Je, Unataka Husnul-Khaatimah (Mwisho Mwema )? Basi Ishi Maisha Mema!

 

Je, Unataka Husnul-Khaatimah (Mwisho Mwema )? Basi Ishi Maisha Mema!

 

Kutoka Khutbah: Lahadhwaatul-Mawt Wa Hayaat Al-Qabr

Imaam Muhammad bin Swaalih Al-‘Uthaymiyn  (Rahimahu-Allaah)

 

Alhidaaya.com

 

 

 

Ee bin Aadam! Mche Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  na jiandae kukutana na Rabb wako kwa maandalizi ya waja wema. Hakika hali ya (kila) mwana Aadam ni kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

يَا أَيُّهَا الْإِنسَانُ إِنَّكَ كَادِحٌ إِلَىٰ رَبِّكَ كَدْحًا فَمُلَاقِيهِ ﴿٦﴾

Ee mwana Aadam! Hakika wewe unajikusurukusuru mno kuelekea kwa Rabb wako kwa juhudi na masumbuko, basi utakutana Naye. [Al-Inshiqaaq 84:6]

 

 

Enyi Waislamu, hakika bin Aadam hajui wapi atafariki wala hajui lini atafariki kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

  وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ مَّاذَا تَكْسِبُ غَدًا ۖ وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ بِأَيِّ أَرْضٍ تَمُوتُ ۚ إِنَّ اللَّـهَ عَلِيمٌ خَبِيرٌ ﴿٣٤﴾

Na nafsi yoyote haijui nini itachuma kesho, na nafsi yoyote haijui itafia katika ardhi gani, hakika Allaah ni Mjuzi wa yote, Mwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika. [Luqmaan: 34]

 

 

Ikiwa hatujui tutakachokichuma kesho, jambo ambalo ni katika matendo yetu, basi hakika hatujui pia lini tutakufa kwani hilo ni katika matendo ya Allaah ('Azza wa Jalla).  Na ikiwa hatujui nchi (au mahali) gani tutakufa juu ya kwamba mtu anakwenda nchi (au mahali) anayoichagua mwenyewe, basi hakika yeye hajui lini atakufa.  Kwa hivyo basi, mahali pa kufariki na wakati wa kufariki haujulikani!

 

Tunamuomba Allaah Aturuzuku husnul-khaatimah (mwisho mwema)

 

Na si muhimu mtu kufariki lini wala kufariki wapi. Si muhimu ikiwa atafariki Makkah au Madiynah au atafariki nchi nyinginezo za Allaah na si muhimu akifariki siku ya Ijumaa au Jumatatu, au siku nyinginezo za wiki. Hakika hakuna la muhimu isipokuwa jambo la muhimu ni katika hali gani mtu atafariki? Hili ndilo la muhimu; atafariki katika hali gani? Je, utafariki ukiwa katika iymaan na ikhlaasw na tawhiyd?  Tunamuomba Allaah Atujaalie hayo yote (kufariki katika hali hizo za iymaan, ikhlaasw na tawhiyd).

 

Au je utafariki katika shaka na shirki na kufuru na ukanushaji?  Hili ndilo  muhimu, hili ndio muhimu enyi Waislamu!

 

Lakini anayetaka kufariki kifo kizuri,  basi afanye kheri kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  ni Mkarimu mno na Mpaji  mno Hatomwacha mja Wake katika dhiki ikiwa mja atakuwa ni mwenye kumkumbuka (na kumdhukuru) Allaah wakati anapokuwa katika (hali ya) raha. Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

تَعَرَّفْ إلَى اللَّهِ فِي الرَّخَاءِ يَعْرِفُك فِي الشِّدَّةِ

Mjue Allaah katika (hali ya raha) Atakujua ukiwa katika shida (au dhiki).

 

Shida gani iliyo kubwa zaidi kama kufikiwa mtu hatima yake? Shida gani kubwa zaidi kwa bin Aadam kuliko kuiga maisha ya dunia? Basi bin Aadam ikiwa atamjua Rabb wake anapokuwa katika hali ya raha kwa utii (wa Allaah) na kumkurubia kwa kumwabudu, na kudumisha kumdhukuru basi Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  Atamjua anapokuwa katika hali ya shida. Allaah Aturuzuku pamoja nanyi hilo. 

 

Jambo kuu na la muhimu ni kujua mtu atafariki akiwa katika hali gani!

 

Imetajwa kutoka kwa Salaf kwamba bin Aadam yanapomfikia mauti, (shaytwaan) humdhihirishia dini ya Kiyahudi, ya Kinaswara (Kikristo) na ya Kiislamu, na kwamba shaytwaan hujifafanisha sura ya baba yake huyo mtu. Kisha husema: “Ee mwanangu! Usiache dini ya Kiyahudi, usiache dini ya Kinaswaara!” (Huendelea kumshawishi) mpaka mtu hufariki katika mojawapo wa dini hizo mbili batili, zilizofutwa ambazo Allaah ('Azza wa Jalla)   Hazikubali! 

 

Wa-Allaahi (naapa kwa Allaah!) hii hakika ni fitnah kubwa kabisa! Lakini kwa neema ya Allaah, na kama alivyosema Shaykhul-Islaami Ibn Taymiyyah (Rahimahu-Allaah)   kwamba dini hazidhihirishwi kwa kila anayefariki. Ikiwa anayefariki ni mwenye niyyah nzuri, na ni mtu aliyenyooka katika ‘ibaadah, basi Allaah humuokoa katika   fitnah hii. Ndio maana ‘Ulamaa wengi wamefasiri kuhusu fitnatul-mamaat (fitnah ya kifo) ambayo tunajikinga nayo katika kila Swalaah  kuwa ni fitnah hii (ya shaytwaan kumjia mtu anapofariki na kumdhihirishia dini mbili. Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ametuamrisha kuwa tunapomaliza  tashahhud zetu za mwisho katika Swalaah tuseme:

 

اللّهُـمَّ إِنِّـي أَعـوذُ بِكَ مِـنْ عَذابِ القَـبْر، وَمِـنْ عَذابِ جَهَـنَّم، وَمِـنْ فِتْـنَةِ المَحْـيا وَالمَمـات، وَمِـنْ شَـرِّ فِتْـنَةِ المَسيحِ الدَّجّال

Allaahumma inniy a’uwdhu Bika min ‘adhaabil qabri, wa min ‘adhaabi jahannam, wamin fitnatil mahyaa wal mamaati, wamin sharri fitnatil-Masiyhid-dajjaal

 

Ee Allaah hakika mimi najikinga Kwako na adhabu za kaburi, na adhabu ya (Moto wa) jahannam, na fitnah ya uhai, na (fitnah) ya kifo, na shari ya fitnah ya Masiyhi-Dajjaal [Hadiyth ya Abu Hurayrah  (Radhwiya Allaahu 'anhu)  - Al-Bukhaariy (2/102), Muslim (1/412), na tamshi la Muslim]

 

‘Ulamaa wengi wakafasiri fitnatul-mamaat kwamba ni fitnah wakati wa mtu anapofariki kwa sababu ndio fitnah kubwa kabisa katika maisha ya mtu kwa vile kuna mzunguko na kugeuka kama ilivyothibiti katika Hadiyth:

 

إِنَّ الرَّجُلَ لَيَعْمَلُ عَمَلَ أَهْلِ الْجَنَّةِ حَتَّى مَا يَكُوْنُ بَيْنَهُ وَبَيْنَهَا ِ إِلاَّ ذِرَاعٌ،  فَيَسْبِقُ عَلَيْهِ الكِتَابُ فَيَعْمَلُ بِعَمَلِ أَهْلِ النَّارِ فَيَدْخُلُهَا،   

…Hakika mtu hufanya ‘amali ya watu wa Jannah mpaka ikawa hapana baina yake na Jannah ila dhiraa, akatanguliwa na aliloandikiwa (majaaliwa yake) akafanya ‘amali ya watu wa Motoni, akaingia Motoni. [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Imehadithiwa kwamba Imaam Ahmad (Rahimahu-Allaah) alipokuwa anakaribia kufariki, akisema: “Bado, bado!” Akaulizwa: “Kwanini unasema bado bado?” Akasema: “Shaytwaan yuko mbele yangu anajitafuna vidole vyake akiniambia: “Umenikwepa sijaweza kukupoteza ee Ahmad”. Ndio nikawa namjibu: Bado bado!”  Ina maana; madamu roho ya bina Aadam bado ipo mwilini mwake, basi hakika anaigopa fitnah. 

 

Enyi Waislamu! Alimjia Malakul-mawt (Malaika anayefisha) kwa Nabiy Muwsaa ('Alayhis-Salaam) ili kumtoa roho yake. Malaika akarudi kwa Allaah kumwambia: “Umenituma kwa mtu asiyetaka kufa bado.”

 

Allaah Akasema: “Je anataka kuishi bado?”. Akajibu: “Ndio”. Akasema (rudi umwambie) aweke mkono wake katika ngozi ya ng’ombe basi kwa kila unywele utakaokuwa mkononi mwake ndio itakuwa ziada ya umri wake”.  Malaika akamwendea Muwsaa ('Alayhis-Salaam)  akamwambia hivyo.  Muwsaa ('Alayhis-Salaam)  akasema: “Kisha baada ya hapo?” Malaika akajibu: “Kisha mauti” Akauliza: “Kisha baada ya hapo?” Malaika akajibu: “Kisha mauti.

  كُلُّ نَفْسٍ ذَائِقَةُ الْمَوْتِ

Kila nafsi itaonja mauti!

 

Muwsaa ('Alayhis-Salaam) akasema: “Basi bora nifishe sasa.”

 

Hivyo ni kwa sababu, vyovyote bin Aadam utakavyorefuka uhai wake (duniani), lakini pale inapomfikia mauti, ni kama kwamba hakuishi (duniani) isipokuwa saa moja ya mchana. Bali hakika Siku ya Qiyaamah itakapofika, itakuwa kama kwamba hawakuishi isipokuwa saa moja katika mchana (wa siku moja) kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

كَأَنَّهُمْ يَوْمَ يَرَوْنَ مَا يُوعَدُونَ لَمْ يَلْبَثُوا إِلَّا سَاعَةً مِنْ نَهَارٍ

Siku watakayoyaona yale waliyoahidiwa itakuwa kama kwamba hawakukaa (duniani) isipokuwa saa moja (tu) ya mchana [Al-Ahqaaf 46: 35]

 

 

Share