Mwanamme Aliyebaka Mwanamke Na Mwanamme Nini Hukmu Yake?

 

 

Mwanamme Aliyebaka Mwanamke Na Mwanamme Nini Hukmu Yake?

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali:

 

Ni nini hukmu ya mwanamme ambaye

 

1) Amembaka mwanamke

2) Amembaka mwanamme?

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Hakika ilikuwa yatakikana sisi ndio tuwe mbali sana na maovu haya. Kwa wakati huu maovu haya yamekuwa ni mema na mema yamekuwa maovu. Mwenye kufanya mema anaonekana kuwa ni mshamba, mjinga na hastahiki kuitwa msomi hata akiwa ni msomi.

 

 

Hatuna budi kuibadilisha hali hii na kurudi katika machimbuko yetu ya Dini ili tuweze kuongoza ulimwengu wote kwa maadili mema tuliyofunzwa na Dini yetu tukufu. Hakuna jambo zuri ila Uislamu umehimiza na kulipatia kipaumbele na hakuna ovu isipokuwa Uislamu umelipiga vita kwa kiasi kikubwa. Kufanya jema ni katika maslahi yetu na pia kuacha baya ni hivyo hivyo.

 

 

Maswali yako mawili yameegemea katika zinaa na liwati lakini ya kutumia mabavu. Haya maovu mawili ni janga na balaa kwa wanadamu mbali na kuwa tunapuuza hilo. Utekelezaji wa maovu haya unaleta magonjwa kama ukimwi, kisonono na kadhalika, huleta mmomonyoko wa maadili, madhara ya kinafsi na kijamii na pia kuleta watoto wasio na nasaba yoyote ile.  Ni wazi kuwa hukumu ya Uislamu kuhusu zinaa ni haraam. Hiyo ni kwa kauli ya Allaah Aliyetukuka:

 

وَلَا تَقْرَبُوا الزِّنَىٰ ۖ 

 'Na Wala usikaribie zinaa' [Al-Israa: 32].

 

Pia Aliyetukuka Ametuelezea sifa za waumini wa kweli pale Aliposema:

 

..وَلَا يَزْنُونَ ۚ وَمَن يَفْعَلْ ذَٰلِكَ يَلْقَ أَثَامًا ﴿٦٨﴾

'…wala hawazini na mwenye kufanya hivyo anapata madhambi' [Al-Furqaan: 68].

 

Na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: 'Hazini mzinifu wakati anapozini na hali ni Muumini' [al-Bukhaariy na Muslim].

 

 

Ama kuhusu adhabu ya zinaa iko wazi kabisa ya kubaka itakuwa ni zaidi ya hiyo kwa yale madhara yanayomfikia aliyebakwa. Zinaa ya kawaida ikiwa aliyefanya hajaoa atapigwa mijeledi mia moja (Tazama Qur-aan 24: 2) na kutolewa mjini kwa mwaka mmoja. Na Imaam au Khaliyfah anaweza kumpatia adhabu ya ziada (ta'aziyr) kama anavyoona ni munasibu na sawa. Na ikiwa atatumia nguvu kama kutumia kisu, panga au bunduki ataingia katika Aayah ifuatayo:

 

إِنَّمَا جَزَاءُ الَّذِينَ يُحَارِبُونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَيَسْعَوْنَ فِي الْأَرْضِ فَسَادًا أَن يُقَتَّلُوا أَوْ يُصَلَّبُوا أَوْ تُقَطَّعَ أَيْدِيهِمْ وَأَرْجُلُهُم مِّنْ خِلَافٍ أَوْ يُنفَوْا مِنَ الْأَرْضِ ۚ ذَٰلِكَ لَهُمْ خِزْيٌ فِي الدُّنْيَا ۖ وَلَهُمْ فِي الْآخِرَةِ عَذَابٌ عَظِيمٌ ﴿٣٣﴾

Hakika jazaa ya wale wanaompiga vita Allaah na Rasuli Wake na wanafanya bidii kufanya ufisadi katika ardhi; ni kwamba wauawe au wasulubiwe au ikatwe mikono yao na miguu yao kwa kutofautisha au watolewe katika nchi. Hiyo ndiyo hizaya yao duniani. Na Aakhirah watapata adhabu kuu. [Al-Maaidah: 33].

 

Ama akiwa ameoa basi anafaa apigwe mawe hadi kufa. Hii ni kwa kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

'Si halali damu ya Muislamu ila kwa moja katika mambo matatu: Mzinifu mwenye mke (au mwenye mume), nafsi kwa nafsi na mwenye kuacha Dini yake, aliyejitenga na Waislamu' [al-Bukhaariy na Muslim].  

 

Liwati nayo imeharamishwa na Uislamu kwa uwazi kabisa. Allaah Aliyetukuka Anasema:

 

أَتَأْتُونَ الذُّكْرَانَ مِنَ الْعَالَمِينَ ﴿١٦٥﴾.... بَلْ أَنتُمْ قَوْمٌ عَادُونَ ﴿١٦٦﴾

Je, mnawaendea wanaume miongoni mwa walimwengu? Bali nyinyi ni watu mliopindukia mipaka. [Ash-Shu'araa: 165 – 166].

 

Na amesema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

 

'Amelaaniwa mwenye kufanya kitendo cha kaumu Luutw; Amelaaniwa mwenye kufanya kitendo cha kaumu Luutw; Amelaaniwa mwenye kufanya kitendo cha kaumu Luutw Amelaaniwa mwenye kufanya kitendo cha kaumu Luutw Amelaaniwa mwenye kufanya kitendo cha kaumu Luutw' [al-Haakim].

 

Pia:

 

'Watu aina nne wanapambazuka na kuingia na usiku wakiwa wameghadhibikiwa na Allaah'. Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) akasema: 'Ni nani hao ee Rasuli wa Allaah?' Akasema: 'Wanaume wenye kujifananisha na wanawake; wanawake wenye kujifananisha na wanaume; wenye kuwajia wanyama (kufanya kitendo cha ndoa na mnyama; na wenye kuwajia wanaume' [Atw-Twabaraaniy na al-Bayhaqiy].

 

Ama adhabu haina utata wowote kwani Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

'Mnayemuona akifanya amali ya kaumu ya watu wa Luutw, muueni anayefanya na anayefanywa' [Abu Daawuud, at-Tirmidhiy na Ibn Maajah].

 

Pengine hapa kutakuja utata kwa kuwa mwenye kufanywa hakufanya kitendo hicho kwa hiyari bali ametenzwa nguvu, itakuwaje? Suala hili linajibiwa na kauli ya Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) pale aliposema:

 

'Hakika Allaah Amenisamehea Ummah wangu kukosea kwao, kusahau kwao na waliyotendeshwa nguvu' [Ibn Maajah, al-Bayhaqiy na wengineo].

 

Hivyo, kwa mujibu wa kauli hii aliyefanywa kwa nguvu anasamehewa na sheria.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

Share