Iyd: Tofauti Ya Takbiyrah Za Iydul-Fitwr Na Iydul-Adhwhaa

Tofauti Ya Takbiyrah Za Iydul-Fitwr Na Iydul-Adhwhaa

 

www.alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Assalaam Alaikum.

Naomba mnisaidie tofauti ya takbira za eid al fitri na eid al hajj.   Wassalaam alaikum

 

 

JIBU:

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Kwa kauli ambayo ina nguvu zaidi hakuna tofauti baina ya Takbiyrah za ‘Iydul-Fitwr na ‘Iydul-Hajj. Katika Swalaah za ‘Iyd zote mbili Imamu anapiga Takbiyrah saba (7) baada ya Takbiyratul Ihraam na Takbiyrah tano (5) baada ya Takbiyrah ya kuinuka kutoka katika sijdah. Hii ni kulingana na Hadiyth ya ‘Amru ibn Shu‘ayb kutoka kwa babake kutoka kwa babu yake kuwa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alitoa takbiyr kumi na mbili (12) katika ‘Iyd; saba katika rakaa ya kwanza na tano katika rakaa ya mwisho, wala hakuswali kabla yake wala baada yake (Ahmad na Ibn Maajah).

 

Na hii ndio kauli yenye nguvu na sahihi zaidi iliyopokewa kutoka kwa Maswahaba, Tabi'iyna, Maimaam na Wanachuoni. Haijapokewa kwa njia hata dhaifu kinyume nayo.

 

Ama ikiwa umekusudia Takbiyrah ambayo inapigwa baada ya kwisha Ramadhwaan hadi Swalaah ya ‘Iydul-Fitwr na Takbiyrah ambayo inapigwa kuanzia jioni mwa siku ya ‘Arafah hadi Ayaamut-Tashriyq ambayo ni masiku matatu baada ya ‘Iydul-Hajj, basi hazina tofauti ya maneno yake ambayo kwa mujibu wa Maswahaba ni kuwa walikuwa wakisema:

“Allaahu Akbar Allaahu Akbar, La Ilaaha Illa Allaah, Allaahu Akbar Allaahu Akbar WaliLlaahil Hamd”

 

Kwa hivyo, makusudio ya swali lako yakiwa ni kuhusu maneno ya Takbiyrah katika sikukuu hizo mbili, basi yako sawa na hayana tofauti kama tulivyoeleza hapo.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share