Talbiynah Inatuliza Moyo Na Kuondosha Baadhi Ya Huzuni

 

Talbiynah Inatuliza Moyo Na Kuondosha Baadhi Ya Huzuni

 

Alhidaaya.com

 

 

Talbiynah ni uji unaotokana na unga unaosagwa wa shayiri.

 

  

 

Talbiynah katika Sunnah ilikuwa ikitumiwa zaidi katika misiba kwa ajili ya kuondosha baadhi ya huzuni kwa dalili ya Hadiyth zifuatazo:

 

عَنْ عَائِشَةَ رضى الله عنها أَنَّهَا كَانَتْ تَأْمُرُ بِالتَّلْبِينِ لِلْمَرِيضِ وَلِلْمَحْزُونِ عَلَى الْهَالِكِ، وَكَانَتْ تَقُولُ: إِنِّي سَمِعْتُ رَسُولَ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم يَقُولُ: ((إِنَّ التَّلْبِينَةَ تُجِمُّ فُؤَادَ الْمَرِيضِ، وَتَذْهَبُ بِبَعْضِ الْحُزْنِ))

Imepokelewa kutoka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba alikuwa akiamrisha talbiynah kwa ajili ya mgonjwa na mtu aliyefikwa na huzuni kwa ajili ya kufariki mtu wake. Akawa anasema: “Nimesikia Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: ((Hakika talbiynah inamtuliza moyo wa mgonjwa na kuufanya mchangamfu na inaondosha baadhi ya huzuni zake)) [Al-Bukhaariy, Kitaab Atw-Twibb, Baab At-Talbiynah Lil-Mariydhw]

 

 

عنْ عَائِشَةَ زَوْجِ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ أَنَّهَا كَانَتْ إِذَا مَاتَ الْمَيِّتُ مِنْ أَهْلِهَا فَاجْتَمَعَ لِذَلِكَ النِّسَاءُ، ثُمَّ تَفَرَّقْنَ إِلا أَهْلَهَا وَخَاصَّتَهَا، أَمَرَتْ بِبُرْمَةٍ مِنْ تَلْبِينَةٍ فَطُبِخَتْ، ثُمَّ صُنِعَ ثَرِيدٌ فَصُبَّتْ التَّلْبِينَةُ عَلَيْهَا، ثُمَّ قَالَتْ: كُلْنَ مِنْهَا، فَإِنِّي سَمِعْتُ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ يقُول: ((التَّلْبِينَةُ مُجِمَّةٌ لِفُؤَادِ الْمَرِيضِ، تَذ هبُ بِبَعْضِ الْحُزْنِ))

Imepokelewa kutoka kwa ‘Aaishah mke wa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kwamba alikuwa pale mtu alipofariki  katika jamaa zake na wanawake wakakusanyika katika nyumba ya aliyefiwa kisha huondoka isipokuwa jamaa zake na rafiki wa karibu kabisa. Huamrisha ipikwe ‘talbiynah’ (uji wa unga wa shayiri). Kisha ‘thariyd’ (mikate katika supu ya nyama) hupikwa na ‘talbiynah’ humiminwa juu yake. Kisha ‘Aaishah huwaambia wanawake: “Kuleni kwani nimesikia Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: “Talbiynah inapooza moyo wa mgonjwa na inaondosha baadhi ya huzuni.” [Al-Bukhaariy katika Kitaab Atw-Twa’aam, Muslim katika Baab As-Salaam]

 

عَنْ عَائِشَةَ رضى الله عنها قَالَتْ قَالَ النَّبِيُّ صلى الله عليه وسلم: ((عَلَيْكُمْ بِالْبَغِيضِ النَّافِعِ التَّلْبِينَةِ))‏‏.‏ يَعْنِي الْحَسَاءَ‏.‏ قَالَتْ وَكَانَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم إِذَا اشْتَكَى أَحَدٌ مِنْ أَهْلِهِ لَمْ تَزَلِ الْبُرْمَةُ عَلَى النَّارِ حَتَّى يَنْتَهِيَ أَحَدُ طَرَفَيْهِ ‏.‏ يَعْنِي يَبْرَأُ أَوْ يَمُوتُ ‏.‏

Imepokelewa kutoka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Kuleni faida ya talbiynah inayochukizwa [asiyeipenda mgonjwa])) Yaani uji. Akasema: “Na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa pindi anapolalamika mtu katika ahli yake, basi sufuria ya kupikia haindokani katika moto mpaka mawili yatokee.” Yaani: ima apone mtu huyo au afariki. [Swahiyh Sunan Ibn Maajah 3446)]

 

عَنْ عَائِشَة رضي الله عنها عن النَّبِيُّ صلى الله عليه وسلم: ((عليكم بالبغيضِ النافعِ التلبينةِ والذي نفسي بيده إنها لتغسل بطن أحدكم كما يغسل أحدكم الوسخ عن وجهه بالما))

Imepokelewa kutoka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Kuleni kitu chenye faida ambacho hakipendwi kuliwa (na mgonjwa); talbiynah. Naapa kwa Ambaye nafsi yangu imo mikononi Mwake, hakika hiyo inasafisha tumbo la mmoja wenu kama anavyosafisha mmoja wenu uchafu wa usoni mwake kwa maji)) [Sunan An-Nasaaiy Al-Kubraa (7575) na Mustadrak ‘Alaa Asw-Swahiyhayn]

 

 

Jinsi ya kutengeneza Talbiynah

 

Shayiri hizo unaweza kuzikaanga kwanza kidogo kisha usage na kutumia unga huo kupika kama uji na kutolea kwa asali safi. Ukipenda tia maziwa kidogo. 

 

Unaweza pia kutumia shayiri hizo kwa kupikia mikate upendavyo au Khubz Raqaaiq. Bonyeza kiungo kifuatacho:

 

Khubz Raqaaiq Mikate Mepesi Mikavu

 

Pia unaweza kutumia talbiynah katika upishi wa ‘Thariyd’, ambao asili yake ni mikate mepesi mikavu inayopikwa kwa unga wa shayiri (talbiynah/barley) na inakatwakatwa na kuchanganywa na supu ya nyama. Kwa hiyo vipimo vyake vikuu ni supu ya nyama na mkate. Mikate hukatwakatwa katika sahani kisha humiminwa supu ya nyama kuirowesha na kuliwa.

 

Thariyd ni katika chakula bora kabisa alichokuwa akikipenda Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Bonyeza upate mafunzo ya upishi wake:

 

Thariyd: Supu Ya Nyama Kwa Khubz Raqaaiq Chakula Alichokuwa Akipenda Mno Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  

 

 

Thariyd ni chakula cha zama za Ujaahiliyyah (Kabla ya Uislamu) na baada ya Uislamu, katika kuwakirimu wageni wa heshima. Ni mfano wa biriani katika jamii yetu ya leo.

 

Inasemekana kuwa aliyeanza mwanzo kukipika ni Nabiy Ibraahiym ('Alayhis-Salaam) kikaendelea kupikwa na vizazi mpaka kumfikia Haashim bin 'Abdi-Manaaf ambaye ni babu wa babu yake Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Aliitwa Haashim kwa kuwa maana ya هشم ni kupondaponda au kuvurugavuruga. Naye alikuwa akiwaandalia Mahujaji wa Al-Haram Makkah thariyd akikatakata au kupondaponda mikate kwa ajili ya thariyd. Na ndio maana thariyd kikawa ndio chakula maarufu kwa Maquraysh wa Makkah katika kuwakirimu wageni wao. Kauli nyengine imesema kuwa هشم maana yake ni "kulisha walio na njaa" basi babu yake Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akaitwa  هشم الجِياع. Na Allaah Anajua zaidi      

 

Na Imaam Ibn Al-Qayyim (Rahimahu Allaah) amesema:

Thariyd ni mchanganyiko wa nyama na mkate, na nyama ni chakula bora kabisa katika vyakula vinavyoliwa na mkate. Na mkate ni chakula bora kati ya vyakula, kwa hiyo vinapochanganywa (viwili hivi) hakuna tena baada yake kilichokuwa bora kuliko hivyo.”  [Zaad Al-Ma’aad (4/271)]

  

Thariyd mpaka hii leo kimekuwa ni chakula  maarufu mno kupikwa khasa pande za Arabuni na pande za Shaam. Na kwa sasa hupikwa kwa kuongezewa aina mbali mbali za mboga na binzari apendazo mtu.  

 

 

Hadiyth kadhaa zimetajwa faida na fadhila za thariyd kama ifuatavyo:

 

1. Thariyd ni chakula kinachosifika kuwa kilichooajiliwa baraka

 

عن سلمان رضي الله عنه قال: قال رسول الله صلى الله عليه وسلم: ((البَرَكةُ في ثلاثةٍ: في الجماعةِ، والثَّريدِ والسُّحُور))ِ

Imepokelewa kutoka kwa Salmaan Al-Faarisy (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Baraka zimo katika vitatu: Al-Jamaa’ah (umoja), Ath-Thariyd (Supu ya nyama ilorowanishwa na mkate), na As-Suhuwr (daku).” [Swahiyh Al-Jaami’ (2882), Swahiyh At-Targhiyb (1065)]

 

 

2. Ubora wa Thariyd umelinganishwa na Mama wa Waumini ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa):

 

عَنْ أَبِي مُوسَى الأَشْعَرِيِّ رضى الله عنه قَالَ: قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم: ((كَمَلَ مِنَ الرِّجَالِ كَثِيرٌ، وَلَمْ يَكْمُلْ مِنَ النِّسَاءِ إِلاَّ مَرْيَمُ بِنْتُ عِمْرَانَ، وَآسِيَةُ امْرَأَةُ فِرْعَوْنَ، وَفَضْلُ عَائِشَةَ عَلَى النِّسَاءِ كَفَضْلِ الثَّرِيدِ عَلَى سَائِرِ الطَّعَامِ ))‏

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Muwsaa Al-Ash’ariyy (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Wanaume wengi wamefikia daraja ya ukamilifu lakini hakuna mwanamke aliyefikia daraja hiyo isipokuwa Aasiyah mke wa Fir'awn, na Maryam bint 'Imraan. Na ubora wa 'Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwa wanawake wengine ni kama mfano wa ubora wa thariyd kwa vyakula vingine.” [Al-Bukhaariy na wengineo]

 

 

Share