Baba Amemkana Binti Yake Kwa Ajili Amekataa Kuolewa

SWALI:

 

 

Assalaamu aleykum, sheikh mimi nina sister yangu ambaye yuwaendelea na kisomo ilhali asha baleghe kitambo, so hivi majuzi mzee wetu alimwita dada na kumwambia ya kwamba ashapanga yeye mzee na rafiki ya kuwa ili wawaozeshe watoto wao (yaani sister yangu na mtoto wa swahiba yake buda) kwa hiyo sister na huyo kijana hawajuani kichwa wala miguu na dada yangu hayuko tayari kuolewa, hapo dada yangu alikataa katakata hiyo harusi! Sasa balaa yenyewe ilitoka kwa mzee alipomwambia bintiye kuanzia saa hii hatujuani kwa la kheri wala la shari kama umekataa hii amri yangu! Sasa sheikh sijui ndio akhir zamani ama kiyama hichi? Nimeshindwa kuelewa. Inshaallah nataraji jibu ambalo litawanufaisha waislamu wote. Sheikh Mungu akupe umri ili upate kutujibia maswali yetu tutakapopata family na cc "amiin".

 

 


 

 

 

 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu baba mzazi kumkana bintiye kwa kukataa kuolewa.  

 

Hakika ni kuwa hicho si Qiyaamah na wala si akhiri zamani japokuwa zipo ishara nyingi ndogo ndogo kuonyesha hayo. Hata hivyo, kukataa kwa dada yako kuolewa na kijana aliyemchagua baba yako si miongoni mwa alama za Qiyaamah. Kwa mujibu wa dini ya Kiislamu zipo alama nyingi za Qiyaamah ambazo tumeelezewa kinaganaga bila utata wa aina yoyote.

 

Katika Uislamu, binti amepatiwa haki ya kuikubali posa au kuikataa kwa sababu moja au nyingine. Baba amekosea kidogo kwa kumletea binti yake mchumba na bila kumjulisha na kumlazimishia. Kipo kisa ambacho kinapatikana katika Swahiyh al-Bukhaariy pale baba alipomchagulia mume binti yake kabla ya kumjulisha. Binti huyo alikuja kushitaki kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam), naye Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akamchaguza baina ya kukubali wito wa baba au kukataa. Yule binti akamwambia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kuwa amekubali uchaguzi wa baba yake lakini alikuwa anataka kuwafundisha wanawake wengine kuhusu haki yao ya uchaguzi katika suala zima la ndoa.

 

Pia yalikuwa makosa kwa baba badala ya kuzungumza na binti yake baada ya hapo kwa njia nzuri ili amkinaishe aolewe akatumia mabavu kwa kumkana binti. Haifai kisheria kwa baba kumkana binti au kijana wake baada ya kuwa amemkubali muda wote huo. Na pia haifai kwa baba kukataa jukumu la bintiye kwa ajili tu amekataa bali ilikuwa azungumze naye kwa makini na upole na pengine ingekuwa ni busara zaidi kumshirikisha mkewe ili azungumze na bintiye kwa hali ya ulaini na urafiki. Ikiwa binti ameshikilia hilo itabidi wazazi wakubali haki hiyo ya binti.

 

Inabidi kwa wakati huu wazee waingilie kati suala hilo ili kurudisha hali ya awali.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share