Matatizo Ya Ndugu Wa Mume


 

SWALI:

asalam aleykum warahmatuh llah wabarakatuh.namshukuru subhanahu wataalah kwa kunipa fursa hii.nina ndugu zake mume wangu ambao wameteta na mimi na ndugu yao wanasema ndugu yao ananiweka mimi mbele kuliko wao na ndugu yao ananiogopa mimi kama mdudu allahu aalam mungu ndie anaejuwa zaidi.sisi tukaenda siku ya idd kuwatembelea wakawa hawapo tukaacha ki note kuwajulisha kuwa tumekwenda,lakini hata simu pia wasitupigie kutujulisha wamepata note.tumeshafanya wajib wetu wa kuwatembelea,na tuna hukmu gani mbele ya m/mungu?shukran jazila

 


JIBU:

 Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Matatizo kama hayo yanatokea sana baina ya ndugu wa mume na mke. Ni wajibu wa kila mmoja wetu kujirudi katika kumkhofu Mola wetu kwa kuacha kufanyiana ubaya na badala yake kutendeana wema.

Wao kukuteta nyuma yako ni dhambi kwao kwani hii ni 'ghiybah' ambayo mtu humpatia mwenzake thawabu zake za bure bila ya yeye kuzifanyia kazi. Hivyo Muislamu anaposengenywa na mwenziwe asiwe anajali sana.

Umefanya wajibu wako wa kuwatembelea siku ya 'Iyd, nao wana makosa ya kutowasiliana na wewe baada ya kuwatembelea.

Endelea wewe kuwatendea wema, japo wao wakikitendea mabaya. Kuwa na moyo mkubwa wa kufanya hivyo kwa kutaka radhi za Mola wako. Watembelee siku nyingine za kawaida ili uwe sababu ya mumeo kuwasiliana na jamaa zake na thawabu utazipata pia na wewe. Usijali wanayosema, bali kumbuka tu kuwa unafanya kwa kutaka Ridhaa ya Mola wako. Hivyo utakuwa wewe pia ni mwenye kupata thawabu ya wema wao kwani wewe ndiye sababu ya kuwafunza.

 Utakapoendelea kuwafanyia wema kila    mara, itakuja siku watabadilika na kutambua makosa yao na ndipo watakaporudisha wema kwako na pengine uwe kipenzi chao baada ya hapo kama Anavyotufundisha Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)  

(وَمَنْ أَحْسَنُ قَوْلًا مِّمَّن دَعَا إِلَى اللَّهِ وَعَمِلَ صَالِحًا وَقَالَ إِنَّنِي مِنَ الْمُسْلِمِينَ ))

((وَلَا تَسْتَوِي الْحَسَنَةُ وَلَا السَّيِّئَةُ ادْفَعْ بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ فَإِذَا الَّذِي بَيْنَكَ وَبَيْنَهُ عَدَاوَةٌ كَأَنَّهُ وَلِيٌّ حَمِيمٌ ))

(( وَمَا يُلَقَّاهَا إِلَّا الَّذِينَ صَبَرُوا وَمَا يُلَقَّاهَا إِلَّا ذُو حَظٍّ عَظِيمٍ ))

((Na ni nani mbora wa kusema kuliko aitaye kwa Allah na akatenda mema, na akasema: Hakika mimi ni katika Waislamu?))

((Mema na maovu hayalingani. Pinga uovu kwa lilio jema zaidi. Hapo yule ambaye baina yako naye pana uadui atakuwa kama rafiki jamaa wa kukuonea uchungu))

((Lakini hawapewi wema huu ila wanaosubiri, wala hawapewi ila wenye bahati kubwa)) [Fusswilat 33-35]

Kama ulivyoona kuwa jambo hili linahitaji kuwa na subra na imaan kubwa, tunakuombea uwe miongoni mwa waliokusudiwa katika Aayah hiyo upate fadhila zake.

Na Allah Anajua zaidi   

 

Share