Kutoa Zakaah Ya Mali Inayoongezeka Kila Mwezi

SWALI:

Asalaam Aleikum

Niliuliza suali langu siku za nyuma lakini bado sijapata majibu, hivyo naomba kuuliza tena. Ikiwa mtu mali yake inaongezeka kila mwezi, vipi ataitolea zaka? Mfano Mwezi wa Shabaan 1425 alikua nazoTsh 2,000.000. ilipofika Shabaan 1426 zilizotimia mwaka ni 2,100,000. Lakini bado anazo 700,000 ambazo zitatimia mwaka kidogo kidogo hadi kufikia Rajab1427. Na Shabaan 1427 anazo 3,500,000 kwa jumla na zimo ambazo zitatimia kidogo kidogo.

Wabillahi Tawfik

 

 


 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako hilo lakini tunaona ajabu kuwa hujapata jibu kwa swali lako hilo ambalo tayari lipo katika tovuti. Ni hakika pia kuwa swali lako la awali lilieleweka kwa ufasaha zaidi lakini hili lina utata wa maneno na mahesabu lakini tutachukua ujumla wake. Tunamuomba Allaah Aliyetukuka Atupatie tawfiki ya kuweza kutekeleza Ibaadah Zake zote kwa kiasi tunachoweza na Atufishe tukiwa katika Iymaan na Uislamu, Aamiyn.

Ama kuhusu swali lako la Zakaah ambayo ni nguzo ya Uislamu na Ibadah kubwa miongoni mwa Ibadah zilizo faradhishwa kwetu na Muumba wetu kwa maslahi yetu. Kutekelza nguzo hii inamletea mtu thawabu nyingi nayo ina masharti yake. Hili si geni kwa Zakaah peke yake kwani hata Ibaadah nyingine kama Swalah, funga, Hijjah pia nazo zina masharti yake. Miongoni mwa masharti ya mtu kutoa Zakaah ni:

  1. Kufikisha kiwango cha chini kwa mtu kutoa Zakaah (Niswaab). Hicho kinakuwa kiwango cha pesa sawa na thamani ya gramu 82½ za dhahabu.

 

  1. Kiwango hicho ni lazima kipitiwe na Hawl (mwaka katika kalenda ya Kiislamu).

Ikiwa masharti hayo mawili yatatimia basi Muislamu anafaa atoe asilimia 2½ (2.5%). Ikiwa kiwango chako uichonacho kimefika niswaab na kikapitiwa na mwaka huku kinaongezeka basi itabidi mwaka unapofika utazame una pesa gani na hizo ndio utazitolea Zakaah.

 

Kama hizo pesa ulizotaja kama zimefika Niswaab (kiwango cha gramu 82½ ya dhahabu). Tuseme kuwa 2,100,000 ndio Niswaab na katika miezi kumi na miwili inayofuatia kiwango hicho kinaongezeka mpaka mwisho wa Hawl kikafika 3,100,000. Itabidi utolee Zakaah kiwango hicho cha mwisho ulichofikia mwisho wa mwaka (yaani 3,100,000). Hivyo itakuwa ni 3,100,000 x 2½% = 77,500.

 

Tunatumai utakuwa umetufahamu sasa inshaAllaah. 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share