Abu Bakr Asw-Swiddiyq (رضي الله عنه)

 

 

Swahaba

 

Alhidaaya.com

 

 

Abu Bakr  Radhwiya Allaahu 'anhu  Na Sababu Za Kupewa Cheo Cha  'As-Swiddiyq' (Msema Kweli)

 

Al-Imaam An-Nawawiy amesema: "Ummah umekubaliana kwa pamoja bila ya kupingana kwamba amepewa cheo cha 'As-Swiddiyq' kutokana na kuitikia kwake haraka kumuamini Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) bila ya kusita na kukubali maneno yake kwamba daima ni ya ukweli. Alibakia kuwa mkweli maishani mwake kote wala hajapata kusema uongo  hata mara moja". 

 

Ibn Kathiyr amesema: "Kuhusu cheo chake cha  'As-Swiddiyq', inasemekana kwamba alipewa tokea zama za Ujaahiliyyah kutokana na ukweli uliojulikana kwamba alikuwa ni mkweli. Vile vile imesemekana kwamba amepewa cheo hicho kwa sababu alikuwa daima yuko tayari kumuamini Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika kila jambo alilosema".

Baadhi ya matukio yaliyodhihirisha ukweli wake na wepesi wake wa kuamini lolote alilosema Nabiy(Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

1.    Katika kisa cha Israa Wal-Mi'raaj alipobakia kuwa thabiti na kuwaambia makafiri kwamba ikiwa Muhammad  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  mwenyewe ametamka maelezo hayo basi ni kweli!

 

Ibn Kathiyr amesema: "Al-Hasan Al-Baswriy na Qataadah wamesema: "Alijulikana kwa mara ya kwanza kwa cheo hiki asubuhi ya siku ya tukio la Israa". Al-Haakim amesimulia kutoka kwa Bibi 'Aishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa) ambaye amesema: Washirikina walikuja kwa Abu Bakr wakamwambia: "Umemsikia rafiki yako anavyodai? Anadai kwamba amesafiri kwenda Baytul-Maqdis kwa usiku mmoja" Akauliza: "Je, amesema mwenyewe hivyo?". Wakajibu: "Ndio". Akasema: "Basi amesema ukweli! Naamini ukweli wake katika mambo yaliyo ya ajabu zaidi kuliko hayo, kama 'habari kutoka mbinguni asubuhi na jioni" (yaani wahyi wa Qur-aan). Tokea hapo Abu Bakr akapewa cheo cha 'As-Swiddiyq'.  [Ibn Kathiyr kasema Isnaad yake ni nzuri].

 

Al-Haakim amesimulia kutoka Nazaal ibn Swabrah ambaye amesema: "Tulimwambia 'Aliy: "Ee kamanda wa waumini! Tuelezee kuhusu Abu Bakr". Akasema: "Ni mtu aliyepewa jina la 'As-Swiddiyq' na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa kauli ya Jibriyl ('Alayhis-salaam) na kauli ya Muhammad  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Alikuwa ni Khalifa  wa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) Yeye Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliridhika naye katika dini yetu na aliridhika naye katika mambo yetu ya kidunia".  [Ibn Kathiyr kasema: Isnaad yake ni nzuri].

 

Na katika Hadiyth ya vita vya Uhud, Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliliambia jabali la Uhud lilipotikisika (kwa kulipapasa)

((أثبت أحد فإنما عليك نبي وصديق وشهيدان))

"Tulia kwani juu yako yumo Nabiy, As-Swiddiyq na mashahidi wawili" (yaani ‘Umar na ‘Uthmaan Radhwiya Allaahu 'anhu) [Al-Bukhaariy]

 

2.    Kuhama (Hijrah) kwake na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akiwa ameacha familia yake ili abakie na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  . Maswahaba wote waliruhusiwa na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kuhama (Hijrah kutoka Makkah kwenda Madiynah) isipokuwa Abu Bakr. Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akimwambia abakie ili awe swahib (rafiki) yake katika Hijrah na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Akatimiza pendekezo la Rasuli Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) .  Kisha yaliyotokea walipokimbilia katika pango la At-Thawr na   Aayah iliyoteremeshwa kuelezea hivyo:

 

إِلَّا تَنصُرُوهُ فَقَدْ نَصَرَهُ اللَّـهُ إِذْ أَخْرَجَهُ الَّذِينَ كَفَرُوا ثَانِيَ اثْنَيْنِ إِذْ هُمَا فِي الْغَارِ إِذْ يَقُولُ لِصَاحِبِهِ لَا تَحْزَنْ إِنَّ اللَّـهَ مَعَنَا ۖ فَأَنزَلَ اللَّـهُ سَكِينَتَهُ عَلَيْهِ وَأَيَّدَهُ بِجُنُودٍ لَّمْ تَرَوْهَا وَجَعَلَ كَلِمَةَ الَّذِينَ كَفَرُوا السُّفْلَىٰ ۗ وَكَلِمَةُ اللَّـهِ هِيَ الْعُلْيَا ۗ وَاللَّـهُ عَزِيزٌ حَكِيمٌ﴿٤٠﴾

Msipomnusuru (Rasuli), basi Allaah Amekwishamnusuru, pale walipomtoa (Makkah) wale waliokufuru akiwa wa pili katika wawili; walipokuwa katika pango, alipomwambia swahibu yake: Usihuzunike, hakika Allaah Yu Pamoja nasi. Basi Allaah Akamteremshia utulivu Wake, na Akamsaidia kwa majeshi msiyoyaona, na Akajaalia neno la waliokufuru kuwa chini. Na Neno la Allaah kuwa ndilo lililo juu. Na Allaah ni Mwenye enzi ya nguvu Asiyeshindika, Mwenye hikmah wa yote. [At-Tawbah:40]

 

3.    Alipolia wakati Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alisema: "Hakika kuna mja alipewa uchaguzi na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)   baina ya Duniya na Akhera, mja akachagua Akhera". Abu Bakr alijua kuwa huyo mja ni Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na alitambua kauli hiyo imemaanisha kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ataaga duniya karibuni. [Al-Bukhaariy]

 

4.  Alipobakia kuwa thabiti katika kifo cha Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam)wakati Swahaba waliduwaa hawakujua la kufanya na khutbah yake aliyotoa ya kuwatuliza.

 

5.    Kuthibitika kwake ingawa alikuwa pekee katika kupeleka jeshi na    kumfanya Usaamah bin Zayd awe mwenye kuongoza jeshi.

 

6.    Kung'ang’ania kwake katika kupigana na watu waliotoka nje ya Uislam baada ya kifo cha Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)

 

7. Alipomchagua 'Umar bnul-Khatwaab (Radhwiya Allaahu 'anhu)kuwa Khaliyfah wa Waislam, lilikuwa ni chaguo tukufu lililokubalika na Ummah na ni jambo ambalo limeainishwa na Maulamaa kuwa ni jambo mojawapo muhimu la mafanikio katika historia.

 

 

 

 

Share