Mke Kuhama Nyumba Na Asiyemtii Mumewe Kwa Sababu Kaoa Mke Mwengine Nini Hukmu Yake

SWALI:

 

Asalamu alaikum

Napenda kuuliza ni ipi hukumu ya mke asiyemtii mumewe? Mimi nina mke na mke wangu ameamua kuondoka nyumbani baada ya kuoa mke wa pili, ameenda kwao na aliporudi ameamua kuwa mbali na nyumba anaishi mahala nisipopajua, Je nifanye nini Kisheria.


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu mke asiyemtii mumewe. Hakika ni kuwa ni vigumu kutoa hukumu ya moja kwa moja kwani tumesikia kesi au kujitetea kwa upande mmoja. Hatujasikia yaliyomfanya mke atoroke. Hata hivyo, katika hali yoyote ile mke kisheria hafai kutoka kwa mumewe kwa sababu yoyote ila iwe kwa ajili ya kisheria ambayo amemnasihi mumewe mpaka akachoka.

 

Suala la mke kutoka mara moja ni ikiwa mume ameritadi kutoka katika Uislamu au maasiya makubwa dhahiri shahiri. Mara nyingi wake kwa wivu ulio nje ya sheria hupandwa na hasira wakafanya mambo kama hayo kisha wakajuta baadaye. Wakati huo huenda majuto kama hayo yakawa hayana faida yoyote ile.

 

Kwa kuwa suala hilo lishatendeka wewe usiwe na hasira bali fuata njia za kisheria kumpata na kumrudisha mkeo. Njia ya rahisi ni kwako kwenda kwa wazazi wake na kutoa taarifa hiyo. Mbali na kuwa wazazi wake huenda wakawa pamoja na binti yao. Hiyo ni kwa kuwa mke wa mtu akaja kwa wazazi na wazazi nao wakamuacha bila kumshurutisha kurudi. Hata hivyo, tukichukulia dhana nzuri ni kuwa huenda wazazi walimwambia arudi kwako naye akatoka lakini asifike kwako. Kwa hiyo, nenda kwa wazazi wake na uzungumze nao kwa upole, ulaini na kwa heshima kuhusu hilo. Allaah Aliyetukuka Anasema:

Na mkichelea kutakuwapo mfarakano baina ya mke na mume basi pelekeni muamuzi kutokana na jamaa za mume, na muamuzi kutokana na jamaa za mke. Wakitaka mapatano Allaah Atawawezesha. Hakika Allaah ni Mjuzi Mwenye khabari” (4: 35).

 

Ikiwa hakutakuwa na natija yoyote na mke akakataa kukaa kwako kwa ajili ya kuoa mke wa pili basi ni afadhali umuache na ubakie na huyo wa pili kwani ukitofanya hivyo utasumbuka pasi na kuwa na haja hiyo.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share