Kisa Cha Aswhaabul-Kahf (Watu Wa Pangoni) - 2

 

Kisa Cha Asw-haabul Kahf (Watu Wa Pangoni) -2

 

Alhidaaya.com

 

 

 

Kauli Zake Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

 وَتَرَى الشَّمْسَ إِذَا طَلَعَت تَّزَاوَرُ عَن كَهْفِهِمْ ذَاتَ الْيَمِينِ وَإِذَا غَرَبَت تَّقْرِضُهُمْ ذَاتَ الشِّمَالِ وَهُمْ فِي فَجْوَةٍ مِّنْهُ ۚ ذَٰلِكَ مِنْ آيَاتِ اللَّـهِ ۗ مَن يَهْدِ اللَّـهُ فَهُوَ الْمُهْتَدِ ۖ وَمَن يُضْلِلْ فَلَن تَجِدَ لَهُ وَلِيًّا مُّرْشِدًا ﴿١٧﴾ وَتَحْسَبُهُمْ أَيْقَاظًا وَهُمْ رُقُودٌ ۚ وَنُقَلِّبُهُمْ ذَاتَ الْيَمِينِ وَذَاتَ الشِّمَالِ ۖ وَكَلْبُهُم بَاسِطٌ ذِرَاعَيْهِ بِالْوَصِيدِ ۚ لَوِ اطَّلَعْتَ عَلَيْهِمْ لَوَلَّيْتَ مِنْهُمْ فِرَارًا وَلَمُلِئْتَ مِنْهُمْ رُعْبًا ﴿١٨﴾كَذَٰلِكَ بَعَثْنَاهُمْ لِيَتَسَاءَلُوا بَيْنَهُمْ ۚ قَالَ قَائِلٌ مِّنْهُمْ كَمْ لَبِثْتُمْ ۖ قَالُوا لَبِثْنَا يَوْمًا أَوْ بَعْضَ يَوْمٍ ۚ قَالُوا رَبُّكُمْ أَعْلَمُ بِمَا لَبِثْتُمْ فَابْعَثُوا أَحَدَكُم بِوَرِقِكُمْ هَـٰذِهِ إِلَى الْمَدِينَةِ فَلْيَنظُرْ أَيُّهَا أَزْكَىٰ طَعَامًا فَلْيَأْتِكُم بِرِزْقٍ مِّنْهُ وَلْيَتَلَطَّفْ وَلَا يُشْعِرَنَّ بِكُمْ أَحَدًا ﴿١٩﴾إِنَّهُمْ إِن يَظْهَرُوا عَلَيْكُمْ يَرْجُمُوكُمْ أَوْ يُعِيدُوكُمْ فِي مِلَّتِهِمْ وَلَن تُفْلِحُوا إِذًا أَبَدًا ﴿٢٠﴾

17. Na ungeliona jua linapochomoza linaelemea pango lao kwa upande wa kulia; na linapokuchwa linawakwepa upande wa kushoto, nao wamo katika uwazi wa humo. Hiyo ni miongoni mwa Aayaat (miujiza, ishara) za Allaah. Ambaye Allaah Amemwongoza, basi yeye ndiye aliyehidika. Na Anayemwacha kupotoka basi hutompatia mlinzi wa kumuongoza. 18. Na utawadhania wamacho na hali wao wamelala. Na Tunawageuza upande wa kulia na upande wa kushoto. Na mbwa wao amenyoosha miguu yake ya mbele kizingitini. Kama ungeliwatokea, bila shaka ungegeuka kuwakimbia, na bila shaka ungejazwa tisho kubwa kuwaogopa. 19. Na hivyo ndivyo Tulivyowainua usingizini ili waulizane baina yao. Msemaji miongoni mwao akasema: Muda gani mmekaa? Wakasema: Tumekaa siku moja au sehemu ya siku.  Wakasema: Rabb wenu Anajua zaidi muda mliokaa. Basi tumeni mmoja wenu mjini kwa noti zenu hizi atazame chakula chake kipi kifaacho zaidi kisha akuleteeni chakula hicho. Na awe makini na busara na wala asikutambulisheni kwa yeyote. 20. Hakika wao wakikugundueni, watakupigeni mawe au watakurudisheni katika dini yao; na hapo hamtofaulu abadani. [Al-Kahf: 17-20].

 

Tunaendelea na Kisa cha Asw-haabul-Kahf, baada ya kukimbilia pangoni vijana hao, na kulala humo kwa muda wa miaka zaidi ya mia tatu, bila ya kujulikana na watu, na hivyo ni kutokana na Rahmah ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) kama Anavosema:

 

وَتَرَى الشَّمْسَ إِذَا طَلَعَت تَّزَاوَرُ عَن كَهْفِهِمْ ذَاتَ الْيَمِينِ وَإِذَا غَرَبَت تَّقْرِضُهُمْ ذَاتَ الشِّمَالِ وَهُمْ فِي فَجْوَةٍ مِّنْهُ ۚ ذَٰلِكَ مِنْ آيَاتِ اللَّـهِ ۗ مَن يَهْدِ اللَّـهُ فَهُوَ الْمُهْتَدِ ۖ وَمَن يُضْلِلْ فَلَن تَجِدَ لَهُ وَلِيًّا مُّرْشِدًا ﴿١٧﴾

 

17. Na ungeliona jua linapochomoza linaelemea pango lao kwa upande wa kulia; na linapokuchwa linawakwepa upande wa kushoto, nao wamo katika uwazi wa humo. Hiyo ni miongoni mwa Aayaat (miujiza, ishara) za Allaah. Ambaye Allaah Amemwongoza, basi yeye ndiye aliyehidika. Na Anayemwacha kupotoka basi hutompatia mlinzi wa kumuongoza

 

 

Hapa inaonyesha kwamba mlango wa pango hilo ulielelekea upande wa Kaskazini kwa sababu Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Anatuambia kwamba jua lilipokuwa linachomoza, mwangaza ulikuwa unaingia katika pango.

 

ذَاتَ الْيَمِينِ

 kuliani mwao

 

 وَتَرَى الشَّمْسَ إِذَا طَلَعَت تَّزَاوَرُ عَن كَهْفِهِمْ ذَاتَ الْيَمِينِ ﴿١٧﴾

17. Na ungeliona jua linapochomoza linaelemea pango lao kwa upande wa kulia;

 

Maana: Kivuli kilipungua upande wa kulia kama alivyosema Ibn 'Abbaas, Sa'iyd bin Jubayr na Qataadah.

 

وَإِذَا غَرَبَت تَّقْرِضُهُمْ ذَاتَ الشِّمَالِ﴿١٧﴾

17.  na linapokuchwa linawakwepa upande wa kushoto,

Maana: Jua liliingia katika pango lao kutoka upande wa kushoto wa mlango wa pango, ina maana kutoka upande wa Magharibi.

 

Ibn 'Abbaas, Mujaahid na Qataadah wamesema kwamba:

 

  تَّقْرِضُهُمْ

 Linawakwepa

 

Yaani Jua lilikuwa likiwaangazia kisha likiwaondokea. [Atw-Twabariy 17: 621,622].

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Ametuambia haya na Ametaka tufahamu na tutafakari maana yake, lakini Hakutuambia sehemu iliyokuwepo hilo pango, yaani nchi gani, kwa sababu hakuna faida kwetu kujua hilo na haipatikani lengo la kujifunza Shariy’ah ndani yake. Na kama ingelikuwa inapatikana maslahi ya kiroho au ya kidini basi Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na Rasuli Wake wangelitufundisha kwa kutupa maelezo yake kama alivyosema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).

 

 

والذي نفسي بيده مَا تَرَكْتُ مِن شَيءٍ يُقَرِّبُكُمْ إِلى الجَنَّةِ إِلاَّ أَمَرْتُكُمْ بِهِ، وَلاَ مِن شيءٍ يُبعدُكُمْ عَنِ النَّارِ إِلاَّ نَهَيْتُكُمْ عَنْهُ

Sijaacha jambo lolote litakalokukurubisheni na Jannah isipokuwa nimekuamrisheni. Na wala lolote litakalokuepusheni na moto isipokuwa nimekuukatazeni)) [Hadiyth ya Abdullaah bin Mas’uwd (Radhwiya Allaahu 'anhu) As-Silsilah Asw-Swahiyhah (2866)]

 

Ibn 'Abbaas anatafsiri kuhusu:

 

 تَّزَاوَرُ عَن كَهْفِهِمْ ذَاتَ الْيَمِينِ وَإِذَا غَرَبَت تَّقْرِضُهُمْ ذَاتَ الشِّمَالِ وَهُمْ فِي فَجْوَةٍ مِّنْهُ ۚ﴿١٧﴾

 

17. …linaelemea pango lao kwa upande wa kulia; na linapokuchwa linawakwepa upande wa kushoto, nao wamo katika uwazi wa humo. …

Maana, jua liliingia katika pango bila ya kuwagusa, kwa sababu lingeliwagusa, lingeliwaunguza miili yao na nguo zao. [Atw-Twabariy 17: 620].

 

 ذَٰلِكَ مِنْ آيَاتِ اللَّـهِ ۗ ...﴿١٧﴾

17...Hiyo ni miongoni mwa Aayaat (miujiza, ishara) za Allaah.

 

Ni Ishara ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Kuwaongoza katika pango na ni miujiza Yake kuwajaalia kuwa hai, na jua na upepo ukipita katika pango kuwahifadhi miili yao.

 

Kisha Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Anasema:

 

مَن يَهْدِ اللَّـهُ فَهُوَ الْمُهْتَدِ ۖ وَمَن يُضْلِلْ فَلَن تَجِدَ لَهُ وَلِيًّا مُّرْشِدًا ﴿١٧﴾

17. Ambaye Allaah Amemwongoza, basi yeye ndiye aliyehidika. Na Anayemwacha kupotoka basi hutompatia mlinzi wa kumuongoza. 

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Ndiye Aliyewaongoza hawa vijana katika uongofu wa haki, kwani yule Anayemuongoa hakuna wa kumpotoa na Anayempotoa hakuna wa kumuongoa kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

 وَتَحْسَبُهُمْ أَيْقَاظًا وَهُمْ رُقُودٌ ۚ وَنُقَلِّبُهُمْ ذَاتَ الْيَمِينِ وَذَاتَ الشِّمَالِ ۖ وَكَلْبُهُم بَاسِطٌ ذِرَاعَيْهِ بِالْوَصِيدِ ۚ لَوِ اطَّلَعْتَ عَلَيْهِمْ لَوَلَّيْتَ مِنْهُمْ فِرَارًا وَلَمُلِئْتَ مِنْهُمْ رُعْبًا ﴿١٨﴾

18. Na utawadhania wamacho na hali wao wamelala. Na Tunawageuza upande wa kulia na upande wa kushoto. Na mbwa wao amenyoosha miguu yake ya mbele kizingitini. Kama ungeliwatokea, bila shaka ungegeuka kuwakimbia, na bila shaka ungejazwa tisho kubwa kuwaogopa. [Al-Kahf: 18] 

 

 

 

Kulala Kwao Katika Pango:

 

 

Baadhi wa wafasiri wa Qur-aan wamesema kuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Alipowafanya walale, kope za macho yao hazikufunga. Kubakia kwa macho yao kuwa wazi ilikuwa ni bora kwa sababu ya kuhifadhi macho yao, kama inavyosemekana kuwa mbwa mwitu akilala anafunga jicho moja na moja huliacha wazi, kisha anabadilisha jicho jingine huku amelala.

 

  وَتَحْسَبُهُمْ أَيْقَاظًا وَهُمْ رُقُودٌ ۚ 

 18. Na utawadhania wamacho na hali wao wamelala. 

 وَنُقَلِّبُهُمْ ذَاتَ الْيَمِينِ وَذَاتَ الشِّمَالِ ۖ 

18. Na Tunawageuza upande wa kulia na upande wa kushoto.

 

Ibn 'Abbaas kasema: Kama wasingelikuwa wanageuka, ardhi ingeliwafanya waoze. [Atw-Twabariy 17: 620].

 

 وَكَلْبُهُم بَاسِطٌ ذِرَاعَيْهِ بِالْوَصِيدِ ۚ 

18. Na mbwa wao amenyoosha miguu yake ya mbele kizingitini…

 

Ibn 'Abbaas, Mujaahid, Sa'iyd bin Jubayr na Qataadah wamesema: Waswiyd ina maana kizingiti. Ibn 'Abbaas kasema: “pembeni mwa mlango”. Pia imesemwa kuwa ni ardhini. Lakini usemi wa rai ya uhakika ni kuwa ni kizingiti cha mlango (wa pango). [Atw-Twabariy 17: 624-625].

 

Kama vile ilivyotajwa katika Aayah ya Suratul-Humazah: 8

 

إِنَّهَا عَلَيْهِم مُّؤْصَدَةٌ ﴿٨﴾

8. Hakika huo utafungiwa juu yao kila upande. 

 

Mbwa wao alilala chini katika mlango. Na hivyo ni tabia ya mbwa. Na kazi yake mbwa kulinda kama alivyosema Ibn Jubayr.  Mbwa huyo alikaa nje ya mlango kwa sababu Malaaika hawaingii nyumba iliyo na mbwa kama ilivyosimuliwa katika Al-Bukhaariy, wala hawaingii katika nyumba iliyo na picha za viumbe zilizochorwa au vinyago.

 

Neema hiyo ya kulala ilimfikia mpaka mbwa wao. Na hii ni mfano wa faida ya kuambatana na watu wema. Ilisemekana, kwamba huyo mbwa alikuwa wa mpishi wa mfalme ambaye aliawaamini vijana hao kuhusu Dini yao ya Tawhiyd. Na Allaah Anajua zaidi.

 

 لَوِ اطَّلَعْتَ عَلَيْهِمْ لَوَلَّيْتَ مِنْهُمْ فِرَارًا وَلَمُلِئْتَ مِنْهُمْ رُعْبًا ﴿١٨﴾

18. Kama ungeliwatokea, bila shaka ungegeuka kuwakimbia, na bila shaka ungejazwa tisho kubwa kuwaogopa.

 

Maana yake ni: Vile Allaah Alivyowafanya waonekane wanatisha ili mtu asiwakaribie kuwagusa na kuwaamsha mpaka muda Alioutaka Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) walale uishe. Hii ni Hikma na Rahmah Yake Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa).

 

Walipoamka wakamtuma mmoja wao sokoni kununua chakula.

 

Anasema Allaah ('Azza wa Jalla):

 

 كَذَٰلِكَ بَعَثْنَاهُمْ لِيَتَسَاءَلُوا بَيْنَهُمْ ۚ قَالَ قَائِلٌ مِّنْهُمْ كَمْ لَبِثْتُمْ ۖ قَالُوا لَبِثْنَا يَوْمًا أَوْ بَعْضَ يَوْمٍ ۚ قَالُوا رَبُّكُمْ أَعْلَمُ بِمَا لَبِثْتُمْ فَابْعَثُوا أَحَدَكُم بِوَرِقِكُمْ هَـٰذِهِ إِلَى الْمَدِينَةِ فَلْيَنظُرْ أَيُّهَا أَزْكَىٰ طَعَامًا فَلْيَأْتِكُم بِرِزْقٍ مِّنْهُ وَلْيَتَلَطَّفْ وَلَا يُشْعِرَنَّ بِكُمْ أَحَدًا ﴿١٩﴾

19. Na hivyo ndivyo Tulivyowainua usingizini ili waulizane baina yao. Msemaji miongoni mwao akasema: Muda gani mmekaa? Wakasema: Tumekaa siku moja au sehemu ya siku.  Wakasema: Rabb wenu Anajua zaidi muda mliokaa. Basi tumeni mmoja wenu mjini kwa noti zenu hizi atazame chakula chake kipi kifaacho zaidi kisha akuleteeni chakula hicho. Na awe makini na busara na wala asikutambulisheni kwa yeyote. 

 

Maana ya kauli hiyo ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) ni: Tulivyowafanya kulala, tumewafufua na miili yao, nywele na ngozi zao, bila ya kuharibika kiungo chochote cha mwili wao na hakuna kilichopunguka katika kuonekana kwao. Hii ni baada ya miaka 309, ndio maana wakawa wanaulizana,

 

كَمْ لَبِثْتُمْ ۖ 

Muda gani mmekaa?

 

Kwa sababu walipoingia katika pango ilikuwa mwanzo wa siku na walipoamka ilikuwa mwisho wa siku ndio maana wakasema:

 

 قَالُوا لَبِثْنَا يَوْمًا أَوْ بَعْضَ يَوْمٍ ۚ

Wakasema: Tumekaa siku moja au sehemu ya siku. 

  قَالُوا رَبُّكُمْ أَعْلَمُ بِمَا لَبِثْتُمْ..

Wakasema: Rabb wenu Anajua zaidi muda mliokaa.

 

Maana: Allaah Anajua zaidi hali yenu. Walikuwa hawana hakika muda waliolala, lakini Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Ndiye Ajuaye. Wakaelekea kutafuta mahitajio yaliyo muhimu kwao nayo ni chakula na kinywaji, hivyo wakasema:

 

 فَابْعَثُوا أَحَدَكُم بِوَرِقِكُمْ هَـٰذِهِ إِلَى الْمَدِينَةِ

Basi tumeni mmoja wenu mjini...

 

Walikuwa na pesa zao za Dirhams; zilokuwa zikitumika wakati huo. Walizitoa baadhi yake katika swadaqah na baadhi waliweka kwa ajili ya matumizi. Wakamtuma mmoja wao aende mjini (mji wao waliokuwa wakiishi) ili kutafuta chakula kilicho safi kabisa.

 

فَلْيَنظُرْ أَيُّهَا أَزْكَىٰ طَعَامًا

Atazame chakula chake kipi kifaacho zaidi..

 

أَزْكَى 

 

Hapa inamaanisha: Kilichotakasika. Maana yake ni kama ilivyotajwa katika Aayah zifautazo:   

 

..ۚ وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ مَا زَكَىٰ مِنكُم مِّنْ أَحَدٍ أَبَدًا .. ﴿٢١﴾

21. Na lau si fadhila ya Allaah juu yenu na rahmah Yake asingelitakasika miongoni mwenu hata mmoja abadani[An-Nuwr:  21].

 

قَدْ أَفْلَحَ مَن تَزَكَّىٰ ﴿١٤﴾

14. Hakika amefaulu ambaye amejitakasa. [Al-A’laa: 14].

 

فَلْيَأْتِكُم بِرِزْقٍ مِّنْهُ

19. Kisha akuleteeni chakula hicho…

 

 وَلْيَتَلَطَّفْ

Na awe makini na busara

 

Kwa maana: Ajihadhari asije kutambulikana anapokwenda kununua chakula na anaporudi.

 

 وَلَا يُشْعِرَنَّ بِكُمْ أَحَدًا

Na wala asikutambulisheni kwa yeyote.

 

Aayah zinaendelea:

 

 إِنَّهُمْ إِن يَظْهَرُوا عَلَيْكُمْ يَرْجُمُوكُمْ أَوْ يُعِيدُوكُمْ فِي مِلَّتِهِمْ وَلَن تُفْلِحُوا إِذًا أَبَدًا﴿٢٠﴾

20. Hakika wao wakikugundueni, watakupigeni mawe au watakurudisheni katika dini yao; na hapo hamtofaulu abadani. 

 

  إنّهُمْ إِن يَظْهَرُوا عَلَيْكُمْ  

Hakika wao wakikugundueni,

 

 يَرْجُمُوكُمْ أَوْ يُعِيدُوكُمْ فِي مِلَّتِهِمْ

Watakupigeni mawe, au watakurudisheni katika dini yao;

 

Walikusudia ni watu wa ule mji wa Decianus, ambao waliogopa kuwa wakiwajua watawaadhibu kwa kuwatesa kwa kila aina ya mateso ili warudi katika dini yao ya kuabudu masanamu, au wawatese mpaka wawaue. Lakini vijana hao, ilikuwa ni bora kwao kufa kuliko kurudia dini ya ushirikina kwani walitambua kuwa hawatofaulu duniani wala akhera, ndio maana wakasema,

 

 وَلَن تُفْلِحُوا إِذًا أَبَدًا﴿٢٠﴾

Na hapo hamtofaulu abadani.

 

 

 

 

Mafunzo Na Mwongozo:

 

 

  1. Kudhihirisha upole wa Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) kwa Awliyaa (Vipenzi) Wake kwa kuwakirimu wanapohajiri kwa ajili Yake.

 

  1. Uongofu umo katika Mikono ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) kwa hiyo aliyeongoka ameongozwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na aliyepotea (kwa kujipotosha mwenyewe) basi, amepotezwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa). Inatupasa tumuombe Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Hidaaya na tujikinge Kwake dhidi ya upotofu.

 

  1. Udhihirisho wa Qudra (Uwezo) wa Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na Ujuzi Wake na Hikma Yake.  

 

 

  1. Inampasa Muislamu kutafuta chakula na kinywaji cha halaal na mengineyo.

 

 

  1. Kufariki katika shirki na kufru kunamzuia mtu kupata kufaulu siku ya Qiyaamah.

 

.../3

 

 

 

 

Share