picha za uchi pornography kuliko kuikemea jamii inayokubali hijabu. Ikiangaliwa kwamba Allaah sio mwanamume wala mwanamke, na ikiangaliwa kwamba Hawatukuzi watu Kwake kwa kigezo cha jinsia zao, ikiangaliwa kwamba Allaah Anatujali sote wanaume kwa wanawake, ikiangaliwa kwamba shahawa za kimwili na shinikizo la mahitaji ya wanaume yapo juu kuliko yale ya wanawake….yakiangaliwa yote haya, basi hakuna maana yoyote kuvurumisha maelezo mabaya kwenye kanuni inayofuata iliyomo ndani ya Qur-aan:

 

قُل لِّلْمُؤْمِنِينَ يَغُضُّوا مِنْ أَبْصَارِهِمْ وَيَحْفَظُوا فُرُوجَهُمْ ۚ ذَٰلِكَ أَزْكَىٰ لَهُمْ ۗ إِنَّ اللَّـهَ خَبِيرٌ بِمَا يَصْنَعُونَ ﴿٣٠﴾وَقُل لِّلْمُؤْمِنَاتِ يَغْضُضْنَ مِنْ أَبْصَارِهِنَّ وَيَحْفَظْنَ فُرُوجَهُنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا ۖ وَلْيَضْرِبْنَ بِخُمُرِهِنَّ عَلَىٰ جُيُوبِهِنَّ ۖ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ

 

Waambie Waumini wanaume wainamishe macho yao na wahifadhi tupu zao. Hivyo ni utakaso zaidi kwao. Hakika Allaah ni Mwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika kwa yale wayatendayo. Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao na wahifadhi tupu zao, na wala wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa yale yanayodhihirika. Na waangushe khimaar (shungi) zao mpaka vifuani mwao, na wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa kwa waume zao.. [An-Nuwr: 30-31]

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ وَبَنَاتِكَ وَنِسَاءِ الْمُؤْمِنِينَ يُدْنِينَ عَلَيْهِنَّ مِن جَلَابِيبِهِنَّ ۚ ذَٰلِكَ أَدْنَىٰ أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ ۗ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا ﴿٥٩﴾

 

Ee Nabiy! Waambie wake zako, na mabinti zako, na wanawake wa Waumini wajiteremshie jilbaab zao. Hivyo kunapeleka karibu zaidi watambulikane (kwa heshima) wasiudhiwe. Na Allaah daima ni Mwingi wa kughufuria, Mwenye kurehemu. [Al-Ahzaab: 59]

 

Kwenye suala hili linaloeleweka vibaya, kuna maelezo marefu ya kuendelea kuandika, mengi yao yakuonesha namna matendo ya sasa ya ardhi zilizo nyingi za Waislamu yanavyokwenda kinyume na amri za Qur-aan na Sunnah, ardhi ambazo wanawake wanafanywa kama vile ni bidhaa (huu sio Uislaam), hawana elimu (huu sio Uislaam), wanazuiwa haki zao za uchumi (huu sio Uislaam), na mengineyo. Hakika katika nukta hii, tunamuhimiza kila mmoja kushauriana na Qur-aan na Sunnah kabla ya kuukosoa Uislaam. Daima kumbuka kwamba Uislaam ni njia kamili ya maisha inayotoka kwa Allaah, na kwamba Waislamu ni watu wanaodai kuifuata njia hiyo ya maisha. Muislamu anaweza kudai kufuata Uislaam, lakini akawa ana makosa.

 

 

.../4

 

 

 

Share